Sala za Katoliki: Sala Muhimu Kwa Mkristu Mkatoliki

LITANIA YA KUWAOMBEA MAPADRE WOTE II

Kwa ajili ya Baba Mtakatifu wetu ..(N); Bwana, umpe moyo wako wa uchungaji mwema
Kwa ajili ya makardinali na maaskofu wakuu; Uwape moyo wa kichungaji ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wa majimbo; Uwajaze na Roho wako ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre watawa; Wakamilishe katika wito wao ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre walioko hatarini; Uwaokoe ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wenye udhaifu; Uwatie nguvu ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wenye hofu; Uwape amani ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre waliokata tamaa; Uwavuvie upya ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wakaao upweke; Uwasindikize ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wamisionari; Uwalinde ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wanaohubiri; Uwaangazie ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre na watawa waliokufa; Uwafikishe kwenye utukufu wako ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wote; Wajalie hekima na ufahamu wako ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wote; Uwajalie elimu na shauri lako
Kwa ajili ya mapadre wako; wajalie wakuheshimu na wakuogope
Kwa ajili ya mapadre wote; Wajalie subira na upendo
Kwa ajili ya mapadre wote; wajalie utii na upole
Kwa ajili ya mapadre wote; uwajalie hamu kuu ya kuokoa roho za watu
Kwa ajili ya mapadre wote; wape fadhila za imani, matumaini na mapendo
Kwa ajili ya mapadre wote; Wajalie upendo mkuu kwa Ekaristi
Tunakuomba uwajalie mapadre wote; Waheshimu uhai na hadhi ya mtu ee Bwana
Tunakuomba uwajalie mapadre wote nguvu na bidii katika kazi zao ee Bwana
Tunakuomba uwajalie mapadre wote amani katika mahangaiko yao ee Bwana
Tunakuomba uwajalie mapadre wote upendo mkuu kwa Utatu Mtakatifu ee Bwana
Tunakuomba uwajalie mapadre wote upendo mkuu kwa Bikira Maria ee Bwana
Uwajalie mapadre wote wawe mwanga wa Kristo ee Bwana
Uwajalie mapadre wote, wawe chumvi kwa ulimwengu ee Bwana
Uwajalie mapadre wote, wajizoeze kujitoa sadaka na kujinyima ee Bwana
Uwajalie mapadre wote, wawe watakatifu kimwili, kiakili na kiroho ee Bwana
Uwajalie mapadre wote wawe watu wa sala ee Bwana
Uwajalie mapadre wote wawe kioo cha imani kwako ee Bwana
Uwajalie mapadre wote wajali sana wongofu wetu ee Bwana
Uwajalie mapadre wote wawe waaminifu kwa wito wao wa kikuhani ee Bwana
Uwajalie mapadre wote, ili mikono yao ibariki na kuponya ee Bwana
Uwajalie mapadre wote wawake moto wa mapendo yako ee Bwana
Uwajalie mapadre wote hatua zao zote ziwe kwa ajili ya utukufu wa Mungu ee Bwana
Uwajalie mapadre wote wajazwe na Roho Mtakatifu na uwajalie karama zake kwa wingi ee Bwana.

Tuombe.
Baba, Mwana na Roho Mtakatifu, usikie sala tunazokutolea kwa ajili ya mapadre wetu. Uwajalie wafahamu waziwazi kazi uliyowaitia kuifanya, uwape neema zote wanazohitaji ili waitikie wito wako kwa ushujaa, kwa upendo, na majitoleo yenye udumifu katika mapenzi yako matakatifu. Amina.

SALA KWA MTAKATIFU YUDA TADEI

Mtakatifu Yuda Tadei,/ Mtume Mtakatifu,/ mtumishi mwaminifu na rafiki wa Yesu./ Jina la yule msaliti aliyemwuza Yesu/ limewafanya wengi wakusahau./ Walakini Kanisa zima linakuheshimu/ na kukuomba kama Msaidizi katika mashaka makubwa,/ na katika mambo yasiyo na matumaini tena./

Uniombee mimi mnyonge./ Ninaomba utumie uwezo ule uliojaliwa/ wa kuleta upesi msaada kwa watu walioukosa./ Unisaidie sasa katika mahitaji yangu,/ ili nipate kitulizo na msaada wa mbinguni/ katika lazima zangu,/ masumbuko na mateso,/ hasa/ (taja shida yako)./ Pia ili niweze kumsifu Mungu nawe na wateule wote milele./

Mtakatifu Yuda Tadei,/ utuombee,/ na uwaombee watu wote wanaokuheshimu na kukuomba msaada./

Moyo Mtakatifu wa Yesu,/ Rafiki mpenzi wa Yuda Tadei,/ nakutumainia./

(Mwisho Sali: Baba yetu (x3), Salamu Maria (x3) na Atukuzwe(x3).

SALA YA KUWAOMBEA MAPADRE

Ee Bwana Yesu Kristo. Mkombozi wetu, kwa mapendo na tamaa yako ya kutaka kulinda vema Kanisa lako, ukachagua Mapadri wawe Wachungaji na Viongozi wa roho za watu. Nakuomba sana; ubariki nia na bidii inayowapasa Mapadri wote katika kazi zao. Uwaongezee Utakatifu.

Uwatie moyo mzuri wenye mapendo makubwa kwako na roho za watu. Hivyo wakiisha kupata wenyewe Utakatifu, waweze kuwaongoza vizuri watu walio chini ya ulinzi wao, katika njia ya Utakatifu na furaha ya milele. Uwajalie neema zote za hali ya Upadri. Uwajalie ili waonyeshe kila siku ya maisha yao mfano wa kila fadhila ya mapendo na ya uaminifu katika Kanisa, kwa Baba Mtakatifu na kwa Maaskofu.

Yesu mpendelevu, uangalie kwa mapendo kazi na mateso ya Mapadri wako; ubariki na ustawishe mafundisho yao; wanapowafundisha watoto, wanapowahubiria watu, wanapowatuliza wakosefu watubu na wanapowasaidia wagonjwa na wale wanaokaribia mauti, Ee Yesu uwe pamoja nao. Uwakinge na hatari zote za roho na za mwili.

Mwokozi Yesu, ulijalie Kanisa liwe na Mapadri wengi walio Watakatifu. Uwajalie watoto na vijana wengi wasikie wito wa Upadri, uwatie furaha na Utakatifu na roho za Mapadri waliokufa uzijalie punziko la amani.

Kwa mimi mwenyewe Ee Yesu mpendelevu, naomba unijalie roho ya imani na utii mnyenyekevu ili niwaheshimu Mapadri kama Mawakili wa Mungu. Niwatii katika njia zote za wokovu wa roho yangu. Amina.

Matendo ya Rozari Takatifu: Mchanganuo kwa siku zote za Saba za Juma

MATENDO YA FURAHA (Jumatatu na Jumamosi)

  1. Tendo la kwanza; Malaika Gabrieli anampasha habari Maria kuwa atakuwa Mama wa Mungu. Tumwombe Mungu atujalie unyenyekevu.
  2. Tendo la pili; Maria Mtakatifu anakwenda kumtembelea Elizabeti. Tumwombe Mungu atujalie mapendo ya jirani.
  3. Tendo la tatu; Yesu anazaliwa Betlehemu. Tumwombe Mungu atujalie moyo wa ufukara
  4. Tendo la nne; Yesu anatolewa hekaluni. Tumwombe Mungu atujalie usafi wa moyo.
  5. Tendo la tano; Maria anamkuta Yesu hekaluni. Tumwombe Mungu atujalie kuwatii wakubwa wetu.

MATENDO YA UCHUNGU (Jumanne na Ijumaa)

  1. Tendo la kwanza; Yesu anatoka jasho la damu kwa ajili yetu. Tumwombe Mungu atujalie sikitiko la dhambi.
  2. Tendo la pili; Yesu anapigwa kwa mijeledi kwa ajili yetu. Tumwombe Mungu atujalie kuacha dhambi za uchafu.
  3. Tendo la tatu; Yesu anatiwa miiba kichwani kwa ajili yetu. Tumwombe Mungu atujalie kushinda kiburi.
  4. Tendo la nne; Yesu anachukua Msalaba kwa ajili yetu. Tumwombe Mungu atujalie kuvumilia taabu.
  5. Tendo la tano; Yesu anakufa Msalabani. Tumwombe Mungu atujalie kuwapenda Yesu na Maria.

MATENDO YA UTUKUFU (Jumatano na Jumapili)

  1. Tendo la kwanza; Yesu anafufuka. Tumwombe Mungu atujalie kugeuka watakatifu.
  2. Tendo la pili; Yesu anapaa mbinguni. Tumwombe Mungu atujalie kwenda mbinguni.
  3. Tendo la tatu; Roho Mtakatifu anawashukia Mitume. Tumwombe Mungu atujalie bidii katika dini yetu.
  4. Tendo la nne; Bikira Maria anapalizwa mbinguni. Tumwombe Mungu atujalie kufa vizuri.
  5. Tendo la tano; Bikira Maria anawekwa Malkia mbinguni. Tumwombe Mungu atujalie kudumu katika njia njema.

MATENDO YA MWANGA (Alhamisi)

  1. Tendo la kwanza; Yesu anabatizwa Mto Jordani. Tumwombe Mungu atujalie uaminifu kwa ahadi zetu za ubatizo.
  2. Tendo la pili; Yesu anageuza maji kuwa divai huko Kana. Tumwombe Mungu atujalie kuukoleza ulimwengu kwa chachu ya enjili.
  3. Tendo la tatu; Yesu anatangaza Ufalme wa Mungu. Tumwombe Mungu atujalie kupokea Ufalme wake kwa toba ya kweli.
  4. Tendo la nne; Yesu anageuka sura. Tumwombe Mungu atujalie neema ya kuung’arisha ulimwengu kwa uso wa Yesu.
  5. Tendo la tano; Yesu anaweka Sakramenti ya Ekaristia. Tumwombe Mungu atujalie neema ya kujitoa sadaka kwa ajili ya wengine.

Karibu Vitatabu vya Kikatoliki

Majitoleo kwa Bikira Maria

(Sala iliyotungwa na Mtk. Aloisi)
Bibi yangu mtukufu Maria, nakuwekea amana ya roho yangu na mwili wangu, nikikuomba uipokee amana yangu, kuitunzia ulinzi mwema ulinzi bora, ninakuaminia na kila neno langu, matumaini na kitulizo na kisongo chote, na masumbuko na uzima na ukomo wa uzima wangu: nitakayo ndiyo unifanyizie kwa maombezi na stahili zako, ili mambo yangu yote yapate kuongoka, yakiwa na kufuata mapenzi yako, pamoja na mapenzi ya Mwanao. Amina.

NOVENA KWA AJILI YA KUJIANDAA KWA SIKUKUU YA MOYO MTAKATIFU WA YESU

Inaweza kusemwa wakati wowote katika mwaka. Kwa ajili ya kujiandaa kwa Sikukuu ya Moyo Mtakatifu wa Yesu,; anza Novena kwa Moyo Mtk wa Yesu katika Alhamisi ya Sikukuu ya Ekaristi Takatifu (Corpus Christi), yaani Alhamisi ya wiki moja kabla ya Sikukuu ya Moyo Mtk (au Alhamisi baada ya Sikukuu ya Utatu Mtk). Endapo Sikukuu hii itaadhimishwa siku ya Dominika inayofuata Sikukuu yenyewe kama inavyofanyika mahali pengi, basi novena inatakiwa ianze Ijumaa ya baada ya Sikukuu ya Utatu Mtk ili imalizike Jumamosi kabla ya Dominika ya sikukuu hii ya Moyo Mtk kwa Yesu.

WIMBO:

YESU KRISTU TWASIFU MOYO WAKO
Yesu Kristu, twasifu Moyo wako, sisi sote, milele mali yako
Tunakupa, nyoyo zote zetu, Mukombozi, Mfalme Mungu wetu;
Tunakupa, nyoyo zote zetu, Mukombozi, Mfalme Mungu wetu!

Watu wengi, wanakaa ugenini, wazunguka, wenye ukiwa chini,
Uwatie huruma yako kuu, roho zao, uziinue juu;
Uwatie huruma yako kuu, roho zao, uziinue juu!

Uwe Mfalme, wa wale washikwao, na ushenzi, na ukaidi wao
Wapelekee ufalme wa Mungu, ni Mchunga mmoja Zizi moja tu;
Wapelekee ufalme wa Mungu, ni Mchunga mmoja Zizi moja tu!

SALA YA KUTUBU

Mungu wangu ninatubu sana, niliyokosa kwako, kwani ndiwe mwema, ndiwe mwenye kupendeza, wachukizwa na dhambi, basi sitaki kukosa tena, nitafanya kitubio, naomba neema yako nipate kurudi wkako. Amina.

ROZARI YA MOYO MTAKATIFU WA YESU

Tumia tasbihi ya kawaida yenye chembe ndogo 53.
Kwenye Msalaba Sali:

“Ee Yesu tupe moyo wako kama amana ya upendo wako na kimbilio letu, ili tupate pumziko salama wakati wa maisha yetu na faraja tamu saa ya kufa kwetu”.
Baba Yetu ……..
Salamu Maria ……. (mara tatu)
Nasadiki ………..

Kwenye chembe kubwa Sali (Badala ya ‘Baba Yetu’):
“Ninakuabudu, ninakutukuza na ninakupenda, Ee Moyo wa Yesu wangu mpenzi, uliopenywa na huzuni nyingi kwa ajili ya dhambi, ambazo zimekuwa zikitendwa hata leo, dhidi ya Sakramenti Takatifu sana ya Altare. Ninakutolea hapo kwa kuridhika, moyo wa Mama yako mpendevu, na mastahili ya watakatifu. Amina”.

Kwenye chembe ndogo sali (Badala ya ‘Salamu Maria’):
“Ee Moyo Mtakatifu wa Yesu, uwakao mapendo kwetu, washa nyoyo zetu kwa mapendo yako”

LITANIA YA MOYO MTAKATIFU WA YESU

Bwana utuhurumie Bwana utuhurumie
Kristo utuhurumie Kristo utuhurumie
Bwana utuhurumie Bwana utuhurumie
Kristo utusikie Kristo utusikilize
Baba wa mbinguni Mungu Utuhurumie
Mwana, Mkombozi wa dunia Mungu Utuhurumie
Roho Mtakatifu Mungu Utuhurumie
Utatu Mtakatifu Mungu mmoja Utuhurumie
Moyo wa Yesu Mwana wa Baba wa Milele Utuhurumie
Moyo wa Yesu uliotungwa na Roho Mtakatifu mwilini mwa Mama Bikira Maria Utuhurumie
Moyo wa Yesu ulioungana na Neno wa Mungu Utuhurumie
Moyo wa Yesu ulio na utukufu pasipo mfano Utuhurumie
Moyo wa Yesu, hekalu takatifu la Mungu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, hema la Yule aliye juu Utuhurumie
Moyo wa Yesu tanuru lenye kuwaka mapendo Utuhurumie
Moyo wa Yesu, nyumba ya Mungu na mlango wa Mbingu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, tanuru yenye kuwaka mapendo Utuhurumie
Moyo wa Yesu, chombo cha haki na upendo Utuhurumie
Moyo wa Yesu, unaojaa upendo na wema Utuhurumie
Moyo wa Yesu, kilindi cha fadhila zote Utuhurumie
Moyo wa Yesu, unaostahili sifa zote Utuhurumie
Moyo wa Yesu, unaotawala mioyo yote Utuhurumie
Moyo wa Yesu, zinamokaa hazina za hekima na elimu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, uliopendelewa na Mungu Baba Utuhurumie
Moyo wa Yesu, uliotuenezea maziada yake Utuhurumie
Moyo wa Yesu, mtamaniwa wa vilima vya milele Utuhurumie
Moyo wa Yesu, wenye uvumilivu na huruma nyingi Utuhurumie
Moyo wa Yesu, tajiri kwa wote wenye kukuomba Utuhurumie
Moyo wa Yesu, chemchemi ya uzima na utakatifu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, malipo kwa dhambi zetu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, ulioshibishwa matusi Utuhurumie
Moyo wa Yesu, uliovunjika kwa sababu ya ubaya wetu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, uliotii mpaka kufa Utuhurumie
Moyo wa Yesu, uliochomwa kwa mkuki Utuhurumie
Moyo wa Yesu, chemchemi ya faraja zote Utuhurumie
Moyo wa Yesu, uzima na ufufuo wetu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, amani na upatanisho wetu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, sadaka ya wakosefu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, unamokaa wokovu wao wenye kukutumaini Utuhurumie
Moyo wa Yesu, matumaini yao wenye kuzimia kwako Utuhurumie
Moyo wa Yesu, sababu ya furaha ya watakatifu wote Utuhurumie
Mwanakondoo wa Mungu, uondoaye dhambi za dunia Utusamehe Bwana
Mwanakondoo wa Mungu, uondoaye dhambi za dunia Utusikilize Bwana
Mwanakondoo wa Mungu, uondoaye dhambi za dunia Utuhurumie

Kiongozi: Yesu mwenye Moyo mpole na mnyenyekevu,
Wote: Ufanye mioyo yetu ifanane na Moyo wako

TUOMBE: (W) Ee Mungu Mwenyezi milele, uuangalie Moyo wa mwanao mpendelevu, pia na heshima na malipo aliyokutolea kwa ajili ya wenye dhambi, uridhike, uwaondolee wenye kuomba toba kwako kwa njia ya huyo Mwanao Yesu Kristo anayeishi na kutawala nawe pamoja na Roho Mtakatifu, Mungu milele. Amina.

P.S. Mwezi wa sita ni wa kuuheshimu Moyo Mtakatifu wa Yesu. Vitu vya kufanya ni pamoja na kushiriki Misa takatifu kila siku, kumtembelea Bwana Yesu katika Ekaristia, kusali Rozari ya Moyo Mtakatifu wa Yesu kila siku, kusali Litania za Moyo Mtakatifu wa Yesu, kuimba nyimbo za kuusifu Moyo Mtakatifu wa Yesu, na kadhalika. Kwa kufanya hayo na mengineyo yanayofanana nayo, waumini hujichotea Baraka na neema nyingi za kimwili na kiroho.

SALA YA NOVENA

Ee Moyo Mtakatifu sana wa Yesu, chemchemi ya kila baraka, ninakuabudu, ninakupenda, na kwa majuto halisi ya dhambi zangu, nakutolea moyo wangu dhaifu. Nifanye mnyenyekevu, mvumilivu na safi, nikikubali na kuyatii kabisa mapenzi yako. Ee Yesu mwema, unijalie niishi nawe na kwa ajili yako. Unilinde niwapo katikati ya hatari, unifariji katika mateso, unipe afya ya mwili na msaada katika mahitaji ya mwili, Baraka yako juu ya kila nilifanyalo, na neema ya kifo chema. Amina.

Ee Yesu uliyesema “Kweli nawaambieni, ombeni nanyi mtapewa, tafuteni nanyi mtapata, gongeni nanyi mtafunguliwa”, tazama ninagonga, ninatafuta na kuomba …….. (Taja ombi lako)
Baba Yetu….., Salamu Maria …….., Atukuzwe Baba……..
Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutumainia kwa moyo wote!

Ee Yesu uliyesema “Kweli nawaambieni, chochote mtakachomwomba Baba kwa jina langu mtapewa”, tazama kwa jina lako ninaomba ……. (Taja ombi lako)
Baba Yetu….., Salamu Maria …….., Atukuzwe Baba……..
Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutumainia kwa moyo wote!

Ee Yesu uliyesema “Kweli nawaambieni, mbingu na dunia zitapita lakini maneno yangu hayatapita kamwe”, tazama, nikitiwa nguvu na maneno yako ya kweli ninaomba …….. (Taja ombi lako)
Baba Yetu….., Salamu Maria …….., Atukuzwe Baba……..
Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutumainia kwa moyo wote!

Ee Moyo Mtakatifu wa Yesu, ambaye kwako ni kitu kimoja tu kisichowezekana, ambacho ni kutoacha kutowaonea huruma wenye huzuni, utuhurumie sisi wakosefu maskini na utujalie neema tukuombayo kwa njia ya Moyo Imakulata wa Maria, Mama yetu mpole.

Sali ‘Salamu Malkia’ na kuongezea, ‘Mtakatifu Yosefu Baba Mlishi wa Yesu, utuombee’.

P.S. – Sala hii ya Novena ilisaliwa kila siku na PADRE PIO kwa ajili ya kuwaombea wale wote waliomwomba msaada wa sala zake. Unaweza kuisali kwa namna tofauti tofauti. Mfano, kama Novena ya siku tisa, ambapo unasali sala hii mara moja au zaidi kila siku kwa siku tisa, au unaweza kuifanya kama Novena ya masaa, ambapo unasali sala hii kila baada ya saa moja kwa masaa tisa kwa siku hiyo hiyo, hasa kama kitu unachokiomba ni cha haraka au umesongwa moyoni. Vilevile unaweza kuifanya sala hii kama sehemu ya sala zako za kila siku katika mwezi Juni ambao ni mwezi uliotengwa na Kanisa kwa ajili ya kuuheshimu Moyo Mtakatifu wa Yesu, na hapo utaitumia kuwaombea watu waliokuomba msaada wa sala zako kama alivyofanya Mtakatifu Padre Pio. Pia unaweza kuitumia kama sala yako ya siku zote au ya mara kwa mara kwa ajili ya mahitaji mbalimbali.

SALA YA MAOMBI

Ee Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakukimbilia, ninakuja kwako katika mikono yako yenye huruma. Ndiwe tegemeo langu na tumaini langu dhabiti. Ndiwe mwenye dawa ya maovu yangu yote, malipizi ya makosa yangu yote. Waweza kunipatia haja zangu na neema ninazoziomba mimi na wengine. Wewe uko ili kutusaidia sote, ndiwe mwanga mkuu usiozimika, ndiwe chanzo cha nguvu, uvumilivu, amani na faraja. Nina hakika kuwa maombi yangu hayatakuchosha, nawe hutaacha kunisaidia, kunilinda, kunipenda, kwani, ee Moyo Mtakatifu , upendo wako hauna mwisho. Ee Moyo Mtakatifu, unihurumie, kwa ajili ya maombi yangu, kadiri ya huruma yako. Nawe katika sisi, na kwa ajili yetu, ufanye lolote unalolihitaji, kwani tunajitoa kwako kwa imani na uhakika thabiti kwamba kamwe hautatuacha, kwa milele. Amina.

SALA KWA BIKIRA MARIA KATIKA UKIWA WAKE

Nakusikitikia sana Mama Mtakatifu Maria kwa sababu ya ukiwa wako mkuu. Uchungu wako ulikuwa mkubwa sana ulipotazama mateso na kifo cha Mwana wako mpenzi. Muda ule uliweza kutuliz kidogo kwa sababu ya kumwona angali hai. Lakini je, baada ya kufa na kumzika? Sasa wewe ni mkiwa mkubwa mno! Uh, ukiwa wa pekee, uniombee mimi ninayempoteza mara nyingi kwa dhambi zangu. Unijalie nisimpoteze tena Yesu wangu kwa ubaya wa uvivu wangu, bali nimtumikie kiaminifu duniani hapa ili nimwone na kumfurahia milele mbinguni. Amina.

ROSARI YA BIKIRA MARIA MAMA WA MSAADA WA DAIMA

Namna ya kusali Rozari kwa Bikira Maria Mama wa Msaada wa Daima

(Tumia rosari ya kawaida)

Mwanzo, kwenye Msalaba:

Kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu. Amina.

Kwenye chembe ndogo za awali:

K: Ee Mungu utuelekezee msaada W: Ee Bwana utusaidie hima
W: Atukuzwe Baba na Mwana na Roho Mtakatifu,
Kama mwanzo na sasa na siku zote na milele. Amina.

Maria ametusaidia,
Maria anataka kutusaidia,
Maria anaweza kutusaidia,
Maria atatusaidia.

KATIKA KILA FUNGU SALI SALA ZIFUATAZO:

Kwenye chembe kubwa:

Atukuzwe Baba na Mwana na Roho Mtakatifu,
Kama mwanzo na sasa, na siku zote, na milele. Amina.

Maria ametusaidia,
Maria anataka kutusaidia,
Maria anaweza kutusaidia,
Maria atatusaidia.

Ee Maria Mama wa Msaada wa daima
Sikiliza maombi ya roho zetu
Unaweza kutusaidia katika mahitaji yetu
Ee Maria kwa matumaini twakuita wewe.

Kwenye chembe ndogo:

Kama unasali mwenyewe: “Ee Maria, utusaidie! (mara kumi)
Kama mnasali zaidi ya mmoja kwa pamoja: K; Ee Maria, W: Utusaidie. (mara kumi)

MWISHO SALI SALA ZIFUATAZO:

Salamu Maria

Salamu Maria, umejaa neema, Bwana yu nawe, umebarikiwa kuliko wanawake wote, na Yesu Mzao wa tumbo lako amebarikiwa. Maria Mtakatifu, Mama wa Mungu, utuombee sisi wakosefu, sasa, na saa ya kufa kwetu. Amina. (mara tatu)

Tunaukimbilia

Tunaukimbilia ulinzi wako, ee Mzazi Mtakatifu wa Mungu, usitunyime tukiomba katika shida zetu, utuokoe siku zote, kila tuingiapo hatarini, ee Bikira Mtukufu na mwenye baraka,. Amina.

SALA YA MAOMBI KWA MOYO MTAKATIFU WA YESU

Ee Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakukimbilia, ninakuja kwako katika mikono yako yenye huruma. Ndiwe tegemeo langu na tumaini langu dhabiti. Ndiwe mwenye dawa ya maovu yangu yote, malipizi ya makosa yangu yote. Waweza kunipatia haja zangu na neema ninazoziomba mimi na wengine. Wewe uko ili kutusaidia sote, ndiwe mwanga mkuu usiozimika, ndiwe chanzo cha nguvu, uvumilivu, amani na faraja. Nina hakika kuwa maombi yangu hayatakuchosha, nawe hutaacha kunisaidia, kunilinda, kunipenda, kwani, ee Moyo Mtakatifu , upendo wako hauna mwisho. Ee Moyo Mtakatifu, unihurumie, kwa ajili ya maombi yangu, kadiri ya huruma yako. Nawe katika sisi, na kwa ajili yetu, ufanye lolote unalolihitaji, kwani tunajitoa kwako kwa imani na uhakika thabiti kwamba kamwe hautatuacha, kwa milele. Amina.

ROZARI YA MOYO MTAKATIFU WA YESU

Tumia tasbihi ya kawaida yenye chembe ndogo 53.

Kwenye Msalaba Sali:

“Ee Yesu tupe moyo wako kama amana ya upendo wako na kimbilio letu, ili tupate pumziko salama wakati wa maisha yetu na faraja tamu saa ya kufa kwetu”.
Baba Yetu ……..
Salamu Maria ……. (mara tatu)
Nasadiki ………..

Kwenye chembe kubwa Sali (Badala ya ‘Baba Yetu’):

“Ninakuabudu, ninakutukuza na ninakupenda, Ee Moyo wa Yesu wangu mpenzi, uliopenywa na huzuni nyingi kwa ajili ya dhambi, ambazo zimekuwa zikitendwa hata leo, dhidi ya Sakramenti Takatifu sana ya Altare. Ninakutolea hapo kwa kuridhika, moyo wa Mama yako mpendevu, na mastahili ya watakatifu. Amina”.

Kwenye chembe ndogo sali (Badala ya ‘Salamu Maria’):

“Ee Moyo Mtakatifu wa Yesu, uwakao mapendo kwetu, washa nyoyo zetu kwa mapendo yako”

Sala ya Saa Tisa

✝⌚✝

Sala ya saa tisa🙏🏾

Kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu. A mina

Yesu, ulikufa, lakini chanzo cha uhai kilitoka kwa ajili ya watu, na bahari ya huruma ilifunguka kwa ajili ya ulimwengu mzima. Ee chemchemi ya Uhai, huruma ya Mungu isiyo na mwisho, ikafunika ulimwengu mzima na ukajimwaga mwenyewe juu yetu.

❣✝❣

✝Ee Damu na Maji, yaliyotoka moyoni mwa Yesu kama chemchemi ya Huruma kwetu. Nakutumainia.

(Mara tatu)

🛐❣🛐

SALA YA JIONI

TUNAKUSHUKURU, EE MUNGU KWA MAPAJI YOTE ULIYOTUJALIA LEO AMINA

BABA YETU……………….. SALAMU MARIA……………….

SALA YA IMANI…….YA MATUMAINI………YA MAPENDO

SALA YA KUTUBU

TUWAZE KATIKA MOYO WETU MAKOSA YA LEO TULIYOMKOSEA MUNGU KWA MAWAZO,KWA MANENO, KWA VITENDO NA KWA KUTOTIMIZA WAJIBU (HUSUBIRI KIDOGO)
NAKUUNGAMIA MUNGU MWENYEZI,NANYI NDUGU ZANGU,KWANI NIMEKOSA MNO KWA MAWAZO,KWA MANENO,KWA VITENDO NA KWA KUTOTIMIZA WAJIBU,NIMEKOSA MIMI,NIMEKOSA SANA.NDIYO MAANA NAKUOMBA MARIA MWENYE HERI,BIKIRA DAIMA,MALAIKA NA WATAKATIFU WOTE,NANYI NDUGU ZANGU,MNIOMBEENI KWA BWANA MUNGU WETU.

MUMNU MWENYEZI ATUHURUMIE ATUSAMEHE DHAMBI ZETU,ATUFIKISHE KWENYE UZIMA WA MILELE.AMINA

SALA YA KUOMBEA WATU……………………
KUSIFU……………………

SALA KWA MT. YOSEFU KWA AJILI YA KULIOMBEA KANISA LA MAHUJAJI

Ee Mtukufu Mt. Yosefu, ulichaguliwa na Mungu kuwa Baba Mlishi wa Yesu, mchumba safi kabisa wa Maria Bikira Milele, na mkubwa wa Familia Takatifu. Umechaguliwa na Mwakilishi wa Kristu kama Msimamizi wa kimbingu na mlinzi wa Kanisa alilolianzisha Kristu. Ndiyo maana ninakuomba kwa matumaini makuu usaidizi wako wenye nguvu kwa ajili ya Kanisa zima duniani.

Mlinde kwa namna ya pekee, kwa upendo wa kikweli wa ki-baba, Baba Mtakatifu na Maaskofu wote na Mapadre wenye ushirika na Kiti cha Petro. Uwe mlinzi wao wote wanaotumikia wokovu wa wanadamu kati ya majaribu na mahangaiko ya maisha haya, na utujalie kwamba watu wote wa dunia hii wamfuate Kristu na Kanisa alilolianzisha.

Mpendwa Mtakatifu Yosefu, ukubali majitoleo ya nafsi yangu ambayo sasa ninafanya. Ninajiweka wakfu kwako kwa ajili ya utumishi wako, ili daima wewe uwe baba yangu, mlinzi wangu, na kiongozi wangu katika njia ya wokovu. Unijalie usafi mkuu wa moyo na matamanio makuu ya maisha ya kiroho. Unijalie ili matendo yangu yote, kwa mfano wako, yawe kwa ajili ya sifa na utukufu wa Mungu, pamoja na Moyo wa kimungu wa Yesu, moyo safi wa Maria, na moyo wako wa ki-baba. Uniombee, nami nishiriki kifo chako cha furaha na kitakatifu.
Amina.

SALA MBELE YA SAKRAMENTI KUU I

Utukuzwe ee Bwana wangu Yesu Kristo./ Uliagua kifo chako./ Katika karamu ya mwisho ulitumia mkate wa kidunia/ ukafanya mwujiza na kuugeuza/ kuwa Mwili wako azizi./ Kwa mapendo ukawapa Mitume Mwili huo/ uwe kumbukumbu la mateso yako mastahivu./ Uliwaosha miguu kwa Mikono yako Mitakatifu./

Uheshimiwe, ee Bwana wangu Yesu Kristo./ Kwa kuhofu mateso na kifo,/ Mwili wako usio na kosa ulitoka jasho la damu/ badala ya maji./ Juu ya hayo uliutimiza wokovu wetu/ uliokuwa umetaka kuufanya./ Hivyo ulionyesha waziwazi mapendo yako/ uliyo nayo kwa wanadamu./

Utukuzwe, ee Bwana wangu Yesu Kristo./ Ulipelekwa kwa Kayafa,/ Wewe uliye Hakimu wa wote./ Ukaruhusu kwa unyenyekevu kutolewa kwa Pilato/ uhukumiwe naye./

Utukufu uwe nawe, Bwana wangu Yesu Kristo,/ kwa kuwa ulivumilia kuchekwa tena/ uliposimama huko,/ umevaa joho jekundu,/ umetiwa taji ya miiba mikali sana Kichwani,/ ukavumilia kwa saburi kubwa/ kutemewa mate katika Uso wako mzuri,/ kufumbwa Macho,/ na kupigwa mno na wajeuri/ ngumi na makofi Mashavuni na Shingoni./

Sifa iwe nawe, Bwana wangu Yesu Kristo,/ Kwa uvumilivu mkubwa ulikubali kufungwa nguzoni,/ kupigwa mijeledi kijeuri,/ kujaa damu na hivyo kusukumwa barazani kwa Pilato./ Ulionekana kama mwanakondoo asiye na kosa./

Heshima iwe nawe, Bwana wangu Yesu Kristo./ Umehukumiwa Mwili wako mzima/ Mtukufu wenye kutoka damu/ ufe msalabani./ Ulichukua msalaba kwa Mabega yako Matakatifu/ na kuumwa sana./ Kwa ghadhabu walikusukuma mbele/ mpaka mahali pa mateso,/ wakakunyang’anya nguo zako./ Hivyo ulikubali kupigiliwa msalabani./

Heshima ya milele upate Wewe,/ Bwana wangu Yesu Kristo./ Ulipokuwa katika taabu kubwa hii,/ ulimkazia Mama yako mstahivu/ Macho yako ya hisani na mapendo/ na unyenyekevu,/ ndiye Mama yako asiyekosa hata mara moja/ wala kukubali dhambi yeyote./ Ulimweka katika ulinzi mwaminifu/ wa Mfuasi wako ili kumtuliza./

Milele utukuzwe, ee Bwana wangu Yesu Kristo./ Ulipokuwa mwenyewe taabani,/ uliwapa wakosefu wote/ matumaini ya kuondolewa dhambi/ kwa kumwahidia mnyang’anyi aliyekuendea/ utukufu wa paradisi kwa huruma yako./

Sifa ya milele iwe nawe, Bwana wangu Yesu Kristo,/ kwa kila saa ulipovumilia uchungu/ na taabu kubwa mno msalabani kwa ajili yetu sisi wakosefu,/ maumivu makali sana/ yaliyotoka katika majeraha yako,/ yakapenya bila huruma Roho yako Takatifu./ Yakaingia kikatili katika Moyo wako Mtakatifu/ hata ukakatika,/ ukapumua Roho yako,/ ukainama Kichwa,/ ukaweka Roho yako mikononi mwa Mungu, Baba yako./ Na baada ya kufa uliacha nyuma Mwili baridi./

Utukuzwe, ee Bwana wangu Yesu Kristo,/ kwa Damu yako azizi na kwa kifo chako kitakatifu/ ulizifidia roho za watu,/ ukazitoa ugenini/ na kuzipeleka kwa hisani yako katika uzima wa milele./

Milele uheshimiwe, Wewe Bwana wangu Yesu Kristo./ Siku ya tatu ulifufuka katika wafu,/ ukajionyesha kwa wafuasi wako,/ ukapaa mbinguni/ mbele ya macho yao siku ya arobaini./

Shangilio na sifa ya milele upate Wewe, Bwana wangu Yesu Kristo,/ kwa kuwa umewapelekea wafuasi wako mioyoni mwao/ Roho Mtakatifu,/ ukawasha rohoni mwao mapendo makuu ya Mungu./

Pia, utukuzwe, usifiwe na kushangiliwa milele, Bwana wangu Yesu Kristo./ Umekaa katika ufalme wako wa mbinguni/ juu ya kiti cha enzi cha Umungu wako,/ ukaishi pamoja na Viungo vyako vyote Vitakatifu./ Na hivyo utakuja tena/ kuzihukumu roho za wazima na wafu wote./ Unaishi na kutawala/ pamoja na Baba na Roho Mtakatifu,/ milele. Amina.

(Na Mt. Birgita wa Sweden)

Sala ya Kuombea Hali njema ya hewa na mvua

Ee Mungu Mwenyezi wa milele, mpaji wa mema yote, unayetusamehe na kutulinda. Utujalie sisi tunaokusihi, tufurahie hali njema ya hewa na mvua tunayoitamani na kuhitaji. Tutumie daima vipawa vya wema wako kwa ajili ya utukufu wa jina lako, na kwa ajili ya wokovu watu. Tunaomba hayo kwa njia ya Bwana watu Yesu Kristo Mwanao, anayeishi na kutawala nawe katika umoja wa Roho Mtakatifu, Mungu, daima na milele. Amina. `

`Baba Yetu………………. Salama Maria………… Atukuzwe Baba……….. `

K: `Bikra Maria mama wa msaada wa daima…. W: Utuombee na Utusaidie`

Shopping Cart
1
    1
    Your Cart
    🏠 Home 📖 Reading 🖼️ Gallery 💬 AI Chat 📘 About