ATUKUZWE BABA
Atukuzwe Baba
na Mwana
na Roho Mtakatifu
Kama mwanzo
na sasa,
na siku zote,
na milele.
Amina.
Atukuzwe Baba
na Mwana
na Roho Mtakatifu
Kama mwanzo
na sasa,
na siku zote,
na milele.
Amina.
Malkia wa mbingu, furahi, aleluya. Kwani uliyestahili kumchukua, Aleluya. Amefufuka alivyosema, Aleluya. Utuombee kwa Mungu, Aleluya. Furahi shangilia, ee Bikira Maria, Alaluya. Kwani hakika Bwana amefufuka Aleluya. Tuombe. Ee Mungu, uliyependa kuifurahisha dunia kwa kufufuka kwake Bwana wetu Yesu Kristu, Mwanao: fanyiza, twakuomba, kwa ajili ya Bikira Maria, tupate nasi furaha za uzima wa milele. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristu Bwana wetu. Amina.
Kwa njia ya Maji haya ya Baraka,
na kwa njia ya Damu yako azizi,
na kwa maombezi ya Moyo Safi wa Maria,
unioshe na uovu wangu wote na uwasaidie roho zinazoteseka toharani. Amina.
Kwa ajili ya Baba Mtakatifu wetu ..(N); Bwana, umpe moyo wako wa uchungaji mwema
Kwa ajili ya warithi wa Mitume; Bwana, uwape wawe na uangalifu uliojaa upendo kwa mapadre wao
Kwa ajili ya Maaskofu wako waliochaguliwa na Roho Mtakatifu; Bwana, uwabakishe karibu na kondoo wako
Kwa ajili ya wachungaji wako; Bwana, uwafundishe kutumikia kuliko kutafuta kutumikiwa
Kwa ajili ya waungamishi na washauri wa kiroho; Bwana, uwafanye kuwa vyombo visikivu kwa Roho wako Mtakatifu
Kwa ajili ya mapadre wanaotangaza neno lako; Bwana, uwawezeshe kushirikisha Roho wako na Uzima wako
Kwa ajili ya mapadre wanaosaidia utume wa walei; Bwana, uwatie moyo wa kuwa mifano bora
Kwa ajili ya mapadre wanaofanya kazi na vijana; Bwana, uwajalie wawakabidhi vijana kwako
Kwa ajili ya mapadre wanaofanya kazi kati ya watu fukara; Bwana, uwajalie wakuone na wakutumikie kupitia hao
Kwa ajili ya mapadre wanaoangalia wagonjwa; Bwana, uwajalie wawafundishe thamani ya mateso
Kwa ajili ya mapadre fukara; – Uwasaidie ee Bwana
Kwa ajili ya mapade wagonjwa; – Uwaponye ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wazee; – Uwapatie tumaini la raha ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wenye huzuni na walioumizwa; -Uwafariji ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wanaohangaishwa na wale wanaosumbuliwa; – Uwape amani yako ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wanaodharauliwa na wanaonyanyaswa; – Uwatetee ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre waliokata tamaa; – Uwatie moyo ee Bwana
Kwa ajili ya wale wanaosomea upadre; – Uwape udumifu ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wote; – Uwape uaminifu kwako na kwa Kanisa lako ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wote; – Uwajalie utii na upendo kwa Baba Mtakatifu na kwa maaskofu wao ee Bwana
Kwa ajili ya mapadre wote; – Uwajalie waishi katika umoja na maaskofu wao ee Bwana
Tunawaombea mapadre wote; – Wawe wamoja kama Wewe na Baba mlivyo wamoja ee Bwana
Tunawaombea mapadre wote; – Waishi na kuendeleza haki yako ee Bwana
Tunawaombea mapadre wote; – Washirikiane katika umoja wa ukuhani wako ee Bwana
Tunawaombea mapadre wote, wakiwa wamejawa na uwepo wako; – Waishi maisha yao ya useja kwa furaha ee Bwana
Tunawaombea mapadre wote; – Wajalie ukamilifu wa Roho wako na uwageuze wafanane nawe ee Bwana
Kwa namna ya pekee, ninawaombea mapadre wale ambao kwa njia yao nimepokea neema zako. Ninamwombea padre aliyenibatiza na wale walioniondolea dhambi zangu, wakinipatanisha na Wewe na Kanisa lako.
Ninawaombea mapadre ambao nimeshiriki Misa walizoadhimisha, na walionipa Mwili wako kama chakula. Ninawaombea mapadre walionishirikisha Neno lako, na wale walionisaidia na kuniongoza kwako. Amina.
Mungu wangu,
nakupenda zaidi ya cho chote,
kwani ndiwe mwema,
ndiwe mwenye kupendeza.
Nampenda na jirani yangu kama nafsi yangu,
kwa ajili yako.
Amina
✝⌚✝
Sala ya saa tisa🙏🏾
Kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu. A mina
Yesu, ulikufa, lakini chanzo cha uhai kilitoka kwa ajili ya watu, na bahari ya huruma ilifunguka kwa ajili ya ulimwengu mzima. Ee chemchemi ya Uhai, huruma ya Mungu isiyo na mwisho, ikafunika ulimwengu mzima na ukajimwaga mwenyewe juu yetu.
❣✝❣
✝Ee Damu na Maji, yaliyotoka moyoni mwa Yesu kama chemchemi ya Huruma kwetu. Nakutumainia.
(Mara tatu)
🛐❣🛐
1. HUDHURIA MISA TAKATIFU DOMINIKA NA SIKUKUU ZILZOAMRIWA
2. FUNGA SIKU YA JUMATANO YA MAJIVU; USILE NYAMA SIKU YA IJUMAA KUU
3. UNGAMA DHAMBI ZAKO WALAU MARA MOJA KILA MWAKA
4. POKEA EKARISTI TAKATIFU HASA WAKATI WA PASAKA
5. SADIA KANISA KATOLIKI KWA ZAKA
6. SHIKA SHERIA KATOLIKI ZA NDOA
Kwa nguvu zangu zote za moyo wangu/ ninakuabudu ee Moyo Mtakatifu/ na Mwabudiwa sana,/ Moyo Mtakatifu wa Bwana wetu Yesu Kristu/ ambao ninataka kumpenda/ na kukusalimu kwa usikivu unaoendelea./ Kamwe nisikuudhi tena/ kwa sababu Wewe ni Mwema sana;/ Ee Mwema sana./ Ee Moyo Mtakatifu sana/ ninakupenda/ na ninataka kukupenda zaidi ya vitu vyote,/ kwa nguvu zangu zote/ na kwa uwezo wangu wote,/ ninatamani kuwa mali yako/ Wewe uliyejitoa Msalabani kwa ajili yangu/ kwa mateso makali./ Unionee huruma na udhaifu wangu/ na usiniruhusu kupotea./
Ninajitoa kabisa kwako/ ee moyo wa mapendo,/ kwa makusudi kuwa utu wangu,/ maisha na mateso yangu/ yalipie kukupenda,/ kukuheshimu/ na kukutukuza Wewe sasa na milele./ Ninakupenda ee Moyo Mwabudiwa wa Mwokozi wangu,/ ninakuomba kwako/ uamuru moyo wangu na kila kitu ndani yangu/ kikutukuze sasa na milele./ Amina.
(Na Mt Margareta Maria Alakoki)
Kumheshimu Mungu wangu, Namtolea roho yangu, Nifanye kazi nipumzike, Amri zake tu nishike, Wazo neno tendo lote, Namtolea Mungu pote, Roho, mwili chote changu, pendo na uzima wangu, Mungu wangu nitampenda, Wala dhambi sitatenda, Jina lako nasifia, Utakalo hutimia, Kwa utii navumilia, Teso na matata pia, Nipe Bwana neema zako, Niongezee sifa yako, Amina.
Ee Mt. Yosefu, ambaye ulinzi wako ni mkubwa, wenye nguvu na wa haraka mbele ya Kiti cha Enzi cha Mungu, ninakukabidhi nia na haja zangu zote. Ee Mt. Yosefu, unisaidie kwa maombezi yako yenye nguvu, na unipatie kutoka kwa Mwanao Mungu, baraka zote za kiroho, kwa njia ya Kristu Bwana wetu, ili nikishapata msaada wako wa mbinguni ningali bado hapa duniani, niweze nami kumsifu, kumwabudu na kumshukuru Mungu aliye Baba mwema kabisa kushinda wote. Ee Mt. Yosefu, sichoki kamwe kufikiri moyoni kwa upendo, jinsi Mtoto Yesu alivyokuwa amesinzia mikononi mwako. Akiwa amepumzika hivyo karibu na moyo wako, sithubutu kujongea, nisije nikamsumbua, bali nakuomba wewe umkumbatie na kumbusu kwa niaba yangu na kumwambia anipe busu lake nitakapovuta pumzi yangu ya mwisho.
Mtakatifu Yosefu Msimamizi wa wanaozimia roho; Utuombee.
Amina.
Sala hii ilipatikana katika mwaka wa hamsini wa Bwana na Mwokozi Wetu Yesu Kristu. Mnamo mwaka 1505 Baba Mtakatifu alimtumia sala hii Mfalme Charles wakati alipokuwa anaenda vitani. Yeyote atakayeisoma sala hii, au kuisikia ikisomwa, au kuibeba, hatakufa kifo cha ghafla,hatazama majini, hatadhurika kwa sumu, wala hataanguka katika mikono ya adui zake, au kuunguzwa katika moto wowote ule, au kushindwa katika vita.
Sali sala hii kwa siku tisa mfululizo, kwa kuomba jambo lolote unalolihitaji. Haijawahi kusikika kuwa sala hii imeshindwa jambo.
Tumia tasbihi ya kawaida yenye chembe ndogo 53.
“Ee Yesu tupe moyo wako kama amana ya upendo wako na kimbilio letu, ili tupate pumziko salama wakati wa maisha yetu na faraja tamu saa ya kufa kwetu”.
Baba Yetu ……..
Salamu Maria ……. (mara tatu)
Nasadiki ………..
“Ninakuabudu, ninakutukuza na ninakupenda, Ee Moyo wa Yesu wangu mpenzi, uliopenywa na huzuni nyingi kwa ajili ya dhambi, ambazo zimekuwa zikitendwa hata leo, dhidi ya Sakramenti Takatifu sana ya Altare. Ninakutolea hapo kwa kuridhika, moyo wa Mama yako mpendevu, na mastahili ya watakatifu. Amina”.
“Ee Moyo Mtakatifu wa Yesu, uwakao mapendo kwetu, washa nyoyo zetu kwa mapendo yako”
Tuusifu Utatu Mtakatifu wa Mungu Mwenyezi, Baba, Mwana na Roho Mtakatifu, milele na milele, Amina.
Ee Utatu Mtakatifu wa Mwenyezi Mungu, Baba, Mwana na Roho Mtakatifu, nasadiki kuwa upo hapa na mahali pote. Ee Mungu wangu, umeniumba, umenikomboa, umenifanya mkristo, umenizidishia neema zako hapa duniani, umenitayarishia makao yangu mbinguni, umenijalia na siku hii nikutumikie. Ee Mungu wangu! Nakuabudu, nakushukuru, nakuomba toba, nakupenda! Ee Mungu wangu, nakutolea roho yangu, na mawazo, na maneno, na kazi, na furaha, na mateso yangu: uyapokee unipe neema yako nisikutende leo dhambi!
Bwana utuhurumie Bwana utuhurumie
Kristo utuhurumie Bwana utuhurumie
Bwana utuhurumie Bwana utuhurumie
Kristo utusikie – Kristo utusikilize
Mungu Baba wa Mbinguni, Utuhurumie
Mungu Mwana, Mkombozi wa dunia Utuhurumie
Mungu Roho Mtakatifu Utuhurumie
Utatu Mtakatifu Mungu MMoja Utuhurumie
Maria Mtakatifu Utuombee (iwe kiitikio)
Mama wa Mkombozi wetu,
Mama mwenye mateso,
Malkia wa mashahidi,
Mama wa wenye uchungu,
Mfariji wa wenye taabu,
Msaada wa wenye shida,
Mlinzi wa wenye upweke,
Nguvu ya dhaifu moyoni,
Makimbilio ya wakosefu,
Afya ya wagonjwa,
Matumaini ya wanaozimia,
Kwa ajili ya ufukara wako ulioona pangoni Bethlehemu, – Utusaidie ee Mama wa mateso (iwe kiitikio)
Kwa ajili ya mateso yako uliyoona katika uaguzi wa Simeoni,
Kwa ajili ya taabu zako ulizopata katika safari ya Misri,
Kwa uchungu wako, Mwanao alipopotea,
Kwa ajili ya huzuni yako Mwanao alipodhulumiwa,
Kwa ajili ya hofu yako Yesu alipokamatwa,
Kwa ajili ya uchungu wako ulipokutana na Yesu katika njia ya Msalaba,
Kwa ajili ya mateso ya Moyo wako aliposulibiwa,
Kwa ajili ya mateso yako makali Yesu alipokufa,
Kwa ajili ya kilio chako juu ya Mwanao mpenzi,
Kwa ajili ya uchungu wako penye kaburi la Mwanao,
Kwa ajili ya upweke wako baada ya maziko ya Mwanao,
Kwa ajili ya uvumilivu wako katika shida zote,
Katika uchungu wetu wote,
Katika ugonjwa na mateso,
Katika huzuni na shida,
Katika umaskini na upweke,
Katika mahangaiko na hatari,
Katika vishawisho vyote,
Katika saa ya kifo chetu,
Katika hukumu ya mwisho,
Mwanakondoo wa Mungu, unayeondoa dhambi za dunia, Utusamehe ee Bwana.
Mwanakondoo wa Mungu, unayeondoa dhambi za dunia, Utusikilize ee Bwana.
Mwanakondoo wa Mungu, unayeondoa dhambi za dunia, Utuhurumie.
Kristo utusikie – Kristo utusikilize
Bwana utuhurumie – Kristo utuhurumie
Bwana utuhurumie.
Baba Yetu ….
Utuombee, ee Mama wa Mateso
Tujaliwe kupewa ahadi za Kristo.
TUOMBE: Ee Bwana Yesu Kristo, utusaidie sasa na saa ya kifo chetu msaada wa Bikira Maria Mama yako, ambaye moyo wake mtakatifu ulichomwa na upanga wa mateso ulipoteswa na kufa msalabani. Unayeishi na kutawala milele na milele. Amina.
Utukuzwe ee Bwana wangu Yesu Kristo./ Uliagua kifo chako./ Katika karamu ya mwisho ulitumia mkate wa kidunia/ ukafanya mwujiza na kuugeuza/ kuwa Mwili wako azizi./ Kwa mapendo ukawapa Mitume Mwili huo/ uwe kumbukumbu la mateso yako mastahivu./ Uliwaosha miguu kwa Mikono yako Mitakatifu./
Uheshimiwe, ee Bwana wangu Yesu Kristo./ Kwa kuhofu mateso na kifo,/ Mwili wako usio na kosa ulitoka jasho la damu/ badala ya maji./ Juu ya hayo uliutimiza wokovu wetu/ uliokuwa umetaka kuufanya./ Hivyo ulionyesha waziwazi mapendo yako/ uliyo nayo kwa wanadamu./
Utukuzwe, ee Bwana wangu Yesu Kristo./ Ulipelekwa kwa Kayafa,/ Wewe uliye Hakimu wa wote./ Ukaruhusu kwa unyenyekevu kutolewa kwa Pilato/ uhukumiwe naye./
Utukufu uwe nawe, Bwana wangu Yesu Kristo,/ kwa kuwa ulivumilia kuchekwa tena/ uliposimama huko,/ umevaa joho jekundu,/ umetiwa taji ya miiba mikali sana Kichwani,/ ukavumilia kwa saburi kubwa/ kutemewa mate katika Uso wako mzuri,/ kufumbwa Macho,/ na kupigwa mno na wajeuri/ ngumi na makofi Mashavuni na Shingoni./
Sifa iwe nawe, Bwana wangu Yesu Kristo,/ Kwa uvumilivu mkubwa ulikubali kufungwa nguzoni,/ kupigwa mijeledi kijeuri,/ kujaa damu na hivyo kusukumwa barazani kwa Pilato./ Ulionekana kama mwanakondoo asiye na kosa./
Heshima iwe nawe, Bwana wangu Yesu Kristo./ Umehukumiwa Mwili wako mzima/ Mtukufu wenye kutoka damu/ ufe msalabani./ Ulichukua msalaba kwa Mabega yako Matakatifu/ na kuumwa sana./ Kwa ghadhabu walikusukuma mbele/ mpaka mahali pa mateso,/ wakakunyang’anya nguo zako./ Hivyo ulikubali kupigiliwa msalabani./
Heshima ya milele upate Wewe,/ Bwana wangu Yesu Kristo./ Ulipokuwa katika taabu kubwa hii,/ ulimkazia Mama yako mstahivu/ Macho yako ya hisani na mapendo/ na unyenyekevu,/ ndiye Mama yako asiyekosa hata mara moja/ wala kukubali dhambi yeyote./ Ulimweka katika ulinzi mwaminifu/ wa Mfuasi wako ili kumtuliza./
Milele utukuzwe, ee Bwana wangu Yesu Kristo./ Ulipokuwa mwenyewe taabani,/ uliwapa wakosefu wote/ matumaini ya kuondolewa dhambi/ kwa kumwahidia mnyang’anyi aliyekuendea/ utukufu wa paradisi kwa huruma yako./
Sifa ya milele iwe nawe, Bwana wangu Yesu Kristo,/ kwa kila saa ulipovumilia uchungu/ na taabu kubwa mno msalabani kwa ajili yetu sisi wakosefu,/ maumivu makali sana/ yaliyotoka katika majeraha yako,/ yakapenya bila huruma Roho yako Takatifu./ Yakaingia kikatili katika Moyo wako Mtakatifu/ hata ukakatika,/ ukapumua Roho yako,/ ukainama Kichwa,/ ukaweka Roho yako mikononi mwa Mungu, Baba yako./ Na baada ya kufa uliacha nyuma Mwili baridi./
Utukuzwe, ee Bwana wangu Yesu Kristo,/ kwa Damu yako azizi na kwa kifo chako kitakatifu/ ulizifidia roho za watu,/ ukazitoa ugenini/ na kuzipeleka kwa hisani yako katika uzima wa milele./
Milele uheshimiwe, Wewe Bwana wangu Yesu Kristo./ Siku ya tatu ulifufuka katika wafu,/ ukajionyesha kwa wafuasi wako,/ ukapaa mbinguni/ mbele ya macho yao siku ya arobaini./
Shangilio na sifa ya milele upate Wewe, Bwana wangu Yesu Kristo,/ kwa kuwa umewapelekea wafuasi wako mioyoni mwao/ Roho Mtakatifu,/ ukawasha rohoni mwao mapendo makuu ya Mungu./
Pia, utukuzwe, usifiwe na kushangiliwa milele, Bwana wangu Yesu Kristo./ Umekaa katika ufalme wako wa mbinguni/ juu ya kiti cha enzi cha Umungu wako,/ ukaishi pamoja na Viungo vyako vyote Vitakatifu./ Na hivyo utakuja tena/ kuzihukumu roho za wazima na wafu wote./ Unaishi na kutawala/ pamoja na Baba na Roho Mtakatifu,/ milele. Amina.
(Na Mt. Birgita wa Sweden)
Baba yetu uliye mbinguni
Jina lako litukuzwe
Ufalme wako ufike
Utakalo lifanyike
Duniani kama mbinguni
Utupe leo mkate wetu wa kila siku
Utusamehe makosa yetu
Kama tunavyowasamehe
Na sisi waliotukosea
Usitutie katika kishawishi
Lakini utuopoe maovuni.
Amina.

Anza kusali Rozari kwa kuibusu miguu ya Bwana Yesu katika taswira (picha) yake Msalabani kisha fanya Ishara ya Msalaba ukiwa unasema “Kwa Jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu, Amina”.
Taja kwa ufupi nia za Rozari hii. Tangaza nia hizo kwa sauti kama mnasali wengi kwa pamoja, Mfano, “Tusali kuombea amani katika nchi yetu na ulimwenguni kote, na tuunganishe nia hizo na nia zetu sisi wenyewe, nk).
Baada ya Sala ya Nasadiki pamoja na ya Baba Yetu, tunamwomba Mungu (Utatu Mtakatifu) fadhila za Imani, Matumaini na Mapendo, zikiambatana na Salamu Maria tatu.
Mojawapo ya maneno yafuatayo huweza kutumika:
“Mungu Baba utuongezee Imani. Salamu Maria, …… Mungu Mwana utuongezee matumaini, Salamu Maria, …… Mungu Roho Mtakatifu washa nyoyo zetu kwa mapendo yako, Salamu Maria, …..”
Au;
“Utuongezee Imani ee Bwana, Salamu Maria,…. Utuongezee matumaini ee Bwana, Salamu Maria,…. Uwashe nyoyo zetu kwa mapendo yako ee Bwana, Salamu Maria, …..” Au;
“Salamu e uliyechaguliwa na Mungu Baba, Salamu Maria,….. Salamu e Mama wa Mungu Mwana, Salamu Maria,….. Salamu e Mchumba wa Mungu Roho Mtakatifu, Salamu Maria,……”
Atukuzwe Baba, na Mwana na Roho Mtakatifu, kama mwanzo na sasa na siku zote, na milele, Amina.
Ee Yesu wangu, utusamehe dhambi zetu, utuepushe na moto wa milele, ongoza roho zote mbinguni, hasa za wale wanaohitaji huruma yako zaidi.
Tuwasifu milele, Yesu, Maria na Yosef.
Kisha endelea na sala zinazofuata kama mpangilio unavyoonyesha hapo juu.
Kila baada ya Tendo moja na makumi ya Salamu Maria…, “Atukuzwe..”, “Ee Yesu wangu…” na “Tuwasifu milele…” kama muda unatosha wimbo ufaao wa Bikira Maria uimbwe (kama muda ni mfupi basi angalau ubeti mmoja mmoja uimbwe kila baada ya makumi hayo). Baada ya Wimbo, Tendo linalofuata litangazwe kwa sauti pamoja na tafakari fupi au ombi linaloambatana na Tendo husika kama inavyoonyeshwa hapa chini.
Tendo la kwanza; Malaika Gabrieli anampasha habari Maria kuwa atakuwa Mama wa Mungu. Tumwombe Mungu atujalie unyenyekevu.
Tendo la pili; Maria Mtakatifu anakwenda kumtembelea Elizabeti. Tumwombe Mungu atujalie mapendo ya jirani.
Tendo la tatu; Yesu anazaliwa Betlehemu. Tumwombe Mungu atujalie moyo wa ufukara
Tendo la nne; Yesu anatolewa hekaluni. Tumwombe Mungu atujalie usafi wa moyo.
Tendo la tano; Maria anamkuta Yesu hekaluni. Tumwombe Mungu atujalie kuwatii wakubwa wetu.
Tendo la kwanza; Yesu anatoka jasho la damu kwa ajili yetu. Tumwombe Mungu atujalie sikitiko la dhambi.
Tendo la pili; Yesu anapigwa kwa mijeledi kwa ajili yetu. Tumwombe Mungu atujalie kuacha dhambi za uchafu.
Tendo la tatu; Yesu anatiwa miiba kichwani kwa ajili yetu. Tumwombe Mungu atujalie kushinda kiburi.
Tendo la nne; Yesu anachukua Msalaba kwa ajili yetu. Tumwombe Mungu atujalie kuvumilia taabu.
Tendo la tano; Yesu anakufa Msalabani. Tumwombe Mungu atujalie kuwapenda Yesu na Maria.
Tendo la kwanza; Yesu anafufuka. Tumwombe Mungu atujalie kugeuka watakatifu.
Tendo la pili; Yesu anapaa mbinguni. Tumwombe Mungu atujalie kwenda mbinguni.
Tendo la tatu; Roho Mtakatifu anawashukia Mitume. Tumwombe Mungu atujalie bidii katika dini yetu.
Tendo la nne; Bikira Maria anapalizwa mbinguni. Tumwombe Mungu atujalie kufa vizuri.
Tendo la tano; Bikira Maria anawekwa Malkia mbinguni. Tumwombe Mungu atujalie kudumu katika njia njema.
Tendo la kwanza; Yesu anabatizwa Mto Jordani. Tumwombe Mungu atujalie uaminifu kwa ahadi zetu za ubatizo.
Tendo la pili; Yesu anageuza maji kuwa divai huko Kana. Tumwombe Mungu atujalie kuukoleza ulimwengu kwa chachu ya enjili.
Tendo la tatu; Yesu anatangaza Ufalme wa Mungu. Tumwombe Mungu atujalie kupokea Ufalme wake kwa toba ya kweli.
Tendo la nne; Yesu anageuka sura. Tumwombe Mungu atujalie neema ya kuung’arisha ulimwengu kwa uso wa Yesu.
Tendo la tano; Yesu anaweka Sakramenti ya Ekaristia. Tumwombe Mungu atujalie neema ya kujitoa sadaka kwa ajili ya wengine.
Ee Bwana Mungu, utujalie sisi watumishi wako afya ya roho na mwili siku zote; na kwa maombezi matukufu ya Maria Mtakaatifu Bikira daima, tuopolewe na mashaka ya saa, tupate na furaha za milele. Kwa Kristo Bwana wetu, Amina.
Karibu Vitatabu vya Kikatoliki
Salamu Maria
Umejaa neema
Bwana yu nawe
Umebarikiwa kuliko wanawake wote
Na Yesu mzao wa tumbo lako amebarikiwa
Maria Mtakatifu
Mama wa Mungu
Utuombee sisi wakosefu
Sasa, na saa ya kufa kwetu.
Amina.
Ufuatao ni mtiririko wa Novena ya Roho Mtakatifu kwa siku zote tisa.
Kusali novena hii unaanza nia wimbo/nyimbo kisha unasali sala ya kila siku na kumalizia na litania na Atukuzwe Baba….x3 kwa siku zote tisa.
/Njoo wangu Mfariji
Yako shusha mapaji
Roho Mungu njoo/
1. Hekima nishushie, Mungu nimfuatie, Roho Mungu njoo
2. Akili nijalie, imani nizidie, Roho Mungu njoo
3. Nieneze shauri, imani nizidie, Roho Mungu njoo
4. Nizidishie nguvu, nsifanye ulegevu, Roho Mungu njoo
5. Elimu nieleze, hakika niongoze, Roho Mungu njoo
6. Ibada niwashie, Peke nikupupie, Roho Mungu njoo
7. Uchaji nitilie, dhambi nizichukie, Roho Mungu njoo.
/Njoo Roho Mtakatifu, shusha mapaji (kweli) niwe imara x2
Leta nuru ya mwanga wako, ifikie moyoni mwangu x2/
1. Roho mwenye hekima, Roho wa shauri na nguvu
2. Nipatie elimu nitambue nafsi yako
3. Nipatie ibada nikusifu daima milele
4. Roho mwenye uchaji washa moto wako wa mapendo
1. Uje Roho Mtakatifu, tuangaze toka mbingu, roho zetu kwa mwangao
2. Uje Baba wa maskini, uje mtoa wa vipaji, uje mwanga wa mioyo
3. Ee Mfariji mwema sana, ee Rafiki Mwanana, ewe raha mustarehe
4. Kwenye kazi u pumziko, kwenye joto burudisho, u mfutaji wa machozi
5. Ewe mwanga wenye heri, uwajaze waumini, neema yako mioyoni
6. Bila nguvu yako Wewe, mwanadamu hana kitu, kwake yote yana kosa
7. Osha machafuko yetu, panyeshee pakavu petu, na kuponya majeraha
8. Ulegeze ukaidi, pasha moto ubaridi, nyosha upotovu wote
9. Wape waamini wako, wenye tumaini kwako, paji zako zote saba
10. Wape tuzo ya fadhila, wape mwisho bila hila, wape heri ya milele.
11. Amina aleluya, amina aleluya, amina aleluya.
1. Njoo Roho Mtakatifu, angalia zetu nyoyo, waletee neema nguvu, wakosefu viumbevyo.
2. Majina yako Mfariji, shina la uzima pendo, wake Mwenyezi upaji, mafuta ya roho moto
3. Ndiwe mnye mapaji saba, wa Mungu kuume mkono, mshika uhadi wa Baba, mtoa kwa ndimi maneno
4. Angalo litung’arie, moyo kwa pendo tushushe, nguvu neema tujalie, wanyonge wasabilitishe
5. Shetani mbali mkimbize, amani utupatie, tukufuate tuongoze, maovu utukingie
6. Baba Mungu tujulishe, pia Mwana tumkubali, Roho tukuungamie, mtokea wao wawili.
Yesu alipokuwa akiagana na mitume wake, kabla ya kupaa mbinguni, aliwaambia wasiondoke Yerusalemu mpaka hapo watakapokuwa wamempokea Roho Mtakatifu. Aliwaambia: “Wakati Roho Mtakatifu atakapowashukieni, mtajazwa nguvu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika nchi yote ya Yuda na Samaria, hata kwenye mipaka yote ya dunia.” (Mdo.1:8)
Waliendelea kusali pamoja toka hapo Yesu alipopaa mbinguni mpaka siku ya Pentekoste. Waliomba Roho Mtakatifu awashukie, awajaze na mapaji yake. Na baada ya siku tisa Roho Mtakatifu aliwashukia hao kundi dogo nao wakawa chanzo cha Kanisa lililopata kuenea duniani kote.
Siku hizo tisa za kusali zinaitwa NOVENA; na kila mwaka wakati huu, wakristu wakifuata mfano wa mitume, wanasali muda wa siku tisa kabla ya Sikukuu ya Pentekoste. Wanamuomba Roho Mtakatifu awashukie, awajaze nguvu na wingi wa mapaji yake.
Wakati huu wa NOVENA , Tunayo mengi ya kuliombea Kanisa na kujiombea sisi wenyewe. Kwa hiyo tumuombe Roho Mtakatifu atusaidie kusali vema na kuomba yale yote tunayohitaji kwa maslahi yetu ya roho na mwili.
Na kama mtume Paulo alivyowaambia wale waKristu wa kwanza, Roho Mtakatifu huja kutufatiji katika udhaifu wetu. Basi tumuombe atufariji kwa sala hizi za NOVENA, Atuwezeshe kusali na kuomba inavyotupasa kusali.
1. Ee Baba wa milele, tunakuomba umtume Roho Mtakatifu atushukie sisi taifa lako awashe ndani yetu moto wa upendo wako.
W. Twakuomba utusikie.
2. Ee Baba mwema, tunakuomba utujalie faraja ya Roho Mtakatifu sisi wana tulio katika dhiki na taabu nyingi mno hapa duniani.
W. Twakuomba utusikie.
3. Ulijalie Kanisa lako mapaji ya Roho wako Mtakatifu, liweze kutekeleza vema utume wake wa kuhudumia watu wote hapa duniani.
W. Twakuomba utusikie.
4. Utujalie sisi kudumu katika NOVENA hii mpaka mwisho kama Maria na mitume walivyodumu pamoja wakisali kabla ya Pentekoste ile ya kwanza.
W. Twakuomba utusikie.
5. Utujalie neema zote zinazohitajika ili tuweze kumshuhudia Kristu popote kwa mwenendo na matendo yetu ya kila siku, tukiongozwa na Roho Mtakatifu.
W. Twakuomba utusikie
6. Uzijalie familia zote za wakristu neema na nguvu za Roho Mtakatifu tupate kuendelea pasipo kuchoka katika sala na katika matendo mema siku zote.
W. Twakuomba utusikie
7. Ewe Roho Mtakatifu, uwajalie vijana wetu moyo wa ujasiri, wapate kulijenga kanisa lako na kueneza utawala wako katika jumuia zetu za Kikristu.
W. Twakuomba utusikie.
Ee Mungu, uliye muumba wa vitu vyote , tunakuomba utusikilize kwa wema sala zetu sisi taifa lako, utuongoze sote tufuate siku zote utaratibu wa mapenzi yako; naye Roho Mtakatifu atutegemeze mpaka mwisho wa novena hii. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristu Bwana wetu .
W. Amina.
“Kweli nakwambia, mtu asipozaliwa kwa maji na Roho, hawezi kamwe kuingia katika utawala wa Mungu,” (Yn. 3:5).
Kanisa limepewa na Yesu ujumbe wa kuwaletea watu wote uzima mpya, uzima wa Mungu. Yesu aliwaambia mitume wake: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani. Nendeni basi mkawafanye watu wa makabila yote kuwa wafuasi wangu. Wabatizeni kwa Jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu. Wafundisheni kuyashika maagizo yote niliyowapeni. Nami nipo pamoja nanyi siku zote mpaka mwisho wa nyakati (Mt.28: 18-20).
Sisi tuliobatizwa tumepata kuwa viungo vilivyo hai vya Mwili wa Fumbo wa Kristu; kwa Kipaimara tumeimarishwa na kuthibitishwa na Roho Mtakatifu. Tumekuwa taifa teule. Tumeshirikishwa ule ukuhani wa Kristu. Tumepokea ujumbe wa kueneza utawala wa Mungu.
Tunapopokea Sakramenti, na hasa ile Sakmenti ya Ekaristi, tunalisha imani na kuongeza mapendo, ambayo ni msingi wa utume wowote ule. Mapendo yanatuhimiza kueneza utawala wa Mungu na kumpenda Yesu Kristu aliyekuja kuwakomboa wanadamu wote.
Kila aliyebatizwa anao wajibu wa kueneza imani ya Mungu na utawala wake. Kwa hiyo tumuombe Roho Mtakatifu atuwezeshe kutimiza wito huo.
1. Ee Baba wa mbinguni tunakuomba umpeleke Roho Mtakatifu aliangaze kanisa na kuliongoza, liweze kuwafikishia mataifa yote habari njema ya wokovu.
W. Twakuomba utusikie
2. Ee Yesu Mkombozi wetu, umtume Roho Mtakatifu awahimize wakristu wapate kutimiza wajibu wao wa kueneza neno lako popote duniani
W. Twakuomba utusikie
3. Ewe Roho Mtakatifu Mfariji, uamshe katika mioyo ya vijana wengi hamu ya kupenda kulitumikia kanisa lako na kulihudumia taifa lako kwa uaminifu.
W. Twakuomba utusikie
4. Ewe mwanga wa mataifa , uwajalie wanafunzi wasikie sauti yako mioyoni mwao, nawe unapowaita wasikose kuisikia sauti yako, wawe tayari kujitoa kwa ajili ya ndugu zao.
W. Twakuomba utusikie.
5. Uwasaidie wazazi wawalee vema watoto wao; uwatie moyo katika wito wao, wapate pia kuishiriki vema ile kazi ya kueneza neno lako kwa jirani zao.
W. Twakuomba utusikie
6. Ewe Roho Mtakatifu, uwasaidie wakristu wote kueneza habari njema ya wokovu, kwa sala, kwa sadaka na kwa mifano ya maisha yao ya uchaji.
W. Twakuomba utusikie
7. Ewe mpaji wa mema, uwajalie waumini mapaji yako saba, wasichoke kulieneza neno lako kwa hekima pasipo hofu.
W. Twakuomba utusikie.
Ee Mungu, unapenda watu wote waokoke, waifikie kweli yako. Tunakuomba uwapeleke wafanyakazi walio wengi na wema katika shamba lako. Uwajalie kulihubiri neno lako kwa imani kuu ili neno lako lienee na kupokewa na mataifa yote, wapate nao kukujua wewe peke yako Mungu wao, Mungu wa kweli. Tunaomba hayo kwa nguvu ya Roho Mtakatifu anayeliongoza kanisa lako sasa na milele.
W. Amina
Bwana alisema kwa kinywa cha nabii Yoeli; “Katika siku zile za mwisho asema Bwana, nitawamiminia binadamu wote Roho wangu. Watoto wenu, waume kwa wake, watautangaza ujumbe wangu; vijana wenu wataona maono, na wazee wenu wataota ndoto….hata watumishi wenu watamiminiwa Roho wangu katika siku zile, nao watautangaza ujumbe wangu. (Mdo.2:17-21)
Siku ile ya Pentekoste, bada ya Roho Mtakatifu kulishukia kanisa, mitume waliwakumbusha watu maneno haya ya nabii Yoeli, na miaka mingi baadae, Petro aliwaandikia barua Wakristu wa kwanza akawaambia; kila mmoja anapaswa kutumia kipaji alichojaliwa na Mungu kwa faida ya wengine, kama vile wakili mwema wa zawadi mbali mbali za Mungu. Anayesema kitu, maneno yake na yawe kama maneno ya Mungu; anayetumikia anapaswa kutumikia kwa nguvu aliyojaliwa na Mungu ili katika mambo yote, Mungu atukuzwe kwa njia ya Yesu Kristu, ambaye utukufu na nguvu ni vyake milele na milele (Pet 4;10-11).
Mtaguso wa Pili wa Vatikano ulitukumbusha jambo hilo hilo uliposema; “Roho Mtakatifu anayetakasa taifa la Mungu kwa njia ya Sakramenti amewapa waumini mapaji ya pekee na kumjalia kila mmoja kadiri apendavyo. Kwa hiyo kila mmoja amgawie mwenzake kadiri ya vipawa alivyopewa, awe mgawaji mwaminifu wa neema ya Mungu, alijenge kanisa zima katika upendo.
Tunao wajibu wa kutumia vipawa tulivyojaliwa na Roho Mtakatifu kwa manufaa ya kanisa zima, na kwa faida ya watu wote. Tuunganike sote pamoja na wachungaji wote katika kazi hiyo ya utume. Tumuombe basi Roho Mtakatifu atusaidie kutumia vema vipawa vyake alivyotujalia.
1. Ewe Roho Mtakatifu uwape wakristu neema na nguvu za kutumia vema vipaji ulivyowajalia kwa ajili ya kujenga kanisa lako popote duniani, kwa ajili ya wokovu wa watu wote
W. Twakuomba utusikie
2. Utujalie sisi sote mapaji yako saba, tupate kukutumikia kwa uchaji
W. Twakuomba utusikie
3. Utujalie tuwe mitume wa kweli wa wenzetu, tushirikiane na wachungaji wetu katika huduma za kuwaongoza watu wote na kuwafikisha mbinguni
W. Twakuomba utusikie.
4. Utujalie hekima na nguvu za kuwahudumia watu wote kwa mapendo ya kweli yasiyo na kinyume
W. Twakuomba utusikie
5. Utujalie neema ya kumpenda Mungu kwa moyo wote na kuwapenda jirani zetu kama tunavyojipenda wenyewe
W. Twakuomba utusikie
6. Utupe neema ya kulisikia neno lako na kulifuata, nayo mawazo yetu na matendo yetu yafuate daima mwongozo wako mtakatifu
W. Twakuomba utusikie
7. Uwazidishie mapaji yako wale wote wanaotumia vyema vipawa vyao, uwarudishe na wale wanaotumia vibaya rehema zako
W. Twakuomba utusikie
=== TUOMBE;
Ewe Roho Mungu ndiwe uliyewapa waumini vipawa vyako kwa kadiri unavyotaka. Utujalie tuyapokee na kuyatumia vyema mapaji yako mengi kwa ajili ya utukufu wa Jina lako na kwa ajili ya wokovu wa watu wote. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristu Bwana wetu.
W. Amina
“Atakapokuja huyu Roho wa kweli , atawaongoza kwenye ukweli wote” (Yn 16:13)
Baada ya kusema hayo, Yesu aliinua macho yake kuelekea mbinguni akasema “Mimi nimekutukuza hapa duniani; nimeikamilisha kazi uliyonipa niifanye. Naomba ili wote wawe kitu kimoja kusudi ulimwengu upate kuamini kwamba Wewe ulinituma (Yn 17:4,21).
Nasi twamuomba Mungu Mwenyezi alijalie kanisa lake umoja wa kweli, awaunganishe wakristu wa madhehebu yote katika zizi moja chini ya mchungaji mmoja.
Popote duniani watu wengi, makundi kwa makundi wanavutwa na neema hiyo ya kuungana na kuufikia umoja wa Kanisa. Hata ndugu zetu waliotengana nasi wanazidi kukubali mwongozo wa Roho Mtakatifu na kutaka kurudi katika nyumba ya Baba na kuwa kundi moja chini ya mchungaji mmoja. Isitoshe, hata sasa tena twaweza kuona kwamba kwa namna fulani wamejiunga nasi katika Roho Mtakatifu, naye Roho Mtakatifu anafanya kazi ndani yao kumshuhudia hata kwa kumwaga damu yao.
Tena katika hao ndugu zetu waliojitenga, Roho Mtakatifu analisha katika mioyo yao ile ya imani inayowaunganisha wafuasi wote wa Kristu. Tumwombe basi Mwenyezi Mungu atujalie hima huo umoja wa Kanisa lake tunaouania mno.
1. Ee Yesu Bwana wetu wewe umetuombea kwa Mungu Baba tuwe itu kimoja kama Wewe ulivyo kitu kimoja na Baba. Utujalie huo umoja, ili ulimwengu uone na kukiri kwamba ndiwe Bwana na Mkombozi wa watu wote
W. Twakuomba utusikie
2. Ee Yesu utujalie moyo wa kulishika neno lako kwa uaminifu, wala usituache kufuata njia zetu sisi wenyewe na kufarakana.
W. Twakuomba utusikie
3. Ee Yesu uliye Mchungaji wetu mwema, ondoa ndani yetu ile tabia ya utengano, tupate kuwa sote kundi moja chini yako wewe uliye mchungaji wetu mmoja.
W. Twakuomba utusikie
4. Ee Yesu, uliye Mchungaji mkuu, uwajalie wachungaji wetu wawe siku zote na upendo wa Jina lako, wasichoke kulichunga vema kundi lako hapa duniani na kuliweka pamoja lisitengane
W. Twakuombaa utusikie
5. Ewe Roho Mtakatifu, uziangaze akili za watu wote, wapende siku zote kuishi kwa amani, umoja na mapendano
W. Twakuomba utusikie
6. Ee Mungu, utufungulie …… wa muungano wako wa kweli sisi tulio ndugu katika Bwana wetu Yesu Kristu.
W. Twakuomba utusikie
7. Utujalie mapatano na amani, tudumu tumeungana katika familia zetu, katika jimbo letu na katika nchi yetu yote.
W. Twakuomba utusikie.
Ee Mungu, utuunganishe sisi kondoo wako tuliotawanyika, tuwe chini ya Mwanao mpenzi, tupate sote kuushiriki ule utawala wako wa kweli na haki, utawala wa neema na amani, utawala wa upendo wako. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristu Bwana wetu
W. Amina
Walio wa Mungu watafuata yaliyo ya Mungu, na walio wa dunia hufuata yaliyo ya dunia,. Ni mauti kutosheka na mambo yaliyo ya dunia. Uzima na faraja ya kweli hupatikana tu katika mambo ya Mungu.
Kwa nguvu zetu sisi wenyewe hatuwezi kutenda lolote jema. Kuweza kwetu kwatoka kwa Mungu, kwatoka kwa Yeye anayetupa kujua, kupenda na kutenda.
Mtu anapotenda dhambi, hawezi kuongoka ila kwa msaada wa Roho Mtakatifu, ndiye anayempa mkosefu neema ya kutambua ubaya wa kosa lakena kuamua kuliacha. Ndiye anayempa pia mkosefu kutambua uzuri wa neema aliyoipoteza na kumrudishia neema hiyo. Ndiye anayempa nguvu za kuidumisha neema hiyo na kuiongeza.
Isitoshe, Roho Mtakatifu ndiye anayemuwezesha mtu kuwa na maendeleo katika fadhila na utakatifu. Ndiye anayemjalia imani iliyo msingi wa maisha ya kiKristu. Ndie anayetujalia akili ya kushika mafumbo ya dini yetu na kuishi imani yetu mpaka kufa.
Lakini imani peke yake haimtoshi mtu aokoke. Imani pasipo matendo haifai kitu; imani bila matendo imekufa (Yak 2:28) Roho Mtakatifu anamuwezesha mtu kumuamini Mungu na kumenda kuliko vitu vyote na kumpenda jirani kama kujipenda mwenyewe. Ndiyo maana Roho Mtakatifu huitwa chanzo cha matendo yetu yote yaliyo mema. Basi, tumuombe Roho Mtakatifu aitakase mioyo yetu sisi waumini wake, atuzidishie imani, atuwezeshe kutenda matendo yaliyojaa imani.
1. Ewe Roho Mtakatifu, utudumishie imani, uyatakase mawazo ya mioyo yetu yafuate daima maongozi yako na amri zako
W. Twakuomba utusikie
2. Uzigeuze nia zetu zipate kumuelekea daima Mungu
W. Twakuomba utusikie
3. Utuwezeshe kuelekea katika utakatifu na kutenda mema kwa imani siku zote za maisha yetu
W. Twakuomba utusikie
4. Utuzidishie imani matumaini na mapendo, tuweze kushika kwa moyo thabiti yale yote tunayofundishwa na kanisa lako takatifu
W. Twakuomba utusikie
5. Uiwashe mioyo yetu na moto wa mapendo yako, tupate kumpenda Mungu kweli na kumpenda jirani yetu pasipo unafiki.
W. Twakuomba utusikie
6. Utusaidie tuishi vema kwa imani na matumaini siku zote za maisha yetu
W. Twakuomba utusikie
7. Utujalie kudumisha mioyoni mwetu ile neema ya utakaso tuliyoipata mwanzo katika ubatizo wetu
W. Twakuomba utusikie
Ee Mungu, mbele yako mioyo yetu i wazi; wewe wayajua yote, wala hakuna siri iliyofichika mbele yako. Uyatakase mawazo ya mioyo yetu kwa kutupelekea Roho Mtakatifu, ili tuweze kukupenda na kukutukuza kama inavyostahili. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristu Bwana wetu
W. Amina
“Nitamuomba Baba , naye atawapelekea Mfariji mwingine atakaye kaa nanyi siku zote”. Katika maisha yenu hapa duniani tunahitaji mno kitulizo cha Mungu. Ni jambo la hekima kutafuta kitulizo hicho kwa Mungu wala si kwa viumbe; maana kitulizo kinachopatikana kwa viumbe hapa duniani hakidumu; bali kitulizo kitokacho kwa Mungu ni cha kudumu.
Roho Mtakatifu ndio kitulizo chetu cha kweli. Baba ndiye aliyetuumba, Mwana ndiye aliyetukomboa, Roho Mtakatifu ndiye aliyetutakasa mioyo yetu na kutufariji.
Kazi ya Roho Mtakatifu sio tu kuwatuliza wale walio na huzuni, bali pia kuwapa moyo wa kuvumilia taabu zozote kwa saburi.
Tunahitaji nguvu ya Roho Mtakatifu ili tuweze kuishi maisha mema ya kikristu. Katika juhudi zetu za kumtumikia Mungu mara nyingi tunakutana na shida; naye Roho Mtakatifu ndie anayetufariji kwa kutupa nguvu za kupambana na matatizo yote. Maisha yetu hapa duniani yamejaa misalaba. Na misalaba hiyo hatuwezi kuichukua kwa nguvu zetu wenyewe. Roho Mtakatifu ndie anayetupa nguvu za kuvumilia. Basi, tumuombe aje kutufariji na kutupa nguvu za kuchukua msalaba wetu kwa saburi kila siku.
1. Ee Yesu Bwana wetu, tunakusihi Wewe na Baba mumtume Roho Mtakatifu atufariji, awajalie kitulizo wale wote walio katika taabu na majonzi
W. Twakuomba utusikie
2. Ewe Roho Mtakatifu, uwafariji wale walio katika tabu za namna zozote ili waweze kuvumilia kwa saburi mateso yao kwa faida ya Roho zao na roho za ndugu zao.
W. Twakuomba utusikie
3. Uwafariji wale walio wagonjwa, uwajalie afya ya roho na ya mwili
W. Twakuomba utusikie
4. Uwasaidie yatima, wajane na wote walioachwa, wasikose kupata siku kwa siku mahitaji yao ya lazima
W. Twakuomba utusikie
5. Wajalie wale wote walio walegevu na wakosefu neema ya kuongoka na kurejea hima katika amani ya upendo wako
W. Twakuomba utusikie
6. Uwaimarishe wale walio wema, uwajalie neema ya kudumu wasilegee katika kutenda mema leo na kesho na siku zote za maisha yao.
W. Twakuomba utusikie
7. Utujalie nguvu za kutafuta na kudumisha amani ya kweli katika mioyo yetu na kati ya ndugu zetu katika jumuia zetu za kikristu
W. Twakuomba utusikie
Ee Bwana Mungu wetu, tunakuomba neema ya Roho Mtakatifu ituangaze akili na mioyo yetu na kutujaza nguvu ya upendo wako. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristu Bwana wetu.
W. Amina
Hekima tunayopewa na Roho Mtakatifu si sawa kama hekima inayopatikana katika ulimwengu huu.
Hekima ya Roho Mtakatifu ni ile Mtk. Paulo aliyowaambia Wakorintho ya kuwa; ni hekima ambayo watawala wa dunia hii hawakuielewa; maana kama wangaliielewa, hawangalimsulubisha Bwana wa utukufu. Lakini, ni kama yasemavyo maandiko; mambo ambayo jicho halijapata kuyaona wala sikio kuyasikia mambo ambayo binadamu hajapata kuyafikiria moyoni, hayo ndiyo Mungu aliyowatayarishia wale wampendao (1Kor 2;8-9).
Mtk. Paulo alisema kama vile roho ya mtu ndiyo yenye kufahamu na kutambua yaliyo ndani yake; hivyo pia Roho Mtakatifu ndiye anayefahamu mambo ya Mungu na kutufumbulia sisi mioyoni mwetu.
Katika Sikukuu hii ya Pentekoste tunatazamia kumpokea Roho Mtakatifu. Yeye aliye hekima ya Mungu atatufumbulia siri za Mungu na ukweli wake. Ndiye atakayeamsha ndani yetu mapendo ya Yesu Msulibiwa , Mkombozi wetu. Ni yeye atakayetuongoza kutenda mema na kuacha mabaya; tunahitaji sana Roho Mtakatifu katika maisha yetu ya kila siku, tupate hekima ya kuchagua na kutenda daima yaliyo mema. Katika novena hii tuzidi kumuomba Mungu atushushie Roho Mtakatifu, atujaze na hekima yake.
1. Ee Mungu, uwabariki viongozi wa dini na wasaidizi wao, wapate kutuongoza kwa hekima na mapendo
W. Twakuomba utusikie
2. Ewe Roho Mtakatifu, utujalie hekima ya kutambua Mambo ya Mungu na kuyatekeleza kwa uchaji
W. Twakuomba utusikie
3. Utujalie kuyajua mapenzi ya Mungu na kuyapokea kwa furaha
W. Twakuomba utusikie
4. Uamshe ndani yetu mapendo ya Yesu msulibiwa , utuwezeshe kutimiza vema wajibu wetu kama wafuasi wa kweli wa Kristu Bwana wetu
W. Twakuomba utusikie
5. Utuwezeshe kuchagua daima yaliyo mema na kuyatekeleza, tupate kulijenga na kulidumisha kanisa lako hapa duniani
W. Twakuomba utusikie
6. Utuepushe na mafundisho yoyote yaliyo na upotovu, utujalie hekima ya kuzidi kutambua ukweli wako na mafundisho yako yaletayo wokovu
W. Twakuomba utusikie
7. Hekima ya Roho Mtakatifu ituongoze katika satfari ya maisha yetu hapa duniani, tupate mwishowe kukurudi Wewe Muumba wetu uliye mwanzo wetu na mwisho wetu
W. Twakuomba utusiki
Ee Mungu, Baba wa utukufu, tunakuomba utupe Roho wako wa hekima, atuwezeshe kukufahamu vema, atuongoze kuishi maisha yenye kukupendeza. Utusaidie kupambana na matatizo ya maisha, tupate kuishi maisha mema hapa duniani na mwisho tupate tunzo la heri na furaha yako huko mbinguni. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristo Bwana wetu.
W. Amina.
Roho Mtakatifu anaangaza akili zetu tuweze kuona ukweli wa Mungu na kuufata. Bila Roho Mtakatifu akili zetu zimo katika giza nene, wala hatuwezi kuona njia ya kutuelekeza kwa Mungu.
Mungu alipoumba ulimwengu, dunia ilikuwa giza tupu, haina kitu. Mungu alisema; “Iwe nuru”, ikawa nuru, Mungu akaiona nuru, ya kuwa ni njema (Mwa 1;3-4) vivyo hivyo akili ya binadamu bila nuru ya mwanga wa Roho Mtakatifu, ni tupu, ina giza, haiwezi kuona mambo yanayotuelekeza kwa Mungu. Tukiwa na nuru ya Roho Mtakatifu tunaona ukweli wa Mungu jinsi ulivyo.
Roho Mtakatifu anapoijia roho ya mtu, anaiangaza akili yake iweze kuona mambo yanayofaa kwa wokovu. Naye akiisha kuiangaza akili ya mtu huimarisha utashi wake na kumwezesha kuchagua daima yaliyo mema.
Roho Mtakatifu huiangaza akili iweze kuona ukweli. Kabla ya kuwaaga mitume, Yesu aliwaambia kuwa atawapelekea mfariji mwingine atakayekaa nao siku zote. Roho wa kweli ambaye dunia haiwezi kumpokea kwa sababu hawakumfahamu, lakini wao mitume watamfahamu kwa maana atakaa nao siku zote. Yesu ametuahidi pia sisi Roho huyo akae nasi
Leo hivi duniani kuna uwongo na udanganyifu mwingi; kuna dhuluma, vita, na maovu ya kila namna. Hii ni kwa sababu dunia haijamtambua bado Roho Mtakatifu na kumpokea Yeye aliye mwanga wa dunia na asili ya kweli yote.
Mtaguso wa Pili wa Vatikano watambua ya kuwa Roho Mtakatifu anakaa katika kanisa na katika mioyo ya waumini kama katika hekalu. Roho Mtakatifu analiongoza kanisa na kulifanya liwe na umoja; analipamba na mapaji yake mabalimbali.
Tumuombe Mungu Baba ampeleke huyo Roho Mtakatifu katika kanisa lake, aliongoze na kulilinda lisipate kutengana, bali lisaidie kueneza utawala wa Mungu popote duniani.
1. Ewe Roho Mtakatifu, utujalie kuona mwanga wa kweli yako na kuifuata
W. Twakuomba utusikie
2. Uwape waregevu neema ya kuirudia tena njia ya kweli yako
W. Twakuomba utusikie
3. Utuwezeshe sisi sote waamini wako tutembee siku zote katika nuru ya kweli yako na sheria zako
W. Twakuomba utusikie
4. Utuangazie akili ya mioyo yetu tuchague daima yale yanayakupendeza
W. Twakuomba utusikie
5. Uwape mwanga wako viongozi wetu wa dini na serikali, wapate kutuongoza kwa hekima na uchaji, wasisahau kamwe kwamba uwezo walionao unatoka kwa Mungu.
W. Twakuomba utusikie
6. Utupe mwanga wako tuwaone watu wote kama ndugu zetu. Tuishi kindugu na kusaidiana kindugu
W. Twakuomba utusikie
7. Ewe Roho Mtakatifu ndiwe mpatanishi wa mioyo,; tunakuomba uondoe udhalimu, uonevu, udanganyifu na maovu yote katika mioyo ya watu wote.
W. Twakuomba utusikie.
Ee Yesu Bwana wetu, uliyesema “Pasipo Mimi hamuwezi kitu” umpeleke Roho Mtakatifu atuangaze akili zetu, tupate kufahamu mapenzi yako na kuyatimiza kwa imani na uchaji. Roho Mtakatifu atuongoze katika mambo yote, yeye anayeishi na kutawala nawe pamoja na Baba daima na milele.
W. Amina
Maandiko Matakatifu yanatuambia ya kuwa, Roho Mtakatifu, Nafsi ya Tatu ya Utatu Mtakatifu, ndiye Upendo katika Baba na Mwana. Upendo hujieneza. Naye Roho Mtakatifu aliye pendo lenyewe la Mungu, hupenda kujieneza na kujishirikisha nasi, na kuwasha ndani yetu moto wa mapendo yake.
Roho Mtakatifu ndiye mwenye kutakatifuza roho zetu kwa neema ya utakaso. Neema hiyo ni uzima wa Mungu, ndio huo upendo wa Mungu tunaoshirikishwa. Roho isiyo na neema ya utakaso imetengana na Mungu, haina uzima wake, haina upendo wake, kwa hiyo haiwezi pia kuwa na mapendo ya kweli ya jirani.
Ingawa tunaona ishara nyingi za watu kupendana kidugu hapa duniani, mapendo hayo si mapendo ya kweli wala si kamili kama hayatokani na neema ya utakaso rohoni mwa mtu. Kama hakuna neema ya utakaso ndani yetu, Mungu pia hayupo kati yetu.
Roho Mtakatifu anatuunganisha na Mungu katika upendo. Pasipo na mapendo hapana mapatano, hapana masikilizano wala mwungano. Watu wanaopendana wanaungana na kulingana katika fikra zao na nia zao. Roho Mtakatifu anayetutia mapendo rohoni na kutuwashia moto wa mapendo, ndiye anayetuwezesha kuwa na mawazo ya namna moja na nia moja.
Watu wanaopendana hupenda kukaa pamoja, kuishi pamoja na kusaidiana. Roho Mtakatifu aliye chanzo cha mapendo ya kweli hutuweka pamoja katika Kanisa lake. Hukaa ndani yetu, hukaa katika Kanisa na kuwasha moto wa mapendo yake ndani yetu. Roho Mtakatifu anatuwezesha kukaa kwa amani nyumbani, kazini na katika jumuiya zetu. Basi, tumwombe sasa Roho Mtakatifu atuongezee hayo mapendo yake ndani yetu.
1. Ewe Roho Mtakatifu, uwashe mioyoni mwetu moto wa mapendo yako, tupate kuwapenda jirani zetu kama tunavyotaka kupendwa nao.
W. Twakuomba utusikie
2. Udumishe ndani yetu neema hiyo ya mapendo yako, tuwezeshe kuishi kwa amani leo na siku zote za maisha yetu.
W. Twakuomba utusikie
3. Utujalie neema na nguvu za kutekeleza mema yote tunayokusudia kuyatenda siku hii ya leo
W. Twakuomba utusikie
4. Uongoze nia zetu na maazimio yetu, yalingane na juhudi zetu za kutaka kuleta mafanikio ya roho na mwili kati yetu
W. Twakuomba utusikie
5. Utubariki, ili baada ya maombi haya, tuwe na juhudi ya kutimiza vema zaidi wajibu wetu wa kikristu kwa moyo mkuu
W. Twakuomba utusikie
6. Utuwezeshe kueneza mapendo na amani kati yetu na katika jumuiya zetu za kikristu
W. Twakuomba utusikie
7. Utuwezeshe kuwa kweli chachu ya wema na mapendano kati ya watu, ili nao wapate rehema zako kwa maombezi yetu.
W. Twakuomba utusikie.
Ee Mungu, tunakushukuru kwa neema ulizotujalia, hata tukaweza kuifanya ibada hii ya Novena takatifu mpaka mwisho. Utujalie mema yote tuliyoomba; utusaidie kutekeleza yote yale tuliyokusudia kutenda. Tunaomba hayo kwa njia ya Kristu Bwana wetu.
W. Amina.
Ee Mungu Baba mwenye huruma tujalie Roho wako alete Mwanga kwetu ili apate kututakasa na kuingiza ndani ya mioyo yetu Baraka za kuweza kutenda yale yaliyo mema.
Tunaomba hayo kupitia kwa Mwanao Mpendwa Bwana wetu Yesu Kristo, anbaye anaishi na kutawala pamoja nawe katika Umoja wa Roho Mtakatifu. AMINA
Baba Yetu uliye mbinguni,
jina lako litukuzwe;
ufalme wako ufike,
utakalo lifanyike
duniani kama mbinguni.
Utupe leo mkate wetu wa kila siku,
utusamehe makosa yetu,
kama tunavyowasamehe na sisi waliotukosea.
Usitutie katika kishawishi,
lakini utuopoe maovuni.
Amina
Recent Comments