Dondoo za Mapishi na Lishe

Kupima lishe au afya ya mtu

Njia za kupima Afya

Njia mbalimbali hutumika kupima hali ya lishe, njia hizi ni;

1. Vipimo vya umbile la mwili

2. Vipimo vya maabara

3. Kuchukua historia ya ulaji na maradhi

Vipimo vya umbile la mwili

Baadhi ya vipimo ambavyo vinaweza kutumika kutoa tahadhari kuhusu magonjwa sugu yasiyo ya kuambukiza ni;

1. Uwiano wa uzito na urefu au Body Mass Index (BMI).

2. Mzunguko wa kiuno.

3. Uwiano wa mzunguko wa kiuno na nyonga.

4. Kulinganisha uzito na umri.

Uwiano wa uzito na urefu au Body Mass Index (BMI).

Hiki ni kipimo kinachotumika kuangalia uwiano wa urefu na uzito wa mtu, ni muhimu kuchukua vipimo kwa usahihi.Uwiano wa uzito katika Kilogramu na urefu katika mita hupatikana kwa kutumia kanuni ifuatayo:

BMI= uzito (Kg)/Urefu2 (m2)

BMI huwa na viwango mbalimbali vilivyowekwa na shirika la Afya duniani (WHO) kutafsiri hali ya lishe ya mtu ambavyo ni

1. BMI chini ya 18.5 = uzito pungufu.

2. BMI kati ya 18.5 mpaka 24.9= uzito unaofaa.

3. BMI kati ya 25.0 mpaka 29.9 = unene uliozidi.

4. BMI ya 30 au zaidi = unene uliokithiri au kiribatumbo.

Mahitaji ya chakula mwilini hutegemea umri, jinsi, hali ya kifiziolojia (kama ujauzito na kunyonyesha), hali ya kiafya, kazi na mtindo wa maisha. Uzito wa mwili hutegemea na chakula unachokula, pamoja na shughuli unazofanya, mara nyingi unene hutokana na kula chakula kwa wingi.
Unene uliokithiri unachangia kwa kiwango kikubwa kupata magonjwa sugu yasiyo ya kuambukiza kama kisukari, magonjwa ya moyo, shinikizo kubwa la damu, na saratani. Uzito uliozidi unapaswa kupunguzwa ili kuepuka magonjwa sugu yasiyo ya kuambukiza

Jinsi ya kupunguza unene uliozidi

1. Tumia mafuta kwa kiasi kidogo kwenye chakula

2. Epuka kula vyakula vyenye mafuta mengi hususani vinavyopikwa kwa kudumbukizwa kwenye mafuta, au vinavyokaangwa kwa mafuta mengi.

3. Epuka matumizi ya vinywaji au vyakula venye sukari nyingi

4. Epuka asusa zenye mafuta mengi au sukari nyingi kati ya mlo na mlo.

5. Ongeza vyakula venye makapi- mlo kwa wingi kama matunda, mboga mboga na nafaka zisizokobolewa.

BMI haitumiki kwa wanawake wajawazito, BMI haitumiki kwa watoto na vijana walio na umri chini ya miaka 18, BMI haitumiki kwa watu wasioweza kusimama vyema, waliovimba miguu, na wanawake wanaonyonyesha katika miezi sita ya mwanzo baada ya kujifungua.

Jinsi ya kutengeneza Biskuti Za Tende Na Ufuta

MAHITAJI

Unga – 3 Vikombe vya chai

Baking powder – 1 ½ Vijiko vya chai

Sukari – 1 Kikombe cha chai

Siagi – 1 Kikombe cha chai

Mayai – 2

Maji – kiasi ya kuchanganyia

Tende – 1 Kikombe

ufuta – ¼kikombe

MAPISHI

  1. Changanya unga, siagi, baking powder, na sukari katika bakuli
  2. Tia mayai, na maji kidogo uchanganye vizuri.
  3. Sukuma kiasi kama unavyosukuma chapati duara kubwa.
  4. Tandaza tende juu yake halafu kunja hadi mwisho.
  5. Paka mayai juu yake halafu mwagia ufuta kisha kata kata vipande.
  6. Vipange kwenye treya ya oveni kisha choma(bake)moto wa 350°F kwa muda wa nusu saa takriban.
  7. Ziepue katika moto naziache zipowe. Panga katika sahani.

Jinsi ya kupika Baklawa Za Pistachio Na Lozi

VIAMBAUPISHI

Philo (thin pastry) manda nyembamba – 1 paketi

Siagi – ¼ Kikombe cha chai

Baking powder – 2 Vijiko vya chai

Pistachio/ lozi – 2 vikombe vya chai

Mafuta – ½ Kikombe

VIAMBAUPISHI VYA SHIRA

Sukari – 2 Vikombe vya chai

Maji – 2 ½ Vikombe vya chai

ndimu – ½ kijiko cha chai

JINSI YA KUANDAA

Tafuta treya iliyokuwa sawa na ukubwa wa hizo manda nyembamba (philo) au zikate hizo manda kwa ukubwa wa treya (mraba au mstatili)
Kisha yeyusha siagi changanya na mafuta.
Kisha panga manda moja pakaza mafuta juu yake kisha weka manda nyingine juu yake kisha pakaza mafuta tena weka manda nyingine juu yake, endelea kufanya hivyo mpaka ziwe kama sita au saba kisha nyunyizia pistachio na lozi halafu panga tena manda na mafuta manda na mafuta tena sita au saba kisha nyunyizia tena pistachio na lozi.
Panga namna hivyo mpaka treya ijae inapofika manda ya mwisho kata vipande vya mraba vidogodogo humo humo kwenye treya kisha nyunyizia mafuta yaliyobaki.
Washa moto wa oven 350°F kwa muda wa dakika 20 au hadi rangi ibadilike kidogo (isikauke sana)
Chemsha syrup yako kama shira ya majimaji lakini isiwe nzito sana ikishakuwa tayari mwisho tia ndimu acha ipoe kidogo kisha miminia juu ya treya yote halafu malizia kunyunyizia pistachio na lozi zilizobaki.
Zikishakuwa tayari zipange kwenye sahani tayari kwa kuliwa.

ANGALIZO

Ukishatoa treya kwenye oven wacha ipoe kidogo na syrup yako pia wacha ipoe kidogo kabla hujamimina, ukitia ya motomoto zitalainika.
Manda nyembamba za baklawa zinauzwa tiyari madukani kwenye pakiti.

Jinsi ya kupika vizuri Wali Wa Karoti Na Nyama

MAHITAJI YA WALI

Mchele – 3 Magi

Mafuta – 1/4 kikombe

Karoti unakata refu refu – 3

Vitunguu maji kata vikubwa vikubwa – 1 kikubwa

Pilipli manga – 1/2 kijicho chai

Hiliki – 1/2 kijiko chai

Karafuu ya unga – 1/4 kijiko cha chai

Mdalasini wa unga – 1/2 kijiko cha chai

Zaafarani (ukipenda) roweka katika maji – 1 kijiko cha chai

Zabibu kavu (ukipenda) – 1/4 kikombe

Chumvi kiasi

KUPIKA WALI

Kwenye sufuria tia mafuta na kaanga karoti kidogo.
Tia vitunguu kisha tia bizari zote.
Tia maji kiasi (kutegemea aina ya mchele) na chumvi
Tia mchele upike uwive.
Karibu na kuwvia tia zabibu ukipenda.
Funika endelea kuupika hadi uwive.

MAHITAJI KWA NYAMA

Nyama – 2 Ratili (LB)

Chumvi – Kiasi

Mafuta – 1/4 kikombe

Kitunguu (kata virefu virefu) – 1 Kikubwa

Pilipili mboga kubwa – 2 ukipenda moja nyekundu moja kijani unazikata vipande virefu virefu.

Figili mwitu (celery) kata vipande virefu virefu- Miche miwili.

KUPIKA NYAMA

Chemsha nyama hadi iwive
Ikaange kwa mafuta hadi iwe nyekundu
Weka vitunguu, pilipili mboga na figili mwitu
Kaanga kidogo tu kama dakika moja.
Tayari kuliwa na wali.

Jinsi ya kupika Pilau Ya Nafaka Na Nyama Ya Kusaga

Viambaupishi

Mchele 3 vikombe

Nyama ya kusaga 1 LB

Mchanganyiko wa Nafaka (upendavyo) 1 kikopo

(maharagwe, njegere, mbaazi, na kadhalika)

Vitunguu maji kata vipande vipande 3 vya kiasi

Kitunguu saumu(thomu/galic) na Tangawizi 2 vijiko vya supu

Mafuta ½ Kikombe

Mchanganyiko wa bizari (Garam Masala) 2 vijiko vya chai

Vipande vya supu (Maggi cubes) 3

Maji (inategemea mchele) 5

Chumvi Kiasi

Jinsi ya kuandaa na kupika

1) Osha mchele na roweka.

2) Weka mafuta katika sufuria na kaanga vitunguu mpaka viwe brown.

3) Tia Thomu na tangawizi, kaanga kidogo.

4) Weka nyama ya kusaga, chumvi na garam masala, endelea kukaanga mpaka nyama iwive.

5) Mwaga maji yaliomo katika kopo la nafaka na utie nafaka pekee humo.

6) Tia maji na vipande vya supu (Maggi cubes) huku unavivuruga, koroga kidogo.

7) Tia mchele, koroga kidogo.

8) Funika na pika kwa moto mdogo mpaka karibu na kukauka ukikorogoka kidogo. (kama unavyopika pilau ya kawaida)

9) *Epua uipike katika moto wa oven 350-400 Deg kwa muda wa dakika 15.

*Kama sufuria uliyotumia sio ya kupikia katika oven, mimina katika chombo chochote kinachotumika kwa oven kama bakuli la pyrex au treya za foil.

10) Pakua katika sahani na iko tayari kuliwa.

Mapishi – Fish Finger

Leo tunaangalia mapishi ya fish finger ( sijui kama unaweza kusema kidole cha samaki)!, Ni mlo mzuri hasa kuliwa kama kitafunio au mboga ya pembeni.

Mahitaji

500g Fileti ya samaki
120g Chenga za mkate
100g Unga wa ngano
Mayai 2
Ndimu 1
Kitunguu saumu 1
Kotmiri
Mafuta ya kupikia

Matayarisho

Menya vitunguu saumu kisha visage

Katakata fileti kwa muundo wa mraba (kama vidole) kisha paka mchanganyiko wa vitunguu saumu

Kata ndimu na kamulia kwenye fillet yako

Weka chenga za mkate kwenye bakuli kisha uchanganye chumvi kiasi na kata kata kotmiri majani 3 na uchanganye pamoja.

Kwenye bakuli lingine weka mayai na uyapigepige yawe kama uji mzito

Weka unga kwenye bakuli jingine.

Chukua kipande cha fillet kiweke unga kidogo kisha kizamishe kwenye yai na baada ya hapo kizamishe kwenye mchanganyiko wa chenga za mkate. Fanya hivyo kwa vipande vyote.

Weka mafuta kwenye kikaago na subiri yachemke kisha weka fillet zako vizuri na zikaange pande zote hadi zimekuwa rangi ya brown ( hakikisha moto sio mkali sana).

Epua na weka pembeni mafuta yote yakauke

Weka kwenye sahani tayari kwa kula.

Jinsi ya kupika Biskuti Za Tende

Viamba upishi

Unga 4 Vikombe vya chai

Sukari ya laini (icing sugar) 1 Kikombe cha chai

Baking powder 2 Vijiko vya chai

Mayai 2

Siagi au margarine 1 Kikombe cha chai

Vanilla 1 Kijiko cha chai

Maziwa ya kuchanganyia kiasi

Tende iliyotolewa koko 1 Kikombe

ufuta (sasame) kiasi 1/4 kikombe

Jinsi ya kuandaa na kupika

1. Changanya unga, siagi, baking powder, na sukari katika mashine.

2. Kisha tia mayai, vanilla na halafu maziwa kidogo kidogo hadi mchanganyiko ushikamane.

3. Gawanya madonge mawili na usukume kama chapati, lakini sio nyembamba sana.

4. Tandaza tende robo ya duara na unyunyize ufuta duara zima: kisha kunja hadi mwisho na ukate kate, kisha upange katika trei ya kuvumbika.

5. Vumbika (bake) moto wa 350°F kwa muda wa dakika 20 au hadi vigeuke rangi na viwive.

6. Zikisha iiva ziache zipowe na zitakuwa tayari kuliwa.

Mapishi ya Wali Wa Karoti Na Kuku Wa Kukaanga

Vipimo Vya Wali

Mchele wa Basmati/Pishori – 1 kilo moja

Vitunguu maji – 3

Karoti – 2

Siagi – 3 vijiko vya supu

Kidonge cha supu (stock) – 1 kimoja

Chumvi – kiasi

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Ósha mchele uroweke kama saa moja au mbili
Katakata vitunguu vipande vidogodogo (chopped) weka kando.
Kwaruza karoti (grate) weka kando.
Tia siagi katika sufuria ya kupikia wali, weka katika moto iyayuke
Kaanga vitunguu hadi vigeuke rangi kiasi tu.
Tia maji kiasi ya kupikia wali, changanya na kidonge cha supu.
Yakichemka tia mchele, koroga, funika uweke moto mdogo mdogo.
Kabla ya maji kukauka tia karoti changanya wali kisha funika uive kama unavyopika pilau.

Vipimo Vya Kuku Wa Kukaanga

Kuku alokatwakatwa – 1

Kitunguu saumu(thomu/galic) na tangawizi ilosagwa – 2 vijiko vya supu

Bizari ya mchanganyiko/garam masala – kijiko cha supu

Mtindi/Yoghurt – 1 kijiko cha supu

Ndimu – 1

Chumvi – kiasi

Mafuta ya kukaangia – kiasi

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Ukishamuosha kuku, mchuje atoke maji yote.
Changanya viungo vyote katika kibakuli kidogo.
Changanya pamoja na kuku kisha acha akolee viungo (marinate) kwa muda wa masaa mawili takriban.
Weka mafuta katika karai na kaanga kuku, akiwiva yu tayari kuliwa na wali.

Mapishi ya Mchemsho wa ndizi na nyama

Mahitaji

Ndizi mbichi 6
Nyama ya ng’ombe (nusu kilo)
Viazi mviringo 2
Kitunguu swaum
Tangawizi
Kitunguu maji
Nyanya 1 kubwa
Mafuta (vegetable oil)
Chumvi
Limao
Pilipili

Matayarisho

Chemsha nyama na limao, kitunguu swaum, tangawizi chumvi na maji kiasi mpaka nyama iive, Hakikisha unaiacha na supu kiasi kwa ajili ya kuwekea kwenye ndizi.Kisha katakata nyanya na vitunguu na uweke pembeni .Menya ndizi na viazi kisha zichemshe pamoja na vitunguu, nyanya, maji kidogo, mafuta na uhakikishe haziivi kabisa. Baada ya hapo tia nyama na supu yake, pilipili mzima na chumvi na uache uchemke mpaka ndizi na viazi viive.Na baada ya hapo mchemsho wako utakuwa tayari kwa kuliwa

Mapishi ya Supu ya makongoro

Mahitaji

Makongoro (miguu ya ng’ombe) kiasi
Limao 1 kubwa
Kitunguu swaum
Tangawizi
Chumvi
Pilipili

Matayarisho

Safisha makongoro kisha yatie kwenye pressure cooker. Kisha tia kitunguu swaum, tangawizi, chumvi,limao na maji kiasi. Baada ya hapo yachemshe mpake yaive na yawe malaini na pia ubakize supu kiasi inaweza kuchukua kama dk 45 au saa 1 hivi. Baada ya hapo yaipue na upakue supu yako kwenye bakuli katia pilipili kiasi kisha itakuwa tayari kwa kuliwa.

Note:
Ukiwa unanunua makongoro hakikisha unachukuwa yale yasiyokuwa na manyoya na pia
hakikisha usiyachemshe kupitiliza kwani yakiwa malaini sana utashindwa kuyaenjoy.

Mapishi ya Dagaa wa nazi, nyanya chungu na bamia

Mahitaji

Dagaa waliokaushwa (dried anchovy 2 kikombe cha chai)
Bamia (okra 5)
Nyanya chungu (garden egg 5)
Tui la nazi (coconut milk 1 kikombe cha chai)
Nyanya (fresh tomato 2)
Kitunguu (onion 1)
Curry powder 1/2 ya kijiko cha chai
Turmeric powder 1/2 kijiko cha chai
Limao (lemon 1/2)
Chumvi (salt kiasi)
Pilipili (scotch bonnet 1)
Mafuta (veg oil)

Matayarisho

Safisha dagaa na uwaweke pembeni. Baada ya hapo kaanga vitunguu vikianza kuwa vya brown tia dagaa wakaange kidogo kisha tia chumvi, pilipili, curry powder, turmeric, bamia na nyanya chungu, koroga vizuri mpaka mchanganyiko wote uchanganyike vizuri kisha tia nyanya na ufunike. Pika mpaka nyanya iive kisha kamulia limao,na pia hakikisha nyanya chungu na bamia zimeiva kidogo(usiache mpaka ziive sana manake zitavurugika pindi utakapotia tui la nazi) kisha malizia kwa kutia tui la nazi na uache lichemke mpaka rojo ibakie kidogo. Hakikisha nyanya chungu na bamia zimeiva ndo uipue. Na hapo dagaa wako watakuwa tayari kwa kuliwa na wali au ugali.

Vidokezo vya kukusaidia ule mboga za majani zaidi

Ulaji wa mboga za majani ni muhimu kwa sababu zina vitamini na madini mengi na viwango vidogo vya kalori. Ili uongeze mboga zaidi za majani katika milo yako, fuata vidokezi hivi vifuatavyo;

Gundua njia za kupika haraka

Pika mboga mpya za majani au zilizogandishwa kwa barafu katika wimbi mikro kwa mlo wa haraka na rahisi kuongeza kwa mlo wowote. Pika maharagwe ya kijani, karoti, au brokoli kwa mvuke katika bakuli na kiwango kidogo cha maji katika wimbi mikro kwa mlo wa haraka.

Kuwa mbele ya mambo

Katakata bechi ya pilipili hoto, karoti, au brokoli.Ziweke ili uzitumie wakati zimeadimika. Unaweza kuzifurahia kwenye saladi, na mboji au sandwichi ya mboga za majani.

Chagua mboga za majani zilizo na rangi nyingi

Ng’arisha sahani yako na mboga za majani zilizo na rangi nyekundu, ya machungwa, au kijani. Ziko na vitamini na madini. Jaribu boga ya tunda la muoka, nyanya cheri, viazi vitamu, au kale (sukuma wiki). Hazionji vizuri tu bali ni nzuri kwako pia.

Angalia mpangilio wa friza

Mboga za majani zilizogandishwa kwenye barafu hutumika haraka na kwa urahisi na ziko na lishe kama mboga mpya za majani. Jaribu kuongeza mahindi, dengu, maharagwe ya kijani, spinachi, au mbaazi barafu kwa milo yako kadhaa uipendayo au au ule kama mlo wa kando.

Weka mboga nyingi za majani

Mboga za majani za mkebe ni ongezo muhimu kwa mlo wowote, kwa hivyo weka nyanya, maharagwe mekundu, uyoga, na viazisukari vya mkebe tayari. Chagua zilizo na lebo kama “sodiamu iliyo punguzwa,” “sodiamu kidogo,” au “hakuna chumvi imeongezwa.”

Fanya saladi yako ya bustani ing’ae kwa rangi

Ng’arisha saladi yako kwa kutumia mboga za majani zilizo na rangi nzuri kama vile maharagwe meusi, pilipili hoho zilizokatakatwa, figili zilizokatakatwa, kabichi nyekundu iliyokatakatwa au wotakresi. Saladi yako haitapendeza tu lakini pia itaonja vizuri.

Kunywa supu ya mboga za majani

Ipashe moto na uile. Jaribu supu ya nyanya, boga kikazio, au mboga za majani za bustani. Tafuta supu iliyopunguzwa sodiamu au iliyo na kiwango cha chini cha sodiamu.

Ukiwa nje

Kama chakula cha jioni ni nje ya nyumbani, usijali. Unapoagiza, itisha mboga zaidi za majani au saladi zaidi badala ya mlo wa kawaida wa kando uliokarangwa.

Onja ladha ya mboga za majani za msimu

Nunua mboga za majani ambazo ni msimu wake kwa ladha ya kiwango cha juu kwa bei ya chini. Angalia bidhaa zilizo na bei maalumu katika duka kuu la karibu kwa ununuzi wa bei nafuu. Au tembelea soko la wakulima lililokaribu.

Jaribu kitu kipya

Huwezijua unachoweza kupenda. Chagua mboga mpya ya majani – iongeze kwa mapishi yako au tafuta mtandaoni jinsi ya kuipika.

Mapishi ya Ugali Kwa Mchuzi Wa Samaki Wa Kuchoma

Vipimo Vya Ugali

Unga wa mahindi – 4 vikombe

Maji – 6 kiasi

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Tia maji kiasi katika sufuria wacha yachemke hasa

Tia unga kidogo kidogo huku ukikoroga mpaka ukamatane

Punguza moto huku ukiendelea kuusonga

Endelea kusonga kwa dakika kadhaa mpaka uanze kuchambuka

Kisha mimina kwenye bakuli au sahani na itakuwa tayari

Vipimo Ya Upishi Wa Mchuzi Wa Samaki Wa Kuchoma Wa Nazi

Samaki:

Samaki wa Nguru – kiasi vipande 5 – 6

Pilipili mbichi – 3

Kitunguu saumu(thomu/galic) – 5 chembe

Tangawizi mbichi – 1 kipande

Bizari ya samaki – 1 kijiko cha supu

Pilipili nyekundu ya unga – 1 kijiko cha chai

Ndimu – 3 kamua

Chumvi – kiasi

Ukipenda mkate samaki vipande kiasi.
Saga vipimo vyote vinginevyo katika mashine. Mchanganyiko ukiwa mzito ongezea ndimu
Changanya pamoja na samaki upake vizuri vipande vya samaki
Acha kwa muda wa nusu saa vikolee mchanganyiko
Panga samaki katika treya ya kupikia ndani ya oveni, kisha mchome (grill) samaki huku ukigeuza hadi viwive.
Epua weka kando.

Kuandaa Mchuzi:

Nyanya/tungule – 3

Kitunguu – 2

Bizari ya manjano/haldi – ¼ kijiko cha chai

Mafuta – 3 vijiko vya supu

Tui la nazi zito – 3 vikombe

Chumvi – kiasi

Katakata vitunguu na nyanya vidogodogo (chopped) weka kando

Weka mafuta katika karai au sufuria, kaanga vitunguu hadi vianze kugeuka rangi

Tia nyanya kaanga pamoja na tia bizari ya njano/haldi .

Tia tui la nazi, chumvi koroga .

Mwishowe tia vipande vya samaki na rojo lake litakalobakia katika treya, mchuzi uko tayari

Mapishi ya Pasta za cream na uyoga

Mahitaji

Pasta (2 na 1/2 vikombe vya chai)
Uyoga (mashroom 2 vikombe vya chai)
Cream (1 kikombe cha chai)
Mafuta (vegetable oil)
Kitunguu (onion 1)
Chumvi
Majani ya basil (dried basil leaves 1/2 kijiko cha chai)

Matayarisho

Chemsha maji ya kutosha kisha tia chumvi na mafuta kidogo katika hayo maji na baadae tia pasta na uzichemshe mpaka ziive kisha uzichuje maji na uziweka pembeni. Baada ya hapo weka mafuta kidogo katika sufuria kisha tia uyoga uliokatwa na uupike mpaka uive. Baada ya hapo tia majani ya basil, chumvi na cream kisha acha ichemke kisha weka vitunguu na upike kwa muda wa dakika 4 kisha malizia kwa kutia pasta. Zichanganye vizuri na mchanganyiko wote kisha zipike kwa muda wa dakika 5. Na hapo zitakuwa tayari kwa kuliwa.

Unaweza kupika nyama ya kuku (chiken breast) iliyokatwa vipande vidogo vidogo kama saizi na shape ya pasta. Vizuri kuikaanga pembeni mpaka iwe brown na kuiva alafu kuimix kwenye chakula baada ya uyoga na vitunguu kuiva alafu unamix cream kumalizia mapishi.

Jinsi ya kutengeneza Fagi Ya Kumumunyuka Mdomoni

VIAMBAUPISHI

Maziwa mazito matamu (condensed milk) – 2 vibati

Sukari – 1 kikombe

Samli 1 ½ kikombe

Vanilla 2 kifuniko cha chupa yake

Hiliki ilosagwa – 2 vijiko vya chai

Sinia kubwa ya bati Paka samli

MAANDALIZI

Changanya maziwa, sukari na samli katika sufuria isiyogandisha chakula (non-stick) uweke katika moto.
Koroga huku ikipikika hadi ianze kugeuka rangi na kuanza kuachana. Usiache mkono kuroga isije kufanya madonge.
Tia hiliki na vanilla, endelea kuipika.
Itakapogeuka rangi vizuri mimina katika sinia na haraka uitandaze kwa mwiko huku ukiuchovya katika maji na kuendelea kuitandaza hadi ikae sawa kote.
Pitisha kisu kuikataka ili ikipoa iwe wepesi kuitoa vipande.

Kila inapozidi kupoa na kukaa ndipo fagi inakauka na kumumunyuka.

Mapishi ya Bilinganya

Mahitaji

Bilinganya 2 za wastani
Nyanya kubwa 1
Kitunguu maji 1 kikubwa
Swaum 1/2 kijiko cha chai
Limao 1/4
Pilipili ya unga 1/2 kijiko cha chai
Parpika 1/4 kijiko cha chai
Pilipili mtama 1/4 kijiko cha chai
Curry powder1/4 kijiko cha chai
Chumvi kiasi
Coriander
Olive oil

Matayarisho

Katakata bilinganya slice nyembamba kisha ziweke pembeni. Baada ya hapo kaanga kitunguu maji mpaka kiwe cha brown kisha tia swaum na spice zote, zikaange kidogo kisha tia nyanya na chumvi kiasi. Pika nyanya mpaka iive na itengane na mafuta. Baada ya hapo tia mabilinganya na ukamulie limao kisha punguza moto na uyafunike na mfuniko usioruhusu kutoa mvuke ili yaivie na huo mvuke. Baada ya hapo yaonje kama yameiva na malizia kwa kutia fresh coriander na baada ya hapo yatakuwa tayari kwa kuliwa. kwa kawaida mi hupendaga kuyalia na wali na maharage badala ya kachumari kwahiyo nakuwa naitumia hiyo kama kachumbari

Mapishi ya Sambusa za nyama

Mahitaji

Nyama ya kusaga (minced beef 1/4 kilo)
Vitunguu maji vilivyokatwakatwa(diced onion 2 vikubwa )
Kitunguu swaum/ tangawizi (garlic and ginger paste 1 kijiko cha chakula)
Chumvi (salt)
Pilipili iliyokatwakatwa (scotch bonnet 1)
Limao (lemon 1/2)
Curry powder 1/2 kijiko cha chai
Cinnamon powder 1/4 kijiko cha chai
Coriander powder 1/4 kijiko cha chai
Cumin powder 1/4 kijiko cha chai
Unga wa ngano (all purpose flour kidogo)
Manda za kufungia (spring roll pastry)
Giligilani (fresh coriander kiasi)
Mafuta ya kukaangia

Matayarisho

Changanya nyama na limao, chumvi, pilipili,kitunguu swaum, tangawizi na spice zote, kisha pika katika moto wa kawaida mpaka nyama iive na maji yote yakauke. Baada ya hapo kabla hujaipua nyama tia vitunguu na giligilani na uvipike pamoja kwa muda wa dakika 2 na uipue weka pembeni na uache viipoe. Baada ya hapo tia unga kidogo katika bakuli nauchanganye na maji kidogo kupata uji mzito kwa ajili ya kugundishia manda. Baada ya hapo tia nyama katika manda na kisha zifunge kwa kugundishia na unga wa ngano.Ukisha maliza kuzifunga zote zikaange mpaka ziwe za brown na uzitoe. Na hapo zitakuwa tayari kwa kuliwa.

Mapishi ya Wali Wa Kichina Wa Kuku Na Mboga Mchanganyiko

Vipimo

Mchele wa basmati/pishori – 4 vikombe vikubwa (mugs)

Kuku – 2

Vitnguu vya kijani (sprin onions) katakata – 5 miche

Maharage machanga (spring beans) katakata – kiasi kujaza mug moja

Pilipili boga la (capsicum) katakata – 1

Karoti katakata vipande virefu – 1

Kitunguu thomu (garlic) kuna (grate) – 1 kubwa

Tangawizi mbichi kuna (grate) – 1 kubwa

Sosi ya soya (soy sauce) – 2 vijiko vya supu

Kidonge cha supu – 1

Mafuta ya kupikia – ¼ kikombe cha chai

Chumvi – kiasi

Pilipili manga – 1 kijiko cha supu

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Osha kuku vizuri, katakata vipande, weka katika sufuria, tia chumvi, pilipili manga, mfunike, umkaushe motoni huku ukimgeuza geuza.

Roweka mchele kisha uchemshe uive nusu. Chuja maji, tia siagi kidogo ili usigandane.

Weka karai ya kupika mboga (wok) au sufuria kisha tia mafuta yashite moto.

Tia kitunguu thomu, tangawizi, kaanga kidogo.

Tia mboga zote, ulizokatakata.

kaanga kidogo, kisha tia sosi ya soya na kidonge cha supu. Usizipike sana mboga mpaka zikalainika mno. Sababu zitaiva katika mchele

Changanya kuku na mboga kisha changanya vyote katika mchele, urudishe katika moto.

Funika upike hadi uive kamilifu.

Pakua kwenye sahani.

Jinsi ya kupika Mkate

Mahitaji

Unga wa ngano ( self risen flour) kikombe 1 na 1/2
Hamira (yeast) 1 kijiko cha chai
Sukari (sugar) 1 kijiko cha chakula
Chumvi (salt) 1/2 kijiko cha chai
Siagi iliyoyeyushwa (melted butter) 1 kijiko cha chakula
Maji ya uvuguvugu ( warm water) kiasi

Matayarisho

Changanya vitu vyote katika bakuli kubwa kisha aanza kukanda mpaka upate donge laini.Baada ya hapo liweke hilo donge kwenye bakuli la plastic na weke katika sehemu yenye joto ili unga uumuke. Hakikisha unga unaumuka zaidi (yani unaji double size) unaweza kuchukua kama saa 1 na nusu hivi. Baada ya hapo ukande tena na uache uumuke tena kwa mara ya pili, Ukisha umuka pakaza butter katika baking tin (chombo cha kuokea) na upakaze mkate butter kwa juu,kisha uoke katika oven kwa muda wa dakika 30 (katika moto wa 200C) (hakikisha juu na chini unakuwa wa brown Na hapo mkate wako utakuwa tayari

Mapishi ya tambi za mayai

Tambi za mayai ni moja kati ya vyakula ambavyo napenda kuandaa pale ninapokua ninaharaka au sina muda mrefu wakukaa jikoni.pishi hili huchukuca muda mfupi sana na nimlo uliokamilika.

Mahitaji

  1. Tambi ½ paketi
  2. Vitunguu maji 2 vikubwa
  3. Karoti 1
  4. Hoho 1
  5. Vitunguu swaumu(kata vipande vidogo) kijiko 1 cha chakula
  6. Carry powder kijiko 1 cha chai
  7. Njegere zilizochemshwa ½ kikombe
  8. Mafuta kwa kiasi upendacho
  9. Mayai 2
  10. Chumvi kwa ladha upendayo

Njia

1.Chemsha maji yamoto yanayotokota,ongeza chumvi na mafuta kidogo,weka tambi kwenye maji hayo chemsha adi ziive.Chuja maji yote ili kupata tambi kavu
2.Katika bakuli piga mayai kisha weka pembeni
3.Katika kikaango,weka mafuta,vitunguu maji ,vitunguu swaumu,hoho, karoti na carry powder,kaanga kwa pamoja katika moto mdogo kwa muda mfupi kwani mboga hazitakiwi kuiva.
4.Ongeza tambi na njegere katika kikaango,geuza kila mara ili kuchanganya .
5.Ongeza mayai kwenye tambi kisha geuza kwa haraka bila kupumzika adi mayai yaive na tambi ziwe kavu.Tayari kwa kula

Katika hatua hii ongeza moto uwe wa wastani,moto ukiwa mdogo mayai yatafanya tambi zishikane na kufanya mabonge.

Shopping Cart
🏠 Home 📖 Reading 🖼️ Gallery 💬 AI Chat 📘 About