Sala za Katoliki: Sala Muhimu Kwa Mkristu Mkatoliki

SALA YA KUMWOMBA MTAKATIFU TERESIA WA MTOTO YESU

Ee Mtakatifu Teresia wa mtoto Yesu, ulistahili kuitwa Msimamizi wa misioni katoliki za dunia yote. Kumbuka ile tamaa yako kuu uliyoonyesha huku duniani ya ” kusimika Msalaba wa Yesu Kristu, katika nchi zote na kuhubiri Injili mpaka mwisho wa dunia” . Twakuomba kwa ajili ya maagano yako, wasaidie mapadre, wamisionari, na kanisa zima.

Ee Mtakatifu Teresia wa mtoto Yesu ” Msimamizi wa misioni” UTUOMBEE

ROZARI YA MATESO SABA YA BIKIRA MARIA

Tumia Rozari ya Mateso Saba ya Bikira Maria iliyo na mafungu 7 yaani mateso 7 yenye Salamu Maria saba kwa kila teso.

TESO LA KWANZA

Mzee Simeoni aliagua kuwa Moyo wa Mama Maria utachomwa kwa upanga.
Tuombe neema ya kuvumilia mateso.
Mama wa mateso utuombee.
Baba Yetu ……… Salamu Maria x7. Atukuzwe Baba ……
Mateso na majonzi ya Mama Maria hayana mfano.

TESO LA PILI

Maria na Yosefu walikimbilia Misri usiku ili kumficha Mtoto Yesu asiuawe na Herodi.
Tuombe neema ili miili yetu iwe kimbilio lake Yesu.
Mama wa mateso utuombee.
Baba Yetu ……… Salamu Maria x7. Atukuzwe Baba ……
Mateso na majonzi ya Mama Maria hayana mfano.

TESO LA TATU

Mama Maria aliona uchungu sana Mtoto Yesu alipopotea kwa siku tatu.
Tuombe neema ya kudumu na Yesu mioyoni mwetu.
Mama wa mateso utuombee.
Baba Yetu ……… Salamu Maria x7. Atukuzwe Baba ……
Mateso na majonzi ya Mama Maria hayana mfano.

TESO LA NNE

Mama Maria aliona uchungu sana alipokutana na Mwanae Yesu katika njia ya Msalaba.
Tuombe neema ya kudumu na Yesu siku zote.
Mama wa mateso utuombee.
Baba Yetu ……… Salamu Maria x7. Atukuzwe Baba ……
Mateso na majonzi ya Mama Maria hayana mfano.

TESO LA TANO

Mama Maria aliona uchungu sana alipomwona Mwanae Yesu akisulibiwa Msalabani.
Tuombe neema ya kufa mikononi mwa Yesu na Maria.
Mama wa mateso utuombee.
Baba Yetu ……… Salamu Maria x7. Atukuzwe Baba ……
Mateso na majonzi ya Mama Maria hayana mfano.

TESO LA SITA

Mama Maria aliona uchungu sana alipopakata maiti ya Mwanae Yesu baada ya kushushwa Msalabani.
Tuombe neema ya kutotenda dhambi.
Mama wa mateso utuombee.
Baba Yetu ……… Salamu Maria x7. Atukuzwe Baba ……
Mateso na majonzi ya Mama Maria hayana mfano.

TESO LA SABA

Mama Maria aliona uchungu sana aliporudi nyumbani baada ya kumzika Mwanae Yesu
Tuombe neema ya kitulizo kwa Mama Maria.
Mama wa mateso utuombee.
Baba Yetu ……… Salamu Maria x7. Atukuzwe Baba ……
Mateso na majonzi ya Mama Maria hayana mfano.

SALA YA NOVENA YA SIKU TISA KWA MT. YOSEFU, YA ZAMANI, MIAKA 1900 ILIYOPITA

Ee Mt. Yosefu, ambaye ulinzi wako ni mkubwa, wenye nguvu na wa haraka mbele ya Kiti cha Enzi cha Mungu, ninakukabidhi nia na haja zangu zote. Ee Mt. Yosefu, unisaidie kwa maombezi yako yenye nguvu, na unipatie kutoka kwa Mwanao Mungu, baraka zote za kiroho, kwa njia ya Kristu Bwana wetu, ili nikishapata msaada wako wa mbinguni ningali bado hapa duniani, niweze nami kumsifu, kumwabudu na kumshukuru Mungu aliye Baba mwema kabisa kushinda wote. Ee Mt. Yosefu, sichoki kamwe kufikiri moyoni kwa upendo, jinsi Mtoto Yesu alivyokuwa amesinzia mikononi mwako. Akiwa amepumzika hivyo karibu na moyo wako, sithubutu kujongea, nisije nikamsumbua, bali nakuomba wewe umkumbatie na kumbusu kwa niaba yangu na kumwambia anipe busu lake nitakapovuta pumzi yangu ya mwisho.
Mtakatifu Yosefu Msimamizi wa wanaozimia roho; Utuombee.
Amina.

Sala hii ilipatikana katika mwaka wa hamsini wa Bwana na Mwokozi Wetu Yesu Kristu. Mnamo mwaka 1505 Baba Mtakatifu alimtumia sala hii Mfalme Charles wakati alipokuwa anaenda vitani. Yeyote atakayeisoma sala hii, au kuisikia ikisomwa, au kuibeba, hatakufa kifo cha ghafla,hatazama majini, hatadhurika kwa sumu, wala hataanguka katika mikono ya adui zake, au kuunguzwa katika moto wowote ule, au kushindwa katika vita.

Sali sala hii kwa siku tisa mfululizo, kwa kuomba jambo lolote unalolihitaji. Haijawahi kusikika kuwa sala hii imeshindwa jambo.

SALA KWA MT. YOSEFU KWA AJILI YA KULIOMBEA KANISA LA MAHUJAJI

Ee Mtukufu Mt. Yosefu, ulichaguliwa na Mungu kuwa Baba Mlishi wa Yesu, mchumba safi kabisa wa Maria Bikira Milele, na mkubwa wa Familia Takatifu. Umechaguliwa na Mwakilishi wa Kristu kama Msimamizi wa kimbingu na mlinzi wa Kanisa alilolianzisha Kristu. Ndiyo maana ninakuomba kwa matumaini makuu usaidizi wako wenye nguvu kwa ajili ya Kanisa zima duniani.

Mlinde kwa namna ya pekee, kwa upendo wa kikweli wa ki-baba, Baba Mtakatifu na Maaskofu wote na Mapadre wenye ushirika na Kiti cha Petro. Uwe mlinzi wao wote wanaotumikia wokovu wa wanadamu kati ya majaribu na mahangaiko ya maisha haya, na utujalie kwamba watu wote wa dunia hii wamfuate Kristu na Kanisa alilolianzisha.

Mpendwa Mtakatifu Yosefu, ukubali majitoleo ya nafsi yangu ambayo sasa ninafanya. Ninajiweka wakfu kwako kwa ajili ya utumishi wako, ili daima wewe uwe baba yangu, mlinzi wangu, na kiongozi wangu katika njia ya wokovu. Unijalie usafi mkuu wa moyo na matamanio makuu ya maisha ya kiroho. Unijalie ili matendo yangu yote, kwa mfano wako, yawe kwa ajili ya sifa na utukufu wa Mungu, pamoja na Moyo wa kimungu wa Yesu, moyo safi wa Maria, na moyo wako wa ki-baba. Uniombee, nami nishiriki kifo chako cha furaha na kitakatifu.
Amina.

Novena ya Noeli

Novena ya Noeli (maarufu kama novena ya Mt. Andrea)

Husaliwa kuanzia tar 30 Nov hadi usiku wa Noeli, tar 24 Disemba. Inajulikana kama novena ya Mt. Andrea kwa sababu novena hii huanza kusaliwa katika siku ya kumbukumbu ya Mt. Andrea Mtume.

“IHESHIMIWE, NA IBARIKIWE, SAA ILE NA WAKATI ULE, AMBAO MWANA WA MUNGU, ALIZALIWA NA BIKIRA MBARIKIWA SANA, USIKU WA MANANE, KULE BETHLEHEM, WAKATI WA BARIDI KALI.
WAKATI HUO, UPENDE E MUNGU WANGU, KUSIKIA MAOMBI YANGU, NA KUNIJALIA YALE NINAYOYAOMBA KWAKO, KWA NJIA YA MASTAHILI YA MWOKOZI WETU YESU KRISTO, NA YA MAMA YAKE MBARIKIWA. AMINA. (Sali mara 15 kwa siku).

Inasadikika kuwa chochote uombacho kwa imani kwa sala hii utakipata mradi kipatane na mapenzi ya Mungu. Sali na watoto/ familia kuwatafakarisha na kuwaongezea matazamio juu ya sikukuu ya Noeli.

Isambaze sala hii kwa wengine.

Kanuni ya imani

Nasadiki kwa Mungu, Baba Mwenyezi,/ mwumba mbingu na dunia./ Na kwa Yesu Kristu, Mwanaye wa pekee, Bwana wetu;/ aliyetungwa kwa Roho Mtakatifu,/ akazaliwa na Bikira Maria,/ akateswa kwa mamlaka ya Ponsyo Pilato,/ akasulubiwa, akafa, akazikwa,/ akashukia kuzimu;/ siku ya tatu akafufuka katika wafu;/ akapaa mbinguni;/ amekaa kuume kwa Mungu Baba Mwenyezi;/ toka huko atakuja kuwahukumu wazima na wafu. Nasadiki kwa Roho Mtakatifu,/ Kanisa takatifu katoliki,/ ushirika wa Watakatifu,/ maondoleo ya dhambi,/ ufufuko wa miili,/ uzima wa milele. Amina.

SALA YA MAJITOLEO KWA MAMA WA HUZUNI

Mama Mtakatifu, Mama wa Mungu na Malkia wa Mashahidi, leo nakuchagua Wewe uwe mfano wangu, mkingaji na mteteaji wangu. Naweka roho fukara katika moyo wako uliotobolewa na panga nyingi za mateso. Unipokee mimi niwe mtumishi wako wa pekee na mshiriki wa mateso yako. Nijalie nguvu niwe daima karibu na msalaba ule alikosulibiwa Yesu. Nakutolea nafsi yangu na mali yangu yote. Pokea kila tendo langu jema ukalisindikize kwa Mwanao, Mama, nifanye nistahili kuitwa mtumishi wa Maria, Simama karibu yangu katika matendo yangu yote ili yafanwe kwa sifa ya Mungu. Ulivyosimama karibu kabisa ya Mwanao alipokufa msalabani uwe karibu nami saa ya kufa kwangu. Nijalie niweze kutaja jina lako na la Mwana wako nikisema: “Yesu, Maria na Yosef mnisaidie saa ya kufa kwangu. Yesu, maria na Yosef, naomba nife kwa amani kati yenu!” . Amina.

SALA MBELE YA KITI CHA ENZI CHA MUNGU

Sali Atukuzwe 7 kwa heshima ya Malaika 7 wateule ujipatie neema ya kuepa dhambi mbaya saba na kutujaza mapaji saba ya Roho Mtakatifu.

TUOMBE
Ee Mungu Mwenyezi wa milele, kwa wema na huruma yako ya ajabu, umetaka watu wako waokoke, ukamweka Malaika Mkuu Mikaeli kuwa Mkuu wa Kanisa lako, Utukinge na adui zetu, wasitusmbue saa ya kufa kwetu, bali tuongozwe naye kwenye utukufu wako Mkuu. Tunaomba hayo kwa njia ya Bwana Wetu Yesu Kristo. Amina.

Utuombee Ee Mtukufu Mtakatifu Mikaeli Mkuu wa Kanisa la Yesu Kristo, tujaliwe ahadi za Kristo. Amina.

Sala ya Malaika wa Bwana

Malaika wa Bwana alimpasha habari Maria, naye akapata mimba kwa uwezo wa Roho Mtakatifu. Salamu Maria,….

Ndimi Mtumishi wa Bwana, nitendewe ulivyonena. Salamu Maria, ……
Neno wa Bwana akatwaa Mwili, akakaa kwetu. Salamu Maria, …..

Utuombee, ee Mzazi Mtakatifu wa Mungu, tujaliwe ahadi za Kristo.

Tuombe:

Tunakuomba ee Bwana, utie neema yako mioyoni mwetu, ili sisi tuliojua kwa maelezo ya Malaika, kwamba, Kristo Mwanao amejifanya mtu: kwa mateso na Msalaba wake, utufikishe kwenye utukufu wa ufufuko. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristo Bwana wetu, Amina.

SALA MBELE YA SAKRAMENTI KUU I

Utukuzwe ee Bwana wangu Yesu Kristo./ Uliagua kifo chako./ Katika karamu ya mwisho ulitumia mkate wa kidunia/ ukafanya mwujiza na kuugeuza/ kuwa Mwili wako azizi./ Kwa mapendo ukawapa Mitume Mwili huo/ uwe kumbukumbu la mateso yako mastahivu./ Uliwaosha miguu kwa Mikono yako Mitakatifu./

Uheshimiwe, ee Bwana wangu Yesu Kristo./ Kwa kuhofu mateso na kifo,/ Mwili wako usio na kosa ulitoka jasho la damu/ badala ya maji./ Juu ya hayo uliutimiza wokovu wetu/ uliokuwa umetaka kuufanya./ Hivyo ulionyesha waziwazi mapendo yako/ uliyo nayo kwa wanadamu./

Utukuzwe, ee Bwana wangu Yesu Kristo./ Ulipelekwa kwa Kayafa,/ Wewe uliye Hakimu wa wote./ Ukaruhusu kwa unyenyekevu kutolewa kwa Pilato/ uhukumiwe naye./

Utukufu uwe nawe, Bwana wangu Yesu Kristo,/ kwa kuwa ulivumilia kuchekwa tena/ uliposimama huko,/ umevaa joho jekundu,/ umetiwa taji ya miiba mikali sana Kichwani,/ ukavumilia kwa saburi kubwa/ kutemewa mate katika Uso wako mzuri,/ kufumbwa Macho,/ na kupigwa mno na wajeuri/ ngumi na makofi Mashavuni na Shingoni./

Sifa iwe nawe, Bwana wangu Yesu Kristo,/ Kwa uvumilivu mkubwa ulikubali kufungwa nguzoni,/ kupigwa mijeledi kijeuri,/ kujaa damu na hivyo kusukumwa barazani kwa Pilato./ Ulionekana kama mwanakondoo asiye na kosa./

Heshima iwe nawe, Bwana wangu Yesu Kristo./ Umehukumiwa Mwili wako mzima/ Mtukufu wenye kutoka damu/ ufe msalabani./ Ulichukua msalaba kwa Mabega yako Matakatifu/ na kuumwa sana./ Kwa ghadhabu walikusukuma mbele/ mpaka mahali pa mateso,/ wakakunyang’anya nguo zako./ Hivyo ulikubali kupigiliwa msalabani./

Heshima ya milele upate Wewe,/ Bwana wangu Yesu Kristo./ Ulipokuwa katika taabu kubwa hii,/ ulimkazia Mama yako mstahivu/ Macho yako ya hisani na mapendo/ na unyenyekevu,/ ndiye Mama yako asiyekosa hata mara moja/ wala kukubali dhambi yeyote./ Ulimweka katika ulinzi mwaminifu/ wa Mfuasi wako ili kumtuliza./

Milele utukuzwe, ee Bwana wangu Yesu Kristo./ Ulipokuwa mwenyewe taabani,/ uliwapa wakosefu wote/ matumaini ya kuondolewa dhambi/ kwa kumwahidia mnyang’anyi aliyekuendea/ utukufu wa paradisi kwa huruma yako./

Sifa ya milele iwe nawe, Bwana wangu Yesu Kristo,/ kwa kila saa ulipovumilia uchungu/ na taabu kubwa mno msalabani kwa ajili yetu sisi wakosefu,/ maumivu makali sana/ yaliyotoka katika majeraha yako,/ yakapenya bila huruma Roho yako Takatifu./ Yakaingia kikatili katika Moyo wako Mtakatifu/ hata ukakatika,/ ukapumua Roho yako,/ ukainama Kichwa,/ ukaweka Roho yako mikononi mwa Mungu, Baba yako./ Na baada ya kufa uliacha nyuma Mwili baridi./

Utukuzwe, ee Bwana wangu Yesu Kristo,/ kwa Damu yako azizi na kwa kifo chako kitakatifu/ ulizifidia roho za watu,/ ukazitoa ugenini/ na kuzipeleka kwa hisani yako katika uzima wa milele./

Milele uheshimiwe, Wewe Bwana wangu Yesu Kristo./ Siku ya tatu ulifufuka katika wafu,/ ukajionyesha kwa wafuasi wako,/ ukapaa mbinguni/ mbele ya macho yao siku ya arobaini./

Shangilio na sifa ya milele upate Wewe, Bwana wangu Yesu Kristo,/ kwa kuwa umewapelekea wafuasi wako mioyoni mwao/ Roho Mtakatifu,/ ukawasha rohoni mwao mapendo makuu ya Mungu./

Pia, utukuzwe, usifiwe na kushangiliwa milele, Bwana wangu Yesu Kristo./ Umekaa katika ufalme wako wa mbinguni/ juu ya kiti cha enzi cha Umungu wako,/ ukaishi pamoja na Viungo vyako vyote Vitakatifu./ Na hivyo utakuja tena/ kuzihukumu roho za wazima na wafu wote./ Unaishi na kutawala/ pamoja na Baba na Roho Mtakatifu,/ milele. Amina.

(Na Mt. Birgita wa Sweden)

ROZARI, MATENDO NA LITANI YA MAMA BIKIRA MARIA

Rozari ya Bikira Maria
Mwongozo wa namna ya Kusali Rozari Takatifu ya Mama Bikira Maria

Anza kusali Rozari kwa kuibusu miguu ya Bwana Yesu katika taswira (picha) yake Msalabani kisha fanya Ishara ya Msalaba ukiwa unasema “Kwa Jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina”.

Taja kwa ufupi nia za Rozari hii. Tangaza nia hizo kwa sauti kama mnasali wengi kwa pamoja, Mfano, “Tusali kuombea amani katika nchi yetu na ulimwenguni kote, na tuunganishe nia hizo na nia zetu sisi wenyewe, nk).

Baada ya Sala ya Nasadiki pamoja na ya Baba Yetu, tunamwomba Mungu (Utatu Mtakatifu) fadhila za Imani, Matumaini na Mapendo, zikiambatana na Salamu Maria tatu.

Mojawapo ya maneno yafuatayo huweza kutumika:
“Mungu Baba utuongezee Imani. Salamu Maria, …… Mungu Mwana utuongezee matumaini, Salamu Maria, …… Mungu Roho Mtakatifu washa nyoyo zetu kwa mapendo yako, Salamu Maria, …..”

Au;

“Utuongezee Imani ee Bwana, Salamu Maria,…. Utuongezee matumaini ee Bwana, Salamu Maria,…. Uwashe nyoyo zetu kwa mapendo yako ee Bwana, Salamu Maria, …..” Au;
“Salamu e uliyechaguliwa na Mungu Baba, Salamu Maria,….. Salamu e Mama wa Mungu Mwana, Salamu Maria,….. Salamu e Mchumba wa Mungu Roho Mtakatifu, Salamu Maria,……”
Atukuzwe Baba, na Mwana na Roho Mtakatifu, kama mwanzo na sasa na siku zote, na milele, Amina.

Ee Yesu wangu, utusamehe dhambi zetu, utuepushe na moto wa milele, ongoza roho zote mbinguni, hasa za wale wanaohitaji huruma yako zaidi.
Tuwasifu milele, Yesu, Maria na Yosef.

Kisha endelea na sala zinazofuata kama mpangilio unavyoonyesha hapo juu.

Kila baada ya Tendo moja na makumi ya Salamu Maria…, “Atukuzwe..”, “Ee Yesu wangu…” na “Tuwasifu milele…” kama muda unatosha wimbo ufaao wa Bikira Maria uimbwe (kama muda ni mfupi basi angalau ubeti mmoja mmoja uimbwe kila baada ya makumi hayo). Baada ya Wimbo, Tendo linalofuata litangazwe kwa sauti pamoja na tafakari fupi au ombi linaloambatana na Tendo husika kama inavyoonyeshwa hapa chini.

MATENDO YA ROZARI TAKATIFU

MATENDO YA FURAHA (Jumatatu na Jumamosi)

Tendo la kwanza; Malaika Gabrieli anampasha habari Maria kuwa atakuwa Mama wa Mungu. Tumwombe Mungu atujalie unyenyekevu.

Tendo la pili; Maria Mtakatifu anakwenda kumtembelea Elizabeti. Tumwombe Mungu atujalie mapendo ya jirani.

Tendo la tatu; Yesu anazaliwa Betlehemu. Tumwombe Mungu atujalie moyo wa ufukara

Tendo la nne; Yesu anatolewa hekaluni. Tumwombe Mungu atujalie usafi wa moyo.

Tendo la tano; Maria anamkuta Yesu hekaluni. Tumwombe Mungu atujalie kuwatii wakubwa wetu.

MATENDO YA UCHUNGU (Jumanne na Ijumaa)

Tendo la kwanza; Yesu anatoka jasho la damu kwa ajili yetu. Tumwombe Mungu atujalie sikitiko la dhambi.

Tendo la pili; Yesu anapigwa kwa mijeledi kwa ajili yetu. Tumwombe Mungu atujalie kuacha dhambi za uchafu.

Tendo la tatu; Yesu anatiwa miiba kichwani kwa ajili yetu. Tumwombe Mungu atujalie kushinda kiburi.

Tendo la nne; Yesu anachukua Msalaba kwa ajili yetu. Tumwombe Mungu atujalie kuvumilia taabu.

Tendo la tano; Yesu anakufa Msalabani. Tumwombe Mungu atujalie kuwapenda Yesu na Maria.

MATENDO YA UTUKUFU (Jumatano na Jumapili)

Tendo la kwanza; Yesu anafufuka. Tumwombe Mungu atujalie kugeuka watakatifu.

Tendo la pili; Yesu anapaa mbinguni. Tumwombe Mungu atujalie kwenda mbinguni.

Tendo la tatu; Roho Mtakatifu anawashukia Mitume. Tumwombe Mungu atujalie bidii katika dini yetu.

Tendo la nne; Bikira Maria anapalizwa mbinguni. Tumwombe Mungu atujalie kufa vizuri.

Tendo la tano; Bikira Maria anawekwa Malkia mbinguni. Tumwombe Mungu atujalie kudumu katika njia njema.

MATENDO YA MWANGA (Alhamisi)

Tendo la kwanza; Yesu anabatizwa Mto Jordani. Tumwombe Mungu atujalie uaminifu kwa ahadi zetu za ubatizo.

Tendo la pili; Yesu anageuza maji kuwa divai huko Kana. Tumwombe Mungu atujalie kuukoleza ulimwengu kwa chachu ya enjili.

Tendo la tatu; Yesu anatangaza Ufalme wa Mungu. Tumwombe Mungu atujalie kupokea Ufalme wake kwa toba ya kweli.

Tendo la nne; Yesu anageuka sura. Tumwombe Mungu atujalie neema ya kuung’arisha ulimwengu kwa uso wa Yesu.

Tendo la tano; Yesu anaweka Sakramenti ya Ekaristia. Tumwombe Mungu atujalie neema ya kujitoa sadaka kwa ajili ya wengine.

LITANIA YA BIKIRA MARIA

  • Bwana utuhurumie
  • Bwana utuhurumie
  • Kristo utuhurumie
  • Bwana utuhurumie
  • Bwana utuhurumie
  • Kristo utusikie
  • Kristo utusikilize
  • Mungu Baba wa Mbinguni,…… Utuhurumie
  • Mungu Mwana Mkombozi wa dunia ……… Utuhurumie
  • Mungu Roho Mtakatifu …….. Utuhurumie
  • Utatu Mtakatifu Mungu Mmoja …….. Utuhurumie
  • Maria Mtakatifu ………. utuombee
  • Mzazi Mtakatifu wa Mungu …….. utuombee
  • Bikira Mtakatifu Mkuu wa Mabikira …….. utuombee
  • Mama wa Kristo ……… utuombee
  • Mama wa Neema ya Mungu ………….. utuombee
  • Mama Mtakatifu sana ……… utuombee
  • Mama mwenye usafi wa Moyo ……….. utuombee
  • Mama mwenye ubikira ……….. utuombee
  • Mama usiye na doa ……….. utuombee
  • Mama mpendelevu ………. utuombee
  • Mama mstajabivu ………. utuombee
  • Mama wa Muumba ………. utuombee
  • Mama wa Mkombozi ………….. utuombee
  • Mama wa Kanisa……….. utuombee
  • Bikira mwenye utaratibu ………….. utuombee
  • Bikira mwenye heshima ………….. utuombee
  • Bikira mwenye sifa ………….. utuombee
  • Bikira mwenye uwezo ………….. utuombee
  • Bikra mweye huruma ………….. utuombee
  • Bikra mwaminifu………….. utuombee
  • Kioo cha haki ………….. utuombee
  • Kikao cha hekima ………….. utuombee
  • Sababu ya furaha yetu ………….. utuombee
  • Chombo cha neema ………….. utuombee
  • Chombo cha kuheshimiwa ………….. utuombee
  • Chombo bora cha ibada ………….. utuombee
  • Waridi lenye fumbo ………….. utuombee
  • Mnara wa Daudi ………….. utuombee
  • Mnara wa pembe ………….. utuombee
  • Nyumba ya dhahabu ………….. utuombee
  • Sanduku la Agano ………….. utuombee
  • Mlango wa Mbingu ………….. utuombee
  • Nyota ya asubuhi ………….. utuombee
  • Afya ya wagonjwa ………….. utuombee
  • Kimbilio la wakosefu ………….. utuombee
  • Mtuliza wenye huzuni ………….. utuombee
  • Msaada wa waKristo ………….. utuombee
  • Malkia wa Malaika ………….. utuombee
  • Malkia wa Mababu ………….. utuombee
  • Malkia wa Manabii ………….. utuombee
  • Malkia wa Mitume ………….. utuombee
  • Malkia wa Mashahidi ………….. utuombee
  • Malkia wa Waungama dini ………….. utuombee
  • Malkia wa Mabikira ………….. utuombee
  • Malkia wa Watakatifu wote ………….. utuombee
  • Malkia uliyepalizwa Mbinguni ………….. utuombee
  • Malkia wa Rozari takatifu ………….. utuombee
  • Malkia wa amani ………….. utuombee

  • Mwanakodoo wa Mungu uondoaye dhambi za dunia,…………..Utusamehe ee Bwana.
  • Mwanakondoo wa Mungu uondoaye dhambi za dunia,…………..Utusikilize ee Bwana
  • Mwanakondoo wa Mungu uondoaye dhambi za dunia,…………..Utuhurumie.

  • Utuombee, Mzazi Mtakatifu wa Mungu,…………..Tujaliwe ahadi za Kristo.

Tuombe

Ee Bwana Mungu, utujalie sisi watumishi wako afya ya roho na mwili siku zote; na kwa maombezi matukufu ya Maria Mtakaatifu Bikira daima, tuopolewe na mashaka ya saa, tupate na furaha za milele. Kwa Kristo Bwana wetu, Amina.

Karibu Vitatabu vya Kikatoliki

SALA YA NOVENA KWA MOYO MTAKATIFU WA YESU

Ee Moyo Mtakatifu sana wa Yesu, chemchemi ya kila baraka, ninakuabudu, ninakupenda, na kwa majuto halisi ya dhambi zangu, nakutolea moyo wangu dhaifu. Nifanye mnyenyekevu, mvumilivu na safi, nikikubali na kuyatii kabisa mapenzi yako. Ee Yesu mwema, unijalie niishi nawe na kwa ajili yako. Unilinde niwapo katikati ya hatari, unifariji katika mateso, unipe afya ya mwili na msaada katika mahitaji ya mwili, Baraka yako juu ya kila nilifanyalo, na neema ya kifo chema. Amina.

Ee Yesu uliyesema “Kweli nawaambieni, ombeni nanyi mtapewa, tafuteni nanyi mtapata, gongeni nanyi mtafunguliwa”, tazama ninagonga, ninatafuta na kuomba …….. (Taja ombi lako)
Baba Yetu….., Salamu Maria …….., Atukuzwe Baba……..
Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutumainia kwa moyo wote!

Ee Yesu uliyesema “Kweli nawaambieni, chochote mtakachomwomba Baba kwa jina langu mtapewa”, tazama kwa jina lako ninaomba ……. (Taja ombi lako)
Baba Yetu….., Salamu Maria …….., Atukuzwe Baba……..
Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutumainia kwa moyo wote!

Ee Yesu uliyesema “Kweli nawaambieni, mbingu na dunia zitapita lakini maneno yangu hayatapita kamwe”, tazama, nikitiwa nguvu na maneno yako ya kweli ninaomba …….. (Taja ombi lako)
Baba Yetu….., Salamu Maria …….., Atukuzwe Baba……..
Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutumainia kwa moyo wote!

Ee Moyo Mtakatifu wa Yesu, ambaye kwako ni kitu kimoja tu kisichowezekana, ambacho ni kutoacha kutowaonea huruma wenye huzuni, utuhurumie sisi wakosefu maskini na utujalie neema tukuombayo kwa njia ya Moyo Imakulata wa Maria, Mama yetu mpole.

Sali ‘Salamu Malkia’ na kuongezea, ‘Mtakatifu Yosefu Baba Mlishi wa Yesu, utuombee’.

P.S. – Sala hii ya Novena ilisaliwa kila siku na PADRE PIO kwa ajili ya kuwaombea wale wote waliomwomba msaada wa sala zake. Unaweza kuisali kwa namna tofauti tofauti. Mfano, kama Novena ya siku tisa, ambapo unasali sala hii mara moja au zaidi kila siku kwa siku tisa, au unaweza kuifanya kama Novena ya masaa, ambapo unasali sala hii kila baada ya saa moja kwa masaa tisa kwa siku hiyo hiyo, hasa kama kitu unachokiomba ni cha haraka au umesongwa moyoni. Vilevile unaweza kuifanya sala hii kama sehemu ya sala zako za kila siku katika mwezi Juni ambao ni mwezi uliotengwa na Kanisa kwa ajili ya kuuheshimu Moyo Mtakatifu wa Yesu, na hapo utaitumia kuwaombea watu waliokuomba msaada wa sala zako kama alivyofanya Mtakatifu Padre Pio. Pia unaweza kuitumia kama sala yako ya siku zote au ya mara kwa mara kwa ajili ya mahitaji mbalimbali.

SALA KWA BIKIRA MARIA KATIKA UKIWA WAKE

Nakusikitikia sana Mama Mtakatifu Maria kwa sababu ya ukiwa wako mkuu. Uchungu wako ulikuwa mkubwa sana ulipotazama mateso na kifo cha Mwana wako mpenzi. Muda ule uliweza kutuliz kidogo kwa sababu ya kumwona angali hai. Lakini je, baada ya kufa na kumzika? Sasa wewe ni mkiwa mkubwa mno! Uh, ukiwa wa pekee, uniombee mimi ninayempoteza mara nyingi kwa dhambi zangu. Unijalie nisimpoteze tena Yesu wangu kwa ubaya wa uvivu wangu, bali nimtumikie kiaminifu duniani hapa ili nimwone na kumfurahia milele mbinguni. Amina.

SALA KWA MAMA WA UCHUNGU KUOMBA NEEMA YA PEKEE

Ee Mama mbarikiwa na Bikira mwenye uchungu, Malkia wa Mashahidi, uliyesimama chini ya msalaba na uliyemtazama Mwana wako akifa, unitazame kwa huruma ya kimama ninayekusikitikia. Kwa sababu ya upanga uliochoma moyo wako, kwa mateso ya maisha yako nakuomba uniangalie kwa wema ukasikilize maombi yangu. Nakuomba, ee Mama, uniombee daima kwa Mwana wako, najua hawezi kukuvyima wewe kitu chochote. Basi, ufanye, Moyo wa Mwanao ukubali kunijalia ombi langu hili …………………(taja ombi lako).
Maana nitamkimbilia nani katika mahitaji na misiba yangu isipokuwa kwako, ee Mama wa huruma? Wewe hasa unaweza kutusaidia sisi tulio bado katika bonde la machozi kwa sababu ulishiriki mateso ya Mwanao kutukomboa. Umtolee Yesu tone moja la Damu yake takatifu. Umkumbushe ya kuwa wewe ni matumaini, furaha na maisha yetu ukanipatie jambo ninalokuomba kwa Yesu Kristo, bwana wetu. Amina.

Sala za kuheshimu Damu Takatifu ya Yesu

Tusali kila siku sala hizi, angalau kwa mwezi wa saba (Julai) kila mwaka, mwezi wa kuheshimu Damu Takatifu ya Mkombozi wetu.

Yesu alimwahidi Mt. Brigita wa Sweden kwamba wale watakaosali Baba Yetu 7 na Salamu Maria 7 kwa miaka 12 kwa kuheshimu damu yake takatifu na kutafakari juu ya Kutahiriwa kwake, jasho lake la damu, kupigwa kwake mijeledi, kuvikwa taji la miiba, kuchukua kwake Msalaba, kusuliwa kwake na kuchomwa ubavuni; watapata neema 5 zifuatazo: (1) Hawataingia toharani, (2) Yesu atawapa cheo cha mashahidi waliomwaga damu yao kwa ajili ya imani, (3) Yesu atawadumisha jamaa zake watatu katika hali ya neema, (4) Roho za jamaa zake zitakingwa na Jehanam mpaka kizazi cha nne, (5) Mwezi kabla ya kufa, Yesu atawajulisha. Wakifa kabla ya kutimiza miaka ile, watahesabiwa wamemaliza.

Ee Yesu, sasa ninataka kusali Baba yetu mara saba nikiungana na ule upendo ambao kwao uliitakasa sala hii katika Moyo wako. Uichukue kutoka mdomoni mwangu hadi moyoni mwako. Uiboreshe na kuikamilisha hivyo kwamba iupatie heshima na furaha kwa Utatu Mtakatifu kama vile Wewe ulivyoupatia kupitia sala hii wakati ulipokuwa bado hapa duniani. Utukuzwe ee Yesu, itukuzwe Damu Yako Takatifu sana uliyoimwaga kutoka katika Majeraha Yako Matakatifu.

1. Yesu anatahiriwa.

Tafakari fupi (kimya kidogo). Baba Yetu …. Salamu Maria …. Baba wa Milele, kupitia mikono safi ya Maria na Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutolea Majeraha ya kwanza, maumivu ya kwanza na Damu ya kwanza aliyomwaga Mwanao mpenzi, Bwana wetu Yesu Kristu, kwa ajili ya malipizi ya dhambi zangu na dhambi za dunia nzima, kwa ajili ya ulinzi dhidi ya dhambi ya kwanza ya mauti, hasa kati ya ndugu zangu.

2. Yesu anatokwa Jasho la Damu bustanini Gethsemane.

Tafakari fupi (kimya kidogo). Baba Yetu …. Salamu Maria …. Baba wa Milele, kupitia mikono safi ya Maria na Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutolea mateso na mahangaiko makali sana ya moyoni, ya Bwana wetu Yesu Kristu katika mlima wa mizeituni na kila tone la jasho lake la damu, kwa ajili ya malipizi ya dhambi zangu za kimoyomoyo, na dhambi za namna hiyo zinazotendwa na dunia nzima, kwa ajili ya ulinzi dhidi ya dhambi za moyoni na kwa ajili ya kueneza upendo wa kiMungu na wa kindugu.

3. Yesu anapigwa mijeledi.

Tafakari fupi (kimya kidogo). Baba Yetu …. Salamu Maria …. Baba wa Milele, kupitia mikono safi ya Maria na Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutolea majeraha elfu elfu aliyopata, maumivu makali sana na Damu Takatifu sana aliyomwaga, alipopigwa mijeledi, kwa ajili ya malipizi ya dhambi zangu za tamaa ya mwili, kwa malipizi ya dhambi za tamaa ya mwili za wanadamu wote, kwa ajili ya ulinzi dhidi ya dhambi za tamaa ya mwili, na kwa kulinda usafi wa moyo, hasa kati ya ndugu zangu.

4. Yesu anavikwa taji la miiba.

Tafakari fupi (kimya kidogo). Baba Yetu …. Salamu Maria …. Baba wa Milele, kupitia mikono safi ya Maria na Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutolea majeraha, maumivu na Damu Takatifu kutoka katika Kichwa Kitakatifu cha Yesu wakati alipovikwa taji la miiba, kwa ajili ya malipizi ya dhambi zangu za rohoni, kwa malipizi ya dhambi za rohoni za wanadamu wote, kwa ajili ya ulinzi dhidi ya dhambi za rohoni, na kwa ajili ya kueneza Ufalme wa Kristu hapa duniani.

5. Yesu anachukua Msalaba.

Tafakari fupi (kimya kidogo). Baba Yetu …. Salamu Maria …. Baba wa Milele, kupitia mikono safi ya Maria na Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutolea mateso ya njia ya Msalaba, hasa donda lake la begani na Damu Takatifu iliyomwagika, kwa ajili ya malipizi ya dhambi zangu za ukaidi dhidi ya msalaba, na dhambi za ukaidi dhidi ya msalaba za wanadamu wote, malalamiko yote dhidi ya mipango yako mitakatifu na dhambi zote za ulimi, kwa ajili ya ulinzi dhidi ya dhambi za ulimi na kwa ajili ya upendo wa kweli kwa Msalaba.

6. Yesu anasulibiwa.

Tafakari fupi (kimya kidogo). Baba Yetu …. Salamu Maria …. Baba wa Milele, kupitia mikono safi ya Maria na Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutolea Mwanao Msalabani, kupigwa kwake misumari na kuinuliwa kwake, madonda yake mikononi na miguuni na mifereji mitatu ya Damu yake Takatifu iliyomwagika kutoka katika majeraha haya, mateso yake makali sana ya mwili na roho, kifo chake kitakatifu, ukumbusho usio wa kumwaga wa damu wa kifo hiki katika Misa zote Takatifu ulimwenguni, kwa ajili ya majeraha yote yanayosababishwa na ukaidi wa nadhiri na kanuni katika madaraja matakatifu, kwa ajili ya malipizi ya dhambi zangu zote na za ulimwenguni mzima, kwa ajili ya wagonjwa na wanaokufa, kwa ajili ya mapadre watakatifu na walei, kwa ajili ya nia za Baba Mtakatifu za kukarabati familia za kikristu, kwa ajili ya kuimarika kwa imani ya kikristu ulimwenguni, kwa ajili ya nchi yetu na muungano kati ya mataifa ndani ya Kristu na Kanisa lake, na kwa ajili ya wokovu wa dunia nzima.

7. Yesu anachomwa kwa mkuki moyoni.

Tafakari fupi (kimya kidogo). Baba Yetu …. Salamu Maria …. Baba wa Milele, ukubali kupokea, kwa ajili ya mahitaji ya Kanisa Takatifu na kwa ajili ya malipizi ya dhambi za wanadamu wote, Damu na Maji Takatifu vilivyomwagika kutoka jeraha la Moyo Mtakatifu wa Yesu. Utuhurumie. Damu Takatifu ya Yesu, tone lile la mwisho lililomwagika kutoka katika Moyo wake Mtakatifu, unioshe mimi na wengine wote dhambi zetu zote! Ee Maji kutoka katika Moyo Mtakatifu wa Yesu, unioshe na adhabu zote za dhambi zangu na uizime miale ya moto wa toharani kwa ajili yangu na kwa ajili ya roho zote zilizomo toharani. Amina.

Katika mwaka wa Kanisa wa kiliturjia, mwezi Julai ni wa kuiheshimu Damu Takatifu ya Yesu.

Shopping Cart
15
    15
    Your Cart
    🏠 Home 📖 Reading 🖼️ Gallery 💬 AI Chat 📘 About