Dondoo za Mapishi na Lishe

Mapishi ya bagia na chatney ya machicha ya nazi

Mahitaji

Kunde (Ila mimi nilitumia Nigerian brown beans 1/2 kilo)
Vitunguu maji (onion 2)
Pilipili (scotch bonnet pepper 2)
Vitunguu swaum (garlic 4 cloves)
Chumvi (salt)
Barking powder (1/2 kijiko cha chai)
Machicha ya nazi (grated coconut 1 kikombe cha chai)
Limao (lemon 1)
Mafuta (vegetable oil)

Matayarisho

Loweka kunde usiku mzima kisha ziondoe maganda na uzitie kwenye blender pamoja na vitunguu maji, vitunguu swaum, pilipili, chumvi,barking powder na maji kiasi. Visage vitu vyote mpaka viwe laini na kisha uutoe na kuweka kwenye chujio ili uchuje maji. baada ya hapo zikaange katika mafuta mpaka ziwe za brown na uzitoe na kuziweka kwenye kitchen towel ili zichuje mafuta.Baada ya hapo saga machicha ya nazi,limao, pilipili chumvi pamoja na maji kidogo na hapo chatney yako itakuwa tayari kwa kuseviwa na bagia.

Jinsi ya kutengeneza Biskuti Za Tende

MAHITAJI

Unga – 4 Vikombe vya chai
Sukari ya laini (icing sugar) – 1 Kikombe cha chai
Baking powder – 2 Vijiko vya chai
Mayai – 2
Siagi au margarine – 1 Kikombe cha chai
Vanilla -1 Kijiko cha chai
Maziwa ya kuchanganyia – kiasi
Tende iliyotolewa koko – 1 Kikombe
ufuta (sasame) kiasi 1/4 kikombe

MAANDALIZI

Changanya unga, siagi, baking powder, na sukari katika mashine.
Kisha tia mayai, vanilla na halafu maziwa kidogo kidogo hadi mchanganyiko ushikamane.
Gawanya madonge mawili na usukume kama chapati, lakini sio nyembamba sana.
Tandaza tende robo ya duara na unyunyize ufuta duara zima: kisha kunja hadi mwisho na ukate kate, kisha upange katika trei ya kuvumbika.
Vumbika (bake) moto wa 350°F kwa muda wa dakika 20 au hadi vigeuke rangi na viwive.
Zikisha iiva ziache zipowe na zitakuwa tayari kuliwa.

Jinsi ya kuishi maisha marefu (Mambo ya kuzingatia ili uishi maisha marefu)

Kuishi ukiwa na afya na kuishi maisha marefu kunawezekana kwa kubadili hali ya maisha unayoishi inayoharibu afya yako mfano uvutaji wa sigara, unywaji wa pombe kupita kiasi,kutokufanya mazoezi na kutokula matunda na mbogamboga.

Mambo yanayoweza kukusaidia kuishi maisha marefu ni kama yafuatayo

  1. Kuuandaa mwili kwa maisha marefu kwa kufanya mazoezi
  2. Kuwa makini kutambua na kutibu matatizo ya kiafya
  3. Kuepuka mazingira na kufanya kazi kwa namna au kazi zinazoweza kudhuru maisha yako. Mfano kuendesha gari bila kufuata utaratibu, kutokuvaa vifaa vya kujikinga wakati wa kazi
  4. Epuka vitu vyenye sumu vinavyoweza kudhuru afya yako na kukuletea matatizo ya kiafya kama dawa za mimea na mifugo, zitumie kama inavyotakiwa
  5. Usinywe pombe, usivute sigara wala kutumia dawa za kulevya
  6. Kula mlo kamili
  7. Usile vyakula vyenye chumvi na mafuta mengi
  8. Kunywa maji mengi ili kusafisha mwili
  9. Epuka msongo wa mawazo

Mapishi ya Wali Wa Nazi Kwa Mchuzi Wa Samaki Na Rojo La Bilingani Na Viazi/Mbatata

Wali Wa Nazi

Mpunga – 4 vikombe

Tui la nazi – 6 vikombe

Chumvi – Kiasi

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Osha mchele kisha
Bandika tui jikoni likichemka tia mchele na chumvi.
Funika uchemke, tui likikauka wacha moto mdogomdogo hadi wali uive ukiwa tayari. Ikiwa unatumia mkaa unapalia juu yake.

Mchuzi Wa Samaki Nguru

Samaki – 4

Kitunguu saumu(thomu/galic) na tangawizi – 2 viijiko vya supu

Kitunguu maji kilokatwakawa – 2 slice ndogo

Nyanya/tungule – 4

Nyanya kopo – 3 vijiko vya supu

Pilipili mbichi – 2

Kotmiri ilokatwakatwa – 3 msongo (bunches)

Bizari ya mchuzi (simba 2) – I kijiko cha chai

Ndimu – 1 kamua

Mafuta – ¼ kikombe

Chumvi kiasi

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Katakata samaki mkaange kwa kumtia viungo.
Weka mafuta katika sufuria, kaanga kitunguu. Vinapogeuka rangi thomu na tangawizi mbichi, nyanya, nyanya kopo, kitunguu na bizari ya mchuzi endelea kukaanga.
Tia maji kiasi na ndimu, pilipili mbichi ilosagwa kisha tia kotmiri.
Mwisho tia nusu ya samaki alokaangwa ukiwa tayari

Bilingani Za Kukaanga Na Viazi

Bilingani – 4 madogodogo

Viazi/mbatata – 3

Nyanya – 3

Majani ya mchuzi/mvuje/curry leaves – kiasi 6-7

Nnyanya kopo – 2 vijiko vya supu

Methi/uwatu ulosagwa – 1 kijiko cha chia

Rai/mustard seeds – 1 kijiko cha supu

Bizari ya manjano/haldi/turmeric – 1 kijiko cha chai

Chumvi – kiasi

Mafuta ya kukaangia – kiasi

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

1. Weka mafuta ya kukaangia katika karai

2. Katakakata bilingani vipande vipande vya mraba (cubes) kaanga katika mafuta ya moto hadi yageuke rangi. Eupa weka kando.

3. Katakataka viazi/mbatata vipande vidogodogo vya mraba (cubes) Kaanga hadi viive epua weka kando.

4. Ondosha mafuta yote katika karai bakisha kidogo tu kiasi ya vijiko 2 vya supu.

5. Kaanga rai kisha majani ya mchuzi, na methi/uwatu kisha kaanga nyanya.

6. Tia nyanya ya kopo kisha changanya pamoja bilingani na viazi ikiwa tayari.

Jinsi ya kutengeneza Slesi Za Chokoleti Na Karameli

VIAMBAUPISHI

Unga – 1 Magi (vikombe vya chai)

Sukari ya browni – ½ Magi

Siagi iliyoyayushwa – 125 g

Nazi iliyokunwa – ½ Magi

MJAZO WA KARMEL (Caramel filling)

Syrup – 1/3 kikombe cha chai

Siagi iliyoyayushwa – 125 g

Maziwa matamu ya mgando – 2 vikopo (condensed milk)

MJAZO WA CHOKOLETI (Chocolate filling)

Chokoleti – 185 g (dark chocolate)

Mafuta – 3 Vijiko vya chai

MAANDALIZI

Changanya unga, sukari, siagi na nazi iliyokunwa kwenye bakuli mpaka unga ushikamane.
Paka mafuta treya ya kuchomea kisha utandaze kwenye treya ya 20cm kwa 30 cm au (8 in kwa 12 in) unaweza kuweka karatasi ya kuchomea chini ukipenda.
Choma kwenye moto 325˚C kwa muda wa dakika 15 mpaka 18 au mpaka ibadilike kuwa rangi ya browni.
Kwenye sufuria ndogo tia syrup siagi na maziwa matamu ya mgando na changanya kwa moto mdogo mpaka uwe mzito kasha mimina juu ya keki uliyochoma na choma tena kwa muda wa dakika 20 mpaka karameli iwe rangi ya dhahabu.
Kwenye sufuria ndogo nyingine tia vipande vya chokoleti na mafuta na ukoroge kwa moto mdogo mpaka iyayuke kisha wacha ipoe kidogo mimina juu ya mjazo wa karameli kisha weka kwenye friji mpaka ishikamane.
Kata vipande weka kwenye sahani tiyari kwa kuliwa

Mapishi ya Chicken Curry

Leo wapendwa nitaenda kuzungumzia mapishi ya mchuzi wa kuku (chicken curry).

Mahitaji

Kuku mzima
Nyanya kubwa 3
Karoti mbili
Pilipili hoho
Kotmiri
Tangawizi
Kitunguu maji
Kitunguu saumu kidogo
Ndimu
Mafuta ya kupikia
Chumvi (pilipili ukipenda)

Matayarisho

1. Menya vitunguu saumu na tangawizi na uvitwange pamoja.
2. Katakata kuku vipande vidogo kisha ukamulie ndimu na kupaka mchanganyiko wa tangawizi na vitunguu saumu (kiasi tu).
3. Katakata vitunguu maji na pilipili hoho uweke pembeni.
4. Grind (Kwangua) kwenye grater nyanya na karoti pia uweke pembeni.
5.Katakata kotmiri vipande vidogo uweke pembeni.
6. Andaa kikaango na jiko.

Mapishi

1. Bandika kikaango jikoni na mafuta kiasi, yakishachemka weka vitunguu maji na kaanga hadi vimelainika na kuiva (hakikisha haviungui).
2. Weka pilipili hoho na karoti na endelea kukoroga hadi vyote viive na kulainika, Kisha weka chumvi.
3. Sasa weka vipande vya nyama koroga na funikia kwa dakika 3, kisha weka nyanya zako ulizo grind na koroga ili zichanganyike vizuri, vikishachanganyika weka kotmiri na pilipili kama utapenda. Acha vichemke kwa dakika 5. Hakikisha moto sio mkali sana.
4. Angalia kama nyama zimeiva vizuri kisha epua mchuzi wako.
5. Pakua kwenye bakuli na katakata kotmiri uweke kwa juu.
Unaweza kula kwa ugali, wali, ndizi rost au chipsi.

JINSI YA KUANDAA VILEJA

MAHITAJI

Unga wa mchele – 500g

Samli – 250g

Sukari – 250g

Hiliki iliyosagwa – 1/2 kijiko cha chai

Arki (rose flavour) – 1/2 kijiko cha chai

Baking powder – 1 kijiko cha chai

Mayai – 4

Maji ya baridi – 1/2 kikombe cha chai

MAANDALIZI

Saga sukari iwe laini kiasi, changanya unga wa mchele, baking powder, hiliki na sukari.
Pasha moto samli mpaka iwe nyepesi kama maji mimina kwenye ule mchanganyiko wa unga wa mchele, kisha uchanganye pamoja na arki.
Ongeza mayai yaliopigwa endelea kuchanganya mpaka unga umeanza kuchanganyika vizuri.
Ongeza maji ya baridi sana kama nusu kikombe tu ili uchanganyike vizuri.
Kata kwa design unayotaka viwe vinene visiwe kama cookies za kawaida kama ilivyo kwenye picha na ukipenda utaweka kidoto kwa kutumia zaafarani katikati ya kileja kama inavyoonesha hapo juu.
Choma kwa moto wa baina ya 300F na 350F kwa dakika 15 mpaka 20 visiwe vyekundu toa na tayari kwa kuliwa.

Mapishi ya Tende Ya Kusonga Ya Lozi Na Cornflakes

VIAMBAUPISHI

Tende zilizotolewa kokwa – 1 Kilo

Cornflakes – 1 ½ kikombe

Lozi Zilokatwa katwa – 1 kikombe

Siagi – ¼ kilo

MANDALIZI

Mimina tende na siagi kwenye sufuria bandika motoni moto mdogo mdogo mpaka zilainike. Kwa muda wa dakika 10.
Isonge kidogo kwa mwiko au kuikoroga ichanganyike vizuri.
Changanya Cornflakes na lozi kwenye tende mpaka zichanganyika vizuri.
Pakaza treya au sinia mafuta au siagi kidogo.
Mimina mchanganyiko wa tende, zitandaze vizuri na ukate vipande saizi unayopenda. Zikiwa tayari kuliwa kwa kahawa.

Mapishi ya Wali Wa Kichina Wa Kamba Na Kuku

MAHITAJI

Mchele wa pishori (basmati) – 4

Nyama ya kuku bila mafupa – 1 Lb

Kamba saizi kubwa – 1Lb

Mchanganyiko wa mboga – njegere, karoti,

mahindi, maharage ya kijani (spring beans) – 2 vikombe

Figili mwitu (Cellery) – 2 mche

Vitunguu vya majani (spring onions) – 4-5 miche

Kebeji – 2 vikombe

Pilipili ya unga nyekundu – 1 kijiko cha chai

Pilipili manga ya unga – 1 kijiko cha chai

Sosi ya soya – 3 vijiko vya supu

Mafuta – 1/4 kikombe

Chumvi – kiasi

MAPISHI

Osha na roweka mchele.
Tia kamba chumvi na pilipili nyekundu ya unga. Tia mafuta vijiko viwili katika kikaango (frying pan), kaanga kamba kidogo tu, weka kando.
Katakata kuku vipande vidogo vidogo, tia chumvi na pilipili manga. Kaanga kaTika kikaango (ongeza mafuta kidogo) Weka kando.
Katika karai, tia mafuta kidogo kama vijiko vitatu vya supu, tia kamba na kuku, tia mboga za mchanganyiko, sosi ya soya na chumvi, kaanga kidogo. (Kama mboga sio za barafu) itabidi uchemshe kidogo.
Katakata kebeji, figili mwitu (cellery) na vitunguu vya majani (spring onions) utie katika mchaganyiko. acha kwa muda wa chini ya dakika moja katika moto.
Chemsha mchele, tia mafuta kidogo au siagi, chumvi upikie uive nusu kiini, mwaga maji uchuje.
Changanya vyote na wali rudisha katika sufuria au bakuli la oveni, funika na upike kwa moto wa kiasi kwa muda wa dakika 15-20 takriban.
Epua na upakue katika sahani ukiwa tayari kuliwa.

Mapishi ya Pilau Ya Samaki Wa Tuna Na Mboga

Mahitaji

Mchele – 2 Mugs

Mboga mchanganyiko za barafu (Frozen veg) – Mug

Tuna (samaki/jodari) – 2 kopo

Kitunguu saumu(thomu/galic) na tangawizi -2 vijiko vya supu

Garam masala – 1 kijiko cha supu

Nyanya – 2

Kitungu maji – 1

Mdalasini nzima – 2 vijiti

Karafuu – 6 chembe

Pilipili mbichi – 1

Chumvi – kiasi

Viazi – 3

Maji – 2 ½ Mugs

Mafuta – 3 vijiko vya supu

Maandalizi

Osha mchele na uroweke kwa muda wa dakika 20
Tia mafuta katika sufuria, kaanga kitunguu maji mpaka kigeuke rangi ya hudhurungi (brown).
Mimina viazi, thomu na tangawizi, bizari zote na kaanga.
Tia nyanya uliyokatakata ikaange mpaka iwive.
Tia tuna endelea kukaanga kidogo tu.
Tia maji, yatakapochemka tia mchele.
Punguza moto uwe mdogo funika kwa muda wa ½ saa hadi wali ukauke na uwive. Utakuwa tayari kuliwa.

Jinsi ya kupika Magimbi Kwa Nyama Ya Ng’ombe

Vipimo

Majimbi (Eddoes) kiasi 6 au 7

Nyama ng’ombe ½ kilos

Tangawizi ilosagwa 1 kijiko cha kulia

Haldi (bizari manjano/turmeric) ½ kijiko cha chai

Tui zito la nazi vikombe 2

Chumvi kiasi

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Safisha nyama kisha weka chumvi, bizari ya manjano, tangawizi mbichi, ukaushe kwanza katika sufuria kwa kukaanga kaanga.
Ikianza kukauka, weka maji funika uchemshe iwive.
Menya majimbi ukate kate na uweke katika sufuria nyengine.
Mimina supu na nyama katika majimbi uchemshe yawive majimbi.
Mwisho weka tui zito la nazi uchanganye vizuri kisha weka katika moto kidogo tu bila kufunika yakiwa tayari.

Mapishi ya Tambi za sukari

Mahitaji

Tambi (spaghetti 1/2 ya packet)
Mafuta (vegetable oil)
Sukari (sugar 1/2 kikombe cha chai)
Hiliki (cardamon 1/2 kijiko cha chai)
Chumvi (salt 1/2 kijiko cha chai)
Tui la nazi (coconut oil 1 kikombe cha chai)
Maji kiasi

Matayarisho

Tia mafuta kiasi kwenye sufuria kisha ibandike jikoni (katika moto wa wastani) yakisha pata moto kiasi tia tambi na uanze kuzikaanga kwa kuzigeuzageuza kila mara mpaka zitakapokuwa za yangi ya light brown. baada ya hapo ipua na umwage mafuta ya kwenye tambi (bakiza kidogo sana kwani usipofanya hivyo tambi zitakuwa na mafuta sana) Baada ya hapo zirudishe jikoni na kisha utie hiliki, chumvi, sukari, tui la nazi na maji kiasi. Zifunike kisha ziache zichemke mpaka maji yakauke. Baada ya hapo zigeuze na uzipike mpaka ziive. Nahapo zitakuwa tayari kwa kuliwa.

Mapishi mazuri ya Wali Wa Kukaanga Kwa Kidari Cha Kuku

Vipimo vya Wali:

Mchele – 3 vikombe

*Maji ya kupikia – 5 vikombe

*Kidonge cha supu – 1

Samli – 2 vijiko vya supu

Chumvi kiasi

Hiliki – 3 chembe

Bay leaf – 1

Vipimo Vya Kuku

Kidari (chicken breast) – 1Kilo

Kitunguu – 1

Tangawizi mbichi – ½ kipande

Kitunguu saumu(thomu/galic) – 7 chembe

Pilipili mbichi – 3

Ndimu – 2

Pilipilimanga – 1 kijiko cha chai

Mdalasini – ½ kijiko cha chai

Jira/Cummin ya unga – 1 kijiko cha chai

Maji – ¼ kikombe

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Wali:

Osha na roweka mchele kisha weka sufuria katika moto tia samli ipashe moto.
Tia hiliki, bay leaf, kaanga, kisha tia mchele ukaange kidogo.
Tia maji, chumvi na kidonge cha supu, upike wali kama unavyopika pilau.
*Maji kisia kwa kutegemea mchele ulivyo.
*Unaweza kutumia supu yoyote badala ya kidonge.

Kuku:

Katakata kidari cha kuku vipande vya kiasi, weka katika sufuria, tia ndimu, bizari zote, chumvi.
Katakata kitunguu vipande vidogodogo, pilipili, na kitunguu thomu (chopped), tia katika kuku.
Chuna tangawizi mbichi tia katika kuku. Changanya vitu vyote vizuri.
Tia maji kiasi ¼ kikombe tu kiasi cha kumkaushia kuku. Weka katika moto mpike huku unageuzageuza. Anapokaribia kukauka epua akiwa tayari kuliwa na wali (na saladi upendayo)

Mapishi ya Borhowa

Mahitaji

Daal (lentils) nyekundu au/na kijani – 1 Kikombe kikubwa

Bizari ya manjano ya unga – 1/2 Kijiko cha chai

Pili pili ya unga – 1/2 kijiko cha chai

Chumvi – Kiasi

Maji ya ndimu – 3 Vijiko vya supu

Kitunguu – 1 kiasi

Kitunguu saumu(thomu/galic) – 1 Kijiko cha chai

Bizari ya unga (cummin powder) – 1 Kijiko cha chai

Mafuta ya kukaangia – Kiasi

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Safisha daal kwa kutoa mawe ikiwa yapo, kisha osha na roweka dakika 15 hivi.
Kisha chemsha kwa kutia maji, bizari ya manjano, chumvi, pili pili ya unga na maji ya ndimu hadi iive na kuvurujika.
Halafu chukua kisufuria na kaanga kitungu, kisha thomu na mwisho tia bizari ya pilau.
Kisha mimina mchanganyiko wa kitunguu kwenye sufuria ya daal (iliyokwisha iiva)na uchanganye na iwache motoni kidogo itokote.
Ukipenda mimina mchanganyiko kwenye blenda na usage mpaka iwe laini.
Tia kwenye bakuli na itakuwa tayari kuliwa na wali na samaki ukipenda

Jinsi ya kupika Biriani ya Nyama Ng’ombe Na Mtindi

Mahitaji

Mchele wa biriani – 5 gilasi

Nyama ya ngombe ya mifupa – 1 ½ kilo na nusu

Vitunguu – 2 kilo

Tangawizi mbichi – ¼ kikombe

Thomu (saumu/garlic) – 3 vijiko vya supu

Mtindi – 2 vikombe

Nyanya ilokatwakatwa (chopped) – 3

Nyanya kopo – 1 kikombe

Masala ya biriani – 2 vijiko vya supu

Hiliki ya unga – 2 vijiko vya chai

Pilipili mbichi ilosagwa – 3 kiasi

Kotmiri ilokatwakatwa – 1 msongo (bunch)

Rangi ya biriani ya manjano – ½ kijiko cha chai

Zaafarani au zaafarani flavour – 1 kijiko cha supu

Mafuta ya kukaangia

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Katakata vitunguu ukaangae katika mafuta mpaka vigeuke rangi ya brown ilokoza.
Weka nyama iwe ilokatwakatwa katika treya au bakuli kubwa la oveni.
Chaganya pamoja na tangawizi, thomu, nyanya, nyanya kopo, mtindi, masala ya biriani, chumvi, pilipili.
Acha irowanike kwa muda wa masaa mawili takriban.
Funika kwa karatasi ya jalbosi (foil paper) utie katika oveni upike muda wa dakika 45 takriban mpaka nyama iwive na huku unachanganya changanya sosi. Ikiwa ina maji ongezea nyanya kopo iwe nzito.
Epua funua, kisha vuruga vitungu umwagie pamoja na kotmiri na umwagie mafuta ya moto kiasi.
Ongezea kutia masala ya biriani na hiliki ya unga.
Chemsha mchele nusu kiini, mwaga maji chuja, umwagie juu ya sosi ya nyama ukipenda kuchanganya au chemsha wali pekee.
Nyunyizia rangi ya biriani pamoja na zaafarani flavour au zaafarani yenyewe ukipenda.
Mimina mchele juu ya masala ya nyama, funika urudishe ndani ya oven upike muda wa kiasi ya dakika ishirini.
Epua upake kwa kuchota wali kwanza kisha masala uwekee juu yake, kiwa tayari.

Mapishi ya Biriani Ya Samaki Nguru, Njegere Na Snuwbar (UAE)

Mahitaji

Mchele wa basmati – 4 cups

Samaki nguru (king fish) – 7 vipande au zaidi

Kitunguu – 5

Nyanya/tungule – 3

Njegere – 1 kikombe

Snuwbar (njugu za pine) – 1 kikombe

Viazi – 2 kata kata mapande makubwa

Tangawizi mbichi – 1 kijiko cha supu

Kitunguu saumu – 1 kijiko cha supu

Pilipili nyekundu – 1 kijiko cha chai

Bizari ya biriani/garama masala – 1 kijiko cha supu

Namna Ya Kupika:

Kaanga samaki mbali kwa viungo upendavyo umkoleze vizuri. Au choma (bake/grill) katika oveni ukipenda.
Weka mafuta katika sufuria, tia vitunguu kaanga hadi vigeuka rangi. Gawa sehemu mbili.
Sehemu moja bakisha katika sufuria kisha tia tangawizi mbichi na kitunguu thomu ukaange.
Tia nyanya kaanga kisha tia bizari zote endelea kukaanga, tia njegere, njugu za snuwbar na ndimu kavu.
Tia viazi ulivyokwishakaanga, na vitunguu vilobakia.
Tia mapande ya samaki, changanya na masala bila ya kumvuruga samaki.
Chemsha wali kisha mwagia juu yake, funika upike ndani ya oveni au mkaa hadi wali uive kama unavyopika kawaida ya biriani.
Epua pakua huku ukichanganya na masala ya samaki.

Jinsi ya kutengeneza saladi

Mahitaji

Tango 1/2
Kitunguu 1/2
Cherry tomato 8
Lettice kiasi
Green olives kidogo
Black olives kidogo
Hoho jekundu 1
Carrot
Giligilani kidogo

Salad dressing
Yogurt 1/2 kikombe
Swaum 1/2 kijiko cha chai
Limao 1/2
Pilipili ya unga 1/4 kijiko cha chai
Chumvi kidogo
Olive oil kiasi

Matayarisho

Osha vitu vyote kisha vikaushe maji. Baada ya hapo ktk bakuli kubwa katakata, lettice, tango,hoho, kitunguu,giligilani na kisha ikwangue carrot na utie bila kusahau nyanya zote pamoja na olives.Baada ya hapo ichanganye vizuri, kisha tengeneza salad dressing kwa kuchanganya vitu vyote vilivyo (kwenye list ya salad dressing) kisha koroga vizuri.Baada ya hapo ichanganye na salad.Na hapo salad yako itakuwa tayari kwa kuliwa. Unaweza kuila na chochote upendacho kama vile chips, nyama choma au au chakula kikuu.

LISHE BORA KWA WATU WENYE AFYA NZURI

• Kula chakula bora kunamaanisha kula vyakula aina tofauti ya vyakula kila siku kama vile matunda, mboga, maziwa na aina ya vyakula vyenye asili ya nyama wa kufuga kama kuku, mbuzi, ngombe, samaki na na vyakula vya nafaka.

• Lishe bora linamaanisha pia kula chakula ambacho hakina mafuta mengi, sukari au chumvi nyingi

• Zingatia angalau vyakula vya nafaka kama vile mtama, mahindi, mchele, ngano, wimbi, ndegu, njegere. n.k

• Ni bora kula matunda mengi kama ‘maembe, ndizimbivu, papai, pera, chungwa, ubuyu, nanasi, pesheni, zambarau” na mbogamboga kama vile “mchicha, majani ya mboga, karoti, nyanya chungu, nyanya, mkunde, biringanya” mara tano kwa siku.

• Kama mboga na matunda hazipatikani ni bora kununua zile ambazo zimehifadhiwa tayari kwenye mikebe au zile ziko kwenye jokofu (friji).

• Punguza kula vyakula ambavyo vinapikwa kwa mafuta mengi na chumvi nyingi

• Lishe bora hukusaidia wewe na jamii yako kuishi vyema, kuwa na afya bora, kufanya kazi vizuri na kwa bidii, shuleni na hata kucheza.

Jinsi ya Kupika skonzi

Mahitaji

Unga wa ngano (self risen flour 2 vikombe vya chai)
Sukari (sugar 1/2 kijiko cha chakula)
Chumvi (salt 1/2 kijiko cha chai)
Hamira (yeast 1/2 kijiko cha chakula)
Baking powder 1/2 kijiko cha chai
Siagi (butter 1/4 ya kikombe cha chai)
Maziwa (fresh milk 3/4 ya kikombe cha chai)(unaweza kutumia maji badala ya maziwa)

Matayarisho

Pasha maziwa yawe ya uvuguvugu kisha weka pembeni, pia yeyusha siagi na uweke pembeni.Baada ya hapo tia kila kitu kwenye bakuli la kukandia kasoro maziwa, na uchanganye vizuri kisha tia maziwa kidogo kidogo katika mchanganyiko huo kisha ukande. Ukimaliza uweke kwenye sehemu ya joto na uache uumuke. Ukisha umuka utawanyishe katika madonge saba Kisha .pakaza mafuta au siagi katika chombo cha kuokea kisha yapange hayo madonge katika hicho chombo na uyaache yaumuke tena (kwa mara ya pili). Baada ya hapo pakaza mafuta juu ya hayo madonge na uyaoke (bake) katika oven (moto 200°C ) kwa muda wa dakika 25 na hapo scones au maskonzi yatakuwa tayari

Namna ya kupika Vitumbua

Vitumbua ni aina ya vitafunwa vya chai ambavyo hutengenezwa kwa kutumia unga wa mchele. Kiasili vitumbua ni chakula ambacho hupendelewa sana na watu wa pwani. Na mara nyingi wamekuwa wakipika kwa kuchanganya na nazi ili kuvifanya view na ladha nzuri zaidi

Mahitaji:

Unga wa mchele ½ kg
Sukari vijiko 4 vya mezani
Tui bubu la nazi
Mafuta ya kupikia
Unga wa hiliki ½ kijiko cha chai
Hamira kijiko 1 cha chai
Chuma cha vitumbua

Maandalizi:

Chukua unga wa mchele na weka kwenye bakuli au sufuria ya kilo moja
Weka hamira kisha weka sukari kisha miminia tui katika mchanganyiko wako
Weka hiliki koroga hadi view uji mzito
Acha uji huo kwa muda wa saa moja hadi uumuke, mara nyingi kuumuka kunategemea na hali ya hewa,
Baada ya hapo weka mafuta kijiko kimoja cha chakula kila kishimo acha yapate moto Kisha kaanga virumbua vyako

Shopping Cart
20
    20
    Your Cart
    Kitabu cha SMS Maalumu kwa Umpendaye
    Kitabu cha SMS Maalumu kwa Umpendaye
    1 X Sh2,500 = Sh2,500
    🏠 Home 📖 Reading 🖼️ Gallery 💬 AI Chat 📘 About