Dondoo za Mapishi na Lishe

Jinsi ya kutengeneza biskuti za Matunda Makavu Na Cornflakes

VIAMBAUPISHI

Unga – 4 Vikombe

Sukari – 1 Kikombe

Baking powder 1 kijiko cha chai mfuto

Siagi – 454 gms

Mayai – 2

Matunda makavu (tende, zabibu, lozi) – 1 Kikombe

Vanilla – 2 Vijiko vya chai

Cornflakes – ½ kikombe

JINSI YA KUANDAA

Changanya sukari na siagi katika mashine ya keki (cake mixer) mpaka iwe laini (creamy)
Tia yai moja moja huku unachanganya mpaka iwe laini kama sufi. (fluffy)
Tia unga, baking powder, matunda makavu, changanya na mwiko.
Chota mchanganyiko wa biskuti kwa mkono kama (kiasi cha kijiko kimoja cha supu) fanya duara na uchovye katika cornflakes iliyopondwa kwa mkono (crushed)
Zipange katika treya ya kupikia na zipike (bake) katika moto wa 375°F kwa muda wa kiasi dakika 15 huku unazitazama tazama.

Jinsi ya kupika Mgagani

Viamba upishi

Mgagani mkono 1
Mafuta vijiko vikubwa 4
Karanga zilizosagwa kikombe ½
Maji kikombe 1
Kitunguu 1
Karoti 2
Maziwa kikombe 1
Chumvi kiasi

Hatua

• Chambua mgagani, oshana katakata.
• Chemsha maji, weka chumvi kisha ongeza mgagani, funika zichemmke kwa
• dakika 5-10.
• Menye osha na katakata kitunguu.
• Osha, menya na kwaruza karoti.
• Kaanga karanga, ondoa maganda na saga.
• Kaanga vitunguu na karoti mpaka zilainike ukikoroga.
• Weka mgagani uliochemshwa koroga sawasa na funika kwa dakika 5 zilainike.
• Changanya maziwa na karanga ongeza kwenye mgagani ukikoroga kasha punguza moto kwa dakika 5 ziive.
• Onja chumvi na pakua kama kitoweo.

Jinsi ya kupika Pilau ya Nyama ya Kusaga Na Mboga Mchanganyiko

Mahitaji

Mchele – 2 Mugs

Viazi – 3

Nyama ya Kusaga – 1 Pound

Mboga mchanganyiko za barafu – 1 Mug

(Frozen vegetable)

Kitunguu saumu(thomu/galic) na tangawizi – 2 vijiko vya supu

Garam masala – 1 kijiko cha supu

Nyanya – 1

Kitungu maji – 1

Mdalasini nzima – 1 vijiti

Karafuu – 3 chembe

Pilipili mbichi – 1

Chumvi – kiasi

Maji – 2 ½ Mugs

Mafuta – 3 vijiko vya supu

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Osha mchele na uroweke kiasi kutegemea aina ya mchele.
Katakata viazi kaanga katika mafuta, toa weka kando.
Tia mafuta katika sufuria, kaanga kitunguu maji mpaka kigeuke rangi ya hudhurungi (brown).
Tia nyama ya kusaga, thomu na tangawizi, pilipili, bizari zote na chumvi. Kaanga hadi nyama iwive.
Katakata nyanya uliyokatakata itie katika mchanganyiko wa nyama na endelea kukaanga kidogo tu.
Tia mboga ya barafu (frozen vegetables)
Tia maji, kidonge cha supu.
Yatakapochemka tia mchele.
Punguza moto uwe mdogo funika kwa muda wa ½ saa hadi wali ukauke na uwive. Utakuwa tayari kuliwa.

Mapishi ya Mandazi Matamu

Mahitaji

Unga wa ngano (nusu kilo)
Sukari (Kikombe 1 cha chai)
Chumvi (nusu kijiko cha chai)
Hamira (kijiko kimoja cha chai)
Yai (1)
Maziwa ya unga (vijiko 2 vya chakula)
Butter (kijiko 1 cha chakula)
Hiliki (kijiko1 cha chai)
Maji ya uvuguvugu ya kukandia
Mafuta ya kuchomea

Matayarisho

Tia unga kwenye bakuli kisha tia sukari, chumvi, yai, maziwa ya unga, butter na hiliki kisha uchanganye pamoja mpaka mchanganyiko wote uchanganyike vizuri. Baada ya hapo tia maji ya uvuguvugu kiasi na uanze kuukanda. Ni vizuri ukaukanda kwa muda wa dakika 15 ili kuhakikisha donge lote la unga limelainika vizuri.
Baada ya hapo Tawanyishaa unga uliokwandwa katika madonge 4. Tia unga wa ngano kidogo katika kibao cha kusukumia na uanze kusukuma donge moja katika shape ya chapati na hakikisha haiwi nyembamba sana wala nene sana yani inatakiwa iwe ya wastani.Ukishamaliza kusukuma unatakiwa ukate shape uipendayo na uyatandaze katika kitu kilichopo flat na kiwe kimenyunyuziwa unga wa ngano ili kuyazuia yasigandie. Rudia hiyo process kwa madonge yote yaliyobakia. Baada ya hapo yaweke mandazi katika sehemu iliyokuwa na joto ili yaweze kuumuka (inaweza kuchukua masaa 3 kuumuka). Yakisha umuka unatakiwa uweke mafuta katika karai la kuchomea. Yakisha pata joto la kiasi unatakiwa utumbukize mandazi na unaze kuyachoma mpaka yawe ya brown. Yakisha iva yaipue na uyaweke kwenye kitchen towel iliyakauke mafuta. Yakisha poa yatakuwa tayari kwa kuliwa.

Mapishi – Fish Finger

Leo tunaangalia mapishi ya fish finger ( sijui kama unaweza kusema kidole cha samaki)!, Ni mlo mzuri hasa kuliwa kama kitafunio au mboga ya pembeni.

Mahitaji

500g Fileti ya samaki
120g Chenga za mkate
100g Unga wa ngano
Mayai 2
Ndimu 1
Kitunguu saumu 1
Kotmiri
Mafuta ya kupikia

Matayarisho

Menya vitunguu saumu kisha visage

Katakata fileti kwa muundo wa mraba (kama vidole) kisha paka mchanganyiko wa vitunguu saumu

Kata ndimu na kamulia kwenye fillet yako

Weka chenga za mkate kwenye bakuli kisha uchanganye chumvi kiasi na kata kata kotmiri majani 3 na uchanganye pamoja.

Kwenye bakuli lingine weka mayai na uyapigepige yawe kama uji mzito

Weka unga kwenye bakuli jingine.

Chukua kipande cha fillet kiweke unga kidogo kisha kizamishe kwenye yai na baada ya hapo kizamishe kwenye mchanganyiko wa chenga za mkate. Fanya hivyo kwa vipande vyote.

Weka mafuta kwenye kikaago na subiri yachemke kisha weka fillet zako vizuri na zikaange pande zote hadi zimekuwa rangi ya brown ( hakikisha moto sio mkali sana).

Epua na weka pembeni mafuta yote yakauke

Weka kwenye sahani tayari kwa kula.

Jinsi ya kutengeneza saladi

Mahitaji

Tango 1/2
Kitunguu 1/2
Cherry tomato 8
Lettice kiasi
Green olives kidogo
Black olives kidogo
Hoho jekundu 1
Carrot
Giligilani kidogo

Salad dressing
Yogurt 1/2 kikombe
Swaum 1/2 kijiko cha chai
Limao 1/2
Pilipili ya unga 1/4 kijiko cha chai
Chumvi kidogo
Olive oil kiasi

Matayarisho

Osha vitu vyote kisha vikaushe maji. Baada ya hapo ktk bakuli kubwa katakata, lettice, tango,hoho, kitunguu,giligilani na kisha ikwangue carrot na utie bila kusahau nyanya zote pamoja na olives.Baada ya hapo ichanganye vizuri, kisha tengeneza salad dressing kwa kuchanganya vitu vyote vilivyo (kwenye list ya salad dressing) kisha koroga vizuri.Baada ya hapo ichanganye na salad.Na hapo salad yako itakuwa tayari kwa kuliwa. Unaweza kuila na chochote upendacho kama vile chips, nyama choma au au chakula kikuu.

Mapishi ya Viazi vya nyama

Mahitaji

Viazi (potato) 1 kilo
Nyama ya ng’ombe 1/2 kilo
Nyanya ya kopo iliyosagwa 1/2 tin
Vitunguu maji 2
Tangawizi/ swaum 1 kijiko cha chai
Hoho 1
Curry powder 1 kijiko cha chai
Pilipili ya unga 1/2 kijiko cha chai
Limao 1/2
Chumvi
Coriander
Mafuta ya kupikia

Matayarisho

Safisha na katakata nyama ktk vipande vidogovidogo kisha weka pembeni. Baada ya hapo kaanga vitunguu mpaka viwe vya brown kisha tia nyama, swaum/ tangawizi, chumvi na limao. Ichanganye vizuri kisha funika na uipike mpaka iive na maji yote yakauke yani yabaki mafuta tu. Baada ya hapo tia viazi vilivyokatwa vipande vya wastani vikaange kwa muda wa dakika 10 kisha tia pilipili na curry powder na nyanya. Funika na punguza moto.Pika mpaka nyanya iive vigeuze kisha tia vimaji kidogo vya kuivishia viazi. Viazi vikikaribia kuiva(hakikisha vinabaki na rojo kidogo) tia hoho na upike kwa muda wa dk 5 kisha malizia kwa kutia coriander. Changanya vizuri kisha ipua na viazi vyako vitakuwa tayari kwa kuliwa.

Mapishi ya Ugali Kwa Mchuzi Wa Kamba Wa Nazi, Kisamvu Na Kachumbari Ya Papa Mkavu

Vipimo – Ugali

Maji – 4 vikombe kiasi inategemea na unga wenyewe.

Unga wa sembe – 2 vikombe

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Tia maji kiasi katika sufuria, weka motoni, yakipata moto korogea unga wa sembe kiasi na ufanye uji mzito uache uchemke vizuri huku ukikoroga.
Chota kibakuli kimoja cha uji huo weka pembeni kisha mimina unga wote uliobaki upigepige uchanganyike vizuri kwenye uji huo mpaka ushikamane
Punguza moto anza kuusonga taratibu huku ukiongeza ule uji ulioweka pembeni kidogo kidogo mpaka uone sasa umeshikamana vizuri.
Endelea kusonga mpaka ulainike kisha mimina kwenye bakuli au sahani iliyolowanishwa na maji kisha upete pete huku ukiugeuza geuza mpaka ukae shepu nzuri ya duara.Weka tayari kwa kuliwa.

Vipimo – Mchuzi wa kamba wa nazi

Kitunguu – 1

Nyanya – 2

Kamba waliomenywa – 1 Kilo

Pilipili mbichi iliyosagwa – ½ kijiko cha chai

Kitunguu saumu na tangawizi ilivyosagwa – 1 kijiko cha supu

Nazi nzito iliyochujwa – 1 kikombe

Bizari ya mchuzi – ½ kijiko cha chai

Chumvi – Kiasi

Ndimu – Nusu

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Safisha na osha kamba vizuri kisha mtie katika sufuria. Katia kitunguu, nyanya, tia chumvi, pilipili mbichi ya kusaga, thomu na tangawizi, bizari ya mchuzi na ndimu. Tia maji kidogo kiasi acha ichemke.
Watakapoiva na karibu kukauka, mimina tui la nazi taratibu koroga kiasi
Punguza moto aacha ichemke kidogo ukiwa mchuzi tayari.

Vipimo – Kisamvu

Kisamvu – 2 vikombe

Kunde mbichi zilizochemshwa – 1 kikombe

Kitunguu – 1

Nazi nzito iliyochujwa – 1 vikombe

Chumvi – Kiasi

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Weka kisamvu katika sufuria, katia kitunguu, tia chumvi, maji kidogo acha kichemke.
Huku ikichemka mimina kunde mbichi zilizochemshwa acha zipikikie kidogo mpaka kisamvu kikaribie kukauka na kunde kuiva.
Mimina nazi nzito punguza moto acha ichemke kidogo, mimina kwenye bakuli tayari kwa kuliwa.

Vipimo – Kachumbari Ya Papa

Papa mkavu (au nguru) – kipande

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Muoshe papa vizuri atoke mchanga kisha mchome kwenye jiko la mkaa au unaweza kumtia kwenye treya kisha kwenye oven kwa moto wa 350 kwa dakika 15 mpaka 20.
Akikauka mchambue chambue weka kando.
Tengeneza kachumbari, kwa kukata kitunguu, nyanya na pilipili mbichi, tia ndimu na chumvi.
Changanya na papa mkavu uliyemchambu ikiwa tayari.

Jinsi ya kutengeneza Slesi Za Chokoleti Na Karameli

VIAMBAUPISHI

Unga – 1 Magi (vikombe vya chai)

Sukari ya browni – ½ Magi

Siagi iliyoyayushwa – 125 g

Nazi iliyokunwa – ½ Magi

MJAZO WA KARMEL (Caramel filling)

Syrup – 1/3 kikombe cha chai

Siagi iliyoyayushwa – 125 g

Maziwa matamu ya mgando – 2 vikopo (condensed milk)

MJAZO WA CHOKOLETI (Chocolate filling)

Chokoleti – 185 g (dark chocolate)

Mafuta – 3 Vijiko vya chai

MAANDALIZI

Changanya unga, sukari, siagi na nazi iliyokunwa kwenye bakuli mpaka unga ushikamane.
Paka mafuta treya ya kuchomea kisha utandaze kwenye treya ya 20cm kwa 30 cm au (8 in kwa 12 in) unaweza kuweka karatasi ya kuchomea chini ukipenda.
Choma kwenye moto 325˚C kwa muda wa dakika 15 mpaka 18 au mpaka ibadilike kuwa rangi ya browni.
Kwenye sufuria ndogo tia syrup siagi na maziwa matamu ya mgando na changanya kwa moto mdogo mpaka uwe mzito kasha mimina juu ya keki uliyochoma na choma tena kwa muda wa dakika 20 mpaka karameli iwe rangi ya dhahabu.
Kwenye sufuria ndogo nyingine tia vipande vya chokoleti na mafuta na ukoroge kwa moto mdogo mpaka iyayuke kisha wacha ipoe kidogo mimina juu ya mjazo wa karameli kisha weka kwenye friji mpaka ishikamane.
Kata vipande weka kwenye sahani tiyari kwa kuliwa

Jinsi ya kupika Biskuti Za Tende

Viamba upishi

Unga 4 Vikombe vya chai

Sukari ya laini (icing sugar) 1 Kikombe cha chai

Baking powder 2 Vijiko vya chai

Mayai 2

Siagi au margarine 1 Kikombe cha chai

Vanilla 1 Kijiko cha chai

Maziwa ya kuchanganyia kiasi

Tende iliyotolewa koko 1 Kikombe

ufuta (sasame) kiasi 1/4 kikombe

Jinsi ya kuandaa na kupika

1. Changanya unga, siagi, baking powder, na sukari katika mashine.

2. Kisha tia mayai, vanilla na halafu maziwa kidogo kidogo hadi mchanganyiko ushikamane.

3. Gawanya madonge mawili na usukume kama chapati, lakini sio nyembamba sana.

4. Tandaza tende robo ya duara na unyunyize ufuta duara zima: kisha kunja hadi mwisho na ukate kate, kisha upange katika trei ya kuvumbika.

5. Vumbika (bake) moto wa 350°F kwa muda wa dakika 20 au hadi vigeuke rangi na viwive.

6. Zikisha iiva ziache zipowe na zitakuwa tayari kuliwa.

Jinsi ya kutengeneza Fagi Ya Kumumunyuka Mdomoni

VIAMBAUPISHI

Maziwa mazito matamu (condensed milk) – 2 vibati

Sukari – 1 kikombe

Samli 1 ½ kikombe

Vanilla 2 kifuniko cha chupa yake

Hiliki ilosagwa – 2 vijiko vya chai

Sinia kubwa ya bati Paka samli

MAANDALIZI

Changanya maziwa, sukari na samli katika sufuria isiyogandisha chakula (non-stick) uweke katika moto.
Koroga huku ikipikika hadi ianze kugeuka rangi na kuanza kuachana. Usiache mkono kuroga isije kufanya madonge.
Tia hiliki na vanilla, endelea kuipika.
Itakapogeuka rangi vizuri mimina katika sinia na haraka uitandaze kwa mwiko huku ukiuchovya katika maji na kuendelea kuitandaza hadi ikae sawa kote.
Pitisha kisu kuikataka ili ikipoa iwe wepesi kuitoa vipande.

Kila inapozidi kupoa na kukaa ndipo fagi inakauka na kumumunyuka.

Tofauti kati ya yai la kuku wa kienyeji na la kuku wa kisasa

Kilishe mayai yote ni sawa. Virutubishi vinavyopatikana kwenye yai la kuku wa kienyeji kama protini, vitamini A, madini ya chuma na virutubishi vya aina nyingine, ndivyo hivyo vinavyopatikana pia kwenye yai la kuku wa kisasa.

Tatizo linaweza kutokea pale ambapo wafugaji wa kuku wa kisasa hawafuati taratibu za ufugaji na pengine hawawapi kuku vyakula muhimu wanavyohitaji au wanawapa dawa na vyakula visivyo bora kiafya, hivyo wakati mwingine kiini cha yai la kuku wa kisasa huonekana kupungua rangi ya njano kuliko kiini cha yai la kuku wa kienyeji.

Mtu anashauriwa kula yai bila kujali ni la kuku gani, kwa kutegemea ni yai lipi linapatikana kwa urahisi. Lakini nivizuri kula mayai ambayo yapo salama.

Mapishi ya wali mtamu Wa Nazi Kwa Maharage Na Samaki Nguru Wa Kukaanga

Vipimo

Wali:

Mchele mpunga – 4 Vikombe

Tui la nazi – 6 vikombe

Chumvi – kiasi

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Osha mchele weka kando.
Bandika tui jikoni likichemka tia mchele na chumvi.
Funika uchemke, tui likikauka wacha moto mdogomdogo hadi wali uive ukiwa tayari. Ikiwa unatumia mkaa unapalia juu yake.

Maharage Ya Nazi

Maharage – 3 vikombe

Tui la nazi zito – 1 kikombe

Tui la nazi jepesi – 1 kikombe

Kitunguu maji – 1

Kitunguu saumu(thomu/galic) kilosagwa -1 kijiko cha chai

Chumvi – kiasi

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Chemsha maharage mpaka yaive.
Katiakatia kitunguu maji na tia thomu, tia na tui jepesi kikombe kimoja.
Tia tui zito endelea kuweka katika moto mdogomdogo hadi yakaribie kukauka yakiwa tayari.

Samaki Nguru Wa Kukaanga

Samaki Wa Nguru – 4 vipande

Kitunguu saumu(thomu/galic) & tangawizi ilosagwa – 1 kijiko cha supu

Pilipili mbichi – 4

Ndimu – 2 kamua

Bizari ya samaki -1 kijiko cha chai

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Mwoshe samaki kisha mtie kitunguu thomu, tangawizi ilosagwa, chumvi, pilipilimbichi ilosagwa, ndimu na bizari ya samaki.
Mwache akolee viungo kwa muda kidogo.
Makaange katika mafuta hadi aive akiwa tayari.

Mapishi ya Chapati za Kusukuma kitaalamu

Mahitaji

Unga wa ngano (plain flour 1/2 of kilo)
Siagi (butter vijiko 2 vya chakula)
Yai (egg 1)
Chumvi (1/2 ya kijiko cha chai)
Hiliki (ground cardamon 1/4 ya kijiko cha chai)
Maji ya uvuguvugu (warm water)
Mafuta (vegetable oil)

Matayarisho

Weka unga wa ngano katika bakuli la kukandia, kisha tia chumvi na hiliki na uchanganye kwanza, baada ya hapo tia siagi na uichanganye vizuri na unga mpaka ipotee. Baada ya hapo tia tena yai na uchanganye vizuri. Mchanganyiko ukishachanganyika vizuri sasa unaweza kutia maji ya uvuguvugu kidogo, kidogo huku ukiwa unauchanganya ili kupata donge. Baada ya hapo anza kukanda hilo donge mpaka mabuje yote yapotee na unga uwe mlaini, ambapo itakuchukua kama dakika 15. Baada ya hapo tawanyisha unga katika madonge ya wastani (yasiwe makubwa sana au madogo sana) Ukimaliza hapo, andaa kibao cha kusukumia chapati kwa kukitia unga kidogo ili chapati isinatie kwenye kibao. Sukuma donge moja la chapati mpaka liwe flat na kisha weka kijiko kimoja cha mafuta na usambaze. ukisha maliza ikunje (roll). Fanya hivyo kwa madonge yote yaliyobakia.
Baada ya hapo andaa chuma cha kuchomea (fry-pan) katika moto wa wastani. Kisha anza kusukuma chapati (ni vizuri ukaanza na zile ulizozikunja mwanzo ili kuzipa nafasi zile za mwisho ziweze kulainika) ukiwa unasukuma hakikisha zinakuwa flat (na zisiwe nene sana au nyembamba sana) Ukishamaliza hapo tia kwenye chuma cha kuchomea. Acha iive upande mmoja then igeuze upande wa pili. Tia mafuta ama kijiko kimoja kikubwa upande wa chini wa chapati na uanze kuukandamiza kwa juu uku ukiwa unaizungusha. fanya hivyo uku ukiwa unaigeuza kuiangalia kwa chini ili isiungue. ikishakuwa ya brown, geuza upande wa pili na urudie hivyohiyvo mpaka chapati iive. Rudia hii process kwa chapati zote zilizobakia.

Siri ya chapati kuwa laini ni kutia siagi au mafuta ya kutosha kipindi unazikanda na pia kuzikanda mpaka unga uwe laini.

Mapishi ya Supu Ya Maboga

Viamba upishi

Blue band vijiko vikubwa 2
Maziwa vikombe 2
Royco kijiko kikubwa 1-2
Pilipili manga (unga) kijiko cha 1
Chumvi kiasi Maji lita 2-3
Boga kipande ½
Viazi mviringo 2
Vitunguu 2
Karoti 2
Nyanya 2

Hatua

• Menya boga, viazi, karoti, nyanya na kwaruza weka kwenya sufuria kubwa.
• Menya, osha na katakata vitunguu kisha ongeza kwenye mboga.
• Ongeza maji na chumvi chemshwa mpaka vilainike.
• Pekecha ikiwa jikoni na moto kidogo
• Ongeza blue band, maziwa royco na pilipili manga ukikoroga kwa dakika 5.
• Onja chumvi na pakua kama supu.
Uwezekano
Tumia siagi badala ya margarine.

Jinsi ya kutengeneza Biriani Ya Nyama Ya Ng’ombe

Mahitaji

Nyama – 2 Ratili (LB)

Chumvi – kiasi

Mafuta – 1 Kikombe

Samli – ½ Kikombe

Kitungu (Kata virefu virefu) – 3 Vikubwa

Nyanya (kata vipande) – 2

Nyanya kopo – 1 Kijiko cha chakula

Kitunguu saumu(thomu/galic) – 1 Kijiko cha chakula

Tangawazi – 1 Kijiko cha chakula

Pilipili mbichi iliyosagwa – 1 Kijiko cha chai

Pilipili ya unga nyekundu – ½ Kijiko cha chai

Kotmiri iliyokatwa – 2 Vijiko vya chakula

Viazi – 6

Gram masala – 1 Kijiko cha chai

Mtindi – ¼ Kikombe cha chai

Namna Ya kutaarisha Na Kupika

1. Kwenya karai au (sufuria) mimina mafuta na samli. Yakishapata moto mimina vitunguu vikaange mpaka viwe rangi ya hudhurungi. Vitowe viweke pembeni.
2. Kaanga viazi na viweke pembeni.
3. Chukua sufuria tia nyama, thomu, tangawizi, pilipili, nyanya, nyanya ya kopo, mtindi, na pilipili ya unga. Chemsha mpaka iive.
4. Tia vile vitungu ulioyovikaanga, tia viazi, gram masala, kotmiri na yale mafuta uliokaangia vitunguu kama ¼ kikombe, acha moto mdogo mdogo kama ¼ saa, epua weka pembeni.

Vipimo Vya Wali

Mchele – 5 Magi (Kikombe kikubwa)
Hiliki nzima – 4
Mdalasini mzima – 1
Zafarani – ½ kijiko cha chai
Rangi ya biriani – ¼ Kijiko cha
Mafuta yaliyokaangiwa vitunguu – ½ Kikombe
Chumvi – kiasi
Roweka zafarani na rangi kwenye kikombe na ¼ kikombe cha maji. Roweka kabla ya robo saa.

Namna Ya Kutaarisha

Osha mchele uroweke kwenye maji muda wa dakika 20.
Chemsha maji kwenye sufuria kama magi 10.
Tia hiliki na mdalasini.
Yakishachemka unatia mchele,chemsha usiive sana, unamwaga maji.
Unamimina tena ule mchele ½ yake kwenye sufuria, unatia rangi na zafrani kidogo, halafu unamimina
mchele uliyobakia unatia rangi iliyobakia.
Mafuta yake unayachemsha mpaka yachemke unamimina juu ya mchele, unarudisha motoni unaweka
moto mdogo ukisha kuiva, tayari kupakuliwa.
Unapakuwa wali unaweka chini kwenye sahani na juu yake sosi ya nyama

Jinsi ya kupika Viazi Vya Nazi Kwa Nyama

Mahitaji

Viazi – 3lb

Nyama – 1lb

Kitunguu – 1

Nyanya – 2

Kitunguu saumu(thomu/galic) – 1 kijiko cha chai

Manjano – ½ kijiko cha chai

Curry powder – ½ kijiko chai

Nyanya kopo – 1 kijiko cha chai

Pilipili ya unga – kiasi upendavyo

Chumvi – kiasi

Kidonge cha supu – 1

Tui la nazi – 1 kopoau zaidi

Mtindi ukipenda – 3 vijiko vya supu

Kotmiri – kiasi ya kupambia

Nazi ya unga – 4 vijiko vya supu

Mafuta – 2 vijiko vya supu

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Kata nyama vipande vipande kisha chemsha na chumvi mpaka iive.
Menya maganda viazi na ukate slice kubwa weka pembeni
Kata kata kitunguu kisha kaanga na mafuta mpaka vibadilike rangi
Tia thomu, bizari ya manjano, pilipili ya unga, nyanya kopo
Kata kata nyanya nzima vipande vidogo tia na kidonge cha supu.
Kisha tia viazi, nyama na tui la nazi finika mpaka viazi viwive lakini visiwe vikavu.
Tia mtindi na nazi ya unga kama vijiko 4 vya supu iache motoni kidogo kisha pakua, tupia kotmiri juu na itakuwa tayari kuliwa.

Jinsi ya kupika Biriani Ya Nyama Mbuzi Ya Mtindi Na Zaafaraan

Vipimo – Nyama

Nyama mbuzi – 1 kilo

Kitunguu menya katakata – 1

Nyanya/tungule – 2

Thomu (kitunguu saumu/garlic) saga – 5 chembe

Tangawizi mbichi – kuna/grate au saga – 1 kipande

Pilipili mbichi saga – 2

Bizari ya pilau nzima (cumin seeds) – ½ kikombe cha kahawa

Mdalasini – 1 kijiti

Karafuu nzima – 5 chembe

Gilgilani/dania (coriander seeds) – ½ kikombe cha kahawa

Bizari ya mchuzi – 1 Kijiko cha supi

Chumvi – Kiasi

Mtindi – 1 glass

Hiliki ilopondwa – 2 vijiko vya chai

Vitunguu – menya katakata slices kwa ajili ya kukaanga- 7- 9

Mafuta – Kiasi ya kukaangai vitunguu

Vipimo – Wali

Mchele wa pishori/basmati – 4 glass

Zaafarani roweka katika kikombe cha kahawa – Kiasi

Mafuta – Kiasi

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Katika sufuria, changanya nyama pamoja, kitunguu kimoja, tangawizi, thomu, nyanya, na viungo vyake isipokuwa mtindi, hiliki na vitunguu vilobakia.

Tia maji kisha funika ichemke mpaka iwive nyama na ikauke supu.

Tia mtindi na hiliki changanya pamoja.

Weka mafuta katika karai, kaanga vitunguu mpaka viwe rangi ya hudhurungi. Toa uchuje mafuta. Kisha viponde ponde kwa mkono uchanganye na nyama.

Chemsha mchele uive nusu kiini, mwaga maji.

Mimina katika nyama utie zaafarani, funika upike wali hadi uwive.

Epua ukiwa tayari.

Jinsi ya kuandaa Biriani Na Sosi Ya Nyama Ya Mbuzi

Mahitaji

Nyama Ya Mbuzi – 1 Kilo

Mchele – 4 Magi

Vitunguu – 3

Nyanya – 2

Nyanya kopo – 3 vijiko vya chai

Kitunguu saumu(thomu/galic) na tangawizi iliyosagwa – 2 vijiko vya supu

Pilipili mbichi iliyosagwa – 1 kijiko cha supu

Garam Masala (mchanganyiko wa bizari) – 2 vijiko vya supu

Hiliki – 1 kijiko cha chai

Chumvi – kiasi

Mafuta – ½ kikombe

Zaafarani au rangi za biriani za kijani na manjano/orenji

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika Sosi Ya Nyama

Changanya nyama na thomu, pilipili, chumvi na nusu ya garam masala. Tia katika treya ya oveni uipike nyama (Bake) hadi iwive. Au iwivishe kwa kuichemsha.
Katika kisufuria kingine, tia mafuta (bakisha kidogo ya wali) kaanga vitunguu hadi vigeuke rangi, kisha tia nyanya, nyanya kopo, bizari zote nyingine zilizobakia.

Namna Ya Kupika Wali

Mchele – 4 magi

Mdalasini – 1 kijiti

Hiliki – 3 chembe

Kidonge cha supu – 1

Chumvi

Osha na roweka mchele wa basmati.
Tia maji katika sufuria uweke jikoni. Tia kidonge cha supu, mdalasini, hiliki na chumvi .
Yakichemka maji tia mchele, funika upike hadi nusu kiini kisha uchuje kwa kumwaga maji.
Tia mafuta kidogo katika mchele na zaafarani iliyorowekwa au rangi za biriani kisha rudisha mchele katika sufuria ufunike na upike hadi uwive.
Pakua wali katika sahani kisha mwagia sosi ya nyama juu yake, pambia kwa kukatika nyanya, pilipili mboga na figili mwitu (Celery) au mboga yoyote upendayo.

Mapishi ya Pasta za cream na uyoga

Mahitaji

Pasta (2 na 1/2 vikombe vya chai)
Uyoga (mashroom 2 vikombe vya chai)
Cream (1 kikombe cha chai)
Mafuta (vegetable oil)
Kitunguu (onion 1)
Chumvi
Majani ya basil (dried basil leaves 1/2 kijiko cha chai)

Matayarisho

Chemsha maji ya kutosha kisha tia chumvi na mafuta kidogo katika hayo maji na baadae tia pasta na uzichemshe mpaka ziive kisha uzichuje maji na uziweka pembeni. Baada ya hapo weka mafuta kidogo katika sufuria kisha tia uyoga uliokatwa na uupike mpaka uive. Baada ya hapo tia majani ya basil, chumvi na cream kisha acha ichemke kisha weka vitunguu na upike kwa muda wa dakika 4 kisha malizia kwa kutia pasta. Zichanganye vizuri na mchanganyiko wote kisha zipike kwa muda wa dakika 5. Na hapo zitakuwa tayari kwa kuliwa.

Unaweza kupika nyama ya kuku (chiken breast) iliyokatwa vipande vidogo vidogo kama saizi na shape ya pasta. Vizuri kuikaanga pembeni mpaka iwe brown na kuiva alafu kuimix kwenye chakula baada ya uyoga na vitunguu kuiva alafu unamix cream kumalizia mapishi.

Shopping Cart
41
    41
    Your Cart
    Kitabu cha SMS Maalumu kwa Umpendaye
    Kitabu cha SMS Maalumu kwa Umpendaye
    1 X Sh2,500 = Sh2,500
    🏠 Home 📖 Reading 🖼️ Gallery 💬 AI Chat 📘 About