Sala za Maombi

SALA YA KUWAOMBEA MAPADRE

Ee Bwana Yesu Kristo. Mkombozi wetu, kwa mapendo na tamaa yako ya kutaka kulinda vema Kanisa lako, ukachagua Mapadri wawe Wachungaji na Viongozi wa roho za watu. Nakuomba sana; ubariki nia na bidii inayowapasa Mapadri wote katika kazi zao. Uwaongezee Utakatifu.

Uwatie moyo mzuri wenye mapendo makubwa kwako na roho za watu. Hivyo wakiisha kupata wenyewe Utakatifu, waweze kuwaongoza vizuri watu walio chini ya ulinzi wao, katika njia ya Utakatifu na furaha ya milele. Uwajalie neema zote za hali ya Upadri. Uwajalie ili waonyeshe kila siku ya maisha yao mfano wa kila fadhila ya mapendo na ya uaminifu katika Kanisa, kwa Baba Mtakatifu na kwa Maaskofu.

Yesu mpendelevu, uangalie kwa mapendo kazi na mateso ya Mapadri wako; ubariki na ustawishe mafundisho yao; wanapowafundisha watoto, wanapowahubiria watu, wanapowatuliza wakosefu watubu na wanapowasaidia wagonjwa na wale wanaokaribia mauti, Ee Yesu uwe pamoja nao. Uwakinge na hatari zote za roho na za mwili.

Mwokozi Yesu, ulijalie Kanisa liwe na Mapadri wengi walio Watakatifu. Uwajalie watoto na vijana wengi wasikie wito wa Upadri, uwatie furaha na Utakatifu na roho za Mapadri waliokufa uzijalie punziko la amani.

Kwa mimi mwenyewe Ee Yesu mpendelevu, naomba unijalie roho ya imani na utii mnyenyekevu ili niwaheshimu Mapadri kama Mawakili wa Mungu. Niwatii katika njia zote za wokovu wa roho yangu. Amina.

SALA YA KUMWABUDU BWANA YESU KATIKA SAKRAMENTI TAKATIFU

Ee Yesu Kristu,/ Bwana wangu na Mungu wangu/ ambaye ninasadiki kuwa upo hapa/ katika Sakramenti Takatifu ya Altare;/ pokea kitendo hiki cha kukuangukia kifudi fudi/ kama ishara ya tamaa niliyonayo ya kukuabudu Wewe/ bila kuchoka/ na kukushukuru kwa mapendo yako makubwa/ yasiyo na kipimo/ ambayo Moyo wako Mtakatifu sana/ unawaka katika Sakramenti Takatifu hii./ Siwezi kukushukuru vizuri zaidi/ kuliko kama ningetolea kwako/ matendo yangu yote ya kukuabudu/ unyenyekevu wangu/ uvumilivu na mapendo/ ambayo huu Moyo Mwabudiwa ulifanya,/ bado unafanya/ na utaendelea kufanya katika uzima wa milele mbinguni./ Ninaahidi kupitia Moyo huu,/ nitakupenda,/ nitakutukuza,/ na nitakuabudu kama nitakavyoweza./ Ninajiunganisha na hii Sadaka Takatifu/ ambayo unatoa kwa Baba Mungu/ na ninatolea kwako utu wangu./ Ninakuomba kuangamiza ndani yangu/ dhambi zote pamoja na majeraha yake/ na usikubali kunitenga nawe milele./ Amina.

(Na Mt. Margareta Maria Alakoki)

Majitoleo kwa Bikira Maria

(Sala iliyotungwa na Mtk. Aloisi)
Bibi yangu mtukufu Maria, nakuwekea amana ya roho yangu na mwili wangu, nikikuomba uipokee amana yangu, kuitunzia ulinzi mwema ulinzi bora, ninakuaminia na kila neno langu, matumaini na kitulizo na kisongo chote, na masumbuko na uzima na ukomo wa uzima wangu: nitakayo ndiyo unifanyizie kwa maombezi na stahili zako, ili mambo yangu yote yapate kuongoka, yakiwa na kufuata mapenzi yako, pamoja na mapenzi ya Mwanao. Amina.

Sala ya Kuombea Hali njema ya hewa na mvua

Ee Mungu Mwenyezi wa milele, mpaji wa mema yote, unayetusamehe na kutulinda. Utujalie sisi tunaokusihi, tufurahie hali njema ya hewa na mvua tunayoitamani na kuhitaji. Tutumie daima vipawa vya wema wako kwa ajili ya utukufu wa jina lako, na kwa ajili ya wokovu watu. Tunaomba hayo kwa njia ya Bwana watu Yesu Kristo Mwanao, anayeishi na kutawala nawe katika umoja wa Roho Mtakatifu, Mungu, daima na milele. Amina. `

`Baba Yetu………………. Salama Maria………… Atukuzwe Baba……….. `

K: `Bikra Maria mama wa msaada wa daima…. W: Utuombee na Utusaidie`

Kanuni ya imani

Nasadiki kwa Mungu, Baba Mwenyezi,/ mwumba mbingu na dunia./ Na kwa Yesu Kristu, Mwanaye wa pekee, Bwana wetu;/ aliyetungwa kwa Roho Mtakatifu,/ akazaliwa na Bikira Maria,/ akateswa kwa mamlaka ya Ponsyo Pilato,/ akasulubiwa, akafa, akazikwa,/ akashukia kuzimu;/ siku ya tatu akafufuka katika wafu;/ akapaa mbinguni;/ amekaa kuume kwa Mungu Baba Mwenyezi;/ toka huko atakuja kuwahukumu wazima na wafu. Nasadiki kwa Roho Mtakatifu,/ Kanisa takatifu katoliki,/ ushirika wa Watakatifu,/ maondoleo ya dhambi,/ ufufuko wa miili,/ uzima wa milele. Amina.

SALA YA KUMWOMBA MTAKATIFU TERESIA WA MTOTO YESU

Ee Mtakatifu Teresia wa mtoto Yesu, ulistahili kuitwa Msimamizi wa misioni katoliki za dunia yote. Kumbuka ile tamaa yako kuu uliyoonyesha huku duniani ya ” kusimika Msalaba wa Yesu Kristu, katika nchi zote na kuhubiri Injili mpaka mwisho wa dunia” . Twakuomba kwa ajili ya maagano yako, wasaidie mapadre, wamisionari, na kanisa zima.

Ee Mtakatifu Teresia wa mtoto Yesu ” Msimamizi wa misioni” UTUOMBEE

Novena ya Noeli

Novena ya Noeli (maarufu kama novena ya Mt. Andrea)

Husaliwa kuanzia tar 30 Nov hadi usiku wa Noeli, tar 24 Disemba. Inajulikana kama novena ya Mt. Andrea kwa sababu novena hii huanza kusaliwa katika siku ya kumbukumbu ya Mt. Andrea Mtume.

“IHESHIMIWE, NA IBARIKIWE, SAA ILE NA WAKATI ULE, AMBAO MWANA WA MUNGU, ALIZALIWA NA BIKIRA MBARIKIWA SANA, USIKU WA MANANE, KULE BETHLEHEM, WAKATI WA BARIDI KALI.
WAKATI HUO, UPENDE E MUNGU WANGU, KUSIKIA MAOMBI YANGU, NA KUNIJALIA YALE NINAYOYAOMBA KWAKO, KWA NJIA YA MASTAHILI YA MWOKOZI WETU YESU KRISTO, NA YA MAMA YAKE MBARIKIWA. AMINA. (Sali mara 15 kwa siku).

Inasadikika kuwa chochote uombacho kwa imani kwa sala hii utakipata mradi kipatane na mapenzi ya Mungu. Sali na watoto/ familia kuwatafakarisha na kuwaongezea matazamio juu ya sikukuu ya Noeli.

Isambaze sala hii kwa wengine.

SALA KWA MT. YOSEFU KWA WASIO NA AJIRA WAPATE AJIRA

Ee Mt. Yosefu, tunakuomba kwa ajili ya wale asio na ajira, kwa ajili ya wale wanaotaka kujipatia kipato chao na kulisha familia zao.
Wewe u Msimamizi wa wafanyakazi, tujalie kwamba pasiwepo kati yetu mtu asiye na ajira, na kwamba wale wote ambao wako tayari kufanya kazi waweze kuelekeza nguvu zao na uwezo wao katika kuwatumikia wanadamu wenzao na kujipatia kipato halali.

Wewe u Msimamizi wa familia, usiwaache wale wenye watoto wa kuwatunza na kuwalea wakose namna ya kufanya hivyo. Uwahurumie ndugu zetu waliokosa ajira na kugubikwa na umasikini kwa sababu ya magonjwa au mipango mibaya ya kijamii. Wasaidie viongozi wetu wa kisiasa na walioshika usukani katika nyanja mbalimbali za kiuzalishaji wavumbue suluhu mpya na za haki za jambo hili. Utujalie ili kila mmoja wetu apate kujipatia kipato halali na kufurahia fursa ya kushiriki kadri ya uwezo wake, katika maisha bora zaidi kwa wote. Utujalie ili wote tushiriki pamoja katika raslimali alizotujalia Mungu, na pia utujalie tuwe tayari daima kuwasaidia wale walio wahitaji kuliko sisi.
Amina.

SALA YA KUMWOMBA MT. YOSEFU MSAADA (SALA KUU KWA MTAKATIFU YOSEFU)

Ee Mt. Yosefu mwenye heri, tunakimbilia kwako katika masumbuko yetu, na kisha omba shime ya Mchumba wako Mtakatifu, tunaomba pia kwa matumaini usimamizi wako. Kwa ajili ya mapendo uliyompenda Bikira Mtakatifu Mzazi wa Mungu, na kwa ajili ya kumtunza Mtoto Yesu, twakuomba sana, utuangalie kwa wema sie tuliokuwa fungu lake Yesu Kristu, tukakombolewa kwa damu yake. Tusimamie katika masumbuko yetu kwa enzi na shime yako.

Ee Mlinzi amini wa jamaa takatifu, uwakinge watoto wateule wa Yesu Kristu.
Ee Baba uliyetupenda mno tuepushe na kilema chochote cha madanganyo na upotevu. Ee kinga yetu mwezaji, utusimamie huko juu mbinguni ulipo, tunaposhindana na wenye nguvu wakaao gizani. Kama vile siku za kale ukamwopoa Mtoto Yesu katika hatari ya kuuawa, na leo hivi likinge Kanisa Takatifu la Mungu katika mitego ya adui, na katika shida yote; mtunze daima kila mmoja wetu, tufwate mfano wako, ili tupate na msaada wako, kukaa na utakatifu maisha, kufa kifo chema, na kupata mbinguni makao ya raha milele.
Amina.

SALA YA MTU ALIYEKABILIWA NA MATATIZO MBALIMBALI

Ewe Mtakatifu Yuda Tadei,/ mtume mtukufu na shahidi wa Kristo,/ umesifika pote kwa wepesi wako wa kutoa misaada/ kwa wanaokukimbilia katika matatizo yao mazito./ Pia ni mwombezi wa waliopondeka moyo./

Mimi ni mmoja wa hao./ Nakujia na moyo uliojaa shida na matatizo./ Nakusihi kwa moyo wote/ unisaidie kwa maombezi yako yenye nguvu/ kufikia utatuzi unaofaa kadiri ya mapenzi ya Mungu./ Maisha yangu yamejaa misalaba,/ siku kwa siku matatizo hayapungui./ Moyo wangu umekuwa bahari ya siki chungu sana./ Mapito yangu nayaona yamejaa miiba mikali./ Roho yangu imezama katika dimbwi la machozi na kite./ Nafsi yangu imezingirwa na giza nene./ Ghasia na kukatishwa tamaa ya kuishi/ hunyemelea roho yangu./ Maongozi ya Mungu na imani naviona vinanitoka kidogo kwa kidogo./

Nikielemewa na mawazo kama hayo/ najikuta sina nguvu za kuishi,/ na maisha kwangu ni msalaba mzito/ ninaouogopa hata kuunyakua./ Wewe unaweza kabisa kunitoa katika balaa hili./ Sitaacha kukusihi/ hadi hapo utakaponisaidia/ au kunijulisha mapenzi ya Mungu kwangu./ Natangulia kutoa shukrani kwa jibu liwalo lote.

SALA YA NOVENA KWA MOYO MTAKATIFU WA YESU

Ee Moyo Mtakatifu sana wa Yesu, chemchemi ya kila baraka, ninakuabudu, ninakupenda, na kwa majuto halisi ya dhambi zangu, nakutolea moyo wangu dhaifu. Nifanye mnyenyekevu, mvumilivu na safi, nikikubali na kuyatii kabisa mapenzi yako. Ee Yesu mwema, unijalie niishi nawe na kwa ajili yako. Unilinde niwapo katikati ya hatari, unifariji katika mateso, unipe afya ya mwili na msaada katika mahitaji ya mwili, Baraka yako juu ya kila nilifanyalo, na neema ya kifo chema. Amina.

Ee Yesu uliyesema “Kweli nawaambieni, ombeni nanyi mtapewa, tafuteni nanyi mtapata, gongeni nanyi mtafunguliwa”, tazama ninagonga, ninatafuta na kuomba …….. (Taja ombi lako)
Baba Yetu….., Salamu Maria …….., Atukuzwe Baba……..
Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutumainia kwa moyo wote!

Ee Yesu uliyesema “Kweli nawaambieni, chochote mtakachomwomba Baba kwa jina langu mtapewa”, tazama kwa jina lako ninaomba ……. (Taja ombi lako)
Baba Yetu….., Salamu Maria …….., Atukuzwe Baba……..
Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutumainia kwa moyo wote!

Ee Yesu uliyesema “Kweli nawaambieni, mbingu na dunia zitapita lakini maneno yangu hayatapita kamwe”, tazama, nikitiwa nguvu na maneno yako ya kweli ninaomba …….. (Taja ombi lako)
Baba Yetu….., Salamu Maria …….., Atukuzwe Baba……..
Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutumainia kwa moyo wote!

Ee Moyo Mtakatifu wa Yesu, ambaye kwako ni kitu kimoja tu kisichowezekana, ambacho ni kutoacha kutowaonea huruma wenye huzuni, utuhurumie sisi wakosefu maskini na utujalie neema tukuombayo kwa njia ya Moyo Imakulata wa Maria, Mama yetu mpole.

Sali ‘Salamu Malkia’ na kuongezea, ‘Mtakatifu Yosefu Baba Mlishi wa Yesu, utuombee’.

P.S. – Sala hii ya Novena ilisaliwa kila siku na PADRE PIO kwa ajili ya kuwaombea wale wote waliomwomba msaada wa sala zake. Unaweza kuisali kwa namna tofauti tofauti. Mfano, kama Novena ya siku tisa, ambapo unasali sala hii mara moja au zaidi kila siku kwa siku tisa, au unaweza kuifanya kama Novena ya masaa, ambapo unasali sala hii kila baada ya saa moja kwa masaa tisa kwa siku hiyo hiyo, hasa kama kitu unachokiomba ni cha haraka au umesongwa moyoni. Vilevile unaweza kuifanya sala hii kama sehemu ya sala zako za kila siku katika mwezi Juni ambao ni mwezi uliotengwa na Kanisa kwa ajili ya kuuheshimu Moyo Mtakatifu wa Yesu, na hapo utaitumia kuwaombea watu waliokuomba msaada wa sala zako kama alivyofanya Mtakatifu Padre Pio. Pia unaweza kuitumia kama sala yako ya siku zote au ya mara kwa mara kwa ajili ya mahitaji mbalimbali.

SALA MBELE YA SAKRAMENTI KUU I

Utukuzwe ee Bwana wangu Yesu Kristo./ Uliagua kifo chako./ Katika karamu ya mwisho ulitumia mkate wa kidunia/ ukafanya mwujiza na kuugeuza/ kuwa Mwili wako azizi./ Kwa mapendo ukawapa Mitume Mwili huo/ uwe kumbukumbu la mateso yako mastahivu./ Uliwaosha miguu kwa Mikono yako Mitakatifu./

Uheshimiwe, ee Bwana wangu Yesu Kristo./ Kwa kuhofu mateso na kifo,/ Mwili wako usio na kosa ulitoka jasho la damu/ badala ya maji./ Juu ya hayo uliutimiza wokovu wetu/ uliokuwa umetaka kuufanya./ Hivyo ulionyesha waziwazi mapendo yako/ uliyo nayo kwa wanadamu./

Utukuzwe, ee Bwana wangu Yesu Kristo./ Ulipelekwa kwa Kayafa,/ Wewe uliye Hakimu wa wote./ Ukaruhusu kwa unyenyekevu kutolewa kwa Pilato/ uhukumiwe naye./

Utukufu uwe nawe, Bwana wangu Yesu Kristo,/ kwa kuwa ulivumilia kuchekwa tena/ uliposimama huko,/ umevaa joho jekundu,/ umetiwa taji ya miiba mikali sana Kichwani,/ ukavumilia kwa saburi kubwa/ kutemewa mate katika Uso wako mzuri,/ kufumbwa Macho,/ na kupigwa mno na wajeuri/ ngumi na makofi Mashavuni na Shingoni./

Sifa iwe nawe, Bwana wangu Yesu Kristo,/ Kwa uvumilivu mkubwa ulikubali kufungwa nguzoni,/ kupigwa mijeledi kijeuri,/ kujaa damu na hivyo kusukumwa barazani kwa Pilato./ Ulionekana kama mwanakondoo asiye na kosa./

Heshima iwe nawe, Bwana wangu Yesu Kristo./ Umehukumiwa Mwili wako mzima/ Mtukufu wenye kutoka damu/ ufe msalabani./ Ulichukua msalaba kwa Mabega yako Matakatifu/ na kuumwa sana./ Kwa ghadhabu walikusukuma mbele/ mpaka mahali pa mateso,/ wakakunyang’anya nguo zako./ Hivyo ulikubali kupigiliwa msalabani./

Heshima ya milele upate Wewe,/ Bwana wangu Yesu Kristo./ Ulipokuwa katika taabu kubwa hii,/ ulimkazia Mama yako mstahivu/ Macho yako ya hisani na mapendo/ na unyenyekevu,/ ndiye Mama yako asiyekosa hata mara moja/ wala kukubali dhambi yeyote./ Ulimweka katika ulinzi mwaminifu/ wa Mfuasi wako ili kumtuliza./

Milele utukuzwe, ee Bwana wangu Yesu Kristo./ Ulipokuwa mwenyewe taabani,/ uliwapa wakosefu wote/ matumaini ya kuondolewa dhambi/ kwa kumwahidia mnyang’anyi aliyekuendea/ utukufu wa paradisi kwa huruma yako./

Sifa ya milele iwe nawe, Bwana wangu Yesu Kristo,/ kwa kila saa ulipovumilia uchungu/ na taabu kubwa mno msalabani kwa ajili yetu sisi wakosefu,/ maumivu makali sana/ yaliyotoka katika majeraha yako,/ yakapenya bila huruma Roho yako Takatifu./ Yakaingia kikatili katika Moyo wako Mtakatifu/ hata ukakatika,/ ukapumua Roho yako,/ ukainama Kichwa,/ ukaweka Roho yako mikononi mwa Mungu, Baba yako./ Na baada ya kufa uliacha nyuma Mwili baridi./

Utukuzwe, ee Bwana wangu Yesu Kristo,/ kwa Damu yako azizi na kwa kifo chako kitakatifu/ ulizifidia roho za watu,/ ukazitoa ugenini/ na kuzipeleka kwa hisani yako katika uzima wa milele./

Milele uheshimiwe, Wewe Bwana wangu Yesu Kristo./ Siku ya tatu ulifufuka katika wafu,/ ukajionyesha kwa wafuasi wako,/ ukapaa mbinguni/ mbele ya macho yao siku ya arobaini./

Shangilio na sifa ya milele upate Wewe, Bwana wangu Yesu Kristo,/ kwa kuwa umewapelekea wafuasi wako mioyoni mwao/ Roho Mtakatifu,/ ukawasha rohoni mwao mapendo makuu ya Mungu./

Pia, utukuzwe, usifiwe na kushangiliwa milele, Bwana wangu Yesu Kristo./ Umekaa katika ufalme wako wa mbinguni/ juu ya kiti cha enzi cha Umungu wako,/ ukaishi pamoja na Viungo vyako vyote Vitakatifu./ Na hivyo utakuja tena/ kuzihukumu roho za wazima na wafu wote./ Unaishi na kutawala/ pamoja na Baba na Roho Mtakatifu,/ milele. Amina.

(Na Mt. Birgita wa Sweden)

SALA YA MAJITOLEO KWA MAMA WA HUZUNI

Mama Mtakatifu, Mama wa Mungu na Malkia wa Mashahidi, leo nakuchagua Wewe uwe mfano wangu, mkingaji na mteteaji wangu. Naweka roho fukara katika moyo wako uliotobolewa na panga nyingi za mateso. Unipokee mimi niwe mtumishi wako wa pekee na mshiriki wa mateso yako. Nijalie nguvu niwe daima karibu na msalaba ule alikosulibiwa Yesu. Nakutolea nafsi yangu na mali yangu yote. Pokea kila tendo langu jema ukalisindikize kwa Mwanao, Mama, nifanye nistahili kuitwa mtumishi wa Maria, Simama karibu yangu katika matendo yangu yote ili yafanwe kwa sifa ya Mungu. Ulivyosimama karibu kabisa ya Mwanao alipokufa msalabani uwe karibu nami saa ya kufa kwangu. Nijalie niweze kutaja jina lako na la Mwana wako nikisema: “Yesu, Maria na Yosef mnisaidie saa ya kufa kwangu. Yesu, maria na Yosef, naomba nife kwa amani kati yenu!” . Amina.

Shopping Cart
1
    1
    Your Cart
    🏠 Home 📖 Reading 🖼️ Gallery 💬 AI Chat 📘 About