Masomo ya Misa ya Kanisa Katoliki

MASOMO YA MISA, MACHI 21, 2022: JUMATATU , JUMA LA 3 LA KWARESIMA

SOMO 1

2 Fal. 5:1-15

Naamani, jemadari wa jeshi la mfalme wa Shamu, alikuwa mtu mkubwa mbele ya bwana wake, na mwenye kuheshimiwa, kwa sababu kwa mkono wake Bwana alikuwa amewapa Washami kushinda; tena likuwa mtu hodari wa vita; lakini alikuwa mwenye ukoma. Na Washami walikuwa wametoka vikosi vikosi, wakachukua mfungwa mmoja kijana mwanamke kutoka nchi ya Israeli; naye akamhudumia mkewe Naamani. Akamwambia bibi yake, Laiti bwana wangu angekuwa pamoja na yule nabii aliyeko Samaria! Maana angemponya ukoma wake. Mtu mmoja akaingia, akamwambia bwana wake, akasema, Yule kijana mwanamke aliyetoka nchi ya Israeli asema hivi na hivi. Mfalme wa Sahmu akasema, Haya! Basi, mimi nitampelekea mfalame wa Israeli waraka. Basi akaenda zake, akachukua mikononi mwake talanta kumi za fedha, na vipande vya dhahabu elfu sita, na mavazi kumi.

Akampelekea mfalme wa Israeli waraka ule, kusema, Waraka huu utakapokuwasilia, tazama, nimemtuma mtumishi wangu Naamni kwako, ili upate kumponya ukoma wake. Ikawa, mfalme wa Israeli alipousoma waraka, alirarua mavazi yake, akasema, Je! Mimi ni Mungu, niue na kuhuisha, hata mtu huyu akanipelekea mtu nimponye ukoma wake? Fahamuni, basi, nakusihini, mwone ya kuwa mtu huyu anataka kugombana nami.

Ikawa, Elisha, yule mtu wa Mungu, aliposikia kwamba mfalme wa Israeli ameyararua mavazi yake, ndipo akatuma mtu kwa mfalme, akisema, Mbona umeyararua mavazi yako? Na aje sana kwangu mimi, naye atajua ya kuwa yuko nabii katika Israeli.

Basi Naamani akaja na farasi wake na magari yake, akasimama mlangoni pa nyumba ya Elisha. Naye Elisha akampelekea mjumbe, akisema. Enenda ukaoge katika Yordani mara saba, na nyama ya mwili wako itakurudia nawe utakuwa safi. Lakini Naaman akakasirika, akaondoka, akasema, Tazama, nalidhania, Bila shaka atatoka kwangu, na kusimama, na kuomba kwa jina la Bwana, Mungu wake, na kupitisha mkono wake mahali penye ugonjwa, na kuniponya mimi mwenye ukoma Je! Abana na Farpari, mito ya Dameski, si bora kuliko maji yote ya Israeli? Je! Siwezi kujiosha ndani yake, na kuwa safi? Akageuka, akaondoka kwa hasira.

Watumishi wake wakamkaribia, wakamwambia, wakisema, Baba yangu, kama yule nabii angalikuambia kutenda jambo kubwa, usingalilitenda? Je! Si zaidi basi, akikuambia, Jioshe, uwe safi? Ndipo akashuka, akajichovya mara saba katika Yordani sawasawa na neno lake yule mtu wa Mungu; naye nyama ya wmili wak eikarudi ikawa kama nyam aya mwili wa mtoto mchanga, akawa safi.

Akamrudia yule mtu wa Mungu, yeye na mafuatano yake yote. Akaja, akasimama mbele yake; akasema, Sasa tazama, najua ya kwamba hakuna Mungu duniani mwote, ila katika Israeli, basi nakuomba upokee mbaraka kwa mtumwa wako.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.

WIMBO WA KATIKATI

Zab. 42:1-2, 43:3-4 (K) 42:3

(K) Nafsi yangu inamwonea kiu Mungu, Mungu aliye hai, Lini nitakapokuja nionekane mbele za Mungu.

Kama ayala aioneavyo shauku mito ya maji.

Vivyo hivyo nafsi yangu inakuonea shauku, Ee Mungu. (K)

Nafsi yangu inamwonea kiu Mungu, Mungu aliye hai,

Lini nitakapokuja nionekane mbele za Mungu? (K)

Niletewe nuru yako na kweli yako ziniongoze,

Zinifikishe kwenye mlima wako mtakatifu

Na hata maskani yako. (K)

Hivyo nitakwenda madhabahuni kwa Mungu,

Kwa Mungu aliye furaha yangu na shangwe yangu. (K)

SHANGILIO

Yn. 8:12

Mimi ndimi nuru ya ulimwengu, asema Bwana, Yeye anifuataye, atakuwa na nuru ya uzima.

INJILI

Lk. 4:24-30

Yesu alifika Nazareti akawaambia makutano hekaluni: Amin, nawaambia ya kuwa, Hakuna nabii mwenye kukubaliwa katika nchi yake mwenyewe. Lakini, kwa hakika nawaambia, Palikuwa na wajane wengi katika nchi ya Israeli zamani za Eliya, wakati mbingu zilipofungwa miaka mitatu na miezi sita, njaa kuu ikaingia nchi nzima; wala Eliya hakutumwa kwa mmojawapo, ila kwa mjane mmoja wa Sarepta katika nchi ya Sidoni. Tena, palikuwa na weny eukoma wengi katika Israeli zamani za nabii Elisha, wala hapana aliyetakazwa ila Naamani, mtu wa Shamu.

Wakajaa ghadhabu wote waliokuwa katika sinagogi walipoyasikia hayo. Wakaondoka wakamtoa nje ya mji, wakampeleka mpaka ukingo wa kilima ambacho mji wao umejengwa juu yake, wapate kumtupa chini; lakini yeye alipiita katikati yao, akaenda zake.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

MASOMO YA MISA, APRILI 5, 2022: JUMANNE JUMA LA 5 LA KWARESIMA

SOMO 1

Hes. 21:4-9

Wakasafiri kutoka mlima wa Hori kwa njia ya Bahari ya Shamu; ili kuizunguka nchi ya Edomu watu wakafa moyo kwa sababu ya ile njia. Watu wakamnung’unikia Mungu, na Musa, Mbona mmetupandisha huku kutoka nchi ya Misri, ili tufe jangwani? Maana hapana chakula, wala hapana maji, na roho zetu zinakinai chakula hiki dhaifu.

Bwana akatuma nyoka za moto kati ya watu, wakawauma, watu wengi wakafa. Watu wakamwendea Musa, wakasema, Tumefanya dhambi kwa sababu tumemnung’unikia Mungu, na wewe; utuombee kwa Bwana, atuondolee nyoka hawa. Basi, Musa akawaombea watu. Bwana akamwambia Musa, Jifanyie nyoka ya shaba, ukaiweke juu ya mti, na itakuwa kila mtu aliyeumwa, aitazamapo, ataishi. Musa akafanya nyoka ya shaba, akaiweka juu ya mti, hata ikiwa nyoka amemwuma mtu, alipoitazama ile nyoka ya shaba, akaishi.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.

WIMBO WA KATIKATI

Zab. 102:1-2, 15-20 (K) 1

(K) Ee Bwana, usikie kuomba kwangu, kilio changu kikufikie.

Ee Bwana, usikie kuomba kwangu,

Kilio change kikufikie,

Usinifiche uso wako siku ya shida yangu,

Unitegee sikio lako, siku niitapo unijibu upesi. (K)

Kisha mataifa wataliogopa jina la Bwana,

Na wafalme wote wa dunia utukufu wako;

Bwana atakapokuwa ameijenga Sayuni,

Atakapoonekana katika utukufu wake,

Atakapoyaelekea maombi yake aliye mkiwa,

Asiyadharau maombi yao. (K)

Kizazi kitakachokuja kitaandikiwa hayo,

Na watu watakaoumbwa watamsifu Bwana.

Maana ametazama toka patakatifu pake pa juu,

Toka mbinguni Bwana ameiangalia nchi,

Ili akusikie kuugua kwake aliyefungwa,

Na kuwafungua walioandikiwa kufa. (K)

SHANGILIO

Yn. 8:12

 

Mimi ndimi nuru ya ulimwengu, asema Bwana, yeye anifuataye, atakuwa na nuru ya uzima.

INJILI

 

Yn. 8:21-30

 

Yesu aliwaambia Mafarisayo: Mimi naondoka, nanyi mtanitafuta; nanyi mtakufa katika dhambi yenu; mimi niendako ninyi hamwezi kuja.

Basi, Wayahudi wakasema, Je! Atajiua! Kwa kuwa asema, Mimi niendako ninyi hamwezi kuja?

Akawaambia, Ninyi ni wa chini, mimi ni wa juu; ninyi ni wa ulimwengu huu, mimi si wa ulimwengu huu. Kwa hiyo naliwaambieni ya kwamba mtakufa katika dhambi zenu; kwa sababu msiposadiki ya kuwa mimi ndiye, mtakufa katika dhambi zenu.

Basi wakamwambia, U nani wewe? Yesu akawaambia, Hasa neno lilo hilo ninalowaambia. Ninayo mengi ya kusema na kuhukumu juu yenu; lakini yeye aliyenipeleka ni kweli, nami niliyoyasikia kwake ndiyo ninenayo katika ulimwengu.

Wala hawakutambua ya kuwa anawatajia Baba. Basi Yesu akawaambia, Mtakapokuwa mmekwisha kumwinua Mwana wa Adamu, ndipo mtakapofahamu ya kuwa mimi ndiye; na ya kuwa sifanyi neno kwa nafsi yangu, ila kama Baba alivyonifundisha ndivyo ninenavyo. Naye aliyenipeleka yu pamoja nami; hakuniacha peke yangu; kwa sababu nafanya sikuzote yale yampendezayo.

Naye alipokuwa akisema hayo, wengi walimwamwini.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

MASOMO YA MISA, JULAI 24, 2021: JUMAMOSI, JUMA LA 16 LA MWAKA

SOMO 1

Kut. 24:3-8

Musa aliwambia watu maneno yote ya Bwana, na hukumu zake zote; watu wote wakajibu kwa sauti moja, wakasema, Maneno yote aliyoyanena Bwana tutayatenda. Basi Musa akayaandika maneno yote ya Bwana, akaondoka asubuhi na mapema, akajenga madhabahu chini ya mlima, na nguzo kumi na mbili, kwa hesabu ya kabila kumi na mbili za Israeli, akapeleka vijana wa wana wa Israeli, waliotoa sadaka za kuteketezwa, wakamchinjia Bwana sadaka za amani za ng’ombe. Musa akatwaa nusu ya ile damu, akaitia katika mabakuli; na nusu ya ile damu akainyunyiza juu ya madhabahu. Kisha akakitwaa kitabu cha agano akakisoma masikioni mwa watu; wakasema, Hayo yote aliyoyanena Bwana tutayatenda, nasi tutatii. Musa akaitwaa ile damu, akawanyunyizia watu, akasema, Hii ndiyo damu ya agano alilolifanya Bwana pamoja nanyi katika maneno haya yote.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.

WIMBO WA KATIKATI

Zab. 50:1-2, 5-6, 14-15 (K) 14 (K)

Mtolee Mungu dhabihu za kushukuru. Mungu, Mungu Bwana, amenena, ameiita nchi, Toka maawio ya jua hata machweo yake. Tokea Sayuni,, ukamilifu wa uzuri, Mungu amemulika. (K)

Nikusanyieni wacha Mungu wangu, Waliofanya agano nami kwa dhabihu. Na mbingu zitatangaza haki yake, Kwa maana Mungu ndiye aliye hakimu. (K)

Mtolee Mungu dhabihu za kushukuru; Mtimizie Aliye juu nadhiri zako. Ukaniite siku ya mateso; Nitakuokoa, na wewe utanitukuza. (K)

SHANGILIO

Zab. 8:15

Aleluya, aleluya,

Wanabarikiwa wale ambao kwa unyofu na wema wa mioyo yao, hulisikia neno la Mungu na kulishika.

Aleluya.

INJILI

Mt. 13:24 – 30

Yesu aliwatolea makutano mfano akisema, Ufalme wa mbinguni umefanana na mtu aliyepanda mbegu njema katika konde lake; lakini watu walipolala akaja adui yake akapanda magugu katikati ya agano, akaenda zake. Baadaye majani ya ngano yalipomea na kuzaa, yakaonekana na magugu. Watumwa wa mwenye nyumba wakaenda wakamwambia, Bwana, hukupanda mbegu njema katika konde lako? Limepata wapi basi magugu? Akawaambia, Adui ndiye aliyetenda hivi. Watumwa wakamwambia, Basi, wataka twende tukayakusanye? Akasema, La; msije mkakusanya magugu, na kuzing’oa ngano pamoja nayo. Viacheni vyote vikue hata wakati wa mavuno; na wakati wa mavuno nitawaambia wavunao, Yakusanyeni kwanza magugu, myafunge matita matita mkayachome; bali ngano ikusanyeni ghalani mwangu.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

MASOMO YA MISA, MACHI 30, 2022, JUMATANO: JUMA LA 4 LA KWARESIMA

SOMO 1

 

Isa. 49:8-15
Bwana asema hivi, Wakati uliokubalika nimekujibu, na siku ya wokovu nimekusaidia; nami nitakuhifadhi, nitakutoa uwe agano la watu hawa, ili kuiinua nchi hii, na kuwarithisha urithi uliokuwa ukiwa; kuwaambia waliofungwa, Haya, tokeni; na hao walio katika giza, Jionyesheni.
Watajilisha katika njia, na juu ya majabali watapata malisho. Hawataona njaa, wala hawataona kiu; hari haitawapiga, wala jua; kwa maana yeye aliyewarehemu atawatangulia, naam, karibu na chemchemi za maji atawaongoza. Nami nitafanya milima yangu yote kuwa njia, na njia kuu zangu zitatukuzwa zote.
Tazama, hawa watakuja kutoka mbali; na tazama, hawa kutoka kaskazini, na kutoka magharibi, na hawa kutoka nchi ya sinimu. Imbeni, enyi mbingu; ufurahi, Ee nchi; pazeni sauti ya kuimba, enyi milima; kwa kuwa Bwana amewafariji watu wake, naye atawahurumia watu wake walioteswa.
Bali Sayuni alisema, Yehova ameniacha, Bwana amenisahau. Je! Mwanamke aweza kumsahau mtoto wake anyonyaye, hata asimhurumie mwana wa tumbo lake? Naam, hawa waweza kusahau, lakini mimi sitakusahau wewe.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.

WIMBO WA KATIKATI

 

Zab. 145:8-9, 13-14, 17-18 (K)

(K) Bwana ana fadhili, ni mwingi wa huruma.

Bwana ana fadhili, ni mwingi wa huruma,
Si mwepesi wa hasira, ni mwingi wa rehema.
Bwana ni mwema kwa watu wote,

Na rehema zake zi juu ya kazi zake zote. (K)
Ufalme wako ni ufalme wa zamani zote,
Ni mamlaka yako ni ya vizazi vyote.
Bwana huwategemeza wote waangukao,
Huwainua wote walioinama chini. (K)

Bwana ni mwenye haki katika njia zake zote,
Na mwenye fadhili juu ya kazi zake zote.
Bwana yu karibu na wote wamwitao,
Wote wamwitao kwa uaminifu. (K)

SHANGILIO

Mt. 4:4

Mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu.

INJILI

Yn. 5:17-30
Yesu aliwajibu Wayahudi: Baba yangu anatenda kazi hata sasa, nami ninatenda kazi. Basi kwa sababu hiyo Wayahudi walizidi kutaka kumwua, kwa kuwa hakuivunja sabato tu, bali pamoja na hayo alimwita Mungu Baba yake, akijifanya sawa na Mungu.
Basi Yesu akajibu, akawaambia, Amin, amin, nawaambia, Mwana hawezi kutenda neno mwenyewe ila lile ambalo amwona Baba analitenda; kwa maana yote ayatendayo yeye, ndiyo ayatendayo Mwana vile vile. Kwa kuwa Baba ampenda Mwana, naye humwonyesha yote ayatendayo mwenyewe; hata na kazi kubwa zaidi kuliko hizi atamwonyesha ili ninyi mpate kustaajabu. Maana kama Baba awafufuavyo wafu na kuwahuisha, vivyo hivyo na Mwana ahuisha wale awatakao. Tena Baba hamhukumu mtu yeyote, bali amempa Mwana hukumu yote, ili watu wote wamheshimu Mwana kama vile wanavyomheshimu Baba. Asiyemheshimu Mwana hamheshimu Baba aliyempeleka.
Amin, amin, nawaambia, yeye alisikiaye neno langu na kumwamini yeye aliyenipeleka yuna uzima wa milele; wala haingii hukumuni, bali amepita kutoka mautini kuingia uzimani. Amin, amin, nawaambia, Saa inakuja, na sasa ipo, wafu watakapoisikia sauti ya Mwana wa Mungu, na wale waisikiao watakuwa hai.
Maana kam avile Baba alivyo na uzima nafsini mwake, vivyo hivyo alimpa na Mwana kuwa na uzima nafsini mwake. Naye akampa amri ya kufanya hukumu kwa sababu ni Mwana wa Adamu. Msistaajabie maneno hayo; kwa maana sasa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake. Nao watatoka; wale waliofanya mema kwa ufufuo wa uzima, na wale waliotenda mabaya kwa ufufuo wa hukumu. Mimi siwezi kufanya neno mwenyewe; kama nisikiavyo ndivyo nihukumuvyo na hukumu yangu ni ya haki, kwa sababu siyatafuti mapenzi yangu mimi, bali mapenzi yake aliyenipeleka.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

MASOMO YA MISA, MACHI 19, 2022: JUMAMOSI, JUMA LA 3 LA KWARESIMA

SHEREHE YA MT. YOSEFU, MUME WA BIKIRA MARIA

SOMO 1

2Sam. 7: 4 – 5, 12 – 14, 16

Ikawa usiku uo huo, neno la Bwana likamfikia Nathani kusema, Enenda ukamwambie mtumishi wangu Daudi, Bwana asema hivi, siku zako zitakapo timia, ukalala na Baba zako, nitainua mzao wako nyuma yako, atakayetoka viunoni mwako, nami nitaufanya imara ufalme wake.

Yeye ndiye atakayejenga nyumba kwa jina langu, nacho kiti cha enzi cha ufalme wake nitakifanya imara milele. Mimi nitakuwa baba yake, naye atakuwa mwanangu, akitenda maovu nitamwadhibu kwa fimbo yako, na ufalme wako, vitathibitishwa milele mbele yako. Nacho kiti chako kitafanywa imara milele.

WIMBO WA KATIKATI

Zab. 89:1 – 4, 26, 28 (K) 36(K)

Wazao wake watadumu milele.

Fadhili za Bwana nitaziimba milele;Kwa kinywa changu nitavijulisha vizazi vyote uaminifu wako.

Maana nimesema, Fadhili zitajengwa milele;Katika mbingu utauthibitisha uaminifu wako. (K)

Nimefanya agano na mteule wangu,Nimemwapia Daudi, mtumishi wangu.Wazao wako nitawafanya imara milele,Nitakijenga kiti chako cha enzi hata milele. (K)

Yeye ataniita, Wewe baba yangu,Mungu wangu na mwamba wa wokovu wangu.

Hata milele nitamwekea fadhili zangu,Na agano langu litafanyika amini kwake. (K)

SOMO 2

Rum. 4:13, 16 – 18, 22

Ahadi ile ya kwamba atakuwa mrithi wa ulimwengu alipewa Ibrahimu na uzao wake, si kwa sheria bali kwa haki aliyohesabiwa kwa Imani. Kwa hiyo ilitoka katika Imani, iwe njia ya neema, ili kwamba ile ahadi iwe imara kwa wazao wote; si kwa wale wa torati tu, ila kwa wale wa Imani ya Ibrahimu; aliye baba yetu sisi sote; (kama ilivyoandikwa, Nimekuweka kuwa baba wa mataifa mengi); mbele zake yeye aliyemwamini, yaani Mungu, mwenye kuwahuisha wafu, ayatajaye yale yasiyokuwako kana kwamba yamekuwako.Naye aliamini kwa kutarajia yasiyoweza kutarajiwa, ilia pate kuwa baba wa mataifa mengi, kama ilivyonenwa, Ndivyo utakavyokuwa uzao wako. Kwa hiyo ilihesabiwa kwake kuwa ni haki.Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.

SHANGILIO

Zab. 84:5

Heri wakaao nyumbani mwako, Ee Bwana.

INJILI

Mt. 1:16, 18 – 21, 24

Yakobo alimzaa Yusufu mumewe Mariamu aliyemzaa yesu aitwaye Kristo.Kuzaliwa kwake Yesu Kristo kulikuwa hivi. Mariamu mama yake alipokuwa ameposwa na Yusufu, kabla hawajakaribiana, alionekana ana mimba kwa uweza wa Roho Mtakatifu. Naye Yusufu, mumewe, kwa vile alivyokuwa mtu wa haki, asitake kumwaibisha, aliazimu kumwacha malaika wa Bwana alimtokea katika ndoto, akimchukua Mariamu mkeo, maana mimba yake ni kwa uweza wa Roho Mtakatifu. Naye atazaa mwana, nawe utamwita jina lake Yesu, maana, yeye ndiye atakayewaokoa watu wake na dhambi zao.Naye Yusufu alipoamka katika usingizi, alifanya kama malaika wa Bwana alivyomwagiza; akamchukua mkewe.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

MASOMO YA MISA, JUMAPILI, AGOSTI 20, 2023: JUMA LA 20 LA MWAKA 

SOMO I

Isa. 56:1, 6-7

Bwana asema hivi, Shikeni hukumu, mkatenda haki; kwa maana wokovu wangu u karibu kuja, na haki yangu kufunuliwa. Na wageni, walioandamana na Bwana ili wamhudumu, na kulipenda jina la Bwana, kuwa watumishi wake; kila aishikaye sabato asiivunje, na kulishika sana agano langu; Nitawaleta hao nao hata mlima wangu mtakatifu, na kuwafurahisha katika nyumba yangu ya sala; makafara yao na dhabihu zao zitakubaliwa juu ya madhabahu zangu; kwa maana nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala kwa mataifa yote.

Neno la Bwana…Tumshukuru Mungu

WIMBO WA KATIKATI 

Zab. 67:1-2, 4-5, 7 (K) 5

(K) Watu na wakushukuru, Ee Mungu, 
Watu wote na wakushukuru.

Mungu na atufadhili na kutubariki,

na kutuangazia uso wake.
Njia yake ijulikane duniani,
wokovu wake katikati ya mataifa yote. (K)

mataifa na washangilia,

naam, waimbe kwa furaha.
Maana kwa haki utawahukumu watu,
na kuwaongoza mataifa walioko duniani. (K)

watu na wakushukuru, Ee Mungu,

watu wote na wakushukuru.
Mungu atatubariki sisi;
miisho yote ya dunia itamcha Yeye. (K)

SOMO 2

Rum. 11:13-15, 29-32

Nasema na ninyi, mlio watu wa Mataifa. Basi, kwa kadiri nilivyo mtume wa watu wa Mataifa. Basi, naitukuza huduma iliyo yangu? Huenda nikapata kuwapatia wivu walio damu moja na mimi na kuwaokoa baadhi yao. Maana ikiwa kutupwa kwao kumeleta upatanisho kwa ulimwengu, je! Kukubaliwa kwao kutakuwa nini kama si uhai baada ya kufa. Kwa sababu karama za Mungu hazina majuto, wala mwito wake. Kwa maana kama ninyi zamani mlivyomwasi Mungu, lakini sasa mmepata rehema kwa kuasi kwao; kadhalika na hao wameasi sasa, ili kwa kupata rehema kwenu wao nao wapate rehema. Maana Mungu amewafunga wote pamoja katika kuasi ili awarehemu wote.

Neno la Bwana…Tumshukuru Mungu

SHANGILIO

Mdo. 16:14


Aleluya, aleluya,

Fungua mioyo yetu, Ee Bwana, 
Ili tuyatuze maneno ya Mwanao.
Aleluya

INJILI 

Mt. 15:21-28

Yesu aliondoka huko, akaenda kando pande za tiro na Sidoni. Na tazama, mwanamke Mkananayo wa mipaka ile akatokea, akampazia sauti akisema, Unirehemu, Bwana, mwana wa Daudi; binti yangu amepagawa sana na pepo. Wala yeye hakumjibu neno. Nao wanafunzi wake wakamwendea, wakamwomba, wakisema, Mwache aende zake; kwa maana anapiga kelele nyuma yetu. Akajibu, akasema, Sikutumwa ila kwa kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli. Naye akaja akamsujudia, akisema, Bwana unisaidie. Akajibu, akasema, Si vema kukitwaa chakula cha watoto na kuwatupia mbwa. Akasema, Ndiyo, Bwana, lakini hata mbwa hula makombo yaangukayo mezani pa bwana zao. Ndipo Yesu akajibu, akamwambia, Mama, imani yako ni kubwa; na iwe kwako kama utakavyo. Akapona binti yake tangu saa ile.

Neno la Bwana…Sifa kwako, ee Kristo

MASOMO YA MISA, JUNI 25, 2023: JUMAPILI YA 12 YA MWAKA

SOMO 1

Yer. 20 : 10-13

Nimesikia mashutumu ya watu wengi; hofu ziko pande zote. Rafiki zangu wote wanaonivizia nisite, husema, Mshitaki, nasi tutamshitaki; huenda akahahadaika; nasi tutamshinda, tutajilipiza kisasi kwake. Lakini Bwana yu pamoja nami, mfano wa shujaa mwenye kutisha; kwa hiyo hao wanaonionea watajikwaa, wala hawatashinda; watatahayarika sana. Kwa sababu hawakutenda kwa akili, wataona aibu ya milele, ambayo haitasahauliwa kamwe. Lakini Ee Bwana wa majeshi, wewe wawajaribu wenye haki, waona viuno na mioyo. nijalie kuona kisasi chako juu yao; kwa maana nimekufunulia wewe neno langu.

Mwimbieni Bwana; msifuni Bwana; 
Kwa maana ameiponya roho ya mhitaji 
Katika mikono ya watu watendao maovu.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.

WIMBO WA KATIKATI

Zab. 69 : 7-9, 13,16, 32-34 (K) 13

(K) Kwa wingi wa fadhili zako unijibu.

Kwa ajili yako nimestahimili laumu,
Fedheha imenifunika uso wangu.
Nimekuwa mgeni kwa ndugu zangu,
Na msikwao kwa wana wa mama yangu.
Maana wivu wa nyumba yako umenila,
Na laumu yao wanaokulaumu zimenipata. (K)

Nami maombi yangu nakuomba Wewe, Bwana, 
Wakati ukupendezao; Ee Mungu,
Kwa wingi wa fadhili zako unijibu,
Katika kweli ya wokovu wako.
Ee Bwana, unijibu, maana fadhili zako ni njema,
Kwa kadiri ya rehema zako unielekee. (K)

Walioonewa watakapoona watafurahi;
Enyi mmtafutao Mungu, mioyo yetu ihuishwe.
Kwa kuwa Bwana huwasikia wahitaji,
Wala hawadharau wafunga wake.
Mbingu na nchi zimsifu
Bahari na vyote viendavyo ndani yake. (K)

SOMO 2

Rum. 5:12-15

Kama kwa mtu mmoja dhambi iliingia uli mwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi; maana kabla ya sheria dhambi ilikuwamo ulimwenguni, lakini dhambi haihesabiwi isipokuwapo sheria; walakini mauti ilitawala tangu Adamu mpaka Musa, nayo iliwatawala hata wao wasiofanya dhambi ifananayo na kosa la Adamu, alive mfano wake yeye atakayekuja. Lakini karama ile haikuwa kama lile kosa; kwa maana ikiwa kwa kukosa kwake yule mmoja wengi walikufa, zaidi sana neema ya Mungu, na kipawa kilicho katika neema yake mwanadamu mmoja Yesu Kristo kimezidi kwa ajili ya wale wengi.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.

SHANG1LIO

Mdo. 16:14

Aleluya, aleluya,
Fungua mioyo yetu, ee Bwana, 
Ili tuyatunze maneno ya Mwanao.
Aleluya.

INJILI

Mt. 10:26-33

Yesu aliwaambia mitume wake: Msiwaogope, kwa maana hakuna neno lililositirika, ambalo halitafunuliwa; wala lililofichwa, ambalo halitajulikana. Niwaambialo ninyi katika giza, lisemeni katika nuru; na msikialo kwa siri, lihubirini juu ya nyumba. Msiwaogope wauuao mwili, wasiweze kuiua na roho; afadhali mwogopeni yule awezaye kuangamiza mwili na roho pia katika jehanum, Je! mashomoro wawili hawauzwi kwa senti moja? Wala hata mmoja haanguki chini asipojua Baba yenu; lakini ninyi, hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote. Msiogope basi; bora nyinyi kuliko mashomoro wengi. Basi, kila mtu atakayenikiri mbele ya watu, nami nitamkiri mbele za Baba yangu aliye mbinguni. Bali mtu ye yote atakayenikana mbele ya watu, nami nitamkana mbele za Baba yangu aliye mbinguni.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

MASOMO YA MISA, JUMAPILI, JULAI 2, 2023: DOMINIKA LA 13 LA MWAKA

MWANZO

Zab. 47:2

Enyi watu wote, pigeni makofi, mpigieni Mungu kelele kwa sauti ya shangwe.

SOMO 1 

2 Fal 4:8-11,14-16

Ilikuwa siku moja, Elisha alikwenda Shunemu; na huko kulikuwa na mwanamke mmoja mwenye cheo; nave akamshurutisha aje ale chakula. Ikawa kila alipopita njia ile, huingia kula chakula.

Yule mwanamke akamwambia mumewe, Tazama, mimi naona ya kuwa mtu huyu apitaye kwetu mara kwa mara ni mtu mtakatifu w’a Mungu. Nakuomba, tumfanyie chumba kidogo ukutani; na ndani yake tumwekee kitanda, na meza, na kiti, na kinara cha taa na itakuwa, atujiapo, ataingia humo.

Ikawa siku moja akafikia huko, akaingia katika chumba kile akalala. Akasema, Basi, atendewe nini? Gehazi akajibu, Hakika hana mwana, na mumewe ni mzee. Akamwambia, Kamwite. Naye alipokwisha kuitwa, akasimama mlangoni. Akasema, Panapo wakati huu mwakani, utamkumbatia mwana.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.

WIMBO WA KATIKATI 

Zab. 89 : 1-2, 15-18 (K) 1(K)

Fadhili za Bwana nitaziimba milele. Fadhili za Bwana nitaziimba milele; Kwa kinywa changu nitavijulisha vizazi vyote uaminifu wako. Maana nimesema, Fadhili zitajengwa milele;Katika mbingu utauthibitisha uaminifu wako. (K)

Heri watu wale waijuao sauti ya shangwe, Ee Bwana, kuenenda katika nuru ya uso wako. Kwa jina lako hufurahi mchana kutwa,Na kwa haki yako hutukuzwa. (K)

Maana fahari ya nguvu zao ni Wewe, Na kwa radhi yako pern be yetu itatukuka.

Maana ngao yetu ina Bwana,Na mfalme wetu ni wake Mtakatifu wa Israeli. (K)

SOMO 2 

Rum. 6:3-4,8-11

Hamfahamu ya kuwa sisi sote tuliobatizwa katika Kristo Yesu tulibatizwa katika mauti yake? Basi tulizikwa pamoja naye kwa njia ya ubatizo katika mauti yake, kusudi kama Kristo alivyofufuka katikawafu kwa njia ya utukufu wa Baba, vivyo hivyo na sisi tuenende katika upya wa uzima.

Lakini tukiwa tulikufa pamoja na Kristo, twaamini ya kuwa tutaishi pamoja naye; tukijua ya kuwa Kristo akiisha kufufuka katika wafu hafi tena, wala mauti haimtawali tena. Maana kwa kule kufa kwake, aliifia dhambi mara moja tu; lakini kwa kule kuishi kwake, amwishia Mungu. Vivyo hivyo ninyi nanyi jihesabuni kuwa wafu kwa dhambi, na walio hai kwa Mungu katika Kristo Yesu.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.

SHANGILIO 

Mt. 11:25

Aleluya, aleluya, 
Nakushukuru, Baba, kwa kuwa mambo haya uliwaficha wenye hekima na akili, ukawafunulia watoto wachanga. 
Aleluya.


INJILI 

Mt. 10:37-42


Yesu aliwafundisha mitume wake hivi: Apendaye baba au mama kuliko mimi, hanistahili; wala apendaye mwana au binti kuliko mimi, hanistahili. Wala mtu asiyechukua msalaba wake akanifuata, hanistahili. Mwenye kuiona nafsi yake ataipoteza; naye mwenye kuipoteza nafsi yake kwa ajili yangu ataiona.

Awapokeaye ninyi, anipokea mimi; naye anipokeaye mimi, ampokea yeye aliyenituma. Ampokeave nabii kwa kuwa ni nabii, atapata thawabu ya nabii; naye ampokeaye mwenye haki kwa kuwa ni mwenye haki, atapata thawabu ya mwenye haki.

Na mtu awaye yote atakayemnywesha mmojawapo wa wadogo hawa ngaa kikombe cha maji ya baridi, kwa kuwa ni mwanafunzi, amin, nawaambia. haitampotea kamwe thawabu yake.

Neno la Bwana……..Sifa kwako Ee Kristo

MASOMO YA MISA, MACHI 29, 2022: JUMANNE: JUMA LA 4 LA KWARESIMA

SOMO 1

Eze. 47:1-9, 12

Malaika alinileta mpaka lango la nyumba; na tazama, maji yalitoka chini ya kizingiti cha nyumba, kwa njia ya mashariki, maana upande wa mbele wa nyumba ulielekea upande wa mashariki; nayo maji yakashuka toka chini ya upande wa kuume wa nyumba, upande wa kusini wa madhabahu. Ndipo akanileta nje kwa njia ya lango upande wa kaskazini, akanizungusha kwa njia ya nje mpaka lango la nje, kwa njia yake iliyoelekea mashariki; na tazama, maji yalitoka upande wa kuume. Na alipotoka mtu yule, mwenye uzi wa kupimia mkononi mwake, kwenda masharikini, akapima dhiraa elfu, akanivusha maji yale; maji yakafika mpka viweko vya miguu.

Kisha akapima dhiraa elfu, akanivusha maji yale, maji yakafika mpaka magoti. Kisha akapima dhiraa elfu, akanivusha, maji yakafika mpaka viuno. Kisha akapima dhiraa elfu, yakawa mto nisioweza kuuvuka; maana maji yamezidi, maji ya kuogelea, mto usiovukika. Akaniambia, Mwanadamu, je! Umeona haya? Kisha akanichukua, akanirudisha mpaka ukingo wa mto.

Basi nikiisha kurudi, tazama, kando ya ukingo wa mto ilikuwapo miti mingi sana, upande huu na upande huu. Ndipo akaniambia, Maji haya yanatoka kwenda pande za nchi ya mashariki, nayo yanashuka mpaka Araba, na kuingia katika bahari; maji yatokezwayo yataingia baharini, na maji yake yataponyeka. Tena itakuwa, kila kiumbe hai kisonganamacho, kila mahali itakapofika mito hiyo, kitaishi; kutakuwapo wingi mkubwa wa samaki, kwa sababu maji haya yamefika huko; maana maji yale yataponyeka, na kila kitu kitaishi popote utakapofikilia mto huo.

Na karibu na mto, juu ya ukingo wake, upande huu na upande huu, utamea kila mti wa chakula, ambao majani yake hayatanyauka, wala matunda yake hayatatindika kamwe; utatoa matunda mapya kila mwezi, kwa sababu maji yake yanatoka mahali patakatifu; na matunda yake yatakuwa ni chakula; na majani yake yatakuwa ni dawa.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.

WIMBO WA KATIKATI

Zab. 46:1-2, 4-5, 7-8 (K) 7

(K) Bwana wa majeshi yu pamoja nasi, Mungu wa Yakobo ni ngome yetu.

Mungu kwetu sisi ni kimbilio na nguvu,

Msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso.

Kwa hiyo hatutaogopa ijapobadilika nchi,

Ijapotetemeka milima moyoni mwa bahari. (K)

Kuna mto, vijito vyake vyaufurahisha mji wa Mungu,

Patakatifu pa maskani zake Aliye juu.

Mungu yu katikati yake hautatetemeshwa;

Mungu atausaidia asubuhi na mapema. (K)

Bwana wa majeshi yu pamoja nasi,

Mungu wa Yakobo ni ngome yetu.

Njoni myatazame matendo ya Bwana,

Jinsi alivyofanya ukiwa katika nchi. (K)

SHANGILIO

Amo. 5:14

Tafuteni mema, wala si mabaya, mpate kuishi, hivyo Bwana, atakuwa pamoja nanyi.

INJILI

Yn. 5:1-3, 5-16

Baada ya hayo palikuwa na sikukuu ya Wayahudi; naye Yesu akakwea kwenda Yerusalemu. Na huko Yerusalemu penye mlango wa kondoo pana birika, iitwayo kwa Kiebrania Betzatha, nayo ina matao matano. Ndani ya hayo jamii kubwa ya wagonjwa walikuwa wamelala, vipofu, viwete, nao waliopooza.

Na hapa palikuwa na mtu, ambaye amekuwa hawezi muda wa miaka thelathini na minane. Yesu alipomwona huyu amelala, naye akijua ya kuwa amekuwa hali hiyo siku nyingi, alimwambia, Wataka kuwa mzima? Yule mgonjwa akamjibu, Bwana, mimi sina mtu wa kunitia birikani, maji yanapotibuliwa; ila wakati ninapokuja mimi, mtu mwingine hushuka mbele yangu. Yesu akamwambia, Simama, jitwike godoro lako, uende. Mara yule mtu akawa mzima, akajitwika godoro lake, akaenda.

Nayo ilikuwa ni sabato siku hiyo. Kwa sababu hiyo Wayahudi wakamwambia yule aliyeponywa, Leo ni sabato, wala si halali kwako kujitwika godoro. Akawajibu, Yeye aliyenifanya kuwa mzima ndiye aliyeniambia, Jitwike godoro lako, uende. Basi wakamwuliza, Yule aliyekuambia, Jitwike uende, ni nani? Lakini yule mtu aliyeponywa hakumjua ni nani; maan aYesu alikuwa amejitenga, kwa sababu palikuwa na watu wengi mahali pale.

Baada ya hayo Yesu akamkuta ndani ya hekalu, akamwambia, Angalia, umekuwa mzima; usitende dhambi tena, lisije likakupata jambo lililo baya zaidi. Yule akaenda zake, akawapasha habari Wayahudi ya kwamba ni Yesu aliyemfanya kuwa mzima. Kwa sababu hiyo Wayahudi wakamwudhi Yesu, kwa kuwa alitenda hayo siku ya sabato.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

MASOMO YA MISA, APRILI 4, 2022: JUMATATU, JUMA LA 5 LA KWARESIMA

SOMO 1

 

Dan.13:41-62

 

Palikuwa na mtu mmoja jina lake Yoakimu, akikaa Babeli, naye ameoa mke jina lake Susana binti Helkia, mwanamke mzuri sana na mcha Mungu. Wazee wake nao walikuwa wenye haki, pia wamemfundisha binti yao sawasawa na Torati ya Musa. Basi Yoakimu alikuwa mwungwana tajiri, na karibu na nyumba yake alikuwa na bustani nzuri; hivyo Wayahudi humwendea, maana alikuwa ni mwenye heshima kupita wengineo wote. Mwaka ule ule wakaamriwa wawili miongoni mwa wazee wa watu ili kuamua, watu wa namna ile ambao Bwana aliwanena, ya kama ufisadi ulitoka Babeli kwa wazee waamuzi waliohesabiwa kuwa wanatawala watu. Hao walikuwa wakienda mara nyingi kuzuru kwenye nyumba yake Yoakimu; na wote wenye mashtaka yoyote desturi yao wakawajia huko. Basi watu walipoondoka kwenda zao panapo saa sita, Susana huingia katika bustani ya mumewe ili kutembea. Nao wale wazee humwona kila siku anakwenda kutembea; hata wakawaka tamaa kwa sababu yake. Ndipo walipozipotosha nia zao, wakayageuza upande macho yao wasiweze kutazama mbinguni wala kukumbuka hukumu za haki. Ikawa walipongoja wakati wa kufaa, yeye aliingia bustanini kama ilivyokuwa desturi yake pamoja na wajakazi wawili, naye alitaka kuoga kwa sababu kulikuwa na joto. Wala hapakuwa na mtu yeyote isipokuwa wale wazee wawili, ambao wamejificha wakimvizia. Basi akawaambia wajakazi wake, Nileteeni mafuta na sabuni, mkaifunge milango ya bustani ili nioge . Mara wale wajakazi walipokwishas kutoka, wale wazee wawili waliondoka wakamwendea mbio, wakasema, Tazama, milango ya bustani imefungwa asiweze kutuona mtu yeyote nasi tunakupenda sana; haya! Basi, utukubali na ulale nasi. La! Hutaki tutakushuhudia ya kuwa hapa palikuwapo na kijana pamoja nawe, ndiyo sababu uliwaruhusu wajakazi wako. Basi Susana aliugua akasema, Nimesongwa pande zote, maana nikilitenda hilo ni mauti yangu; nisipolitenda siwezi kuokoka mikononi mwenu. Ni afadhali niangukie katika mikono yenu na kukataa, kuliko kutenda dhambi machoni pa Mungu. Mara Susana akapiga kelele kwa sauti kuu; nao wale wazee wawili wakampigia kelele pia. Kisha mmoja wao akakimbia, akaifungua milango ya bustani. Hivyo watumishi wa nyumbani waliposikia kelele bustanini, wao waliingia kwa kasi kwa mlango wa nyuma ili waone ni nini iliyompata. Lakini wale wazee waliisimulia hadith yao nao watumishi wakaona aibu kabisa, kwa maana Susana hakuchongelewa habari ya namna hiyo wakati wowote.

Ikawa kesho yake watu walipokusanyika kwa Yoakimu mumewe, wale wazee wawili wakaja nao, wamejaa kusudi lao ovu juu ya Susana la kumfisha. Wakasema mbele ya watu, “Mwiteni Susana binti Helkia, mkewe Yoakim, aje hapa”. Basi akaenda kuitwa; naye akaja pamoja na baba yake na mama yake, na watoto wake, na jamaa zake wote. Naye huyo Susana alikuwa mwanamke mwenye adabu, mzuri wa uso; basi hao watu wabaya waliamuru afunuliwe uso, maana alifunikwa utaji, ili washibe uzuri wake. Kwa hiyo rafiki zake na wote waliomtazama wakasikitika. Ndipo wale wazee wawili waliposimama katikati ya watu, wakaweka mikono yao juu ya kichwa chake. Naye akatoka machozi, akatazama juu mbinguni, kwa maana moyo wake ulimtumaini Mungu. Wale wazee wakasema, Sisi tulipokuwa tukitembea bustanini peke yetu, huyu aliingia pamoja na wajakazi wawili, wakaifunga milango ya bustani, naye mara akawaruhusu wajakazi. Kisha kukatokea kijana, ambaye amejificha humo, akamwendea akalala naye. Walakini sisi tungaliko pembeni mwa bustani, tuliona ubaya huo, tukamwendea mbio. Hata tukiwa tumewaona pamoja, yule kijana hatukuweza kumkamata, maana alikuwa mwenye nguvu kuliko sisi, akifungua milango akaepuka. Bali huyu tulimkamata, tukauliza yule kijana yu nani, asikubali kutuambia. Hayo basi, tunashuhudu. Basi waliohudhuria wakawasadiki, wakiwa wazee wa watu na waamuzi; hivyo wakahukumu auawe. Mara Susana akalia kwa sauti kuu, akasema, Ee Mungu wa milele, Wewe wajua yaliyositirika, wajua mambo yote yasijekuwako, Wewe wajua ya kwamba wananishuhudia uongo, na tazama, imenipasa kufa; walakini sikufanya mambo kama hayo, ambayo watu hawa wameyabuni juu yangu kwa ukorofi.

Naye Bwana akaisikia sauti yake. Kwa hiyo, alipochukuliwa huyo kwenda kuuawa, Mungu alimchocheleza roho kijana mmoja, jina lake Danieli; naye akapaza sauti akasema, Mimi simo; mimi sina hatia kwa habari ya damu yake mwanamke huyu. Mara wote wakamgeukia, wakasema, Maneno hayo uyasemayo, maana yake nini? Akasimama katikati, akasema, Enyi bani Israeli, mmekuwa wapumbavu, hata kumhukumu binti Israeli bila kuhoji wala kupata hakika ya kweli? Rudini hukumuni; mradi hao wanamshuhudia uongo.

Basi watu wote walirejea kwa haraka, nao wale wazee wakamwambia, Njoo uketi kati yetu, utujulishe habari hiyo, endapo Mungu amekupa wewe heshima yam zee. Hapo Danieli aliwaambia, Watu hawa wawili watengwe, nami nitawahoji. Basi wakiisha kutengwa, akamwita mmoja wao akamwambia, Ewe uliyepata kuwa mzee katika uovu, sasa dhambi zako zimekukalia, ulizozitenda zamani kwa kuhukumu isivyo haki, kumpatiliza asiye na hatia na kumwachilia mwovu; lakini Bwana asema, Asiye na hatia, mwenye haki, usimwue. Haya! Basi, wewe ulimwona kwa macho; useme; Chini ya mti gani ulipowaona wakikaa pamoja? Naye akajibu, Chini ya msandarusi. Danieli akasema, Hakika umesema uongo juu ya kichwa chako mwenyewe; maana sas hivi malaika wa Mungu amepokea hukumu ya Mungu, akukate vipande viwili. akamtenga huyo tena, akaamuru kumleta yule mwingine, akamwambia, Ewe mzao wa Kanaani, wala si wa Yuda, uzuri umekudanganya, na tamaa imeupotosha moyo wako. Hivyo ndivyo ulivyowafanyia binti za Israeli, na kwa hofu walitembea nawe; bali huyu binti Yuda hakuweza kuustahimili uovu wako. Haya! Basi, nawe useme; Chini ya mti gani ulipowaona wakikaa pamoja? Naye akajibu, Chini ya mkwaju. Danieli akamwambia, Hakika wewe nawe umesema uongo juu ya kichwa chako mwenyewe; maana malaika wa Mungu yu tayari, anakungoja mwenye upanga, akukate vipande viwili; ili awaangamize nyote wawili.

Mara hiyo makusanyiko yote wakapaza sauti kwa nguvu, wakamhimidi Mungu awaokoaye wamtumainio. Wakawaondokea wale wazee wawili, kwa maana Danieli ameuhakikisha ushuhuda wao wa uongo hata vinywani mwao wenyewe. Wakawatenda kwa Torati ya Musa kama vile walivyokusudia kwa ukorofi kumfanyia jirani yao; wakawaua; na mwenye damu isiyo na hatia aliokolewa siku ile.

 

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.

 

WIMBO WA KATIKATI

 

Zab. 23 (K) 4

 

(K) Nijapopita katika bonde la uvuli wa mauti, Sitaogopa mabaya; Kwa maana Wewe upo pamoja nami.

 

Bwana ndiye mchungaji wangu,

Sitapungukiwa na kitu.

Katika malisho ya majani mabichi hunilaza,

Kando ya maji ya utulivu huniongoza. (K)

 

Hunihuisha nafsi yangu; na kuniongoza,

Katika njia za haki kwa ajili ya jina lake.

Naam, nijapopita kati aya bonde la uvuli wa mauti

Sitaogopa mabaya; kwa maana Wewe upo pamoja nami,

Gongo lako na fimbo yako vyanifariji. (K)

 

Waandaa meza mbele yangu,

Machoni pa watesi wangu.

Umenipaka mafuta kichwani pangu,

Na kikombe change kinafurika. (K)

 

Hakika wema na fadhili zinanifuata,

Siku zote za maisha yangu,

Nami nitakaa nyumbani mwa Bwana milele. (K)

 

SHANGILIO

 

Yn. 6:64, 69

 

Maneno yako, Ee Bwana, ni roho, tena ni uzima, Wewe unayo maneno ya uzima wa milele.

 

INJILI

 

Yn. 8:12-20

 

Yesu aliwaambia tena akasema, Mimi ndimi nuru ya ulimwengu, yeye anifuataye hatakwenda gizani kamwe, bali atakuwa na nuru ya uzima.

Basi Mafarisayo wakamwambia, Wewe unajishuhudia mwenyewe; ushuhuda wako si kweli.

Yesu akajibu, akawaambia, Mimi ningawa ninajishuhudia mwenyewe, ushuhuda wangu ndio kweli; kwa sababu najua nilikotoka na niendako; lakini ninyi hamjui nilikotoka wala niendako. Ninyi mwahukumu kwa kufuata mambo ya mwili; mimi simhukumu mtu. Nami nijapohukumu, hukumu yangu ni kweli; kwa kuwa mimi si peke yangu, bali ni mimi nay eye aliyenipeleka. Tena katika torati yenu imeandikwa kwamba, Ushuhuda wa watu wawili ni kweli. Mimi ndimi ninayejishuhudia mwenyewe, naye Baba aliyenipeleka ananishuhudia.

Basi wakamwambia, Yuko wapi Baba yako? Yesu akajibu, Mimi hamnijui, wala Baba yangu hammjui kama mngalinijijua mimi, mngalimjua na Baba yangu.

Maneno hayo aliyasema alipokuwa akifundisha hekaluni, katika chumba cha hazina; wala hakuna mtu aliyemkamata, kwa sababu saa yake ilikuwa haijaja bado.

 

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

MASOMO YA MISA, MACHI 20, 2022: JUMAPILI YA 3 YA KWARESIMA

SOMO 1 – Kut. 3:1-8a, 13-15

Basi, Musa alikuwa akilichunga kunda la Yethro mkwewe, kuhani wa Midiani; akaliongoza kundi nyuma ya jangwa, akafika mpka mlima wa Mungu, hata Horebu. Malaika wa Bwana akamtokea, katika mwali wa moto uliotoka katikati ya kijiti; akatazama, na kumbe! Kile kijiti kiliwaka moto, nacho kijiti hakikuteketea. Musa akasema, Nitageuka sasa, niyaone maono haya makubwa, na sababu kijiti hiki hakiteketei. Bwana alipoona ya kuwa amegeuka ili atazame, Mungu akamwita kutoka katikati ya kile kijiti, akasema, Musa! Musa! Akasema, Mimi hapa. Naye akasema, Usikaribie hapa; vua viatu vyako miguuni mwako; maana mahali hapo unaposimama ni nchi takatifu. Tena akasema, Mimi ni Mungu wa baba yako, Mungu wa Ibrahimu, Mungu wa Isaka, na Mungu wa Yakobo. Musa akaficha uso wake; kwa maana aliogopa kumwangalia Mungu.Bwana akasema, Hakika nimeyaona mateso ya watu wangu walioko Misri, nami nimekisikia kilio chao kwa sababu ya wasimamizi wao; maana nayajua maumivu yao; nami nimeshuka ili niwaokoe na mikono ya Wamisri, niwapandishe kutoka nchi ile, hata nchi njema, kisha pana; nchi ijaayo maziwa na asali.Musa akamwambia Mungu, Tazama, nitakapofika kwa wana wa Israeli, na kuwaambia, Mungu wa baba zenu amenituma kwenu; nao wakaniuliza, Jina lake n’nani? Niwaambie nini? Mungu akamwambia Musa, Mimi niko ambaye niko, akasema, Ndivyo utakavyowaambia wana wa Israeli; Mimi niko amenituma kwenu. Tena Mungu akamwambia Musa, Waambie wana wa Israeli maneno haya, Bwana, Mungu wa baba zenu, Mungu wa Ibrahimu, Mungu wa Isaka, Mungu wa Yakobo, amenituma kwenu; hili ndilo jina langu hata milele, nalo ni kumbukumbu langu hata vizazi vyote.Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.

WIMBO WA KATIKATI – Zab. 103:1-4, 6-8, 11 (K) 8

(K) Bwana amejaa huruma na neema.Ee nafsi yangu umhimidi Bwana.Naam, vyote vilivyo ndani yanguVilihimidi jina lake takatifu.

Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana,Wala usizisahau fadhili zake zote.

(K)Akusamehe maovu yako yote,Akuponya magonywa yako yote,Aukomboa uhai wako na kaburi,Akutia taji ya fadhili na rehema.

(K)

Bwana ndiye afanyaye mambo ya haki,Na hukumu kwa wote wanaoonewa.Alimjulisha Musa njia zake.Wana wa Israeli matendo yake. (K)

Bwana amejaa huruma na neema,Haoni hasira upesi, ni mwingi wa fadhili.Maana mbingu zilivyoinuka juu ya nchi,Kadiri ileile rehema zake ni kuu kwa wamchao. (K)

SOMO 2 – 1 Kor. 10:1-6, 10-12

Ndugu zangu, sipendi mkose kufahamu ya kuwa baba zetu walikuwa wote chini ya wingu; wote wakapita kati ya bahari; wote wakabatizwa wawe na Musa katika wingu na katika bahari; wote wakala chakula kile kile cha roho; wote wakanywa kinywaji kile kile cha roho; kwa maana waliunywea mwamba wa roho uliowafuata; na mwamba ule ulikuwa ni Kristo. Lakini wengi sana katika wao, Mungu hakupendezwa nao; maana waliangamizwa jangwani.Basi mambo hayo yalikuwa mifano kwetu, kusudi sisi tusiwe watu wa kutamani mabaya, kama wale nao walivyotamani.Wala msinung’unike kama wengine wao walivyonung’unika, wakaharibiwa na mharabu.Basi mambo hayo yaliwapata wao kwa jinsi ya mifano, yakaandikwa ili kutuonya sisi, tuliofikiliwa na miisho ya zamani. Kwa hiyo anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke.Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.

SHANGILIO – Zab. 95:8

Msifanye migumu mioyo yenu; Lakini msikie sauti yake Bwana.

INJILI – Lk. 13:1-9

Na wakati uo huo walikuwapo watu waliompasha Yesu habari ya Wagalilaya wale ambao Pilato alichangaya damu yao na dhabihu zao. Akawajibu akawaambia.Je! Mwadahni ya kwamba Wagalilaya hao walikuwa wenye dhambi kuliko Wagalilaya wote, hata wakapatwa na mambo hayo? Nawaambia, Sivyo; lakini msipotubu, ninyi nyote mtaangamia vivyo hivyo. Au wale kumi na wanane, walioangukiwa na mnara huko Siloamu, ukawaua, mwadhani ya kwamb awao walikuwa wakosaji kuliko watu wote waliokaa Yerusalemu? Nawaambia, Sivyo; lakini msipotubu, ninyi nyote mtaangamia vivyo hivyo.Akanena mfano huu; Mtu mmoja alikuwa na mtini umepandwa katika shamba lake la mizabibu; akaenda akitafuta matunda juu yake, asipate. Akamwambia mtunzaji wa shamba la mizabibu, Tazama, miaka mitatu hii naja nikitafuta matunda juu ya mtini huu, nisipate kitu; uukate, mbona hata nchi unaiharibu? Akajibu akamwambia, Bwana, uuache mwaka huu nao, hata niupalilie, niutilie samadi; nao ukizaa matunda baadaye, vema! La, usipozaa, ndipo uukate.Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

MASOMO YA MISA, JUNI 11, 2023: SHEREHE YA MWILI NA DAMU TAKATIFU YA BWANA WETU YESU KRISTU

SOMO 1

Kum. 8:2-3;14-16

Musa aliwaambia makutano: Nawe utaikumbuka njia ile yote Bwana, Mungu wako, aliyokuongoza miaka hii arobaini katika jangwa, ili akutweze, kukujaribu, kuyajua yaliyo moyoni mwako, kwamba utashika amri zake, au sivyo. Akakutweza, akakuacha uone njaa, akakulisha kwa mana, usiyoijua wewe wala baba zako hawakuijua; apate kukujulisha ya kuwa mwanadamu haishi kwa mkate tu, bali huishi kwa kila litokalo katika kinywa cha Bwana. Basi hapo moyo wako usiinuke, ukamsahau Bwana, Mungu wako, aliyekutoa katika nchi ya Misri, katika nyumba ya utumwa; aliyekuongoza katika jangwa lile kubwa lenye kitisho, lenye nyoka za moto na nge, nchi ya kiu isiyokuwa na maji; aliyekutolea maji katika mwamba mgumu, aliyekulisha jangwani kwa mana, wasiyoijua baba zako.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.

WIMBO WA KATIKATI

Zab. 147:12-15,19-20 (K) 12

(K) Msifu Bwana, Ee Yerusalemu.

Msifu Bwana, Ee Yerusalemu;

Msifu Mungu wako, Ee Sayuni.

Maana ameyakaza mapingo ya malango yako,

Amewabariki wanao ndani yako. (K)

Ndiye afanyaye amani mipakani mwako,

Akushibishaye kwa unono wa ngano.

Huipeleka amri yake juu ya nchi,

Neno lake lapiga mbio sana. (K)

Humhubiri Yakobo neno lake,

Na Israeli amri zake na hukumu zake.

Hakulitendea taifa lolote mambo kama hayo,

Wala hukumu zake hawakuzijua.

aleluya. (K)

SOMO 2

1Kor. 10:16-17

Kikombe kile cha baraka tukibarikicho, je! Si ushirika wa damu ya Kristo? Mkate ule tuumegao, si ushirika wa mwili wa Kristo? Kwa kuwa mkate ni mmoja, sisi tulio wengi tu mwili mmoja; kwa maana sisi sote twapokea sehemu ya ule mkate mmoja.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.

SHANG1LIO

Yn. 6:51

Aleluya, aleluya,

Mimi ndimi chakula chenye uzima kilichoshuka kutoka mbinguni; asema Bwana; mtu akila chakula hiki, ataishi milele.

Aleluya.

INJILI

Yn. 6:51-58

Mimi ndimi chakula chenye uzima kilichoshuka kutoka mbinguni; mtu akila chakula hiki, ataishi milele. Na chakula nitakachotoa mimi ni mwili wangu, kwa ajili ya uzima wa ulimwengu. Basi Wayahudi walishindana wao kwa wao wakisema, Awezaje mtu huyu kutupa sisi mwili wake ili tuule? Basi Yesu akawaambia, Amin, amin, nawaambieni, Msipoula mwili wake Mwana wa Adamu na kuinywa damu yake, hamna uzima ndani yenu. Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu anao uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya mwisho. Kwa maana mwili wangu ni chakula cha kweli, na damu yangu ni kinywaji cha kweli. Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu hukaa ndani yangu, nami hukaa ndani yake. Kama vile Baba aliye hai alivyonituma mimi, nami ni hai kwa Baba; kadhalika naye mwenye kunila atakuwa hai kwa mimi. Hiki ndicho chakula kishukacho kutoka mbinguni; si kama mababa walivyokula, wakafa; bali akilaye chakula hicho ataishi milele.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

MASOMO YA MISA, MACHI 28, 2022: JUMATATU: JUMA LA 4 LA KWARESIMA

SOMO 1

Isa. 65:17-21

 

Bwana asema: Tazama, mimi naumba mbingu mpya na nchi mpya, na mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni. Lakini furahini, mkashangilie daima, kwa ajili ya hivi niviumbavyo; maana, tazama, naumba Yerusalemu uwe shangwe, na watu wake wawe furaha.

Nami nitaufurahia Yerusalemu, nitawaonea shangwe watu wangu; sauti ya kulia haitasikiwa ndani yake tena, wala sauti ya kuomboleza. Hatakuwapo tena mtoto wa siku chache, wala mzee asiyetimia siku zake; kwa maana mtoto atakufa mwenye umri wa miaka mia; bali mtenda dhambi mwenye umri wa miaka mia atalaaniwa. Nao watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake.

 

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.

 

WIMBO WA KATIKATI

Zab. 30:1, 3-5, 10-12 (K) 1

 

(K) Nitakutukuza, ee Bwana, kwa maana umeniinua.

 

Ee Bwana, nitakutukuza kwa maana umeniinua,

Wala hukuwafurahisha adui zangu juu yangu.

Umeniinua nafsi yangu,

Ee Bwana, kutoka kuzimu.

Umenihuisha na kunitoa

Miongoni mwao washukao shimoni. (K)

 

Mwimbieni Bwana zaburi,

Enyi watauwa wake.

Na kufanya shukrani.

Kwa kumbukumbu la utakatifu wake.

Maana ghadhabu zake ni za kitambo kidogo,

Katika radhi yake mna uhai.

Huenda kilio huja kukaa usiku,

Lakini asubuhi huwa furaha. (K)

 

Ee Bwana, usikie, unirehemu,

Bwana, uwe msaidizi wangu.

Uligeuza matanga yangu kuwa machezo;

Ulinivua gunia, ukanivika furaha.

Ee Bwana, mungu wangu,

Nitakushukuru milele. (K)

 

SHANGILIO

Eze. 33:11

 

Sikufurahii kufa kwake mtu mwovu, asema Bwana, bali aiache njia yake mbaya, akaishi.

 

INJILI

Yn. 4:43-54

 

Baada ya siku mbili hizo Yesu aliondoka huko, akaenda Galilaya. Kwa maana Yesu mwenyewe alishuhudia ya kwamba nabii hapati heshima katika nchi yake mwenyewe. Basi alipofika Galilaya, Wagalilaya walimpokea; kwa kuwa wameyaona mambo yote aliyoyatenda huko Yerusalemu wakati wa sikukuu; maana hao nao waliiendea sikukuu.

Basi alifika tena Kana ya Galilaya, hapo alipoyafanya yale maji kuwa divai. Na palikuwa na diwani mmoja ambaye mwanawe hawezi huko Kapernaumu. Huyo aliposikia ya kwamba Yesu amekuja kutoka Uyahudi mpaka Galilaya, alimwendea, akamsihi ashuke na kumponya mwanawe; kwa maana alikuwa kufani. Basi Yesu akamwambia, Msipoona ishara na maajabu hamtaamini kabisa? Yule diwani akamwambia, Bwana, ushuke asijakufa mtoto wangu. Yesu akamwambia, Enenda; mwanao yu hai. Mtu yule akalisadiki lile neno aliloambiwa na Yesu, naye akashika njia. Hata alipokuwa akishuka, watumwa wake walimlaki, wakisema ya kwamba mtoto wake yu hai. Basi akawauliza habari ya saa alipoanza kuwa hajambo; nao wakamwambia, jana, saa saba, homa ilimwacha. Basi babaye akafahamu ya kuwa ni saa ile ile alipoambiwa na Yesu, Mwanao yu hai. Akaamini yeye na wote wa nyumbani mwake.

Hiyo ni ishara ya pili aliyoifanya Yesu, alipokuwa ametoka Uyahudi kufika Galilaya.

 

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

MASOMO YA MISA, MEI 21, 2023:
DOMINIKA YA 7 YA PASAKA
SHEREHE YA KUPAA BWANA

MWANZO:
Mdo. 1:11

Enyi watu wa Galilaya, mbona mmesimama mkitazama mbinguni? Atakuja vivyo hivyo mlivyomwona akienda zake mbinguni, Aleluya.

SOMO 1

Mdo. 1:1-11

Kitabu kile cha kwanza nalikiandika, Theofilo, katika habari ya mambo yote aliyoanza Yesu kufanya na kufundisha, hata siku ile alipochukuliwa juu, alipokuwa amekwisha kuwaagiza kwa Roho Mtakatifu wale mitume aliowachagua; wale aliowadhihirishia nafsi yake, kwa dalili nyingi, baada ya kuteswa kwake, ya kwamba yu hai, akiwatokea muda wa siku arobaini, na kuyanena mambo yaliyouhusu ufalme wa Mungu. Hata alipokuwa amekutana nao aliwaagiza wasitoke Yerusalemu, bali waingoje ahadi ya Baba, ambayo mlisikia habari zake kwangu; ya kwamba Yohane alibatiza kwa maji, bali ninyi mtabatizwa katika Roho Mtakatifu baada ya siku hizi chache.

Basi walipokutanika, wakamwuliza, wakisema, Je! Bwana, wakati huu ndipo unapowarudishia Israeli ufalme? Akawaambia, Si kazi yenu kujua nyakati wala majira, Baba aliyoyaweka katika mamlaka yake mwenyewe. Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi.

Akiisha kusema hayo, walipokuwa wakitazama, akainuliwa, wingu likampokea kutoka machoni pao. Walipokuwa wakikaza macho mbinguni, yeye alipokuwa akienda zake, tazama, watu wawili wakasimama karibu nao, wenye nguo nyeupe, wakasema, Enyi watu wa Galilaya, mbona mmesimama mkitazama mbinguni? Huyu Yesu aliyechukuliwa kutoka kwenu kwenda juu mbinguni, atakuja jinsi iyo hiyo mlivyomwona akienda zake mbinguni.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.

WIMBO WA KATIKATI

Zab. 47 : 1-2, 5-6, 7-8, (K) 5

(K) Mungu amepaa kwa kelele za shangwe, Bwana kwa sauti ya baragumu. au: Aleluya

Enyi watu wote, pigeni makofi,
Mpigieni Mungu kelele kwa sauti ya shangwe,
Kwa kuwa Bwana Aliye juu, mwenye kuogofya,
Ndiye mfalme mkuu juu ya dunia yote. (K)

Mungu amepaa kwa kelele za shangwe,
Bwana kwa sauti ya baragumu.
Mwimbieni Mungu, naam, imbeni;
Mwimbieni mfalme wetu, naam, imbeni. (K)

Maana Mungu ndiye mfalme wa dunia yote,
Imbeni kwa akili.
Mungu awamiliki mataifa,
Mungu ameketi katika kiti chake kitakatifu. (K)

SOMO 2

Efe 1 : 17-23

Mungu wa Bwana wetu Yesu Kristo, Baba wa utukufu, awape ninyi roho ya hekima na ya ufunuo katika kumjua yeye; macho ya mioyo yenu yatiwe nuru, mjue tumaini la mwito wake jinsi lilivyo; na utajiri wa utukufu wa urithi wake katika watakatifu jinsi ulivyo; na ubora wa ukuu wa uweza wake ndani yetu tuaminio jinsi ulivyo; kwa kadiri ya utendaji wa nguvu za uweza wake; aliotenda katika Kristo alipomfufua katika wafu, akamweka mkono wake wa kuume katika ulimwengu wa roho; juu sana kuliko ufalme wote, na mamlaka, na nguvu, na usultani, na kila jina litajwalo, wala si ulimwenguni humu tu, bali katika ule ujao pia; akavitia vitu vyote chini ya miguu yake, akamweka awe kichwa juu ya vitu vyote kwa ajili ya kanisa; ambalo ndilo mwili wake, ukamilifu wake anayekamilika kwa vyote katika vyote.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.

SHANGILIO

Mt. 28:19-20

Aleluya, aleluya,
Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, na tazama, mimi nipo pamoja nanyi sikuzote.
Aleluya.

INJILI

Mt. 28:16-20

Wale wanafunzi kumi na mmoja walikwenda Galilaya mpaka mlima ule aliowaagiza Yesu. Nao walipomwona, walimsujudia; lakini baadhi yao waliona shaka. Yesu akaja kwao, akasema nao, akawambia, Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani. Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu; na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi; na tazama, mimi nipo pamoja nanyi sikuzote, hata ukamilifu wa dahari.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

MASOMO YA MISA, MARCHI 31, 2022: ALHAMISI, JUMA LA 4 LA KWARESIMA

SOMO 1

Hek. 2:1, 12-22

Wasiomsadikia Mungu walisema hivi, huku wakimfikiri yasiyo kweli, Zaidi ya hayo na tumwotee mtu wa haki, maana hatuna haja naye, naye yu kinyume cha matendo yetu; atukaripia ya kama tumeiasi torati, na kutushitaki ya kama tumekosa adabu. Asema ya kwamba anamjua Mungu, na kujiita mtumishi wa Bwana. Ametuwia magombezi ya fikira zetu. Hata kumtazama twaona ni kugumu; maan amaisha yake si sawasawa na masiha ya wengine, na mwenendo wake ni wa kigeni. Tuanhesabiwa naye kuwa kama madini hafifu; anajitenga na njia zetu kama na uchafu. Wenye haki asema kuwa mwisho wao ni heri; hujivuna ya kwamba Mungu ndiye baba yake.

Haya na tuone kama maneno yake ni kweli; tufanye kujaribu yatakayompata wakati wa mwisho wake; mradi mwenye haki akiwa ni mwana wa Mungu, Yeye atamtegemeza na kumwokoa mikononi mwa adui zake. Na tumhakikishe kwa jeuri na maumivu, ili tujifunze upole wake na kuithibitisha saburi yake akidhulumiwa. Hata tumhukumu auawe mauti ya aibu, maana ataangaliwa sawasawa na maneno yake.

Ndivyo walivyosemezana, wakakosea kabisa. Kwa maana uovu wao uliwapofusha; hawakuzijua siri za Mungu; wala hawakuutarajia mshahara wa utakatifu, wala kudhani ya kwamba iko thawabu kwao wenye roho zisizo na hatia.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.

WIMBO WA KATIKATI

Zab. 34:16-20, 22 (K) 18

(K) Bwana yu karibu nao waliovunjika moyo.

Uso wa Bwan ani juu ya watenda mabaya,

Aliondoe kumbukumbu lao duniani.

Walilia, naye Bwan akasikia,

Akawaponya na taabu zao zoe. (K)

Bwana yu karibu nao waliovunjika moyo,

Na waliopondeka roho huwaokoa.

Mateso ya mwenye haki ni mengi,

Lakini Bwana humponya nayo yote. (K)

Huihifadhi mifupa yake yote,

Haukuvunjika hata mmoja.

Bwana huzikombo a nafsi za watumishi wake,

Wala hawatahukumiwa wote wamkimbiliao. (K)

SHANGILIO

Lk. 8:15

Heri wale walishikao neno la Mungu katika moyo wao mwema na mnyofu, na wazaao matunda katika uvumilivu.

INJILI

Yn. 7:1-2, 25-30

Baada ya hayo Yesu alikuwa akitembea katika Galilaya; maana hakutaka kutembea katika Uyahudi, kwa sababu Wayahudi walikuw awakitafuta kumwua.

Na sikukuu ya Wayahudi, Sikukuu ya Vibanda, ilikuwa karibu. Hata ndugu zake walipokwisha kukwea kuiendea sikukuu, ndipo yeye naye laipokwea, si kwa wazi bali kana kwamba kwa siri.

Basi baadhi ya watu wa yerusalemu wakasema, Je! Huyu siye wanayemtafuta ili wamwue? Na kumbe! Anena waziwazi, wala hawamwambii neno! Yamkini hao wakuu tuna jua hakika ya kuwa huyu ndiye Kristo? Lakini huyu twamjua atokako; bali Kristo atakapokuja hakuna ajuaye atokako.

Basi Yesu akapaza sauti yake hekaluni, akifundisha na kusema, Mimi mnanijua, na huko nitokako mnakujua; wala sikuja kwa nafsi yangu; ila yeye aliyenipeleka ni wa kweli, msiyemjua ninyi. Mimi namjua, kwa kuwa nimetoka kwake, naye ndiye aliyenituma.

Basi wakatafuta kumkamata; lakini hakuna mtu aliyeunyosha mkono wake ili kumshika, kwa sababu saa yake ilikuwa haijaja bado.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

JUMAPILI YA 19 YA MWAKA A: MASOMO YA MISA AGOSTI 13, 2023

Somo la Kwanza

1Fal 19:9, 11-13

Eliya alifika kunako pango, akalala ndani yake. Na tazama, neno la Bwana likamjia. Akasema, Toka, usimame mlimani mbele za Bwana. Na tazama, Bwana akapita; upepo mwingi wa nguvu ukaipasua milima, ukaivunjavunja miamba mbele za Bwana; lakini Bwana hakuwamo katika upepo ule; na baada ya upepo, tetemeko la nchi; lakini Bwana hakuwamo katika lile tetemeko la nchi: na baada ya tetemeko la nchi kukawa na moto; lakini Bwana hakuwamo katika moto ule; na baada ya moto sauti ndogo, ya utulivu.

Ikawa, Eliya alipoisikia, alijifunika uso wake katika mavazi vake, akatoka, akasimama mlangoni mwa pango.

NENO LA BWANA…….

Wimbo wa Katikati

Zab 85:8-13

Nisikie atakavyosema Mungu Bwana,
Maana atawambia watu wake amani.
Hakika wokovu wake u karibu na wamchao,
Utukufu ukae katika nchi yetu.

(K) Ee Bwana, utuonyeshe rehema zako, Utupe wokovu wako.

Fadhili na kweli zimekutana,
Haki na amani zimebusiana.
Kweli imechipuka katika nchi,
Haki imechungulia kutoka mbinguni.

(K) Ee Bwana, utuonyeshe rehema zako, Utupe wokovu wako.

Naam, Bwana atatoa kilicho chema,
Na nchi yetu itatoa mazao yake.
Haki itakwenda mbelc zake,
Nayo itazifanya hatua zake kuwa njia.

(K) Ee Bwana, utuonyeshe rehema zako, Utupe wokovu wako.

Somo la Pili

Rum 9:1-5

Nasema kweli katika Kristo, sisemi uongo, dhamiri yangu ikinishuhudia katika Roho Mtakatifu, ya kwamba nina huzuni nyingi na maumivu yasiyokoma moyoni mwangu.

Kwa maana ningeweza kuomba mimi mwenyewe niharimishwe na kutengwa na Kristo kwa ajili ya ndugu zangu, jamaa zangu kwa jinsi ya mwili; ambao ni Waisraeli, wenye kule kufanywa wana, na ule utukufu, na maagano, na kupewa torati, na ibada ya Mungu, na ahadi zake; ambao mababu ni wao, na katika hao alitoka Kristo kwa jinsi ya mwili.

Ndiye aliye juu ya mambo yote, Mungu, mwenye kuhimidiwa milele. Amina.

NENO LA BWANA…..

Shangilio

Lk 19:38

Aleluya, aleluya,
Abarikiwe Mfalme ajaye kwa jina la Bwana;
Aleluya.

Somo la Injili

Mt 14:22-33

Yesu aliwalazimisha wanafunzi wake wapande chomboni na kutangulia mbele yake kwenda ng’ambe. wakati yeye alipokuwa akiwaaga makutano. Naye alipokwisha kuwaaga makutano, alipanda mlimani faraghani, kwenda kuomba. Na kulipokuwa jioni, alikuwako huko peke yake.

Na kile chombo kimekwisha kufika katikati ya bahari, kinataabika sana na mawimbi; maana upepo ulikuwa wa mbisho. Hata wakati wa zamu ya nne ya usiku Yesu akawaendea. akienda kwa miguu juu ya bahari.

Wanafunzi walipomwona akienda juu ya bahari, wakafadhaika, wakisema, Ni kivuli, wakapiga yowe kwa hofu. Mara Yesu akanena, akawaambia, Jipeni movo; ni mimi; msiogope. Petro akamjibu, akasema, Bwana, ikiwa ni wewe, niamuru nije kwako juu ya maji. Akasema, Njoo.

Petro akashuka chomboni, akaenda kwa miguu juu ya maji, ili kumwendea Yesu. Lakini alipouona upepo, akaogopa; akaanza kuzama, akapiga yowe akisema, Bwana, niokoe.

Mara Yesu akanyosha mkono wake, akamshika, akamwambia, Ewe mwenye imani haba, mbona uliona shaka? Nao walipopanda chomboni, upepo ulikoma. Nao waliokuwamo ndani ya chombo wakamsujudia wakisema, Hakika wewe ni Mwana wa Mungu.

NENO LA BWANA……….

MASOMO YA MISA, DOMINIKA YA 5 YA KWARESIMA, MWAKA C

SOMO 1: Isa. 43:16-21

Bwana asema hivi, yeye afanyaye njia katika bahari, na mahali pa kupita katika maji yenye nguvu; atoaye gari na farasi, jeshi la askari na uwezo; wamelala, hawataondoka; wametoweka, wamezimwa mfano wa utambi. Msiyakumbuke mambo ya kwanza, wala msiyatafakari mambo ya zamani. Tazama, nitatenda neno jipya; sasa litachipuka; je! Hamtalijua sasa? Nitafanya njia hata jangwani, na mito ya maji nyikani. Wanyama wa kondeni wataniheshimu, mbweha pia na mbuni; kwa sababu nimewapa maji jangwani, na mito nyikani, ili kuwanywesha watu wangu, wateule wangu; watu wale niliojiumbia nafsi yangu, ili wazitangaze sifa zangu.

WIMBO WA KATIKATI: Zab. 126, (K) 3

(K) Bwana alitutendea mambo makuu, tulikuwa tukifurahi.

Bwana alipowarejeza mateka wa Sayuni,

Tulikuwa kama waotao ndoto.

Ndipo kinywa chetu kilipojaa kicheko.

Na ulimi wetu kelele za furaha. (K)

Ndipo waliposema katika mataifa,

Bwana amewatendea mambo makuu.

Bwana alitutendea mambo makuu,

Tulikuwa tukifurahi. (K)

Ee Bwana, uwarejeze watu wetu waliofungwa,

Kama vijito vya Kusini.

Wapandao kwa machozi,

Watavuna kwa kelele za furaha. (K)

Ingawa mtu anakwenda zake akilia,

Azichukuapo mbegu za kupanda.

Hakika atarudi kwa kelele za furaha,

Aichukuapo miganda yake. (K)

SOMO 2: Flp. 3:8-14

Nayahesabu mambo yote kuwa hasara kwa ajili ya uzuri usio na kiasi wa kumjua Kristo Yesu, Bwana wangu; ambaye kwa ajili yake nimepata hasara ya mambo yote nikiyahesabu kuwa kama mavi ili nipate Kristo; tena nionekane katika yeye, nisiwe na haki yangu mwenyewe ipatikanayo kwa sheria, bali ile ipatikanayo kwa Imani iliyo katika Kristo, haki ile itokayo kwa Mungu, kwa Imani; ili nimjue yeye, na uweza wa kufufuka kwake, na ushirika wa mateso yake, nikifananishwa na kufa kwake; ili nipate kwa njia yoyote kuifikia kiyama ya wafu. Si kwamba nimekwisha kufika, au nimekwisha kuwa mkamilifu; la! Bali nakaza mwendo ili nipate kulishika lile ambalo kwa ajili yake nimeshikwa na Kristo Yesu. Ndugu, sijidhanii nafsi yangu kwamba nimekwisha kushika; ila natenda neno moja tu; nikiyasahau yaliyo nyuma, nikiyachuchumilia yaliyo mbele; nakaza mwendo, niifikilie mede ya thawabu ya mwito mkuu wa Mungu katika Kristo Yesu.

SHANGILIO: Yoe. 2:12, 13

Lakini hata sasa, asema Bwana, nirudieni mimi kwa mioyo yenu yote, kwa maana ni mwenye neema na huruma.

INJILI: Yn. 8:1-11

Yesu akaenda mpaka mlima wa Mizeituni. Hata asubuhi kulipokucha akaingia tena hekaluni, na watu wote wakamwendea; naye akaketi, akawa akiwafundisha.

Waandishi na Mafarisayo wakamletea mwanamke aliyefumaniwa katika uzinzi, wakamweka katikati. Wakamwambia, Mwalimu, mwanamke huyu amefumaniwa alipokuwa akizini. Basi katika torati, Musa alituamuru kuwapiga kwa mawe wanawake namna hii; nawe wasemaje? Nao wakasema neno hili wakimjaribu, ili wapate sababu ya kumshitaki.

Lakini Yesu akainama, akaandika kwa kidole chake katika nchi. Nao walipozidi kumhoji, alijiinua, akawaambia, Yeye asiye na dhambi miongoni mwenu na awe wa kwanza wa kumtupia jiwe. Akainama tena, akaandika kwa kidole chake katika nchi. Nao waliposikia, wakashitakiwa na dhamiri zao, wakatoka mmoja mmoja, wakianzia tangu wazee hata wa mwisho wao; akabaki Yesu peke yake, na yule mwanamke amesimama katikati.

Yesu akajiinua asimwone mtu ila yule mwanamke, akamwambia, Mwanamke, wako wapi wale washitaki wako? Hakuna aliyekuhukumu kuwa na hatia? Akamwambia, Hakuna, Bwana. Yesu akamwambia, Wala mimi sikuhukumu. Enenda zako; wala usitende dhambi tena.

MASOMO YA MISA, JUNI 04, 2023: SHEREHE YA UTATU MTAKATIFU – Jumapili baada ya Pentekoste

MWANZO:

Asifiwe Mungu Baba na Mwana na Roho Mtakatifu; kwasababu ametufanyizia huruma yake.

SOMO 1

Kut. 34 : 4-6, 8-9

Musa aliinuka na mapema asubuhi, naye akakwea katika mlima wa Sinai, kama Bwana alivyomwamuru, akazichukua hizo mbao mbili za mawe mkononi mwake.

Bwana akashuka ndani ya lile wingu, akasimama pamoja naye huko, akalitangaza jina la Bwana. Bwana akapita mbele yake, akatangaza, Bwana, Bwana, Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli; Musa akafanya haraka, akainamisha kichwa chake hata nchi, akasujudu. Akasema, Ikiwa sasa nimepata neema mbele zako, Bwana, nakuomba, Bwana, uende kati yetu maana ni watu wenye shingo ngumu; ukasamehe uovu wetu na dhambi yetu, ukatutwae tuwe urithi wako.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu

WIMBO WA KATIKATI

Dan. 3:52-56. (K) 52

(K) Wastahili kusifiwa na kutukuzwa milele.

Umehimidiwa, Ee Bwana, Mungu wa baba zetu:

Wastahili kusifiwa na kutukuzwa milele.

Limehimidiwa jina lako takatifu, tukufu;

Wastahili kusifiwa na kutukuzwa milele. (K)

Umehimidiwa katika hekalu la fahari yako takatifu;

Wastahili kusifiwa na kutukuzwa milele.

Umehimidiwa juu ya kiti cha ufalme wako;

Wastahili kusifiwa na kutukuzwa milele. (K)

Umehimidiwa utazamaye vilindi, uketiye juu ya makerubi;

Wastahili kusifiwa na kutukuzwa milele.

Umehimidiwa katika anga la mbinguni

Wastahili kusifiwa na kutukuzwa milele. (K)

SOMO 2

2 Kor. 13 :11-14

Hatimaye, ndugu, kwaherini; mtimilike, mfariji- ke, nieni mamoja, mkae katika amani; na Mungu wa upendo na amani atakuwa pamoja nanyi. Sali- mianeni kwa busu takatifu. Watakatifu wote wawasalimu. Neema ya Bwana Yesu Kristo, na pendo la Mungu. na ushirika wa Roho Mtakatifu ukae nanyi nyote.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.

SHANG1LIO

Ufu. 1 :8

Aleluya, Aleluya,

Atukuzwe Baba na Mwana na Roho Mtakatifu, Mungu ambaye yupo, aliyekuwako, na atakayekuja.

Aleluya.

INJILI

Yn. 3:16-18

Yesu alimwambia Nikodemu: Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe wa pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele. Maana Mungu hakumtuma Mwana ulimwenguni ili auhu- kumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye. Amwaminiye yeye hahukumiwi; asiyeamini amekwisha kuhukumiwa; kwa sababu hakuliamini jina la Mwana pekee wa Mungu.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

MASOMO YA MISA, MACHI 22, 2022: JUMATANO, JUMA LA 3 LA KWARESIMA

SOMO 1 – Kumb. 4:1, 5-9

Musa aliwaambia makutano: Ee Israeli, zisikilizeni amri na hukumu niwafundishazo, ili mmzitende; mpate kuishi na kuingia na kuimiliki nchi awapayo Bwana, Mungu wa baba zenu.Angalieni nimewafundisha amri na hukumu, vile vile kama Bwana, Mungu wangu, alivyoniamuru, ili mzitende katika nchi mwmingiayo ili kuimiliki. Zishikeni basi,5 mkazitende, maana hii ndiyo hekima yenu na akili zenu, machoni pa mataifa watakaozisikia⁵ amri hizi zote, nao watasema, Hakika taifa hili kubwa ni watu wenye hekima na akili. Kwa maana liko taifa gani kubwa, lililo na Mungu aliye karibu nao, kama Bwana, Mungu wetu, alivyo, kila tumwitapo? Tena liko taifa gani kubwa, lililo na amri na hukumu zenye haki kama torati hii yote, ninayoiweka mbele yenu leo.

Lakini, jihadhari nafsi yako, ukailinde roho yako kwa bidii, usije ukayasahau mambo yale uliyoyaona kwa macho yako, yakaondoka moyoni mwako siku zote za maisha yako; bali uwajulishe watoto wako na watoto wa watoto wako.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.

WIMBO WA KATIKATI – Zab. 147:12-13, 15-16, 19-20 (K) 12(K)

Msifu Bwana, Ee Yerusalemu.Msifu Bwana, Ee Yerusalemu;

Msifu Mungu wako, Ee Sayuni.Maana ameyakaza mapingo ya malango yako,Amewabariki wanao ndani yako. (K)

Huipeleka amri yake juu ya nchi,Neno lake lapiga mbio sana.

Ndiye atoaye theluji kama sufu,Huimwaga barafu yake kama majivu. (K)

Humhubiri Yakobo neno lake,Na Israeli amri zake na hukumu zake.

Hakulitendea taifa lolote mambo kama hayo,Wala hukumu zake hawakuzijua. (K)

SHANGILIO

Mbegu neno la Mungu, mpanzi lakini ni Kristu; Yeyote ampataye, ataishi milele.

INJILI – Mt. 5:17-19

Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Msidhani kuwa nalikuja kuitangua torati au manabii; la, sikuja kutangua, bali kutimiliza. Kwa maana, amin, nawaambia, Mpaka mbingu na nchi zitakapoondoka, yodi moja wala nukta moja ya torati haitaondoka hata yote yatimie. Basi mtu yeyote atakayevunja amri moja katika hizi zilizo ndogo, na kuwafundisha watu hivyo, ataitwa mdogo kabisa katika ufalme wa mbinguni; bali mtu atakayezitenda na kuzifundisha, huyo ataitwa mkubwa katika ufalme mbinguni.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

MASOMO YA MISA, MACHI 26, 2022: JUMAMOSI, JUMA LA 3 LA KWARESIMA

SOMO 1

Hos. 5:15-6:6

Bwana asema: Katika taabu yao watanitafuta kwa bidii:

Njoni, tumrudie Bwana; maana yeye amerarua, na yeye atatuponya; yeye amepiga, na yeye atatufunga jeraha zetu. Baada ya siku mbili atatufufua; siku ya tatu atatuinua, nasi tuataishi mbele zake. Nasi na tujue, naam, tukaendelee kumjua Bwana; kutokea kwake ni yakini kama asubuhi; naye atatujilia kama mvua, kama mvua ya vuli iinyeshayo nchi.

Ee Efraimu, nikutendee nini? Ee Yuda, nikutendee nini? Kwa maana fadhili zenu ni kama wingu la asubuhi na kama umande utowekao mapema. Kwa sababu hiyo nimewakata-kata kwa vinya vya manabii; nimewaua kwa maneno ya kinywa change na hukumu yangu itatokea kama mwanga. Maana nataka fadhili wala si sadaka; na kumjua Mungu kuliko sadaka za kuteketezwa.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.

WIMBO WA KATIKATI

Zab. 51:1-2, 16-19 (K) Hos. 6:6

(K) Ninavyotaka ni fadhili, si sadaka.

Ee Mungu, unirehemu,

Sawasawa na fadhili zako.

Kiasi cha wingi wa rehema zako,

Uyafute makosa yangu.

Unioshe kabisa na uovu wangu,

Unitakase dhambi zangu. (K)

Maana hupendezwi na dhabihu, au ningeitoa,

Wewe huridhii sadaka ya kuteketezwa.

Dhabihu za MUngu ni roho iliyovunjika;

Moyo uliovunjika na kupondeka,

Ee Mungu, hutaudharau. (K)

Uitendee mema Sayuni kwa radhi yako,

Uzijenge kuta za Yerusalemu.

Ndipo utakapopendezwa na dhabihu za haki,

Na sadaka za kuteketezwa, na kafara. (K)

SHANGILIO

Eze. 18:3

Tupilieni mbali nanyi makosa yenu yote mliyoyakosa yote, asema Bwana, jifanyieni moy mpya na roho mpya.

INJILI

Lk. 18:9-14

Yesu aliwaambia mfano huu watu waliojikinai ya kuwa wao ni wenye haki, wakiwadharau wengine wote. Watu wawili walipanda kwenda hekaluni kusali, mmoja Farisayo, wa pili mtoza ushuru. Yule Farisayo akasimama akiomba hivi moyoni mwake; Ee Mungu, nakushukuru kwa kuwa mimi si kama watu wengine, wanyang’anyi, wadhalimu, wazinzi, wala kama huyu mtoza ushuru. Mimi nafunga mara mbili kwa juma; hutoa zaka katika mpato yangu yote. Lakini yule mtoza ushuru alisimama mbali, wala hakuthubutu hata kuinua macho yake mbinguni, bali alijipiga-piga kifua akisema, ee Mungu, uniwie radhi mimi mwenye dhambi. Nawaambia, huyu alishuka kwenda nyumbani kwake amehesabiwa haki kuliko yule; kwa maana kila ajikwezaye atadhiliwa, naye ajidhiliye atakwezwa.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Shopping Cart
🏠 Home 📖 Reading 🖼️ Gallery 💬 AI Chat 📘 About