Namna Mungu anavyojibu Sala au Maombi
Mungu ni mwenye Hekima, anajibu Sala zetu kwa kutupa kile tunachohitaji na chenye kutufaa na Sio kutupa kile tunachokitaka na kukitamani kwa kuwa anatupenda na kututakia mema.
Mungu ni mwenye Hekima, anajibu Sala zetu kwa kutupa kile tunachohitaji na chenye kutufaa na Sio kutupa kile tunachokitaka na kukitamani kwa kuwa anatupenda na kututakia mema.
Upendo wa Mungu hauna mwisho. Mtu anaweza akaacha kukupenda na kukusahau kabisa lakini kamwe Mungu haachi kumpenda Mtu wala hamsahau Mtu.
Mungu ni mwema sana tunapokua wadhambi anapotuadhibu haimaanishi kuwa anatuchukia. Inamaanisha kuwa anatuonya na hapendi turudie makosa.
Upendo wa siku zote huo ndio upendo atakao Mungu. Chuki na unafiki ni tabia ya Shetani, umoja ni tabia ya Mungu.
Uzuri wa Mungu ni kwamba anasamehe na kisha anasahau. Unapotubu dhambi zako na kutaka huruma zake yeye anakufutia uovu wote na kukufanya mpya.
Sala ni Hazina. Kusali ni muhimu sana. Sala unayosali leo inaweza kukusaidia hata miaka kumi ijayo au ikasaidia watoto wa watoto wako. Mungu ni mwenye fadhila na anakumbuka yote. Mwombe Mungu akulinde ukiwa mzima ili uwapo hatarini akukumbuke hata kabla hujamwomba.
Usifadhaike moyoni pale unapokuwa katika matatizo au unapopitia changamoto katika maisha. Kumbuka kuwa Mungu yupo, anayaona hayo na anataka kukusaidia, ni wewe tuu kumpa nafasi ya kukusaidia. Hatumpi Mungu nafasi pale tunapozani tunaweza wenyewe.
Mungu anaporuhusu ukaingia katika majaribu na mateso hana nia ya kukutesa bali anataka kukuimarisha. Mungu ni mwema kila wakati.
Mungu anamjibu mtu sala zake kutokana na anachonuia.
Mungu haangalii matemdo ya mtu ya nje tuu, bali anaangalia ndani kabisa mawazo ya mtu na nia yake. Nia ya mtu ndiyo inayoonyesha mtu alivyo.
Sala pasipo Imani thabiti, ya nia ya kweli, upendo wa kweli, unyenyekevu wa ndani na tumaini la kweli katika Amani ya rohoni; Haijakamilika na haifai kitu.
Unapo mwomba Mungu Usisahau Kushukuru. Kushukuru ni kuomba mara ya pili. Utazidishiwa kile ulichokiomba na kupewa hata usichokiomba kwa shukrani yako.
Uwe na subira Baada ya kuomba kwa Mungu. Sio kila unachoomba kwa Mungu utakipata kwa wakati huo huo au kwa wakati unaofikiri. Mungu ni Mwaminifu Sana Kwenye kujibu maombi lakini vile vile ni mwenye Hekima Kwenye kukujibu, anajua wakati gani ni sahihi kukujibu maombi yako. Anaweza kukujibu saa hiyo hiyo, kesho, keshokutwa au hata mwakani kwa kuangalia wakati ufaao na kwa manufaa yako. Kwa hiyo unapoona hujajibiwa usife moyo, bali uwe na matumaini. Mungu anajua akujibu lini kwa kuwa anajua ni lini wakati ufaao na ni lini kitu kipi kina kufaa.
Usiache kusali na kutenda mema kwa kuwa huwezi jua ni watu wangapi wanategemea sala na matendo yako mema. Kumbuka Mungu alimwambia Abraham kama akikuta Wacha Mungu wengi hataiharibu Sodoma na Gomora. Vivyo hivyo Inawezekana wapo watu wengi wanaonufaika na Sala na matendo yako, hasa watu wako wa karibu uwapendao. Unapokuwa mtu wa Sala na mcha Mungu unabarikiwa wewe na wale wa karibu yako. KAMWE USIACHE KUMCHA MUNGU NA KUSALI. Ukiwa mregevu ni sawa na unakata Mnyororo wa Baraka za Mungu kwako na wenzako.
Wakati wazazi waliweza kuaamua kuzaa mtoto tuu, Mungu yeye alikuchagua wewe utungwe mimba na kukulinda ungali tumboni mwa mama yako….Wakati wazazi wanasubiri kwa shauku kuona muonekano wako wewe, Mungu anawaweka wajukuu wa wazazi wako/ watoto wako ndani mwako…. Wakati wazazi wakitafuta chakula kwa ajili yako, Mungu yeye aliwawezesha kukipata…. Wakati wazazi wakingoja kuona unavyoendelea kukua huku wakiwaza hatima ya maisha yako Mungu anakuendeleza na alishapanga maisha yako tangu alipokuchagua uwe mtu ukiwa tumboni mwa mama yako…. Wazazi wanaweza kukuombea kwa Mungu lakini Mungu ndiye anayeamua akufanyie nini maana Wewe ni wa kwake….Wewe na wazazi wako ni watoto wa Baba mmoja ambaye ndiye Mungu.
Sala sio kitu cha muhimu kufanya wakati wa shida tuu. Sala ni kitu cha muhimu zaidi kila siku katika Maisha kuwe na shida au kusiwe na shida.
Kutubu ndio njia pekee ya kumrudia Mungu. Toba ya kweli ndiyo iletayo maondoleo ya dhambi. Ukiondolewa dhambi unaimarishwa na kufanywa mya. Tubu usamehewe na kufanywa mpya.
Kila jambo lina Mkono wa Mungu juu yake hata kama limefanyika bila kupangwa au kukusudiwa. Mbele ya Mungu hakuna kitu kinachofanyika kwa Ajali au bahati mbaya.
Jifunze na jijengea tabia ya kumsikiliza Mungu rohoni mwako unaposali. Sala ni mazungumzo ya Mungu na mwanadamu. Mazungumzo yanahusisha kuongea na kusikiliza.
Mtumainie Mungu kwa maana Mungu hawatupi wale wamtumainiao na kumgoja. Mkono wake upo tayari kwa ajili ya kuwaokoa wale wanaomwelekea.
Recent Comments