Sala za Katoliki: Sala Muhimu Kwa Mkristu Mkatoliki

SALA YA UHAI KWA MT. YOSEFU

(Sala hii inafaa sana kwa ajili ya kutetea uhai wa watoto wachanga wakiwa tumboni mwa mama zao, dhidi ya utoaji mimba au hatari nyingine dhidi ya uhai wa binadamu)

Ee Mt. Yosefu, wewe ni Mchumba safi na Mpenzi wa Bikira Maria, u Baba Mlishi wa Yesu, mlinzi na mtunzaji wa Familia Takatifu, na wa familia zote. Tuna imani kabisa katika uangalizi wako uliojaa upendo, juu ya uhai mpya, na uaminifu wako kwa familia.

Tunaweka jitihada zetu chini ya ulinzi wa sala zako. Utusaidie daima katika kutetea zawadi ya uhai wa binadamu, ili ukue hadi uzima wa milele ulioahidiwa na kujaliwa kwetu na Mwanao, Ndugu yetu, Yesu Kristu.
Amina.

SALA YA KUWAOMBEA MAPADRE

Ee Bwana Yesu Kristo. Mkombozi wetu, kwa mapendo na tamaa yako ya kutaka kulinda vema Kanisa lako, ukachagua Mapadri wawe Wachungaji na Viongozi wa roho za watu. Nakuomba sana; ubariki nia na bidii inayowapasa Mapadri wote katika kazi zao. Uwaongezee Utakatifu.

Uwatie moyo mzuri wenye mapendo makubwa kwako na roho za watu. Hivyo wakiisha kupata wenyewe Utakatifu, waweze kuwaongoza vizuri watu walio chini ya ulinzi wao, katika njia ya Utakatifu na furaha ya milele. Uwajalie neema zote za hali ya Upadri. Uwajalie ili waonyeshe kila siku ya maisha yao mfano wa kila fadhila ya mapendo na ya uaminifu katika Kanisa, kwa Baba Mtakatifu na kwa Maaskofu.

Yesu mpendelevu, uangalie kwa mapendo kazi na mateso ya Mapadri wako; ubariki na ustawishe mafundisho yao; wanapowafundisha watoto, wanapowahubiria watu, wanapowatuliza wakosefu watubu na wanapowasaidia wagonjwa na wale wanaokaribia mauti, Ee Yesu uwe pamoja nao. Uwakinge na hatari zote za roho na za mwili.

Mwokozi Yesu, ulijalie Kanisa liwe na Mapadri wengi walio Watakatifu. Uwajalie watoto na vijana wengi wasikie wito wa Upadri, uwatie furaha na Utakatifu na roho za Mapadri waliokufa uzijalie punziko la amani.

Kwa mimi mwenyewe Ee Yesu mpendelevu, naomba unijalie roho ya imani na utii mnyenyekevu ili niwaheshimu Mapadri kama Mawakili wa Mungu. Niwatii katika njia zote za wokovu wa roho yangu. Amina.

SALA YA KUMWOMBA MTAKATIFU TERESIA WA MTOTO YESU

Ee Mtakatifu Teresia wa mtoto Yesu, ulistahili kuitwa Msimamizi wa misioni katoliki za dunia yote. Kumbuka ile tamaa yako kuu uliyoonyesha huku duniani ya ” kusimika Msalaba wa Yesu Kristu, katika nchi zote na kuhubiri Injili mpaka mwisho wa dunia” . Twakuomba kwa ajili ya maagano yako, wasaidie mapadre, wamisionari, na kanisa zima.

Ee Mtakatifu Teresia wa mtoto Yesu ” Msimamizi wa misioni” UTUOMBEE

Rozari ya Malaika Mkuu Mikaeli

Rozari ya Malaika Mkuu Mikaeli ni sala nzuri sana ya kumheshimu huyu Malaika Mkuu pamoja na makundi yote tisa ya Malaika. Kuendana na jinsi tunavyofunuliwa katika Maandiko Matakatifu, makundi haya tofauti tofauti ya Malaika hujipanga kuanzia karibu sana na Kiti cha Enzi alipo Mwenyezi Mungu, kwenda chini tulipo sisi wanadamu. Makundi hayo kuanzia juu kwenda chini ni Maserafi, Makerubi, Wenye Enzi, Watawala, Wenye Nguvu, Wenye Mamlaka, Wakuu, Malaika Wakuu na Malaika.

Asili ya Rozari hii ni maono aliyopata Mtumishi wa Mungu Antonia d’Astonac, ambaye alitokewa na Malaika Mkuu Mikaeli aliyemfundisha sala za Rozari hii kwa kumwelekeza kuwa anataka aheshimiwe kwa salamu tisa kufuatana na makundi tisa ya Malaika.

Mtakatifu Mikaeli Malaika Mkuu aliahidi kuwa yeyote anayefanya ibada hii kwa heshima, akaribiapo Meza Takatifu, atasindikizwa na Malaika tisa, mmoja kutoka kila kundi la Malaika. Zaidi ya hayo, kwa kusali rozari hii, aliahidi msaada wa daima, na kwamba Malaika watamsaidia mwenye kuisali duniani na kumtoa toharani akifariki, yeye pamoja na jamaa zake.

ROZARI YA MALAIKA MKUU MIKAELI

Ee Mungu unielekezee msaada, Ee Bwana unisaidie hima!
Atukuzwe Baba na Mwana na Roho Mtakatifu, kama mwanzo na sasa na siku zote, na milele. Amina.

Sali Baba Yetu (mara nne) kwa heshima ya Malaika Wakuu, Mtakatifu Mikaeli, Mtakatifu Gabriel, Mtakatifu Rafaeli na Malaika Mlinzi.

1. Kwa heshima ya Malaika Mkuu Mtakatifu Mikaeli; Baba Yetu uliye mbinguni, Jina lako litukuzwe, ufalme wako ufike, utakalo lifanyike duniani kama mbinguni, utupe leo mkate wetu wa kila siku, utusamehe makosa yetu, kama tunavyowasamehe na sisi waliotukosea. Usitutie katika kishawishi, lakini utuopoe maovuni. Amina
2. Kwa heshima ya Malaika Mkuu Mtakatifu Gabrieli; Baba Yetu, …..
3. Kwa heshima ya Malaika Mkuu Mtakatifu Rafaeli; Baba Yetu, …..
4. Kwa heshima ya Malaika Wangu Mlinzi; Baba Yetu, ……

Sali Baba Yetu moja na Salamu Maria tatu baada ya kila salamu katika tisa zifuatazo kwa heshima ya Makundi Tisa ya Malaika

Baba Yetu (mara moja, – tazama hapo juu)

Salamu Maria
Salamu Maria umejaa neema, Bwana yu nawe, umebarikiwa kuliko wanawake wote, na Yesu Mzao wa tumbo lako amebarikiwa. Maria Mtakatifu, Mama wa Mungu, utuombee sisi wakosefu, sasa na saa ya kufa kwetu, Amina.

1. Kwa maombezi ya Mtakatifu Mikaeli na ya kundi la Serafin, Bwana awashe mioyoni mwetu moto wa mapendo kamili. Amina.
Baba Yetu (mara moja), Salamu Maria (mara tatu)

2. Kwa maombezi ya Mtakatifu Mikaeli na ya Kundi la Kerubin, Bwana atuwezeshe kuacha njia mbaya na kuenenda katika njia ya ukamilifu wa kiKristo. Amina.
Baba Yetu (mara moja), Salamu Maria (mara tatu)

3. Kwa maombezi ya Mtakatifu Mikaeli na ya Kundi la Wenye Enzi, Bwana atujalie roho ya unyofu na unyenyekevu wa kweli. Amina
Baba Yetu (mara moja), Salamu Maria (mara tatu)

4. Kwa maombezi ya Mtakatifu Mikaeli na ya Kundi la Watawala, Bwana atujalie neema ya kushinda maasi yetu na tamaa mbaya. Amina
Baba Yetu (mara moja), Salamu Maria (mara tatu)

5. Kwa maombezi ya Mtakatifu Mikaeli na ya Kundi la Wenye Nguvu, Bwana atukinge na vishawishi na mitego ya shetani. Amina
Baba Yetu (mara moja), Salamu Maria (mara tatu)

6. Kwa maombezi ya Mtakatifu Mikaeli na ya Kundi la Wenye Mamlaka, Bwana atukinge na mwovu wala tusianguke vishawishini. Amina
Baba Yetu (mara moja), Salamu Maria (mara tatu)

7. Kwa maombezi ya Mtakatifu Mikaeli na ya Kundi la Wakuu, Bwana atujalie kuwa na roho ya utii wa kweli. Amina
Baba Yetu (mara moja), Salamu Maria (mara tatu)

8. Kwa maombezi ya Mtakatifu Mikaeli na ya Kundi la Malaika Wakuu, Bwana atudumishe katika imani na katika kazi zote njema ili tujaliwe utukufu wa Milele. Amina.
Baba Yetu (mara moja), Salamu Maria (mara tatu)

9. Kwa maombezi ya Mtakatifu Mikaeli na ya Kundi la Malaika, Bwana atujalie ulinzi wao duniani hapa na baadaye watuongoze kwenye furaha za Mbinguni. Amina.
Baba Yetu (mara moja), Salamu Maria (mara tatu)

SALA MBELE YA KITI CHA ENZI CHA MUNGU

Sali Atukuzwe 7 kwa heshima ya Malaika 7 wateule ujipatie neema ya kuepa dhambi mbaya saba na kutujaza mapaji saba ya Roho Mtakatifu.

TUOMBE
Ee Mungu Mwenyezi wa milele, kwa wema na huruma yako ya ajabu, umetaka watu wako waokoke, ukamweka Malaika Mkuu Mikaeli kuwa Mkuu wa Kanisa lako, Utukinge na adui zetu, wasitusmbue saa ya kufa kwetu, bali tuongozwe naye kwenye utukufu wako Mkuu. Tunaomba hayo kwa njia ya Bwana Wetu Yesu Kristo. Amina.

Utuombee Ee Mtukufu Mtakatifu Mikaeli Mkuu wa Kanisa la Yesu Kristo, tujaliwe ahadi za Kristo. Amina.

SALA KWA MTAKATIFU MIKAELI MALAIKA MKUU

Mtakatifu Mikaeli Malaika Mkuu, utulinde katika vita, uwe kinga yetu katika maovu na maoteo ya shetani, Mungu amtiishe, tunaomba sana, nawe Mkuu wa Majeshi ya Mbinguni kwa nguvu ya Mungu uwaangushe motoni shetani na pepo wabaya wengine wote, wanaozunguka duniani, ili kuzipoteza roho za watu.
Amina.

SALA KWA MALAIKA WAKO MLINZI

Malaika wa Mungu Mlinzi wangu mpenzi,
Ambaye upendo wake unanifanya niwepo hapa,
Uwe nami leo hii,
Kuniangaza na kunilinda,
Kunitawala na kuniongoza.
Amina.

SALA NYINGINE KWA MALAIKA WAKO MLINZI

Ee Malaika wangu Mlinzi, uliyewekwa na Mungu Mwema, naomba unilinde katika hatari zote za roho na za mwili. Amina

Sali mara kwa mara unapokumbuka, hasa asubuhi uamkapo na usiku kabla ya kulala, Atukuzwe mara saba, kwa heshima ya Malaika wako Mlinzi.

SALA MBELE YA SAKRAMENTI KUU II

Yesu, Mungu wangu mpenzi,/ upo hapa katika Altare mbele yangu;/ na mimi napiga magoti mbele yako.// Waniangalia sana,/ siyo kwa kunipeleleza,/ lakini kwa sababu wapenda kuniona hivi karibu na wewe,/ wafurahiwa nikija kukuabudu./ Wayasikiliza maneno yangu yote/ yenye kutoka mdomoni mwangu,/ na zaidi wapokea maneno yangu yanayotoka moyoni./ Nataka kuzungumza na wewe peke yako,/ na kusahau mambo mengine yote/ na watu wengine walioko kanisani pamoja nami./

Yesu wangu,/ nakushukuru/ kwa sababu umekubali kutupa Sakramenti hii kuu kabisa,/ ukitaka kukaa pamoja na sisi,/ na hata ukakubali kuwa chakula chetu/ chenye nguvu ya ajabu./ Mfalme wangu Yesu,/ Sultani wangu Mkuu,/ naamini kabisa kwamba upo katika Altare/ na kwamba umejificha chini ya umbo la mkate./ Ulipokuwapo bado hapa duniani mbele za watu,/ ulikuwa hujifichi kama sasa;/ lakini hata siku zile/ watu hawakuweza kukuona vile ulivyo./ Hawakuweza kuutambua Umungu wako,/ ikalazimu kukuamini tu sawa kama sisi./ Wakainama kichwa wakisema,/ “Bwana wangu na Mungu wangu”./ Na mimi kadhalika naungama/ U Bwana wangu na Mungu wangu/ na Mkombozi wangu/ na salama yangu yote./ U Yesu wangu tu,/ siwezi kusema zaidi./ Nakuabudu ee Yesu./ Najua sana, mimi ni mdogo kabisa,/ sina maana hata kidogo./ Mimi ni dhaifu na maskini mno./ Lakini Wewe katika hruuma yako kubwa/ waniita nije kwako./ Wewe huuangalii umaskini wangu,/ bali wanivuta katika mapendo yako./

Nasikia maneno yako usemayo:/ “Njooni kwangu ninyi nyote mnaoelemewa na mizigo/ nami nitawasaidia”./ Kwa ajili ya maneno hayo/ nakuja kwako bila hofu./ Najua kwamba wanipenda,/ najua wataka kunisaidia na kuniponya,/ najua kuwa wataka kunitakasa./

Nahitaji sana msaada wako, hakika./ Unaniona katika mwendo wangu wa kila siku,/ Jinsi ninavyohangaika na vishawishi mara nyingi;/ jinsi nilivyo na lazima ya kushindana kila siku/ nikitaka kukaa mwema na safi katika utumishi wako./ Naungama mbele yako Wewe Mkombozi wangu,/ kwamba sikukaa imara siku zote vile nilivyopaswa./ Naungama kwamba nimeshindwa mara nyingine/ na kwa hivi naomba toba./ Lakini kwa nini nimeshindwa mara nyingine?/ Kwa nini nikakosa?/ Ni kwa sababu nalikuwa nimekwenda mbali nawe;/ nalianza kujitegemea mwenyewe./ Katika majivuno yangu nikajisifu mwenyewe,/ nikajiona mwema,/ nikasahau udhaifu wangu./ Na kwa ajili hiyo nikajitia katika hatari bure,/ sikujilinda tena,/ nikampa shetani nafasi ya kunishambulia kwa hila zake zote./ Unihurumie ee Yesu wangu./

Sasa nafahamu jinsi nilivyokuwa mjinga kwelikweli./ Ndiyo maana nakuabudu kwa moyo wangu wote./ Najiweka mikononi mwako/ ufanye nami vile unavyotaka./ Wewe utanitunza;/ Wewe utanilinda vema;/ Wewe utaniongoza nijue namna ya kuepa hatari zote,/ na jinsi ya kufukuza kila kishawishi./ Chukua moyo wangu kabisa,/ kwa sababu ni mali yako kamili;/ Wewe ndiwe uliyeniumba,/ ndiwe uliyenipeleka katika Ukristo,/ nawe ndiwe utakayenihukumu siku ya mbele./ Ndivyo ninavyojitolea kwako./ Ndivyo ninavyokuabudu,/ wala sijui njia nyingine ya kukusifu zaidi./

Yesu wangu mpenzi,/ naomba upokee kwa uzuri heshima hiyo yangu./ Angalia: naitolea pamoja na heshima yote/ unayopewa daima na watakatifu wako/ na malaika wako./ Nikipiga magoti hapa mbele yako sasa,/ siko peke yangu,/ nakuabudu pamoja na Mama yako Bikira Maria,/ ambaye sala zake zinakupendeza kabisa./ Sala zangu naweka pamoja na sala zake yeye,/ uzipokee zote pamoja,/ zikupendeze zote sawa./ Ee Mama Maria!/ Nifundishe maneno ya kumsifu Mwanao Yesu vizuri./ Nipeleke kwa Yesu tumwabudu pamoja./ Nifunike na utakatifu wako/ kusudi Yesu asiangalie tena umaskini wangu/ na makosa yangu,/ aniponye katika huruma yake./

Sasa najisikia vizuri, Yesu wangu./ Sasa nina moyo wa kuweza kuendelea vema/ katika njia njema./ Sasa ninatumaini kwamba/ nitakaa mkristo mwema,/ nitakuwa mtumishi wako mwaminifu./ Nasikia amani kubwa sana moyoni mwangu,/ kwa kuwa nimo mikononi mwako./ Baada ya dakika chache/ nitaondoka tena kanisani,/ nitarudi nyumbani kwangu,/ lakini hatutaachana,/ hapana./ Mapendo yetu yatatuunganisha pamoja daima./ Wewe utanikumbuka nikiwa kazini,/ nikilala usingizi,/ nikienda njiani,/ kila mahali nilipo,/ Wewe utaniona,/ utafuatana na mimi./ Kadhalika nitakukumbuka tu./ Nitafanya bidii nisikuache kabisa./ Amina.

Litani ya Bikira Maria

  • Bwana utuhurumie
  • Bwana utuhurumie
  • Kristo utuhurumie
  • Bwana utuhurumie
  • Bwana utuhurumie
  • Kristo utusikie
  • Kristo utusikilize
  • Mungu Baba wa Mbinguni,…… Utuhurumie
  • Mungu Mwana Mkombozi wa dunia ……… Utuhurumie
  • Mungu Roho Mtakatifu …….. Utuhurumie
  • Utatu Mtakatifu Mungu Mmoja …….. Utuhurumie
  • Maria Mtakatifu ………. utuombee
  • Mzazi Mtakatifu wa Mungu …….. utuombee
  • Bikira Mtakatifu Mkuu wa Mabikira …….. utuombee
  • Mama wa Kristo ……… utuombee
  • Mama wa Neema ya Mungu ………….. utuombee
  • Mama Mtakatifu sana ……… utuombee
  • Mama mwenye usafi wa Moyo ……….. utuombee
  • Mama mwenye ubikira ……….. utuombee
  • Mama usiye na doa ……….. utuombee
  • Mama mpendelevu ………. utuombee
  • Mama mstajabivu ………. utuombee
  • Mama wa Muumba ………. utuombee
  • Mama wa Mkombozi ………….. utuombee
  • Mama wa Kanisa……….. utuombee
  • Bikira mwenye utaratibu ………….. utuombee
  • Bikira mwenye heshima ………….. utuombee
  • Bikira mwenye sifa ………….. utuombee
  • Bikira mwenye uwezo ………….. utuombee
  • Bikra mweye huruma ………….. utuombee
  • Bikra mwaminifu………….. utuombee
  • Kioo cha haki ………….. utuombee
  • Kikao cha hekima ………….. utuombee
  • Sababu ya furaha yetu ………….. utuombee
  • Chombo cha neema ………….. utuombee
  • Chombo cha kuheshimiwa ………….. utuombee
  • Chombo bora cha ibada ………….. utuombee
  • Waridi lenye fumbo ………….. utuombee
  • Mnara wa Daudi ………….. utuombee
  • Mnara wa pembe ………….. utuombee
  • Nyumba ya dhahabu ………….. utuombee
  • Sanduku la Agano ………….. utuombee
  • Mlango wa Mbingu ………….. utuombee
  • Nyota ya asubuhi ………….. utuombee
  • Afya ya wagonjwa ………….. utuombee
  • Kimbilio la wakosefu ………….. utuombee
  • Mtuliza wenye huzuni ………….. utuombee
  • Msaada wa waKristo ………….. utuombee
  • Malkia wa Malaika ………….. utuombee
  • Malkia wa Mababu ………….. utuombee
  • Malkia wa Manabii ………….. utuombee
  • Malkia wa Mitume ………….. utuombee
  • Malkia wa Mashahidi ………….. utuombee
  • Malkia wa Waungama dini ………….. utuombee
  • Malkia wa Mabikira ………….. utuombee
  • Malkia wa Watakatifu wote ………….. utuombee
  • Malkia uliyepalizwa Mbinguni ………….. utuombee
  • Malkia wa Rozari takatifu ………….. utuombee
  • Malkia wa amani ………….. utuombee

  • Mwanakodoo wa Mungu uondoaye dhambi za dunia,…………..Utusamehe ee Bwana.
  • Mwanakondoo wa Mungu uondoaye dhambi za dunia,…………..Utusikilize ee Bwana
  • Mwanakondoo wa Mungu uondoaye dhambi za dunia,…………..Utuhurumie.

  • Utuombee, Mzazi Mtakatifu wa Mungu,…………..Tujaliwe ahadi za Kristo.

Tuombe

Ee Bwana Mungu, utujalie sisi watumishi wako afya ya roho na mwili siku zote; na kwa maombezi matukufu ya Maria Mtakaatifu Bikira daima, tuopolewe na mashaka ya saa, tupate na furaha za milele. Kwa Kristo Bwana wetu, Amina.

LITANIA YA BIKIRA MARIA MAMA WA MATESO

Bwana utuhurumie Bwana utuhurumie
Kristo utuhurumie Bwana utuhurumie
Bwana utuhurumie Bwana utuhurumie
Kristo utusikie – Kristo utusikilize
Mungu Baba wa Mbinguni, Utuhurumie
Mungu Mwana, Mkombozi wa dunia Utuhurumie
Mungu Roho Mtakatifu Utuhurumie
Utatu Mtakatifu Mungu MMoja Utuhurumie
Maria Mtakatifu Utuombee (iwe kiitikio)
Mama wa Mkombozi wetu,
Mama mwenye mateso,
Malkia wa mashahidi,
Mama wa wenye uchungu,
Mfariji wa wenye taabu,
Msaada wa wenye shida,
Mlinzi wa wenye upweke,
Nguvu ya dhaifu moyoni,
Makimbilio ya wakosefu,
Afya ya wagonjwa,
Matumaini ya wanaozimia,
Kwa ajili ya ufukara wako ulioona pangoni Bethlehemu, – Utusaidie ee Mama wa mateso (iwe kiitikio)
Kwa ajili ya mateso yako uliyoona katika uaguzi wa Simeoni,
Kwa ajili ya taabu zako ulizopata katika safari ya Misri,
Kwa uchungu wako, Mwanao alipopotea,
Kwa ajili ya huzuni yako Mwanao alipodhulumiwa,
Kwa ajili ya hofu yako Yesu alipokamatwa,
Kwa ajili ya uchungu wako ulipokutana na Yesu katika njia ya Msalaba,
Kwa ajili ya mateso ya Moyo wako aliposulibiwa,
Kwa ajili ya mateso yako makali Yesu alipokufa,
Kwa ajili ya kilio chako juu ya Mwanao mpenzi,
Kwa ajili ya uchungu wako penye kaburi la Mwanao,
Kwa ajili ya upweke wako baada ya maziko ya Mwanao,
Kwa ajili ya uvumilivu wako katika shida zote,
Katika uchungu wetu wote,
Katika ugonjwa na mateso,
Katika huzuni na shida,
Katika umaskini na upweke,
Katika mahangaiko na hatari,
Katika vishawisho vyote,
Katika saa ya kifo chetu,
Katika hukumu ya mwisho,

Mwanakondoo wa Mungu, unayeondoa dhambi za dunia, Utusamehe ee Bwana.
Mwanakondoo wa Mungu, unayeondoa dhambi za dunia, Utusikilize ee Bwana.
Mwanakondoo wa Mungu, unayeondoa dhambi za dunia, Utuhurumie.
Kristo utusikie – Kristo utusikilize
Bwana utuhurumie – Kristo utuhurumie
Bwana utuhurumie.
Baba Yetu ….
Utuombee, ee Mama wa Mateso
Tujaliwe kupewa ahadi za Kristo.
TUOMBE: Ee Bwana Yesu Kristo, utusaidie sasa na saa ya kifo chetu msaada wa Bikira Maria Mama yako, ambaye moyo wake mtakatifu ulichomwa na upanga wa mateso ulipoteswa na kufa msalabani. Unayeishi na kutawala milele na milele. Amina.

NOVENA YA ROHO MTAKATIFU KWA SIKU ZOTE TISA

Ufuatao ni mtiririko wa Novena ya Roho Mtakatifu kwa siku zote tisa.

Kusali novena hii unaanza nia wimbo/nyimbo kisha unasali sala ya kila siku na kumalizia na litania na Atukuzwe Baba….x3 kwa siku zote tisa.

BAADHI YA NYIMBO KWA ROHO MTAKATIFU

NJOO WANGU MFARIJI

/Njoo wangu Mfariji
Yako shusha mapaji
Roho Mungu njoo/

1. Hekima nishushie, Mungu nimfuatie, Roho Mungu njoo
2. Akili nijalie, imani nizidie, Roho Mungu njoo
3. Nieneze shauri, imani nizidie, Roho Mungu njoo
4. Nizidishie nguvu, nsifanye ulegevu, Roho Mungu njoo
5. Elimu nieleze, hakika niongoze, Roho Mungu njoo
6. Ibada niwashie, Peke nikupupie, Roho Mungu njoo
7. Uchaji nitilie, dhambi nizichukie, Roho Mungu njoo.


NJOO ROHO MTAKATIFU

/Njoo Roho Mtakatifu, shusha mapaji (kweli) niwe imara x2
Leta nuru ya mwanga wako, ifikie moyoni mwangu x2/

1. Roho mwenye hekima, Roho wa shauri na nguvu
2. Nipatie elimu nitambue nafsi yako
3. Nipatie ibada nikusifu daima milele
4. Roho mwenye uchaji washa moto wako wa mapendo

UJE ROHO (SEKWENSIA)

1. Uje Roho Mtakatifu, tuangaze toka mbingu, roho zetu kwa mwangao
2. Uje Baba wa maskini, uje mtoa wa vipaji, uje mwanga wa mioyo
3. Ee Mfariji mwema sana, ee Rafiki Mwanana, ewe raha mustarehe
4. Kwenye kazi u pumziko, kwenye joto burudisho, u mfutaji wa machozi
5. Ewe mwanga wenye heri, uwajaze waumini, neema yako mioyoni
6. Bila nguvu yako Wewe, mwanadamu hana kitu, kwake yote yana kosa
7. Osha machafuko yetu, panyeshee pakavu petu, na kuponya majeraha
8. Ulegeze ukaidi, pasha moto ubaridi, nyosha upotovu wote
9. Wape waamini wako, wenye tumaini kwako, paji zako zote saba
10. Wape tuzo ya fadhila, wape mwisho bila hila, wape heri ya milele.
11. Amina aleluya, amina aleluya, amina aleluya.

NJOO ROHO MTAKATIFU

1. Njoo Roho Mtakatifu, angalia zetu nyoyo, waletee neema nguvu, wakosefu viumbevyo.
2. Majina yako Mfariji, shina la uzima pendo, wake Mwenyezi upaji, mafuta ya roho moto
3. Ndiwe mnye mapaji saba, wa Mungu kuume mkono, mshika uhadi wa Baba, mtoa kwa ndimi maneno
4. Angalo litung’arie, moyo kwa pendo tushushe, nguvu neema tujalie, wanyonge wasabilitishe
5. Shetani mbali mkimbize, amani utupatie, tukufuate tuongoze, maovu utukingie
6. Baba Mungu tujulishe, pia Mwana tumkubali, Roho tukuungamie, mtokea wao wawili.

NOVENA YA ROHO MTAKATIFU SIKU YA KWANZA, IJUMAA

ROHO MTAKATIFU ANATUFARIJI

Yesu alipokuwa akiagana na mitume wake, kabla ya kupaa mbinguni, aliwaambia wasiondoke Yerusalemu mpaka hapo watakapokuwa wamempokea Roho Mtakatifu. Aliwaambia: “Wakati Roho Mtakatifu atakapowashukieni, mtajazwa nguvu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika nchi yote ya Yuda na Samaria, hata kwenye mipaka yote ya dunia.” (Mdo.1:8)

Waliendelea kusali pamoja toka hapo Yesu alipopaa mbinguni mpaka siku ya Pentekoste. Waliomba Roho Mtakatifu awashukie, awajaze na mapaji yake. Na baada ya siku tisa Roho Mtakatifu aliwashukia hao kundi dogo nao wakawa chanzo cha Kanisa lililopata kuenea duniani kote.

Siku hizo tisa za kusali zinaitwa NOVENA; na kila mwaka wakati huu, wakristu wakifuata mfano wa mitume, wanasali muda wa siku tisa kabla ya Sikukuu ya Pentekoste. Wanamuomba Roho Mtakatifu awashukie, awajaze nguvu na wingi wa mapaji yake.

Wakati huu wa NOVENA , Tunayo mengi ya kuliombea Kanisa na kujiombea sisi wenyewe. Kwa hiyo tumuombe Roho Mtakatifu atusaidie kusali vema na kuomba yale yote tunayohitaji kwa maslahi yetu ya roho na mwili.

Na kama mtume Paulo alivyowaambia wale waKristu wa kwanza, Roho Mtakatifu huja kutufatiji katika udhaifu wetu. Basi tumuombe atufariji kwa sala hizi za NOVENA, Atuwezeshe kusali na kuomba inavyotupasa kusali.

1. Ee Baba wa milele, tunakuomba umtume Roho Mtakatifu atushukie sisi taifa lako awashe ndani yetu moto wa upendo wako.
W. Twakuomba utusikie.

2. Ee Baba mwema, tunakuomba utujalie faraja ya Roho Mtakatifu sisi wana tulio katika dhiki na taabu nyingi mno hapa duniani.
W. Twakuomba utusikie.

3. Ulijalie Kanisa lako mapaji ya Roho wako Mtakatifu, liweze kutekeleza vema utume wake wa kuhudumia watu wote hapa duniani.
W. Twakuomba utusikie.

4. Utujalie sisi kudumu katika NOVENA hii mpaka mwisho kama Maria na mitume walivyodumu pamoja wakisali kabla ya Pentekoste ile ya kwanza.
W. Twakuomba utusikie.

5. Utujalie neema zote zinazohitajika ili tuweze kumshuhudia Kristu popote kwa mwenendo na matendo yetu ya kila siku, tukiongozwa na Roho Mtakatifu.
W. Twakuomba utusikie

6. Uzijalie familia zote za wakristu neema na nguvu za Roho Mtakatifu tupate kuendelea pasipo kuchoka katika sala na katika matendo mema siku zote.
W. Twakuomba utusikie

7. Ewe Roho Mtakatifu, uwajalie vijana wetu moyo wa ujasiri, wapate kulijenga kanisa lako na kueneza utawala wako katika jumuia zetu za Kikristu.
W. Twakuomba utusikie.

TUOMBE;

Ee Mungu, uliye muumba wa vitu vyote , tunakuomba utusikilize kwa wema sala zetu sisi taifa lako, utuongoze sote tufuate siku zote utaratibu wa mapenzi yako; naye Roho Mtakatifu atutegemeze mpaka mwisho wa novena hii. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristu Bwana wetu .
W. Amina.

LITANIA YA ROHO MTAKATIFU … (soma hapo chini)


NOVENA YA ROHO MTAKATIFU SIKU YA PILI, JUMAMOSI

ROHO MTAKATIFU ANATUSAIDIA KUENEZA INJILI

“Kweli nakwambia, mtu asipozaliwa kwa maji na Roho, hawezi kamwe kuingia katika utawala wa Mungu,” (Yn. 3:5).

Kanisa limepewa na Yesu ujumbe wa kuwaletea watu wote uzima mpya, uzima wa Mungu. Yesu aliwaambia mitume wake: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani. Nendeni basi mkawafanye watu wa makabila yote kuwa wafuasi wangu. Wabatizeni kwa Jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu. Wafundisheni kuyashika maagizo yote niliyowapeni. Nami nipo pamoja nanyi siku zote mpaka mwisho wa nyakati (Mt.28: 18-20).

Sisi tuliobatizwa tumepata kuwa viungo vilivyo hai vya Mwili wa Fumbo wa Kristu; kwa Kipaimara tumeimarishwa na kuthibitishwa na Roho Mtakatifu. Tumekuwa taifa teule. Tumeshirikishwa ule ukuhani wa Kristu. Tumepokea ujumbe wa kueneza utawala wa Mungu.
Tunapopokea Sakramenti, na hasa ile Sakmenti ya Ekaristi, tunalisha imani na kuongeza mapendo, ambayo ni msingi wa utume wowote ule. Mapendo yanatuhimiza kueneza utawala wa Mungu na kumpenda Yesu Kristu aliyekuja kuwakomboa wanadamu wote.

Kila aliyebatizwa anao wajibu wa kueneza imani ya Mungu na utawala wake. Kwa hiyo tumuombe Roho Mtakatifu atuwezeshe kutimiza wito huo.

1. Ee Baba wa mbinguni tunakuomba umpeleke Roho Mtakatifu aliangaze kanisa na kuliongoza, liweze kuwafikishia mataifa yote habari njema ya wokovu.
W. Twakuomba utusikie

2. Ee Yesu Mkombozi wetu, umtume Roho Mtakatifu awahimize wakristu wapate kutimiza wajibu wao wa kueneza neno lako popote duniani
W. Twakuomba utusikie

3. Ewe Roho Mtakatifu Mfariji, uamshe katika mioyo ya vijana wengi hamu ya kupenda kulitumikia kanisa lako na kulihudumia taifa lako kwa uaminifu.
W. Twakuomba utusikie

4. Ewe mwanga wa mataifa , uwajalie wanafunzi wasikie sauti yako mioyoni mwao, nawe unapowaita wasikose kuisikia sauti yako, wawe tayari kujitoa kwa ajili ya ndugu zao.
W. Twakuomba utusikie.

5. Uwasaidie wazazi wawalee vema watoto wao; uwatie moyo katika wito wao, wapate pia kuishiriki vema ile kazi ya kueneza neno lako kwa jirani zao.
W. Twakuomba utusikie

6. Ewe Roho Mtakatifu, uwasaidie wakristu wote kueneza habari njema ya wokovu, kwa sala, kwa sadaka na kwa mifano ya maisha yao ya uchaji.
W. Twakuomba utusikie

7. Ewe mpaji wa mema, uwajalie waumini mapaji yako saba, wasichoke kulieneza neno lako kwa hekima pasipo hofu.
W. Twakuomba utusikie.

TUOMBE;

Ee Mungu, unapenda watu wote waokoke, waifikie kweli yako. Tunakuomba uwapeleke wafanyakazi walio wengi na wema katika shamba lako. Uwajalie kulihubiri neno lako kwa imani kuu ili neno lako lienee na kupokewa na mataifa yote, wapate nao kukujua wewe peke yako Mungu wao, Mungu wa kweli. Tunaomba hayo kwa nguvu ya Roho Mtakatifu anayeliongoza kanisa lako sasa na milele.
W. Amina

LITANIA YA ROHO MTAKATIFU … (soma hapo chini)


NOVENA YA ROHO MTAKATIFU SIKU YA TATU, JUMAPILI

ROHO MTAKATIFU ANATUFANYA KUWA MITUME

Bwana alisema kwa kinywa cha nabii Yoeli; “Katika siku zile za mwisho asema Bwana, nitawamiminia binadamu wote Roho wangu. Watoto wenu, waume kwa wake, watautangaza ujumbe wangu; vijana wenu wataona maono, na wazee wenu wataota ndoto….hata watumishi wenu watamiminiwa Roho wangu katika siku zile, nao watautangaza ujumbe wangu. (Mdo.2:17-21)

Siku ile ya Pentekoste, bada ya Roho Mtakatifu kulishukia kanisa, mitume waliwakumbusha watu maneno haya ya nabii Yoeli, na miaka mingi baadae, Petro aliwaandikia barua Wakristu wa kwanza akawaambia; kila mmoja anapaswa kutumia kipaji alichojaliwa na Mungu kwa faida ya wengine, kama vile wakili mwema wa zawadi mbali mbali za Mungu. Anayesema kitu, maneno yake na yawe kama maneno ya Mungu; anayetumikia anapaswa kutumikia kwa nguvu aliyojaliwa na Mungu ili katika mambo yote, Mungu atukuzwe kwa njia ya Yesu Kristu, ambaye utukufu na nguvu ni vyake milele na milele (Pet 4;10-11).

Mtaguso wa Pili wa Vatikano ulitukumbusha jambo hilo hilo uliposema; “Roho Mtakatifu anayetakasa taifa la Mungu kwa njia ya Sakramenti amewapa waumini mapaji ya pekee na kumjalia kila mmoja kadiri apendavyo. Kwa hiyo kila mmoja amgawie mwenzake kadiri ya vipawa alivyopewa, awe mgawaji mwaminifu wa neema ya Mungu, alijenge kanisa zima katika upendo.

Tunao wajibu wa kutumia vipawa tulivyojaliwa na Roho Mtakatifu kwa manufaa ya kanisa zima, na kwa faida ya watu wote. Tuunganike sote pamoja na wachungaji wote katika kazi hiyo ya utume. Tumuombe basi Roho Mtakatifu atusaidie kutumia vema vipawa vyake alivyotujalia.

1. Ewe Roho Mtakatifu uwape wakristu neema na nguvu za kutumia vema vipaji ulivyowajalia kwa ajili ya kujenga kanisa lako popote duniani, kwa ajili ya wokovu wa watu wote
W. Twakuomba utusikie

2. Utujalie sisi sote mapaji yako saba, tupate kukutumikia kwa uchaji
W. Twakuomba utusikie

3. Utujalie tuwe mitume wa kweli wa wenzetu, tushirikiane na wachungaji wetu katika huduma za kuwaongoza watu wote na kuwafikisha mbinguni
W. Twakuomba utusikie.

4. Utujalie hekima na nguvu za kuwahudumia watu wote kwa mapendo ya kweli yasiyo na kinyume
W. Twakuomba utusikie

5. Utujalie neema ya kumpenda Mungu kwa moyo wote na kuwapenda jirani zetu kama tunavyojipenda wenyewe
W. Twakuomba utusikie

6. Utupe neema ya kulisikia neno lako na kulifuata, nayo mawazo yetu na matendo yetu yafuate daima mwongozo wako mtakatifu
W. Twakuomba utusikie

7. Uwazidishie mapaji yako wale wote wanaotumia vyema vipawa vyao, uwarudishe na wale wanaotumia vibaya rehema zako

W. Twakuomba utusikie

=== TUOMBE;
Ewe Roho Mungu ndiwe uliyewapa waumini vipawa vyako kwa kadiri unavyotaka. Utujalie tuyapokee na kuyatumia vyema mapaji yako mengi kwa ajili ya utukufu wa Jina lako na kwa ajili ya wokovu wa watu wote. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristu Bwana wetu.
W. Amina

Litania ya Roho Mtakatifu …. (soma hapo chini)


NOVENA YA ROHO MTAKATIFU SIKU YA NNE, JUMATATU

ROHO MTAKATIFU ANALIUNGANISHA KANISA

“Atakapokuja huyu Roho wa kweli , atawaongoza kwenye ukweli wote” (Yn 16:13)

Baada ya kusema hayo, Yesu aliinua macho yake kuelekea mbinguni akasema “Mimi nimekutukuza hapa duniani; nimeikamilisha kazi uliyonipa niifanye. Naomba ili wote wawe kitu kimoja kusudi ulimwengu upate kuamini kwamba Wewe ulinituma (Yn 17:4,21).

Nasi twamuomba Mungu Mwenyezi alijalie kanisa lake umoja wa kweli, awaunganishe wakristu wa madhehebu yote katika zizi moja chini ya mchungaji mmoja.

Popote duniani watu wengi, makundi kwa makundi wanavutwa na neema hiyo ya kuungana na kuufikia umoja wa Kanisa. Hata ndugu zetu waliotengana nasi wanazidi kukubali mwongozo wa Roho Mtakatifu na kutaka kurudi katika nyumba ya Baba na kuwa kundi moja chini ya mchungaji mmoja. Isitoshe, hata sasa tena twaweza kuona kwamba kwa namna fulani wamejiunga nasi katika Roho Mtakatifu, naye Roho Mtakatifu anafanya kazi ndani yao kumshuhudia hata kwa kumwaga damu yao.

Tena katika hao ndugu zetu waliojitenga, Roho Mtakatifu analisha katika mioyo yao ile ya imani inayowaunganisha wafuasi wote wa Kristu. Tumwombe basi Mwenyezi Mungu atujalie hima huo umoja wa Kanisa lake tunaouania mno.

1. Ee Yesu Bwana wetu wewe umetuombea kwa Mungu Baba tuwe itu kimoja kama Wewe ulivyo kitu kimoja na Baba. Utujalie huo umoja, ili ulimwengu uone na kukiri kwamba ndiwe Bwana na Mkombozi wa watu wote
W. Twakuomba utusikie

2. Ee Yesu utujalie moyo wa kulishika neno lako kwa uaminifu, wala usituache kufuata njia zetu sisi wenyewe na kufarakana.
W. Twakuomba utusikie

3. Ee Yesu uliye Mchungaji wetu mwema, ondoa ndani yetu ile tabia ya utengano, tupate kuwa sote kundi moja chini yako wewe uliye mchungaji wetu mmoja.
W. Twakuomba utusikie

4. Ee Yesu, uliye Mchungaji mkuu, uwajalie wachungaji wetu wawe siku zote na upendo wa Jina lako, wasichoke kulichunga vema kundi lako hapa duniani na kuliweka pamoja lisitengane
W. Twakuombaa utusikie

5. Ewe Roho Mtakatifu, uziangaze akili za watu wote, wapende siku zote kuishi kwa amani, umoja na mapendano
W. Twakuomba utusikie

6. Ee Mungu, utufungulie …… wa muungano wako wa kweli sisi tulio ndugu katika Bwana wetu Yesu Kristu.
W. Twakuomba utusikie

7. Utujalie mapatano na amani, tudumu tumeungana katika familia zetu, katika jimbo letu na katika nchi yetu yote.
W. Twakuomba utusikie.

TUOMBE;

Ee Mungu, utuunganishe sisi kondoo wako tuliotawanyika, tuwe chini ya Mwanao mpenzi, tupate sote kuushiriki ule utawala wako wa kweli na haki, utawala wa neema na amani, utawala wa upendo wako. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristu Bwana wetu

W. Amina

LITANIA YA ROHO MTAKATIFU …. (soma hapo chini)


NOVENA YA ROHO MTAKATIFU SIKU YA TANO, JUMANNE

ROHO MTAKATIFU ANAWATAKASA WAUMINI

Walio wa Mungu watafuata yaliyo ya Mungu, na walio wa dunia hufuata yaliyo ya dunia,. Ni mauti kutosheka na mambo yaliyo ya dunia. Uzima na faraja ya kweli hupatikana tu katika mambo ya Mungu.

Kwa nguvu zetu sisi wenyewe hatuwezi kutenda lolote jema. Kuweza kwetu kwatoka kwa Mungu, kwatoka kwa Yeye anayetupa kujua, kupenda na kutenda.

Mtu anapotenda dhambi, hawezi kuongoka ila kwa msaada wa Roho Mtakatifu, ndiye anayempa mkosefu neema ya kutambua ubaya wa kosa lakena kuamua kuliacha. Ndiye anayempa pia mkosefu kutambua uzuri wa neema aliyoipoteza na kumrudishia neema hiyo. Ndiye anayempa nguvu za kuidumisha neema hiyo na kuiongeza.

Isitoshe, Roho Mtakatifu ndiye anayemuwezesha mtu kuwa na maendeleo katika fadhila na utakatifu. Ndiye anayemjalia imani iliyo msingi wa maisha ya kiKristu. Ndie anayetujalia akili ya kushika mafumbo ya dini yetu na kuishi imani yetu mpaka kufa.

Lakini imani peke yake haimtoshi mtu aokoke. Imani pasipo matendo haifai kitu; imani bila matendo imekufa (Yak 2:28) Roho Mtakatifu anamuwezesha mtu kumuamini Mungu na kumenda kuliko vitu vyote na kumpenda jirani kama kujipenda mwenyewe. Ndiyo maana Roho Mtakatifu huitwa chanzo cha matendo yetu yote yaliyo mema. Basi, tumuombe Roho Mtakatifu aitakase mioyo yetu sisi waumini wake, atuzidishie imani, atuwezeshe kutenda matendo yaliyojaa imani.

1. Ewe Roho Mtakatifu, utudumishie imani, uyatakase mawazo ya mioyo yetu yafuate daima maongozi yako na amri zako
W. Twakuomba utusikie

2. Uzigeuze nia zetu zipate kumuelekea daima Mungu
W. Twakuomba utusikie

3. Utuwezeshe kuelekea katika utakatifu na kutenda mema kwa imani siku zote za maisha yetu
W. Twakuomba utusikie

4. Utuzidishie imani matumaini na mapendo, tuweze kushika kwa moyo thabiti yale yote tunayofundishwa na kanisa lako takatifu
W. Twakuomba utusikie

5. Uiwashe mioyo yetu na moto wa mapendo yako, tupate kumpenda Mungu kweli na kumpenda jirani yetu pasipo unafiki.
W. Twakuomba utusikie

6. Utusaidie tuishi vema kwa imani na matumaini siku zote za maisha yetu
W. Twakuomba utusikie

7. Utujalie kudumisha mioyoni mwetu ile neema ya utakaso tuliyoipata mwanzo katika ubatizo wetu
W. Twakuomba utusikie

TUOMBE;

Ee Mungu, mbele yako mioyo yetu i wazi; wewe wayajua yote, wala hakuna siri iliyofichika mbele yako. Uyatakase mawazo ya mioyo yetu kwa kutupelekea Roho Mtakatifu, ili tuweze kukupenda na kukutukuza kama inavyostahili. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristu Bwana wetu

W. Amina

LITANIA YA ROHO MTAKATIFU … (soma hapo chini)


NOVENA YA ROHO MTAKATIFU SIKU YA SITA, JUMATANO

ROHO MTAKATIFU ANATUPA NGUVU

“Nitamuomba Baba , naye atawapelekea Mfariji mwingine atakaye kaa nanyi siku zote”. Katika maisha yenu hapa duniani tunahitaji mno kitulizo cha Mungu. Ni jambo la hekima kutafuta kitulizo hicho kwa Mungu wala si kwa viumbe; maana kitulizo kinachopatikana kwa viumbe hapa duniani hakidumu; bali kitulizo kitokacho kwa Mungu ni cha kudumu.

Roho Mtakatifu ndio kitulizo chetu cha kweli. Baba ndiye aliyetuumba, Mwana ndiye aliyetukomboa, Roho Mtakatifu ndiye aliyetutakasa mioyo yetu na kutufariji.

Kazi ya Roho Mtakatifu sio tu kuwatuliza wale walio na huzuni, bali pia kuwapa moyo wa kuvumilia taabu zozote kwa saburi.

Tunahitaji nguvu ya Roho Mtakatifu ili tuweze kuishi maisha mema ya kikristu. Katika juhudi zetu za kumtumikia Mungu mara nyingi tunakutana na shida; naye Roho Mtakatifu ndie anayetufariji kwa kutupa nguvu za kupambana na matatizo yote. Maisha yetu hapa duniani yamejaa misalaba. Na misalaba hiyo hatuwezi kuichukua kwa nguvu zetu wenyewe. Roho Mtakatifu ndie anayetupa nguvu za kuvumilia. Basi, tumuombe aje kutufariji na kutupa nguvu za kuchukua msalaba wetu kwa saburi kila siku.

1. Ee Yesu Bwana wetu, tunakusihi Wewe na Baba mumtume Roho Mtakatifu atufariji, awajalie kitulizo wale wote walio katika taabu na majonzi
W. Twakuomba utusikie

2. Ewe Roho Mtakatifu, uwafariji wale walio katika tabu za namna zozote ili waweze kuvumilia kwa saburi mateso yao kwa faida ya Roho zao na roho za ndugu zao.
W. Twakuomba utusikie

3. Uwafariji wale walio wagonjwa, uwajalie afya ya roho na ya mwili
W. Twakuomba utusikie

4. Uwasaidie yatima, wajane na wote walioachwa, wasikose kupata siku kwa siku mahitaji yao ya lazima
W. Twakuomba utusikie

5. Wajalie wale wote walio walegevu na wakosefu neema ya kuongoka na kurejea hima katika amani ya upendo wako
W. Twakuomba utusikie

6. Uwaimarishe wale walio wema, uwajalie neema ya kudumu wasilegee katika kutenda mema leo na kesho na siku zote za maisha yao.
W. Twakuomba utusikie

7. Utujalie nguvu za kutafuta na kudumisha amani ya kweli katika mioyo yetu na kati ya ndugu zetu katika jumuia zetu za kikristu
W. Twakuomba utusikie

TUOMBE;

Ee Bwana Mungu wetu, tunakuomba neema ya Roho Mtakatifu ituangaze akili na mioyo yetu na kutujaza nguvu ya upendo wako. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristu Bwana wetu.

W. Amina

LITANIA YA ROHO MTAKATIFU … (soma hapo chini)


NOVENA YA ROHO MTAKATIFU SIKU YA SABA, ALHAMISI

ROHO MTAKATIFU ANATUPA HEKIMA

Hekima tunayopewa na Roho Mtakatifu si sawa kama hekima inayopatikana katika ulimwengu huu.

Hekima ya Roho Mtakatifu ni ile Mtk. Paulo aliyowaambia Wakorintho ya kuwa; ni hekima ambayo watawala wa dunia hii hawakuielewa; maana kama wangaliielewa, hawangalimsulubisha Bwana wa utukufu. Lakini, ni kama yasemavyo maandiko; mambo ambayo jicho halijapata kuyaona wala sikio kuyasikia mambo ambayo binadamu hajapata kuyafikiria moyoni, hayo ndiyo Mungu aliyowatayarishia wale wampendao (1Kor 2;8-9).

Mtk. Paulo alisema kama vile roho ya mtu ndiyo yenye kufahamu na kutambua yaliyo ndani yake; hivyo pia Roho Mtakatifu ndiye anayefahamu mambo ya Mungu na kutufumbulia sisi mioyoni mwetu.

Katika Sikukuu hii ya Pentekoste tunatazamia kumpokea Roho Mtakatifu. Yeye aliye hekima ya Mungu atatufumbulia siri za Mungu na ukweli wake. Ndiye atakayeamsha ndani yetu mapendo ya Yesu Msulibiwa , Mkombozi wetu. Ni yeye atakayetuongoza kutenda mema na kuacha mabaya; tunahitaji sana Roho Mtakatifu katika maisha yetu ya kila siku, tupate hekima ya kuchagua na kutenda daima yaliyo mema. Katika novena hii tuzidi kumuomba Mungu atushushie Roho Mtakatifu, atujaze na hekima yake.

1. Ee Mungu, uwabariki viongozi wa dini na wasaidizi wao, wapate kutuongoza kwa hekima na mapendo
W. Twakuomba utusikie

2. Ewe Roho Mtakatifu, utujalie hekima ya kutambua Mambo ya Mungu na kuyatekeleza kwa uchaji
W. Twakuomba utusikie

3. Utujalie kuyajua mapenzi ya Mungu na kuyapokea kwa furaha
W. Twakuomba utusikie

4. Uamshe ndani yetu mapendo ya Yesu msulibiwa , utuwezeshe kutimiza vema wajibu wetu kama wafuasi wa kweli wa Kristu Bwana wetu
W. Twakuomba utusikie

5. Utuwezeshe kuchagua daima yaliyo mema na kuyatekeleza, tupate kulijenga na kulidumisha kanisa lako hapa duniani
W. Twakuomba utusikie

6. Utuepushe na mafundisho yoyote yaliyo na upotovu, utujalie hekima ya kuzidi kutambua ukweli wako na mafundisho yako yaletayo wokovu
W. Twakuomba utusikie

7. Hekima ya Roho Mtakatifu ituongoze katika satfari ya maisha yetu hapa duniani, tupate mwishowe kukurudi Wewe Muumba wetu uliye mwanzo wetu na mwisho wetu
W. Twakuomba utusiki

TUOMBE;

Ee Mungu, Baba wa utukufu, tunakuomba utupe Roho wako wa hekima, atuwezeshe kukufahamu vema, atuongoze kuishi maisha yenye kukupendeza. Utusaidie kupambana na matatizo ya maisha, tupate kuishi maisha mema hapa duniani na mwisho tupate tunzo la heri na furaha yako huko mbinguni. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristo Bwana wetu.

W. Amina.

LITANIA YA ROHO MTAKATIFU … (soma hapo chini)


NOVENA YA ROHO MTAKATIFU SIKU YA NANE, IJUMAA

ROHO MTAKATIFU ANATUPA MWANGA.

Roho Mtakatifu anaangaza akili zetu tuweze kuona ukweli wa Mungu na kuufata. Bila Roho Mtakatifu akili zetu zimo katika giza nene, wala hatuwezi kuona njia ya kutuelekeza kwa Mungu.

Mungu alipoumba ulimwengu, dunia ilikuwa giza tupu, haina kitu. Mungu alisema; “Iwe nuru”, ikawa nuru, Mungu akaiona nuru, ya kuwa ni njema (Mwa 1;3-4) vivyo hivyo akili ya binadamu bila nuru ya mwanga wa Roho Mtakatifu, ni tupu, ina giza, haiwezi kuona mambo yanayotuelekeza kwa Mungu. Tukiwa na nuru ya Roho Mtakatifu tunaona ukweli wa Mungu jinsi ulivyo.

Roho Mtakatifu anapoijia roho ya mtu, anaiangaza akili yake iweze kuona mambo yanayofaa kwa wokovu. Naye akiisha kuiangaza akili ya mtu huimarisha utashi wake na kumwezesha kuchagua daima yaliyo mema.

Roho Mtakatifu huiangaza akili iweze kuona ukweli. Kabla ya kuwaaga mitume, Yesu aliwaambia kuwa atawapelekea mfariji mwingine atakayekaa nao siku zote. Roho wa kweli ambaye dunia haiwezi kumpokea kwa sababu hawakumfahamu, lakini wao mitume watamfahamu kwa maana atakaa nao siku zote. Yesu ametuahidi pia sisi Roho huyo akae nasi
Leo hivi duniani kuna uwongo na udanganyifu mwingi; kuna dhuluma, vita, na maovu ya kila namna. Hii ni kwa sababu dunia haijamtambua bado Roho Mtakatifu na kumpokea Yeye aliye mwanga wa dunia na asili ya kweli yote.

Mtaguso wa Pili wa Vatikano watambua ya kuwa Roho Mtakatifu anakaa katika kanisa na katika mioyo ya waumini kama katika hekalu. Roho Mtakatifu analiongoza kanisa na kulifanya liwe na umoja; analipamba na mapaji yake mabalimbali.

Tumuombe Mungu Baba ampeleke huyo Roho Mtakatifu katika kanisa lake, aliongoze na kulilinda lisipate kutengana, bali lisaidie kueneza utawala wa Mungu popote duniani.

1. Ewe Roho Mtakatifu, utujalie kuona mwanga wa kweli yako na kuifuata
W. Twakuomba utusikie

2. Uwape waregevu neema ya kuirudia tena njia ya kweli yako
W. Twakuomba utusikie

3. Utuwezeshe sisi sote waamini wako tutembee siku zote katika nuru ya kweli yako na sheria zako
W. Twakuomba utusikie

4. Utuangazie akili ya mioyo yetu tuchague daima yale yanayakupendeza
W. Twakuomba utusikie

5. Uwape mwanga wako viongozi wetu wa dini na serikali, wapate kutuongoza kwa hekima na uchaji, wasisahau kamwe kwamba uwezo walionao unatoka kwa Mungu.
W. Twakuomba utusikie

6. Utupe mwanga wako tuwaone watu wote kama ndugu zetu. Tuishi kindugu na kusaidiana kindugu
W. Twakuomba utusikie

7. Ewe Roho Mtakatifu ndiwe mpatanishi wa mioyo,; tunakuomba uondoe udhalimu, uonevu, udanganyifu na maovu yote katika mioyo ya watu wote.
W. Twakuomba utusikie.

TUOMBE;

Ee Yesu Bwana wetu, uliyesema “Pasipo Mimi hamuwezi kitu” umpeleke Roho Mtakatifu atuangaze akili zetu, tupate kufahamu mapenzi yako na kuyatimiza kwa imani na uchaji. Roho Mtakatifu atuongoze katika mambo yote, yeye anayeishi na kutawala nawe pamoja na Baba daima na milele.

W. Amina

LITANIA YA ROHO MTAKATIFU … (soma hapo chini)


NOVENA YA ROHO MTAKATIFU SIKU YA TISA, JUMAMOSI

ROHO MTAKATIFU ANATUPA MAPENDO

Maandiko Matakatifu yanatuambia ya kuwa, Roho Mtakatifu, Nafsi ya Tatu ya Utatu Mtakatifu, ndiye Upendo katika Baba na Mwana. Upendo hujieneza. Naye Roho Mtakatifu aliye pendo lenyewe la Mungu, hupenda kujieneza na kujishirikisha nasi, na kuwasha ndani yetu moto wa mapendo yake.

Roho Mtakatifu ndiye mwenye kutakatifuza roho zetu kwa neema ya utakaso. Neema hiyo ni uzima wa Mungu, ndio huo upendo wa Mungu tunaoshirikishwa. Roho isiyo na neema ya utakaso imetengana na Mungu, haina uzima wake, haina upendo wake, kwa hiyo haiwezi pia kuwa na mapendo ya kweli ya jirani.

Ingawa tunaona ishara nyingi za watu kupendana kidugu hapa duniani, mapendo hayo si mapendo ya kweli wala si kamili kama hayatokani na neema ya utakaso rohoni mwa mtu. Kama hakuna neema ya utakaso ndani yetu, Mungu pia hayupo kati yetu.

Roho Mtakatifu anatuunganisha na Mungu katika upendo. Pasipo na mapendo hapana mapatano, hapana masikilizano wala mwungano. Watu wanaopendana wanaungana na kulingana katika fikra zao na nia zao. Roho Mtakatifu anayetutia mapendo rohoni na kutuwashia moto wa mapendo, ndiye anayetuwezesha kuwa na mawazo ya namna moja na nia moja.

Watu wanaopendana hupenda kukaa pamoja, kuishi pamoja na kusaidiana. Roho Mtakatifu aliye chanzo cha mapendo ya kweli hutuweka pamoja katika Kanisa lake. Hukaa ndani yetu, hukaa katika Kanisa na kuwasha moto wa mapendo yake ndani yetu. Roho Mtakatifu anatuwezesha kukaa kwa amani nyumbani, kazini na katika jumuiya zetu. Basi, tumwombe sasa Roho Mtakatifu atuongezee hayo mapendo yake ndani yetu.

1. Ewe Roho Mtakatifu, uwashe mioyoni mwetu moto wa mapendo yako, tupate kuwapenda jirani zetu kama tunavyotaka kupendwa nao.
W. Twakuomba utusikie

2. Udumishe ndani yetu neema hiyo ya mapendo yako, tuwezeshe kuishi kwa amani leo na siku zote za maisha yetu.
W. Twakuomba utusikie

3. Utujalie neema na nguvu za kutekeleza mema yote tunayokusudia kuyatenda siku hii ya leo
W. Twakuomba utusikie

4. Uongoze nia zetu na maazimio yetu, yalingane na juhudi zetu za kutaka kuleta mafanikio ya roho na mwili kati yetu
W. Twakuomba utusikie

5. Utubariki, ili baada ya maombi haya, tuwe na juhudi ya kutimiza vema zaidi wajibu wetu wa kikristu kwa moyo mkuu
W. Twakuomba utusikie

6. Utuwezeshe kueneza mapendo na amani kati yetu na katika jumuiya zetu za kikristu
W. Twakuomba utusikie

7. Utuwezeshe kuwa kweli chachu ya wema na mapendano kati ya watu, ili nao wapate rehema zako kwa maombezi yetu.
W. Twakuomba utusikie.

TUOMBE;

Ee Mungu, tunakushukuru kwa neema ulizotujalia, hata tukaweza kuifanya ibada hii ya Novena takatifu mpaka mwisho. Utujalie mema yote tuliyoomba; utusaidie kutekeleza yote yale tuliyokusudia kutenda. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristu Bwana wetu.

W. Amina.

LITANIA YA ROHO MTAKATIFU … (soma hapo chini)


LITANIA YA ROHO MTAKATIFU

  • Bwana Utuhurumie………Utuhurumie
  • Kristu utuhurumie……..….Utuhurumie
  • Bwana utuhurumie….. Utuhurumie
  • Baba mweza wa vyote….. Utuhurumie

  • Yesu Mwana wa Pekee wa Baba na Mwokozi wa Dunia……..Utuokoe
  • Roho wa Baba na Mwana aunganishaye maisha ndani ya Baba na Mwana………….Ututakatifuze
  • Roho Mtakatifu……….Utusikie

  • Roho Mtakatifu atokaye kwa Baba na Mwana…………..Njoo ndani ya mioyo yetu
  • Ahadi ya Mungu Baba……………… Njoo ndani ya mioyo yetu
  • Mionzi ya Mwanga kutoka Mbinguni……………… Njoo ndani ya mioyo yetu
  • Mwandishi wa vyote vilivyo vizuri……………… Njoo ndani ya mioyo yetu
  • Chanzo cha Maji ya Uzima……………… Njoo ndani ya mioyo yetu
  • Moto utumikao daima……………… Njoo ndani ya mioyo yetu
  • Muungano Mtakatifu……………… Njoo ndani ya mioyo yetu

  • Roho wa ukweli na upendo……………………Utuhurumie
  • Roho wa hekima na elimu……………………Utuhurumie
  • Roho wa shauri na nguvu……………………Utuhurumie
  • Roho wa akili na neema ya kumtumikia Mungu……………………Utuhurumie
  • Roho wa neema na sala……………………Utuhurumie
  • Roho wa amani na subira……………………Utuhurumie
  • Roho wa usafi na uaminifu……………………Utuhurumie
  • Kitulizo cha Roho……………………Utuhurumie
  • Roho aletaye Utakatifu……………………Utuhurumie
  • Roho uongozaye Kanisa……………………Utuhurumie
  • Zawadi kutoka kwa Mungu juu Mbinguni……………………Utuhurumie
  • Roho ajazaye ulimwengu……………………Utuhurumie

  • Roho Mtakatifu…………………..tupe neema ya kuchukia dhambi
  • Roho Mtakatifu…………………..njoo ufanye upya sura ya ulimwengu
  • Roho Mtakatifu…………………..jaza roho zetu kwa mwanga wako
  • Roho Mtakatifu…………………..ifuraishe mioyo yetu kwa sheria yako
  • Roho Mtakatifu…………………..washa moto wa mapendo ndani yetu
  • Roho Mtakatifu…………………..jaza mioyo yetu na hazina ya neema yako
  • Roho Mtakatifu…………………..tufundishe kusali vyema
  • Roho Mtakatifu…………………..tuangaze kwa nguvu zako za Ki-Mungu zitupatiazo moyo wa kutenda daima yaliyo mema
  • Roho Mtakatifu…………………..tuongoze Kwenye njia ya wokovu
  • Roho Mtakatifu…………………..tuweze kufahamu yale ya muhimu tu
  • Roho Mtakatifu…………………..tupe hamu ya kuitafuta fadhila yako
  • Roho Mtakatifu…………………..tusaidie tuweze Kupata fadhila zote
  • Roho Mtakatifu…………………..tupe uvumilivu tuweze kutenda yaliyo mema tu.
  • Roho Mtakatifu…………………..tunaomba uwe zawadi ya uzima wetu

  • Mwanakondoo wa Mungu uondoaye dhambi za dunia…………….Tushushie Roho wako Mtakatifu
  • Mwanakondoo wa Mungu uondoaye dhambi za dunia…………….jaza mioyo yetu kwa mapaji yako ya Roho Mtakatifu
  • Mwanakondoo wa Mungu uondoaye dhambi za dunia…………….tupe roho ya hekima na neema ya kumsifu Mungu.
  • Njoo Roho Mtakatifu uzijaze roho za waumini wako uwashe moto wa mapendo yako ndani ya mioyo yetu (W)

TUOMBE

Ee Mungu Baba mwenye huruma tujalie Roho wako alete Mwanga kwetu ili apate kututakasa na kuingiza ndani ya mioyo yetu Baraka za kuweza kutenda yale yaliyo mema.
Tunaomba hayo kupitia kwa Mwanao Mpendwa Bwana wetu Yesu Kristo, anbaye anaishi na kutawala pamoja nawe katika Umoja wa Roho Mtakatifu. AMINA

Atukuzwe Baba…..x3

Sala ya Malaika wa Bwana

Malaika wa Bwana alimpasha habari Maria, naye akapata mimba kwa uwezo wa Roho Mtakatifu. Salamu Maria,….

Ndimi Mtumishi wa Bwana, nitendewe ulivyonena. Salamu Maria, ……
Neno wa Bwana akatwaa Mwili, akakaa kwetu. Salamu Maria, …..

Utuombee, ee Mzazi Mtakatifu wa Mungu, tujaliwe ahadi za Kristo.

Tuombe:

Tunakuomba ee Bwana, utie neema yako mioyoni mwetu, ili sisi tuliojua kwa maelezo ya Malaika, kwamba, Kristo Mwanao amejifanya mtu: kwa mateso na Msalaba wake, utufikishe kwenye utukufu wa ufufuko. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristo Bwana wetu, Amina.

SALA YA KUMWOMBA MT. YOSEFU MSAADA (SALA KUU KWA MTAKATIFU YOSEFU)

Ee Mt. Yosefu mwenye heri, tunakimbilia kwako katika masumbuko yetu, na kisha omba shime ya Mchumba wako Mtakatifu, tunaomba pia kwa matumaini usimamizi wako. Kwa ajili ya mapendo uliyompenda Bikira Mtakatifu Mzazi wa Mungu, na kwa ajili ya kumtunza Mtoto Yesu, twakuomba sana, utuangalie kwa wema sie tuliokuwa fungu lake Yesu Kristu, tukakombolewa kwa damu yake. Tusimamie katika masumbuko yetu kwa enzi na shime yako.

Ee Mlinzi amini wa jamaa takatifu, uwakinge watoto wateule wa Yesu Kristu.
Ee Baba uliyetupenda mno tuepushe na kilema chochote cha madanganyo na upotevu. Ee kinga yetu mwezaji, utusimamie huko juu mbinguni ulipo, tunaposhindana na wenye nguvu wakaao gizani. Kama vile siku za kale ukamwopoa Mtoto Yesu katika hatari ya kuuawa, na leo hivi likinge Kanisa Takatifu la Mungu katika mitego ya adui, na katika shida yote; mtunze daima kila mmoja wetu, tufwate mfano wako, ili tupate na msaada wako, kukaa na utakatifu maisha, kufa kifo chema, na kupata mbinguni makao ya raha milele.
Amina.

Shopping Cart
2
    2
    Your Cart
    🏠 Home 📖 Reading 🖼️ Gallery 💬 AI Chat 📘 About