Tusali daima
Sala sio kitu cha muhimu kufanya wakati wa shida tuu. Sala ni kitu cha muhimu zaidi kila siku katika Maisha kuwe na shida au kusiwe na shida.
Sala sio kitu cha muhimu kufanya wakati wa shida tuu. Sala ni kitu cha muhimu zaidi kila siku katika Maisha kuwe na shida au kusiwe na shida.
Mungu ni mwenye Hekima, anajibu Sala zetu kwa kutupa kile tunachohitaji na chenye kutufaa na Sio kutupa kile tunachokitaka na kukitamani kwa kuwa anatupenda na kututakia mema.
Upendo hauandamani na ubinafsi. Huwezi kusema una upendo wa kweli kama huwezi kujinyima vile unavyovipenda kwa ajili ya yule au wale unaowapenda. Upendo wa kweli ni kujitoa.
Mungu anamjibu mtu sala zake kutokana na anachonuia.
Sala ni ufunguo wa kufungulia mema na kufungia Mabaya. Tusali ili tufungue mema katika maisha yetu na tufunge mabaya katika maisha yetu.
Fikiria umenunua zawadi nzuri ya gharama sana na unataka kumpa mtu umpendaye sana. Akipokea zawadi yako unafurahi sana, akikataa kuipokea zawadi inaumiza sana, lakini inaumiza zaidi akiipokea kisha akaitupa mbele yako na kuona haina maana. Hiki ndicho kinachotokea kwa Yesu. Yesu yupo kwa ajili ya kutupa zawadi ya Wokovu alyogharamia kwa uhai wake. Tunapoipokea tunamfurahisha sana, tukiikataa tunamhuzunisha na tunapoipokea na kuiacha baadae tunamhuzunisha kwelikweli.
Upendo wa Mungu hauna mwisho. Mtu anaweza akaacha kukupenda na kukusahau kabisa lakini kamwe Mungu haachi kumpenda Mtu wala hamsahau Mtu.
Njia pekee ya Kumrudia Mungu tunapoanguka dhambini ni Njia ya Toba ya kweli ikiambatana na kukiri makosa na kusamehewa. Mara nyingi tunapotubu tunasahau dhambi za mawazo na kukumbuka za matendo tuu. Dhambi ya Mawazo pia ni dhambi yapaswa toba na maondoleo.
Hakuna kitu cha Muhimu zaidi Duniani kama kumjua Mungu na kumuishi Mungu. Kila binadamu ameumbwa kwa ajili hii. Na Mungu anachotaka ndicho hichi, kumjua na kumuishi. Mengine yote ni maziada. Ukimuishi Mungu atakufanikisha katika yote.
Inashangaza kwa sasa watu wengi hawapendi kuambiwa kuhusu kutubu dhambi zao bali wanataka waambiwe watabarikiwa. Kama vile wewe huwezi kumvika mwanao nguo nzuri kabla ya kumuogesha vivyo hivyo na Mungu hawezi kukubariki kabla ya kukutakasa. Unapotubu unasamehewa na kutakaswa dhambi zako kisha unakua umefungua milango ya baraka. Huwezi kubarikiwa bila kutubu kweli.
Unapo mwomba Mungu Usisahau Kushukuru. Kushukuru ni kuomba mara ya pili. Utazidishiwa kile ulichokiomba na kupewa hata usichokiomba kwa shukrani yako.
Mungu anasubiri sala zako kila siku. Anasubiri sala zako akujibu ili uone utukufu wake. Anasubiri sala zako ili akuze mahusiano yake na wewe. Sali daima kwani Mungu yupo milele kukusikiliza na kukuhudumia.
Kwa njia ya sala Binadamu anampa Mungu Utukufu, Mungu anampa Binadamu Wokovu na Neema.
Sala ndiyo chimbuko la fadhila. Kwa njia ya sala tunapata fadhila za Kimungu na Neema za Mungu. Asaliye daima hujazwa neema na fadhila.
Hakuna Binadamu anayemchukia Mungu kama hajichukii yeye mwenyewe na wale wanaomzunguka. Huwezi kusema humtaki Mungu kama hujichukii mwenyewe na wale waliokuzunguka vivyo hivyo huwezi kusema Unampenda Mungu kama hupendi wengine waliokuzunguka.
Kukosa hata mara moja inahesabika ni kukosea mbele ya Mungu. Kwa kuwa kwa Mungu hakuna kusema, ‘Kukosea mara moja sio kosa bali kurudia kosa ndio kosa’. Mbele ya Mungu kila kosa lina uzito wake haijalishi ni kosa la mara ya kwanza.
Uwe na subira Baada ya kuomba kwa Mungu. Sio kila unachoomba kwa Mungu utakipata kwa wakati huo huo au kwa wakati unaofikiri. Mungu ni Mwaminifu Sana Kwenye kujibu maombi lakini vile vile ni mwenye Hekima Kwenye kukujibu, anajua wakati gani ni sahihi kukujibu maombi yako. Anaweza kukujibu saa hiyo hiyo, kesho, keshokutwa au hata mwakani kwa kuangalia wakati ufaao na kwa manufaa yako. Kwa hiyo unapoona hujajibiwa usife moyo, bali uwe na matumaini. Mungu anajua akujibu lini kwa kuwa anajua ni lini wakati ufaao na ni lini kitu kipi kina kufaa.
Sala pasipo Imani thabiti, ya nia ya kweli, upendo wa kweli, unyenyekevu wa ndani na tumaini la kweli katika Amani ya rohoni; Haijakamilika na haifai kitu.
Sala ni Hazina. Kusali ni muhimu sana. Sala unayosali leo inaweza kukusaidia hata miaka kumi ijayo au ikasaidia watoto wa watoto wako. Mungu ni mwenye fadhila na anakumbuka yote. Mwombe Mungu akulinde ukiwa mzima ili uwapo hatarini akukumbuke hata kabla hujamwomba.
Hakuna sala yeyote itolewayo kwa unyenyekevu wa kweli katika imani, matumaini na mapendo inayopita bure mbele ya Mungu. Mungu hamtupi mwenye unyoofu wa moyo.
Recent Comments