Tumaini kwa Mungu
Mtumainie Mungu kwa maana Mungu hawatupi wale wamtumainiao na kumgoja. Mkono wake upo tayari kwa ajili ya kuwaokoa wale wanaomwelekea.
Mtumainie Mungu kwa maana Mungu hawatupi wale wamtumainiao na kumgoja. Mkono wake upo tayari kwa ajili ya kuwaokoa wale wanaomwelekea.
Mungu anasubiri sala zako kila siku. Anasubiri sala zako akujibu ili uone utukufu wake. Anasubiri sala zako ili akuze mahusiano yake na wewe. Sali daima kwani Mungu yupo milele kukusikiliza na kukuhudumia.
Mungu ni mwenye Huruma na Upendo na Anataka watu wote waokolewe naye. Mungu hayupo kwa ajili ya kukuhukumu bali kwa ajili ya kukuhurumia na kukurehemu.
Hakuna kitu cha Muhimu zaidi Duniani kama kumjua Mungu na kumuishi Mungu. Kila binadamu ameumbwa kwa ajili hii. Na Mungu anachotaka ndicho hichi, kumjua na kumuishi. Mengine yote ni maziada. Ukimuishi Mungu atakufanikisha katika yote.
Fikiria umenunua zawadi nzuri ya gharama sana na unataka kumpa mtu umpendaye sana. Akipokea zawadi yako unafurahi sana, akikataa kuipokea zawadi inaumiza sana, lakini inaumiza zaidi akiipokea kisha akaitupa mbele yako na kuona haina maana. Hiki ndicho kinachotokea kwa Yesu. Yesu yupo kwa ajili ya kutupa zawadi ya Wokovu alyogharamia kwa uhai wake. Tunapoipokea tunamfurahisha sana, tukiikataa tunamhuzunisha na tunapoipokea na kuiacha baadae tunamhuzunisha kwelikweli.
Mungu ni mwenye Hekima, anajibu Sala zetu kwa kutupa kile tunachohitaji na chenye kutufaa na Sio kutupa kile tunachokitaka na kukitamani kwa kuwa anatupenda na kututakia mema.
Upendo wa Mungu hauna kikomo. Mama anaweza kumchoka na kumtelekeza mwanae lakini Mungu kamwe hamchoki mtu.
Mungu ni Mwaminifu Sana na mwenye mipango na subira katika kila kitu hasa Sala na maombi yetu kwake. Tunaposali leo Mungu anatusikia na kujibu leo, kesho au hata miaka kumi ijayo. Inawezekana hata baraka zako za leo ni majibu ya Sala zako miaka kumi iliyopita. Sali bila kuchoka kwani hujui Sala zako zitakusaidia lini. Usitegemee majibu ya Sala zako wakati huo huo, amini katika uaminifu wa Mungu kwani anajua lini ni siku sahii ya kukujibu.
Uzuri wa Mungu ni kwamba anasamehe na kisha anasahau. Unapotubu dhambi zako na kutaka huruma zake yeye anakufutia uovu wote na kukufanya mpya.
Kwa njia ya sala Binadamu anampa Mungu Utukufu, Mungu anampa Binadamu Wokovu na Neema.
Mungu daima ni Mwaminifu na mwenye Huruma. Kinachotakiwa ni kuamini kwamba kipo na kitakuwepo. Kusadiki kwamba kitafanyika na kitafanyika. Hii ndiyo Siri ya Imani.
Kufanya Mambo mema ndipo kunaleta furaha ya kweli kwa Binadamu yeyote yule. Hakuna Binadamu anayefurahia kufanya maovu. Mema hayaambatani na majuto lakini uovu wowote unamajuto. Hata waovu wanafanyiana mema ili wapate furaha.
Upendo hauandamani na ubinafsi. Huwezi kusema una upendo wa kweli kama huwezi kujinyima vile unavyovipenda kwa ajili ya yule au wale unaowapenda. Upendo wa kweli ni kujitoa.
Hakuna Maisha ya Kikristo bila Kusali. Kama kuna Mkristo anaishi bila kusali huyo siyo Mkristo bali Mkristo mfu. Sala ndiyo uhai wa Mkristo. Hakuna Njia nyingine yoyote ya kumfikia Mungu isipokua sala.
Hakuna sala yeyote itolewayo kwa unyenyekevu wa kweli katika imani, matumaini na mapendo inayopita bure mbele ya Mungu. Mungu hamtupi mwenye unyoofu wa moyo.
Uhuru Na Amani Ya Moyoni hupatikana kwa kusali wala sio kwa kusoma vitabu na kujua sana Mambo mengi.
Sala ni Hazina. Kusali ni muhimu sana. Sala unayosali leo inaweza kukusaidia hata miaka kumi ijayo au ikasaidia watoto wa watoto wako. Mungu ni mwenye fadhila na anakumbuka yote. Mwombe Mungu akulinde ukiwa mzima ili uwapo hatarini akukumbuke hata kabla hujamwomba.
Kila jambo lina Mkono wa Mungu juu yake hata kama limefanyika bila kupangwa au kukusudiwa. Mbele ya Mungu hakuna kitu kinachofanyika kwa Ajali au bahati mbaya.
Inashangaza kwa sasa watu wengi hawapendi kuambiwa kuhusu kutubu dhambi zao bali wanataka waambiwe watabarikiwa. Kama vile wewe huwezi kumvika mwanao nguo nzuri kabla ya kumuogesha vivyo hivyo na Mungu hawezi kukubariki kabla ya kukutakasa. Unapotubu unasamehewa na kutakaswa dhambi zako kisha unakua umefungua milango ya baraka. Huwezi kubarikiwa bila kutubu kweli.
Hakuna Binadamu anayemchukia Mungu kama hajichukii yeye mwenyewe na wale wanaomzunguka. Huwezi kusema humtaki Mungu kama hujichukii mwenyewe na wale waliokuzunguka vivyo hivyo huwezi kusema Unampenda Mungu kama hupendi wengine waliokuzunguka.
Recent Comments