Sala za Katoliki: Sala Muhimu Kwa Mkristu Mkatoliki
Sala ya Baba Yetu: Sala ya Bwana
Baba Yetu uliye mbinguni,
jina lako litukuzwe;
ufalme wako ufike,
utakalo lifanyike
duniani kama mbinguni.
Utupe leo mkate wetu wa kila siku,
utusamehe makosa yetu,
kama tunavyowasamehe na sisi waliotukosea.
Usitutie katika kishawishi,
lakini utuopoe maovuni.
Amina
Matendo ya Rozari Takatifu: Mchanganuo kwa siku zote za Saba za Juma
MATENDO YA FURAHA (Jumatatu na Jumamosi)
- Tendo la kwanza; Malaika Gabrieli anampasha habari Maria kuwa atakuwa Mama wa Mungu. Tumwombe Mungu atujalie unyenyekevu.
- Tendo la pili; Maria Mtakatifu anakwenda kumtembelea Elizabeti. Tumwombe Mungu atujalie mapendo ya jirani.
- Tendo la tatu; Yesu anazaliwa Betlehemu. Tumwombe Mungu atujalie moyo wa ufukara
- Tendo la nne; Yesu anatolewa hekaluni. Tumwombe Mungu atujalie usafi wa moyo.
- Tendo la tano; Maria anamkuta Yesu hekaluni. Tumwombe Mungu atujalie kuwatii wakubwa wetu.
MATENDO YA UCHUNGU (Jumanne na Ijumaa)
- Tendo la kwanza; Yesu anatoka jasho la damu kwa ajili yetu. Tumwombe Mungu atujalie sikitiko la dhambi.
- Tendo la pili; Yesu anapigwa kwa mijeledi kwa ajili yetu. Tumwombe Mungu atujalie kuacha dhambi za uchafu.
- Tendo la tatu; Yesu anatiwa miiba kichwani kwa ajili yetu. Tumwombe Mungu atujalie kushinda kiburi.
- Tendo la nne; Yesu anachukua Msalaba kwa ajili yetu. Tumwombe Mungu atujalie kuvumilia taabu.
- Tendo la tano; Yesu anakufa Msalabani. Tumwombe Mungu atujalie kuwapenda Yesu na Maria.
MATENDO YA UTUKUFU (Jumatano na Jumapili)
- Tendo la kwanza; Yesu anafufuka. Tumwombe Mungu atujalie kugeuka watakatifu.
- Tendo la pili; Yesu anapaa mbinguni. Tumwombe Mungu atujalie kwenda mbinguni.
- Tendo la tatu; Roho Mtakatifu anawashukia Mitume. Tumwombe Mungu atujalie bidii katika dini yetu.
- Tendo la nne; Bikira Maria anapalizwa mbinguni. Tumwombe Mungu atujalie kufa vizuri.
- Tendo la tano; Bikira Maria anawekwa Malkia mbinguni. Tumwombe Mungu atujalie kudumu katika njia njema.
MATENDO YA MWANGA (Alhamisi)
- Tendo la kwanza; Yesu anabatizwa Mto Jordani. Tumwombe Mungu atujalie uaminifu kwa ahadi zetu za ubatizo.
- Tendo la pili; Yesu anageuza maji kuwa divai huko Kana. Tumwombe Mungu atujalie kuukoleza ulimwengu kwa chachu ya enjili.
- Tendo la tatu; Yesu anatangaza Ufalme wa Mungu. Tumwombe Mungu atujalie kupokea Ufalme wake kwa toba ya kweli.
- Tendo la nne; Yesu anageuka sura. Tumwombe Mungu atujalie neema ya kuung’arisha ulimwengu kwa uso wa Yesu.
- Tendo la tano; Yesu anaweka Sakramenti ya Ekaristia. Tumwombe Mungu atujalie neema ya kujitoa sadaka kwa ajili ya wengine.
Karibu Vitatabu vya Kikatoliki
-
Vitabu Vya Dini
KITABU CHA NOVENA KWA MTAKATIFU RITA WA KASHIA
Original price was: Sh5,000.Sh0Current price is: Sh0. Download Now -
Vitabu Vya Dini
Kitabu cha Mwongozo wa kusali Rozari Takatifu ya Mama Bikira Maria
Original price was: Sh5,000.Sh0Current price is: Sh0. Download Now -
Vitabu Vya Dini
📕Kitabu cha Sala Muhimu: Mkusanyiko wa SALA, LITANIA NA NOVENA
Original price was: Sh12,500.Sh0Current price is: Sh0. Download Now -
Vitabu Vya Dini
Kitabu cha Novena Ya Huruma ya Mungu
Original price was: Sh2,500.Sh0Current price is: Sh0. Download Now -
Vitabu Vya Dini
Biblia Takatifu Agano Jipya
Original price was: Sh3,000.Sh0Current price is: Sh0. Download Now -
Vitabu Vya Dini
Kitabu cha Mwongozo wa Sala na Nyimbo za Ibada ya Njia ya Msalaba
Original price was: Sh6,000.Sh0Current price is: Sh0. Download Now -
Vitabu Vya Dini
Kwa nini Wakatoliki wanaweka Sanamu Kanisani?
Original price was: Sh5,000.Sh0Current price is: Sh0. Download Now -
Vitabu Vya Dini
KITABU CHA SALA ZA KILA SIKU ASUBUHI NA JIONI
Original price was: Sh4,000.Sh0Current price is: Sh0. Download Now -
Vitabu Vya Dini
Kitabu cha Tafakari kwa Mkristu Mkatoliki (Sehemu ya I)
Original price was: Sh3,000.Sh0Current price is: Sh0. Download Now -
Vitabu Vya Dini
Biblia Takatifu Agano la Kale
Original price was: Sh7,000.Sh0Current price is: Sh0. Download Now -
Vitabu Vya Dini
Kitabu cha Novena ya Roho Mtakatifu
Original price was: Sh5,000.Sh0Current price is: Sh0. Download Now
SALA KWA MTAKATIFU MIKAELI MALAIKA MKUU
Mtakatifu Mikaeli Malaika Mkuu, utulinde katika vita, uwe kinga yetu katika maovu na maoteo ya shetani, Mungu amtiishe, tunaomba sana, nawe Mkuu wa Majeshi ya Mbinguni kwa nguvu ya Mungu uwaangushe motoni shetani na pepo wabaya wengine wote, wanaozunguka duniani, ili kuzipoteza roho za watu. Amina.
Sala ya Saa Tisa
✝⌚✝
Sala ya saa tisa🙏🏾
Kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu. A mina
Yesu, ulikufa, lakini chanzo cha uhai kilitoka kwa ajili ya watu, na bahari ya huruma ilifunguka kwa ajili ya ulimwengu mzima. Ee chemchemi ya Uhai, huruma ya Mungu isiyo na mwisho, ikafunika ulimwengu mzima na ukajimwaga mwenyewe juu yetu.
❣✝❣
✝Ee Damu na Maji, yaliyotoka moyoni mwa Yesu kama chemchemi ya Huruma kwetu. Nakutumainia.
(Mara tatu)
🛐❣🛐
SALA WAKATI WA KUJIBARIKI NA MAJI YA BARAKA
Kwa njia ya Maji haya ya Baraka,
na kwa njia ya Damu yako azizi,
na kwa maombezi ya Moyo Safi wa Maria,
unioshe na uovu wangu wote na uwasaidie roho zinazoteseka toharani. Amina.
SALA MBELE YA SAKRAMENTI KUU II
Yesu, Mungu wangu mpenzi,/ upo hapa katika Altare mbele yangu;/ na mimi napiga magoti mbele yako.// Waniangalia sana,/ siyo kwa kunipeleleza,/ lakini kwa sababu wapenda kuniona hivi karibu na wewe,/ wafurahiwa nikija kukuabudu./ Wayasikiliza maneno yangu yote/ yenye kutoka mdomoni mwangu,/ na zaidi wapokea maneno yangu yanayotoka moyoni./ Nataka kuzungumza na wewe peke yako,/ na kusahau mambo mengine yote/ na watu wengine walioko kanisani pamoja nami./
Yesu wangu,/ nakushukuru/ kwa sababu umekubali kutupa Sakramenti hii kuu kabisa,/ ukitaka kukaa pamoja na sisi,/ na hata ukakubali kuwa chakula chetu/ chenye nguvu ya ajabu./ Mfalme wangu Yesu,/ Sultani wangu Mkuu,/ naamini kabisa kwamba upo katika Altare/ na kwamba umejificha chini ya umbo la mkate./ Ulipokuwapo bado hapa duniani mbele za watu,/ ulikuwa hujifichi kama sasa;/ lakini hata siku zile/ watu hawakuweza kukuona vile ulivyo./ Hawakuweza kuutambua Umungu wako,/ ikalazimu kukuamini tu sawa kama sisi./ Wakainama kichwa wakisema,/ “Bwana wangu na Mungu wangu”./ Na mimi kadhalika naungama/ U Bwana wangu na Mungu wangu/ na Mkombozi wangu/ na salama yangu yote./ U Yesu wangu tu,/ siwezi kusema zaidi./ Nakuabudu ee Yesu./ Najua sana, mimi ni mdogo kabisa,/ sina maana hata kidogo./ Mimi ni dhaifu na maskini mno./ Lakini Wewe katika hruuma yako kubwa/ waniita nije kwako./ Wewe huuangalii umaskini wangu,/ bali wanivuta katika mapendo yako./
Nasikia maneno yako usemayo:/ “Njooni kwangu ninyi nyote mnaoelemewa na mizigo/ nami nitawasaidia”./ Kwa ajili ya maneno hayo/ nakuja kwako bila hofu./ Najua kwamba wanipenda,/ najua wataka kunisaidia na kuniponya,/ najua kuwa wataka kunitakasa./
Nahitaji sana msaada wako, hakika./ Unaniona katika mwendo wangu wa kila siku,/ Jinsi ninavyohangaika na vishawishi mara nyingi;/ jinsi nilivyo na lazima ya kushindana kila siku/ nikitaka kukaa mwema na safi katika utumishi wako./ Naungama mbele yako Wewe Mkombozi wangu,/ kwamba sikukaa imara siku zote vile nilivyopaswa./ Naungama kwamba nimeshindwa mara nyingine/ na kwa hivi naomba toba./ Lakini kwa nini nimeshindwa mara nyingine?/ Kwa nini nikakosa?/ Ni kwa sababu nalikuwa nimekwenda mbali nawe;/ nalianza kujitegemea mwenyewe./ Katika majivuno yangu nikajisifu mwenyewe,/ nikajiona mwema,/ nikasahau udhaifu wangu./ Na kwa ajili hiyo nikajitia katika hatari bure,/ sikujilinda tena,/ nikampa shetani nafasi ya kunishambulia kwa hila zake zote./ Unihurumie ee Yesu wangu./
Sasa nafahamu jinsi nilivyokuwa mjinga kwelikweli./ Ndiyo maana nakuabudu kwa moyo wangu wote./ Najiweka mikononi mwako/ ufanye nami vile unavyotaka./ Wewe utanitunza;/ Wewe utanilinda vema;/ Wewe utaniongoza nijue namna ya kuepa hatari zote,/ na jinsi ya kufukuza kila kishawishi./ Chukua moyo wangu kabisa,/ kwa sababu ni mali yako kamili;/ Wewe ndiwe uliyeniumba,/ ndiwe uliyenipeleka katika Ukristo,/ nawe ndiwe utakayenihukumu siku ya mbele./ Ndivyo ninavyojitolea kwako./ Ndivyo ninavyokuabudu,/ wala sijui njia nyingine ya kukusifu zaidi./
Yesu wangu mpenzi,/ naomba upokee kwa uzuri heshima hiyo yangu./ Angalia: naitolea pamoja na heshima yote/ unayopewa daima na watakatifu wako/ na malaika wako./ Nikipiga magoti hapa mbele yako sasa,/ siko peke yangu,/ nakuabudu pamoja na Mama yako Bikira Maria,/ ambaye sala zake zinakupendeza kabisa./ Sala zangu naweka pamoja na sala zake yeye,/ uzipokee zote pamoja,/ zikupendeze zote sawa./ Ee Mama Maria!/ Nifundishe maneno ya kumsifu Mwanao Yesu vizuri./ Nipeleke kwa Yesu tumwabudu pamoja./ Nifunike na utakatifu wako/ kusudi Yesu asiangalie tena umaskini wangu/ na makosa yangu,/ aniponye katika huruma yake./
Sasa najisikia vizuri, Yesu wangu./ Sasa nina moyo wa kuweza kuendelea vema/ katika njia njema./ Sasa ninatumaini kwamba/ nitakaa mkristo mwema,/ nitakuwa mtumishi wako mwaminifu./ Nasikia amani kubwa sana moyoni mwangu,/ kwa kuwa nimo mikononi mwako./ Baada ya dakika chache/ nitaondoka tena kanisani,/ nitarudi nyumbani kwangu,/ lakini hatutaachana,/ hapana./ Mapendo yetu yatatuunganisha pamoja daima./ Wewe utanikumbuka nikiwa kazini,/ nikilala usingizi,/ nikienda njiani,/ kila mahali nilipo,/ Wewe utaniona,/ utafuatana na mimi./ Kadhalika nitakukumbuka tu./ Nitafanya bidii nisikuache kabisa./ Amina.
SALA MUHIMU ZA MKRISTO ZA KILA SIKU ASUBUHI
SALA YA ASUBUHI
Tuusifu Utatu Mtakatifu wa Mungu Mwenyezi, Baba, Mwana na Roho Mtakatifu, milele na milele, Amina.
Ee Utatu Mtakatifu wa Mwenyezi Mungu, Baba, Mwana na Roho Mtakatifu, nasadiki kuwa upo hapa na mahali pote. Ee Mungu wangu, umeniumba, umenikomboa, umenifanya mkristo, umenizidishia neema zako hapa duniani, umenitayarishia makao yangu mbinguni, umenijalia na siku hii nikutumikie. Ee Mungu wangu! Nakuabudu, nakushukuru, nakuomba toba, nakupenda! Ee Mungu wangu, nakutolea roho yangu, na mawazo, na maneno, na kazi, na furaha, na mateso yangu: uyapokee unipe neema yako nisikutende leo dhambi!
Majitoleo ya Asubuhi
Ee Baba yetu Mungu Mkuu, Umenilinda usiku huu, Ninakushukuru kwa moyo, Ee Baba, Mwana na Roho, Nilinde tena siku hii, Niache dhambi nikutii, Naomba sana Baba wee, Baraka yako nipokee, Bikira safi ee Maria, Nisipotee unisimamie, Mlinzi Mkuu Malaika wee, Kwa Mungu wetu niombee, Nitake nitende mema tu, Na mwisho nije kwake juu, Amina.
Kuweka nia njema
Kumheshimu Mungu wangu, Namtolea roho yangu, Nifanye kazi nipumzike, Amri zake tu nishike, Wazo neno tendo lote, Namtolea Mungu pote, Roho, mwili chote changu, pendo na uzima wangu, Mungu wangu nitampenda, Wala dhambi sitatenda, Jina lako nasifia, Utakalo hutimia, Kwa utii navumilia, Teso na matata pia, Nipe Bwana neema zako, Niongezee sifa yako, Amina.
Majitoleo
Ee Yesu, kupitia mikono safi ya Bikira Maria, na kwa maungano na sadaka yako kuu, ninakutolea sala, matendo, kazi, masumbuko, na furaha zangu zote za siku hii ya leo, kwa ajili ya nia za Moyo wako Mtakatifu, Ee Yesu ufalme wako utufikie!
Baba Yetu….
Salamu Maria, …..
Nasadiki …….
Amri za Mungu ……
Amri za Kanisa ……
Sala ya Malaika wa Bwana
Malaika wa Bwana alimpasha habari Maria, naye akapata mimba kwa uwezo wa Roho Mtakatifu. Salamu Maria,….
Ndimi Mtumishi wa Bwana, nitendewe ulivyonena. Salamu Maria, ……
Neno wa Bwana akatwaa Mwili, akakaa kwetu. Salamu Maria, …..
Utuombee, ee Mzazi Mtakatifu wa Mungu, tujaliwe ahadi za Kristo.
Tuombe:
Tunakuomba ee Bwana, utie neema yako mioyoni mwetu, ili sisi tuliojua kwa maelezo ya Malaika, kwamba, Kristo Mwanao amejifanya mtu: kwa mateso na Msalaba wake, utufikishe kwenye utukufu wa ufufuko. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristo Bwana wetu, Amina.
Sala kwa Malaika Mlinzi
Ee Malaika wangu, uliyewekwa na Mungu mwema unilinde, naomba uniongoze leo, unitunze, unisimamie, unishauri. Amina.
Sala kwa wenye kuzimia
Ee Yesu mwenye huruma, mpenda roho za watu, nakuomba kwa ajili ya kuzimia kwa Moyo wako Mtakatifu, na kwa ajili ya Mama Yako asiye na doa, uwatakase kwa damu yako, watu wote wenye dhambi wanaokufa sasa, na watakaokufa leo.
Moyo wa Yesu uliozomia, uwahurumie watu wanaokufa X3.
Sala kwa Mtakatifu Yosef
Ee Yosef mwenye heri, tunakimbilia kwako, katika masumbuko yetu, na kishaomba shime ya Mchumba wako Mtakatifu, tunaomba pia kwa matumaini usimamizi wako. Kwa ajili ya mapendo uliyompenda nayo Bikira Mtakatifu, Mzazi wa Mungu, na kwa ajili ya tunza ya Baba, uliyomtunza nayo Mtoto Yesu, tunakuomba sana, utuangalie kwa wema, sisi tuliokuwa fungu lake Yesu Kristo, tuliokombolewa kwa damu yake, utusimamie katika masumbuko yetu, kwa enzi na shime yako.
Ee Mlinzi amini wa Jamaa Takatifu, uwakinge watoto wateule wa Yesu Kristo, ee Baba uliyetupenda mno, utuepusha na kilema chochote cha madanganyo na upotevu. Ee kinga yetu mwezaji,utusimamie huko juu mbinguni ulipo, tunaposhindana na wenye nguvu wakaao gizani. Kama vile siku za kale ukamwokoa Mtoto Yesu katika hatari ya kuuawa, na leo hivi, ulikinge Kanisa Takatifu la Mungu katika mitego ya adui, na katika shida yote, mtunze daima kila mmoja wetu, tupate mfano wako, tusaidie kwa msaada wako, kukaa na utakatifu maisha, kufa kifo chema, na kupokelewa mbinguni makao ya raha milele. Amina
Sala kwa Mtakatifu Yuda Thadei
(Sala hii inaweza kusaliwa kila siku au kama Novena ya siku tisa mfululizo kuomba kitu kilekile)
Mtakatifu Yuda Tadei,/ Mtume Mtakatifu,/ Mtumishi mwaminifu na rafiki wa Yesu./ Jina la yule msaliti aliyemwuza Yesu/ limewafanya wengi wakusahau./ Walakini Kanisa zima linakuheshimu/ na kukuomba kama Msaidizi katika mashaka makubwa,/ na katika mambo yasiyo na matumaini tena./
Uniombee mimi mnyonge./ Ninaomba utumie uwezo ule uliojaliwa/ wa kuleta upesi msaada kwa watu walioukosa./ Unisaidie sasa katika mahitaji yangu,/ ili nipate kitulizo na msaada wa mbinguni/ katika lazima zangu,/ masumbuko na mateso,/ hasa/ (taja shida yako)./ Pia ili niweze kumsifu Mungu nawe na wateule wote milele./
Mtakatifu Yuda Tadei,/ utuombee,/ na uwaombee watu wote wanaokuheshimu na kukuomba msaada./
Baba yetu……. Salamu Maria ……… Atukuzwe ……….
Sala ya Medali ya Mwujiza
Ee Bikira Maria uliyekingiwa dhambi ya asili, utuombee sisi wenye kukimbilia kwako, uwaombee na wale wasioukimbilia kwako, hasa maadui wa Kanisa Takatifu, na wale waliokabidhiwa kwako. Amina.
Majitoleo kwa Bikira Maria
(Sala iliyotungwa na Mtk. Aloisi)
Bibi yangu mtukufu Maria, nakuwekea amana ya roho yangu na mwili wangu, nikikuomba uipokee amana yangu, kuitunzia ulinzi mwema ulinzi bora, ninakuaminia na kila neno langu, matumaini na kitulizo na kisongo chote, na masumbuko na uzima na ukomo wa uzima wangu: nitakayo ndiyo unifanyizie kwa maombezi na stahili zako, ili mambo yangu yote yapate kuongoka, yakiwa na kufuata mapenzi yako, pamoja na mapenzi ya Mwanao. Amina.
SALA KWA MAMA WA UCHUNGU KUOMBA NEEMA YA PEKEE
Ee Mama mbarikiwa na Bikira mwenye uchungu, Malkia wa Mashahidi, uliyesimama chini ya msalaba na uliyemtazama Mwana wako akifa, unitazame kwa huruma ya kimama ninayekusikitikia. Kwa sababu ya upanga uliochoma moyo wako, kwa mateso ya maisha yako nakuomba uniangalie kwa wema ukasikilize maombi yangu. Nakuomba, ee Mama, uniombee daima kwa Mwana wako, najua hawezi kukuvyima wewe kitu chochote. Basi, ufanye, Moyo wa Mwanao ukubali kunijalia ombi langu hili …………………(taja ombi lako).
Maana nitamkimbilia nani katika mahitaji na misiba yangu isipokuwa kwako, ee Mama wa huruma? Wewe hasa unaweza kutusaidia sisi tulio bado katika bonde la machozi kwa sababu ulishiriki mateso ya Mwanao kutukomboa. Umtolee Yesu tone moja la Damu yake takatifu. Umkumbushe ya kuwa wewe ni matumaini, furaha na maisha yetu ukanipatie jambo ninalokuomba kwa Yesu Kristo, bwana wetu. Amina.
ROZARI YA MATESO SABA YA BIKIRA MARIA
Tumia Rozari ya Mateso Saba ya Bikira Maria iliyo na mafungu 7 yaani mateso 7 yenye Salamu Maria saba kwa kila teso.
TESO LA KWANZA
Mzee Simeoni aliagua kuwa Moyo wa Mama Maria utachomwa kwa upanga.
Tuombe neema ya kuvumilia mateso.
Mama wa mateso utuombee.
Baba Yetu ……… Salamu Maria x7. Atukuzwe Baba ……
Mateso na majonzi ya Mama Maria hayana mfano.
TESO LA PILI
Maria na Yosefu walikimbilia Misri usiku ili kumficha Mtoto Yesu asiuawe na Herodi.
Tuombe neema ili miili yetu iwe kimbilio lake Yesu.
Mama wa mateso utuombee.
Baba Yetu ……… Salamu Maria x7. Atukuzwe Baba ……
Mateso na majonzi ya Mama Maria hayana mfano.
TESO LA TATU
Mama Maria aliona uchungu sana Mtoto Yesu alipopotea kwa siku tatu.
Tuombe neema ya kudumu na Yesu mioyoni mwetu.
Mama wa mateso utuombee.
Baba Yetu ……… Salamu Maria x7. Atukuzwe Baba ……
Mateso na majonzi ya Mama Maria hayana mfano.
TESO LA NNE
Mama Maria aliona uchungu sana alipokutana na Mwanae Yesu katika njia ya Msalaba.
Tuombe neema ya kudumu na Yesu siku zote.
Mama wa mateso utuombee.
Baba Yetu ……… Salamu Maria x7. Atukuzwe Baba ……
Mateso na majonzi ya Mama Maria hayana mfano.
TESO LA TANO
Mama Maria aliona uchungu sana alipomwona Mwanae Yesu akisulibiwa Msalabani.
Tuombe neema ya kufa mikononi mwa Yesu na Maria.
Mama wa mateso utuombee.
Baba Yetu ……… Salamu Maria x7. Atukuzwe Baba ……
Mateso na majonzi ya Mama Maria hayana mfano.
TESO LA SITA
Mama Maria aliona uchungu sana alipopakata maiti ya Mwanae Yesu baada ya kushushwa Msalabani.
Tuombe neema ya kutotenda dhambi.
Mama wa mateso utuombee.
Baba Yetu ……… Salamu Maria x7. Atukuzwe Baba ……
Mateso na majonzi ya Mama Maria hayana mfano.
TESO LA SABA
Mama Maria aliona uchungu sana aliporudi nyumbani baada ya kumzika Mwanae Yesu
Tuombe neema ya kitulizo kwa Mama Maria.
Mama wa mateso utuombee.
Baba Yetu ……… Salamu Maria x7. Atukuzwe Baba ……
Mateso na majonzi ya Mama Maria hayana mfano.
SALAMU MARIA
Salamu Maria
Umejaa neema
Bwana yu nawe
Umebarikiwa kuliko wanawake wote
Na Yesu mzao wa tumbo lako amebarikiwa
Maria Mtakatifu
Mama wa Mungu
Utuombee sisi wakosefu
Sasa, na saa ya kufa kwetu.
Amina.
LITANIA YA MOYO MTAKATIFU WA YESU
Bwana utuhurumie Bwana utuhurumie
Kristo utuhurumie Kristo utuhurumie
Bwana utuhurumie Bwana utuhurumie
Kristo utusikie Kristo utusikilize
Baba wa mbinguni Mungu Utuhurumie
Mwana, Mkombozi wa dunia Mungu Utuhurumie
Roho Mtakatifu Mungu Utuhurumie
Utatu Mtakatifu Mungu mmoja Utuhurumie
Moyo wa Yesu Mwana wa Baba wa Milele Utuhurumie
Moyo wa Yesu uliotungwa na Roho Mtakatifu mwilini mwa Mama Bikira Maria Utuhurumie
Moyo wa Yesu ulioungana na Neno wa Mungu Utuhurumie
Moyo wa Yesu ulio na utukufu pasipo mfano Utuhurumie
Moyo wa Yesu, hekalu takatifu la Mungu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, hema la Yule aliye juu Utuhurumie
Moyo wa Yesu tanuru lenye kuwaka mapendo Utuhurumie
Moyo wa Yesu, nyumba ya Mungu na mlango wa Mbingu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, tanuru yenye kuwaka mapendo Utuhurumie
Moyo wa Yesu, chombo cha haki na upendo Utuhurumie
Moyo wa Yesu, unaojaa upendo na wema Utuhurumie
Moyo wa Yesu, kilindi cha fadhila zote Utuhurumie
Moyo wa Yesu, unaostahili sifa zote Utuhurumie
Moyo wa Yesu, unaotawala mioyo yote Utuhurumie
Moyo wa Yesu, zinamokaa hazina za hekima na elimu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, uliopendelewa na Mungu Baba Utuhurumie
Moyo wa Yesu, uliotuenezea maziada yake Utuhurumie
Moyo wa Yesu, mtamaniwa wa vilima vya milele Utuhurumie
Moyo wa Yesu, wenye uvumilivu na huruma nyingi Utuhurumie
Moyo wa Yesu, tajiri kwa wote wenye kukuomba Utuhurumie
Moyo wa Yesu, chemchemi ya uzima na utakatifu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, malipo kwa dhambi zetu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, ulioshibishwa matusi Utuhurumie
Moyo wa Yesu, uliovunjika kwa sababu ya ubaya wetu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, uliotii mpaka kufa Utuhurumie
Moyo wa Yesu, uliochomwa kwa mkuki Utuhurumie
Moyo wa Yesu, chemchemi ya faraja zote Utuhurumie
Moyo wa Yesu, uzima na ufufuo wetu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, amani na upatanisho wetu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, sadaka ya wakosefu Utuhurumie
Moyo wa Yesu, unamokaa wokovu wao wenye kukutumaini Utuhurumie
Moyo wa Yesu, matumaini yao wenye kuzimia kwako Utuhurumie
Moyo wa Yesu, sababu ya furaha ya watakatifu wote Utuhurumie
Mwanakondoo wa Mungu, uondoaye dhambi za dunia Utusamehe Bwana
Mwanakondoo wa Mungu, uondoaye dhambi za dunia Utusikilize Bwana
Mwanakondoo wa Mungu, uondoaye dhambi za dunia Utuhurumie
Kiongozi: Yesu mwenye Moyo mpole na mnyenyekevu,
Wote: Ufanye mioyo yetu ifanane na Moyo wako
TUOMBE: (W) Ee Mungu Mwenyezi milele, uuangalie Moyo wa mwanao mpendelevu, pia na heshima na malipo aliyokutolea kwa ajili ya wenye dhambi, uridhike, uwaondolee wenye kuomba toba kwako kwa njia ya huyo Mwanao Yesu Kristo anayeishi na kutawala nawe pamoja na Roho Mtakatifu, Mungu milele. Amina.
SALA YA BWANA: SALA YA BABA YETU
Baba yetu uliye mbinguni
Jina lako litukuzwe
Ufalme wako ufike
Utakalo lifanyike
Duniani kama mbinguni
Utupe leo mkate wetu wa kila siku
Utusamehe makosa yetu
Kama tunavyowasamehe
Na sisi waliotukosea
Usitutie katika kishawishi
Lakini utuopoe maovuni.
Amina.
Malkia wa Mbingu
Malkia wa mbingu, furahi, aleluya. Kwani uliyestahili kumchukua, Aleluya. Amefufuka alivyosema, Aleluya. Utuombee kwa Mungu, Aleluya. Furahi shangilia, ee Bikira Maria, Alaluya. Kwani hakika Bwana amefufuka Aleluya. Tuombe. Ee Mungu, uliyependa kuifurahisha dunia kwa kufufuka kwake Bwana wetu Yesu Kristu, Mwanao: fanyiza, twakuomba, kwa ajili ya Bikira Maria, tupate nasi furaha za uzima wa milele. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristu Bwana wetu. Amina.
Majitoleo ya Asubuhi
Ee Baba yetu Mungu Mkuu, Umenilinda usiku huu, Ninakushukuru kwa moyo, Ee Baba, Mwana na Roho, Nilinde tena siku hii, Niache dhambi nikutii, Naomba sana Baba wee, Baraka yako nipokee, Bikira safi ee Maria, Nisipotee unisimamie, Mlinzi Mkuu Malaika wee, Kwa Mungu wetu niombee, Nitake nitende mema tu, Na mwisho nije kwake juu, Amina.
LITANIA YA KUWAOMBEA MAPADRE WOTE II
Kwa ajili ya Baba Mtakatifu wetu ..(N); Bwana, umpe moyo wako wa uchungaji mwema
Kwa ajili ya makardinali na maaskofu wakuu; Uwape moyo wa kichungaji ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wa majimbo; Uwajaze na Roho wako ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre watawa; Wakamilishe katika wito wao ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre walioko hatarini; Uwaokoe ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wenye udhaifu; Uwatie nguvu ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wenye hofu; Uwape amani ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre waliokata tamaa; Uwavuvie upya ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wakaao upweke; Uwasindikize ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wamisionari; Uwalinde ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wanaohubiri; Uwaangazie ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre na watawa waliokufa; Uwafikishe kwenye utukufu wako ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wote; Wajalie hekima na ufahamu wako ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wote; Uwajalie elimu na shauri lako
Kwa ajili ya mapadre wako; wajalie wakuheshimu na wakuogope
Kwa ajili ya mapadre wote; Wajalie subira na upendo
Kwa ajili ya mapadre wote; wajalie utii na upole
Kwa ajili ya mapadre wote; uwajalie hamu kuu ya kuokoa roho za watu
Kwa ajili ya mapadre wote; wape fadhila za imani, matumaini na mapendo
Kwa ajili ya mapadre wote; Wajalie upendo mkuu kwa Ekaristi
Tunakuomba uwajalie mapadre wote; Waheshimu uhai na hadhi ya mtu ee Bwana
Tunakuomba uwajalie mapadre wote nguvu na bidii katika kazi zao ee Bwana
Tunakuomba uwajalie mapadre wote amani katika mahangaiko yao ee Bwana
Tunakuomba uwajalie mapadre wote upendo mkuu kwa Utatu Mtakatifu ee Bwana
Tunakuomba uwajalie mapadre wote upendo mkuu kwa Bikira Maria ee Bwana
Uwajalie mapadre wote wawe mwanga wa Kristo ee Bwana
Uwajalie mapadre wote, wawe chumvi kwa ulimwengu ee Bwana
Uwajalie mapadre wote, wajizoeze kujitoa sadaka na kujinyima ee Bwana
Uwajalie mapadre wote, wawe watakatifu kimwili, kiakili na kiroho ee Bwana
Uwajalie mapadre wote wawe watu wa sala ee Bwana
Uwajalie mapadre wote wawe kioo cha imani kwako ee Bwana
Uwajalie mapadre wote wajali sana wongofu wetu ee Bwana
Uwajalie mapadre wote wawe waaminifu kwa wito wao wa kikuhani ee Bwana
Uwajalie mapadre wote, ili mikono yao ibariki na kuponya ee Bwana
Uwajalie mapadre wote wawake moto wa mapendo yako ee Bwana
Uwajalie mapadre wote hatua zao zote ziwe kwa ajili ya utukufu wa Mungu ee Bwana
Uwajalie mapadre wote wajazwe na Roho Mtakatifu na uwajalie karama zake kwa wingi ee Bwana.
Tuombe.
Baba, Mwana na Roho Mtakatifu, usikie sala tunazokutolea kwa ajili ya mapadre wetu. Uwajalie wafahamu waziwazi kazi uliyowaitia kuifanya, uwape neema zote wanazohitaji ili waitikie wito wako kwa ushujaa, kwa upendo, na majitoleo yenye udumifu katika mapenzi yako matakatifu. Amina.
SALA YA NOVENA KWA MOYO MTAKATIFU WA YESU
Ee Moyo Mtakatifu sana wa Yesu, chemchemi ya kila baraka, ninakuabudu, ninakupenda, na kwa majuto halisi ya dhambi zangu, nakutolea moyo wangu dhaifu. Nifanye mnyenyekevu, mvumilivu na safi, nikikubali na kuyatii kabisa mapenzi yako. Ee Yesu mwema, unijalie niishi nawe na kwa ajili yako. Unilinde niwapo katikati ya hatari, unifariji katika mateso, unipe afya ya mwili na msaada katika mahitaji ya mwili, Baraka yako juu ya kila nilifanyalo, na neema ya kifo chema. Amina.
Ee Yesu uliyesema “Kweli nawaambieni, ombeni nanyi mtapewa, tafuteni nanyi mtapata, gongeni nanyi mtafunguliwa”, tazama ninagonga, ninatafuta na kuomba …….. (Taja ombi lako)
Baba Yetu….., Salamu Maria …….., Atukuzwe Baba……..
Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutumainia kwa moyo wote!
Ee Yesu uliyesema “Kweli nawaambieni, chochote mtakachomwomba Baba kwa jina langu mtapewa”, tazama kwa jina lako ninaomba ……. (Taja ombi lako)
Baba Yetu….., Salamu Maria …….., Atukuzwe Baba……..
Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutumainia kwa moyo wote!
Ee Yesu uliyesema “Kweli nawaambieni, mbingu na dunia zitapita lakini maneno yangu hayatapita kamwe”, tazama, nikitiwa nguvu na maneno yako ya kweli ninaomba …….. (Taja ombi lako)
Baba Yetu….., Salamu Maria …….., Atukuzwe Baba……..
Moyo Mtakatifu wa Yesu, ninakutumainia kwa moyo wote!
Ee Moyo Mtakatifu wa Yesu, ambaye kwako ni kitu kimoja tu kisichowezekana, ambacho ni kutoacha kutowaonea huruma wenye huzuni, utuhurumie sisi wakosefu maskini na utujalie neema tukuombayo kwa njia ya Moyo Imakulata wa Maria, Mama yetu mpole.
Sali ‘Salamu Malkia’ na kuongezea, ‘Mtakatifu Yosefu Baba Mlishi wa Yesu, utuombee’.
P.S. – Sala hii ya Novena ilisaliwa kila siku na PADRE PIO kwa ajili ya kuwaombea wale wote waliomwomba msaada wa sala zake. Unaweza kuisali kwa namna tofauti tofauti. Mfano, kama Novena ya siku tisa, ambapo unasali sala hii mara moja au zaidi kila siku kwa siku tisa, au unaweza kuifanya kama Novena ya masaa, ambapo unasali sala hii kila baada ya saa moja kwa masaa tisa kwa siku hiyo hiyo, hasa kama kitu unachokiomba ni cha haraka au umesongwa moyoni. Vilevile unaweza kuifanya sala hii kama sehemu ya sala zako za kila siku katika mwezi Juni ambao ni mwezi uliotengwa na Kanisa kwa ajili ya kuuheshimu Moyo Mtakatifu wa Yesu, na hapo utaitumia kuwaombea watu waliokuomba msaada wa sala zako kama alivyofanya Mtakatifu Padre Pio. Pia unaweza kuitumia kama sala yako ya siku zote au ya mara kwa mara kwa ajili ya mahitaji mbalimbali.
Novena ya Siku tisa kwa Mtakatifu Agustino wa Hippo: Sala zote na Litania
Anza Novena hii tarehe 19 Agosti ili kumalizia tarehe 27 Agosti na kusheherekea tarehe 28 Agosti, Sikukuu ya Mtk. Augustino wa Hippo.
SIKU YA KWANZA – kutafuta ukweli – kweli ni nini?
Kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina
Tafakari
Pamoja na Mtakatifu Augustino tunasema “ Umetuumba kwa ajili yako ee Bwana, kwani ni wewe peke yako ndie Mungu wetu, na nyoyo zetu hazitapumzika, hadi tupumzike ndani mwako.”
Tunapoanza Novena yetu kwa Mtakatifu Augustino tunamwomba Mungu neema ya kuwa na roho kama yake katika safari yetu katika kuzitambua nafsi zetu. Tunatafakari sisi ni nani na tunaelekea wapi kama wafuasi wa Mtakatifu Augustino katika dunia ya leo. Kama Mt Augustino alivyoutafuta ukweli bila kuchoka, nasi tutulie na kuruhusu maswali haya yaguse ufahamu wetu. Ni nini kinachonisababisha niendelee kumtafuta Mungu? Baada ya kumpata Mungu, ninamfanyaje awe hai kwa watu wale ninaoishi nao?
Kama kuna jambo moja Mt Augustino anasisitiza tena na tena kuhusu kumtafuta Mungu, ni kuwa lazima tuanze kumtafuta ndani mwetu. Huko ndiko tutakuta ukweli, mwanga na furaha katika Kristu mwenyewe. Ndani ya nafsi zetu ndiko tutasikilizwa tunaposali, katika nafsi zetu ndiko tutampenda Mungu na kumwabudu.
Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino
Bwana utuhurumie Bwana utuhurumie
Kristu utuhurumie Kristu utuhurumie
Bwana utuhurumie Bwana utuhurumie
Kristu utusikie Kristu utusikilize
Baba wa mbinguni Mungu utuhurumie
Mwana Mkombozi wa dunia Mungu utuhurumie
Roho Mtakatifu Mungu utuhurumie
Utatu Mtakatifu Mungu mmoja utuhurumie
Maria Mama wa Yesu utuombee
Maria Mama wa faraja utuombee
Maria Mama wa shauri jema utuombee
Mt. Augustimo nyota angavu ya Kanisa utuombee
Mt Augustino uliyejawa bidii kwa ajili ya kuutafuta utukufu wa Mungu utuombee
Mt. Augustino mtetezi jasiri wa Ukweli utuombee
Mt Augustino ushindi wa neema ya Mungu utuombee
Mt Augustino uliyewaka mapendo kwa Mungu utuombee
Mt Augustino mkuu sana na mnyenyekevu sana utuombee
Mt Augustino mfalme wa maaskofu na wanateolojia utuombee
Mt Augustino baba wa maisha ya kitawa utuombee
Mt Augustino mtakatifu kati ya wenye hekima na mwenye hekima kati ya watakatifu utuombee
Utuombee Mtakatifu Augustino – ili tustahili maagano ya Kristu.
Tuombe: Umetuumba kwa ajili yako ee Bwana, na nyoyo zetu hazitapumzika kamwe, hadi tutakapopumzika ndani mwako. Tunakuomba utubariki katika mahangaiko yetu ya kukutafuta wewe na utusaidie tunapokutana na makwazo. Tunapokupata, tunaomba utujalie neema ya kuwa waaminifu kwako ee Mungu wa historia, tuwe waaminifu kwa Yesu Kristu Mkombozi wetu, kwa Kanisa letu na mafundisho yake, na tuwe waaminifu katika wito wetu tuliouchagua katika kukutumikia wewe. Tunaomba hayo kwako wewe Baba mwema, kwa njia ya Kristu Bwana wetu na kwa maombezi ya Mtakatifu Augustino Msimamizi wa Jumuiya yetu, Amina.
Baba yetu……, Salamu Maria….., Atukuzwe Baba……
Siku ya pili – Utulivu
Kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina
Tafakari
“Ingia sasa, ndani ya moyo wako (Isaya 46:8) na uwe na imani, utamkuta Kristu humo. Humo anaongea na wewe, mimi, mwalimu, napaaza tu sauti yake lakini Yeye ndiye anayekufunza wewe kwa ufanisi zaidi katika utulivu wako”
Je tunapenda maisha ya utulivu ambapo tunapata muda wa kumtafakari Mungu na mambo anayotutendea katika maisha yetu? Kwa vile Yesu anaongea nasi katika utulivu, inatupasa tujifunze namna ya kuutunza utulivu ndani ya nafsi zetu licha ya mahangaiko na misukosuko ya maisha. Tutenge muda katika siku yetu ambapo tunaweza kutulia na Kristu na kumsikiliza, na wala sio sisi kuongea nae tu bila kumsikiliza naye pia. Soma Neno la Mungu kwa utulivu na kwa tafakari, na uone kama kuna kitu gani Mungu anakuaombia leo. Lazima tusafishe macho ya nyoyo zetu, ili tuweze kumwona Mungu ndani mwetu. Tunafanya hivyo kwa njia ya toba na maungamo. Kusafishwa vizuri ni jambo linaloweza kuambatana na maumivu, lakini tunahitaji usafi wa nafsi ili tuweze kuwa wasikivu zaidi kwa sauti ya Mungu ndani mwetu.
Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino
(Angalia siku ya kwanza)
Tuombe: Ee Baba mwema, tunataka kumfuata Mwanao Yesu kwa ukaribu zaidi. Utuwezeshe kuumbika upya nawe kwa mfano wa Mtakatifu Augustino katika maisha yake ya utulivu. Utusaidie kuacha mambo ya dunia hii yanayopita ili tupate hamu kubwa zaidi ya kukufuata. Imarisha imani yetu ili tusikie sauti yako katika maandiko: ili tuweze kukuona Wewe katika matukio ya maisha yetu. Tunaomba haya kwa njia ya Kristu Bwana wetu, anayeishi na kutawala nawe na Roho Mtakatifu, Mungu mmoja milele na milele. Amina.
Baba yetu……, Salamu Maria….., Atukuzwe Baba……
Siku ya tatu – matendo-tafakari na matendo
Katika wito wetu uwao wote wa maisha yetu, tunaalikwa na Yesu tutafakari jinsi Martha alivyolalamika kuwa dada yake Maria alitumia muda wote katika kumsikiliza Yesu badala ya kusaidia kazi. Mt. Augustino akiwa kama mtawa aliuchukua mfano wa Martha na Maria kwa kushiriki kwa ukamilifu pia katika ujenzi wa uhai wa Kanisa kwa njia ya maandishi na kazi zake njema. Je mimi ninaoanishaje kati ya kutenda, kusali na tafakari takatifu?
Mt. Augustino anatufundisha kuwa tuwe tayari kuwatumikia wengine. Asiwepo mtu anayedhani kuwa anaweza kusali tu muda wote bila matendo, na wala asiwepo anayedhani atafaidika kwa matendo mengi yasiyosindikizwa na wingi wa sala. Tunapozigundua karama zetu Mungu alizotupa, tuwe tayari kuzishirikisha kwa wengine, kwani siku ya mwisho tutahukumiwa kwa namna ambavyo tuliwajali wengine. Kwa hiyo baada ya kumpata Mungu ndani mwako, usibaki humo, bali mgeukia yeye aliyekuumba. “Tupande mlimani lakini tusijenge vibanda, tushuke tuwatumikie wengine”
Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino
(Angalia siku ya kwanza)
Tuombe: Mungu Baba yetu, tunakutukuza na kukushukuru kwa kulijalia Kanisa lako mtakatifu mkuu namna hii. Tunapojitahidi kuishi roho na karama zake, utujalie neema za kukua katika utumishi wetu kwa wengine kwa njia ya matendo mema na pia katika maisha yetu ya sala, kwa mfano wa Mt. Augustino. Tunaomba hayo kwa Jina la Mwanao, Bwana na Mwokozi wetu. Amina.
Baba yetu……, Salamu Maria….., Atukuzwe Baba……
Siku ya nne – umaskini wa kiinjili – maisha ya kujitoa
Kwa Jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina.
Kuna wakati Mt. Augustino alikosa kitu chochote cha kuwapatia wasiojiweza, kwa sababu alikuwa anagawa kila alichoweza kwa wenye shida. Alipoishiwa kabisa, aliuza baadhi ya vitu alivyokuwa navyo ili kupata pesa iliyohitajika kwa ajili ya wenye shida.
Je, mimi pamoja na karama zote alizonijalia Mungu na vipaji vyote nilivyo navyo, ninajitahidi kuiga mfano wa Mt. Augustino katika kujitoa kwa wengine?
Umaskini wa kiinjili ni tofauti na umaskini wa kukosa mali au pesa. Ni namna moyo wa mtu anavyopenda kujitoa hata nje ya Jumuiya yake. Yesu Kristu alijitoa kabisa kwetu kwa kuuacha Umungu wake na kujitwalia ufukara wetu ili aweze kututajirisha. Hii ni changamoto kwetu kuwa tuwe tayari kujitoa kwa ajili ya wale wanaotuhitaji na Augustino ni mfano katika hilo. Tujitolee kufanya kazi za huruma, kwani mtu hataishi kwa mkate tu. Je tunawasaidiaje maskini walioko katika eneo letu? Ufalme wa Mungu utawafikiaje wengine kupitia kwetu. Mt Augustino anatupa changamoto leo kuwa tukubali kwa moyo mmoja kutoa vitu tulivyo navyo kwa ajili ya wengine, na tumfuate Kristu kwa moyo mpya na wa dhati.
Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino
(Angalia siku ya kwanza)
Tuombe: Tunakutukuza ee Bwana kwa kila unatupowezesha kushirikisha vile ulivyotujalia kwa ajili ya wahitaji, na kushikama katika upendo wako. Tunakuomba utujalie neema ya kudumu katika kushirikiana na kupendana ili tuwe mashahidi wa ukarimu wako mkuu. Tunaomba hayo kwa njia ya Bwana wetu Yesu Kristu, anayeishi na kutawala pamoja nawe na Roho Mtakatifu, Mungu mmoja daima na milele, Amina.
Baba yetu……, Salamu Maria….., Atukuzwe Baba……
Siku ya tano – urafiki katika jumuiya yetu
Kwa Jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina.
Mt. Augustino anashuhudia kuwa kitu kilichomweka karibu na marafiki zake kaka na dada zake ni kulekuongea na kucheka pamoja, kusaidiana, kusoma vitabu vinavyofanana vyenye mambo ya kujenga, kutaniana, kutofautiana mara kwa mara bila kukasirikiana, na alama za urafiki wetu zilijionyesha katika nyuso zetu, sauti zetu, macho yetu, na namna nyingi nyingine”. Je mimi nafurahia mahusiano yaliyoko katika Jumuiya yetu? Kuna jambo gani naweza kufanya ili kuboresha mahusiano na wanajumuiya wenzangu?
Ushahidi wa mapendo ya kweli unakuja pale tunapokuwa tayari kubebeana mizigo yetu. Tunapojitahidi kuboresha mambo yanayohusu Jumuiya, ukweli ni kuwa tunaboresha mambo yetu binafsi pia. Tumwombe Mungu ili tuweze kuona namna ambavyo Jumuiya yetu inatutegema katika hali na namna mbalimbali na tuweze kuboresha mahusiano ili kukuza urafiki kati yetu kama anavyotufundisha Kristu.
Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino
(Angalia siku ya kwanza)
Tuombe: Bwana Mungu wetu, ulimfunulia Mt. Augustino uzuri ulioko katika urafiki uliojengwa katika misingi yako. Utujalie sisi tunaosimamiwa naye hapa duniani, tukue katika urafiki mtakatifu wa kijumuiya. Utujalie tufikie ukamilifu wa urafiki huo katika makao yetu ya mbinguni unakoishi na kutawala daima na milele, Amina.
Baba yetu……, Salamu Maria….., Atukuzwe Baba……
Siku ya sita – augustino mfano wa unyenyekevu
Kwa Jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina.
Unyenyekevu unapatikana tu katika vita vya kiroho. Umuhimu wa majaribu katika maisha yako ya kiroho ni kuwa ni kwa kupitia tu majaribu hayo unajipatia unyenyekevu. Hapo ndio unauona umuhimu wa kumpokea yesu kuwa Mwokozi wako. Ukiwa na kiburi itakuwa ni kikwazo kikubwa kumpokea Mwokozi.
Kwa Augustino, unyenyekevu sio kujidharau, bali ni kujitahidi kufahamu karama alizotujalia Mungu na kuziendeleza. Ili kuwa mtu mnyenyekevu, jifahamu kuwa u mdhambi, na kuwa Mungu ndie anayeweza kukuweka huru. Fanya maungamo ya dhambi zako ili uwe wa kundi lake Mungu. Je, kama unyenyekevu ndio ukweli, ninajitahidije kuushirikisha ukweli huu kwa wengine katika Jumuiya yetu?
Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino
(Angalia siku ya kwanza)
Tuombe: Tuelekezee nyoyo zetu katika wema wako ee bwana, na geuza macho yetu mbali na kiburi na puuzi za dunia ili tuwe wafuasi wa maneno yako: Jifunzeni kwangu kwani mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo. Utujalie tukue kila siku katika unyenyekevu ambao unampendeza sana moyo wa Msimamizi wetu mt. Augustino. Amina.
Baba yetu……, Salamu Maria….., Atukuzwe Baba……
Siku ya saba – uangalizi wa imani yetu
Kwa Jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina.
Na tumpende Bwana wetu, tulipende kanisa lake. Tunampokea Roho Mtakatifu kadri tunavyolipenda Kanisa lake, kama tukiunganika pamoja kwa upendo, kama tukilifurahia jina katoliki na Imani yake. Tuamini kuwa tutakuwa na Roho Mtakatifu kwa kipimo cha upendo wetu kwa Kanisa lake. Tunalipenda Kanisa kama tulisimama imara katika ushirika na upendo.
Je ninalipenda Kanisa Katoliki? Ninajitahidi kujifunza imani hii na kuwashirikisha wengine au ninafuata mkumbo tu? Tunaalikwa kuishi kwa mfano wa Mt. Augustino ambaye alijielimisha kuhusu imani ya Kanisa Katoliki na kuikumbatia, kuitetea na kuishirikisha kwa wengine. Tusisite kujitoa katika dunia yetu ya leo pale tunapohitajika katika kueneza imani yetu. Tumwombe Mungu atujalie kwa mfano wa Mt. Augustino, moyo wa kusukumwa kuwashirikisha wengine imani iliyo hai kwa njia ya maneno, na matendo yetu, na hivyo kulitetea Kanisa la Bwana wetu Yesu Kristu kila wakati kwa injili iliyo hai.
Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino
(Angalia siku ya kwanza)
Tuombe: Baba mwenye upendo, tunakushukuru kwa zawadi ya Mt. Augustino uliyolipatia Kanisa lako. Kwa maombezi yake, sisi tunakuomba mwanga na ujasiri wa kujitoa bila masharti kwa unyenyekevu na daima katika huduma kwa wengine hasa wenye shida mbalimbali katika mahitaji ya mwili na ya roho. Tunaomba hayo, kwa njia ya Kristu Bwana wetu, Amina.
Baba yetu……, Salamu Maria….., Atukuzwe Baba……
Siku ya nane – utayari katika kulisaidia kanisa letu
Kwa Jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina.
Jumuiya ni kiini cha Kanisa la leo, kama ilivyokuwa wakati wa mitume, wakifundishwa na mitume. Kama Jumuiya za kwanza za wakristu, tunaalikwa nasi leo tuwe na utayari katika kulisaidia Kanisa letu kwa njia mbalimbali hasa kwa kutoa zaka kwa wakati. Wakati huohuo pia tuelewe kuwa Roho Mtakatifu anatupatia vipaji na karama kuendana na mahitaji ya Kanisa lake, na hivyo tusisahau kushirikisha karama na vipaji hivyo kanisani kwetu ili kuujenga mwili wa Kristu. Kwa njia hiyohiyo, kazi zetu za kitume ziendane na mahitaji ya Kanisa letu leo hii kwani yote tunapewa na Roho wa Mungu kwa ajili ya utumishi kwa wengine. Je, shughuli zetu kama Jumuiya zinaendana na mahitaji ya Kanisa la Mungu kwa wakati huu? Ni mabadiliko gani tunaitwa kuyafanya kama Jumuiya na kama mtu mmoja mmoja ili kuboresha Kanisa kupitia Jumuiya yetu?
Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino
(Angalia siku ya kwanza)
Tuombe: Baba mwema, tunakuheshimu na kukutukuza kwa kutupatia Mt. Augustino. Tukiwa tumejiweka chini ya mafundisho yake, tunaomba neema na maongozi yako ili tuweze daima kuwa na utayari wa kulisaidia Kanisa letu kwa njia ya zaka na majitoleo kadri ya mahitaji, na utujalie neema tunazokuomba kwa njia ya Yesu Kristu, Bwana na Mwokozi wetu. Amina.
Baba yetu……, Salamu Maria….., Atukuzwe Baba……
Siku ya tisa – utayari wa kuwasaidia wenzetu
Kwa Jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina.
Mt. Augustine daima alikuwa tayari kuwasaidia wahitaji. Alitoa kila alichoweza vikiwemo vile vitu alivyotengewa kwa ajili ya matumizi yake yeye mwenyewe, na alipokosa kitu zaidi cha kutoa, aliyeyusha baadhi ya vyombo vya dhahabu vilivyokuwa vimewekwa wakfu kwa ajili ya kuuza na kisha aliwagawia maskini pesa iliyopatikana. Nasi mara nyingine inawezekana hatuna pesa mfukoni za kuwapa wale wanaohitaji tuwasaidie, lakini bila shaka tuna vitu. Mazao ya mashambani, mifugo, na vitu aina mbalimbali alivyotujalia Mungu. Kwa hiyo kila mmoja wetu ana kitu anachoweza kumpa mwenzake, pengine kama sina chochote zaidi angalau nina muda wa kusali na kuwaombea wengine kuendana na mahitaji ya Jumuiya yetu, au kuwatembelea wapweke, wenye majonzi na kuwafariji wengine. Cha msingi ni kumtazama Kristu, ambaye ana njaa na anateseka, ndani ya wenzetu.
Tunafanya vyema kushikamana na maskini. Sio maskini wa mali na pesa tu tunazungumzia hapa, bali pia maskini wa kiroho, wale wanaohitaji kuelekezwa, wenye mashaka, wapweke, wagonjwa, na wanaoteseka na dhambi. Tumwombe Mungu ili tuimarike kiroho, maana tutaweza kuwasaidia hao maskini tu pale ambapo sisi wenyewe tuna utajiri wa kiroho, yaani tunaye Kristu ndani mwetu.
Tunapomalizia Novena yetu ya siku tisa, tutafakari kuwa, kama Mt. Augustino angekuwa hai leo, angewajibika namna gani, angewasaidiaje maskini walioko katika Jumuiya yetu, mahali petu pa kazi na hata katika familia zetu?
Litania kwa heshima ya Mtakatifu Augustino
(Angalia siku ya kwanza)
Tuombe: Bwana, tunakuomba urejeshe upya katika Kanisa lako roho kama ile uliyompa Mt. Augustino. Kwa mfano wake, tujazwe na kiu ya kukupata wewe peke yako kama chemchem ya hekima na chanzo cha upendo wa milele ili tuwe na utayari wa kuwasaidia wenzetu wote wenye shida za aina mbalimbali. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristu Bwana wetu. Amina.
Baba yetu……, Salamu Maria….., Atukuzwe Baba……
Litani ya Bikira Maria
- Bwana utuhurumie
- Bwana utuhurumie
- Kristo utuhurumie
- Bwana utuhurumie
- Bwana utuhurumie
- Kristo utusikie
- Kristo utusikilize
- Mungu Baba wa Mbinguni,…… Utuhurumie
- Mungu Mwana Mkombozi wa dunia ……… Utuhurumie
- Mungu Roho Mtakatifu …….. Utuhurumie
- Utatu Mtakatifu Mungu Mmoja …….. Utuhurumie
- Maria Mtakatifu ………. utuombee
- Mzazi Mtakatifu wa Mungu …….. utuombee
- Bikira Mtakatifu Mkuu wa Mabikira …….. utuombee
- Mama wa Kristo ……… utuombee
- Mama wa Neema ya Mungu ………….. utuombee
- Mama Mtakatifu sana ……… utuombee
- Mama mwenye usafi wa Moyo ……….. utuombee
- Mama mwenye ubikira ……….. utuombee
- Mama usiye na doa ……….. utuombee
- Mama mpendelevu ………. utuombee
- Mama mstajabivu ………. utuombee
- Mama wa Muumba ………. utuombee
- Mama wa Mkombozi ………….. utuombee
- Mama wa Kanisa……….. utuombee
- Bikira mwenye utaratibu ………….. utuombee
- Bikira mwenye heshima ………….. utuombee
- Bikira mwenye sifa ………….. utuombee
- Bikira mwenye uwezo ………….. utuombee
- Bikra mweye huruma ………….. utuombee
- Bikra mwaminifu………….. utuombee
- Kioo cha haki ………….. utuombee
- Kikao cha hekima ………….. utuombee
- Sababu ya furaha yetu ………….. utuombee
- Chombo cha neema ………….. utuombee
- Chombo cha kuheshimiwa ………….. utuombee
- Chombo bora cha ibada ………….. utuombee
- Waridi lenye fumbo ………….. utuombee
- Mnara wa Daudi ………….. utuombee
- Mnara wa pembe ………….. utuombee
- Nyumba ya dhahabu ………….. utuombee
- Sanduku la Agano ………….. utuombee
- Mlango wa Mbingu ………….. utuombee
- Nyota ya asubuhi ………….. utuombee
- Afya ya wagonjwa ………….. utuombee
- Kimbilio la wakosefu ………….. utuombee
- Mtuliza wenye huzuni ………….. utuombee
- Msaada wa waKristo ………….. utuombee
- Malkia wa Malaika ………….. utuombee
- Malkia wa Mababu ………….. utuombee
- Malkia wa Manabii ………….. utuombee
- Malkia wa Mitume ………….. utuombee
- Malkia wa Mashahidi ………….. utuombee
- Malkia wa Waungama dini ………….. utuombee
- Malkia wa Mabikira ………….. utuombee
- Malkia wa Watakatifu wote ………….. utuombee
- Malkia uliyepalizwa Mbinguni ………….. utuombee
- Malkia wa Rozari takatifu ………….. utuombee
- Malkia wa amani ………….. utuombee
- Mwanakodoo wa Mungu uondoaye dhambi za dunia,…………..Utusamehe ee Bwana.
- Mwanakondoo wa Mungu uondoaye dhambi za dunia,…………..Utusikilize ee Bwana
- Mwanakondoo wa Mungu uondoaye dhambi za dunia,…………..Utuhurumie.
- Utuombee, Mzazi Mtakatifu wa Mungu,…………..Tujaliwe ahadi za Kristo.
Tuombe
Ee Bwana Mungu, utujalie sisi watumishi wako afya ya roho na mwili siku zote; na kwa maombezi matukufu ya Maria Mtakaatifu Bikira daima, tuopolewe na mashaka ya saa, tupate na furaha za milele. Kwa Kristo Bwana wetu, Amina.
SALA YA JIONI
TUNAKUSHUKURU, EE MUNGU KWA MAPAJI YOTE ULIYOTUJALIA LEO AMINA
BABA YETU……………….. SALAMU MARIA……………….
SALA YA IMANI…….YA MATUMAINI………YA MAPENDO
SALA YA KUTUBU
TUWAZE KATIKA MOYO WETU MAKOSA YA LEO TULIYOMKOSEA MUNGU KWA MAWAZO,KWA MANENO, KWA VITENDO NA KWA KUTOTIMIZA WAJIBU (HUSUBIRI KIDOGO)
NAKUUNGAMIA MUNGU MWENYEZI,NANYI NDUGU ZANGU,KWANI NIMEKOSA MNO KWA MAWAZO,KWA MANENO,KWA VITENDO NA KWA KUTOTIMIZA WAJIBU,NIMEKOSA MIMI,NIMEKOSA SANA.NDIYO MAANA NAKUOMBA MARIA MWENYE HERI,BIKIRA DAIMA,MALAIKA NA WATAKATIFU WOTE,NANYI NDUGU ZANGU,MNIOMBEENI KWA BWANA MUNGU WETU.
MUMNU MWENYEZI ATUHURUMIE ATUSAMEHE DHAMBI ZETU,ATUFIKISHE KWENYE UZIMA WA MILELE.AMINA
SALA YA KUOMBEA WATU……………………
KUSIFU……………………






































































I’m so happy you’re here! 🥳







Recent Comments