Sala za Katoliki: Sala Muhimu Kwa Mkristu Mkatoliki

Sala ya Saa Tisa

✝⌚✝

Sala ya saa tisa🙏🏾

Kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu. A mina

Yesu, ulikufa, lakini chanzo cha uhai kilitoka kwa ajili ya watu, na bahari ya huruma ilifunguka kwa ajili ya ulimwengu mzima. Ee chemchemi ya Uhai, huruma ya Mungu isiyo na mwisho, ikafunika ulimwengu mzima na ukajimwaga mwenyewe juu yetu.

❣✝❣

✝Ee Damu na Maji, yaliyotoka moyoni mwa Yesu kama chemchemi ya Huruma kwetu. Nakutumainia.

(Mara tatu)

🛐❣🛐

Novena ya Noeli

Novena ya Noeli (maarufu kama novena ya Mt. Andrea)

Husaliwa kuanzia tar 30 Nov hadi usiku wa Noeli, tar 24 Disemba. Inajulikana kama novena ya Mt. Andrea kwa sababu novena hii huanza kusaliwa katika siku ya kumbukumbu ya Mt. Andrea Mtume.

“IHESHIMIWE, NA IBARIKIWE, SAA ILE NA WAKATI ULE, AMBAO MWANA WA MUNGU, ALIZALIWA NA BIKIRA MBARIKIWA SANA, USIKU WA MANANE, KULE BETHLEHEM, WAKATI WA BARIDI KALI.
WAKATI HUO, UPENDE E MUNGU WANGU, KUSIKIA MAOMBI YANGU, NA KUNIJALIA YALE NINAYOYAOMBA KWAKO, KWA NJIA YA MASTAHILI YA MWOKOZI WETU YESU KRISTO, NA YA MAMA YAKE MBARIKIWA. AMINA. (Sali mara 15 kwa siku).

Inasadikika kuwa chochote uombacho kwa imani kwa sala hii utakipata mradi kipatane na mapenzi ya Mungu. Sali na watoto/ familia kuwatafakarisha na kuwaongezea matazamio juu ya sikukuu ya Noeli.

Isambaze sala hii kwa wengine.

SALA YA KUANGUKA MIGUUNI PA BWANA YESU KATIKA EKARISTI

Ee Yesu Mfungwa wa Upendo wa Mungu,/ ninapofikiri Upendo wako na jinsi ulivyojitolea kwa ajili yangu,/ nashindwa kuelewa./ Unaficha Ukuu wako usiofahamika/ na kujidhihirisha kwa ajili yangu mimi mnyonge./ Ee Mfalme wa utukufu,/ unaficha uzuri wako,/ lakini jicho la moyo wangu/ linapenya pazia na kuona Majeshi ya Malaika/ wakikuimbia kwa heshima bila kukoma/ na nguvu zote mbinguni zikikusifu bila mwisho zikisema:/ “Mtakatifu, Mtakatifu, Mtakatifu..”/

Ni nani awezaye kufahamu Upendo wako/ na huruma yako isiyo na kipimo kwa ajili yetu!/ Ee Mfungwa wa Upendo,/ nafungia moyo wangu masikini/ kwenye Tabarnakulo hii/ ili niweze kukuabudu usiku na mchana bila mwisho./ Najua hakuna kizuizi/ na hata kama naonekana kukaa mbali,/ lakini moyo wangu u pamoja nawe/ katika ibada hii./ Hakuna kinachoweza kuzuia upendo wangu kwako./ Kwangu hakuna kizuizi chochote./

Ee Utatu Mtakatifu,/ Mungu Mmoja usiyegawanyika,/ utukuzwe kwa zawadi yako hii kuu/ na agano hili la huruma!/

Nakuabudu,/ Bwana na Muumba uliyefichika katika Sakramenti Takatifu!/ Ee Bwana,/ nakuabudu kwa kazi zote za mikono yako/ zinazonifunulia Hekima yako kuu,/ Wema wako na Huruma yako kuu./ Uzuri uliousambaza hapa/ Uzuri ulio nao Wewe mwenyewe/ ambaye U Uzuri usioelezeka;/ na ingawaje umejificha na kusitiri uzuri wako,/ jicho langu,/ kwa mwanga wa imani linafika kwako,/ na roho yangu inapata kumtambua Muumba wake/ aliye Uzuri usiopimika,/ ulio juu ya kila uzuri,/ na moyo wangu unazama kabisa katika sala ya kukuabudu./

Bwana wangu na Muumba wangu,/ wema wako wanitia moyo wa kuongea nawe,/ Huruma yako huondoa kiambaza/ kitenganishacho Muumba na kiumbe./ Furaha ya moyo wangu,/ ee Mungu, ni kuongea na Wewe./ Yote ambayo moyo wangu unayatamni nayapata kwako./ Hapa ndipo mwanga wako unaponiangaza akili yangu/ na kuiwezesha kukujua Wewe zaidi na zaidi/ – ndipo mikondo ya neema inapoutiririkia moyo wangu,/ ndipo roho yangu inapochota uzima wa milele./ Ee Bwana na Muumba wangu,/ licha ya mapaji yote haya,/ unajitoa mwenyewe kwangu,/ ili uweze kujiunganisha na kiumbe dhaifu na maskini./

Ee Kristu,/ nafurahi sana nionapo kwamba unapendwa/ na kwamba sifa na utukufu wako vinaongezwa/ hasa ya Huruma yako./ Ee Kristu,/ sitaacha kamwe kuutukuza wema wako na huruma yako,/ hadi dakika ya mwisho ya maisha yangu./ Kwa kila tone la damu yangu/ na kwa kila pigo la moyo wangu/ naitukuza Huruma yako./ Natamani kugeuzwa kabisa/ na kuwa utenzi wa utukufu wako./ Naomba siku ya kufa kwangu/ popote nitakapokuwa nimelala,/ pigo la mwisho la moyo wangu/ liwe utenzi mpendevu/ usifuo Huruma yako isiyo na kipimo./ Amina

(Na Mt. Faustina Kowalska).

SALA KWA MT. YOSEFU KWA WASIO NA AJIRA WAPATE AJIRA

Ee Mt. Yosefu, tunakuomba kwa ajili ya wale asio na ajira, kwa ajili ya wale wanaotaka kujipatia kipato chao na kulisha familia zao.
Wewe u Msimamizi wa wafanyakazi, tujalie kwamba pasiwepo kati yetu mtu asiye na ajira, na kwamba wale wote ambao wako tayari kufanya kazi waweze kuelekeza nguvu zao na uwezo wao katika kuwatumikia wanadamu wenzao na kujipatia kipato halali.

Wewe u Msimamizi wa familia, usiwaache wale wenye watoto wa kuwatunza na kuwalea wakose namna ya kufanya hivyo. Uwahurumie ndugu zetu waliokosa ajira na kugubikwa na umasikini kwa sababu ya magonjwa au mipango mibaya ya kijamii. Wasaidie viongozi wetu wa kisiasa na walioshika usukani katika nyanja mbalimbali za kiuzalishaji wavumbue suluhu mpya na za haki za jambo hili. Utujalie ili kila mmoja wetu apate kujipatia kipato halali na kufurahia fursa ya kushiriki kadri ya uwezo wake, katika maisha bora zaidi kwa wote. Utujalie ili wote tushiriki pamoja katika raslimali alizotujalia Mungu, na pia utujalie tuwe tayari daima kuwasaidia wale walio wahitaji kuliko sisi.
Amina.

SALA YA JIONI

TUNAKUSHUKURU, EE MUNGU KWA MAPAJI YOTE ULIYOTUJALIA LEO AMINA

BABA YETU……………….. SALAMU MARIA……………….

SALA YA IMANI…….YA MATUMAINI………YA MAPENDO

SALA YA KUTUBU

TUWAZE KATIKA MOYO WETU MAKOSA YA LEO TULIYOMKOSEA MUNGU KWA MAWAZO,KWA MANENO, KWA VITENDO NA KWA KUTOTIMIZA WAJIBU (HUSUBIRI KIDOGO)
NAKUUNGAMIA MUNGU MWENYEZI,NANYI NDUGU ZANGU,KWANI NIMEKOSA MNO KWA MAWAZO,KWA MANENO,KWA VITENDO NA KWA KUTOTIMIZA WAJIBU,NIMEKOSA MIMI,NIMEKOSA SANA.NDIYO MAANA NAKUOMBA MARIA MWENYE HERI,BIKIRA DAIMA,MALAIKA NA WATAKATIFU WOTE,NANYI NDUGU ZANGU,MNIOMBEENI KWA BWANA MUNGU WETU.

MUMNU MWENYEZI ATUHURUMIE ATUSAMEHE DHAMBI ZETU,ATUFIKISHE KWENYE UZIMA WA MILELE.AMINA

SALA YA KUOMBEA WATU……………………
KUSIFU……………………

NOVENA KWA AJILI YA KUJIANDAA KWA SIKUKUU YA MOYO MTAKATIFU WA YESU

Inaweza kusemwa wakati wowote katika mwaka. Kwa ajili ya kujiandaa kwa Sikukuu ya Moyo Mtakatifu wa Yesu,; anza Novena kwa Moyo Mtk wa Yesu katika Alhamisi ya Sikukuu ya Ekaristi Takatifu (Corpus Christi), yaani Alhamisi ya wiki moja kabla ya Sikukuu ya Moyo Mtk (au Alhamisi baada ya Sikukuu ya Utatu Mtk). Endapo Sikukuu hii itaadhimishwa siku ya Dominika inayofuata Sikukuu yenyewe kama inavyofanyika mahali pengi, basi novena inatakiwa ianze Ijumaa ya baada ya Sikukuu ya Utatu Mtk ili imalizike Jumamosi kabla ya Dominika ya sikukuu hii ya Moyo Mtk kwa Yesu.

WIMBO:

YESU KRISTU TWASIFU MOYO WAKO
Yesu Kristu, twasifu Moyo wako, sisi sote, milele mali yako
Tunakupa, nyoyo zote zetu, Mukombozi, Mfalme Mungu wetu;
Tunakupa, nyoyo zote zetu, Mukombozi, Mfalme Mungu wetu!

Watu wengi, wanakaa ugenini, wazunguka, wenye ukiwa chini,
Uwatie huruma yako kuu, roho zao, uziinue juu;
Uwatie huruma yako kuu, roho zao, uziinue juu!

Uwe Mfalme, wa wale washikwao, na ushenzi, na ukaidi wao
Wapelekee ufalme wa Mungu, ni Mchunga mmoja Zizi moja tu;
Wapelekee ufalme wa Mungu, ni Mchunga mmoja Zizi moja tu!

SALA YA KUTUBU

Mungu wangu ninatubu sana, niliyokosa kwako, kwani ndiwe mwema, ndiwe mwenye kupendeza, wachukizwa na dhambi, basi sitaki kukosa tena, nitafanya kitubio, naomba neema yako nipate kurudi wkako. Amina.

ROZARI YA MOYO MTAKATIFU WA YESU

Tumia tasbihi ya kawaida yenye chembe ndogo 53.
Kwenye Msalaba Sali:

“Ee Yesu tupe moyo wako kama amana ya upendo wako na kimbilio letu, ili tupate pumziko salama wakati wa maisha yetu na faraja tamu saa ya kufa kwetu”.
Baba Yetu ……..
Salamu Maria ……. (mara tatu)
Nasadiki ………..

Kwenye chembe kubwa Sali (Badala ya ‘Baba Yetu’):
“Ninakuabudu, ninakutukuza na ninakupenda, Ee Moyo wa Yesu wangu mpenzi, uliopenywa na huzuni nyingi kwa ajili ya dhambi, ambazo zimekuwa zikitendwa hata leo, dhidi ya Sakramenti Takatifu sana ya Altare. Ninakutolea hapo kwa kuridhika, moyo wa Mama yako mpendevu, na mastahili ya watakatifu. Amina”.

Kwenye chembe ndogo sali (Badala ya ‘Salamu Maria’):
“Ee Moyo Mtakatifu wa Yesu, uwakao mapendo kwetu, washa nyoyo zetu kwa mapendo yako”

LITANIA YA MOYO MTAKATIFU WA YESU

Bwana utuhurumie Bwana utuhurumie
Kristo utuhurumie Kristo utuhurumie
Bwana utuhurumie Bwana utuhurumie
Kristo utusikie Kristo utusikilize
Baba wa mbinguni Mungu Utuhurumie
Mwana, Mkombozi wa dunia Mungu Utuhurumie
Roho Mtakatifu Mungu Utuhurumie
Utatu Mtakatifu Mungu mmoja Utuhurumie
Moyo wa Yesu Mwana wa Baba wa Milele Utuhurumie
Moyo wa Yesu uliotungwa na Roho Mtakatifu mwilini mwa Mama Bikira Maria Utuhurumie
Moyo wa Yesu ulioungana na Neno wa Mungu Utuhurumie
Moyo wa Yesu ulio na utukufu pasipo mfano Utuhurumie
Moyo wa Yesu, hekalu takatifu la Mungu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, hema la Yule aliye juu Utuhurumie
Moyo wa Yesu tanuru lenye kuwaka mapendo Utuhurumie
Moyo wa Yesu, nyumba ya Mungu na mlango wa Mbingu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, tanuru yenye kuwaka mapendo Utuhurumie
Moyo wa Yesu, chombo cha haki na upendo Utuhurumie
Moyo wa Yesu, unaojaa upendo na wema Utuhurumie
Moyo wa Yesu, kilindi cha fadhila zote Utuhurumie
Moyo wa Yesu, unaostahili sifa zote Utuhurumie
Moyo wa Yesu, unaotawala mioyo yote Utuhurumie
Moyo wa Yesu, zinamokaa hazina za hekima na elimu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, uliopendelewa na Mungu Baba Utuhurumie
Moyo wa Yesu, uliotuenezea maziada yake Utuhurumie
Moyo wa Yesu, mtamaniwa wa vilima vya milele Utuhurumie
Moyo wa Yesu, wenye uvumilivu na huruma nyingi Utuhurumie
Moyo wa Yesu, tajiri kwa wote wenye kukuomba Utuhurumie
Moyo wa Yesu, chemchemi ya uzima na utakatifu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, malipo kwa dhambi zetu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, ulioshibishwa matusi Utuhurumie
Moyo wa Yesu, uliovunjika kwa sababu ya ubaya wetu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, uliotii mpaka kufa Utuhurumie
Moyo wa Yesu, uliochomwa kwa mkuki Utuhurumie
Moyo wa Yesu, chemchemi ya faraja zote Utuhurumie
Moyo wa Yesu, uzima na ufufuo wetu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, amani na upatanisho wetu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, sadaka ya wakosefu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, unamokaa wokovu wao wenye kukutumaini Utuhurumie
Moyo wa Yesu, matumaini yao wenye kuzimia kwako Utuhurumie
Moyo wa Yesu, sababu ya furaha ya watakatifu wote Utuhurumie
Mwanakondoo wa Mungu, uondoaye dhambi za dunia Utusamehe Bwana
Mwanakondoo wa Mungu, uondoaye dhambi za dunia Utusikilize Bwana
Mwanakondoo wa Mungu, uondoaye dhambi za dunia Utuhurumie

Kiongozi: Yesu mwenye Moyo mpole na mnyenyekevu,
Wote: Ufanye mioyo yetu ifanane na Moyo wako

TUOMBE: (W) Ee Mungu Mwenyezi milele, uuangalie Moyo wa mwanao mpendelevu, pia na heshima na malipo aliyokutolea kwa ajili ya wenye dhambi, uridhike, uwaondolee wenye kuomba toba kwako kwa njia ya huyo Mwanao Yesu Kristo anayeishi na kutawala nawe pamoja na Roho Mtakatifu, Mungu milele. Amina.

P.S. Mwezi wa sita ni wa kuuheshimu Moyo Mtakatifu wa Yesu. Vitu vya kufanya ni pamoja na kushiriki Misa takatifu kila siku, kumtembelea Bwana Yesu katika Ekaristia, kusali Rozari ya Moyo Mtakatifu wa Yesu kila siku, kusali Litania za Moyo Mtakatifu wa Yesu, kuimba nyimbo za kuusifu Moyo Mtakatifu wa Yesu, na kadhalika. Kwa kufanya hayo na mengineyo yanayofanana nayo, waumini hujichotea Baraka na neema nyingi za kimwili na kiroho.

SALA YA NOVENA

Ee Moyo Mtakatifu sana wa Yesu, chemchemi ya kila baraka, ninakuabudu, ninakupenda, na kwa majuto halisi ya dhambi zangu, nakutolea moyo wangu dhaifu. Nifanye mnyenyekevu, mvumilivu na safi, nikikubali na kuyatii kabisa mapenzi yako. Ee Yesu mwema, unijalie niishi nawe na kwa ajili yako. Unilinde niwapo katikati ya hatari, unifariji katika mateso, unipe afya ya mwili na msaada katika mahitaji ya mwili, Baraka yako juu ya kila nilifanyalo, na neema ya kifo chema. Amina.

Ee Yesu uliyesema “Kweli nawaambieni, ombeni nanyi mtapewa, tafuteni nanyi mtapata, gongeni nanyi mtafunguliwa”, tazama ninagonga, ninatafuta na kuomba …….. (Taja ombi lako)
Baba Yetu….., Salamu Maria …….., Atukuzwe Baba……..
Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutumainia kwa moyo wote!

Ee Yesu uliyesema “Kweli nawaambieni, chochote mtakachomwomba Baba kwa jina langu mtapewa”, tazama kwa jina lako ninaomba ……. (Taja ombi lako)
Baba Yetu….., Salamu Maria …….., Atukuzwe Baba……..
Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutumainia kwa moyo wote!

Ee Yesu uliyesema “Kweli nawaambieni, mbingu na dunia zitapita lakini maneno yangu hayatapita kamwe”, tazama, nikitiwa nguvu na maneno yako ya kweli ninaomba …….. (Taja ombi lako)
Baba Yetu….., Salamu Maria …….., Atukuzwe Baba……..
Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutumainia kwa moyo wote!

Ee Moyo Mtakatifu wa Yesu, ambaye kwako ni kitu kimoja tu kisichowezekana, ambacho ni kutoacha kutowaonea huruma wenye huzuni, utuhurumie sisi wakosefu maskini na utujalie neema tukuombayo kwa njia ya Moyo Imakulata wa Maria, Mama yetu mpole.

Sali ‘Salamu Malkia’ na kuongezea, ‘Mtakatifu Yosefu Baba Mlishi wa Yesu, utuombee’.

P.S. – Sala hii ya Novena ilisaliwa kila siku na PADRE PIO kwa ajili ya kuwaombea wale wote waliomwomba msaada wa sala zake. Unaweza kuisali kwa namna tofauti tofauti. Mfano, kama Novena ya siku tisa, ambapo unasali sala hii mara moja au zaidi kila siku kwa siku tisa, au unaweza kuifanya kama Novena ya masaa, ambapo unasali sala hii kila baada ya saa moja kwa masaa tisa kwa siku hiyo hiyo, hasa kama kitu unachokiomba ni cha haraka au umesongwa moyoni. Vilevile unaweza kuifanya sala hii kama sehemu ya sala zako za kila siku katika mwezi Juni ambao ni mwezi uliotengwa na Kanisa kwa ajili ya kuuheshimu Moyo Mtakatifu wa Yesu, na hapo utaitumia kuwaombea watu waliokuomba msaada wa sala zako kama alivyofanya Mtakatifu Padre Pio. Pia unaweza kuitumia kama sala yako ya siku zote au ya mara kwa mara kwa ajili ya mahitaji mbalimbali.

SALA YA MAOMBI

Ee Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakukimbilia, ninakuja kwako katika mikono yako yenye huruma. Ndiwe tegemeo langu na tumaini langu dhabiti. Ndiwe mwenye dawa ya maovu yangu yote, malipizi ya makosa yangu yote. Waweza kunipatia haja zangu na neema ninazoziomba mimi na wengine. Wewe uko ili kutusaidia sote, ndiwe mwanga mkuu usiozimika, ndiwe chanzo cha nguvu, uvumilivu, amani na faraja. Nina hakika kuwa maombi yangu hayatakuchosha, nawe hutaacha kunisaidia, kunilinda, kunipenda, kwani, ee Moyo Mtakatifu , upendo wako hauna mwisho. Ee Moyo Mtakatifu, unihurumie, kwa ajili ya maombi yangu, kadiri ya huruma yako. Nawe katika sisi, na kwa ajili yetu, ufanye lolote unalolihitaji, kwani tunajitoa kwako kwa imani na uhakika thabiti kwamba kamwe hautatuacha, kwa milele. Amina.

SALA YA MAJITOLEO KWA MAMA WA HUZUNI

Mama Mtakatifu, Mama wa Mungu na Malkia wa Mashahidi, leo nakuchagua Wewe uwe mfano wangu, mkingaji na mteteaji wangu. Naweka roho fukara katika moyo wako uliotobolewa na panga nyingi za mateso. Unipokee mimi niwe mtumishi wako wa pekee na mshiriki wa mateso yako. Nijalie nguvu niwe daima karibu na msalaba ule alikosulibiwa Yesu. Nakutolea nafsi yangu na mali yangu yote. Pokea kila tendo langu jema ukalisindikize kwa Mwanao, Mama, nifanye nistahili kuitwa mtumishi wa Maria, Simama karibu yangu katika matendo yangu yote ili yafanwe kwa sifa ya Mungu. Ulivyosimama karibu kabisa ya Mwanao alipokufa msalabani uwe karibu nami saa ya kufa kwangu. Nijalie niweze kutaja jina lako na la Mwana wako nikisema: “Yesu, Maria na Yosef mnisaidie saa ya kufa kwangu. Yesu, maria na Yosef, naomba nife kwa amani kati yenu!” . Amina.

Rozari ya Malaika Mkuu Mikaeli

Rozari ya Malaika Mkuu Mikaeli ni sala nzuri sana ya kumheshimu huyu Malaika Mkuu pamoja na makundi yote tisa ya Malaika. Kuendana na jinsi tunavyofunuliwa katika Maandiko Matakatifu, makundi haya tofauti tofauti ya Malaika hujipanga kuanzia karibu sana na Kiti cha Enzi alipo Mwenyezi Mungu, kwenda chini tulipo sisi wanadamu. Makundi hayo kuanzia juu kwenda chini ni Maserafi, Makerubi, Wenye Enzi, Watawala, Wenye Nguvu, Wenye Mamlaka, Wakuu, Malaika Wakuu na Malaika.

Asili ya Rozari hii ni maono aliyopata Mtumishi wa Mungu Antonia d’Astonac, ambaye alitokewa na Malaika Mkuu Mikaeli aliyemfundisha sala za Rozari hii kwa kumwelekeza kuwa anataka aheshimiwe kwa salamu tisa kufuatana na makundi tisa ya Malaika.

Mtakatifu Mikaeli Malaika Mkuu aliahidi kuwa yeyote anayefanya ibada hii kwa heshima, akaribiapo Meza Takatifu, atasindikizwa na Malaika tisa, mmoja kutoka kila kundi la Malaika. Zaidi ya hayo, kwa kusali rozari hii, aliahidi msaada wa daima, na kwamba Malaika watamsaidia mwenye kuisali duniani na kumtoa toharani akifariki, yeye pamoja na jamaa zake.

ROZARI YA MALAIKA MKUU MIKAELI

Ee Mungu unielekezee msaada, Ee Bwana unisaidie hima!
Atukuzwe Baba na Mwana na Roho Mtakatifu, kama mwanzo na sasa na siku zote, na milele. Amina.

Sali Baba Yetu (mara nne) kwa heshima ya Malaika Wakuu, Mtakatifu Mikaeli, Mtakatifu Gabriel, Mtakatifu Rafaeli na Malaika Mlinzi.

1. Kwa heshima ya Malaika Mkuu Mtakatifu Mikaeli; Baba Yetu uliye mbinguni, Jina lako litukuzwe, ufalme wako ufike, utakalo lifanyike duniani kama mbinguni, utupe leo mkate wetu wa kila siku, utusamehe makosa yetu, kama tunavyowasamehe na sisi waliotukosea. Usitutie katika kishawishi, lakini utuopoe maovuni. Amina
2. Kwa heshima ya Malaika Mkuu Mtakatifu Gabrieli; Baba Yetu, …..
3. Kwa heshima ya Malaika Mkuu Mtakatifu Rafaeli; Baba Yetu, …..
4. Kwa heshima ya Malaika Wangu Mlinzi; Baba Yetu, ……

Sali Baba Yetu moja na Salamu Maria tatu baada ya kila salamu katika tisa zifuatazo kwa heshima ya Makundi Tisa ya Malaika

Baba Yetu (mara moja, – tazama hapo juu)

Salamu Maria
Salamu Maria umejaa neema, Bwana yu nawe, umebarikiwa kuliko wanawake wote, na Yesu Mzao wa tumbo lako amebarikiwa. Maria Mtakatifu, Mama wa Mungu, utuombee sisi wakosefu, sasa na saa ya kufa kwetu, Amina.

1. Kwa maombezi ya Mtakatifu Mikaeli na ya kundi la Serafin, Bwana awashe mioyoni mwetu moto wa mapendo kamili. Amina.
Baba Yetu (mara moja), Salamu Maria (mara tatu)

2. Kwa maombezi ya Mtakatifu Mikaeli na ya Kundi la Kerubin, Bwana atuwezeshe kuacha njia mbaya na kuenenda katika njia ya ukamilifu wa kiKristo. Amina.
Baba Yetu (mara moja), Salamu Maria (mara tatu)

3. Kwa maombezi ya Mtakatifu Mikaeli na ya Kundi la Wenye Enzi, Bwana atujalie roho ya unyofu na unyenyekevu wa kweli. Amina
Baba Yetu (mara moja), Salamu Maria (mara tatu)

4. Kwa maombezi ya Mtakatifu Mikaeli na ya Kundi la Watawala, Bwana atujalie neema ya kushinda maasi yetu na tamaa mbaya. Amina
Baba Yetu (mara moja), Salamu Maria (mara tatu)

5. Kwa maombezi ya Mtakatifu Mikaeli na ya Kundi la Wenye Nguvu, Bwana atukinge na vishawishi na mitego ya shetani. Amina
Baba Yetu (mara moja), Salamu Maria (mara tatu)

6. Kwa maombezi ya Mtakatifu Mikaeli na ya Kundi la Wenye Mamlaka, Bwana atukinge na mwovu wala tusianguke vishawishini. Amina
Baba Yetu (mara moja), Salamu Maria (mara tatu)

7. Kwa maombezi ya Mtakatifu Mikaeli na ya Kundi la Wakuu, Bwana atujalie kuwa na roho ya utii wa kweli. Amina
Baba Yetu (mara moja), Salamu Maria (mara tatu)

8. Kwa maombezi ya Mtakatifu Mikaeli na ya Kundi la Malaika Wakuu, Bwana atudumishe katika imani na katika kazi zote njema ili tujaliwe utukufu wa Milele. Amina.
Baba Yetu (mara moja), Salamu Maria (mara tatu)

9. Kwa maombezi ya Mtakatifu Mikaeli na ya Kundi la Malaika, Bwana atujalie ulinzi wao duniani hapa na baadaye watuongoze kwenye furaha za Mbinguni. Amina.
Baba Yetu (mara moja), Salamu Maria (mara tatu)

SALA MBELE YA KITI CHA ENZI CHA MUNGU

Sali Atukuzwe 7 kwa heshima ya Malaika 7 wateule ujipatie neema ya kuepa dhambi mbaya saba na kutujaza mapaji saba ya Roho Mtakatifu.

TUOMBE
Ee Mungu Mwenyezi wa milele, kwa wema na huruma yako ya ajabu, umetaka watu wako waokoke, ukamweka Malaika Mkuu Mikaeli kuwa Mkuu wa Kanisa lako, Utukinge na adui zetu, wasitusmbue saa ya kufa kwetu, bali tuongozwe naye kwenye utukufu wako Mkuu. Tunaomba hayo kwa njia ya Bwana Wetu Yesu Kristo. Amina.

Utuombee Ee Mtukufu Mtakatifu Mikaeli Mkuu wa Kanisa la Yesu Kristo, tujaliwe ahadi za Kristo. Amina.

SALA KWA MTAKATIFU MIKAELI MALAIKA MKUU

Mtakatifu Mikaeli Malaika Mkuu, utulinde katika vita, uwe kinga yetu katika maovu na maoteo ya shetani, Mungu amtiishe, tunaomba sana, nawe Mkuu wa Majeshi ya Mbinguni kwa nguvu ya Mungu uwaangushe motoni shetani na pepo wabaya wengine wote, wanaozunguka duniani, ili kuzipoteza roho za watu.
Amina.

SALA KWA MALAIKA WAKO MLINZI

Malaika wa Mungu Mlinzi wangu mpenzi,
Ambaye upendo wake unanifanya niwepo hapa,
Uwe nami leo hii,
Kuniangaza na kunilinda,
Kunitawala na kuniongoza.
Amina.

SALA NYINGINE KWA MALAIKA WAKO MLINZI

Ee Malaika wangu Mlinzi, uliyewekwa na Mungu Mwema, naomba unilinde katika hatari zote za roho na za mwili. Amina

Sali mara kwa mara unapokumbuka, hasa asubuhi uamkapo na usiku kabla ya kulala, Atukuzwe mara saba, kwa heshima ya Malaika wako Mlinzi.

SALA YA KUWAOMBEA MAPADRE

Ee Bwana Yesu Kristo. Mkombozi wetu, kwa mapendo na tamaa yako ya kutaka kulinda vema Kanisa lako, ukachagua Mapadri wawe Wachungaji na Viongozi wa roho za watu. Nakuomba sana; ubariki nia na bidii inayowapasa Mapadri wote katika kazi zao. Uwaongezee Utakatifu.

Uwatie moyo mzuri wenye mapendo makubwa kwako na roho za watu. Hivyo wakiisha kupata wenyewe Utakatifu, waweze kuwaongoza vizuri watu walio chini ya ulinzi wao, katika njia ya Utakatifu na furaha ya milele. Uwajalie neema zote za hali ya Upadri. Uwajalie ili waonyeshe kila siku ya maisha yao mfano wa kila fadhila ya mapendo na ya uaminifu katika Kanisa, kwa Baba Mtakatifu na kwa Maaskofu.

Yesu mpendelevu, uangalie kwa mapendo kazi na mateso ya Mapadri wako; ubariki na ustawishe mafundisho yao; wanapowafundisha watoto, wanapowahubiria watu, wanapowatuliza wakosefu watubu na wanapowasaidia wagonjwa na wale wanaokaribia mauti, Ee Yesu uwe pamoja nao. Uwakinge na hatari zote za roho na za mwili.

Mwokozi Yesu, ulijalie Kanisa liwe na Mapadri wengi walio Watakatifu. Uwajalie watoto na vijana wengi wasikie wito wa Upadri, uwatie furaha na Utakatifu na roho za Mapadri waliokufa uzijalie punziko la amani.

Kwa mimi mwenyewe Ee Yesu mpendelevu, naomba unijalie roho ya imani na utii mnyenyekevu ili niwaheshimu Mapadri kama Mawakili wa Mungu. Niwatii katika njia zote za wokovu wa roho yangu. Amina.

Majitoleo kwa Bikira Maria

(Sala iliyotungwa na Mtk. Aloisi)
Bibi yangu mtukufu Maria, nakuwekea amana ya roho yangu na mwili wangu, nikikuomba uipokee amana yangu, kuitunzia ulinzi mwema ulinzi bora, ninakuaminia na kila neno langu, matumaini na kitulizo na kisongo chote, na masumbuko na uzima na ukomo wa uzima wangu: nitakayo ndiyo unifanyizie kwa maombezi na stahili zako, ili mambo yangu yote yapate kuongoka, yakiwa na kufuata mapenzi yako, pamoja na mapenzi ya Mwanao. Amina.

Shopping Cart
33
    33
    Your Cart
    🏠 Home 📖 Reading 🖼️ Gallery 💬 AI Chat 📘 About