Sala za Katoliki: Sala Muhimu Kwa Mkristu Mkatoliki

SALA YA KUANGUKA MIGUUNI PA BWANA YESU KATIKA EKARISTI

Ee Yesu Mfungwa wa Upendo wa Mungu,/ ninapofikiri Upendo wako na jinsi ulivyojitolea kwa ajili yangu,/ nashindwa kuelewa./ Unaficha Ukuu wako usiofahamika/ na kujidhihirisha kwa ajili yangu mimi mnyonge./ Ee Mfalme wa utukufu,/ unaficha uzuri wako,/ lakini jicho la moyo wangu/ linapenya pazia na kuona Majeshi ya Malaika/ wakikuimbia kwa heshima bila kukoma/ na nguvu zote mbinguni zikikusifu bila mwisho zikisema:/ “Mtakatifu, Mtakatifu, Mtakatifu..”/

Ni nani awezaye kufahamu Upendo wako/ na huruma yako isiyo na kipimo kwa ajili yetu!/ Ee Mfungwa wa Upendo,/ nafungia moyo wangu masikini/ kwenye Tabarnakulo hii/ ili niweze kukuabudu usiku na mchana bila mwisho./ Najua hakuna kizuizi/ na hata kama naonekana kukaa mbali,/ lakini moyo wangu u pamoja nawe/ katika ibada hii./ Hakuna kinachoweza kuzuia upendo wangu kwako./ Kwangu hakuna kizuizi chochote./

Ee Utatu Mtakatifu,/ Mungu Mmoja usiyegawanyika,/ utukuzwe kwa zawadi yako hii kuu/ na agano hili la huruma!/

Nakuabudu,/ Bwana na Muumba uliyefichika katika Sakramenti Takatifu!/ Ee Bwana,/ nakuabudu kwa kazi zote za mikono yako/ zinazonifunulia Hekima yako kuu,/ Wema wako na Huruma yako kuu./ Uzuri uliousambaza hapa/ Uzuri ulio nao Wewe mwenyewe/ ambaye U Uzuri usioelezeka;/ na ingawaje umejificha na kusitiri uzuri wako,/ jicho langu,/ kwa mwanga wa imani linafika kwako,/ na roho yangu inapata kumtambua Muumba wake/ aliye Uzuri usiopimika,/ ulio juu ya kila uzuri,/ na moyo wangu unazama kabisa katika sala ya kukuabudu./

Bwana wangu na Muumba wangu,/ wema wako wanitia moyo wa kuongea nawe,/ Huruma yako huondoa kiambaza/ kitenganishacho Muumba na kiumbe./ Furaha ya moyo wangu,/ ee Mungu, ni kuongea na Wewe./ Yote ambayo moyo wangu unayatamni nayapata kwako./ Hapa ndipo mwanga wako unaponiangaza akili yangu/ na kuiwezesha kukujua Wewe zaidi na zaidi/ – ndipo mikondo ya neema inapoutiririkia moyo wangu,/ ndipo roho yangu inapochota uzima wa milele./ Ee Bwana na Muumba wangu,/ licha ya mapaji yote haya,/ unajitoa mwenyewe kwangu,/ ili uweze kujiunganisha na kiumbe dhaifu na maskini./

Ee Kristu,/ nafurahi sana nionapo kwamba unapendwa/ na kwamba sifa na utukufu wako vinaongezwa/ hasa ya Huruma yako./ Ee Kristu,/ sitaacha kamwe kuutukuza wema wako na huruma yako,/ hadi dakika ya mwisho ya maisha yangu./ Kwa kila tone la damu yangu/ na kwa kila pigo la moyo wangu/ naitukuza Huruma yako./ Natamani kugeuzwa kabisa/ na kuwa utenzi wa utukufu wako./ Naomba siku ya kufa kwangu/ popote nitakapokuwa nimelala,/ pigo la mwisho la moyo wangu/ liwe utenzi mpendevu/ usifuo Huruma yako isiyo na kipimo./ Amina

(Na Mt. Faustina Kowalska).

ROSARI YA BIKIRA MARIA MAMA WA MSAADA WA DAIMA

Namna ya kusali Rozari kwa Bikira Maria Mama wa Msaada wa Daima

(Tumia rosari ya kawaida)

Mwanzo, kwenye Msalaba:

Kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu. Amina.

Kwenye chembe ndogo za awali:

K: Ee Mungu utuelekezee msaada W: Ee Bwana utusaidie hima
W: Atukuzwe Baba na Mwana na Roho Mtakatifu,
Kama mwanzo na sasa na siku zote na milele. Amina.

Maria ametusaidia,
Maria anataka kutusaidia,
Maria anaweza kutusaidia,
Maria atatusaidia.

KATIKA KILA FUNGU SALI SALA ZIFUATAZO:

Kwenye chembe kubwa:

Atukuzwe Baba na Mwana na Roho Mtakatifu,
Kama mwanzo na sasa, na siku zote, na milele. Amina.

Maria ametusaidia,
Maria anataka kutusaidia,
Maria anaweza kutusaidia,
Maria atatusaidia.

Ee Maria Mama wa Msaada wa daima
Sikiliza maombi ya roho zetu
Unaweza kutusaidia katika mahitaji yetu
Ee Maria kwa matumaini twakuita wewe.

Kwenye chembe ndogo:

Kama unasali mwenyewe: “Ee Maria, utusaidie! (mara kumi)
Kama mnasali zaidi ya mmoja kwa pamoja: K; Ee Maria, W: Utusaidie. (mara kumi)

MWISHO SALI SALA ZIFUATAZO:

Salamu Maria

Salamu Maria, umejaa neema, Bwana yu nawe, umebarikiwa kuliko wanawake wote, na Yesu Mzao wa tumbo lako amebarikiwa. Maria Mtakatifu, Mama wa Mungu, utuombee sisi wakosefu, sasa, na saa ya kufa kwetu. Amina. (mara tatu)

Tunaukimbilia

Tunaukimbilia ulinzi wako, ee Mzazi Mtakatifu wa Mungu, usitunyime tukiomba katika shida zetu, utuokoe siku zote, kila tuingiapo hatarini, ee Bikira Mtukufu na mwenye baraka,. Amina.

NOVENA KWA AJILI YA KUJIANDAA KWA SIKUKUU YA MOYO MTAKATIFU WA YESU

Inaweza kusemwa wakati wowote katika mwaka. Kwa ajili ya kujiandaa kwa Sikukuu ya Moyo Mtakatifu wa Yesu,; anza Novena kwa Moyo Mtk wa Yesu katika Alhamisi ya Sikukuu ya Ekaristi Takatifu (Corpus Christi), yaani Alhamisi ya wiki moja kabla ya Sikukuu ya Moyo Mtk (au Alhamisi baada ya Sikukuu ya Utatu Mtk). Endapo Sikukuu hii itaadhimishwa siku ya Dominika inayofuata Sikukuu yenyewe kama inavyofanyika mahali pengi, basi novena inatakiwa ianze Ijumaa ya baada ya Sikukuu ya Utatu Mtk ili imalizike Jumamosi kabla ya Dominika ya sikukuu hii ya Moyo Mtk kwa Yesu.

WIMBO:

YESU KRISTU TWASIFU MOYO WAKO
Yesu Kristu, twasifu Moyo wako, sisi sote, milele mali yako
Tunakupa, nyoyo zote zetu, Mukombozi, Mfalme Mungu wetu;
Tunakupa, nyoyo zote zetu, Mukombozi, Mfalme Mungu wetu!

Watu wengi, wanakaa ugenini, wazunguka, wenye ukiwa chini,
Uwatie huruma yako kuu, roho zao, uziinue juu;
Uwatie huruma yako kuu, roho zao, uziinue juu!

Uwe Mfalme, wa wale washikwao, na ushenzi, na ukaidi wao
Wapelekee ufalme wa Mungu, ni Mchunga mmoja Zizi moja tu;
Wapelekee ufalme wa Mungu, ni Mchunga mmoja Zizi moja tu!

SALA YA KUTUBU

Mungu wangu ninatubu sana, niliyokosa kwako, kwani ndiwe mwema, ndiwe mwenye kupendeza, wachukizwa na dhambi, basi sitaki kukosa tena, nitafanya kitubio, naomba neema yako nipate kurudi wkako. Amina.

ROZARI YA MOYO MTAKATIFU WA YESU

Tumia tasbihi ya kawaida yenye chembe ndogo 53.
Kwenye Msalaba Sali:

“Ee Yesu tupe moyo wako kama amana ya upendo wako na kimbilio letu, ili tupate pumziko salama wakati wa maisha yetu na faraja tamu saa ya kufa kwetu”.
Baba Yetu ……..
Salamu Maria ……. (mara tatu)
Nasadiki ………..

Kwenye chembe kubwa Sali (Badala ya ‘Baba Yetu’):
“Ninakuabudu, ninakutukuza na ninakupenda, Ee Moyo wa Yesu wangu mpenzi, uliopenywa na huzuni nyingi kwa ajili ya dhambi, ambazo zimekuwa zikitendwa hata leo, dhidi ya Sakramenti Takatifu sana ya Altare. Ninakutolea hapo kwa kuridhika, moyo wa Mama yako mpendevu, na mastahili ya watakatifu. Amina”.

Kwenye chembe ndogo sali (Badala ya ‘Salamu Maria’):
“Ee Moyo Mtakatifu wa Yesu, uwakao mapendo kwetu, washa nyoyo zetu kwa mapendo yako”

LITANIA YA MOYO MTAKATIFU WA YESU

Bwana utuhurumie Bwana utuhurumie
Kristo utuhurumie Kristo utuhurumie
Bwana utuhurumie Bwana utuhurumie
Kristo utusikie Kristo utusikilize
Baba wa mbinguni Mungu Utuhurumie
Mwana, Mkombozi wa dunia Mungu Utuhurumie
Roho Mtakatifu Mungu Utuhurumie
Utatu Mtakatifu Mungu mmoja Utuhurumie
Moyo wa Yesu Mwana wa Baba wa Milele Utuhurumie
Moyo wa Yesu uliotungwa na Roho Mtakatifu mwilini mwa Mama Bikira Maria Utuhurumie
Moyo wa Yesu ulioungana na Neno wa Mungu Utuhurumie
Moyo wa Yesu ulio na utukufu pasipo mfano Utuhurumie
Moyo wa Yesu, hekalu takatifu la Mungu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, hema la Yule aliye juu Utuhurumie
Moyo wa Yesu tanuru lenye kuwaka mapendo Utuhurumie
Moyo wa Yesu, nyumba ya Mungu na mlango wa Mbingu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, tanuru yenye kuwaka mapendo Utuhurumie
Moyo wa Yesu, chombo cha haki na upendo Utuhurumie
Moyo wa Yesu, unaojaa upendo na wema Utuhurumie
Moyo wa Yesu, kilindi cha fadhila zote Utuhurumie
Moyo wa Yesu, unaostahili sifa zote Utuhurumie
Moyo wa Yesu, unaotawala mioyo yote Utuhurumie
Moyo wa Yesu, zinamokaa hazina za hekima na elimu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, uliopendelewa na Mungu Baba Utuhurumie
Moyo wa Yesu, uliotuenezea maziada yake Utuhurumie
Moyo wa Yesu, mtamaniwa wa vilima vya milele Utuhurumie
Moyo wa Yesu, wenye uvumilivu na huruma nyingi Utuhurumie
Moyo wa Yesu, tajiri kwa wote wenye kukuomba Utuhurumie
Moyo wa Yesu, chemchemi ya uzima na utakatifu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, malipo kwa dhambi zetu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, ulioshibishwa matusi Utuhurumie
Moyo wa Yesu, uliovunjika kwa sababu ya ubaya wetu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, uliotii mpaka kufa Utuhurumie
Moyo wa Yesu, uliochomwa kwa mkuki Utuhurumie
Moyo wa Yesu, chemchemi ya faraja zote Utuhurumie
Moyo wa Yesu, uzima na ufufuo wetu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, amani na upatanisho wetu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, sadaka ya wakosefu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, unamokaa wokovu wao wenye kukutumaini Utuhurumie
Moyo wa Yesu, matumaini yao wenye kuzimia kwako Utuhurumie
Moyo wa Yesu, sababu ya furaha ya watakatifu wote Utuhurumie
Mwanakondoo wa Mungu, uondoaye dhambi za dunia Utusamehe Bwana
Mwanakondoo wa Mungu, uondoaye dhambi za dunia Utusikilize Bwana
Mwanakondoo wa Mungu, uondoaye dhambi za dunia Utuhurumie

Kiongozi: Yesu mwenye Moyo mpole na mnyenyekevu,
Wote: Ufanye mioyo yetu ifanane na Moyo wako

TUOMBE: (W) Ee Mungu Mwenyezi milele, uuangalie Moyo wa mwanao mpendelevu, pia na heshima na malipo aliyokutolea kwa ajili ya wenye dhambi, uridhike, uwaondolee wenye kuomba toba kwako kwa njia ya huyo Mwanao Yesu Kristo anayeishi na kutawala nawe pamoja na Roho Mtakatifu, Mungu milele. Amina.

P.S. Mwezi wa sita ni wa kuuheshimu Moyo Mtakatifu wa Yesu. Vitu vya kufanya ni pamoja na kushiriki Misa takatifu kila siku, kumtembelea Bwana Yesu katika Ekaristia, kusali Rozari ya Moyo Mtakatifu wa Yesu kila siku, kusali Litania za Moyo Mtakatifu wa Yesu, kuimba nyimbo za kuusifu Moyo Mtakatifu wa Yesu, na kadhalika. Kwa kufanya hayo na mengineyo yanayofanana nayo, waumini hujichotea Baraka na neema nyingi za kimwili na kiroho.

SALA YA NOVENA

Ee Moyo Mtakatifu sana wa Yesu, chemchemi ya kila baraka, ninakuabudu, ninakupenda, na kwa majuto halisi ya dhambi zangu, nakutolea moyo wangu dhaifu. Nifanye mnyenyekevu, mvumilivu na safi, nikikubali na kuyatii kabisa mapenzi yako. Ee Yesu mwema, unijalie niishi nawe na kwa ajili yako. Unilinde niwapo katikati ya hatari, unifariji katika mateso, unipe afya ya mwili na msaada katika mahitaji ya mwili, Baraka yako juu ya kila nilifanyalo, na neema ya kifo chema. Amina.

Ee Yesu uliyesema “Kweli nawaambieni, ombeni nanyi mtapewa, tafuteni nanyi mtapata, gongeni nanyi mtafunguliwa”, tazama ninagonga, ninatafuta na kuomba …….. (Taja ombi lako)
Baba Yetu….., Salamu Maria …….., Atukuzwe Baba……..
Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutumainia kwa moyo wote!

Ee Yesu uliyesema “Kweli nawaambieni, chochote mtakachomwomba Baba kwa jina langu mtapewa”, tazama kwa jina lako ninaomba ……. (Taja ombi lako)
Baba Yetu….., Salamu Maria …….., Atukuzwe Baba……..
Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutumainia kwa moyo wote!

Ee Yesu uliyesema “Kweli nawaambieni, mbingu na dunia zitapita lakini maneno yangu hayatapita kamwe”, tazama, nikitiwa nguvu na maneno yako ya kweli ninaomba …….. (Taja ombi lako)
Baba Yetu….., Salamu Maria …….., Atukuzwe Baba……..
Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutumainia kwa moyo wote!

Ee Moyo Mtakatifu wa Yesu, ambaye kwako ni kitu kimoja tu kisichowezekana, ambacho ni kutoacha kutowaonea huruma wenye huzuni, utuhurumie sisi wakosefu maskini na utujalie neema tukuombayo kwa njia ya Moyo Imakulata wa Maria, Mama yetu mpole.

Sali ‘Salamu Malkia’ na kuongezea, ‘Mtakatifu Yosefu Baba Mlishi wa Yesu, utuombee’.

P.S. – Sala hii ya Novena ilisaliwa kila siku na PADRE PIO kwa ajili ya kuwaombea wale wote waliomwomba msaada wa sala zake. Unaweza kuisali kwa namna tofauti tofauti. Mfano, kama Novena ya siku tisa, ambapo unasali sala hii mara moja au zaidi kila siku kwa siku tisa, au unaweza kuifanya kama Novena ya masaa, ambapo unasali sala hii kila baada ya saa moja kwa masaa tisa kwa siku hiyo hiyo, hasa kama kitu unachokiomba ni cha haraka au umesongwa moyoni. Vilevile unaweza kuifanya sala hii kama sehemu ya sala zako za kila siku katika mwezi Juni ambao ni mwezi uliotengwa na Kanisa kwa ajili ya kuuheshimu Moyo Mtakatifu wa Yesu, na hapo utaitumia kuwaombea watu waliokuomba msaada wa sala zako kama alivyofanya Mtakatifu Padre Pio. Pia unaweza kuitumia kama sala yako ya siku zote au ya mara kwa mara kwa ajili ya mahitaji mbalimbali.

SALA YA MAOMBI

Ee Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakukimbilia, ninakuja kwako katika mikono yako yenye huruma. Ndiwe tegemeo langu na tumaini langu dhabiti. Ndiwe mwenye dawa ya maovu yangu yote, malipizi ya makosa yangu yote. Waweza kunipatia haja zangu na neema ninazoziomba mimi na wengine. Wewe uko ili kutusaidia sote, ndiwe mwanga mkuu usiozimika, ndiwe chanzo cha nguvu, uvumilivu, amani na faraja. Nina hakika kuwa maombi yangu hayatakuchosha, nawe hutaacha kunisaidia, kunilinda, kunipenda, kwani, ee Moyo Mtakatifu , upendo wako hauna mwisho. Ee Moyo Mtakatifu, unihurumie, kwa ajili ya maombi yangu, kadiri ya huruma yako. Nawe katika sisi, na kwa ajili yetu, ufanye lolote unalolihitaji, kwani tunajitoa kwako kwa imani na uhakika thabiti kwamba kamwe hautatuacha, kwa milele. Amina.

Litani ya Bikira Maria

  • Bwana utuhurumie
  • Bwana utuhurumie
  • Kristo utuhurumie
  • Bwana utuhurumie
  • Bwana utuhurumie
  • Kristo utusikie
  • Kristo utusikilize
  • Mungu Baba wa Mbinguni,…… Utuhurumie
  • Mungu Mwana Mkombozi wa dunia ……… Utuhurumie
  • Mungu Roho Mtakatifu …….. Utuhurumie
  • Utatu Mtakatifu Mungu Mmoja …….. Utuhurumie
  • Maria Mtakatifu ………. utuombee
  • Mzazi Mtakatifu wa Mungu …….. utuombee
  • Bikira Mtakatifu Mkuu wa Mabikira …….. utuombee
  • Mama wa Kristo ……… utuombee
  • Mama wa Neema ya Mungu ………….. utuombee
  • Mama Mtakatifu sana ……… utuombee
  • Mama mwenye usafi wa Moyo ……….. utuombee
  • Mama mwenye ubikira ……….. utuombee
  • Mama usiye na doa ……….. utuombee
  • Mama mpendelevu ………. utuombee
  • Mama mstajabivu ………. utuombee
  • Mama wa Muumba ………. utuombee
  • Mama wa Mkombozi ………….. utuombee
  • Mama wa Kanisa……….. utuombee
  • Bikira mwenye utaratibu ………….. utuombee
  • Bikira mwenye heshima ………….. utuombee
  • Bikira mwenye sifa ………….. utuombee
  • Bikira mwenye uwezo ………….. utuombee
  • Bikra mweye huruma ………….. utuombee
  • Bikra mwaminifu………….. utuombee
  • Kioo cha haki ………….. utuombee
  • Kikao cha hekima ………….. utuombee
  • Sababu ya furaha yetu ………….. utuombee
  • Chombo cha neema ………….. utuombee
  • Chombo cha kuheshimiwa ………….. utuombee
  • Chombo bora cha ibada ………….. utuombee
  • Waridi lenye fumbo ………….. utuombee
  • Mnara wa Daudi ………….. utuombee
  • Mnara wa pembe ………….. utuombee
  • Nyumba ya dhahabu ………….. utuombee
  • Sanduku la Agano ………….. utuombee
  • Mlango wa Mbingu ………….. utuombee
  • Nyota ya asubuhi ………….. utuombee
  • Afya ya wagonjwa ………….. utuombee
  • Kimbilio la wakosefu ………….. utuombee
  • Mtuliza wenye huzuni ………….. utuombee
  • Msaada wa waKristo ………….. utuombee
  • Malkia wa Malaika ………….. utuombee
  • Malkia wa Mababu ………….. utuombee
  • Malkia wa Manabii ………….. utuombee
  • Malkia wa Mitume ………….. utuombee
  • Malkia wa Mashahidi ………….. utuombee
  • Malkia wa Waungama dini ………….. utuombee
  • Malkia wa Mabikira ………….. utuombee
  • Malkia wa Watakatifu wote ………….. utuombee
  • Malkia uliyepalizwa Mbinguni ………….. utuombee
  • Malkia wa Rozari takatifu ………….. utuombee
  • Malkia wa amani ………….. utuombee

  • Mwanakodoo wa Mungu uondoaye dhambi za dunia,…………..Utusamehe ee Bwana.
  • Mwanakondoo wa Mungu uondoaye dhambi za dunia,…………..Utusikilize ee Bwana
  • Mwanakondoo wa Mungu uondoaye dhambi za dunia,…………..Utuhurumie.

  • Utuombee, Mzazi Mtakatifu wa Mungu,…………..Tujaliwe ahadi za Kristo.

Tuombe

Ee Bwana Mungu, utujalie sisi watumishi wako afya ya roho na mwili siku zote; na kwa maombezi matukufu ya Maria Mtakaatifu Bikira daima, tuopolewe na mashaka ya saa, tupate na furaha za milele. Kwa Kristo Bwana wetu, Amina.

Sala ya Usiku kabla ya kulala

Kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu. Amina.

SALA YA KUSHUKURU

Tunakushukuru, ee Mungu, kwa mapaji uliyotujalia leo. Amina.

Baba yetu …

Salamu Maria …

SALA YA IMANI

Mungu wangu, nasadiki maneno yote. Linayosadiki na linayofundisha Kanisa Katoliki la Roma. Kwani ndiwe uliyetufumbulia hayo. Wala hudanganyiki, wala hudanganyi. Amina.

SALA YA MATUMAINI

Mungu wangu, natumaini kwako, nitapewa kwa njia ya Yesu Kristo. Neema zako hapa duniani, na utukufu mbinguni. Kwani ndiwe uliye agana hayo nasi, nawe mwamini. Amina.

SALA YA MAPENDO

Mungu wangu, nakupenda zaidi ya chochote. Kwani ndiwe mwema, ndiwe mwenye kupendeza. Nampenda na jirani yangu, kama nafsi yangu, kwa ajili yako. Amina.

KUTUBU DHAMBI

Tuwaze katika moyo wetu makosa ya leo tuliyomkosea Mungu kwa mawazo, kwa maneno, kwa vitendo na kwa kutotimiza wajibu. (Husubiri kidogo ).

Nakuungamia Mungu Mwenyezi, nanyi ndugu zangu, kwani nimekosa mno, kwa mawazo, kwa maneno, kwa vitendo, na kwa kutotimiza wajibu.
Nimekosa mimi, nimekosa mimi, nimekosa sana. Ndiyo maana nakuomba Maria mwenye heri, Bikira daima, Malaika na Watakatifu wote, nanyi ndugu zangu, niombeeni kwa Bwana Mungu wetu.
Mungu Mwenyezi atuhurumie, atusamehe dhambi zetu, atufikishe kwenye uzima wa milele. Amina.

SALA YA KUWAOMBEA WATU

Ee Mungu, nawaombea watu wa nchi hii, wapate kusikia maneno yako na kukupenda wewe Bwana Mungu wetu.

SALA KWA MALAIKA MLINZI

Malaika mlinzi wangu, unilinde katika hatari zote za roho na za mwili. Amina.

MALAIKA WA BWANA

(kipindi kisicho cha Pasaka)
Malaika wa Bwana alimpasha habari Maria.
Naye akapata mimba kwa uwezo wa Roho Mtakatifu.
Salamu, Maria,…..
Ndimi mtumishi wa Bwana.
Nitendewe ulivyonena.
Salamu, Maria….
Neno la Mungu akatwaa mwili.
Akakaa kwetu.
Salamu, Maria….
Utuombee, Mzazi mtakatifu wa Mungu.
Tujaliwe ahadi za Kristu.
Tuombe:
Tunakuomba, Ee Bwana, utie neema yako mioyoni mwetu, ili sisi tuliojua kwa maelezo ya Malaika kwamba Mwanao amejifanya Mtu kwa mateso na msalaba wake tufikishwe kwenye utukufu wa ufufuko. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristu Bwana wetu. AMINA.

AU;

MALKIA WA MBINGU (kipindi cha Pasaka)

Malkia wa mbingu, furahi, aleluya.
Kwani uliyestahili kumchukua, Aleluya.
Amefufuka alivyosema, Aleluya.
Utuombee kwa Mungu, Aleluya.
Furahi shangilia, ee Bikira Maria, Alaluya.
Kwani hakika Bwana amefufuka Aleluya.
Tuombe.
Ee Mungu, uliyependa kuifurahisha dunia kwa kufufuka kwake Bwana wetu Yesu Kristu, Mwanao, fanyiza, twakuomba, kwa ajili ya Bikira Maria, tupate nasi furaha za uzima wa milele. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristu Bwana wetu. Amina.

ATUKUZWE (mara tatu)
Atukuzwe Baba na Mwana na Roho Mtakatifu. Kama mwanzo na sasa na siku zote na milele. Amina.

KUJIKABIDHI

Enyi Yesu, Maria na Yosefu nawatolea moyo na roho na uzima wangu!
Enyi Yesu, Maria na Yosefu mnijilie saa ya kufa kwangu!
Enyi Yesu, Maria na Yosefu mnijalie nife mikononi mwenu!

(Rehema ya siku 300).

WIMBO:

Kwa heri Yesu mpenzi mwema,
Naenda usiudhike mno.
Nakushukuru, nakupenda,
Kwa hizo nyimbo za mwisho.
Asubuhi nitarudi.
Yesu kwa heri.

Kwa heri Mama mtakatifu,
Sasa napita pumzika.
Asante kwa moyo na nguvu,
Leo umeniombea.
Asubuhi nitarudi.
Mama kwa heri.

Kwa heri Yosefu mnyenyekevu,
Kazi zatimilizika.
Kama mchana, leo usiku,
Nisimamie salama.
Asubuhi nitarudi.
Yosefu kwa heri.

Kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu. Amina.

KUOMBA ULINZI WA USIKU

Mungu wangu naenda kulala naomba malaika 14, waende nami, wawili juu, wawili chini, wawili upande wa kuume, wawili upande wa kushoto, wawili wanifunike, wawili waniamshe, wawili wanipeleke juu mbinguni. Mimi mtoto mdogo, roho yangu ni ndogo, haina nafasi kwa mtu yoyote ila kwa Yesu pekee. Amina.

Malkia wa Mbingu

Malkia wa mbingu, furahi, aleluya. Kwani uliyestahili kumchukua, Aleluya. Amefufuka alivyosema, Aleluya. Utuombee kwa Mungu, Aleluya. Furahi shangilia, ee Bikira Maria, Alaluya. Kwani hakika Bwana amefufuka Aleluya. Tuombe. Ee Mungu, uliyependa kuifurahisha dunia kwa kufufuka kwake Bwana wetu Yesu Kristu, Mwanao: fanyiza, twakuomba, kwa ajili ya Bikira Maria, tupate nasi furaha za uzima wa milele. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristu Bwana wetu. Amina.

Majitoleo kwa Bikira Maria

(Sala iliyotungwa na Mtk. Aloisi)
Bibi yangu mtukufu Maria, nakuwekea amana ya roho yangu na mwili wangu, nikikuomba uipokee amana yangu, kuitunzia ulinzi mwema ulinzi bora, ninakuaminia na kila neno langu, matumaini na kitulizo na kisongo chote, na masumbuko na uzima na ukomo wa uzima wangu: nitakayo ndiyo unifanyizie kwa maombezi na stahili zako, ili mambo yangu yote yapate kuongoka, yakiwa na kufuata mapenzi yako, pamoja na mapenzi ya Mwanao. Amina.

SALA YA KUMWOMBA MT. YOSEFU MSAADA (SALA KUU KWA MTAKATIFU YOSEFU)

Ee Mt. Yosefu mwenye heri, tunakimbilia kwako katika masumbuko yetu, na kisha omba shime ya Mchumba wako Mtakatifu, tunaomba pia kwa matumaini usimamizi wako. Kwa ajili ya mapendo uliyompenda Bikira Mtakatifu Mzazi wa Mungu, na kwa ajili ya kumtunza Mtoto Yesu, twakuomba sana, utuangalie kwa wema sie tuliokuwa fungu lake Yesu Kristu, tukakombolewa kwa damu yake. Tusimamie katika masumbuko yetu kwa enzi na shime yako.

Ee Mlinzi amini wa jamaa takatifu, uwakinge watoto wateule wa Yesu Kristu.
Ee Baba uliyetupenda mno tuepushe na kilema chochote cha madanganyo na upotevu. Ee kinga yetu mwezaji, utusimamie huko juu mbinguni ulipo, tunaposhindana na wenye nguvu wakaao gizani. Kama vile siku za kale ukamwopoa Mtoto Yesu katika hatari ya kuuawa, na leo hivi likinge Kanisa Takatifu la Mungu katika mitego ya adui, na katika shida yote; mtunze daima kila mmoja wetu, tufwate mfano wako, ili tupate na msaada wako, kukaa na utakatifu maisha, kufa kifo chema, na kupata mbinguni makao ya raha milele.
Amina.

SALA KWA MT. YOSEFU KWA WASIO NA AJIRA WAPATE AJIRA

Ee Mt. Yosefu, tunakuomba kwa ajili ya wale asio na ajira, kwa ajili ya wale wanaotaka kujipatia kipato chao na kulisha familia zao.
Wewe u Msimamizi wa wafanyakazi, tujalie kwamba pasiwepo kati yetu mtu asiye na ajira, na kwamba wale wote ambao wako tayari kufanya kazi waweze kuelekeza nguvu zao na uwezo wao katika kuwatumikia wanadamu wenzao na kujipatia kipato halali.

Wewe u Msimamizi wa familia, usiwaache wale wenye watoto wa kuwatunza na kuwalea wakose namna ya kufanya hivyo. Uwahurumie ndugu zetu waliokosa ajira na kugubikwa na umasikini kwa sababu ya magonjwa au mipango mibaya ya kijamii. Wasaidie viongozi wetu wa kisiasa na walioshika usukani katika nyanja mbalimbali za kiuzalishaji wavumbue suluhu mpya na za haki za jambo hili. Utujalie ili kila mmoja wetu apate kujipatia kipato halali na kufurahia fursa ya kushiriki kadri ya uwezo wake, katika maisha bora zaidi kwa wote. Utujalie ili wote tushiriki pamoja katika raslimali alizotujalia Mungu, na pia utujalie tuwe tayari daima kuwasaidia wale walio wahitaji kuliko sisi.
Amina.

SALA YA MTU ALIYEKABILIWA NA MATATIZO MBALIMBALI

Ewe Mtakatifu Yuda Tadei,/ mtume mtukufu na shahidi wa Kristo,/ umesifika pote kwa wepesi wako wa kutoa misaada/ kwa wanaokukimbilia katika matatizo yao mazito./ Pia ni mwombezi wa waliopondeka moyo./

Mimi ni mmoja wa hao./ Nakujia na moyo uliojaa shida na matatizo./ Nakusihi kwa moyo wote/ unisaidie kwa maombezi yako yenye nguvu/ kufikia utatuzi unaofaa kadiri ya mapenzi ya Mungu./ Maisha yangu yamejaa misalaba,/ siku kwa siku matatizo hayapungui./ Moyo wangu umekuwa bahari ya siki chungu sana./ Mapito yangu nayaona yamejaa miiba mikali./ Roho yangu imezama katika dimbwi la machozi na kite./ Nafsi yangu imezingirwa na giza nene./ Ghasia na kukatishwa tamaa ya kuishi/ hunyemelea roho yangu./ Maongozi ya Mungu na imani naviona vinanitoka kidogo kwa kidogo./

Nikielemewa na mawazo kama hayo/ najikuta sina nguvu za kuishi,/ na maisha kwangu ni msalaba mzito/ ninaouogopa hata kuunyakua./ Wewe unaweza kabisa kunitoa katika balaa hili./ Sitaacha kukusihi/ hadi hapo utakaponisaidia/ au kunijulisha mapenzi ya Mungu kwangu./ Natangulia kutoa shukrani kwa jibu liwalo lote.

Sala za kuheshimu Damu Takatifu ya Yesu

Tusali kila siku sala hizi, angalau kwa mwezi wa saba (Julai) kila mwaka, mwezi wa kuheshimu Damu Takatifu ya Mkombozi wetu.

Yesu alimwahidi Mt. Brigita wa Sweden kwamba wale watakaosali Baba Yetu 7 na Salamu Maria 7 kwa miaka 12 kwa kuheshimu damu yake takatifu na kutafakari juu ya Kutahiriwa kwake, jasho lake la damu, kupigwa kwake mijeledi, kuvikwa taji la miiba, kuchukua kwake Msalaba, kusuliwa kwake na kuchomwa ubavuni; watapata neema 5 zifuatazo: (1) Hawataingia toharani, (2) Yesu atawapa cheo cha mashahidi waliomwaga damu yao kwa ajili ya imani, (3) Yesu atawadumisha jamaa zake watatu katika hali ya neema, (4) Roho za jamaa zake zitakingwa na Jehanam mpaka kizazi cha nne, (5) Mwezi kabla ya kufa, Yesu atawajulisha. Wakifa kabla ya kutimiza miaka ile, watahesabiwa wamemaliza.

Ee Yesu, sasa ninataka kusali Baba yetu mara saba nikiungana na ule upendo ambao kwao uliitakasa sala hii katika Moyo wako. Uichukue kutoka mdomoni mwangu hadi moyoni mwako. Uiboreshe na kuikamilisha hivyo kwamba iupatie heshima na furaha kwa Utatu Mtakatifu kama vile Wewe ulivyoupatia kupitia sala hii wakati ulipokuwa bado hapa duniani. Utukuzwe ee Yesu, itukuzwe Damu Yako Takatifu sana uliyoimwaga kutoka katika Majeraha Yako Matakatifu.

1. Yesu anatahiriwa.

Tafakari fupi (kimya kidogo). Baba Yetu …. Salamu Maria …. Baba wa Milele, kupitia mikono safi ya Maria na Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutolea Majeraha ya kwanza, maumivu ya kwanza na Damu ya kwanza aliyomwaga Mwanao mpenzi, Bwana wetu Yesu Kristu, kwa ajili ya malipizi ya dhambi zangu na dhambi za dunia nzima, kwa ajili ya ulinzi dhidi ya dhambi ya kwanza ya mauti, hasa kati ya ndugu zangu.

2. Yesu anatokwa Jasho la Damu bustanini Gethsemane.

Tafakari fupi (kimya kidogo). Baba Yetu …. Salamu Maria …. Baba wa Milele, kupitia mikono safi ya Maria na Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutolea mateso na mahangaiko makali sana ya moyoni, ya Bwana wetu Yesu Kristu katika mlima wa mizeituni na kila tone la jasho lake la damu, kwa ajili ya malipizi ya dhambi zangu za kimoyomoyo, na dhambi za namna hiyo zinazotendwa na dunia nzima, kwa ajili ya ulinzi dhidi ya dhambi za moyoni na kwa ajili ya kueneza upendo wa kiMungu na wa kindugu.

3. Yesu anapigwa mijeledi.

Tafakari fupi (kimya kidogo). Baba Yetu …. Salamu Maria …. Baba wa Milele, kupitia mikono safi ya Maria na Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutolea majeraha elfu elfu aliyopata, maumivu makali sana na Damu Takatifu sana aliyomwaga, alipopigwa mijeledi, kwa ajili ya malipizi ya dhambi zangu za tamaa ya mwili, kwa malipizi ya dhambi za tamaa ya mwili za wanadamu wote, kwa ajili ya ulinzi dhidi ya dhambi za tamaa ya mwili, na kwa kulinda usafi wa moyo, hasa kati ya ndugu zangu.

4. Yesu anavikwa taji la miiba.

Tafakari fupi (kimya kidogo). Baba Yetu …. Salamu Maria …. Baba wa Milele, kupitia mikono safi ya Maria na Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutolea majeraha, maumivu na Damu Takatifu kutoka katika Kichwa Kitakatifu cha Yesu wakati alipovikwa taji la miiba, kwa ajili ya malipizi ya dhambi zangu za rohoni, kwa malipizi ya dhambi za rohoni za wanadamu wote, kwa ajili ya ulinzi dhidi ya dhambi za rohoni, na kwa ajili ya kueneza Ufalme wa Kristu hapa duniani.

5. Yesu anachukua Msalaba.

Tafakari fupi (kimya kidogo). Baba Yetu …. Salamu Maria …. Baba wa Milele, kupitia mikono safi ya Maria na Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutolea mateso ya njia ya Msalaba, hasa donda lake la begani na Damu Takatifu iliyomwagika, kwa ajili ya malipizi ya dhambi zangu za ukaidi dhidi ya msalaba, na dhambi za ukaidi dhidi ya msalaba za wanadamu wote, malalamiko yote dhidi ya mipango yako mitakatifu na dhambi zote za ulimi, kwa ajili ya ulinzi dhidi ya dhambi za ulimi na kwa ajili ya upendo wa kweli kwa Msalaba.

6. Yesu anasulibiwa.

Tafakari fupi (kimya kidogo). Baba Yetu …. Salamu Maria …. Baba wa Milele, kupitia mikono safi ya Maria na Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutolea Mwanao Msalabani, kupigwa kwake misumari na kuinuliwa kwake, madonda yake mikononi na miguuni na mifereji mitatu ya Damu yake Takatifu iliyomwagika kutoka katika majeraha haya, mateso yake makali sana ya mwili na roho, kifo chake kitakatifu, ukumbusho usio wa kumwaga wa damu wa kifo hiki katika Misa zote Takatifu ulimwenguni, kwa ajili ya majeraha yote yanayosababishwa na ukaidi wa nadhiri na kanuni katika madaraja matakatifu, kwa ajili ya malipizi ya dhambi zangu zote na za ulimwenguni mzima, kwa ajili ya wagonjwa na wanaokufa, kwa ajili ya mapadre watakatifu na walei, kwa ajili ya nia za Baba Mtakatifu za kukarabati familia za kikristu, kwa ajili ya kuimarika kwa imani ya kikristu ulimwenguni, kwa ajili ya nchi yetu na muungano kati ya mataifa ndani ya Kristu na Kanisa lake, na kwa ajili ya wokovu wa dunia nzima.

7. Yesu anachomwa kwa mkuki moyoni.

Tafakari fupi (kimya kidogo). Baba Yetu …. Salamu Maria …. Baba wa Milele, ukubali kupokea, kwa ajili ya mahitaji ya Kanisa Takatifu na kwa ajili ya malipizi ya dhambi za wanadamu wote, Damu na Maji Takatifu vilivyomwagika kutoka jeraha la Moyo Mtakatifu wa Yesu. Utuhurumie. Damu Takatifu ya Yesu, tone lile la mwisho lililomwagika kutoka katika Moyo wake Mtakatifu, unioshe mimi na wengine wote dhambi zetu zote! Ee Maji kutoka katika Moyo Mtakatifu wa Yesu, unioshe na adhabu zote za dhambi zangu na uizime miale ya moto wa toharani kwa ajili yangu na kwa ajili ya roho zote zilizomo toharani. Amina.

Katika mwaka wa Kanisa wa kiliturjia, mwezi Julai ni wa kuiheshimu Damu Takatifu ya Yesu.

Shopping Cart
2
    2
    Your Cart
    🏠 Home 📖 Reading 🖼️ Gallery 💬 AI Chat 📘 About