Sala za Maombi

Novena ya Siku tisa kwa Mtakatifu Agustino wa Hippo: Sala zote na Litania

Anza Novena hii tarehe 19 Agosti ili kumalizia tarehe 27 Agosti na kusheherekea tarehe 28 Agosti, Sikukuu ya Mtk. Augustino wa Hippo.

SIKU YA KWANZA – kutafuta ukweli – kweli ni nini?

Kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina

Tafakari
Pamoja na Mtakatifu Augustino tunasema “ Umetuumba kwa ajili yako ee Bwana, kwani ni wewe peke yako ndie Mungu wetu, na nyoyo zetu hazitapumzika, hadi tupumzike ndani mwako.”

Tunapoanza Novena yetu kwa Mtakatifu Augustino tunamwomba Mungu neema ya kuwa na roho kama yake katika safari yetu katika kuzitambua nafsi zetu. Tunatafakari sisi ni nani na tunaelekea wapi kama wafuasi wa Mtakatifu Augustino katika dunia ya leo. Kama Mt Augustino alivyoutafuta ukweli bila kuchoka, nasi tutulie na kuruhusu maswali haya yaguse ufahamu wetu. Ni nini kinachonisababisha niendelee kumtafuta Mungu? Baada ya kumpata Mungu, ninamfanyaje awe hai kwa watu wale ninaoishi nao?

Kama kuna jambo moja Mt Augustino anasisitiza tena na tena kuhusu kumtafuta Mungu, ni kuwa lazima tuanze kumtafuta ndani mwetu. Huko ndiko tutakuta ukweli, mwanga na furaha katika Kristu mwenyewe. Ndani ya nafsi zetu ndiko tutasikilizwa tunaposali, katika nafsi zetu ndiko tutampenda Mungu na kumwabudu.

Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino

Bwana utuhurumie Bwana utuhurumie

Kristu utuhurumie Kristu utuhurumie

Bwana utuhurumie Bwana utuhurumie

Kristu utusikie Kristu utusikilize

Baba wa mbinguni Mungu utuhurumie

Mwana Mkombozi wa dunia Mungu utuhurumie

Roho Mtakatifu Mungu utuhurumie

Utatu Mtakatifu Mungu mmoja utuhurumie

Maria Mama wa Yesu utuombee

Maria Mama wa faraja utuombee

Maria Mama wa shauri jema utuombee

Mt. Augustimo nyota angavu ya Kanisa utuombee

Mt Augustino uliyejawa bidii kwa ajili ya kuutafuta utukufu wa Mungu utuombee

Mt. Augustino mtetezi jasiri wa Ukweli utuombee

Mt Augustino ushindi wa neema ya Mungu utuombee

Mt Augustino uliyewaka mapendo kwa Mungu utuombee

Mt Augustino mkuu sana na mnyenyekevu sana utuombee

Mt Augustino mfalme wa maaskofu na wanateolojia utuombee

Mt Augustino baba wa maisha ya kitawa utuombee

Mt Augustino mtakatifu kati ya wenye hekima na mwenye hekima kati ya watakatifu utuombee

Utuombee Mtakatifu Augustino – ili tustahili maagano ya Kristu.

Tuombe: Umetuumba kwa ajili yako ee Bwana, na nyoyo zetu hazitapumzika kamwe, hadi tutakapopumzika ndani mwako. Tunakuomba utubariki katika mahangaiko yetu ya kukutafuta wewe na utusaidie tunapokutana na makwazo. Tunapokupata, tunaomba utujalie neema ya kuwa waaminifu kwako ee Mungu wa historia, tuwe waaminifu kwa Yesu Kristu Mkombozi wetu, kwa Kanisa letu na mafundisho yake, na tuwe waaminifu katika wito wetu tuliouchagua katika kukutumikia wewe. Tunaomba hayo kwako wewe Baba mwema, kwa njia ya Kristu Bwana wetu na kwa maombezi ya Mtakatifu Augustino Msimamizi wa Jumuiya yetu, Amina.

Baba yetu……, Salamu Maria….., Atukuzwe Baba……

Siku ya pili – Utulivu

Kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina

Tafakari

“Ingia sasa, ndani ya moyo wako (Isaya 46:8) na uwe na imani, utamkuta Kristu humo. Humo anaongea na wewe, mimi, mwalimu, napaaza tu sauti yake lakini Yeye ndiye anayekufunza wewe kwa ufanisi zaidi katika utulivu wako”

Je tunapenda maisha ya utulivu ambapo tunapata muda wa kumtafakari Mungu na mambo anayotutendea katika maisha yetu? Kwa vile Yesu anaongea nasi katika utulivu, inatupasa tujifunze namna ya kuutunza utulivu ndani ya nafsi zetu licha ya mahangaiko na misukosuko ya maisha. Tutenge muda katika siku yetu ambapo tunaweza kutulia na Kristu na kumsikiliza, na wala sio sisi kuongea nae tu bila kumsikiliza naye pia. Soma Neno la Mungu kwa utulivu na kwa tafakari, na uone kama kuna kitu gani Mungu anakuaombia leo. Lazima tusafishe macho ya nyoyo zetu, ili tuweze kumwona Mungu ndani mwetu. Tunafanya hivyo kwa njia ya toba na maungamo. Kusafishwa vizuri ni jambo linaloweza kuambatana na maumivu, lakini tunahitaji usafi wa nafsi ili tuweze kuwa wasikivu zaidi kwa sauti ya Mungu ndani mwetu.

Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino

(Angalia siku ya kwanza)

Tuombe: Ee Baba mwema, tunataka kumfuata Mwanao Yesu kwa ukaribu zaidi. Utuwezeshe kuumbika upya nawe kwa mfano wa Mtakatifu Augustino katika maisha yake ya utulivu. Utusaidie kuacha mambo ya dunia hii yanayopita ili tupate hamu kubwa zaidi ya kukufuata. Imarisha imani yetu ili tusikie sauti yako katika maandiko: ili tuweze kukuona Wewe katika matukio ya maisha yetu. Tunaomba haya kwa njia ya Kristu Bwana wetu, anayeishi na kutawala nawe na Roho Mtakatifu, Mungu mmoja milele na milele. Amina.

Baba yetu……, Salamu Maria….., Atukuzwe Baba……

Siku ya tatu – matendo-tafakari na matendo

Katika wito wetu uwao wote wa maisha yetu, tunaalikwa na Yesu tutafakari jinsi Martha alivyolalamika kuwa dada yake Maria alitumia muda wote katika kumsikiliza Yesu badala ya kusaidia kazi. Mt. Augustino akiwa kama mtawa aliuchukua mfano wa Martha na Maria kwa kushiriki kwa ukamilifu pia katika ujenzi wa uhai wa Kanisa kwa njia ya maandishi na kazi zake njema. Je mimi ninaoanishaje kati ya kutenda, kusali na tafakari takatifu?

Mt. Augustino anatufundisha kuwa tuwe tayari kuwatumikia wengine. Asiwepo mtu anayedhani kuwa anaweza kusali tu muda wote bila matendo, na wala asiwepo anayedhani atafaidika kwa matendo mengi yasiyosindikizwa na wingi wa sala. Tunapozigundua karama zetu Mungu alizotupa, tuwe tayari kuzishirikisha kwa wengine, kwani siku ya mwisho tutahukumiwa kwa namna ambavyo tuliwajali wengine. Kwa hiyo baada ya kumpata Mungu ndani mwako, usibaki humo, bali mgeukia yeye aliyekuumba. “Tupande mlimani lakini tusijenge vibanda, tushuke tuwatumikie wengine”

Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino

(Angalia siku ya kwanza)

Tuombe: Mungu Baba yetu, tunakutukuza na kukushukuru kwa kulijalia Kanisa lako mtakatifu mkuu namna hii. Tunapojitahidi kuishi roho na karama zake, utujalie neema za kukua katika utumishi wetu kwa wengine kwa njia ya matendo mema na pia katika maisha yetu ya sala, kwa mfano wa Mt. Augustino. Tunaomba hayo kwa Jina la Mwanao, Bwana na Mwokozi wetu. Amina.

Baba yetu……, Salamu Maria….., Atukuzwe Baba……

Siku ya nne – umaskini wa kiinjili – maisha ya kujitoa

Kwa Jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina.

Kuna wakati Mt. Augustino alikosa kitu chochote cha kuwapatia wasiojiweza, kwa sababu alikuwa anagawa kila alichoweza kwa wenye shida. Alipoishiwa kabisa, aliuza baadhi ya vitu alivyokuwa navyo ili kupata pesa iliyohitajika kwa ajili ya wenye shida.

Je, mimi pamoja na karama zote alizonijalia Mungu na vipaji vyote nilivyo navyo, ninajitahidi kuiga mfano wa Mt. Augustino katika kujitoa kwa wengine?

Umaskini wa kiinjili ni tofauti na umaskini wa kukosa mali au pesa. Ni namna moyo wa mtu anavyopenda kujitoa hata nje ya Jumuiya yake. Yesu Kristu alijitoa kabisa kwetu kwa kuuacha Umungu wake na kujitwalia ufukara wetu ili aweze kututajirisha. Hii ni changamoto kwetu kuwa tuwe tayari kujitoa kwa ajili ya wale wanaotuhitaji na Augustino ni mfano katika hilo. Tujitolee kufanya kazi za huruma, kwani mtu hataishi kwa mkate tu. Je tunawasaidiaje maskini walioko katika eneo letu? Ufalme wa Mungu utawafikiaje wengine kupitia kwetu. Mt Augustino anatupa changamoto leo kuwa tukubali kwa moyo mmoja kutoa vitu tulivyo navyo kwa ajili ya wengine, na tumfuate Kristu kwa moyo mpya na wa dhati.

Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino

(Angalia siku ya kwanza)

Tuombe: Tunakutukuza ee Bwana kwa kila unatupowezesha kushirikisha vile ulivyotujalia kwa ajili ya wahitaji, na kushikama katika upendo wako. Tunakuomba utujalie neema ya kudumu katika kushirikiana na kupendana ili tuwe mashahidi wa ukarimu wako mkuu. Tunaomba hayo kwa njia ya Bwana wetu Yesu Kristu, anayeishi na kutawala pamoja nawe na Roho Mtakatifu, Mungu mmoja daima na milele, Amina.

Baba yetu……, Salamu Maria….., Atukuzwe Baba……

Siku ya tano – urafiki katika jumuiya yetu

Kwa Jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina.

Mt. Augustino anashuhudia kuwa kitu kilichomweka karibu na marafiki zake kaka na dada zake ni kulekuongea na kucheka pamoja, kusaidiana, kusoma vitabu vinavyofanana vyenye mambo ya kujenga, kutaniana, kutofautiana mara kwa mara bila kukasirikiana, na alama za urafiki wetu zilijionyesha katika nyuso zetu, sauti zetu, macho yetu, na namna nyingi nyingine”. Je mimi nafurahia mahusiano yaliyoko katika Jumuiya yetu? Kuna jambo gani naweza kufanya ili kuboresha mahusiano na wanajumuiya wenzangu?

Ushahidi wa mapendo ya kweli unakuja pale tunapokuwa tayari kubebeana mizigo yetu. Tunapojitahidi kuboresha mambo yanayohusu Jumuiya, ukweli ni kuwa tunaboresha mambo yetu binafsi pia. Tumwombe Mungu ili tuweze kuona namna ambavyo Jumuiya yetu inatutegema katika hali na namna mbalimbali na tuweze kuboresha mahusiano ili kukuza urafiki kati yetu kama anavyotufundisha Kristu.

Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino

(Angalia siku ya kwanza)

Tuombe: Bwana Mungu wetu, ulimfunulia Mt. Augustino uzuri ulioko katika urafiki uliojengwa katika misingi yako. Utujalie sisi tunaosimamiwa naye hapa duniani, tukue katika urafiki mtakatifu wa kijumuiya. Utujalie tufikie ukamilifu wa urafiki huo katika makao yetu ya mbinguni unakoishi na kutawala daima na milele, Amina.

Baba yetu……, Salamu Maria….., Atukuzwe Baba……

Siku ya sita – augustino mfano wa unyenyekevu

Kwa Jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina.

Unyenyekevu unapatikana tu katika vita vya kiroho. Umuhimu wa majaribu katika maisha yako ya kiroho ni kuwa ni kwa kupitia tu majaribu hayo unajipatia unyenyekevu. Hapo ndio unauona umuhimu wa kumpokea yesu kuwa Mwokozi wako. Ukiwa na kiburi itakuwa ni kikwazo kikubwa kumpokea Mwokozi.

Kwa Augustino, unyenyekevu sio kujidharau, bali ni kujitahidi kufahamu karama alizotujalia Mungu na kuziendeleza. Ili kuwa mtu mnyenyekevu, jifahamu kuwa u mdhambi, na kuwa Mungu ndie anayeweza kukuweka huru. Fanya maungamo ya dhambi zako ili uwe wa kundi lake Mungu. Je, kama unyenyekevu ndio ukweli, ninajitahidije kuushirikisha ukweli huu kwa wengine katika Jumuiya yetu?

Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino

(Angalia siku ya kwanza)

Tuombe: Tuelekezee nyoyo zetu katika wema wako ee bwana, na geuza macho yetu mbali na kiburi na puuzi za dunia ili tuwe wafuasi wa maneno yako: Jifunzeni kwangu kwani mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo. Utujalie tukue kila siku katika unyenyekevu ambao unampendeza sana moyo wa Msimamizi wetu mt. Augustino. Amina.

Baba yetu……, Salamu Maria….., Atukuzwe Baba……

Siku ya saba – uangalizi wa imani yetu

Kwa Jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina.

Na tumpende Bwana wetu, tulipende kanisa lake. Tunampokea Roho Mtakatifu kadri tunavyolipenda Kanisa lake, kama tukiunganika pamoja kwa upendo, kama tukilifurahia jina katoliki na Imani yake. Tuamini kuwa tutakuwa na Roho Mtakatifu kwa kipimo cha upendo wetu kwa Kanisa lake. Tunalipenda Kanisa kama tulisimama imara katika ushirika na upendo.

Je ninalipenda Kanisa Katoliki? Ninajitahidi kujifunza imani hii na kuwashirikisha wengine au ninafuata mkumbo tu? Tunaalikwa kuishi kwa mfano wa Mt. Augustino ambaye alijielimisha kuhusu imani ya Kanisa Katoliki na kuikumbatia, kuitetea na kuishirikisha kwa wengine. Tusisite kujitoa katika dunia yetu ya leo pale tunapohitajika katika kueneza imani yetu. Tumwombe Mungu atujalie kwa mfano wa Mt. Augustino, moyo wa kusukumwa kuwashirikisha wengine imani iliyo hai kwa njia ya maneno, na matendo yetu, na hivyo kulitetea Kanisa la Bwana wetu Yesu Kristu kila wakati kwa injili iliyo hai.

Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino

(Angalia siku ya kwanza)

Tuombe: Baba mwenye upendo, tunakushukuru kwa zawadi ya Mt. Augustino uliyolipatia Kanisa lako. Kwa maombezi yake, sisi tunakuomba mwanga na ujasiri wa kujitoa bila masharti kwa unyenyekevu na daima katika huduma kwa wengine hasa wenye shida mbalimbali katika mahitaji ya mwili na ya roho. Tunaomba hayo, kwa njia ya Kristu Bwana wetu, Amina.

Baba yetu……, Salamu Maria….., Atukuzwe Baba……

Siku ya nane – utayari katika kulisaidia kanisa letu

Kwa Jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina.

Jumuiya ni kiini cha Kanisa la leo, kama ilivyokuwa wakati wa mitume, wakifundishwa na mitume. Kama Jumuiya za kwanza za wakristu, tunaalikwa nasi leo tuwe na utayari katika kulisaidia Kanisa letu kwa njia mbalimbali hasa kwa kutoa zaka kwa wakati. Wakati huohuo pia tuelewe kuwa Roho Mtakatifu anatupatia vipaji na karama kuendana na mahitaji ya Kanisa lake, na hivyo tusisahau kushirikisha karama na vipaji hivyo kanisani kwetu ili kuujenga mwili wa Kristu. Kwa njia hiyohiyo, kazi zetu za kitume ziendane na mahitaji ya Kanisa letu leo hii kwani yote tunapewa na Roho wa Mungu kwa ajili ya utumishi kwa wengine. Je, shughuli zetu kama Jumuiya zinaendana na mahitaji ya Kanisa la Mungu kwa wakati huu? Ni mabadiliko gani tunaitwa kuyafanya kama Jumuiya na kama mtu mmoja mmoja ili kuboresha Kanisa kupitia Jumuiya yetu?

Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino

(Angalia siku ya kwanza)

Tuombe: Baba mwema, tunakuheshimu na kukutukuza kwa kutupatia Mt. Augustino. Tukiwa tumejiweka chini ya mafundisho yake, tunaomba neema na maongozi yako ili tuweze daima kuwa na utayari wa kulisaidia Kanisa letu kwa njia ya zaka na majitoleo kadri ya mahitaji, na utujalie neema tunazokuomba kwa njia ya Yesu Kristu, Bwana na Mwokozi wetu. Amina.

Baba yetu……, Salamu Maria….., Atukuzwe Baba……

Siku ya tisa – utayari wa kuwasaidia wenzetu

Kwa Jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina.

Mt. Augustine daima alikuwa tayari kuwasaidia wahitaji. Alitoa kila alichoweza vikiwemo vile vitu alivyotengewa kwa ajili ya matumizi yake yeye mwenyewe, na alipokosa kitu zaidi cha kutoa, aliyeyusha baadhi ya vyombo vya dhahabu vilivyokuwa vimewekwa wakfu kwa ajili ya kuuza na kisha aliwagawia maskini pesa iliyopatikana. Nasi mara nyingine inawezekana hatuna pesa mfukoni za kuwapa wale wanaohitaji tuwasaidie, lakini bila shaka tuna vitu. Mazao ya mashambani, mifugo, na vitu aina mbalimbali alivyotujalia Mungu. Kwa hiyo kila mmoja wetu ana kitu anachoweza kumpa mwenzake, pengine kama sina chochote zaidi angalau nina muda wa kusali na kuwaombea wengine kuendana na mahitaji ya Jumuiya yetu, au kuwatembelea wapweke, wenye majonzi na kuwafariji wengine. Cha msingi ni kumtazama Kristu, ambaye ana njaa na anateseka, ndani ya wenzetu.

Tunafanya vyema kushikamana na maskini. Sio maskini wa mali na pesa tu tunazungumzia hapa, bali pia maskini wa kiroho, wale wanaohitaji kuelekezwa, wenye mashaka, wapweke, wagonjwa, na wanaoteseka na dhambi. Tumwombe Mungu ili tuimarike kiroho, maana tutaweza kuwasaidia hao maskini tu pale ambapo sisi wenyewe tuna utajiri wa kiroho, yaani tunaye Kristu ndani mwetu.

Tunapomalizia Novena yetu ya siku tisa, tutafakari kuwa, kama Mt. Augustino angekuwa hai leo, angewajibika namna gani, angewasaidiaje maskini walioko katika Jumuiya yetu, mahali petu pa kazi na hata katika familia zetu?

Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino

(Angalia siku ya kwanza)

Tuombe: Bwana, tunakuomba urejeshe upya katika Kanisa lako roho kama ile uliyompa Mt. Augustino. Kwa mfano wake, tujazwe na kiu ya kukupata wewe peke yako kama chemchem ya hekima na chanzo cha upendo wa milele ili tuwe na utayari wa kuwasaidia wenzetu wote wenye shida za aina mbalimbali. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristu Bwana wetu. Amina.

Baba yetu……, Salamu Maria….., Atukuzwe Baba……

SALA KWA MTAKATIFU YUDA TADEI

Mtakatifu Yuda Tadei,/ Mtume Mtakatifu,/ mtumishi mwaminifu na rafiki wa Yesu./ Jina la yule msaliti aliyemwuza Yesu/ limewafanya wengi wakusahau./ Walakini Kanisa zima linakuheshimu/ na kukuomba kama Msaidizi katika mashaka makubwa,/ na katika mambo yasiyo na matumaini tena./

Uniombee mimi mnyonge./ Ninaomba utumie uwezo ule uliojaliwa/ wa kuleta upesi msaada kwa watu walioukosa./ Unisaidie sasa katika mahitaji yangu,/ ili nipate kitulizo na msaada wa mbinguni/ katika lazima zangu,/ masumbuko na mateso,/ hasa/ (taja shida yako)./ Pia ili niweze kumsifu Mungu nawe na wateule wote milele./

Mtakatifu Yuda Tadei,/ utuombee,/ na uwaombee watu wote wanaokuheshimu na kukuomba msaada./

Moyo Mtakatifu wa Yesu,/ Rafiki mpenzi wa Yuda Tadei,/ nakutumainia./

(Mwisho Sali: Baba yetu (x3), Salamu Maria (x3) na Atukuzwe(x3).

SALA YA KUUABUDU MOYO MTAKATIFU WA YESU KATIKA EKARISTI TAKATIFU

Kwa nguvu zangu zote za moyo wangu/ ninakuabudu ee Moyo Mtakatifu/ na Mwabudiwa sana,/ Moyo Mtakatifu wa Bwana wetu Yesu Kristu/ ambao ninataka kumpenda/ na kukusalimu kwa usikivu unaoendelea./ Kamwe nisikuudhi tena/ kwa sababu Wewe ni Mwema sana;/ Ee Mwema sana./ Ee Moyo Mtakatifu sana/ ninakupenda/ na ninataka kukupenda zaidi ya vitu vyote,/ kwa nguvu zangu zote/ na kwa uwezo wangu wote,/ ninatamani kuwa mali yako/ Wewe uliyejitoa Msalabani kwa ajili yangu/ kwa mateso makali./ Unionee huruma na udhaifu wangu/ na usiniruhusu kupotea./

Ninajitoa kabisa kwako/ ee moyo wa mapendo,/ kwa makusudi kuwa utu wangu,/ maisha na mateso yangu/ yalipie kukupenda,/ kukuheshimu/ na kukutukuza Wewe sasa na milele./ Ninakupenda ee Moyo Mwabudiwa wa Mwokozi wangu,/ ninakuomba kwako/ uamuru moyo wangu na kila kitu ndani yangu/ kikutukuze sasa na milele./ Amina.

(Na Mt Margareta Maria Alakoki)

SALA YA MAOMBI KWA MOYO MTAKATIFU WA YESU

Ee Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakukimbilia, ninakuja kwako katika mikono yako yenye huruma. Ndiwe tegemeo langu na tumaini langu dhabiti. Ndiwe mwenye dawa ya maovu yangu yote, malipizi ya makosa yangu yote. Waweza kunipatia haja zangu na neema ninazoziomba mimi na wengine. Wewe uko ili kutusaidia sote, ndiwe mwanga mkuu usiozimika, ndiwe chanzo cha nguvu, uvumilivu, amani na faraja. Nina hakika kuwa maombi yangu hayatakuchosha, nawe hutaacha kunisaidia, kunilinda, kunipenda, kwani, ee Moyo Mtakatifu , upendo wako hauna mwisho. Ee Moyo Mtakatifu, unihurumie, kwa ajili ya maombi yangu, kadiri ya huruma yako. Nawe katika sisi, na kwa ajili yetu, ufanye lolote unalolihitaji, kwani tunajitoa kwako kwa imani na uhakika thabiti kwamba kamwe hautatuacha, kwa milele. Amina.

SALA KWA MT. YOSEFU KWA WASIO NA AJIRA WAPATE AJIRA

Ee Mt. Yosefu, tunakuomba kwa ajili ya wale asio na ajira, kwa ajili ya wale wanaotaka kujipatia kipato chao na kulisha familia zao.
Wewe u Msimamizi wa wafanyakazi, tujalie kwamba pasiwepo kati yetu mtu asiye na ajira, na kwamba wale wote ambao wako tayari kufanya kazi waweze kuelekeza nguvu zao na uwezo wao katika kuwatumikia wanadamu wenzao na kujipatia kipato halali.

Wewe u Msimamizi wa familia, usiwaache wale wenye watoto wa kuwatunza na kuwalea wakose namna ya kufanya hivyo. Uwahurumie ndugu zetu waliokosa ajira na kugubikwa na umasikini kwa sababu ya magonjwa au mipango mibaya ya kijamii. Wasaidie viongozi wetu wa kisiasa na walioshika usukani katika nyanja mbalimbali za kiuzalishaji wavumbue suluhu mpya na za haki za jambo hili. Utujalie ili kila mmoja wetu apate kujipatia kipato halali na kufurahia fursa ya kushiriki kadri ya uwezo wake, katika maisha bora zaidi kwa wote. Utujalie ili wote tushiriki pamoja katika raslimali alizotujalia Mungu, na pia utujalie tuwe tayari daima kuwasaidia wale walio wahitaji kuliko sisi.
Amina.

SALA YA UHAI KWA MT. YOSEFU

(Sala hii inafaa sana kwa ajili ya kutetea uhai wa watoto wachanga wakiwa tumboni mwa mama zao, dhidi ya utoaji mimba au hatari nyingine dhidi ya uhai wa binadamu)

Ee Mt. Yosefu, wewe ni Mchumba safi na Mpenzi wa Bikira Maria, u Baba Mlishi wa Yesu, mlinzi na mtunzaji wa Familia Takatifu, na wa familia zote. Tuna imani kabisa katika uangalizi wako uliojaa upendo, juu ya uhai mpya, na uaminifu wako kwa familia.

Tunaweka jitihada zetu chini ya ulinzi wa sala zako. Utusaidie daima katika kutetea zawadi ya uhai wa binadamu, ili ukue hadi uzima wa milele ulioahidiwa na kujaliwa kwetu na Mwanao, Ndugu yetu, Yesu Kristu.
Amina.

Sala ya Kuombea Hali njema ya hewa na mvua

Ee Mungu Mwenyezi wa milele, mpaji wa mema yote, unayetusamehe na kutulinda. Utujalie sisi tunaokusihi, tufurahie hali njema ya hewa na mvua tunayoitamani na kuhitaji. Tutumie daima vipawa vya wema wako kwa ajili ya utukufu wa jina lako, na kwa ajili ya wokovu watu. Tunaomba hayo kwa njia ya Bwana watu Yesu Kristo Mwanao, anayeishi na kutawala nawe katika umoja wa Roho Mtakatifu, Mungu, daima na milele. Amina. `

`Baba Yetu………………. Salama Maria………… Atukuzwe Baba……….. `

K: `Bikra Maria mama wa msaada wa daima…. W: Utuombee na Utusaidie`

Sala fupi ya Asubuhi

Tuusifu Utatu Mtakatifu wa Mungu Mwenyezi, Baba, Mwana na Roho Mtakatifu, milele na milele, Amina.

Ee Utatu Mtakatifu wa Mwenyezi Mungu, Baba, Mwana na Roho Mtakatifu, nasadiki kuwa upo hapa na mahali pote. Ee Mungu wangu, umeniumba, umenikomboa, umenifanya mkristo, umenizidishia neema zako hapa duniani, umenitayarishia makao yangu mbinguni, umenijalia na siku hii nikutumikie. Ee Mungu wangu! Nakuabudu, nakushukuru, nakuomba toba, nakupenda! Ee Mungu wangu, nakutolea roho yangu, na mawazo, na maneno, na kazi, na furaha, na mateso yangu: uyapokee unipe neema yako nisikutende leo dhambi!

SALA YA KUMWOMBA MT. YOSEFU MSAADA (SALA KUU KWA MTAKATIFU YOSEFU)

Ee Mt. Yosefu mwenye heri, tunakimbilia kwako katika masumbuko yetu, na kisha omba shime ya Mchumba wako Mtakatifu, tunaomba pia kwa matumaini usimamizi wako. Kwa ajili ya mapendo uliyompenda Bikira Mtakatifu Mzazi wa Mungu, na kwa ajili ya kumtunza Mtoto Yesu, twakuomba sana, utuangalie kwa wema sie tuliokuwa fungu lake Yesu Kristu, tukakombolewa kwa damu yake. Tusimamie katika masumbuko yetu kwa enzi na shime yako.

Ee Mlinzi amini wa jamaa takatifu, uwakinge watoto wateule wa Yesu Kristu.
Ee Baba uliyetupenda mno tuepushe na kilema chochote cha madanganyo na upotevu. Ee kinga yetu mwezaji, utusimamie huko juu mbinguni ulipo, tunaposhindana na wenye nguvu wakaao gizani. Kama vile siku za kale ukamwopoa Mtoto Yesu katika hatari ya kuuawa, na leo hivi likinge Kanisa Takatifu la Mungu katika mitego ya adui, na katika shida yote; mtunze daima kila mmoja wetu, tufwate mfano wako, ili tupate na msaada wako, kukaa na utakatifu maisha, kufa kifo chema, na kupata mbinguni makao ya raha milele.
Amina.

Malkia wa Mbingu

Malkia wa mbingu, furahi, aleluya. Kwani uliyestahili kumchukua, Aleluya. Amefufuka alivyosema, Aleluya. Utuombee kwa Mungu, Aleluya. Furahi shangilia, ee Bikira Maria, Alaluya. Kwani hakika Bwana amefufuka Aleluya. Tuombe. Ee Mungu, uliyependa kuifurahisha dunia kwa kufufuka kwake Bwana wetu Yesu Kristu, Mwanao: fanyiza, twakuomba, kwa ajili ya Bikira Maria, tupate nasi furaha za uzima wa milele. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristu Bwana wetu. Amina.

SALA YA KUWAOMBEA MAPADRE

Ee Bwana Yesu Kristo. Mkombozi wetu, kwa mapendo na tamaa yako ya kutaka kulinda vema Kanisa lako, ukachagua Mapadri wawe Wachungaji na Viongozi wa roho za watu. Nakuomba sana; ubariki nia na bidii inayowapasa Mapadri wote katika kazi zao. Uwaongezee Utakatifu.

Uwatie moyo mzuri wenye mapendo makubwa kwako na roho za watu. Hivyo wakiisha kupata wenyewe Utakatifu, waweze kuwaongoza vizuri watu walio chini ya ulinzi wao, katika njia ya Utakatifu na furaha ya milele. Uwajalie neema zote za hali ya Upadri. Uwajalie ili waonyeshe kila siku ya maisha yao mfano wa kila fadhila ya mapendo na ya uaminifu katika Kanisa, kwa Baba Mtakatifu na kwa Maaskofu.

Yesu mpendelevu, uangalie kwa mapendo kazi na mateso ya Mapadri wako; ubariki na ustawishe mafundisho yao; wanapowafundisha watoto, wanapowahubiria watu, wanapowatuliza wakosefu watubu na wanapowasaidia wagonjwa na wale wanaokaribia mauti, Ee Yesu uwe pamoja nao. Uwakinge na hatari zote za roho na za mwili.

Mwokozi Yesu, ulijalie Kanisa liwe na Mapadri wengi walio Watakatifu. Uwajalie watoto na vijana wengi wasikie wito wa Upadri, uwatie furaha na Utakatifu na roho za Mapadri waliokufa uzijalie punziko la amani.

Kwa mimi mwenyewe Ee Yesu mpendelevu, naomba unijalie roho ya imani na utii mnyenyekevu ili niwaheshimu Mapadri kama Mawakili wa Mungu. Niwatii katika njia zote za wokovu wa roho yangu. Amina.

Shopping Cart
🏠 Home 📖 Reading 🖼️ Gallery 💬 AI Chat 📘 About