Sala za Katoliki: Sala Muhimu Kwa Mkristu Mkatoliki

Novena ya Siku tisa kwa Mtakatifu Agustino wa Hippo: Sala zote na Litania

Anza Novena hii tarehe 19 Agosti ili kumalizia tarehe 27 Agosti na kusheherekea tarehe 28 Agosti, Sikukuu ya Mtk. Augustino wa Hippo.

SIKU YA KWANZA – kutafuta ukweli – kweli ni nini?

Kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina

Tafakari
Pamoja na Mtakatifu Augustino tunasema “ Umetuumba kwa ajili yako ee Bwana, kwani ni wewe peke yako ndie Mungu wetu, na nyoyo zetu hazitapumzika, hadi tupumzike ndani mwako.”

Tunapoanza Novena yetu kwa Mtakatifu Augustino tunamwomba Mungu neema ya kuwa na roho kama yake katika safari yetu katika kuzitambua nafsi zetu. Tunatafakari sisi ni nani na tunaelekea wapi kama wafuasi wa Mtakatifu Augustino katika dunia ya leo. Kama Mt Augustino alivyoutafuta ukweli bila kuchoka, nasi tutulie na kuruhusu maswali haya yaguse ufahamu wetu. Ni nini kinachonisababisha niendelee kumtafuta Mungu? Baada ya kumpata Mungu, ninamfanyaje awe hai kwa watu wale ninaoishi nao?

Kama kuna jambo moja Mt Augustino anasisitiza tena na tena kuhusu kumtafuta Mungu, ni kuwa lazima tuanze kumtafuta ndani mwetu. Huko ndiko tutakuta ukweli, mwanga na furaha katika Kristu mwenyewe. Ndani ya nafsi zetu ndiko tutasikilizwa tunaposali, katika nafsi zetu ndiko tutampenda Mungu na kumwabudu.

Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino

Bwana utuhurumie Bwana utuhurumie

Kristu utuhurumie Kristu utuhurumie

Bwana utuhurumie Bwana utuhurumie

Kristu utusikie Kristu utusikilize

Baba wa mbinguni Mungu utuhurumie

Mwana Mkombozi wa dunia Mungu utuhurumie

Roho Mtakatifu Mungu utuhurumie

Utatu Mtakatifu Mungu mmoja utuhurumie

Maria Mama wa Yesu utuombee

Maria Mama wa faraja utuombee

Maria Mama wa shauri jema utuombee

Mt. Augustimo nyota angavu ya Kanisa utuombee

Mt Augustino uliyejawa bidii kwa ajili ya kuutafuta utukufu wa Mungu utuombee

Mt. Augustino mtetezi jasiri wa Ukweli utuombee

Mt Augustino ushindi wa neema ya Mungu utuombee

Mt Augustino uliyewaka mapendo kwa Mungu utuombee

Mt Augustino mkuu sana na mnyenyekevu sana utuombee

Mt Augustino mfalme wa maaskofu na wanateolojia utuombee

Mt Augustino baba wa maisha ya kitawa utuombee

Mt Augustino mtakatifu kati ya wenye hekima na mwenye hekima kati ya watakatifu utuombee

Utuombee Mtakatifu Augustino – ili tustahili maagano ya Kristu.

Tuombe: Umetuumba kwa ajili yako ee Bwana, na nyoyo zetu hazitapumzika kamwe, hadi tutakapopumzika ndani mwako. Tunakuomba utubariki katika mahangaiko yetu ya kukutafuta wewe na utusaidie tunapokutana na makwazo. Tunapokupata, tunaomba utujalie neema ya kuwa waaminifu kwako ee Mungu wa historia, tuwe waaminifu kwa Yesu Kristu Mkombozi wetu, kwa Kanisa letu na mafundisho yake, na tuwe waaminifu katika wito wetu tuliouchagua katika kukutumikia wewe. Tunaomba hayo kwako wewe Baba mwema, kwa njia ya Kristu Bwana wetu na kwa maombezi ya Mtakatifu Augustino Msimamizi wa Jumuiya yetu, Amina.

Baba yetu……, Salamu Maria….., Atukuzwe Baba……

Siku ya pili – Utulivu

Kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina

Tafakari

“Ingia sasa, ndani ya moyo wako (Isaya 46:8) na uwe na imani, utamkuta Kristu humo. Humo anaongea na wewe, mimi, mwalimu, napaaza tu sauti yake lakini Yeye ndiye anayekufunza wewe kwa ufanisi zaidi katika utulivu wako”

Je tunapenda maisha ya utulivu ambapo tunapata muda wa kumtafakari Mungu na mambo anayotutendea katika maisha yetu? Kwa vile Yesu anaongea nasi katika utulivu, inatupasa tujifunze namna ya kuutunza utulivu ndani ya nafsi zetu licha ya mahangaiko na misukosuko ya maisha. Tutenge muda katika siku yetu ambapo tunaweza kutulia na Kristu na kumsikiliza, na wala sio sisi kuongea nae tu bila kumsikiliza naye pia. Soma Neno la Mungu kwa utulivu na kwa tafakari, na uone kama kuna kitu gani Mungu anakuaombia leo. Lazima tusafishe macho ya nyoyo zetu, ili tuweze kumwona Mungu ndani mwetu. Tunafanya hivyo kwa njia ya toba na maungamo. Kusafishwa vizuri ni jambo linaloweza kuambatana na maumivu, lakini tunahitaji usafi wa nafsi ili tuweze kuwa wasikivu zaidi kwa sauti ya Mungu ndani mwetu.

Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino

(Angalia siku ya kwanza)

Tuombe: Ee Baba mwema, tunataka kumfuata Mwanao Yesu kwa ukaribu zaidi. Utuwezeshe kuumbika upya nawe kwa mfano wa Mtakatifu Augustino katika maisha yake ya utulivu. Utusaidie kuacha mambo ya dunia hii yanayopita ili tupate hamu kubwa zaidi ya kukufuata. Imarisha imani yetu ili tusikie sauti yako katika maandiko: ili tuweze kukuona Wewe katika matukio ya maisha yetu. Tunaomba haya kwa njia ya Kristu Bwana wetu, anayeishi na kutawala nawe na Roho Mtakatifu, Mungu mmoja milele na milele. Amina.

Baba yetu……, Salamu Maria….., Atukuzwe Baba……

Siku ya tatu – matendo-tafakari na matendo

Katika wito wetu uwao wote wa maisha yetu, tunaalikwa na Yesu tutafakari jinsi Martha alivyolalamika kuwa dada yake Maria alitumia muda wote katika kumsikiliza Yesu badala ya kusaidia kazi. Mt. Augustino akiwa kama mtawa aliuchukua mfano wa Martha na Maria kwa kushiriki kwa ukamilifu pia katika ujenzi wa uhai wa Kanisa kwa njia ya maandishi na kazi zake njema. Je mimi ninaoanishaje kati ya kutenda, kusali na tafakari takatifu?

Mt. Augustino anatufundisha kuwa tuwe tayari kuwatumikia wengine. Asiwepo mtu anayedhani kuwa anaweza kusali tu muda wote bila matendo, na wala asiwepo anayedhani atafaidika kwa matendo mengi yasiyosindikizwa na wingi wa sala. Tunapozigundua karama zetu Mungu alizotupa, tuwe tayari kuzishirikisha kwa wengine, kwani siku ya mwisho tutahukumiwa kwa namna ambavyo tuliwajali wengine. Kwa hiyo baada ya kumpata Mungu ndani mwako, usibaki humo, bali mgeukia yeye aliyekuumba. “Tupande mlimani lakini tusijenge vibanda, tushuke tuwatumikie wengine”

Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino

(Angalia siku ya kwanza)

Tuombe: Mungu Baba yetu, tunakutukuza na kukushukuru kwa kulijalia Kanisa lako mtakatifu mkuu namna hii. Tunapojitahidi kuishi roho na karama zake, utujalie neema za kukua katika utumishi wetu kwa wengine kwa njia ya matendo mema na pia katika maisha yetu ya sala, kwa mfano wa Mt. Augustino. Tunaomba hayo kwa Jina la Mwanao, Bwana na Mwokozi wetu. Amina.

Baba yetu……, Salamu Maria….., Atukuzwe Baba……

Siku ya nne – umaskini wa kiinjili – maisha ya kujitoa

Kwa Jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina.

Kuna wakati Mt. Augustino alikosa kitu chochote cha kuwapatia wasiojiweza, kwa sababu alikuwa anagawa kila alichoweza kwa wenye shida. Alipoishiwa kabisa, aliuza baadhi ya vitu alivyokuwa navyo ili kupata pesa iliyohitajika kwa ajili ya wenye shida.

Je, mimi pamoja na karama zote alizonijalia Mungu na vipaji vyote nilivyo navyo, ninajitahidi kuiga mfano wa Mt. Augustino katika kujitoa kwa wengine?

Umaskini wa kiinjili ni tofauti na umaskini wa kukosa mali au pesa. Ni namna moyo wa mtu anavyopenda kujitoa hata nje ya Jumuiya yake. Yesu Kristu alijitoa kabisa kwetu kwa kuuacha Umungu wake na kujitwalia ufukara wetu ili aweze kututajirisha. Hii ni changamoto kwetu kuwa tuwe tayari kujitoa kwa ajili ya wale wanaotuhitaji na Augustino ni mfano katika hilo. Tujitolee kufanya kazi za huruma, kwani mtu hataishi kwa mkate tu. Je tunawasaidiaje maskini walioko katika eneo letu? Ufalme wa Mungu utawafikiaje wengine kupitia kwetu. Mt Augustino anatupa changamoto leo kuwa tukubali kwa moyo mmoja kutoa vitu tulivyo navyo kwa ajili ya wengine, na tumfuate Kristu kwa moyo mpya na wa dhati.

Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino

(Angalia siku ya kwanza)

Tuombe: Tunakutukuza ee Bwana kwa kila unatupowezesha kushirikisha vile ulivyotujalia kwa ajili ya wahitaji, na kushikama katika upendo wako. Tunakuomba utujalie neema ya kudumu katika kushirikiana na kupendana ili tuwe mashahidi wa ukarimu wako mkuu. Tunaomba hayo kwa njia ya Bwana wetu Yesu Kristu, anayeishi na kutawala pamoja nawe na Roho Mtakatifu, Mungu mmoja daima na milele, Amina.

Baba yetu……, Salamu Maria….., Atukuzwe Baba……

Siku ya tano – urafiki katika jumuiya yetu

Kwa Jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina.

Mt. Augustino anashuhudia kuwa kitu kilichomweka karibu na marafiki zake kaka na dada zake ni kulekuongea na kucheka pamoja, kusaidiana, kusoma vitabu vinavyofanana vyenye mambo ya kujenga, kutaniana, kutofautiana mara kwa mara bila kukasirikiana, na alama za urafiki wetu zilijionyesha katika nyuso zetu, sauti zetu, macho yetu, na namna nyingi nyingine”. Je mimi nafurahia mahusiano yaliyoko katika Jumuiya yetu? Kuna jambo gani naweza kufanya ili kuboresha mahusiano na wanajumuiya wenzangu?

Ushahidi wa mapendo ya kweli unakuja pale tunapokuwa tayari kubebeana mizigo yetu. Tunapojitahidi kuboresha mambo yanayohusu Jumuiya, ukweli ni kuwa tunaboresha mambo yetu binafsi pia. Tumwombe Mungu ili tuweze kuona namna ambavyo Jumuiya yetu inatutegema katika hali na namna mbalimbali na tuweze kuboresha mahusiano ili kukuza urafiki kati yetu kama anavyotufundisha Kristu.

Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino

(Angalia siku ya kwanza)

Tuombe: Bwana Mungu wetu, ulimfunulia Mt. Augustino uzuri ulioko katika urafiki uliojengwa katika misingi yako. Utujalie sisi tunaosimamiwa naye hapa duniani, tukue katika urafiki mtakatifu wa kijumuiya. Utujalie tufikie ukamilifu wa urafiki huo katika makao yetu ya mbinguni unakoishi na kutawala daima na milele, Amina.

Baba yetu……, Salamu Maria….., Atukuzwe Baba……

Siku ya sita – augustino mfano wa unyenyekevu

Kwa Jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina.

Unyenyekevu unapatikana tu katika vita vya kiroho. Umuhimu wa majaribu katika maisha yako ya kiroho ni kuwa ni kwa kupitia tu majaribu hayo unajipatia unyenyekevu. Hapo ndio unauona umuhimu wa kumpokea yesu kuwa Mwokozi wako. Ukiwa na kiburi itakuwa ni kikwazo kikubwa kumpokea Mwokozi.

Kwa Augustino, unyenyekevu sio kujidharau, bali ni kujitahidi kufahamu karama alizotujalia Mungu na kuziendeleza. Ili kuwa mtu mnyenyekevu, jifahamu kuwa u mdhambi, na kuwa Mungu ndie anayeweza kukuweka huru. Fanya maungamo ya dhambi zako ili uwe wa kundi lake Mungu. Je, kama unyenyekevu ndio ukweli, ninajitahidije kuushirikisha ukweli huu kwa wengine katika Jumuiya yetu?

Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino

(Angalia siku ya kwanza)

Tuombe: Tuelekezee nyoyo zetu katika wema wako ee bwana, na geuza macho yetu mbali na kiburi na puuzi za dunia ili tuwe wafuasi wa maneno yako: Jifunzeni kwangu kwani mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo. Utujalie tukue kila siku katika unyenyekevu ambao unampendeza sana moyo wa Msimamizi wetu mt. Augustino. Amina.

Baba yetu……, Salamu Maria….., Atukuzwe Baba……

Siku ya saba – uangalizi wa imani yetu

Kwa Jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina.

Na tumpende Bwana wetu, tulipende kanisa lake. Tunampokea Roho Mtakatifu kadri tunavyolipenda Kanisa lake, kama tukiunganika pamoja kwa upendo, kama tukilifurahia jina katoliki na Imani yake. Tuamini kuwa tutakuwa na Roho Mtakatifu kwa kipimo cha upendo wetu kwa Kanisa lake. Tunalipenda Kanisa kama tulisimama imara katika ushirika na upendo.

Je ninalipenda Kanisa Katoliki? Ninajitahidi kujifunza imani hii na kuwashirikisha wengine au ninafuata mkumbo tu? Tunaalikwa kuishi kwa mfano wa Mt. Augustino ambaye alijielimisha kuhusu imani ya Kanisa Katoliki na kuikumbatia, kuitetea na kuishirikisha kwa wengine. Tusisite kujitoa katika dunia yetu ya leo pale tunapohitajika katika kueneza imani yetu. Tumwombe Mungu atujalie kwa mfano wa Mt. Augustino, moyo wa kusukumwa kuwashirikisha wengine imani iliyo hai kwa njia ya maneno, na matendo yetu, na hivyo kulitetea Kanisa la Bwana wetu Yesu Kristu kila wakati kwa injili iliyo hai.

Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino

(Angalia siku ya kwanza)

Tuombe: Baba mwenye upendo, tunakushukuru kwa zawadi ya Mt. Augustino uliyolipatia Kanisa lako. Kwa maombezi yake, sisi tunakuomba mwanga na ujasiri wa kujitoa bila masharti kwa unyenyekevu na daima katika huduma kwa wengine hasa wenye shida mbalimbali katika mahitaji ya mwili na ya roho. Tunaomba hayo, kwa njia ya Kristu Bwana wetu, Amina.

Baba yetu……, Salamu Maria….., Atukuzwe Baba……

Siku ya nane – utayari katika kulisaidia kanisa letu

Kwa Jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina.

Jumuiya ni kiini cha Kanisa la leo, kama ilivyokuwa wakati wa mitume, wakifundishwa na mitume. Kama Jumuiya za kwanza za wakristu, tunaalikwa nasi leo tuwe na utayari katika kulisaidia Kanisa letu kwa njia mbalimbali hasa kwa kutoa zaka kwa wakati. Wakati huohuo pia tuelewe kuwa Roho Mtakatifu anatupatia vipaji na karama kuendana na mahitaji ya Kanisa lake, na hivyo tusisahau kushirikisha karama na vipaji hivyo kanisani kwetu ili kuujenga mwili wa Kristu. Kwa njia hiyohiyo, kazi zetu za kitume ziendane na mahitaji ya Kanisa letu leo hii kwani yote tunapewa na Roho wa Mungu kwa ajili ya utumishi kwa wengine. Je, shughuli zetu kama Jumuiya zinaendana na mahitaji ya Kanisa la Mungu kwa wakati huu? Ni mabadiliko gani tunaitwa kuyafanya kama Jumuiya na kama mtu mmoja mmoja ili kuboresha Kanisa kupitia Jumuiya yetu?

Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino

(Angalia siku ya kwanza)

Tuombe: Baba mwema, tunakuheshimu na kukutukuza kwa kutupatia Mt. Augustino. Tukiwa tumejiweka chini ya mafundisho yake, tunaomba neema na maongozi yako ili tuweze daima kuwa na utayari wa kulisaidia Kanisa letu kwa njia ya zaka na majitoleo kadri ya mahitaji, na utujalie neema tunazokuomba kwa njia ya Yesu Kristu, Bwana na Mwokozi wetu. Amina.

Baba yetu……, Salamu Maria….., Atukuzwe Baba……

Siku ya tisa – utayari wa kuwasaidia wenzetu

Kwa Jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina.

Mt. Augustine daima alikuwa tayari kuwasaidia wahitaji. Alitoa kila alichoweza vikiwemo vile vitu alivyotengewa kwa ajili ya matumizi yake yeye mwenyewe, na alipokosa kitu zaidi cha kutoa, aliyeyusha baadhi ya vyombo vya dhahabu vilivyokuwa vimewekwa wakfu kwa ajili ya kuuza na kisha aliwagawia maskini pesa iliyopatikana. Nasi mara nyingine inawezekana hatuna pesa mfukoni za kuwapa wale wanaohitaji tuwasaidie, lakini bila shaka tuna vitu. Mazao ya mashambani, mifugo, na vitu aina mbalimbali alivyotujalia Mungu. Kwa hiyo kila mmoja wetu ana kitu anachoweza kumpa mwenzake, pengine kama sina chochote zaidi angalau nina muda wa kusali na kuwaombea wengine kuendana na mahitaji ya Jumuiya yetu, au kuwatembelea wapweke, wenye majonzi na kuwafariji wengine. Cha msingi ni kumtazama Kristu, ambaye ana njaa na anateseka, ndani ya wenzetu.

Tunafanya vyema kushikamana na maskini. Sio maskini wa mali na pesa tu tunazungumzia hapa, bali pia maskini wa kiroho, wale wanaohitaji kuelekezwa, wenye mashaka, wapweke, wagonjwa, na wanaoteseka na dhambi. Tumwombe Mungu ili tuimarike kiroho, maana tutaweza kuwasaidia hao maskini tu pale ambapo sisi wenyewe tuna utajiri wa kiroho, yaani tunaye Kristu ndani mwetu.

Tunapomalizia Novena yetu ya siku tisa, tutafakari kuwa, kama Mt. Augustino angekuwa hai leo, angewajibika namna gani, angewasaidiaje maskini walioko katika Jumuiya yetu, mahali petu pa kazi na hata katika familia zetu?

Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino

(Angalia siku ya kwanza)

Tuombe: Bwana, tunakuomba urejeshe upya katika Kanisa lako roho kama ile uliyompa Mt. Augustino. Kwa mfano wake, tujazwe na kiu ya kukupata wewe peke yako kama chemchem ya hekima na chanzo cha upendo wa milele ili tuwe na utayari wa kuwasaidia wenzetu wote wenye shida za aina mbalimbali. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristu Bwana wetu. Amina.

Baba yetu……, Salamu Maria….., Atukuzwe Baba……

SALA YA KUUABUDU MOYO MTAKATIFU WA YESU KATIKA EKARISTI TAKATIFU

Kwa nguvu zangu zote za moyo wangu/ ninakuabudu ee Moyo Mtakatifu/ na Mwabudiwa sana,/ Moyo Mtakatifu wa Bwana wetu Yesu Kristu/ ambao ninataka kumpenda/ na kukusalimu kwa usikivu unaoendelea./ Kamwe nisikuudhi tena/ kwa sababu Wewe ni Mwema sana;/ Ee Mwema sana./ Ee Moyo Mtakatifu sana/ ninakupenda/ na ninataka kukupenda zaidi ya vitu vyote,/ kwa nguvu zangu zote/ na kwa uwezo wangu wote,/ ninatamani kuwa mali yako/ Wewe uliyejitoa Msalabani kwa ajili yangu/ kwa mateso makali./ Unionee huruma na udhaifu wangu/ na usiniruhusu kupotea./

Ninajitoa kabisa kwako/ ee moyo wa mapendo,/ kwa makusudi kuwa utu wangu,/ maisha na mateso yangu/ yalipie kukupenda,/ kukuheshimu/ na kukutukuza Wewe sasa na milele./ Ninakupenda ee Moyo Mwabudiwa wa Mwokozi wangu,/ ninakuomba kwako/ uamuru moyo wangu na kila kitu ndani yangu/ kikutukuze sasa na milele./ Amina.

(Na Mt Margareta Maria Alakoki)

SALA YA NOVENA YA SIKU TISA KWA MT. YOSEFU, YA ZAMANI, MIAKA 1900 ILIYOPITA

Ee Mt. Yosefu, ambaye ulinzi wako ni mkubwa, wenye nguvu na wa haraka mbele ya Kiti cha Enzi cha Mungu, ninakukabidhi nia na haja zangu zote. Ee Mt. Yosefu, unisaidie kwa maombezi yako yenye nguvu, na unipatie kutoka kwa Mwanao Mungu, baraka zote za kiroho, kwa njia ya Kristu Bwana wetu, ili nikishapata msaada wako wa mbinguni ningali bado hapa duniani, niweze nami kumsifu, kumwabudu na kumshukuru Mungu aliye Baba mwema kabisa kushinda wote. Ee Mt. Yosefu, sichoki kamwe kufikiri moyoni kwa upendo, jinsi Mtoto Yesu alivyokuwa amesinzia mikononi mwako. Akiwa amepumzika hivyo karibu na moyo wako, sithubutu kujongea, nisije nikamsumbua, bali nakuomba wewe umkumbatie na kumbusu kwa niaba yangu na kumwambia anipe busu lake nitakapovuta pumzi yangu ya mwisho.
Mtakatifu Yosefu Msimamizi wa wanaozimia roho; Utuombee.
Amina.

Sala hii ilipatikana katika mwaka wa hamsini wa Bwana na Mwokozi Wetu Yesu Kristu. Mnamo mwaka 1505 Baba Mtakatifu alimtumia sala hii Mfalme Charles wakati alipokuwa anaenda vitani. Yeyote atakayeisoma sala hii, au kuisikia ikisomwa, au kuibeba, hatakufa kifo cha ghafla,hatazama majini, hatadhurika kwa sumu, wala hataanguka katika mikono ya adui zake, au kuunguzwa katika moto wowote ule, au kushindwa katika vita.

Sali sala hii kwa siku tisa mfululizo, kwa kuomba jambo lolote unalolihitaji. Haijawahi kusikika kuwa sala hii imeshindwa jambo.

Malkia wa Mbingu

Malkia wa mbingu, furahi, aleluya. Kwani uliyestahili kumchukua, Aleluya. Amefufuka alivyosema, Aleluya. Utuombee kwa Mungu, Aleluya. Furahi shangilia, ee Bikira Maria, Alaluya. Kwani hakika Bwana amefufuka Aleluya. Tuombe. Ee Mungu, uliyependa kuifurahisha dunia kwa kufufuka kwake Bwana wetu Yesu Kristu, Mwanao: fanyiza, twakuomba, kwa ajili ya Bikira Maria, tupate nasi furaha za uzima wa milele. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristu Bwana wetu. Amina.

SALA MBELE YA SAKRAMENTI KUU II

Yesu, Mungu wangu mpenzi,/ upo hapa katika Altare mbele yangu;/ na mimi napiga magoti mbele yako.// Waniangalia sana,/ siyo kwa kunipeleleza,/ lakini kwa sababu wapenda kuniona hivi karibu na wewe,/ wafurahiwa nikija kukuabudu./ Wayasikiliza maneno yangu yote/ yenye kutoka mdomoni mwangu,/ na zaidi wapokea maneno yangu yanayotoka moyoni./ Nataka kuzungumza na wewe peke yako,/ na kusahau mambo mengine yote/ na watu wengine walioko kanisani pamoja nami./

Yesu wangu,/ nakushukuru/ kwa sababu umekubali kutupa Sakramenti hii kuu kabisa,/ ukitaka kukaa pamoja na sisi,/ na hata ukakubali kuwa chakula chetu/ chenye nguvu ya ajabu./ Mfalme wangu Yesu,/ Sultani wangu Mkuu,/ naamini kabisa kwamba upo katika Altare/ na kwamba umejificha chini ya umbo la mkate./ Ulipokuwapo bado hapa duniani mbele za watu,/ ulikuwa hujifichi kama sasa;/ lakini hata siku zile/ watu hawakuweza kukuona vile ulivyo./ Hawakuweza kuutambua Umungu wako,/ ikalazimu kukuamini tu sawa kama sisi./ Wakainama kichwa wakisema,/ “Bwana wangu na Mungu wangu”./ Na mimi kadhalika naungama/ U Bwana wangu na Mungu wangu/ na Mkombozi wangu/ na salama yangu yote./ U Yesu wangu tu,/ siwezi kusema zaidi./ Nakuabudu ee Yesu./ Najua sana, mimi ni mdogo kabisa,/ sina maana hata kidogo./ Mimi ni dhaifu na maskini mno./ Lakini Wewe katika hruuma yako kubwa/ waniita nije kwako./ Wewe huuangalii umaskini wangu,/ bali wanivuta katika mapendo yako./

Nasikia maneno yako usemayo:/ “Njooni kwangu ninyi nyote mnaoelemewa na mizigo/ nami nitawasaidia”./ Kwa ajili ya maneno hayo/ nakuja kwako bila hofu./ Najua kwamba wanipenda,/ najua wataka kunisaidia na kuniponya,/ najua kuwa wataka kunitakasa./

Nahitaji sana msaada wako, hakika./ Unaniona katika mwendo wangu wa kila siku,/ Jinsi ninavyohangaika na vishawishi mara nyingi;/ jinsi nilivyo na lazima ya kushindana kila siku/ nikitaka kukaa mwema na safi katika utumishi wako./ Naungama mbele yako Wewe Mkombozi wangu,/ kwamba sikukaa imara siku zote vile nilivyopaswa./ Naungama kwamba nimeshindwa mara nyingine/ na kwa hivi naomba toba./ Lakini kwa nini nimeshindwa mara nyingine?/ Kwa nini nikakosa?/ Ni kwa sababu nalikuwa nimekwenda mbali nawe;/ nalianza kujitegemea mwenyewe./ Katika majivuno yangu nikajisifu mwenyewe,/ nikajiona mwema,/ nikasahau udhaifu wangu./ Na kwa ajili hiyo nikajitia katika hatari bure,/ sikujilinda tena,/ nikampa shetani nafasi ya kunishambulia kwa hila zake zote./ Unihurumie ee Yesu wangu./

Sasa nafahamu jinsi nilivyokuwa mjinga kwelikweli./ Ndiyo maana nakuabudu kwa moyo wangu wote./ Najiweka mikononi mwako/ ufanye nami vile unavyotaka./ Wewe utanitunza;/ Wewe utanilinda vema;/ Wewe utaniongoza nijue namna ya kuepa hatari zote,/ na jinsi ya kufukuza kila kishawishi./ Chukua moyo wangu kabisa,/ kwa sababu ni mali yako kamili;/ Wewe ndiwe uliyeniumba,/ ndiwe uliyenipeleka katika Ukristo,/ nawe ndiwe utakayenihukumu siku ya mbele./ Ndivyo ninavyojitolea kwako./ Ndivyo ninavyokuabudu,/ wala sijui njia nyingine ya kukusifu zaidi./

Yesu wangu mpenzi,/ naomba upokee kwa uzuri heshima hiyo yangu./ Angalia: naitolea pamoja na heshima yote/ unayopewa daima na watakatifu wako/ na malaika wako./ Nikipiga magoti hapa mbele yako sasa,/ siko peke yangu,/ nakuabudu pamoja na Mama yako Bikira Maria,/ ambaye sala zake zinakupendeza kabisa./ Sala zangu naweka pamoja na sala zake yeye,/ uzipokee zote pamoja,/ zikupendeze zote sawa./ Ee Mama Maria!/ Nifundishe maneno ya kumsifu Mwanao Yesu vizuri./ Nipeleke kwa Yesu tumwabudu pamoja./ Nifunike na utakatifu wako/ kusudi Yesu asiangalie tena umaskini wangu/ na makosa yangu,/ aniponye katika huruma yake./

Sasa najisikia vizuri, Yesu wangu./ Sasa nina moyo wa kuweza kuendelea vema/ katika njia njema./ Sasa ninatumaini kwamba/ nitakaa mkristo mwema,/ nitakuwa mtumishi wako mwaminifu./ Nasikia amani kubwa sana moyoni mwangu,/ kwa kuwa nimo mikononi mwako./ Baada ya dakika chache/ nitaondoka tena kanisani,/ nitarudi nyumbani kwangu,/ lakini hatutaachana,/ hapana./ Mapendo yetu yatatuunganisha pamoja daima./ Wewe utanikumbuka nikiwa kazini,/ nikilala usingizi,/ nikienda njiani,/ kila mahali nilipo,/ Wewe utaniona,/ utafuatana na mimi./ Kadhalika nitakukumbuka tu./ Nitafanya bidii nisikuache kabisa./ Amina.

SALA YA MAJITOLEO KWA MAMA WA HUZUNI

Mama Mtakatifu, Mama wa Mungu na Malkia wa Mashahidi, leo nakuchagua Wewe uwe mfano wangu, mkingaji na mteteaji wangu. Naweka roho fukara katika moyo wako uliotobolewa na panga nyingi za mateso. Unipokee mimi niwe mtumishi wako wa pekee na mshiriki wa mateso yako. Nijalie nguvu niwe daima karibu na msalaba ule alikosulibiwa Yesu. Nakutolea nafsi yangu na mali yangu yote. Pokea kila tendo langu jema ukalisindikize kwa Mwanao, Mama, nifanye nistahili kuitwa mtumishi wa Maria, Simama karibu yangu katika matendo yangu yote ili yafanwe kwa sifa ya Mungu. Ulivyosimama karibu kabisa ya Mwanao alipokufa msalabani uwe karibu nami saa ya kufa kwangu. Nijalie niweze kutaja jina lako na la Mwana wako nikisema: “Yesu, Maria na Yosef mnisaidie saa ya kufa kwangu. Yesu, maria na Yosef, naomba nife kwa amani kati yenu!” . Amina.

LITANIA YA KUWAOMBEA MAPADRE WOTE 1

Kwa ajili ya Baba Mtakatifu wetu ..(N); Bwana, umpe moyo wako wa uchungaji mwema
Kwa ajili ya warithi wa Mitume; Bwana, uwape wawe na uangalifu uliojaa upendo kwa mapadre wao
Kwa ajili ya Maaskofu wako waliochaguliwa na Roho Mtakatifu; Bwana, uwabakishe karibu na kondoo wako
Kwa ajili ya wachungaji wako; Bwana, uwafundishe kutumikia kuliko kutafuta kutumikiwa
Kwa ajili ya waungamishi na washauri wa kiroho; Bwana, uwafanye kuwa vyombo visikivu kwa Roho wako Mtakatifu
Kwa ajili ya mapadre wanaotangaza neno lako; Bwana, uwawezeshe kushirikisha Roho wako na Uzima wako
Kwa ajili ya mapadre wanaosaidia utume wa walei; Bwana, uwatie moyo wa kuwa mifano bora
Kwa ajili ya mapadre wanaofanya kazi na vijana; Bwana, uwajalie wawakabidhi vijana kwako
Kwa ajili ya mapadre wanaofanya kazi kati ya watu fukara; Bwana, uwajalie wakuone na wakutumikie kupitia hao
Kwa ajili ya mapadre wanaoangalia wagonjwa; Bwana, uwajalie wawafundishe thamani ya mateso
Kwa ajili ya mapadre fukara; – Uwasaidie ee Bwana
Kwa ajili ya mapade wagonjwa; – Uwaponye ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wazee; – Uwapatie tumaini la raha ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wenye huzuni na walioumizwa; -Uwafariji ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wanaohangaishwa na wale wanaosumbuliwa; – Uwape amani yako ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wanaodharauliwa na wanaonyanyaswa; – Uwatetee ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre waliokata tamaa; – Uwatie moyo ee Bwana
Kwa ajili ya wale wanaosomea upadre; – Uwape udumifu ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wote; – Uwape uaminifu kwako na kwa Kanisa lako ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wote; – Uwajalie utii na upendo kwa Baba Mtakatifu na kwa maaskofu wao ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wote; – Uwajalie waishi katika umoja na maaskofu wao ee Bwana
Tunawaombea mapadre wote; – Wawe wamoja kama Wewe na Baba mlivyo wamoja ee Bwana
Tunawaombea mapadre wote; – Waishi na kuendeleza haki yako ee Bwana
Tunawaombea mapadre wote; – Washirikiane katika umoja wa ukuhani wako ee Bwana
Tunawaombea mapadre wote, wakiwa wamejawa na uwepo wako; – Waishi maisha yao ya useja kwa furaha ee Bwana
Tunawaombea mapadre wote; – Wajalie ukamilifu wa Roho wako na uwageuze wafanane nawe ee Bwana
Kwa namna ya pekee, ninawaombea mapadre wale ambao kwa njia yao nimepokea neema zako. Ninamwombea padre aliyenibatiza na wale walioniondolea dhambi zangu, wakinipatanisha na Wewe na Kanisa lako.
Ninawaombea mapadre ambao nimeshiriki Misa walizoadhimisha, na walionipa Mwili wako kama chakula. Ninawaombea mapadre walionishirikisha Neno lako, na wale walionisaidia na kuniongoza kwako. Amina.

SALA KWA MT. YOSEFU KWA AJILI YA KULIOMBEA KANISA LA MAHUJAJI

Ee Mtukufu Mt. Yosefu, ulichaguliwa na Mungu kuwa Baba Mlishi wa Yesu, mchumba safi kabisa wa Maria Bikira Milele, na mkubwa wa Familia Takatifu. Umechaguliwa na Mwakilishi wa Kristu kama Msimamizi wa kimbingu na mlinzi wa Kanisa alilolianzisha Kristu. Ndiyo maana ninakuomba kwa matumaini makuu usaidizi wako wenye nguvu kwa ajili ya Kanisa zima duniani.

Mlinde kwa namna ya pekee, kwa upendo wa kikweli wa ki-baba, Baba Mtakatifu na Maaskofu wote na Mapadre wenye ushirika na Kiti cha Petro. Uwe mlinzi wao wote wanaotumikia wokovu wa wanadamu kati ya majaribu na mahangaiko ya maisha haya, na utujalie kwamba watu wote wa dunia hii wamfuate Kristu na Kanisa alilolianzisha.

Mpendwa Mtakatifu Yosefu, ukubali majitoleo ya nafsi yangu ambayo sasa ninafanya. Ninajiweka wakfu kwako kwa ajili ya utumishi wako, ili daima wewe uwe baba yangu, mlinzi wangu, na kiongozi wangu katika njia ya wokovu. Unijalie usafi mkuu wa moyo na matamanio makuu ya maisha ya kiroho. Unijalie ili matendo yangu yote, kwa mfano wako, yawe kwa ajili ya sifa na utukufu wa Mungu, pamoja na Moyo wa kimungu wa Yesu, moyo safi wa Maria, na moyo wako wa ki-baba. Uniombee, nami nishiriki kifo chako cha furaha na kitakatifu.
Amina.

SALA KWA BIKIRA MARIA KATIKA UKIWA WAKE

Nakusikitikia sana Mama Mtakatifu Maria kwa sababu ya ukiwa wako mkuu. Uchungu wako ulikuwa mkubwa sana ulipotazama mateso na kifo cha Mwana wako mpenzi. Muda ule uliweza kutuliz kidogo kwa sababu ya kumwona angali hai. Lakini je, baada ya kufa na kumzika? Sasa wewe ni mkiwa mkubwa mno! Uh, ukiwa wa pekee, uniombee mimi ninayempoteza mara nyingi kwa dhambi zangu. Unijalie nisimpoteze tena Yesu wangu kwa ubaya wa uvivu wangu, bali nimtumikie kiaminifu duniani hapa ili nimwone na kumfurahia milele mbinguni. Amina.

Sala fupi ya Asubuhi

Tuusifu Utatu Mtakatifu wa Mungu Mwenyezi, Baba, Mwana na Roho Mtakatifu, milele na milele, Amina.

Ee Utatu Mtakatifu wa Mwenyezi Mungu, Baba, Mwana na Roho Mtakatifu, nasadiki kuwa upo hapa na mahali pote. Ee Mungu wangu, umeniumba, umenikomboa, umenifanya mkristo, umenizidishia neema zako hapa duniani, umenitayarishia makao yangu mbinguni, umenijalia na siku hii nikutumikie. Ee Mungu wangu! Nakuabudu, nakushukuru, nakuomba toba, nakupenda! Ee Mungu wangu, nakutolea roho yangu, na mawazo, na maneno, na kazi, na furaha, na mateso yangu: uyapokee unipe neema yako nisikutende leo dhambi!

LITANIA YA KUWAOMBEA MAPADRE WOTE II

Kwa ajili ya Baba Mtakatifu wetu ..(N); Bwana, umpe moyo wako wa uchungaji mwema
Kwa ajili ya makardinali na maaskofu wakuu; Uwape moyo wa kichungaji ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wa majimbo; Uwajaze na Roho wako ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre watawa; Wakamilishe katika wito wao ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre walioko hatarini; Uwaokoe ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wenye udhaifu; Uwatie nguvu ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wenye hofu; Uwape amani ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre waliokata tamaa; Uwavuvie upya ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wakaao upweke; Uwasindikize ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wamisionari; Uwalinde ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wanaohubiri; Uwaangazie ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre na watawa waliokufa; Uwafikishe kwenye utukufu wako ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wote; Wajalie hekima na ufahamu wako ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wote; Uwajalie elimu na shauri lako
Kwa ajili ya mapadre wako; wajalie wakuheshimu na wakuogope
Kwa ajili ya mapadre wote; Wajalie subira na upendo
Kwa ajili ya mapadre wote; wajalie utii na upole
Kwa ajili ya mapadre wote; uwajalie hamu kuu ya kuokoa roho za watu
Kwa ajili ya mapadre wote; wape fadhila za imani, matumaini na mapendo
Kwa ajili ya mapadre wote; Wajalie upendo mkuu kwa Ekaristi
Tunakuomba uwajalie mapadre wote; Waheshimu uhai na hadhi ya mtu ee Bwana
Tunakuomba uwajalie mapadre wote nguvu na bidii katika kazi zao ee Bwana
Tunakuomba uwajalie mapadre wote amani katika mahangaiko yao ee Bwana
Tunakuomba uwajalie mapadre wote upendo mkuu kwa Utatu Mtakatifu ee Bwana
Tunakuomba uwajalie mapadre wote upendo mkuu kwa Bikira Maria ee Bwana
Uwajalie mapadre wote wawe mwanga wa Kristo ee Bwana
Uwajalie mapadre wote, wawe chumvi kwa ulimwengu ee Bwana
Uwajalie mapadre wote, wajizoeze kujitoa sadaka na kujinyima ee Bwana
Uwajalie mapadre wote, wawe watakatifu kimwili, kiakili na kiroho ee Bwana
Uwajalie mapadre wote wawe watu wa sala ee Bwana
Uwajalie mapadre wote wawe kioo cha imani kwako ee Bwana
Uwajalie mapadre wote wajali sana wongofu wetu ee Bwana
Uwajalie mapadre wote wawe waaminifu kwa wito wao wa kikuhani ee Bwana
Uwajalie mapadre wote, ili mikono yao ibariki na kuponya ee Bwana
Uwajalie mapadre wote wawake moto wa mapendo yako ee Bwana
Uwajalie mapadre wote hatua zao zote ziwe kwa ajili ya utukufu wa Mungu ee Bwana
Uwajalie mapadre wote wajazwe na Roho Mtakatifu na uwajalie karama zake kwa wingi ee Bwana.

Tuombe.
Baba, Mwana na Roho Mtakatifu, usikie sala tunazokutolea kwa ajili ya mapadre wetu. Uwajalie wafahamu waziwazi kazi uliyowaitia kuifanya, uwape neema zote wanazohitaji ili waitikie wito wako kwa ushujaa, kwa upendo, na majitoleo yenye udumifu katika mapenzi yako matakatifu. Amina.

Litani ya Bikira Maria

  • Bwana utuhurumie
  • Bwana utuhurumie
  • Kristo utuhurumie
  • Bwana utuhurumie
  • Bwana utuhurumie
  • Kristo utusikie
  • Kristo utusikilize
  • Mungu Baba wa Mbinguni,…… Utuhurumie
  • Mungu Mwana Mkombozi wa dunia ……… Utuhurumie
  • Mungu Roho Mtakatifu …….. Utuhurumie
  • Utatu Mtakatifu Mungu Mmoja …….. Utuhurumie
  • Maria Mtakatifu ………. utuombee
  • Mzazi Mtakatifu wa Mungu …….. utuombee
  • Bikira Mtakatifu Mkuu wa Mabikira …….. utuombee
  • Mama wa Kristo ……… utuombee
  • Mama wa Neema ya Mungu ………….. utuombee
  • Mama Mtakatifu sana ……… utuombee
  • Mama mwenye usafi wa Moyo ……….. utuombee
  • Mama mwenye ubikira ……….. utuombee
  • Mama usiye na doa ……….. utuombee
  • Mama mpendelevu ………. utuombee
  • Mama mstajabivu ………. utuombee
  • Mama wa Muumba ………. utuombee
  • Mama wa Mkombozi ………….. utuombee
  • Mama wa Kanisa……….. utuombee
  • Bikira mwenye utaratibu ………….. utuombee
  • Bikira mwenye heshima ………….. utuombee
  • Bikira mwenye sifa ………….. utuombee
  • Bikira mwenye uwezo ………….. utuombee
  • Bikra mweye huruma ………….. utuombee
  • Bikra mwaminifu………….. utuombee
  • Kioo cha haki ………….. utuombee
  • Kikao cha hekima ………….. utuombee
  • Sababu ya furaha yetu ………….. utuombee
  • Chombo cha neema ………….. utuombee
  • Chombo cha kuheshimiwa ………….. utuombee
  • Chombo bora cha ibada ………….. utuombee
  • Waridi lenye fumbo ………….. utuombee
  • Mnara wa Daudi ………….. utuombee
  • Mnara wa pembe ………….. utuombee
  • Nyumba ya dhahabu ………….. utuombee
  • Sanduku la Agano ………….. utuombee
  • Mlango wa Mbingu ………….. utuombee
  • Nyota ya asubuhi ………….. utuombee
  • Afya ya wagonjwa ………….. utuombee
  • Kimbilio la wakosefu ………….. utuombee
  • Mtuliza wenye huzuni ………….. utuombee
  • Msaada wa waKristo ………….. utuombee
  • Malkia wa Malaika ………….. utuombee
  • Malkia wa Mababu ………….. utuombee
  • Malkia wa Manabii ………….. utuombee
  • Malkia wa Mitume ………….. utuombee
  • Malkia wa Mashahidi ………….. utuombee
  • Malkia wa Waungama dini ………….. utuombee
  • Malkia wa Mabikira ………….. utuombee
  • Malkia wa Watakatifu wote ………….. utuombee
  • Malkia uliyepalizwa Mbinguni ………….. utuombee
  • Malkia wa Rozari takatifu ………….. utuombee
  • Malkia wa amani ………….. utuombee

  • Mwanakodoo wa Mungu uondoaye dhambi za dunia,…………..Utusamehe ee Bwana.
  • Mwanakondoo wa Mungu uondoaye dhambi za dunia,…………..Utusikilize ee Bwana
  • Mwanakondoo wa Mungu uondoaye dhambi za dunia,…………..Utuhurumie.

  • Utuombee, Mzazi Mtakatifu wa Mungu,…………..Tujaliwe ahadi za Kristo.

Tuombe

Ee Bwana Mungu, utujalie sisi watumishi wako afya ya roho na mwili siku zote; na kwa maombezi matukufu ya Maria Mtakaatifu Bikira daima, tuopolewe na mashaka ya saa, tupate na furaha za milele. Kwa Kristo Bwana wetu, Amina.

SALA ZA IBADA KWA BIKIRA MARIA WA MATESO

ROZARI YA MATESO SABA YA BIKIRA MARIA

Tumia Rozari ya Mateso Saba ya Bikira Maria iliyo na mafungu 7 yaani mateso 7 yenye Salamu Maria saba kwa kila teso.

TESO LA KWANZA

Mzee Simeoni aliagua kuwa Moyo wa Mama Maria utachomwa kwa upanga.
Tuombe neema ya kuvumilia mateso.
Mama wa mateso utuombee.
Baba Yetu ……… Salamu Maria x7. Atukuzwe Baba ……
Mateso na majonzi ya Mama Maria hayana mfano.

TESO LA PILI

Maria na Yosefu walikimbilia Misri usiku ili kumficha Mtoto Yesu asiuawe na Herodi.
Tuombe neema ili miili yetu iwe kimbilio lake Yesu.
Mama wa mateso utuombee.
Baba Yetu ……… Salamu Maria x7. Atukuzwe Baba ……
Mateso na majonzi ya Mama Maria hayana mfano.

TESO LA TATU

Mama Maria aliona uchungu sana Mtoto Yesu alipopotea kwa siku tatu.
Tuombe neema ya kudumu na Yesu mioyoni mwetu.
Mama wa mateso utuombee.
Baba Yetu ……… Salamu Maria x7. Atukuzwe Baba ……
Mateso na majonzi ya Mama Maria hayana mfano.

TESO LA NNE

Mama Maria aliona uchungu sana alipokutana na Mwanae Yesu katika njia ya Msalaba.
Tuombe neema ya kudumu na Yesu siku zote.
Mama wa mateso utuombee.
Baba Yetu ……… Salamu Maria x7. Atukuzwe Baba ……
Mateso na majonzi ya Mama Maria hayana mfano.

TESO LA TANO

Mama Maria aliona uchungu sana alipomwona Mwanae Yesu akisulibiwa Msalabani.
Tuombe neema ya kufa mikononi mwa Yesu na Maria.
Mama wa mateso utuombee.
Baba Yetu ……… Salamu Maria x7. Atukuzwe Baba ……
Mateso na majonzi ya Mama Maria hayana mfano.

TESO LA SITA

Mama Maria aliona uchungu sana alipopakata maiti ya Mwanae Yesu baada ya kushushwa Msalabani.
Tuombe neema ya kutotenda dhambi.
Mama wa mateso utuombee.
Baba Yetu ……… Salamu Maria x7. Atukuzwe Baba ……
Mateso na majonzi ya Mama Maria hayana mfano.

TESO LA SABA

Mama Maria aliona uchungu sana aliporudi nyumbani baada ya kumzika Mwanae Yesu
Tuombe neema ya kitulizo kwa Mama Maria.
Mama wa mateso utuombee.
Baba Yetu ……… Salamu Maria x7. Atukuzwe Baba ……
Mateso na majonzi ya Mama Maria hayana mfano.

LITANIA YA MAMA WA MATESO

Bwana utuhurumie Bwana utuhurumie
Kristo utuhurumie Bwana utuhurumie
Bwana utuhurumie Bwana utuhurumie
Kristo utusikie – Kristo utusikilize
Mungu Baba wa Mbinguni, Utuhurumie
Mungu Mwana, Mkombozi wa dunia Utuhurumie
Mungu Roho Mtakatifu Utuhurumie
Utatu Mtakatifu Mungu MMoja Utuhurumie
Maria Mtakatifu Utuombee (iwe kiitikio)
Mama wa Mkombozi wetu,
Mama mwenye mateso,
Malkia wa mashahidi,
Mama wa wenye uchungu,
Mfariji wa wenye taabu,
Msaada wa wenye shida,
Mlinzi wa wenye upweke,
Nguvu ya dhaifu moyoni,
Makimbilio ya wakosefu,
Afya ya wagonjwa,
Matumaini ya wanaozimia,
Kwa ajili ya ufukara wako ulioona pangoni Bethlehemu, – Utusaidie ee Mama wa mateso (iwe kiitikio)
Kwa ajili ya mateso yako uliyoona katika uaguzi wa Simeoni,
Kwa ajili ya taabu zako ulizopata katika safari ya Misri,
Kwa uchungu wako, Mwanao alipopotea,
Kwa ajili ya huzuni yako Mwanao alipodhulumiwa,
Kwa ajili ya hofu yako Yesu alipokamatwa,
Kwa ajili ya uchungu wako ulipokutana na Yesu katika njia ya Msalaba,
Kwa ajili ya mateso ya Moyo wako aliposulibiwa,
Kwa ajili ya mateso yako makali Yesu alipokufa,
Kwa ajili ya kilio chako juu ya Mwanao mpenzi,
Kwa ajili ya uchungu wako penye kaburi la Mwanao,
Kwa ajili ya upweke wako baada ya maziko ya Mwanao,
Kwa ajili ya uvumilivu wako katika shida zote,
Katika uchungu wetu wote,
Katika ugonjwa na mateso,
Katika huzuni na shida,
Katika umaskini na upweke,
Katika mahangaiko na hatari,
Katika vishawisho vyote,
Katika saa ya kifo chetu,
Katika hukumu ya mwisho,

Mwanakondoo wa Mungu, unayeondoa dhambi za dunia, Utusamehe ee Bwana.
Mwanakondoo wa Mungu, unayeondoa dhambi za dunia, Utusikilize ee Bwana.
Mwanakondoo wa Mungu, unayeondoa dhambi za dunia, Utuhurumie.
Kristo utusikie – Kristo utusikilize
Bwana utuhurumie – Kristo utuhurumie
Bwana utuhurumie.
Baba Yetu ….
Utuombee, ee Mama wa Mateso
Tujaliwe kupewa ahadi za Kristo.
TUOMBE: Ee Bwana Yesu Kristo, utusaidie sasa na saa ya kifo chetu msaada wa Bikira Maria Mama yako, ambaye moyo wake mtakatifu ulichomwa na upanga wa mateso ulipoteswa na kufa msalabani. Unayeishi na kutawala milele na milele. Amina.

SALA KWA BIKIRA MARIA KATIKA UKIWA WAKE

Nakusikitikia sana Mama Mtakatifu Maria kwa sababu ya ukiwa wako mkuu. Uchungu wako ulikuwa mkubwa sana ulipotazama mateso na kifo cha Mwana wako mpenzi. Muda ule uliweza kutuliz kidogo kwa sababu ya kumwona angali hai. Lakini je, baada ya kufa na kumzika? Sasa wewe ni mkiwa mkubwa mno! Uh, ukiwa wa pekee, uniombee mimi ninayempoteza mara nyingi kwa dhambi zangu. Unijalie nisimpoteze tena Yesu wangu kwa ubaya wa uvivu wangu, bali nimtumikie kiaminifu duniani hapa ili nimwone na kumfurahia milele mbinguni. Amina.

SALA YA MAJITOLEO KWA MAMA WA HUZUNI

Mama Mtakatifu, Mama wa Mungu na Malkia wa Mashahidi, leo nakuchagua Wewe uwe mfano wangu, mkingaji na mteteaji wangu. Naweka roho fukara katika moyo wako uliotobolewa na panga nyingi za mateso. Unipokee mimi niwe mtumishi wako wa pekee na mshiriki wa mateso yako. Nijalie nguvu niwe daima karibu na msalaba ule alikosulibiwa Yesu. Nakutolea nafsi yangu na mali yangu yote. Pokea kila tendo langu jema ukalisindikize kwa Mwanao, Mama, nifanye nistahili kuitwa mtumishi wa Maria, Simama karibu yangu katika matendo yangu yote ili yafanwe kwa sifa ya Mungu. Ulivyosimama karibu kabisa ya Mwanao alipokufa msalabani uwe karibu nami saa ya kufa kwangu. Nijalie niweze kutaja jina lako na la Mwana wako nikisema: “Yesu, Maria na Yosef mnisaidie saa ya kufa kwangu. Yesu, maria na Yosef, naomba nife kwa amani kati yenu!” . Amina.

SALA KWA MAMA WA UCHUNGU KUOMBA NEEMA YA PEKEE

Ee Mama mbarikiwa na Bikira mwenye uchungu, Malkia wa Mashahidi, uliyesimama chini ya msalaba na uliyemtazama Mwana wako akifa, unitazame kwa huruma ya kimama ninayekusikitikia. Kwa sababu ya upanga uliochoma moyo wako, kwa mateso ya maisha yako nakuomba uniangalie kwa wema ukasikilize maombi yangu. Nakuomba, ee Mama, uniombee daima kwa Mwana wako, najua hawezi kukuvyima wewe kitu chochote. Basi, ufanye, Moyo wa Mwanao ukubali kunijalia ombi langu hili …………………(taja ombi lako).
Maana nitamkimbilia nani katika mahitaji na misiba yangu isipokuwa kwako, ee Mama wa huruma? Wewe hasa unaweza kutusaidia sisi tulio bado katika bonde la machozi kwa sababu ulishiriki mateso ya Mwanao kutukomboa. Umtolee Yesu tone moja la Damu yake takatifu. Umkumbushe ya kuwa wewe ni matumaini, furaha na maisha yetu ukanipatie jambo ninalokuomba kwa Yesu Kristo, bwana wetu. Amina.

Sala za kuheshimu Damu Takatifu ya Yesu

Tusali kila siku sala hizi, angalau kwa mwezi wa saba (Julai) kila mwaka, mwezi wa kuheshimu Damu Takatifu ya Mkombozi wetu.

Yesu alimwahidi Mt. Brigita wa Sweden kwamba wale watakaosali Baba Yetu 7 na Salamu Maria 7 kwa miaka 12 kwa kuheshimu damu yake takatifu na kutafakari juu ya Kutahiriwa kwake, jasho lake la damu, kupigwa kwake mijeledi, kuvikwa taji la miiba, kuchukua kwake Msalaba, kusuliwa kwake na kuchomwa ubavuni; watapata neema 5 zifuatazo: (1) Hawataingia toharani, (2) Yesu atawapa cheo cha mashahidi waliomwaga damu yao kwa ajili ya imani, (3) Yesu atawadumisha jamaa zake watatu katika hali ya neema, (4) Roho za jamaa zake zitakingwa na Jehanam mpaka kizazi cha nne, (5) Mwezi kabla ya kufa, Yesu atawajulisha. Wakifa kabla ya kutimiza miaka ile, watahesabiwa wamemaliza.

Ee Yesu, sasa ninataka kusali Baba yetu mara saba nikiungana na ule upendo ambao kwao uliitakasa sala hii katika Moyo wako. Uichukue kutoka mdomoni mwangu hadi moyoni mwako. Uiboreshe na kuikamilisha hivyo kwamba iupatie heshima na furaha kwa Utatu Mtakatifu kama vile Wewe ulivyoupatia kupitia sala hii wakati ulipokuwa bado hapa duniani. Utukuzwe ee Yesu, itukuzwe Damu Yako Takatifu sana uliyoimwaga kutoka katika Majeraha Yako Matakatifu.

1. Yesu anatahiriwa.

Tafakari fupi (kimya kidogo). Baba Yetu …. Salamu Maria …. Baba wa Milele, kupitia mikono safi ya Maria na Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutolea Majeraha ya kwanza, maumivu ya kwanza na Damu ya kwanza aliyomwaga Mwanao mpenzi, Bwana wetu Yesu Kristu, kwa ajili ya malipizi ya dhambi zangu na dhambi za dunia nzima, kwa ajili ya ulinzi dhidi ya dhambi ya kwanza ya mauti, hasa kati ya ndugu zangu.

2. Yesu anatokwa Jasho la Damu bustanini Gethsemane.

Tafakari fupi (kimya kidogo). Baba Yetu …. Salamu Maria …. Baba wa Milele, kupitia mikono safi ya Maria na Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutolea mateso na mahangaiko makali sana ya moyoni, ya Bwana wetu Yesu Kristu katika mlima wa mizeituni na kila tone la jasho lake la damu, kwa ajili ya malipizi ya dhambi zangu za kimoyomoyo, na dhambi za namna hiyo zinazotendwa na dunia nzima, kwa ajili ya ulinzi dhidi ya dhambi za moyoni na kwa ajili ya kueneza upendo wa kiMungu na wa kindugu.

3. Yesu anapigwa mijeledi.

Tafakari fupi (kimya kidogo). Baba Yetu …. Salamu Maria …. Baba wa Milele, kupitia mikono safi ya Maria na Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutolea majeraha elfu elfu aliyopata, maumivu makali sana na Damu Takatifu sana aliyomwaga, alipopigwa mijeledi, kwa ajili ya malipizi ya dhambi zangu za tamaa ya mwili, kwa malipizi ya dhambi za tamaa ya mwili za wanadamu wote, kwa ajili ya ulinzi dhidi ya dhambi za tamaa ya mwili, na kwa kulinda usafi wa moyo, hasa kati ya ndugu zangu.

4. Yesu anavikwa taji la miiba.

Tafakari fupi (kimya kidogo). Baba Yetu …. Salamu Maria …. Baba wa Milele, kupitia mikono safi ya Maria na Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutolea majeraha, maumivu na Damu Takatifu kutoka katika Kichwa Kitakatifu cha Yesu wakati alipovikwa taji la miiba, kwa ajili ya malipizi ya dhambi zangu za rohoni, kwa malipizi ya dhambi za rohoni za wanadamu wote, kwa ajili ya ulinzi dhidi ya dhambi za rohoni, na kwa ajili ya kueneza Ufalme wa Kristu hapa duniani.

5. Yesu anachukua Msalaba.

Tafakari fupi (kimya kidogo). Baba Yetu …. Salamu Maria …. Baba wa Milele, kupitia mikono safi ya Maria na Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutolea mateso ya njia ya Msalaba, hasa donda lake la begani na Damu Takatifu iliyomwagika, kwa ajili ya malipizi ya dhambi zangu za ukaidi dhidi ya msalaba, na dhambi za ukaidi dhidi ya msalaba za wanadamu wote, malalamiko yote dhidi ya mipango yako mitakatifu na dhambi zote za ulimi, kwa ajili ya ulinzi dhidi ya dhambi za ulimi na kwa ajili ya upendo wa kweli kwa Msalaba.

6. Yesu anasulibiwa.

Tafakari fupi (kimya kidogo). Baba Yetu …. Salamu Maria …. Baba wa Milele, kupitia mikono safi ya Maria na Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutolea Mwanao Msalabani, kupigwa kwake misumari na kuinuliwa kwake, madonda yake mikononi na miguuni na mifereji mitatu ya Damu yake Takatifu iliyomwagika kutoka katika majeraha haya, mateso yake makali sana ya mwili na roho, kifo chake kitakatifu, ukumbusho usio wa kumwaga wa damu wa kifo hiki katika Misa zote Takatifu ulimwenguni, kwa ajili ya majeraha yote yanayosababishwa na ukaidi wa nadhiri na kanuni katika madaraja matakatifu, kwa ajili ya malipizi ya dhambi zangu zote na za ulimwenguni mzima, kwa ajili ya wagonjwa na wanaokufa, kwa ajili ya mapadre watakatifu na walei, kwa ajili ya nia za Baba Mtakatifu za kukarabati familia za kikristu, kwa ajili ya kuimarika kwa imani ya kikristu ulimwenguni, kwa ajili ya nchi yetu na muungano kati ya mataifa ndani ya Kristu na Kanisa lake, na kwa ajili ya wokovu wa dunia nzima.

7. Yesu anachomwa kwa mkuki moyoni.

Tafakari fupi (kimya kidogo). Baba Yetu …. Salamu Maria …. Baba wa Milele, ukubali kupokea, kwa ajili ya mahitaji ya Kanisa Takatifu na kwa ajili ya malipizi ya dhambi za wanadamu wote, Damu na Maji Takatifu vilivyomwagika kutoka jeraha la Moyo Mtakatifu wa Yesu. Utuhurumie. Damu Takatifu ya Yesu, tone lile la mwisho lililomwagika kutoka katika Moyo wake Mtakatifu, unioshe mimi na wengine wote dhambi zetu zote! Ee Maji kutoka katika Moyo Mtakatifu wa Yesu, unioshe na adhabu zote za dhambi zangu na uizime miale ya moto wa toharani kwa ajili yangu na kwa ajili ya roho zote zilizomo toharani. Amina.

Katika mwaka wa Kanisa wa kiliturjia, mwezi Julai ni wa kuiheshimu Damu Takatifu ya Yesu.

SALA YA UHAI KWA MT. YOSEFU

(Sala hii inafaa sana kwa ajili ya kutetea uhai wa watoto wachanga wakiwa tumboni mwa mama zao, dhidi ya utoaji mimba au hatari nyingine dhidi ya uhai wa binadamu)

Ee Mt. Yosefu, wewe ni Mchumba safi na Mpenzi wa Bikira Maria, u Baba Mlishi wa Yesu, mlinzi na mtunzaji wa Familia Takatifu, na wa familia zote. Tuna imani kabisa katika uangalizi wako uliojaa upendo, juu ya uhai mpya, na uaminifu wako kwa familia.

Tunaweka jitihada zetu chini ya ulinzi wa sala zako. Utusaidie daima katika kutetea zawadi ya uhai wa binadamu, ili ukue hadi uzima wa milele ulioahidiwa na kujaliwa kwetu na Mwanao, Ndugu yetu, Yesu Kristu.
Amina.

Shopping Cart
1
    1
    Your Cart
    🏠 Home 📖 Reading 🖼️ Gallery 💬 AI Chat 📘 About