Dondoo za Mapishi na Lishe

Jinsi ya kutengeneza Biskuti Za Ufuta Na Jam

VIAMBAUPISHI

Unga vikombe 2

Sukari ya kusaga 1/4 Kikombe

Siagi 250 gms

Jam kisia

Ufuta kisia

Vanilla 1 kijiko cha chai

MAPISHI

Tia kwenye mashine ya kusaga (blender) au mashine ya keki, siagi, yai, sukari na vanilla uchanganye hadi ichanganyike vizuri.
Tia baking powder, na unga na changanya kwa mkono vizuri.
Paka siagi sinia ya kupikia ya oveni.
Tengeneza viduara vidogo vidogo.
Bonyeza kila kiduara katikati kwa kidole, kisha weka jam, halafu juu yake paka mayai na unynyuzie ufuta.
Pika katika moto wa chini 350ºF kwa muda wa dakika 20-25.
Tayari kwa kuliwa.

Mapishi ya Chapati za maji za vitunguu

Mahitaji

Unga wa ngano (plain flour) 1/4
Kitunguu kikubwa (chopped/slice onion) 1
Yai (egg) 1
Chumvi (salt)
Mafuta (cooking oil)

Matayarisho

Tia unga, chumvi na maji kiasi katika bakuli kisha koroga mpaka madonge yote yaondoke. Baada ya hapo tia yai na vitunguu kisha koroga tena mpaka mchanganyiko wote uchanganyike vizuri. baada ya hapo choma chapati zako kama kawaida (jinsi ya kuchoma unaweza kuangalia kwenye recipe yangu ya chapati za maji katika older posts) na baada ya hapo zitakuwa tayari kwa kuliwa.

Mapishi ya Boga La Nazi

Vipimo

Boga la kiasi – nusu yake

Tui zito la nazi 1 ½ gilasi

Sukari ½ kikombe

Hiliki ½ kijiko cha chai

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Menya boga kisha katakata vipande vya kiasi.
Weka katika sufuri tia maji kiasi ya kuchemshia na kuwiva bila ya kubakia maji mengi.
Changanya tui na sukari na hiliki kisha mimina juu ya boga wacha katika moto dakika chache tu bila ya kufunika.
Epua mimina katika chombo likiwa tayari.

Mapishi ya Ugali Kwa Mchuzi Wa Nazi Wa Nyanya Chungu/Mshumaa/Ngogwe Na Bamia, Mboga Ya Matembele Na Samaki Wa Kukaanga

Vipimo Vya Ugali

Unga wa mahindi – 4

Maji – 6 kiasi kutegemea na aina ya unga

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Weka maji katika moto.

Tia unga kidogo katika kibakuli, koroga ufanye uji.

Maji yakichemka tia kwenye maji uwe uji.

Ujii ikiiva punguza kidogo tia unga kidogokidogo na usonge ugali. Ikiwa unga ni mgumu utaongeza maji ya ule uji ulopunguza usonge hadi uive ukiwa tayari.

Vipimo Vya Mchuzi Wa Nazi Kwa Nyanya Chungu/Mshumaa/Ngogwe Na Bamia

Nyanya chungu/mshumaa/Ngogwe – 7

Bamia – 10

Kitunguu maji – 2

Nyanya/tungule – 2

Tui la nazi jepesi – 2 viwili

Tui la nazi zito – 2

Chumvi – kiasi

Ndimu – 2 mbili kamua

Bizari manjano/haldi/turmeric – ½ kijiko cha chai

Pilipili mbuzi – 3

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Katakata kitunguu maji na nyanya vipande vidogodogo sana kisha weka katika sufuria.

Iache ichemke kwa maji yake ya nyanya, ikishachemka tia maji kidogo kama robo kikombe.

Tia nyanya chungu, bamia na koleza ndimu, chumvi.

Iache ichemke. Inapokuwa tayari imeiva tia tui jepesi endelea kuacha katika moto huku unakoroga kidogo kidogo.

Tui jepesi likipungua kiasi chake, tia tui zito, kisha usiachie mkono koroga ikichemka kidog kiasi cha kuiva tui mchuzi tayari.

Vipimo Vya Mboga Ya Matembele

Matembele – 5 mafungu

Mafuta – ¼ kikombe

Kitunguu maji kilokatwakatwa – 1

Nyanya/tungule – 4

Chumvi – 1

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Punguza miche ya matembele kwa kuikata ncha kisha osha majani yake. Acha yachuje maji .
Weka mafuta katika sufuria, kaanga kitunguu maji na nyanya hadi viivie.
Tia mboga, Iache ichemke kwa maji yake hadi iive. Ukiona bado haikuiva tia maji kidogo tu.
Ukipenda unatia ndimu kiasi cha kipande kimoja ukamue .

Samaki Wa Nguru Wa Kukaanga

Samaki Wa Nguru – 4 vipande

Kitunguu saumu(thom/galic) na tangawizi ilosagwa – 1 kijiko cha supu

Pilipili mbichi – 4

Ndimu – 2 kamua

Bizari ya samaki – 1 kijiko cha chai

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Mwoshe samaki kisha mtie kitunguu thomu, tangawizi ilosagwa, chumvi, pilipilimbichi ilosagwa, ndimu na bizari ya samaki.
Mwache akolee viungo kwa muda kidogo.
Makaange katika mafuta hadi aive akiwa tayari.

Mapishi ya wali wa hoho nyekundu

Mahitaji

Pilipili hoho (Red pepper 3)
Cougette 1
Kitunguu (onion 1)
Uyoga (mashroom 1 kikombe cha chai)
Carrot 1
Nyanya (fresh tomato 1)
Nyanya ya kopo iliyosagwa (tomato paste 3 vijiko vya chai)
Giligilani (fresh coriander)
Binzari manjano (Turmaric 1/2 ya kijiko cha chai)
Curry powder 1/2 ya kijiko cha chai
Chumvi (salt)
Mafuta (vegetable oil)

Matayarisho

Kata hoho kati na utoe moyo wake kisha ziweke pembeni, Kisha katakata cougette, kitunguu, uyoga, carrot, nyanya katika vipande vidogo vidogo, Weka sufuria jikoni na uanze kupika uyoga kwa muda wa dakika 5, kisha weka curry powder, turmaric na chumvi na kaanga kidogo kisha weka vegetable zilizobakia pamoja na nyanya ya kusaga pamoja na giligilani. Zikaange kwa muda wa dakika 5 kisha zitie kwenye hoho na kisha uzibake kwa muda wa dakika 20 na hapo zitakuwa tayari kuseviwa na wali.
Wali: angalia katika recipe zilizopita

Jinsi ya kupika Eggchop

Mahitaji

Mayai yaliochemshwa 4
Nyama ya kusaga robo kilo
Kitunguu swaum
Tangawizi
Limao
Chumvi
Pilipili
Breadcrambs
Carry powder
Binzari nyembamba ya unga
Yai moja bichi
Mafuta

Matayarisho

Marinate nyama na pilipili, kitunguu swaum, tangawizi, limao, chumvi, carry powder, binzari nyembamba na breadcrambs pamoja. Kisha vunja yai moja bichi kwenye kibakuli na ulikoroge kisha tia kwenye mchanganyiko wa nyama.Gawanisha matonge manne kwa ajili ya kuzungushia kwenye mayai .Chemsha mayai kwa muda wa dakika 20. Yakisha iva acha yapoe na kisha yamenye maganda na uyaweke pembeni. Baada ya hapo chukua yai moja lililochemshwa na ulizungushie donge moja la mchanganyiko wa nyama. fanya hivyo kwa mayai yote yaliobakia. Baada ya hapo paka mafuta kwa nje ya hizo eggchop na kisha paka mafuta kwenye sinia la kuokea na uziokee kwenye oven kwa moto wa kawaida, kwa muda wa dakika 20.Na eggchop zako zitakuwa tayari kwa kuliwa

Jinsi ya kupika Biskuti Ya Keki Kavu kwa kizungu Shortcake

Viamba upishi

Unga 2 Magi (vikombe vya chai)

Sukari iliyosagwa 2/3 Magi (kikombe cha chai)

Siagi   220 g

Unga wa mchele ½ Magi

Yai 1

Vanilla 1 kijiko cha chai

Jinsi ya kuandaa na kupika

1. Changanya vitu vyote hivyo kwenye bakuli mpaka unga ushikamane.

2. Paka mafuta treya ya kuchomea kisha utandaze kwenye treya ya 20cm kwa 30 cm au (8 in kwa 12 in)

3. Choma kwenye moto 325˚C kwa muda wa saa nzima au mpaka ibadilike kuwa rangi ya dhahabu.

4. Epua acha ipoe kisha kata vipande kama mstatili, weak kwenye sahani tayari kunywewa na chai.

Mapishi ya Mchemsho wa ndizi na nyama

Mahitaji

Ndizi mbichi 6
Nyama ya ng’ombe (nusu kilo)
Viazi mviringo 2
Kitunguu swaum
Tangawizi
Kitunguu maji
Nyanya 1 kubwa
Mafuta (vegetable oil)
Chumvi
Limao
Pilipili

Matayarisho

Chemsha nyama na limao, kitunguu swaum, tangawizi chumvi na maji kiasi mpaka nyama iive, Hakikisha unaiacha na supu kiasi kwa ajili ya kuwekea kwenye ndizi.Kisha katakata nyanya na vitunguu na uweke pembeni .Menya ndizi na viazi kisha zichemshe pamoja na vitunguu, nyanya, maji kidogo, mafuta na uhakikishe haziivi kabisa. Baada ya hapo tia nyama na supu yake, pilipili mzima na chumvi na uache uchemke mpaka ndizi na viazi viive.Na baada ya hapo mchemsho wako utakuwa tayari kwa kuliwa

Mapishi ya Ndizi na Nyama Ya Ng’ombe

Mahitaji

Ndizi mbichi – 10-12

Nyama ng’ombe – 1 kilo moja

Kitunguu maji – 2

Nyanya/tungule – 2

Kitunguu saumu(thomu/galic) – 7

Tangawizi mbichi – 1 kipande

Ndimu – 2 kamua

Chumvi – kiasi

Mafuta – 3 vijiko vya supu

Tui la nazi – 3 vikombe

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Saga kitunguu thomu na tangawiz mbichi.
Weka nyama katika sufuria tia kijiko kimoja cha kitunguu thomu na tangawizi, chumvi na ndimu kisha chemsha hadi iive.
Menya ndizi ukatekate
Weka mafuta katika sufuria tia kitunguu maji kilokatwakatwa ukaange kidogo tu kisha tia nyanya/tungule uendelea kukaanga.
Tia tangawizi na thomu ilobakia.
Tia ndizi, kaanga kidogo kisha tia supu ya nyama na nyama yake.
Ziache ndizi ziive zikiwa tayari tia tui la nazi zikiwa tayari.

Mapishi ya Wali, samaki, bilinganya na spinach

Mahitaji

Samaki
Spinach
Bilinganya
Nyanya ya kopo (Kopo 1)
Vitunguu maji
Vitunguu swaumu
Tangawizi
Pilipli mbuzi
Chumvi
Limao
Carry powder
Mchele
Mafuta ya kupikia
Coriander
Hiliki
Amdalasini
Karafuu

Matayarisho

Osha samaki na kisha wamarinate na vitunguu swaumu, tangawizi, limao, chumvi na pilipili kwa muda wa masaa matatu. Baada ya hapo wakaange samaki na uwaweke pembeni kwa ajili ya mchuzi.
Osha spinach na kisha zikatekate na ziweke pembeni
Osha mchele na kisha uloweke kwenye maji kwa muda wa dakika kumi
Osha bilinganya kisha likatekate vipande vidogo dogo

Jinsi ya kupika

Mchuzi

Saga pamoja vitunguu maji, vitunguu saumu, tangawizi, nyanya.Kisha weka mchanganya katika sufuria na uinjike jikoni kwenye moto wa kawaida. Pika mchanganyiko mpaka ukauke kisha tia mafuta, chumvi na carry powder. pika kwa muda wa dakika kumi kisha tia samaki na tui la nazi. Acha mchuzi uchemke mpaka tui la nazi liive.kishaipua na tia coriander

Spinach

Kaanga vitunguu maji na mafuta, baada ya hapo tia spinach na chumvi acha ziive kidogo kisha ipua tayari kwa kuliwa.

Mabilinganya

Kaanga vitunguu maji na mafuta mpaka viwe vya brown kisha tia nyanya. Acha ziive kisha tiai mabilinganya na chumvi. Yakishaiva ipua weka pembeni tayari kwa kuliwa.

Wali

Chemsha maji ya wali kwenye sufuria, kisha tia hiliki, pilipili mtama mzima, karafuu na amdalasini, chumvi na mafuta. Kisha tia mchele na uufunike na uache uchemke mpaka utakapokauka maji. Geuza na uache mpaka uive. Kisha ipua. Tayari kwa kuliwa

Jinsi ya kupika Vileja

VIPIMO

Unga wa mchele 500g

Samli 250g

Sukari 250g

Hiliki iliyosagwa 1/2 kijiko cha chai

Arki (rose flavour) 1/2 kijiko cha chai

Baking powder 1 kijiko cha chai

Mayai 4

Maji ya baridi 1/2 kikombe cha chai

NAMNA YA KUTAYRISHA NA KUPIKA

1. Saga sukari iwe laini kiasi, changanya unga wa mchele, baking powder, hiliki na sukari.

2. Pasha moto samli mpaka iwe nyepesi kama maji mimina kwenye ule mchanganyiko wa unga wa mchele, kisha uchanganye pamoja na arki.

3. Ongeza mayai yaliopigwa endelea kuchanganya mpaka unga umeanza kuchanganyika vizuri.

4. Ongeza maji ya baridi sana kama nusu kikombe tu ili uchanganyike vizuri.

5. Kata kwa design unayotaka viwe vinene visiwe kama cookies za kawaida kama ilivyo kwenye picha na ukipenda utaweka kidoto kwa kutumia zaafarani katikati ya kileja kama inavyoonesha hapo juu.

6. Choma kwa moto wa baina ya 300F na 350F kwa dakika 15 mpaka 20 visiwe vyekundu toa na tayari kwa kuliwa

Mapishi ya Kabichi

Mahitaji

Kabichi 1/2 kilo
Nyanya ya kopo 1/2
Kitunguu 1
Curry powder 1/2 kijiko cha chai
Chumvi
Olive oil

Matayarisho

Kwanza kabisa bandua magada ya juu ya kabichi, kisha ioshe na uikaushe maji baaba ya hapo katakata kabichi (inapendeza zaidi kama ikikatwa nyembamba) kisha saga pamoja nyanya na kitunguu. Baada yahapo tia katika sufuria ya kupikia, ipike mpaka maji yote yatakapokauka kisha tia chumvi, curry powder na mafuta pika kwa muda kiasi kisha tia kabichi na upunguze moto. Pika mpaka kabishi itakapoiva kisha ipua na itakuwa tayari kwa kuliwa. Unaweza kuila kwa wali au ugali.

Mapishi ya Sponge keki

Mahitaji

Unga wa ngano (self risen flour) 100g
Sukari (sugar) 100g
Siagi isiyokuwa na chumvi (unsalted butter) 100g
Mayai (eggs) 2
Vanila 1 kijiko cha chai
Chumvi pinch
Warm water 3 vijiko vya chakula

Matayarisho

Kwanza washa oven moto wa 200 C. Baada ya hapo saga butter na sukari mpaka viwe laini kisha tia mayai na uendelee kusaga mpaka vichanganyike vizuri kisha tia unga, vanila, chumvi na na maji na usage mpaka upate uji usiokuwa mzito sana au mwepesi sana. Baada ya hapo utie kwenye baking tin na u bake kwa muda wa dakika 25 na mpaka cake yako iive yani juu na chini iwe ya brown na ukidumbukiza kijiti katikati kinatoka kikiwa clean. Baada ya hapo itoe kwenye tin na uiache ipoe. Ikisha poa itakuwa tayari kwa kuliwa.

Mapishi ya Pilau Ya Bilingani Na Kuku

Viambaupishi

Mchele wa basmati – 3 vikombe

Kuku – ½

Bilingani – 2 ya kiasi

Viazi – 4

Vitunguu – 2

Kitunguu (thomu/galic) iliyosagwa – 2 vijiko vya supu

Pilipili mbichi iliyosagwa – 2

Chumvi – kiasi

Garama masala (mchanganyiko wa bizari) – 1 kijiko cha chai

Hiliki ya unga – ¼ kijiko cha chai

Mafuta ya kupikia wali – ¼ kikombe

Mafuta ya kukaangia viazi na bilingani – kiasi

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika:

Osha mchele na roweka kwa muda kutegemea na aina ya mchele.
Kata kuku vipande upendavyo safisha
Kisha mchemshe kwa chumvi, pilipili iliyosagwa, thomu, na bizari mchanganyiko (garama masala).
Akiwiva kuku, mtoe weka kando, bakisha supu katika sufuria.
Menya na kata viazi kaanga weka kando.
Kata kata bilingani slesi nene kaanga, chuja mafuta weka kando.
Katika sufuria, kaanga vitunguu hadi vigeuke rangu ya hudhurungi. Tia vipande vya kuku, ukaange kidogo.
Tia supu ya kuku, mchele, tia hiliki, ufunike hadi karibu na kuwiva kabisa.
Tia viazi na bilingani uchanganye kidogo, kisha tia katika oven imalizike kupikika pilau humo au unaweza kuendelea kufunika juu ya jiko hadi pilau iwive.
Pakua katika sahani ikiwa tayari kuliwa kwa saladi ya mtindi.

Namna ya kupika Vitumbua

Vitumbua ni aina ya vitafunwa vya chai ambavyo hutengenezwa kwa kutumia unga wa mchele. Kiasili vitumbua ni chakula ambacho hupendelewa sana na watu wa pwani. Na mara nyingi wamekuwa wakipika kwa kuchanganya na nazi ili kuvifanya view na ladha nzuri zaidi

Mahitaji:

Unga wa mchele ½ kg
Sukari vijiko 4 vya mezani
Tui bubu la nazi
Mafuta ya kupikia
Unga wa hiliki ½ kijiko cha chai
Hamira kijiko 1 cha chai
Chuma cha vitumbua

Maandalizi:

Chukua unga wa mchele na weka kwenye bakuli au sufuria ya kilo moja
Weka hamira kisha weka sukari kisha miminia tui katika mchanganyiko wako
Weka hiliki koroga hadi view uji mzito
Acha uji huo kwa muda wa saa moja hadi uumuke, mara nyingi kuumuka kunategemea na hali ya hewa,
Baada ya hapo weka mafuta kijiko kimoja cha chakula kila kishimo acha yapate moto Kisha kaanga virumbua vyako

Mapishi ya Wali Wa Nazi Kwa Mchuzi Wa Samaki Na Rojo La Bilingani Na Viazi/Mbatata

Wali Wa Nazi

Mpunga – 4 vikombe

Tui la nazi – 6 vikombe

Chumvi – Kiasi

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Osha mchele kisha
Bandika tui jikoni likichemka tia mchele na chumvi.
Funika uchemke, tui likikauka wacha moto mdogomdogo hadi wali uive ukiwa tayari. Ikiwa unatumia mkaa unapalia juu yake.

Mchuzi Wa Samaki Nguru

Samaki – 4

Kitunguu saumu(thomu/galic) na tangawizi – 2 viijiko vya supu

Kitunguu maji kilokatwakawa – 2 slice ndogo

Nyanya/tungule – 4

Nyanya kopo – 3 vijiko vya supu

Pilipili mbichi – 2

Kotmiri ilokatwakatwa – 3 msongo (bunches)

Bizari ya mchuzi (simba 2) – I kijiko cha chai

Ndimu – 1 kamua

Mafuta – ¼ kikombe

Chumvi kiasi

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Katakata samaki mkaange kwa kumtia viungo.
Weka mafuta katika sufuria, kaanga kitunguu. Vinapogeuka rangi thomu na tangawizi mbichi, nyanya, nyanya kopo, kitunguu na bizari ya mchuzi endelea kukaanga.
Tia maji kiasi na ndimu, pilipili mbichi ilosagwa kisha tia kotmiri.
Mwisho tia nusu ya samaki alokaangwa ukiwa tayari

Bilingani Za Kukaanga Na Viazi

Bilingani – 4 madogodogo

Viazi/mbatata – 3

Nyanya – 3

Majani ya mchuzi/mvuje/curry leaves – kiasi 6-7

Nnyanya kopo – 2 vijiko vya supu

Methi/uwatu ulosagwa – 1 kijiko cha chia

Rai/mustard seeds – 1 kijiko cha supu

Bizari ya manjano/haldi/turmeric – 1 kijiko cha chai

Chumvi – kiasi

Mafuta ya kukaangia – kiasi

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

1. Weka mafuta ya kukaangia katika karai

2. Katakakata bilingani vipande vipande vya mraba (cubes) kaanga katika mafuta ya moto hadi yageuke rangi. Eupa weka kando.

3. Katakataka viazi/mbatata vipande vidogodogo vya mraba (cubes) Kaanga hadi viive epua weka kando.

4. Ondosha mafuta yote katika karai bakisha kidogo tu kiasi ya vijiko 2 vya supu.

5. Kaanga rai kisha majani ya mchuzi, na methi/uwatu kisha kaanga nyanya.

6. Tia nyanya ya kopo kisha changanya pamoja bilingani na viazi ikiwa tayari.

Jinsi ya kupika wali wa Tuna (samaki/jodari)

VIAMBAUPISHI VYA TUNA

Tuna (samaki/jodari) – 2 Vikopo

Vitunguu (kata kata) – 4

Nyanya zilizosagwa – 5

Nyanya kopo – 3 Vijiko vya supu

Viazi (vilivyokatwa vipande vidogo – cubes) – 4

Dengu (chick peas) – 1 kikombe

Kitunguu saumu(thomu/galic)&Tangawizi iliyosagwa 1 Kijiko cha supu

Hiliki – 1/4 kijiko cha chai

Mchanganyiko wa bizari – 1 kijiko cha supu

Chumvi – kiasi

Pilipili manga – 1 Kijiko cha chai

Vipande cha Maggi (Cube) – 2

VIAMBAUPISHI VYA WALI

Mchele – 3 Vikombe vikubwa (Mugs)

Mdalasini – 2 Vijiti

Karafuu – chembe 5

Zaafarani – kiasi
Jirsh (Komamanga kavu au zabibu kavu -raisins) – 1/2 Kikombe

JINSI YA KUANDAA

Kosha Mchele na roweka.
Kaanga vitunguu hadi viwe rangi ya hudhurungi (brown) chuja mafuta uweke kando.
Kaanga viazi, epua
Punguza mafuta, kaanga nyanya.
Tia thomu/tangawizi, bizari zote, vipande vya Maggi, nyanya kopo, chumvi.
Mwaga maji ya tuna iwe kavu, changanyisha kwenye sosi.
Tia zaafarani kidogo katika sosi na bakisha ya wali.
Chemsha mchele pamoja na mdalasini na karafuu.
Karibu na kuwiva, chuja maji utie katika chombo cha kupikia katika jiko (oven)
Nyunyizia zaafarani, mwagia vitunguu, viazi, na dengu juu ya wali.
Mwagia sosi ya tuna na pambia jirshi (au zabibu).
Funika wali na upike katika jiko moto wa 450º kwa muda wa kupikika wali. Epua upakue.

Mapishi ya Ugali Kwa Mchuzi Wa Kamba Wa Nazi, Kisamvu Na Kachumbari Ya Papa Mkavu

Vipimo – Ugali

Maji – 4 vikombe kiasi inategemea na unga wenyewe.

Unga wa sembe – 2 vikombe

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Tia maji kiasi katika sufuria, weka motoni, yakipata moto korogea unga wa sembe kiasi na ufanye uji mzito uache uchemke vizuri huku ukikoroga.
Chota kibakuli kimoja cha uji huo weka pembeni kisha mimina unga wote uliobaki upigepige uchanganyike vizuri kwenye uji huo mpaka ushikamane
Punguza moto anza kuusonga taratibu huku ukiongeza ule uji ulioweka pembeni kidogo kidogo mpaka uone sasa umeshikamana vizuri.
Endelea kusonga mpaka ulainike kisha mimina kwenye bakuli au sahani iliyolowanishwa na maji kisha upete pete huku ukiugeuza geuza mpaka ukae shepu nzuri ya duara.Weka tayari kwa kuliwa.

Vipimo – Mchuzi wa kamba wa nazi

Kitunguu – 1

Nyanya – 2

Kamba waliomenywa – 1 Kilo

Pilipili mbichi iliyosagwa – ½ kijiko cha chai

Kitunguu saumu na tangawizi ilivyosagwa – 1 kijiko cha supu

Nazi nzito iliyochujwa – 1 kikombe

Bizari ya mchuzi – ½ kijiko cha chai

Chumvi – Kiasi

Ndimu – Nusu

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Safisha na osha kamba vizuri kisha mtie katika sufuria. Katia kitunguu, nyanya, tia chumvi, pilipili mbichi ya kusaga, thomu na tangawizi, bizari ya mchuzi na ndimu. Tia maji kidogo kiasi acha ichemke.
Watakapoiva na karibu kukauka, mimina tui la nazi taratibu koroga kiasi
Punguza moto aacha ichemke kidogo ukiwa mchuzi tayari.

Vipimo – Kisamvu

Kisamvu – 2 vikombe

Kunde mbichi zilizochemshwa – 1 kikombe

Kitunguu – 1

Nazi nzito iliyochujwa – 1 vikombe

Chumvi – Kiasi

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Weka kisamvu katika sufuria, katia kitunguu, tia chumvi, maji kidogo acha kichemke.
Huku ikichemka mimina kunde mbichi zilizochemshwa acha zipikikie kidogo mpaka kisamvu kikaribie kukauka na kunde kuiva.
Mimina nazi nzito punguza moto acha ichemke kidogo, mimina kwenye bakuli tayari kwa kuliwa.

Vipimo – Kachumbari Ya Papa

Papa mkavu (au nguru) – kipande

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Muoshe papa vizuri atoke mchanga kisha mchome kwenye jiko la mkaa au unaweza kumtia kwenye treya kisha kwenye oven kwa moto wa 350 kwa dakika 15 mpaka 20.
Akikauka mchambue chambue weka kando.
Tengeneza kachumbari, kwa kukata kitunguu, nyanya na pilipili mbichi, tia ndimu na chumvi.
Changanya na papa mkavu uliyemchambu ikiwa tayari.

Mapishi ya wali mtamu Wa Nazi Kwa Maharage Na Samaki Nguru Wa Kukaanga

Vipimo

Wali:

Mchele mpunga – 4 Vikombe

Tui la nazi – 6 vikombe

Chumvi – kiasi

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Osha mchele weka kando.
Bandika tui jikoni likichemka tia mchele na chumvi.
Funika uchemke, tui likikauka wacha moto mdogomdogo hadi wali uive ukiwa tayari. Ikiwa unatumia mkaa unapalia juu yake.

Maharage Ya Nazi

Maharage – 3 vikombe

Tui la nazi zito – 1 kikombe

Tui la nazi jepesi – 1 kikombe

Kitunguu maji – 1

Kitunguu saumu(thomu/galic) kilosagwa -1 kijiko cha chai

Chumvi – kiasi

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Chemsha maharage mpaka yaive.
Katiakatia kitunguu maji na tia thomu, tia na tui jepesi kikombe kimoja.
Tia tui zito endelea kuweka katika moto mdogomdogo hadi yakaribie kukauka yakiwa tayari.

Samaki Nguru Wa Kukaanga

Samaki Wa Nguru – 4 vipande

Kitunguu saumu(thomu/galic) & tangawizi ilosagwa – 1 kijiko cha supu

Pilipili mbichi – 4

Ndimu – 2 kamua

Bizari ya samaki -1 kijiko cha chai

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Mwoshe samaki kisha mtie kitunguu thomu, tangawizi ilosagwa, chumvi, pilipilimbichi ilosagwa, ndimu na bizari ya samaki.
Mwache akolee viungo kwa muda kidogo.
Makaange katika mafuta hadi aive akiwa tayari.

Mapishi ya Pilau Ya Nyama Ng’ombe Karoti Na Zabibu

Vipimo – Nyama

Nyama ng’ombe ya mifupa ilokatwa vipande – 1 kilo

Tangawizi na thomu (somu/garlic) ilosagwa – 2 vijiko vya supu

Bizari mchanganyiko/garama masala – 1 kijiko cha chai

Chumvi – Kiasi

Vipimo – Wali

Mchele – 4 glass

Mbatata/viazi menya katakata – 3 kubwa

Vitunguu katakata – 5

Kitunguu thomu kilosagwa (garlic/somu) – 1 kijiko cha supu

Hiliki ya unga – 1 kijiko cha chai

Bizari nzima ya pilau/cumin – 1 mti

Samli au mafuta – 2 Vijiko vya supu

Karoti zilokatwakatwa nyembamba – 6-7

Zabibu – Kiasi

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Katika sufuria weka mafuta kijiko kimoja cha supu tia nyama na viungo vyake.
kaushe katika moto hadi ikaribie kukauka kisha tia maji kiasi cha kuivisha na kubakisha supu ya mchele.
Katika sufuria ya kupikia weka samli au mafuta ishike moto.
Tia mbatata/viazi kaanga, tia vitunguu kaanga kidogo.
Tia kitunguu thomu, hiliki, bizari ya pilau endelea kukaanga hadi viwe rangi ya brown kidogo.
Tia mchele kaanga kidogo, kisha mimina nyama na supu yake. Funika wali uwive.
Weka kikaangio katika moto, tia samli kijiko kimoja kisha tia karoti na zabibu, kaanga kwa sekunde chache tu kwa ajili ya kulainisha karoti na zabibu.
Utakapopakuwa wali, pambia juu karoti na zabibu.

Shopping Cart
🏠 Home 📖 Reading 🖼️ Gallery 💬 AI Chat 📘 About