SALA KWA MALAIKA WAKO MLINZI
Malaika wa Mungu Mlinzi wangu mpenzi,
Ambaye upendo wake unanifanya niwepo hapa,
Uwe nami leo hii,
Kuniangaza na kunilinda,
Kunitawala na kuniongoza.
Amina.
Malaika wa Mungu Mlinzi wangu mpenzi,
Ambaye upendo wake unanifanya niwepo hapa,
Uwe nami leo hii,
Kuniangaza na kunilinda,
Kunitawala na kuniongoza.
Amina.
TUNAKUSHUKURU, EE MUNGU KWA MAPAJI YOTE ULIYOTUJALIA LEO AMINA
BABA YETUβ¦β¦β¦β¦β¦β¦.. SALAMU MARIAβ¦β¦β¦β¦β¦β¦.
SALA YA IMANIβ¦β¦.YA MATUMAINIβ¦β¦β¦YA MAPENDO
SALA YA KUTUBU
TUWAZE KATIKA MOYO WETU MAKOSA YA LEO TULIYOMKOSEA MUNGU KWA MAWAZO,KWA MANENO, KWA VITENDO NA KWA KUTOTIMIZA WAJIBU (HUSUBIRI KIDOGO)
NAKUUNGAMIA MUNGU MWENYEZI,NANYI NDUGU ZANGU,KWANI NIMEKOSA MNO KWA MAWAZO,KWA MANENO,KWA VITENDO NA KWA KUTOTIMIZA WAJIBU,NIMEKOSA MIMI,NIMEKOSA SANA.NDIYO MAANA NAKUOMBA MARIA MWENYE HERI,BIKIRA DAIMA,MALAIKA NA WATAKATIFU WOTE,NANYI NDUGU ZANGU,MNIOMBEENI KWA BWANA MUNGU WETU.
MUMNU MWENYEZI ATUHURUMIE ATUSAMEHE DHAMBI ZETU,ATUFIKISHE KWENYE UZIMA WA MILELE.AMINA
SALA YA KUOMBEA WATUβ¦β¦β¦β¦β¦β¦β¦β¦
KUSIFUβ¦β¦β¦β¦β¦β¦β¦β¦
Mtakatifu Mikaeli Malaika Mkuu, utulinde katika vita, uwe kinga yetu katika maovu na maoteo ya shetani, Mungu amtiishe, tunaomba sana, nawe Mkuu wa Majeshi ya Mbinguni kwa nguvu ya Mungu uwaangushe motoni shetani na pepo wabaya wengine wote, wanaozunguka duniani, ili kuzipoteza roho za watu.Β Amina.
Kwa ajili ya Baba Mtakatifu wetu ..(N); Bwana, umpe moyo wako wa uchungaji mwema
Kwa ajili ya warithi wa Mitume; Bwana, uwape wawe na uangalifu uliojaa upendo kwa mapadre wao
Kwa ajili ya Maaskofu wako waliochaguliwa na Roho Mtakatifu; Bwana, uwabakishe karibu na kondoo wako
Kwa ajili ya wachungaji wako; Bwana, uwafundishe kutumikia kuliko kutafuta kutumikiwa
Kwa ajili ya waungamishi na washauri wa kiroho; Bwana, uwafanye kuwa vyombo visikivu kwa Roho wako Mtakatifu
Kwa ajili ya mapadre wanaotangaza neno lako; Bwana, uwawezeshe kushirikisha Roho wako na Uzima wako
Kwa ajili ya mapadre wanaosaidia utume wa walei; Bwana, uwatie moyo wa kuwa mifano bora
Kwa ajili ya mapadre wanaofanya kazi na vijana; Bwana, uwajalie wawakabidhi vijana kwako
Kwa ajili ya mapadre wanaofanya kazi kati ya watu fukara; Bwana, uwajalie wakuone na wakutumikie kupitia hao
Kwa ajili ya mapadre wanaoangalia wagonjwa; Bwana, uwajalie wawafundishe thamani ya mateso
Kwa ajili ya mapadre fukara; – Uwasaidie ee Bwana
Kwa ajili ya mapade wagonjwa; – Uwaponye ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wazee; – Uwapatie tumaini la raha ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wenye huzuni na walioumizwa; -Uwafariji ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wanaohangaishwa na wale wanaosumbuliwa; – Uwape amani yako ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wanaodharauliwa na wanaonyanyaswa; – Uwatetee ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre waliokata tamaa; – Uwatie moyo ee Bwana
Kwa ajili ya wale wanaosomea upadre; – Uwape udumifu ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wote; – Uwape uaminifu kwako na kwa Kanisa lako ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wote; – Uwajalie utii na upendo kwa Baba Mtakatifu na kwa maaskofu wao ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wote; – Uwajalie waishi katika umoja na maaskofu wao ee Bwana
Tunawaombea mapadre wote; – Wawe wamoja kama Wewe na Baba mlivyo wamoja ee Bwana
Tunawaombea mapadre wote; – Waishi na kuendeleza haki yako ee Bwana
Tunawaombea mapadre wote; – Washirikiane katika umoja wa ukuhani wako ee Bwana
Tunawaombea mapadre wote, wakiwa wamejawa na uwepo wako; – Waishi maisha yao ya useja kwa furaha ee Bwana
Tunawaombea mapadre wote; – Wajalie ukamilifu wa Roho wako na uwageuze wafanane nawe ee Bwana
Kwa namna ya pekee, ninawaombea mapadre wale ambao kwa njia yao nimepokea neema zako. Ninamwombea padre aliyenibatiza na wale walioniondolea dhambi zangu, wakinipatanisha na Wewe na Kanisa lako.
Ninawaombea mapadre ambao nimeshiriki Misa walizoadhimisha, na walionipa Mwili wako kama chakula. Ninawaombea mapadre walionishirikisha Neno lako, na wale walionisaidia na kuniongoza kwako. Amina.
Ee Mt. Yosefu mwenye heri, tunakimbilia kwako katika masumbuko yetu, na kisha omba shime ya Mchumba wako Mtakatifu, tunaomba pia kwa matumaini usimamizi wako. Kwa ajili ya mapendo uliyompenda Bikira Mtakatifu Mzazi wa Mungu, na kwa ajili ya kumtunza Mtoto Yesu, twakuomba sana, utuangalie kwa wema sie tuliokuwa fungu lake Yesu Kristu, tukakombolewa kwa damu yake. Tusimamie katika masumbuko yetu kwa enzi na shime yako.
Ee Mlinzi amini wa jamaa takatifu, uwakinge watoto wateule wa Yesu Kristu.
Ee Baba uliyetupenda mno tuepushe na kilema chochote cha madanganyo na upotevu. Ee kinga yetu mwezaji, utusimamie huko juu mbinguni ulipo, tunaposhindana na wenye nguvu wakaao gizani. Kama vile siku za kale ukamwopoa Mtoto Yesu katika hatari ya kuuawa, na leo hivi likinge Kanisa Takatifu la Mungu katika mitego ya adui, na katika shida yote; mtunze daima kila mmoja wetu, tufwate mfano wako, ili tupate na msaada wako, kukaa na utakatifu maisha, kufa kifo chema, na kupata mbinguni makao ya raha milele.
Amina.
Ee Yesu Mfungwa wa Upendo wa Mungu,/ ninapofikiri Upendo wako na jinsi ulivyojitolea kwa ajili yangu,/ nashindwa kuelewa./ Unaficha Ukuu wako usiofahamika/ na kujidhihirisha kwa ajili yangu mimi mnyonge./ Ee Mfalme wa utukufu,/ unaficha uzuri wako,/ lakini jicho la moyo wangu/ linapenya pazia na kuona Majeshi ya Malaika/ wakikuimbia kwa heshima bila kukoma/ na nguvu zote mbinguni zikikusifu bila mwisho zikisema:/ βMtakatifu, Mtakatifu, Mtakatifu..β/
Ni nani awezaye kufahamu Upendo wako/ na huruma yako isiyo na kipimo kwa ajili yetu!/ Ee Mfungwa wa Upendo,/ nafungia moyo wangu masikini/ kwenye Tabarnakulo hii/ ili niweze kukuabudu usiku na mchana bila mwisho./ Najua hakuna kizuizi/ na hata kama naonekana kukaa mbali,/ lakini moyo wangu u pamoja nawe/ katika ibada hii./ Hakuna kinachoweza kuzuia upendo wangu kwako./ Kwangu hakuna kizuizi chochote./
Ee Utatu Mtakatifu,/ Mungu Mmoja usiyegawanyika,/ utukuzwe kwa zawadi yako hii kuu/ na agano hili la huruma!/
Nakuabudu,/ Bwana na Muumba uliyefichika katika Sakramenti Takatifu!/ Ee Bwana,/ nakuabudu kwa kazi zote za mikono yako/ zinazonifunulia Hekima yako kuu,/ Wema wako na Huruma yako kuu./ Uzuri uliousambaza hapa/ Uzuri ulio nao Wewe mwenyewe/ ambaye U Uzuri usioelezeka;/ na ingawaje umejificha na kusitiri uzuri wako,/ jicho langu,/ kwa mwanga wa imani linafika kwako,/ na roho yangu inapata kumtambua Muumba wake/ aliye Uzuri usiopimika,/ ulio juu ya kila uzuri,/ na moyo wangu unazama kabisa katika sala ya kukuabudu./
Bwana wangu na Muumba wangu,/ wema wako wanitia moyo wa kuongea nawe,/ Huruma yako huondoa kiambaza/ kitenganishacho Muumba na kiumbe./ Furaha ya moyo wangu,/ ee Mungu, ni kuongea na Wewe./ Yote ambayo moyo wangu unayatamni nayapata kwako./ Hapa ndipo mwanga wako unaponiangaza akili yangu/ na kuiwezesha kukujua Wewe zaidi na zaidi/ β ndipo mikondo ya neema inapoutiririkia moyo wangu,/ ndipo roho yangu inapochota uzima wa milele./ Ee Bwana na Muumba wangu,/ licha ya mapaji yote haya,/ unajitoa mwenyewe kwangu,/ ili uweze kujiunganisha na kiumbe dhaifu na maskini./
Ee Kristu,/ nafurahi sana nionapo kwamba unapendwa/ na kwamba sifa na utukufu wako vinaongezwa/ hasa ya Huruma yako./ Ee Kristu,/ sitaacha kamwe kuutukuza wema wako na huruma yako,/ hadi dakika ya mwisho ya maisha yangu./ Kwa kila tone la damu yangu/ na kwa kila pigo la moyo wangu/ naitukuza Huruma yako./ Natamani kugeuzwa kabisa/ na kuwa utenzi wa utukufu wako./ Naomba siku ya kufa kwangu/ popote nitakapokuwa nimelala,/ pigo la mwisho la moyo wangu/ liwe utenzi mpendevu/ usifuo Huruma yako isiyo na kipimo./ Amina
(Na Mt. Faustina Kowalska).
Ee Mungu Mwenyezi wa milele, mpaji wa mema yote, unayetusamehe na kutulinda. Utujalie sisi tunaokusihi, tufurahie hali njema ya hewa na mvua tunayoitamani na kuhitaji. Tutumie daima vipawa vya wema wako kwa ajili ya utukufu wa jina lako, na kwa ajili ya wokovu watu. Tunaomba hayo kwa njia ya Bwana watu Yesu Kristo Mwanao, anayeishi na kutawala nawe katika umoja wa Roho Mtakatifu, Mungu, daima na milele. Amina. `
`Baba Yetu………………. Salama Maria………… Atukuzwe Baba……….. `
K: `Bikra Maria mama wa msaada wa daima…. W: Utuombee na Utusaidie`
Ee Mtakatifu Teresia wa mtoto Yesu, ulistahili kuitwa Msimamizi wa misioni katoliki za dunia yote. Kumbuka ile tamaa yako kuu uliyoonyesha huku duniani ya ” kusimika Msalaba wa Yesu Kristu, katika nchi zote na kuhubiri Injili mpaka mwisho wa dunia” . Twakuomba kwa ajili ya maagano yako, wasaidie mapadre, wamisionari, na kanisa zima.
Ee Mtakatifu Teresia wa mtoto Yesu ” Msimamizi wa misioni” UTUOMBEE
Nakusikitikia sana Mama Mtakatifu Maria kwa sababu ya ukiwa wako mkuu. Uchungu wako ulikuwa mkubwa sana ulipotazama mateso na kifo cha Mwana wako mpenzi. Muda ule uliweza kutuliz kidogo kwa sababu ya kumwona angali hai. Lakini je, baada ya kufa na kumzika? Sasa wewe ni mkiwa mkubwa mno! Uh, ukiwa wa pekee, uniombee mimi ninayempoteza mara nyingi kwa dhambi zangu. Unijalie nisimpoteze tena Yesu wangu kwa ubaya wa uvivu wangu, bali nimtumikie kiaminifu duniani hapa ili nimwone na kumfurahia milele mbinguni. Amina.
Tuusifu Utatu Mtakatifu wa Mungu Mwenyezi, Baba, Mwana na Roho Mtakatifu, milele na milele, Amina.
Ee Utatu Mtakatifu wa Mwenyezi Mungu, Baba, Mwana na Roho Mtakatifu, nasadiki kuwa upo hapa na mahali pote. Ee Mungu wangu, umeniumba, umenikomboa, umenifanya mkristo, umenizidishia neema zako hapa duniani, umenitayarishia makao yangu mbinguni, umenijalia na siku hii nikutumikie. Ee Mungu wangu! Nakuabudu, nakushukuru, nakuomba toba, nakupenda! Ee Mungu wangu, nakutolea roho yangu, na mawazo, na maneno, na kazi, na furaha, na mateso yangu: uyapokee unipe neema yako nisikutende leo dhambi!
Ee Mama mbarikiwa na Bikira mwenye uchungu, Malkia wa Mashahidi, uliyesimama chini ya msalaba na uliyemtazama Mwana wako akifa, unitazame kwa huruma ya kimama ninayekusikitikia. Kwa sababu ya upanga uliochoma moyo wako, kwa mateso ya maisha yako nakuomba uniangalie kwa wema ukasikilize maombi yangu. Nakuomba, ee Mama, uniombee daima kwa Mwana wako, najua hawezi kukuvyima wewe kitu chochote. Basi, ufanye, Moyo wa Mwanao ukubali kunijalia ombi langu hili β¦β¦β¦β¦β¦β¦β¦(taja ombi lako).
Maana nitamkimbilia nani katika mahitaji na misiba yangu isipokuwa kwako, ee Mama wa huruma? Wewe hasa unaweza kutusaidia sisi tulio bado katika bonde la machozi kwa sababu ulishiriki mateso ya Mwanao kutukomboa. Umtolee Yesu tone moja la Damu yake takatifu. Umkumbushe ya kuwa wewe ni matumaini, furaha na maisha yetu ukanipatie jambo ninalokuomba kwa Yesu Kristo, bwana wetu. Amina.
Kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu. Amina.
Tunakushukuru, ee Mungu, kwa mapaji uliyotujalia leo. Amina.
Baba yetu β¦
Salamu Maria β¦
Mungu wangu, nasadiki maneno yote. Linayosadiki na linayofundisha Kanisa Katoliki la Roma. Kwani ndiwe uliyetufumbulia hayo. Wala hudanganyiki, wala hudanganyi. Amina.
Mungu wangu, natumaini kwako, nitapewa kwa njia ya Yesu Kristo. Neema zako hapa duniani, na utukufu mbinguni. Kwani ndiwe uliye agana hayo nasi, nawe mwamini. Amina.
Mungu wangu, nakupenda zaidi ya chochote. Kwani ndiwe mwema, ndiwe mwenye kupendeza. Nampenda na jirani yangu, kama nafsi yangu, kwa ajili yako. Amina.
Tuwaze katika moyo wetu makosa ya leo tuliyomkosea Mungu kwa mawazo, kwa maneno, kwa vitendo na kwa kutotimiza wajibu. (Husubiri kidogo ).
Nakuungamia Mungu Mwenyezi, nanyi ndugu zangu, kwani nimekosa mno, kwa mawazo, kwa maneno, kwa vitendo, na kwa kutotimiza wajibu.
Nimekosa mimi, nimekosa mimi, nimekosa sana. Ndiyo maana nakuomba Maria mwenye heri, Bikira daima, Malaika na Watakatifu wote, nanyi ndugu zangu, niombeeni kwa Bwana Mungu wetu.
Mungu Mwenyezi atuhurumie, atusamehe dhambi zetu, atufikishe kwenye uzima wa milele. Amina.
Ee Mungu, nawaombea watu wa nchi hii, wapate kusikia maneno yako na kukupenda wewe Bwana Mungu wetu.
Malaika mlinzi wangu, unilinde katika hatari zote za roho na za mwili. Amina.
(kipindi kisicho cha Pasaka)
Malaika wa Bwana alimpasha habari Maria.
Naye akapata mimba kwa uwezo wa Roho Mtakatifu.
Salamu, Maria,β¦..
Ndimi mtumishi wa Bwana.
Nitendewe ulivyonena.
Salamu, Mariaβ¦.
Neno la Mungu akatwaa mwili.
Akakaa kwetu.
Salamu, Mariaβ¦.
Utuombee, Mzazi mtakatifu wa Mungu.
Tujaliwe ahadi za Kristu.
Tuombe:
Tunakuomba, Ee Bwana, utie neema yako mioyoni mwetu, ili sisi tuliojua kwa maelezo ya Malaika kwamba Mwanao amejifanya Mtu kwa mateso na msalaba wake tufikishwe kwenye utukufu wa ufufuko. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristu Bwana wetu. AMINA.
Malkia wa mbingu, furahi, aleluya.
Kwani uliyestahili kumchukua, Aleluya.
Amefufuka alivyosema, Aleluya.
Utuombee kwa Mungu, Aleluya.
Furahi shangilia, ee Bikira Maria, Alaluya.
Kwani hakika Bwana amefufuka Aleluya.
Tuombe.
Ee Mungu, uliyependa kuifurahisha dunia kwa kufufuka kwake Bwana wetu Yesu Kristu, Mwanao, fanyiza, twakuomba, kwa ajili ya Bikira Maria, tupate nasi furaha za uzima wa milele. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristu Bwana wetu. Amina.
ATUKUZWE (mara tatu)
Atukuzwe Baba na Mwana na Roho Mtakatifu. Kama mwanzo na sasa na siku zote na milele. Amina.
Enyi Yesu, Maria na Yosefu nawatolea moyo na roho na uzima wangu!
Enyi Yesu, Maria na Yosefu mnijilie saa ya kufa kwangu!
Enyi Yesu, Maria na Yosefu mnijalie nife mikononi mwenu!
(Rehema ya siku 300).
Kwa heri Yesu mpenzi mwema,
Naenda usiudhike mno.
Nakushukuru, nakupenda,
Kwa hizo nyimbo za mwisho.
Asubuhi nitarudi.
Yesu kwa heri.
Kwa heri Mama mtakatifu,
Sasa napita pumzika.
Asante kwa moyo na nguvu,
Leo umeniombea.
Asubuhi nitarudi.
Mama kwa heri.
Kwa heri Yosefu mnyenyekevu,
Kazi zatimilizika.
Kama mchana, leo usiku,
Nisimamie salama.
Asubuhi nitarudi.
Yosefu kwa heri.
Kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu. Amina.
Mungu wangu naenda kulala naomba malaika 14, waende nami, wawili juu, wawili chini, wawili upande wa kuume, wawili upande wa kushoto, wawili wanifunike, wawili waniamshe, wawili wanipeleke juu mbinguni. Mimi mtoto mdogo, roho yangu ni ndogo, haina nafasi kwa mtu yoyote ila kwa Yesu pekee. Amina.
Anza Novena hii tarehe 19 Agosti ili kumalizia tarehe 27 Agosti na kusheherekea tarehe 28 Agosti, Sikukuu ya Mtk. Augustino wa Hippo.
Kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina
Tafakari
Pamoja na Mtakatifu Augustino tunasema β Umetuumba kwa ajili yako ee Bwana, kwani ni wewe peke yako ndie Mungu wetu, na nyoyo zetu hazitapumzika, hadi tupumzike ndani mwako.β
Tunapoanza Novena yetu kwa Mtakatifu Augustino tunamwomba Mungu neema ya kuwa na roho kama yake katika safari yetu katika kuzitambua nafsi zetu. Tunatafakari sisi ni nani na tunaelekea wapi kama wafuasi wa Mtakatifu Augustino katika dunia ya leo. Kama Mt Augustino alivyoutafuta ukweli bila kuchoka, nasi tutulie na kuruhusu maswali haya yaguse ufahamu wetu. Ni nini kinachonisababisha niendelee kumtafuta Mungu? Baada ya kumpata Mungu, ninamfanyaje awe hai kwa watu wale ninaoishi nao?
Kama kuna jambo moja Mt Augustino anasisitiza tena na tena kuhusu kumtafuta Mungu, ni kuwa lazima tuanze kumtafuta ndani mwetu. Huko ndiko tutakuta ukweli, mwanga na furaha katika Kristu mwenyewe. Ndani ya nafsi zetu ndiko tutasikilizwa tunaposali, katika nafsi zetu ndiko tutampenda Mungu na kumwabudu.
Bwana utuhurumie Bwana utuhurumie
Kristu utuhurumie Kristu utuhurumie
Bwana utuhurumie Bwana utuhurumie
Kristu utusikie Kristu utusikilize
Baba wa mbinguni Mungu utuhurumie
Mwana Mkombozi wa dunia Mungu utuhurumie
Roho Mtakatifu Mungu utuhurumie
Utatu Mtakatifu Mungu mmoja utuhurumie
Maria Mama wa Yesu utuombee
Maria Mama wa faraja utuombee
Maria Mama wa shauri jema utuombee
Mt. Augustimo nyota angavu ya Kanisa utuombee
Mt Augustino uliyejawa bidii kwa ajili ya kuutafuta utukufu wa Mungu utuombee
Mt. Augustino mtetezi jasiri wa Ukweli utuombee
Mt Augustino ushindi wa neema ya Mungu utuombee
Mt Augustino uliyewaka mapendo kwa Mungu utuombee
Mt Augustino mkuu sana na mnyenyekevu sana utuombee
Mt Augustino mfalme wa maaskofu na wanateolojia utuombee
Mt Augustino baba wa maisha ya kitawa utuombee
Mt Augustino mtakatifu kati ya wenye hekima na mwenye hekima kati ya watakatifu utuombee
Utuombee Mtakatifu Augustino β ili tustahili maagano ya Kristu.
Tuombe: Umetuumba kwa ajili yako ee Bwana, na nyoyo zetu hazitapumzika kamwe, hadi tutakapopumzika ndani mwako. Tunakuomba utubariki katika mahangaiko yetu ya kukutafuta wewe na utusaidie tunapokutana na makwazo. Tunapokupata, tunaomba utujalie neema ya kuwa waaminifu kwako ee Mungu wa historia, tuwe waaminifu kwa Yesu Kristu Mkombozi wetu, kwa Kanisa letu na mafundisho yake, na tuwe waaminifu katika wito wetu tuliouchagua katika kukutumikia wewe. Tunaomba hayo kwako wewe Baba mwema, kwa njia ya Kristu Bwana wetu na kwa maombezi ya Mtakatifu Augustino Msimamizi wa Jumuiya yetu, Amina.
Baba yetuβ¦β¦, Salamu Mariaβ¦.., Atukuzwe Babaβ¦β¦
Kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina
Tafakari
βIngia sasa, ndani ya moyo wako (Isaya 46:8) na uwe na imani, utamkuta Kristu humo. Humo anaongea na wewe, mimi, mwalimu, napaaza tu sauti yake lakini Yeye ndiye anayekufunza wewe kwa ufanisi zaidi katika utulivu wakoβ
Je tunapenda maisha ya utulivu ambapo tunapata muda wa kumtafakari Mungu na mambo anayotutendea katika maisha yetu? Kwa vile Yesu anaongea nasi katika utulivu, inatupasa tujifunze namna ya kuutunza utulivu ndani ya nafsi zetu licha ya mahangaiko na misukosuko ya maisha. Tutenge muda katika siku yetu ambapo tunaweza kutulia na Kristu na kumsikiliza, na wala sio sisi kuongea nae tu bila kumsikiliza naye pia. Soma Neno la Mungu kwa utulivu na kwa tafakari, na uone kama kuna kitu gani Mungu anakuaombia leo. Lazima tusafishe macho ya nyoyo zetu, ili tuweze kumwona Mungu ndani mwetu. Tunafanya hivyo kwa njia ya toba na maungamo. Kusafishwa vizuri ni jambo linaloweza kuambatana na maumivu, lakini tunahitaji usafi wa nafsi ili tuweze kuwa wasikivu zaidi kwa sauti ya Mungu ndani mwetu.
Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino
(Angalia siku ya kwanza)
Tuombe: Ee Baba mwema, tunataka kumfuata Mwanao Yesu kwa ukaribu zaidi. Utuwezeshe kuumbika upya nawe kwa mfano wa Mtakatifu Augustino katika maisha yake ya utulivu. Utusaidie kuacha mambo ya dunia hii yanayopita ili tupate hamu kubwa zaidi ya kukufuata. Imarisha imani yetu ili tusikie sauti yako katika maandiko: ili tuweze kukuona Wewe katika matukio ya maisha yetu. Tunaomba haya kwa njia ya Kristu Bwana wetu, anayeishi na kutawala nawe na Roho Mtakatifu, Mungu mmoja milele na milele. Amina.
Baba yetuβ¦β¦, Salamu Mariaβ¦.., Atukuzwe Babaβ¦β¦
Katika wito wetu uwao wote wa maisha yetu, tunaalikwa na Yesu tutafakari jinsi Martha alivyolalamika kuwa dada yake Maria alitumia muda wote katika kumsikiliza Yesu badala ya kusaidia kazi. Mt. Augustino akiwa kama mtawa aliuchukua mfano wa Martha na Maria kwa kushiriki kwa ukamilifu pia katika ujenzi wa uhai wa Kanisa kwa njia ya maandishi na kazi zake njema. Je mimi ninaoanishaje kati ya kutenda, kusali na tafakari takatifu?
Mt. Augustino anatufundisha kuwa tuwe tayari kuwatumikia wengine. Asiwepo mtu anayedhani kuwa anaweza kusali tu muda wote bila matendo, na wala asiwepo anayedhani atafaidika kwa matendo mengi yasiyosindikizwa na wingi wa sala. Tunapozigundua karama zetu Mungu alizotupa, tuwe tayari kuzishirikisha kwa wengine, kwani siku ya mwisho tutahukumiwa kwa namna ambavyo tuliwajali wengine. Kwa hiyo baada ya kumpata Mungu ndani mwako, usibaki humo, bali mgeukia yeye aliyekuumba. βTupande mlimani lakini tusijenge vibanda, tushuke tuwatumikie wengineβ
Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino
(Angalia siku ya kwanza)
Tuombe: Mungu Baba yetu, tunakutukuza na kukushukuru kwa kulijalia Kanisa lako mtakatifu mkuu namna hii. Tunapojitahidi kuishi roho na karama zake, utujalie neema za kukua katika utumishi wetu kwa wengine kwa njia ya matendo mema na pia katika maisha yetu ya sala, kwa mfano wa Mt. Augustino. Tunaomba hayo kwa Jina la Mwanao, Bwana na Mwokozi wetu. Amina.
Baba yetuβ¦β¦, Salamu Mariaβ¦.., Atukuzwe Babaβ¦β¦
Kwa Jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina.
Kuna wakati Mt. Augustino alikosa kitu chochote cha kuwapatia wasiojiweza, kwa sababu alikuwa anagawa kila alichoweza kwa wenye shida. Alipoishiwa kabisa, aliuza baadhi ya vitu alivyokuwa navyo ili kupata pesa iliyohitajika kwa ajili ya wenye shida.
Je, mimi pamoja na karama zote alizonijalia Mungu na vipaji vyote nilivyo navyo, ninajitahidi kuiga mfano wa Mt. Augustino katika kujitoa kwa wengine?
Umaskini wa kiinjili ni tofauti na umaskini wa kukosa mali au pesa. Ni namna moyo wa mtu anavyopenda kujitoa hata nje ya Jumuiya yake. Yesu Kristu alijitoa kabisa kwetu kwa kuuacha Umungu wake na kujitwalia ufukara wetu ili aweze kututajirisha. Hii ni changamoto kwetu kuwa tuwe tayari kujitoa kwa ajili ya wale wanaotuhitaji na Augustino ni mfano katika hilo. Tujitolee kufanya kazi za huruma, kwani mtu hataishi kwa mkate tu. Je tunawasaidiaje maskini walioko katika eneo letu? Ufalme wa Mungu utawafikiaje wengine kupitia kwetu. Mt Augustino anatupa changamoto leo kuwa tukubali kwa moyo mmoja kutoa vitu tulivyo navyo kwa ajili ya wengine, na tumfuate Kristu kwa moyo mpya na wa dhati.
Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino
(Angalia siku ya kwanza)
Tuombe: Tunakutukuza ee Bwana kwa kila unatupowezesha kushirikisha vile ulivyotujalia kwa ajili ya wahitaji, na kushikama katika upendo wako. Tunakuomba utujalie neema ya kudumu katika kushirikiana na kupendana ili tuwe mashahidi wa ukarimu wako mkuu. Tunaomba hayo kwa njia ya Bwana wetu Yesu Kristu, anayeishi na kutawala pamoja nawe na Roho Mtakatifu, Mungu mmoja daima na milele, Amina.
Baba yetuβ¦β¦, Salamu Mariaβ¦.., Atukuzwe Babaβ¦β¦
Kwa Jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina.
Mt. Augustino anashuhudia kuwa kitu kilichomweka karibu na marafiki zake kaka na dada zake ni kulekuongea na kucheka pamoja, kusaidiana, kusoma vitabu vinavyofanana vyenye mambo ya kujenga, kutaniana, kutofautiana mara kwa mara bila kukasirikiana, na alama za urafiki wetu zilijionyesha katika nyuso zetu, sauti zetu, macho yetu, na namna nyingi nyingineβ. Je mimi nafurahia mahusiano yaliyoko katika Jumuiya yetu? Kuna jambo gani naweza kufanya ili kuboresha mahusiano na wanajumuiya wenzangu?
Ushahidi wa mapendo ya kweli unakuja pale tunapokuwa tayari kubebeana mizigo yetu. Tunapojitahidi kuboresha mambo yanayohusu Jumuiya, ukweli ni kuwa tunaboresha mambo yetu binafsi pia. Tumwombe Mungu ili tuweze kuona namna ambavyo Jumuiya yetu inatutegema katika hali na namna mbalimbali na tuweze kuboresha mahusiano ili kukuza urafiki kati yetu kama anavyotufundisha Kristu.
Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino
(Angalia siku ya kwanza)
Tuombe: Bwana Mungu wetu, ulimfunulia Mt. Augustino uzuri ulioko katika urafiki uliojengwa katika misingi yako. Utujalie sisi tunaosimamiwa naye hapa duniani, tukue katika urafiki mtakatifu wa kijumuiya. Utujalie tufikie ukamilifu wa urafiki huo katika makao yetu ya mbinguni unakoishi na kutawala daima na milele, Amina.
Baba yetuβ¦β¦, Salamu Mariaβ¦.., Atukuzwe Babaβ¦β¦
Kwa Jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina.
Unyenyekevu unapatikana tu katika vita vya kiroho. Umuhimu wa majaribu katika maisha yako ya kiroho ni kuwa ni kwa kupitia tu majaribu hayo unajipatia unyenyekevu. Hapo ndio unauona umuhimu wa kumpokea yesu kuwa Mwokozi wako. Ukiwa na kiburi itakuwa ni kikwazo kikubwa kumpokea Mwokozi.
Kwa Augustino, unyenyekevu sio kujidharau, bali ni kujitahidi kufahamu karama alizotujalia Mungu na kuziendeleza. Ili kuwa mtu mnyenyekevu, jifahamu kuwa u mdhambi, na kuwa Mungu ndie anayeweza kukuweka huru. Fanya maungamo ya dhambi zako ili uwe wa kundi lake Mungu. Je, kama unyenyekevu ndio ukweli, ninajitahidije kuushirikisha ukweli huu kwa wengine katika Jumuiya yetu?
Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino
(Angalia siku ya kwanza)
Tuombe: Tuelekezee nyoyo zetu katika wema wako ee bwana, na geuza macho yetu mbali na kiburi na puuzi za dunia ili tuwe wafuasi wa maneno yako: Jifunzeni kwangu kwani mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo. Utujalie tukue kila siku katika unyenyekevu ambao unampendeza sana moyo wa Msimamizi wetu mt. Augustino. Amina.
Baba yetuβ¦β¦, Salamu Mariaβ¦.., Atukuzwe Babaβ¦β¦
Kwa Jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina.
Na tumpende Bwana wetu, tulipende kanisa lake. Tunampokea Roho Mtakatifu kadri tunavyolipenda Kanisa lake, kama tukiunganika pamoja kwa upendo, kama tukilifurahia jina katoliki na Imani yake. Tuamini kuwa tutakuwa na Roho Mtakatifu kwa kipimo cha upendo wetu kwa Kanisa lake. Tunalipenda Kanisa kama tulisimama imara katika ushirika na upendo.
Je ninalipenda Kanisa Katoliki? Ninajitahidi kujifunza imani hii na kuwashirikisha wengine au ninafuata mkumbo tu? Tunaalikwa kuishi kwa mfano wa Mt. Augustino ambaye alijielimisha kuhusu imani ya Kanisa Katoliki na kuikumbatia, kuitetea na kuishirikisha kwa wengine. Tusisite kujitoa katika dunia yetu ya leo pale tunapohitajika katika kueneza imani yetu. Tumwombe Mungu atujalie kwa mfano wa Mt. Augustino, moyo wa kusukumwa kuwashirikisha wengine imani iliyo hai kwa njia ya maneno, na matendo yetu, na hivyo kulitetea Kanisa la Bwana wetu Yesu Kristu kila wakati kwa injili iliyo hai.
Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino
(Angalia siku ya kwanza)
Tuombe: Baba mwenye upendo, tunakushukuru kwa zawadi ya Mt. Augustino uliyolipatia Kanisa lako. Kwa maombezi yake, sisi tunakuomba mwanga na ujasiri wa kujitoa bila masharti kwa unyenyekevu na daima katika huduma kwa wengine hasa wenye shida mbalimbali katika mahitaji ya mwili na ya roho. Tunaomba hayo, kwa njia ya Kristu Bwana wetu, Amina.
Baba yetuβ¦β¦, Salamu Mariaβ¦.., Atukuzwe Babaβ¦β¦
Kwa Jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina.
Jumuiya ni kiini cha Kanisa la leo, kama ilivyokuwa wakati wa mitume, wakifundishwa na mitume. Kama Jumuiya za kwanza za wakristu, tunaalikwa nasi leo tuwe na utayari katika kulisaidia Kanisa letu kwa njia mbalimbali hasa kwa kutoa zaka kwa wakati. Wakati huohuo pia tuelewe kuwa Roho Mtakatifu anatupatia vipaji na karama kuendana na mahitaji ya Kanisa lake, na hivyo tusisahau kushirikisha karama na vipaji hivyo kanisani kwetu ili kuujenga mwili wa Kristu. Kwa njia hiyohiyo, kazi zetu za kitume ziendane na mahitaji ya Kanisa letu leo hii kwani yote tunapewa na Roho wa Mungu kwa ajili ya utumishi kwa wengine. Je, shughuli zetu kama Jumuiya zinaendana na mahitaji ya Kanisa la Mungu kwa wakati huu? Ni mabadiliko gani tunaitwa kuyafanya kama Jumuiya na kama mtu mmoja mmoja ili kuboresha Kanisa kupitia Jumuiya yetu?
Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino
(Angalia siku ya kwanza)
Tuombe: Baba mwema, tunakuheshimu na kukutukuza kwa kutupatia Mt. Augustino. Tukiwa tumejiweka chini ya mafundisho yake, tunaomba neema na maongozi yako ili tuweze daima kuwa na utayari wa kulisaidia Kanisa letu kwa njia ya zaka na majitoleo kadri ya mahitaji, na utujalie neema tunazokuomba kwa njia ya Yesu Kristu, Bwana na Mwokozi wetu. Amina.
Baba yetuβ¦β¦, Salamu Mariaβ¦.., Atukuzwe Babaβ¦β¦
Kwa Jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina.
Mt. Augustine daima alikuwa tayari kuwasaidia wahitaji. Alitoa kila alichoweza vikiwemo vile vitu alivyotengewa kwa ajili ya matumizi yake yeye mwenyewe, na alipokosa kitu zaidi cha kutoa, aliyeyusha baadhi ya vyombo vya dhahabu vilivyokuwa vimewekwa wakfu kwa ajili ya kuuza na kisha aliwagawia maskini pesa iliyopatikana. Nasi mara nyingine inawezekana hatuna pesa mfukoni za kuwapa wale wanaohitaji tuwasaidie, lakini bila shaka tuna vitu. Mazao ya mashambani, mifugo, na vitu aina mbalimbali alivyotujalia Mungu. Kwa hiyo kila mmoja wetu ana kitu anachoweza kumpa mwenzake, pengine kama sina chochote zaidi angalau nina muda wa kusali na kuwaombea wengine kuendana na mahitaji ya Jumuiya yetu, au kuwatembelea wapweke, wenye majonzi na kuwafariji wengine. Cha msingi ni kumtazama Kristu, ambaye ana njaa na anateseka, ndani ya wenzetu.
Tunafanya vyema kushikamana na maskini. Sio maskini wa mali na pesa tu tunazungumzia hapa, bali pia maskini wa kiroho, wale wanaohitaji kuelekezwa, wenye mashaka, wapweke, wagonjwa, na wanaoteseka na dhambi. Tumwombe Mungu ili tuimarike kiroho, maana tutaweza kuwasaidia hao maskini tu pale ambapo sisi wenyewe tuna utajiri wa kiroho, yaani tunaye Kristu ndani mwetu.
Tunapomalizia Novena yetu ya siku tisa, tutafakari kuwa, kama Mt. Augustino angekuwa hai leo, angewajibika namna gani, angewasaidiaje maskini walioko katika Jumuiya yetu, mahali petu pa kazi na hata katika familia zetu?
Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino
(Angalia siku ya kwanza)
Tuombe: Bwana, tunakuomba urejeshe upya katika Kanisa lako roho kama ile uliyompa Mt. Augustino. Kwa mfano wake, tujazwe na kiu ya kukupata wewe peke yako kama chemchem ya hekima na chanzo cha upendo wa milele ili tuwe na utayari wa kuwasaidia wenzetu wote wenye shida za aina mbalimbali. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristu Bwana wetu. Amina.
Baba yetuβ¦β¦, Salamu Mariaβ¦.., Atukuzwe Babaβ¦β¦
Malaika wa Bwana alimpasha habari Maria, naye akapata mimba kwa uwezo wa Roho Mtakatifu. Salamu Maria,β¦.
Ndimi Mtumishi wa Bwana, nitendewe ulivyonena. Salamu Maria, β¦β¦
Neno wa Bwana akatwaa Mwili, akakaa kwetu. Salamu Maria, β¦..
Utuombee, ee Mzazi Mtakatifu wa Mungu, tujaliwe ahadi za Kristo.
Tuombe:
Tunakuomba ee Bwana, utie neema yako mioyoni mwetu, ili sisi tuliojua kwa maelezo ya Malaika, kwamba, Kristo Mwanao amejifanya mtu: kwa mateso na Msalaba wake, utufikishe kwenye utukufu wa ufufuko. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristo Bwana wetu, Amina.
Ee Mt. Yosefu, tunakuomba kwa ajili ya wale asio na ajira, kwa ajili ya wale wanaotaka kujipatia kipato chao na kulisha familia zao.
Wewe u Msimamizi wa wafanyakazi, tujalie kwamba pasiwepo kati yetu mtu asiye na ajira, na kwamba wale wote ambao wako tayari kufanya kazi waweze kuelekeza nguvu zao na uwezo wao katika kuwatumikia wanadamu wenzao na kujipatia kipato halali.
Wewe u Msimamizi wa familia, usiwaache wale wenye watoto wa kuwatunza na kuwalea wakose namna ya kufanya hivyo. Uwahurumie ndugu zetu waliokosa ajira na kugubikwa na umasikini kwa sababu ya magonjwa au mipango mibaya ya kijamii. Wasaidie viongozi wetu wa kisiasa na walioshika usukani katika nyanja mbalimbali za kiuzalishaji wavumbue suluhu mpya na za haki za jambo hili. Utujalie ili kila mmoja wetu apate kujipatia kipato halali na kufurahia fursa ya kushiriki kadri ya uwezo wake, katika maisha bora zaidi kwa wote. Utujalie ili wote tushiriki pamoja katika raslimali alizotujalia Mungu, na pia utujalie tuwe tayari daima kuwasaidia wale walio wahitaji kuliko sisi.
Amina.
Mungu wangu,
nasadiki maneno yote linalosadiki na linalofundisha kanisa katoliki la Roma;
Kwani ndiwe uliyefundisha hayo,
wala hudanganyiki,
wala hudanganyi. Amina
Kwa nguvu zangu zote za moyo wangu/ ninakuabudu ee Moyo Mtakatifu/ na Mwabudiwa sana,/ Moyo Mtakatifu wa Bwana wetu Yesu Kristu/ ambao ninataka kumpenda/ na kukusalimu kwa usikivu unaoendelea./ Kamwe nisikuudhi tena/ kwa sababu Wewe ni Mwema sana;/ Ee Mwema sana./ Ee Moyo Mtakatifu sana/ ninakupenda/ na ninataka kukupenda zaidi ya vitu vyote,/ kwa nguvu zangu zote/ na kwa uwezo wangu wote,/ ninatamani kuwa mali yako/ Wewe uliyejitoa Msalabani kwa ajili yangu/ kwa mateso makali./ Unionee huruma na udhaifu wangu/ na usiniruhusu kupotea./
Ninajitoa kabisa kwako/ ee moyo wa mapendo,/ kwa makusudi kuwa utu wangu,/ maisha na mateso yangu/ yalipie kukupenda,/ kukuheshimu/ na kukutukuza Wewe sasa na milele./ Ninakupenda ee Moyo Mwabudiwa wa Mwokozi wangu,/ ninakuomba kwako/ uamuru moyo wangu na kila kitu ndani yangu/ kikutukuze sasa na milele./ Amina.
(Na Mt Margareta Maria Alakoki)
Ee uliye Mkuu, Mt. Yosefu, uliyatii kabisa maongozi ya Roho Mt. Unijalie neema ya kufahamu aina ya maisha ambayo Mungu anapenda mimi niishi. Usiniache nidanganyike katika jambo muhimu kama hili, ambalo furaha yangu hapa duniani inalitegemea, na hata pia wokovu wa roho yangu.
Unijalie, nikiangazwa na matakwa matakatifu na nikiwa mwaminifu katika kuyatimiza, nikumbatie aina ya maisha ambayo Mungu ameniandalia na yatakayoniongoza kwenye furaha ya milele.
Amina.
Yesu, Mungu wangu mpenzi,/ upo hapa katika Altare mbele yangu;/ na mimi napiga magoti mbele yako.// Waniangalia sana,/ siyo kwa kunipeleleza,/ lakini kwa sababu wapenda kuniona hivi karibu na wewe,/ wafurahiwa nikija kukuabudu./ Wayasikiliza maneno yangu yote/ yenye kutoka mdomoni mwangu,/ na zaidi wapokea maneno yangu yanayotoka moyoni./ Nataka kuzungumza na wewe peke yako,/ na kusahau mambo mengine yote/ na watu wengine walioko kanisani pamoja nami./
Yesu wangu,/ nakushukuru/ kwa sababu umekubali kutupa Sakramenti hii kuu kabisa,/ ukitaka kukaa pamoja na sisi,/ na hata ukakubali kuwa chakula chetu/ chenye nguvu ya ajabu./ Mfalme wangu Yesu,/ Sultani wangu Mkuu,/ naamini kabisa kwamba upo katika Altare/ na kwamba umejificha chini ya umbo la mkate./ Ulipokuwapo bado hapa duniani mbele za watu,/ ulikuwa hujifichi kama sasa;/ lakini hata siku zile/ watu hawakuweza kukuona vile ulivyo./ Hawakuweza kuutambua Umungu wako,/ ikalazimu kukuamini tu sawa kama sisi./ Wakainama kichwa wakisema,/ βBwana wangu na Mungu wanguβ./ Na mimi kadhalika naungama/ U Bwana wangu na Mungu wangu/ na Mkombozi wangu/ na salama yangu yote./ U Yesu wangu tu,/ siwezi kusema zaidi./ Nakuabudu ee Yesu./ Najua sana, mimi ni mdogo kabisa,/ sina maana hata kidogo./ Mimi ni dhaifu na maskini mno./ Lakini Wewe katika hruuma yako kubwa/ waniita nije kwako./ Wewe huuangalii umaskini wangu,/ bali wanivuta katika mapendo yako./
Nasikia maneno yako usemayo:/ βNjooni kwangu ninyi nyote mnaoelemewa na mizigo/ nami nitawasaidiaβ./ Kwa ajili ya maneno hayo/ nakuja kwako bila hofu./ Najua kwamba wanipenda,/ najua wataka kunisaidia na kuniponya,/ najua kuwa wataka kunitakasa./
Nahitaji sana msaada wako, hakika./ Unaniona katika mwendo wangu wa kila siku,/ Jinsi ninavyohangaika na vishawishi mara nyingi;/ jinsi nilivyo na lazima ya kushindana kila siku/ nikitaka kukaa mwema na safi katika utumishi wako./ Naungama mbele yako Wewe Mkombozi wangu,/ kwamba sikukaa imara siku zote vile nilivyopaswa./ Naungama kwamba nimeshindwa mara nyingine/ na kwa hivi naomba toba./ Lakini kwa nini nimeshindwa mara nyingine?/ Kwa nini nikakosa?/ Ni kwa sababu nalikuwa nimekwenda mbali nawe;/ nalianza kujitegemea mwenyewe./ Katika majivuno yangu nikajisifu mwenyewe,/ nikajiona mwema,/ nikasahau udhaifu wangu./ Na kwa ajili hiyo nikajitia katika hatari bure,/ sikujilinda tena,/ nikampa shetani nafasi ya kunishambulia kwa hila zake zote./ Unihurumie ee Yesu wangu./
Sasa nafahamu jinsi nilivyokuwa mjinga kwelikweli./ Ndiyo maana nakuabudu kwa moyo wangu wote./ Najiweka mikononi mwako/ ufanye nami vile unavyotaka./ Wewe utanitunza;/ Wewe utanilinda vema;/ Wewe utaniongoza nijue namna ya kuepa hatari zote,/ na jinsi ya kufukuza kila kishawishi./ Chukua moyo wangu kabisa,/ kwa sababu ni mali yako kamili;/ Wewe ndiwe uliyeniumba,/ ndiwe uliyenipeleka katika Ukristo,/ nawe ndiwe utakayenihukumu siku ya mbele./ Ndivyo ninavyojitolea kwako./ Ndivyo ninavyokuabudu,/ wala sijui njia nyingine ya kukusifu zaidi./
Yesu wangu mpenzi,/ naomba upokee kwa uzuri heshima hiyo yangu./ Angalia: naitolea pamoja na heshima yote/ unayopewa daima na watakatifu wako/ na malaika wako./ Nikipiga magoti hapa mbele yako sasa,/ siko peke yangu,/ nakuabudu pamoja na Mama yako Bikira Maria,/ ambaye sala zake zinakupendeza kabisa./ Sala zangu naweka pamoja na sala zake yeye,/ uzipokee zote pamoja,/ zikupendeze zote sawa./ Ee Mama Maria!/ Nifundishe maneno ya kumsifu Mwanao Yesu vizuri./ Nipeleke kwa Yesu tumwabudu pamoja./ Nifunike na utakatifu wako/ kusudi Yesu asiangalie tena umaskini wangu/ na makosa yangu,/ aniponye katika huruma yake./
Sasa najisikia vizuri, Yesu wangu./ Sasa nina moyo wa kuweza kuendelea vema/ katika njia njema./ Sasa ninatumaini kwamba/ nitakaa mkristo mwema,/ nitakuwa mtumishi wako mwaminifu./ Nasikia amani kubwa sana moyoni mwangu,/ kwa kuwa nimo mikononi mwako./ Baada ya dakika chache/ nitaondoka tena kanisani,/ nitarudi nyumbani kwangu,/ lakini hatutaachana,/ hapana./ Mapendo yetu yatatuunganisha pamoja daima./ Wewe utanikumbuka nikiwa kazini,/ nikilala usingizi,/ nikienda njiani,/ kila mahali nilipo,/ Wewe utaniona,/ utafuatana na mimi./ Kadhalika nitakukumbuka tu./ Nitafanya bidii nisikuache kabisa./ Amina.
Roho ya Kristo unitakase
Mwili wa Kristo uniokoe
Damu ya Kristo unifurahishe
Maji ya ubavu wake Kristo yanioshe
Mateso ya Kristo nguvu yanizidishie
Ee Yesu mwema unisikilize
Katika madonda yako unifiche
Usikubali nitengwe nawe
Na adui mwovu unikinge
Saa ya kufa kwangu uniite
Uniamuru kwako nije
Na watakatifu wako nikutukuze
Milele na milele.
Amina.
Recent Comments