Sala za Katoliki: Sala Muhimu Kwa Mkristu Mkatoliki

SALA YA KUMWOMBA MTAKATIFU TERESIA WA MTOTO YESU

Ee Mtakatifu Teresia wa mtoto Yesu, ulistahili kuitwa Msimamizi wa misioni katoliki za dunia yote. Kumbuka ile tamaa yako kuu uliyoonyesha huku duniani ya ” kusimika Msalaba wa Yesu Kristu, katika nchi zote na kuhubiri Injili mpaka mwisho wa dunia” . Twakuomba kwa ajili ya maagano yako, wasaidie mapadre, wamisionari, na kanisa zima.

Ee Mtakatifu Teresia wa mtoto Yesu ” Msimamizi wa misioni” UTUOMBEE

SALA KWA MT. YOSEFU KWA AJILI YA KULIOMBEA KANISA LA MAHUJAJI

Ee Mtukufu Mt. Yosefu, ulichaguliwa na Mungu kuwa Baba Mlishi wa Yesu, mchumba safi kabisa wa Maria Bikira Milele, na mkubwa wa Familia Takatifu. Umechaguliwa na Mwakilishi wa Kristu kama Msimamizi wa kimbingu na mlinzi wa Kanisa alilolianzisha Kristu. Ndiyo maana ninakuomba kwa matumaini makuu usaidizi wako wenye nguvu kwa ajili ya Kanisa zima duniani.

Mlinde kwa namna ya pekee, kwa upendo wa kikweli wa ki-baba, Baba Mtakatifu na Maaskofu wote na Mapadre wenye ushirika na Kiti cha Petro. Uwe mlinzi wao wote wanaotumikia wokovu wa wanadamu kati ya majaribu na mahangaiko ya maisha haya, na utujalie kwamba watu wote wa dunia hii wamfuate Kristu na Kanisa alilolianzisha.

Mpendwa Mtakatifu Yosefu, ukubali majitoleo ya nafsi yangu ambayo sasa ninafanya. Ninajiweka wakfu kwako kwa ajili ya utumishi wako, ili daima wewe uwe baba yangu, mlinzi wangu, na kiongozi wangu katika njia ya wokovu. Unijalie usafi mkuu wa moyo na matamanio makuu ya maisha ya kiroho. Unijalie ili matendo yangu yote, kwa mfano wako, yawe kwa ajili ya sifa na utukufu wa Mungu, pamoja na Moyo wa kimungu wa Yesu, moyo safi wa Maria, na moyo wako wa ki-baba. Uniombee, nami nishiriki kifo chako cha furaha na kitakatifu.
Amina.

Majitoleo kwa Bikira Maria

(Sala iliyotungwa na Mtk. Aloisi)
Bibi yangu mtukufu Maria, nakuwekea amana ya roho yangu na mwili wangu, nikikuomba uipokee amana yangu, kuitunzia ulinzi mwema ulinzi bora, ninakuaminia na kila neno langu, matumaini na kitulizo na kisongo chote, na masumbuko na uzima na ukomo wa uzima wangu: nitakayo ndiyo unifanyizie kwa maombezi na stahili zako, ili mambo yangu yote yapate kuongoka, yakiwa na kufuata mapenzi yako, pamoja na mapenzi ya Mwanao. Amina.

SALA YA KUWAOMBEA MAPADRE

Ee Bwana Yesu Kristo. Mkombozi wetu, kwa mapendo na tamaa yako ya kutaka kulinda vema Kanisa lako, ukachagua Mapadri wawe Wachungaji na Viongozi wa roho za watu. Nakuomba sana; ubariki nia na bidii inayowapasa Mapadri wote katika kazi zao. Uwaongezee Utakatifu.

Uwatie moyo mzuri wenye mapendo makubwa kwako na roho za watu. Hivyo wakiisha kupata wenyewe Utakatifu, waweze kuwaongoza vizuri watu walio chini ya ulinzi wao, katika njia ya Utakatifu na furaha ya milele. Uwajalie neema zote za hali ya Upadri. Uwajalie ili waonyeshe kila siku ya maisha yao mfano wa kila fadhila ya mapendo na ya uaminifu katika Kanisa, kwa Baba Mtakatifu na kwa Maaskofu.

Yesu mpendelevu, uangalie kwa mapendo kazi na mateso ya Mapadri wako; ubariki na ustawishe mafundisho yao; wanapowafundisha watoto, wanapowahubiria watu, wanapowatuliza wakosefu watubu na wanapowasaidia wagonjwa na wale wanaokaribia mauti, Ee Yesu uwe pamoja nao. Uwakinge na hatari zote za roho na za mwili.

Mwokozi Yesu, ulijalie Kanisa liwe na Mapadri wengi walio Watakatifu. Uwajalie watoto na vijana wengi wasikie wito wa Upadri, uwatie furaha na Utakatifu na roho za Mapadri waliokufa uzijalie punziko la amani.

Kwa mimi mwenyewe Ee Yesu mpendelevu, naomba unijalie roho ya imani na utii mnyenyekevu ili niwaheshimu Mapadri kama Mawakili wa Mungu. Niwatii katika njia zote za wokovu wa roho yangu. Amina.

SALA MUHIMU ZA MKRISTO ZA KILA SIKU ASUBUHI

SALA YA ASUBUHI

Tuusifu Utatu Mtakatifu wa Mungu Mwenyezi, Baba, Mwana na Roho Mtakatifu, milele na milele, Amina.

Ee Utatu Mtakatifu wa Mwenyezi Mungu, Baba, Mwana na Roho Mtakatifu, nasadiki kuwa upo hapa na mahali pote. Ee Mungu wangu, umeniumba, umenikomboa, umenifanya mkristo, umenizidishia neema zako hapa duniani, umenitayarishia makao yangu mbinguni, umenijalia na siku hii nikutumikie. Ee Mungu wangu! Nakuabudu, nakushukuru, nakuomba toba, nakupenda! Ee Mungu wangu, nakutolea roho yangu, na mawazo, na maneno, na kazi, na furaha, na mateso yangu: uyapokee unipe neema yako nisikutende leo dhambi!

Majitoleo ya Asubuhi

Ee Baba yetu Mungu Mkuu, Umenilinda usiku huu, Ninakushukuru kwa moyo, Ee Baba, Mwana na Roho, Nilinde tena siku hii, Niache dhambi nikutii, Naomba sana Baba wee, Baraka yako nipokee, Bikira safi ee Maria, Nisipotee unisimamie, Mlinzi Mkuu Malaika wee, Kwa Mungu wetu niombee, Nitake nitende mema tu, Na mwisho nije kwake juu, Amina.

Kuweka nia njema

Kumheshimu Mungu wangu, Namtolea roho yangu, Nifanye kazi nipumzike, Amri zake tu nishike, Wazo neno tendo lote, Namtolea Mungu pote, Roho, mwili chote changu, pendo na uzima wangu, Mungu wangu nitampenda, Wala dhambi sitatenda, Jina lako nasifia, Utakalo hutimia, Kwa utii navumilia, Teso na matata pia, Nipe Bwana neema zako, Niongezee sifa yako, Amina.

Majitoleo

Ee Yesu, kupitia mikono safi ya Bikira Maria, na kwa maungano na sadaka yako kuu, ninakutolea sala, matendo, kazi, masumbuko, na furaha zangu zote za siku hii ya leo, kwa ajili ya nia za Moyo wako Mtakatifu, Ee Yesu ufalme wako utufikie!

Baba Yetu….
Salamu Maria, …..
Nasadiki …….
Amri za Mungu ……
Amri za Kanisa ……

Sala ya Malaika wa Bwana

Malaika wa Bwana alimpasha habari Maria, naye akapata mimba kwa uwezo wa Roho Mtakatifu. Salamu Maria,….

Ndimi Mtumishi wa Bwana, nitendewe ulivyonena. Salamu Maria, ……
Neno wa Bwana akatwaa Mwili, akakaa kwetu. Salamu Maria, …..

Utuombee, ee Mzazi Mtakatifu wa Mungu, tujaliwe ahadi za Kristo.

Tuombe:

Tunakuomba ee Bwana, utie neema yako mioyoni mwetu, ili sisi tuliojua kwa maelezo ya Malaika, kwamba, Kristo Mwanao amejifanya mtu: kwa mateso na Msalaba wake, utufikishe kwenye utukufu wa ufufuko. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristo Bwana wetu, Amina.

Sala kwa Malaika Mlinzi

Ee Malaika wangu, uliyewekwa na Mungu mwema unilinde, naomba uniongoze leo, unitunze, unisimamie, unishauri. Amina.

Sala kwa wenye kuzimia

Ee Yesu mwenye huruma, mpenda roho za watu, nakuomba kwa ajili ya kuzimia kwa Moyo wako Mtakatifu, na kwa ajili ya Mama Yako asiye na doa, uwatakase kwa damu yako, watu wote wenye dhambi wanaokufa sasa, na watakaokufa leo.
Moyo wa Yesu uliozomia, uwahurumie watu wanaokufa X3.

Sala kwa Mtakatifu Yosef

Ee Yosef mwenye heri, tunakimbilia kwako, katika masumbuko yetu, na kishaomba shime ya Mchumba wako Mtakatifu, tunaomba pia kwa matumaini usimamizi wako. Kwa ajili ya mapendo uliyompenda nayo Bikira Mtakatifu, Mzazi wa Mungu, na kwa ajili ya tunza ya Baba, uliyomtunza nayo Mtoto Yesu, tunakuomba sana, utuangalie kwa wema, sisi tuliokuwa fungu lake Yesu Kristo, tuliokombolewa kwa damu yake, utusimamie katika masumbuko yetu, kwa enzi na shime yako.
Ee Mlinzi amini wa Jamaa Takatifu, uwakinge watoto wateule wa Yesu Kristo, ee Baba uliyetupenda mno, utuepusha na kilema chochote cha madanganyo na upotevu. Ee kinga yetu mwezaji,utusimamie huko juu mbinguni ulipo, tunaposhindana na wenye nguvu wakaao gizani. Kama vile siku za kale ukamwokoa Mtoto Yesu katika hatari ya kuuawa, na leo hivi, ulikinge Kanisa Takatifu la Mungu katika mitego ya adui, na katika shida yote, mtunze daima kila mmoja wetu, tupate mfano wako, tusaidie kwa msaada wako, kukaa na utakatifu maisha, kufa kifo chema, na kupokelewa mbinguni makao ya raha milele. Amina

Sala kwa Mtakatifu Yuda Thadei

(Sala hii inaweza kusaliwa kila siku au kama Novena ya siku tisa mfululizo kuomba kitu kilekile)
Mtakatifu Yuda Tadei,/ Mtume Mtakatifu,/ Mtumishi mwaminifu na rafiki wa Yesu./ Jina la yule msaliti aliyemwuza Yesu/ limewafanya wengi wakusahau./ Walakini Kanisa zima linakuheshimu/ na kukuomba kama Msaidizi katika mashaka makubwa,/ na katika mambo yasiyo na matumaini tena./
Uniombee mimi mnyonge./ Ninaomba utumie uwezo ule uliojaliwa/ wa kuleta upesi msaada kwa watu walioukosa./ Unisaidie sasa katika mahitaji yangu,/ ili nipate kitulizo na msaada wa mbinguni/ katika lazima zangu,/ masumbuko na mateso,/ hasa/ (taja shida yako)./ Pia ili niweze kumsifu Mungu nawe na wateule wote milele./
Mtakatifu Yuda Tadei,/ utuombee,/ na uwaombee watu wote wanaokuheshimu na kukuomba msaada./
Baba yetu……. Salamu Maria ……… Atukuzwe ……….

Sala ya Medali ya Mwujiza

Ee Bikira Maria uliyekingiwa dhambi ya asili, utuombee sisi wenye kukimbilia kwako, uwaombee na wale wasioukimbilia kwako, hasa maadui wa Kanisa Takatifu, na wale waliokabidhiwa kwako. Amina.

Majitoleo kwa Bikira Maria

(Sala iliyotungwa na Mtk. Aloisi)
Bibi yangu mtukufu Maria, nakuwekea amana ya roho yangu na mwili wangu, nikikuomba uipokee amana yangu, kuitunzia ulinzi mwema ulinzi bora, ninakuaminia na kila neno langu, matumaini na kitulizo na kisongo chote, na masumbuko na uzima na ukomo wa uzima wangu: nitakayo ndiyo unifanyizie kwa maombezi na stahili zako, ili mambo yangu yote yapate kuongoka, yakiwa na kufuata mapenzi yako, pamoja na mapenzi ya Mwanao. Amina.

SALA YA KUMWOMBA MT. YOSEFU MSAADA (SALA KUU KWA MTAKATIFU YOSEFU)

Ee Mt. Yosefu mwenye heri, tunakimbilia kwako katika masumbuko yetu, na kisha omba shime ya Mchumba wako Mtakatifu, tunaomba pia kwa matumaini usimamizi wako. Kwa ajili ya mapendo uliyompenda Bikira Mtakatifu Mzazi wa Mungu, na kwa ajili ya kumtunza Mtoto Yesu, twakuomba sana, utuangalie kwa wema sie tuliokuwa fungu lake Yesu Kristu, tukakombolewa kwa damu yake. Tusimamie katika masumbuko yetu kwa enzi na shime yako.

Ee Mlinzi amini wa jamaa takatifu, uwakinge watoto wateule wa Yesu Kristu.
Ee Baba uliyetupenda mno tuepushe na kilema chochote cha madanganyo na upotevu. Ee kinga yetu mwezaji, utusimamie huko juu mbinguni ulipo, tunaposhindana na wenye nguvu wakaao gizani. Kama vile siku za kale ukamwopoa Mtoto Yesu katika hatari ya kuuawa, na leo hivi likinge Kanisa Takatifu la Mungu katika mitego ya adui, na katika shida yote; mtunze daima kila mmoja wetu, tufwate mfano wako, ili tupate na msaada wako, kukaa na utakatifu maisha, kufa kifo chema, na kupata mbinguni makao ya raha milele.
Amina.

ROZARI YA MOYO MTAKATIFU WA YESU

Tumia tasbihi ya kawaida yenye chembe ndogo 53.

Kwenye Msalaba Sali:

“Ee Yesu tupe moyo wako kama amana ya upendo wako na kimbilio letu, ili tupate pumziko salama wakati wa maisha yetu na faraja tamu saa ya kufa kwetu”.
Baba Yetu ……..
Salamu Maria ……. (mara tatu)
Nasadiki ………..

Kwenye chembe kubwa Sali (Badala ya ‘Baba Yetu’):

“Ninakuabudu, ninakutukuza na ninakupenda, Ee Moyo wa Yesu wangu mpenzi, uliopenywa na huzuni nyingi kwa ajili ya dhambi, ambazo zimekuwa zikitendwa hata leo, dhidi ya Sakramenti Takatifu sana ya Altare. Ninakutolea hapo kwa kuridhika, moyo wa Mama yako mpendevu, na mastahili ya watakatifu. Amina”.

Kwenye chembe ndogo sali (Badala ya ‘Salamu Maria’):

“Ee Moyo Mtakatifu wa Yesu, uwakao mapendo kwetu, washa nyoyo zetu kwa mapendo yako”

Sala ya Kuombea Hali njema ya hewa na mvua

Ee Mungu Mwenyezi wa milele, mpaji wa mema yote, unayetusamehe na kutulinda. Utujalie sisi tunaokusihi, tufurahie hali njema ya hewa na mvua tunayoitamani na kuhitaji. Tutumie daima vipawa vya wema wako kwa ajili ya utukufu wa jina lako, na kwa ajili ya wokovu watu. Tunaomba hayo kwa njia ya Bwana watu Yesu Kristo Mwanao, anayeishi na kutawala nawe katika umoja wa Roho Mtakatifu, Mungu, daima na milele. Amina. `

`Baba Yetu………………. Salama Maria………… Atukuzwe Baba……….. `

K: `Bikra Maria mama wa msaada wa daima…. W: Utuombee na Utusaidie`

Malkia wa Mbingu

Malkia wa mbingu, furahi, aleluya. Kwani uliyestahili kumchukua, Aleluya. Amefufuka alivyosema, Aleluya. Utuombee kwa Mungu, Aleluya. Furahi shangilia, ee Bikira Maria, Alaluya. Kwani hakika Bwana amefufuka Aleluya. Tuombe. Ee Mungu, uliyependa kuifurahisha dunia kwa kufufuka kwake Bwana wetu Yesu Kristu, Mwanao: fanyiza, twakuomba, kwa ajili ya Bikira Maria, tupate nasi furaha za uzima wa milele. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristu Bwana wetu. Amina.

Rozari ya Malaika Mkuu Mikaeli

Rozari ya Malaika Mkuu Mikaeli ni sala nzuri sana ya kumheshimu huyu Malaika Mkuu pamoja na makundi yote tisa ya Malaika. Kuendana na jinsi tunavyofunuliwa katika Maandiko Matakatifu, makundi haya tofauti tofauti ya Malaika hujipanga kuanzia karibu sana na Kiti cha Enzi alipo Mwenyezi Mungu, kwenda chini tulipo sisi wanadamu. Makundi hayo kuanzia juu kwenda chini ni Maserafi, Makerubi, Wenye Enzi, Watawala, Wenye Nguvu, Wenye Mamlaka, Wakuu, Malaika Wakuu na Malaika.

Asili ya Rozari hii ni maono aliyopata Mtumishi wa Mungu Antonia d’Astonac, ambaye alitokewa na Malaika Mkuu Mikaeli aliyemfundisha sala za Rozari hii kwa kumwelekeza kuwa anataka aheshimiwe kwa salamu tisa kufuatana na makundi tisa ya Malaika.

Mtakatifu Mikaeli Malaika Mkuu aliahidi kuwa yeyote anayefanya ibada hii kwa heshima, akaribiapo Meza Takatifu, atasindikizwa na Malaika tisa, mmoja kutoka kila kundi la Malaika. Zaidi ya hayo, kwa kusali rozari hii, aliahidi msaada wa daima, na kwamba Malaika watamsaidia mwenye kuisali duniani na kumtoa toharani akifariki, yeye pamoja na jamaa zake.

ROZARI YA MALAIKA MKUU MIKAELI

Ee Mungu unielekezee msaada, Ee Bwana unisaidie hima!
Atukuzwe Baba na Mwana na Roho Mtakatifu, kama mwanzo na sasa na siku zote, na milele. Amina.

Sali Baba Yetu (mara nne) kwa heshima ya Malaika Wakuu, Mtakatifu Mikaeli, Mtakatifu Gabriel, Mtakatifu Rafaeli na Malaika Mlinzi.

1. Kwa heshima ya Malaika Mkuu Mtakatifu Mikaeli; Baba Yetu uliye mbinguni, Jina lako litukuzwe, ufalme wako ufike, utakalo lifanyike duniani kama mbinguni, utupe leo mkate wetu wa kila siku, utusamehe makosa yetu, kama tunavyowasamehe na sisi waliotukosea. Usitutie katika kishawishi, lakini utuopoe maovuni. Amina
2. Kwa heshima ya Malaika Mkuu Mtakatifu Gabrieli; Baba Yetu, …..
3. Kwa heshima ya Malaika Mkuu Mtakatifu Rafaeli; Baba Yetu, …..
4. Kwa heshima ya Malaika Wangu Mlinzi; Baba Yetu, ……

Sali Baba Yetu moja na Salamu Maria tatu baada ya kila salamu katika tisa zifuatazo kwa heshima ya Makundi Tisa ya Malaika

Baba Yetu (mara moja, – tazama hapo juu)

Salamu Maria
Salamu Maria umejaa neema, Bwana yu nawe, umebarikiwa kuliko wanawake wote, na Yesu Mzao wa tumbo lako amebarikiwa. Maria Mtakatifu, Mama wa Mungu, utuombee sisi wakosefu, sasa na saa ya kufa kwetu, Amina.

1. Kwa maombezi ya Mtakatifu Mikaeli na ya kundi la Serafin, Bwana awashe mioyoni mwetu moto wa mapendo kamili. Amina.
Baba Yetu (mara moja), Salamu Maria (mara tatu)

2. Kwa maombezi ya Mtakatifu Mikaeli na ya Kundi la Kerubin, Bwana atuwezeshe kuacha njia mbaya na kuenenda katika njia ya ukamilifu wa kiKristo. Amina.
Baba Yetu (mara moja), Salamu Maria (mara tatu)

3. Kwa maombezi ya Mtakatifu Mikaeli na ya Kundi la Wenye Enzi, Bwana atujalie roho ya unyofu na unyenyekevu wa kweli. Amina
Baba Yetu (mara moja), Salamu Maria (mara tatu)

4. Kwa maombezi ya Mtakatifu Mikaeli na ya Kundi la Watawala, Bwana atujalie neema ya kushinda maasi yetu na tamaa mbaya. Amina
Baba Yetu (mara moja), Salamu Maria (mara tatu)

5. Kwa maombezi ya Mtakatifu Mikaeli na ya Kundi la Wenye Nguvu, Bwana atukinge na vishawishi na mitego ya shetani. Amina
Baba Yetu (mara moja), Salamu Maria (mara tatu)

6. Kwa maombezi ya Mtakatifu Mikaeli na ya Kundi la Wenye Mamlaka, Bwana atukinge na mwovu wala tusianguke vishawishini. Amina
Baba Yetu (mara moja), Salamu Maria (mara tatu)

7. Kwa maombezi ya Mtakatifu Mikaeli na ya Kundi la Wakuu, Bwana atujalie kuwa na roho ya utii wa kweli. Amina
Baba Yetu (mara moja), Salamu Maria (mara tatu)

8. Kwa maombezi ya Mtakatifu Mikaeli na ya Kundi la Malaika Wakuu, Bwana atudumishe katika imani na katika kazi zote njema ili tujaliwe utukufu wa Milele. Amina.
Baba Yetu (mara moja), Salamu Maria (mara tatu)

9. Kwa maombezi ya Mtakatifu Mikaeli na ya Kundi la Malaika, Bwana atujalie ulinzi wao duniani hapa na baadaye watuongoze kwenye furaha za Mbinguni. Amina.
Baba Yetu (mara moja), Salamu Maria (mara tatu)

SALA MBELE YA KITI CHA ENZI CHA MUNGU

Sali Atukuzwe 7 kwa heshima ya Malaika 7 wateule ujipatie neema ya kuepa dhambi mbaya saba na kutujaza mapaji saba ya Roho Mtakatifu.

TUOMBE
Ee Mungu Mwenyezi wa milele, kwa wema na huruma yako ya ajabu, umetaka watu wako waokoke, ukamweka Malaika Mkuu Mikaeli kuwa Mkuu wa Kanisa lako, Utukinge na adui zetu, wasitusmbue saa ya kufa kwetu, bali tuongozwe naye kwenye utukufu wako Mkuu. Tunaomba hayo kwa njia ya Bwana Wetu Yesu Kristo. Amina.

Utuombee Ee Mtukufu Mtakatifu Mikaeli Mkuu wa Kanisa la Yesu Kristo, tujaliwe ahadi za Kristo. Amina.

SALA KWA MTAKATIFU MIKAELI MALAIKA MKUU

Mtakatifu Mikaeli Malaika Mkuu, utulinde katika vita, uwe kinga yetu katika maovu na maoteo ya shetani, Mungu amtiishe, tunaomba sana, nawe Mkuu wa Majeshi ya Mbinguni kwa nguvu ya Mungu uwaangushe motoni shetani na pepo wabaya wengine wote, wanaozunguka duniani, ili kuzipoteza roho za watu.
Amina.

SALA KWA MALAIKA WAKO MLINZI

Malaika wa Mungu Mlinzi wangu mpenzi,
Ambaye upendo wake unanifanya niwepo hapa,
Uwe nami leo hii,
Kuniangaza na kunilinda,
Kunitawala na kuniongoza.
Amina.

SALA NYINGINE KWA MALAIKA WAKO MLINZI

Ee Malaika wangu Mlinzi, uliyewekwa na Mungu Mwema, naomba unilinde katika hatari zote za roho na za mwili. Amina

Sali mara kwa mara unapokumbuka, hasa asubuhi uamkapo na usiku kabla ya kulala, Atukuzwe mara saba, kwa heshima ya Malaika wako Mlinzi.

SALA YA MAOMBI KWA MOYO MTAKATIFU WA YESU

Ee Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakukimbilia, ninakuja kwako katika mikono yako yenye huruma. Ndiwe tegemeo langu na tumaini langu dhabiti. Ndiwe mwenye dawa ya maovu yangu yote, malipizi ya makosa yangu yote. Waweza kunipatia haja zangu na neema ninazoziomba mimi na wengine. Wewe uko ili kutusaidia sote, ndiwe mwanga mkuu usiozimika, ndiwe chanzo cha nguvu, uvumilivu, amani na faraja. Nina hakika kuwa maombi yangu hayatakuchosha, nawe hutaacha kunisaidia, kunilinda, kunipenda, kwani, ee Moyo Mtakatifu , upendo wako hauna mwisho. Ee Moyo Mtakatifu, unihurumie, kwa ajili ya maombi yangu, kadiri ya huruma yako. Nawe katika sisi, na kwa ajili yetu, ufanye lolote unalolihitaji, kwani tunajitoa kwako kwa imani na uhakika thabiti kwamba kamwe hautatuacha, kwa milele. Amina.

Sala kwa Mtakatifu Yosefu

Ee Yosef mwenye heri, tunakimbilia kwako, katika masumbuko yetu, na kishaomba shime ya Mchumba wako Mtakatifu, tunaomba pia kwa matumaini usimamizi wako. Kwa ajili ya mapendo uliyompenda nayo Bikira Mtakatifu, Mzazi wa Mungu, na kwa ajili ya tunza ya Baba, uliyomtunza nayo Mtoto Yesu, tunakuomba sana, utuangalie kwa wema, sisi tuliokuwa fungu lake Yesu Kristo, tuliokombolewa kwa damu yake, utusimamie katika masumbuko yetu, kwa enzi na shime yako.
Ee Mlinzi amini wa Jamaa Takatifu, uwakinge watoto wateule wa Yesu Kristo, ee Baba uliyetupenda mno, utuepusha na kilema chochote cha madanganyo na upotevu. Ee kinga yetu mwezaji,utusimamie huko juu mbinguni ulipo, tunaposhindana na wenye nguvu wakaao gizani. Kama vile siku za kale ukamwokoa Mtoto Yesu katika hatari ya kuuawa, na leo hivi, ulikinge Kanisa Takatifu la Mungu katika mitego ya adui, na katika shida yote, mtunze daima kila mmoja wetu, tupate mfano wako, tusaidie kwa msaada wako, kukaa na utakatifu maisha, kufa kifo chema, na kupokelewa mbinguni makao ya raha milele. Amina

Sala ya Malaika wa Bwana

Malaika wa Bwana alimpasha habari Maria, naye akapata mimba kwa uwezo wa Roho Mtakatifu. Salamu Maria,….

Ndimi Mtumishi wa Bwana, nitendewe ulivyonena. Salamu Maria, ……
Neno wa Bwana akatwaa Mwili, akakaa kwetu. Salamu Maria, …..

Utuombee, ee Mzazi Mtakatifu wa Mungu, tujaliwe ahadi za Kristo.

Tuombe:

Tunakuomba ee Bwana, utie neema yako mioyoni mwetu, ili sisi tuliojua kwa maelezo ya Malaika, kwamba, Kristo Mwanao amejifanya mtu: kwa mateso na Msalaba wake, utufikishe kwenye utukufu wa ufufuko. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristo Bwana wetu, Amina.

SALA YA KUOMBEA FAMILIA

Ewe Mungu Mwenyezi, sisi kama familia tunakushukuru kwa zawadi ya Mama Kanisa Katoliki ambaye siku zote hutupatia malezi bora kwa ajili ya wokovu wetu. Kanisa halichoki kutuhimiza tutafakari na kuishi utakatifu wa familia ya Nazareti ya Yesu, Maria na Yosefu. Familia hii iliishi upendo uliojengwa kwa fadhila za imani, uaminifu, utii, uvumilivu na upole hata wakawa watakatifu. Tunapoadhimisha mwaka wa Familia, tunaiweka mbele yetu familia ya Nazareti iwe dira, baraka na mfano kwa familia zetu.

Tunakushukuru Baba kwa ajili ya familia zote zinazojitahidi kuishi fadhila hizo za Familia takatifu na tunakuomba uzidi kuwaimarisha wanandoa ili tupate kwao mifano mingi na bora ya kuigwa. Ee Bwana, tunaomba Roho Mtakatifu atuangazie tuweze: kutambua familia kuwa Kanisa la nyumbani na shule ya imani na upendo; kuimarisha familia kwa sala, sakramenti na tunu za kiinjili na kushirikiana kwa heshima katika familia kwa usitawi wa roho na wa mwili kwa wanafamilia wote.

Tunaziombea familia zetu na Jumuiya Ndogondogo za Kikristo ziwe bustani bora na salama za kuchipusha na kulea miito mitakatifu ya Ndoa, Utawa na Upadre. Tunawaombea vijana na watoto wetu Uchaji wa Mungu ili wawe na bidii ya kujitunza kwa kushika amri za Mungu na kuishi fadhila za kiinjili, wawe na roho ya kimisionari yaani walipende Kanisa na kuwa na moyo wa kueneza ufalme wako kwa matendo ya imani. Baba wa huruma, tunakukabidhi familia zenye misukosuko ya mafarakano, ulevi, ubinafsi, uregevu-dini, uvivu, ushirikina, hofu, magonjwa sugu na mengineyo yenye kuleta huzuni; kwa hisani yako uwape neema, mwanga na nguvu za kuanza maisha mapya yenye amani, waweze kufurahia upatanisho na uponyi wa pendo lako la kibaba kati yao.

Tunaomba toba na msamaha kwa ukatili, manyanyaso na hata mauaji katika familia zetu na uwaponye wote waliojeruhiwa kwa maneno, matendo na makwazo ya aina yeyote. Aidha tunakuomba uwe kitulizo na faraja kwa wagonjwa na wazee, pia tegemeo la yatima na wajane. Wenye matatizo ya kiafya au ya kijamii wasikate tamaa bali waunganishe hali zao na msalaba wa Mwanao na kukutumaini wewe Mweza yote. Jamii iwajibike nao kwa kuzijali haki zao na kuwapa misaada wanayohitaji.

Tunakuomba ubariki miradi na kazi zetu ili familia zipate usitawi na maendeleo; na utujalie hekima ya kukushukuru kwa maisha ya haki, amani na ukarimu na mwisho tukaimbe sifa zako pamoja na familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefuna jeshi lote la mbinguni. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristo Bwana wetu. Amina.

Baba yetu… …..Salamu Maria….…Atukuzwe Baba………

LITANIA YA KUWAOMBEA MAPADRE WOTE 1

Kwa ajili ya Baba Mtakatifu wetu ..(N); Bwana, umpe moyo wako wa uchungaji mwema
Kwa ajili ya warithi wa Mitume; Bwana, uwape wawe na uangalifu uliojaa upendo kwa mapadre wao
Kwa ajili ya Maaskofu wako waliochaguliwa na Roho Mtakatifu; Bwana, uwabakishe karibu na kondoo wako
Kwa ajili ya wachungaji wako; Bwana, uwafundishe kutumikia kuliko kutafuta kutumikiwa
Kwa ajili ya waungamishi na washauri wa kiroho; Bwana, uwafanye kuwa vyombo visikivu kwa Roho wako Mtakatifu
Kwa ajili ya mapadre wanaotangaza neno lako; Bwana, uwawezeshe kushirikisha Roho wako na Uzima wako
Kwa ajili ya mapadre wanaosaidia utume wa walei; Bwana, uwatie moyo wa kuwa mifano bora
Kwa ajili ya mapadre wanaofanya kazi na vijana; Bwana, uwajalie wawakabidhi vijana kwako
Kwa ajili ya mapadre wanaofanya kazi kati ya watu fukara; Bwana, uwajalie wakuone na wakutumikie kupitia hao
Kwa ajili ya mapadre wanaoangalia wagonjwa; Bwana, uwajalie wawafundishe thamani ya mateso
Kwa ajili ya mapadre fukara; – Uwasaidie ee Bwana
Kwa ajili ya mapade wagonjwa; – Uwaponye ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wazee; – Uwapatie tumaini la raha ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wenye huzuni na walioumizwa; -Uwafariji ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wanaohangaishwa na wale wanaosumbuliwa; – Uwape amani yako ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wanaodharauliwa na wanaonyanyaswa; – Uwatetee ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre waliokata tamaa; – Uwatie moyo ee Bwana
Kwa ajili ya wale wanaosomea upadre; – Uwape udumifu ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wote; – Uwape uaminifu kwako na kwa Kanisa lako ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wote; – Uwajalie utii na upendo kwa Baba Mtakatifu na kwa maaskofu wao ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wote; – Uwajalie waishi katika umoja na maaskofu wao ee Bwana
Tunawaombea mapadre wote; – Wawe wamoja kama Wewe na Baba mlivyo wamoja ee Bwana
Tunawaombea mapadre wote; – Waishi na kuendeleza haki yako ee Bwana
Tunawaombea mapadre wote; – Washirikiane katika umoja wa ukuhani wako ee Bwana
Tunawaombea mapadre wote, wakiwa wamejawa na uwepo wako; – Waishi maisha yao ya useja kwa furaha ee Bwana
Tunawaombea mapadre wote; – Wajalie ukamilifu wa Roho wako na uwageuze wafanane nawe ee Bwana
Kwa namna ya pekee, ninawaombea mapadre wale ambao kwa njia yao nimepokea neema zako. Ninamwombea padre aliyenibatiza na wale walioniondolea dhambi zangu, wakinipatanisha na Wewe na Kanisa lako.
Ninawaombea mapadre ambao nimeshiriki Misa walizoadhimisha, na walionipa Mwili wako kama chakula. Ninawaombea mapadre walionishirikisha Neno lako, na wale walionisaidia na kuniongoza kwako. Amina.

Shopping Cart
48
    48
    Your Cart
    Kitabu cha SMS Maalumu kwa Umpendaye
    Kitabu cha SMS Maalumu kwa Umpendaye
    1 X Sh2,500 = Sh2,500
    🏠 Home 📖 Reading 🖼️ Gallery 💬 AI Chat 📘 About