Mafundisho ya Msingi ya Kanisa Katoliki: Makala za Katoliki

MITAGUSO MIKUU YA KANISA KATOLIKI

MITAGUSO MIKUU

Yesu Kristo aliwakabidhi mitume kumi na wawili uongozi wa Kanisa wakiwa kundi moja lenye mkuu wake, yaani Petro. Vilevile waandamizi wao, yaani maaskofu wote, ni kundi moja na Papa wa Roma ndiye mkuu wao. Huyo peke yake, na kundi la maaskofu likiwa pamoja naye na chini yake, ndio wenye mamlaka ya juu katika Kanisa lote. Mamlaka hiyo inatumika kwa namna ya pekee unapofanyika mtaguso mkuu, yaani mkutano maalumu wa maaskofu uliokubaliwa na Papa kuwa unawakilisha kundi hilo lote. Hakuna uamuzi wa kudumu kuhusu ipi ni mikuu kati ya mitaguso yote iliyofanyika katika historia ya Kanisa. Tangu karne XVI Wakatoliki wataalamu wa sheria za Kanisa wanatoa orodha yao, ambayo kwa sasa ni kama ifuatavyo.

ORODHA YA MITAGUSO MIKUU

• Katika milenia ya kwanza ilifanyika mashariki (Uturuki wa leo):
1. Nisea I (mwaka 325)
2. Kostantinopoli I (381)
3. Efeso (431)
4. Kalsedonia (451)
5. Kostantinopoli II (553)
6. Kostantinopoli III (680-681)
7. Nisea II (787)
8. Kostantinopoli IV (869-870)
• Katika milenia ya pili ilifanyika magharibi (Italia, Ufaransa, Ujerumani, Uswisi na Vatikano ya leo):
9. Laterano I (1123)
10. Laterano II (1139)
11. Laterano III (1179)
12. Laterano IV (1215)
13. Lyon I (1245)
14. Lyon II (1274)
15. Vienne (1311-1312)
16. Konstanz (1414-1418)
17. Firenze (1431-1445)
18. Laterano V (1512-1517)
19. Trento (1545-1563)
20. Vatikano I (1869-1870)
21. Vatikano II (1962-1965)

HISTORIA YA MITAGUSO MIKUU

Mitaguso mikuu ya kwanza ilifanyika hasa ili kubainisha katika mafundisho yaliyogongana yapi yanalingana na imani sahihi. Mwisho wake ulikuwa kutangaza dogma fulani na kutenga na Kanisa watakaokataa kuiamini na watakaofundisha tofauti.
Mitaguso iliyofanyika baada ya farakano la mwaka 1054 kati ya Kanisa la mashariki na la magharibi, pamoja na kulenga umoja uliovunjika na kufundisha dogma mpya, ilishughulikia zaidi urekebisho wa Kanisa katika ngazi na nyanja zote. Kwa namna ya pekee Mtaguso II wa Vatikano tangu uitishwe ulijulikana kuwa wa kichungaji, yaani usio na lengo la kufundisha dogma mpya wala kulaani mafundisho mengine.

Mtaguso I wa Nisea (325)

Mtaguso I wa Nisea ndio mtaguso wa kwanza kuitwa (tangu mwaka 338) mtaguso wa kiekumeni, yaani mtaguso wa dunia yote au mtaguso mkuu. Ndiyo sababu inashika nafasi ya pekee kati ya mitaguso yote.
Uliitishwa na kusimamiwa na kaisari Konstantino Mkuu, aliyehofia mabishano kati ya raia wake Wakristo kuhusu Yesu Kristo, ambayo yalihatarisha umoja na usalama wa Dola la Roma lililoanza kuelekea kusambaratika. Yeye aliwaalika maaskofu wote wa dola, waliokuwa kama 1000 mashariki na kama 800 magharibi. Washiriki walitokea hata nje ya dola hilo, kama vile Persia na Armenia. 2
Katika hali hiyo mtaguso ulianza tarehe 20 Mei 325; washiriki walikuwa kama 318, wengi wao wakitokea upande wa mashariki wa dola hilo. Upande wa magharibi uliwakilishwa na watu 4 kutoka Ulaya na 1 kutoka Afrika. Papa Silvesta I (314-335) aliwakilishwa na mapadri wawili.
Asili ya mabishano ilitokea katika Kanisa la Aleksandria (Misri), ambapo kasisi Arios alikuwa amekanusha umungu wa Yesu, na hivyo alihukumiwa na Sinodi ya Aleksandria ya mwaka 321, iliyoitishwa na askofu Aleksanda wa Aleksandria. Hata hivyo Arios hakuacha mafundisho yake, akakimbilia Palestina kwa rafiki yake Eusebio wa Nikomedia.
Basi, mtaguso ulikiri karibu kwa kauli moja kwamba Yesu Kristo ni Mwana wa Mungu kwa maana ana ousìa (yaani dhati) ileile ya Kimungu aliyonayo Baba. Ndiyo kiini cha Kanuni ya imani ya Nisea iliyopitishwa na mtaguso.
Uamuzi mwingine wa mtaguso ulikuwa kupanga siku ya Pasaka, sherehe kuu ya Kanisa, iwe Jumapili inayofuata mbalamwezi ya kwanza ya majira ya Springi, tofauti na kalenda ya Kiyahudi. Pia zilitungwa kanuni 20 kuratibu mambo mbalimbali.
Mtaguso ulipomalizika tarehe 25 Julai 325, Konstantino alifikiri uamuzi juu ya dogma utamaliza mabishano, lakini haikuwa hivyo, kwa sababu Wagiriki wengi, ingawa hawakukubaliana na Arios, hawakuridhika na msamiati uliotumika kuelezea uhusiano wa Baba na Mwana.

Mtaguso I wa Konstantinopoli (381)

Mtaguso I wa Konstantinopoli ndio wa pili kati ya mitaguso ya kiekumene yaliyofanyika wakati wa mababu wa Kanisa. Uliitishwa na kaisari Theodosius I ukafanyika Konstantinopoli mwaka 381.
Maaskofu 150 waliohudhuria walilaani aina mbalimbali za uzushi, hasa ule wa Masedoni wa Konstantinopoli aliyekanusha umungu wa Roho Mtakatifu, wakathibitisha maamuzi ya mtaguso mkuu wa kwanza (Mtaguso I wa Nisea), uliofanyika mwaka 325.
Hivyo walikiri kwamba Roho Mtakatifu pia, kama vile Yesu Mwana wa Mungu, anachanga dhati ileile ya Baba.
Pamoja na hayo, walikamilisha kanuni ya imani ya Nisea ambayo kwa sababu hiyo inaitwa sasa kanuni ya imani ya Nisea-Konstantinopoli na ambayo inatumika sana hata leo katika madhehebu mbalimbali ya Ukristo, hasa katika liturujia.

Mtaguso wa Efeso (431)

Mtaguso wa Efeso unahesabiwa na Wakristo walio wengi kama mtaguso mkuu wa tatu. Ulifanyika Efeso katika mkoa wa Asia Ndogo, kwa amri ya kaisari Theodosi II; Papa Selestini I (422-432) alimteua Sirili wa Aleksandria kuuendesha; washiriki walikuwa zaidi ya 150 na kujadili vikali hasa uzushi wa Nestori wa Konstantinopoli.
Patriarki huyo alikuwa anasisitiza ubinadamu wa Yesu Kristo kuliko umungu wake, akisema Bikira Maria alimzaa mtu Yesu, si Mungu, wala si Neno wa Mungu aliyehifadhiwa ndani ya nafsi ya Kristo kama hekaluni. Kwa hiyo Kristo alikuwa Theophoros, yaani “mbeba Mungu”, na Maria Christotokos, “Mama wa Kristo” si Theotokos, “Mama wa Mungu”.
Mtaguso huo ulilaani haraka mafundisho hayo ukikiri kwamba nafsi ya Yesu Kristo ni moja tu, ile ya milele ya Mwana wa Mungu, na kwamba nafsi hiyo ilitwaa ubinadamu kamili wenye mwili na roho. Hivyo Maria ni Theotokos kwa kuwa alimzaa Mungu kama binadamu.
Wajumbe wa Papa walipofika walithibitisha uamuzi huo, lakini maaskofu kutoka Antiokia hawakuridhika, na uzushi huo uliendelea Mesopotamia na kuenea hata Asia mashariki.
Mtaguso ulitangaza kuwa Kanuni ya Imani ya Nisea-Konstantinopoli ni kamili ukakataza isibadilishwe kwa namna yoyote. Pia ulilaani Upelaji, uzushi kutoka Ulaya magharibi kuhusu uwezo wa binadamu kutenda mema bila kusaidiwa na neema ya Mungu.

Mtaguso wa Kalsedonia (451)

Mtaguso wa Kalsedonia (leo katika nchi ya Uturuki) unahesabiwa na Wakristo wengi kuwa wa nne kati ya mitaguso ya kiekumeni iliyofanyika katika historia ya Kanisa.
Mtaguso huo uliitishwa na kaisari Marcianus wa Dola la Roma Mashariki pamoja na mke wake Pulkeria wa Bizanti miaka 20 baada ya Mtaguso wa Efeso.
Hao waliona haja ya kudumisha umoja wa Wakristo, uliokuwa msingi wa uimara wa dola hilo, hasa wakati huo ambapo makabila yasiyo na ustaarabu kutoka Asia yalikuwa yanajaribu kuteka Ulaya.
Umoja huo uliingia hatari ya kuvunjika kutokana na uamuzi wa mtaguso mkuu wa Efeso kuhusu imani sahihi juu ya Yesu Kristo kutoeleweka kwa namna moja.
Hasa baadhi ya walioshinda mtaguso huo walionekana kusisitiza mno umungu wake hata kutia shaka kama wanaamini sawasawa ubinadamu wake.
Vikao vilianza tarehe 8 Oktoba 451 vikiwa na washiriki zaidi ya 350: mara nyingi inatajwa idadi ya 600 hivi. Hatimaye mafundisho ya Eutike na Dioskoro wa Aleksandria yalilaaniwa.
Ufanisi wa mtaguso ulichangiwa na msimamo wa kaisari Valentiniano III wa Dola la Roma Magharibi, binamu wa Pulkeria. Kaisari huyo alimuunga mkono Papa Leo I (440-461) aliyekuwa ametoa msimamo wake na wa Kanisa la Roma tangu mwaka 449 katika Tomus ad Flavianum, yaani Waraka kwa Flaviano, Patriarki wa Konstantinopoli aliyeuawa na wafuasi wa Eutike. 3
Ingawa msimamo huo wa kati ulikubaliwa na wengi, wengine waliuona ni kinyume cha uamuzi wa Efeso, hivyo walishikilia sana mtazamo hao hata walipodhulumiwa na serikali. Ndiyo asili ya farakano la Misri, Syria, Armenia n.k. linalodumu hata leo.
Mtaguso huo ulitunga pia kanuni mbalimbali, kama vile kwa kumpatia Patriarki wa Konstantinopoli nafasi ya pili kati ya maaskofu wote.

Mtaguso II wa Konstantinopoli (553)

Mtaguso II wa Konstantinopoli uliitishwa na kaisari Justiniani I mwaka 553 kwa lengo la kupatanisha tena na Kanisa Katoliki Wakristo wote wa Misri, Syria n.k. waliojitenga miaka 100 iliyopita kufuatana na Mtaguso wa Kalsedonia.
Kwa ajili hiyo kaisari huyo alifanya yalaaniwe maandishi ya Wanestori watatu (Teodoro wa Mopsuestia, Teodoreto wa Kiro na Iba wa Edesa) yaliyochukiwa sana na Wamisri.
Pia mtaguso mkuu huo ulilaani baadhi ya mafundisho wa Origene.
Walihudhuria maaskofu 168; kati yao 11 walitokea magharibi. Kumbe Papa Vigili (537-555) na maaskofu wengine 12 wa magharibi walikataa kuhudhuria ingawa walikuwepo Konstantinopoli, ila mwaka uliofuata alikubali maamuzi ya mtaguso.
Hatimaye Papa Gregori I (590-604) aliutambua kama mtaguso mkuu kwa sababu haukuharibu kitu. Hivyo Wakristo wengi wanauhesabu kuwa wa tano kati ya mitaguso ya kiekumeni, ingawa lengo halikufikiwa, kwa kuwa Wamisri waliendelea kukataa Mtaguso wa Kalsedonia.

Mtaguso III wa Konstantinopoli (680-681)

Mtaguso III wa Konstantinopoli unahesabiwa na Wakristo wengi kuwa wa sita kati ya Mitaguso ya kiekumeni.
Kaisari Konstantino IV wa Konstantinopoli ndiye aliyeuitisha na kuuendesha kuanzia tarehe 7 Novemba 680 hadi tarehe 16 Septemba 681.
Suala kuu lililosumbua Wakristo wa karne VII lilimhusu Yesu Kristo upande wa utashi. Ulikuwa unaenea mtazamo wa kwamba hakuwa na utashi wa kibinadamu, bali ule wa Kimungu tu.
Lakini wamonaki Sofronio wa Yerusalemu na Maksimo Muungamadini walipinga vikali jaribio hilo la kuleta upatanisho wa Waorthodoksi wa Mashariki (Wamisri n.k.) kwa kumpunguza Yesu katika ubinadamu wake kamili uliosisitizwa na Mtaguso wa Kalsedonia (451).
Vilevile Papa Martin I (649-655), katika mtaguso uliofanyika Laterani, alilaani mtazamo huo, kinyume cha Kaisari na Patriarki wa Konstantinopoli.
Konstantino IV alikubaliana na Papa Agatoni (678-681), na hivyo Mtaguso III wa Konstantinopoli ulilaani rasmi mtazamo wa kwamba Yesu hakuwa na utashi wa kibinadamu.

Mtaguso II wa Nisea (787)

Mtaguso II wa Nisea uliitishwa na malkia Irene wa Bizanti mwaka 787 ili kujadili matumizi ya sanamu katika Ukristo, kutokana na ombi la Papa Adrian I (772-795).
Wakristo wengi wanauhesabu kuwa wa saba kati ya Mitaguso ya kiekumeni. Ni wa mwisho kufanyika wakati wa mababu wa Kanisa.
Mtaguso mkuu huo ulihitajika ili kumaliza mabishano makali kuhusu sanamu za Kikristo yaliyochukua zaidi ya miaka 100 hasa katika Dola la Roma Mashariki yakimalizika mwaka 843 tu.
Chanzo ni uamuzi wa kaisari Leo III wa Konstantinopoli (717-741) wa kuteketeza sanamu zote ili kujilinganisha na Waislamu waliotishia utawala wake.
Patriarki wa Konstantinopoli alilazimika kujiuzulu, lakini uamuzi wa kaisari ulizidi kupingwa hasa na wamonaki na mwanateolojia Yohane wa Damasko. Mapapa wa Roma pia walipinga uamuzi huo.
Sera ya dola ilibadilika aliposhika uongozi Irene kwa niaba ya mtoto wake mdogo Konstantino VI.
Mtaguso ulianza Konstantinopoli mwaka 786, lakini ulipoingiliwa na jeshi waliowaunga mkono maaskofu wengi waliopinga sanamu, Irene aliuhamishia Nisea ambapo vilifanyika vikao 7 kuanzia tarehe 28 Septemba 787. Cha mwisho kilifanyika katika ikulu tarehe 23 Oktoba 787.
Pamoja na maaskofu 300 hivi wa dola hilo, walihudhuria wamonaki wengi. Papa alituma mabalozi wake wawili na barua moja.
Mtaguso ulitofautisha heshima inayokubalika kwa sanamu na ibada isiyovumilika. Hoja kuu ni kwamba sanamu si kitu, ila inamwakilisha yule aliyechorwa ndani yake. Kimsingi sanamu zinakubalika kutokana na umwilisho wa Mwana wa Mungu uliomfanya atwae sura na kuonekana.
Mtaguso ulichukua pia maamuzi mbalimbali ili kurekebisha Kanisa.

Mtaguso IV wa Konstantinopoli (869-870)

Mtaguso IV wa Konstantinopoli ni jina linalotumiwa na Wakristo kwa namna tofauti, kadiri wanavyokubali au kukataa uhalali na uekumeni wa mitaguso fulanifulani.
Kanisa Katoliki linahesabu kuwa Mtaguso Mkuu IV wa Konstantinopoli ule uliofanyika tangu tarehe 5 Oktoba 869 hadi 28 Februari 870.
Uliitishwa na Kaisari Basili I wa Konstantinopoli na Papa Adrian II (867-872), kwa sababu mwisho wa ikonoklastia katika sinodi ya mwaka 843 ulikuwa umeacha athari kubwa katika Kanisa la Mashariki. 4
Patriarki Metodi wa Konstantinopoli (843-847) alijitahidi kutuliza pande zote, lakini hakufaulu.
Alipofariki, malkia Teodora, akitawala kwa niaba ya mtoto Mikaeli III, alilazimisha nafasi yake ishikwe na Ignas I, mmonaki mwenye msimamo mkali, ambaye hatimaye aliondoshwa.
Badala yake alichaguliwa mlei msomi Fosyo ambaye kwa siku chache alipewa daraja na kutawazwa, lakini kufikia Februari 859 lililotea farakano kati ya waliomkubali yeye na waliomkubali Ignas I.
Ndipo Fosyo alipojitahidi kuungwa mkono na Papa Nikolaus I (858-867), ambaye kwanza alimkubali pamoja na pendekezo la Kaisari Mikaeli III la kuitisha mtaguso uliofanyika Konstantinopoli kati ya Aprili na Agosti 861 wakihudhuria maaskofu zaidi ya 300.
Papa hakupendezwa na maamuzi ya mtaguso huo, akashindana na Kaisari kimaandishi kwa sababu za kiutamaduni na za kisiasa pia.
Hapo Fosyo alipata nguvu dhidi ya Papa akaitisha mtaguso uliovunja umoja kati ya Makanisa ya Mashariki na yale ya Magharibi mwaka 867, akithubutu kwa mara ya kwanza kumhukumu Papa kama mzushi na kutaka kumuondoa madarakani.
Kumbe Kaisari mpya alimrudisha Ignas I kuwa Patriarki na pamoja naye akamuomba Papa atume mabalozi kwa mtaguso mwingine wa kufanyika Konstantinopoli.
Mtaguso ulipoanza tarehe 5 Oktoba 869 walikuwepo tu maaskofu wakuu 5 na maaskofu wengine 7, lakini walikuwepo mabalozi wa Mapatriarki wa Antiokia na Yerusalemu (wale wa Aleksandria walifika baadaye).
Waliokuwa upande wa Fosyo walikubaliwa kuhudhuria kuanzia tarehe 7 Oktoba wakamtetea sana dhidi ya msimamo wa Papa, lakini wakashindwa na kutengwa (29 Oktoba).
Baada ya miezi mitatu mtaguso uliendelea tarehe 12 Februari 870, wakiwepo maaskofu 67 walioongezeka tena hadi kufikia 103 siku ya mwisho (28 Februari), lilipotolewa tamko la imani pamoja na kanuni 26 kuhusu teolojia na sheria, bila kutoa mafundisho mapya. Pamoja na idadi yenyewe kutokuwa kubwa sana, ni muhimu kwamba walikuwepo maaskofu wakuu 37 kati ya 40.
Kwa kuwa mtaguso huu haukukubaliwa sana huko Konstantinopoli (hasa baada ya Fosyo kurudia Upatriarki mwaka 877), na pande mbili zilishindwa zaidi na zaidi kuelewana, uliitishwa mtaguso mwingine, ambapo wafuasi wa Fosyo walikuwa ndio wengi.
Baadhi ya Waorthodoksi wanahesabu mtaguso huo mpya (879-880), uliofuta maamuzi dhidi ya Fosyo, kuwa wa kiekumeni na kuukataa ule wa miaka 10 ya nyuma. Lakini wengine hawakubali kuwa wa kiekumeni kwa sababu haukutoa mafundisho ya imani.
Ingawa wajumbe wa Papa Yohane VIII (872-882) walikubali kwanza maamuzi wa mtaguso huo ili kudumisha amani, na labda hata yeye mwenyewe, waandamizi wake waliukataa, na Fosyo mwenyewe aliondoshwa tena mwaka 886.

Mtaguso I wa Laterano (1123)

Mtaguso I wa Laterano unahesabiwa na Kanisa Katoliki mtaguso mkuu wa tisa katika historia yake, wa kwanza kufanyika Magharibi. Ulianza tarehe 18 Machi ukamalizika tarehe 11 Aprili 1123.
Mahali pake ni kwenye Kanisa Kuu la Roma (Italia) katika mtaa wa Laterano, alipokuwa anaishi askofu wake. Hukohuko baadaye ilifanyika mitaguso mingine minne ya Karne za Kati, halafu umuhimu wake ukapungua Papa alipohamia Vatikano.
Mtaguso uliitishwa na Papa Kalisti II (1119-1124) mnamo Desemba 1122, mara baada ya Mapatano ya Worms, ya kwanza kufanyika kati ya Papa na Dola Takatifu la Kirumi, iliyofurahisha sana wanakanisa, hata mwaka huo ulitajwa kuwa mwanzo wa kipindi kipya.
Mapatano hayo yalikomesha desturi ya walei kuteua viongozi wa Kanisa na wa utawa, yakitenganisha shughuli za kiserikali na zile za kidini, na kukubali kwamba mamlaka ya kiroho inatokana na daraja takatifu.
Ili kuthibitisha mapatano hayo, Papa alialika Roma maaskofu wote wa Magharibi. Waliohudhuria kweli walikuwa zaidi ya 900 kati ya maaskofu zaidi ya 300 na maabati 600 hivi). Papa mwenyewe aliendesha vikao.
Hakuna hati za mtaguso, ila matunda yake. Tunachojua ni kwamba Mapatano hayo yalisomwa yakapitishwa rasmi, pamoja na kanuni 22 au 25, ambazo nyingi zilikuwa zimeshapitishwa zamani.

Mtaguso II wa Laterano (1139)

Mtaguso II wa Laterano, uliofanyika kuanzia tarehe 4 hadi 11 Aprili 1139 chini ya Papa Inosenti II (1130-1143), unahesabiwa na Kanisa Katoliki kuwa mtaguso mkuu wa kumi. Ni wa pili kufanyika Magharibi, kwenye Kanisa kuu la Roma (Italia).
Mtaguso ulihitajika kutokana na farakano lililotokea mwaka 1130 alipofariki Papa Honori II (1124-1130): hapo makardinali waligawanyika kuhusu Mapatano ya Worms, ambayo mwaka 1122 yalikuwa yamekomesha mashindano kuhusu uteuzi wa maaskofu.
Isitoshe, kulikuwa na ushindani kati ya koo mbili za Roma, yaani Frangipane na Pierleoni.
Tarehe 14 Februari 1130, makardinali 16 waliosimama upande wa familia ya Frangipane walimchagua Gregorio Papareschi, aliyejiita Papa Inosenti II. Saa chache baadaye, Pietro Pierleoni alichaguliwa na makardinali wengine na kujiita Anakleti II.
Hatimaye, kwa msaada wa Bernardo wa Clairvaux, Inosenti II alishinda na kukubaliwa na wengi, ingawa hakuweza kuhamia Roma mpaka baada ya mpinzani wake kufa (1138). 5
Mtaguso ulipaswa kurekebisha matokeo ya farakano hilo. Basi, Inosenti II alifungua kikao na kuondoa madarakani maaskofu waliomfuata mpinzani wake.
Halafu papa alikusudia kuendeleza juhudi za urekebisho za Mtaguso I wa Laterano. Hivyo zikapitishwa kanuni 30, ambazo nyingi kati yake zilikuwa za kurudia zile za zamani kuhusu usimoni, mapadri wenye wake n.k.

Mtaguso III wa Laterano (1179)

Mtaguso III wa Laterano uliitishwa na Papa Aleksanda III (1159-1181) ufanyike huko Roma mwaka 1179, kutokana na Amani ya Venezia kati ya Kaisari Federiko I wa Ujerumani na Lega Lombarda ya Italia kaskazini.
Unahesabiwa na Kanisa Katoliki kama mtaguso mkuu wa kumi na moja. Ulijadili masuala mbalimbali na kuyatungia kanuni. Kati ya maamuzi muhimu zaidi, mmojawapo ulihusu uchaguzi wa Papa, ukidai thuluthi mbili za kura za makardinali wote, bila kutofautisha haki za makundi yao matatu.

Mtaguso IV wa Laterano (1215)

Mtaguso IV wa Laterano unahesabiwa na Kanisa Katoliki kama mtaguso mkuu wa kumi na mbili.
Uliitishwa na Papa Inosenti III (1198-1216) kama kilele cha kazi yake.
Ulihudhuriwa na maaskofu zaidi ya 400 (wakiwemo mapatriarki wa Kilatini wa Konstantinopoli na Yerusalemu na wawakilishi wa wale wa Antiokia na Aleksandria), na wakuu wa watawa zaidi ya 800, mbali na mabalozi wa watawala wa nchi mbalimbali.
Mada kuu zilikuwa Vita vya msalaba, Mashindano kuhusu uteuzi wa viongozi wa Kanisa, mamlaka ya Papa, mwenendo wa makleri, mashirika ya kitawa, imani (kuhusu ekaristi n.k.) na wajibu wa Wakristo wote kupokea sakramenti ya kitubio walau mara moja kwa mwaka.
Kutokana na wingi na umuhimu wa mafundisho na maamuzi yaliyotolewa, mtaguso huo unahesabiwa kuwa kati ya ile iliyoathiri zaidi Kanisa hadi leo.

Mtaguso I wa Lyon (1245)

Mtaguso I wa Lyon uliitishwa na Papa Inosenti IV (1243-1254) tarehe 24 Juni 1245 akiwa huko Lyon (Ufaransa), alipokimbilia usalama. Waliushiriki karibu viongozi 150 wa Kanisa Katoliki, ambalo linauhesabu kuwa mtaguso mkuu wa kumi na tatu.
Baada ya mashindano makali kati ya mamlaka ya kiroho ya Papa na ile ya kisiasa ya kaisari huko Ulaya, mtaguso huo uliitishwa ili kumhukumu moja kwa moja kaisari Federiko II kuwa Mpinga Kristo.
Mtaguso ulianza tarehe 28 Juni 1245 wakiwepo maaskofu 144, halafu ukawa na vikao viwili vingine tena tarehe 5 Julai na 17 Julai. Hatimaye maaskofu walikuwa 225.
Mwanzoni papa alitangaza matatizo 5 yanayotesa Kanisa:
• kuharibika kwa imani na maadili;
• kushindwa kuikomboa Nchi takatifu (Yerusalemu ulitekwa tena na Waturuki mwaka 1244);
• kudumu kwa farakano la Waorthodoksi;
• kujitokeza hatari ya kuvamiwa na Watartari;
• kupambana na Federiko II.
Maamuzi yalitangazwa tarehe 25 Agosti tu, baada ya papa na wasaidizi wake kurekebisha miswada, yakapokewa na kufafanuliwa na vyuo vikuu. Lakini uamuzi wa kumuondoa madarakani kaisari haukuweza kutekelezwa hata kwa vita.

Mtaguso II wa Lyon (1274)

Mtaguso II wa Lyon unahesabiwa na Kanisa Katoliki kama mtaguso mkuu wa kumi na nne. Ulikusudiwa hasa kurudisha umoja kamili kati ya Wakatoliki na Waorthodoksi, uliotafutwa katika karne XIII yote.
Mnamo Februari 1274, katika ikulu ya Konstantinopoli, kaisari Mikaeli VIII ilifaulu kufanya maaskofu wengi wakiri ungamo la imani lililodaiwa na Papa Klementi IV (1265-1268).
Ndipo Papa Gregori X (1271-1276) alipoitisha mtaguso huko Lyon, ambao uhudhuriwe na wawakilishi wa Waorthodoksi ili kukamilisha umoja.
Papa Gregori X alifungua mtaguso tarehe 7 Mei 1274 akitangaza tena malengo yake matatu:
• kusaidia Wakristo wa Nchi takatifu,
• kuungana tena na Waorthodoksi,
• kurekebisha maadili ndani ya Kanisa.
Vilifuata vikao viwili tarehe 18 Mei na 4 Juni. Halafu tarehe 24 Juni ulifika na kupokewa kwa shangwe ujumbe kutoka Ugiriki, ukiundwa na maaskofu 2 na katibu wa kaisari.
Tarehe 6 Julai kilifanyika kikao cha nne kwa ajili ya muungano na hatimaye tarehe 16 Julai kile cha mwisho kilichopitisha hati mbalimbali za urekebisho. Kesho yake mtaguso ulifungwa.
Muungano haukuweza kudumu, kwa sababu, alivyoandika Papa Paulo VI (1963-1978) tarehe 19 Oktoba 1974, ulifanyika «bila kulipatia Kanisa la Kigiriki nafasi ya kutokeza kwa hiari mtazamo wake kuhusu jambo hilo. Wakristo wa Kilatini ndio waliotunga hati na matamko kufuatana na mafundisho juu ya Kanisa yaliyofafanuliwa na kupangwa magharibi». 6
Mikaeli VIII alijaribu kulazimisha raia zake wapokee mambo wasiyoyakubali kwa moyo, hata akatumia nguvu kuwadhulumu waliokataa; akilaumiwa na watu wa Roma kwa kushindwa kufanikisha muungano, akaja kutengwa na Kanisa. Alipokufa (1282), mwanae Androniko II aliyemrithi, alifuta maamuzi ya baba yake kwa ajili ya muungano.
Vilevile mipango kwa ajili ya vita vya msalaba haikutekelezwa, na hatimaye (1291) Waturuki waliteka Akri, mji wa mwisho kubaki mikononi mwa Wakristo huko Mashariki ya Kati.
Maamuzi mengine yalihusu utaratibu mpya wa kumchagua Papa kwa lengo la kuzuia uchelewaji uliojitokeza hapo nyuma, na katazo la mashirika mapya ya kitawa.

Mtaguso wa Vienne (1311-1312)

Mtaguso wa Vienne unahesabiwa na Kanisa Katoliki kama mtaguso mkuu wa kumi na tano.
Mtaguso huu ulifanyika Vienne (Ufaransa) baada ya mashindano kati ya Papa Bonifas VIII (1294-1303) na mfalme wa Ufaransa Filipo IV.
Hatimaye mwaka 1309 mwandamizi wake, Papa Klementi V (1305-1314) alikubali kubaki Avignon (leo nchini Ufaransa), karibu na himaya ya mfalme huyo.
Mapapa walibaki huko hadi mwaka 1377, waliporudi Roma.
Kwa shinikizo la mfalme, Papa alitoa hati Regnans in excelsis (12 Agosti 1308) ili kuitisha mtaguso mkuu huko Vienne tarehe 1 Novemba 1310, kwa lengo la kujadili mada 4:
• suala la Wahekalu;
• vita vya msalaba;
• hali ya imani na Kanisa kwa jumla;
• urekebisho wa Kanisa.
Mtaguso ulichelewa kuanza hadi tarehe 16 Oktoba 1311, walipokuwepo washiriki 170 hivi, ambao kati yao Wafaransa walikuwa zaidi ya thuluthi moja. Wengine walizuiwa na mfalme wa Ufaransa.
Vikao rasmi vikawa vitatu hadi Machi 1312.
Kuhusu Wahekalu, mtaguso uliamua kufuta shirika lao kama alivyopenda mfalme, bila kulifanyia utafiti wala kulitolea hukumu.
Kuhusu Vita vya Msalaba, uliamua kuvianza upya na kwa ajili hiyo kutoza zaka kwa miaka sita, lakini mfalme alijitwalia hizo pesa bila kutekeleza ahadi yake ya kuongoza vita hivyo.
Kuhusu imani, ulijadili baadhi ya mafundisho hasa ya makundi kadhaa ya watawa, lakini uamuzi ulichukuliwa baadaye tu.
Kuhusu urekebisho, ulidai haki za Kanisa ziheshimiwe na serikali za nchi. Pia ulijadili kirefu mahusiano ya ndani, hasa kati ya maaskofu, maparoko na watawa.

Mtaguso wa Konstanz (1414-1418)

Mtaguso wa Konstanz (Ujerumani) unahesabiwa na Kanisa Katoliki kama mtaguso mkuu wa kumi na sita. Uliitishwa na antipapa Yohane XXIII kwa ombi la kaisari Sigismund wa Ujerumani ukathibitishwa na Papa Gregori XII (1406-1415).
Lengo kuu lilikuwa kumaliza Farakano la Magharibi lililofikia hatua ya kuona maaskofu watatu kujidai Papa kwa wakati mmoja. Malengo mengine yalikuwa kung’oa uzushi na kurekebisha Kanisa “katika kichwa na viungo vyake”.
Hatimaye Papa Gregori XII alikubali kujiuzulu, wapinzani wake wawili waliondolewa, na Papa Martin V akachaguliwa.
Ulikuwa mtaguso muhimu kwa wingi wa waliohudhuria (makardinali 29, maaskofu 186, maabati zaidi ya 100 na wataalamu 300 hivi), muda (vikao 55) na mafanikio, ingawa majaribio yake ya mapinduzi yalishindikana, hasa ulipodai kuwa na mamlaka ya juu kuliko Papa.
Kati ya maamuzi mengine kuna hukumu dhidi ya John Wyclif na Jan Hus kama wazushi.

Mtaguso wa Firenze (1431-1445)

Mtaguso wa Firenze uliitishwa na Papa Martin V (1417-1431) mwaka wa mwisho wa uongozi wake ili kutekeleza shingo upande agizo la Mtaguso wa Konstanz la kwamba mtaguso ufanyike mara kwa mara.
Mtaguso ulianza Basel (Uswisi) chini ya Papa Eugenio IV (1431-1447), ukiwa na maaskofu wachache kulingana na mapadri na walei wenye haki ya kupiga kura.
Ingawa mtaguso ulifaulu kupatanisha wafuasi wa Hus na Kanisa, na kutoa sheria kadhaa za urekebisho kwa kibali cha Papa, baadaye ulianza kumshambulia yeye pamoja na makardinali, ukionyesha wazi wengi waliuona una mamlaka ya juu kuliko Papa, kinyume cha mapokeo.
Hapo Eugenio IV aliuvunja halafu akauhamishia Ferrara (Italia), ulipokutanika tarehe 8-1-1438, bila kujali upinzani wa wale ambao walibaki Basel na kumchagua antipapa wa mwisho, Felix V.
Huko Italia ulifika ujumbe mkubwa kutoka Konstantinopoli kwa ajili ya kurudisha umoja kati ya Kanisa Katoliki na Waorthodoksi. Kati ya wajumbe 700 kulikuwa na kaisari na patriarki wa Konstantinopoli, walioogopa Waturuki watateka mji wao (kama ilivyotokea kweli tarehe 29 Mei 1453); hivyo walihitaji msaada wa Wakristo wenzao wa magharibi.
Ferrara iliachwa kutokana na uhaba wa majengo na hofu ya tauni. 7
Mwaka 1439 mtaguso ulihamia Firenze ukafikia makubaliano ya kurudisha umoja (6-7-1439), ingawa uamuzi ukashindwa kutekelezwa kwa kiasi kikubwa kutokana na upinzani wa waumini wa Konstantinopoli.
Vilevile tarehe 22-11-1439 yalifikiwa makubaliano na Waarmenia na tarehe 4-2-1440 yale na Wamisri.
Hatimaye tarehe 24-9-1443 mtaguso ulihamia Roma kwenye Laterano. Huko yalifikiwa makubaliano ya kurudisha umoja na Wasiria kadhaa (30-4-1444) na Wakaldayo na Wamaroni wa Kupro (7-8-1445).
Hakuna hati kuhusu mwisho wa mtaguso. Lakini waliobaki Basel na kujitenga na Papa, kufikia tarehe 19-4-1449 walimkubali Nikolaus V na siku sita baadaye walifunga mkutano wao.
Mtaguso huo ulichochea Wakristo wa magharibi kutamani mawasiliano na wenzao wa Ethiopia na India, jambo lililowafanya waanze zile safari za mbali kupitia baharini zilizowafikisha Afrika Kusini na Mashariki, China na Amerika.

Mtaguso V wa Laterano (1512-1517)

Mtaguso V wa Laterano ulifanyika kuanzia mwaka 1512 hadi 1517 huko Roma. Kanisa Katoliki linauhesabu kama mtaguso mkuu wa kumi na nane.
Uliitishwa na Papa Julius II (1503-1513) ambaye alianza kuusimamia tarehe 3 Mei 1512. Baada ya kifo chake, uliendelezwa na Papa Leo X (1513-1521) hadi kikao cha 12 na cha mwisho kilichofanyika tarehe 16 Machi 1517.
Ulihudhuriwa na maaskofu 100 hivi, wengi wao wakitokea Italia. Kutofika kwa wajumbe kutoka nchi nyingine, pamoja na wengi kukosa nia ya kujirekebisha, kulichangia kufanya utekelezaji wa maamuzi ya mtaguso ushindikane.
Maamuzi hayo yalitolewa kwa hati za Papa. Mengine yanahusu mafundisho ya imani, mengine maagizo ya urekebisho wa Kanisa.
Kabla yake kilifanyika “Kitaguso” cha Pisa: kwa kuwa Papa Julius II alikuwa hatekelezi kiapo chake cha kuitisha mtaguso kwa ajili ya urekebisho, baadhi ya makardinali, wakihimizwa na watawala wa Ujerumani na Ufaransa, waliuitisha huko Pisa (Italia) kuanzia tarehe 1 Septemba 1511. Walikusanyika wachache tarehe 1 Oktoba, halafu katika kikao cha nane walimsimamisha Papa wakahamia Lyon (Ufaransa).
Papa aliitikia “kitaguso” hicho kwa hati ya tarehe 18 Julai 1511, ambayo pamoja na kukipinga na kujitetea aliitisha mtaguso mkuu ukusanyike tarehe 19 Aprili 1512 huko Laterano.
Vita vilichelewesha mwanzo wa mtaguso wenyewe hadi tarehe 3 Mei 1512, walipokusanyika katika basilika la Laterano makardinali 15, mapatriarki 2, maaskofu wakuu 10, maaskofu 56, maabati na wakuu wa mashirika ya kitawa wachache pamoja na mabalozi wa nchi 3. Mwisho walikuwepo makardinali 23 na maaskofu 122.
Upande wa matokeo, utekelezaji wa maagizo ya mtaguso ulikuwa mdogo sana, la sivyo pengine Matengenezo ya Kiprotestanti yasingetokea. Ukweli ni kwamba Martin Luther aliyaanzisha miezi sita tu baada ya mtaguso kwisha.

Mtaguso wa Trento (1545-1563)

Mtaguso wa Trento (uliofanyika kwa kwikwi kuanzia mwaka 1545 hadi 1563), unahesabiwa na Kanisa Katoliki kuwa mtaguso mkuu wa kumi na tisa.
Mtaguso huo, uliochukua muda mrefu kuliko yote ya historia, ulieneza urekebisho wa Kanisa na kuchukua msimamo kuhusu mafundisho ya Waprotestanti waliojitokeza katika hiyo karne XVI.
Mtu wa kwanza kulilia mtaguso ambao uamue kati yake na papa alikuwa Martin Luther (1517): huko Ujerumani ombi lake liliungwa mkono na wengi, pamoja na kaisari Karolo V aliyeuona kuwa njia ya kurekebisha Kanisa lakini pia ya kujiimarisha kimamlaka. Ndiyo sababu kuu iliyomfanya Papa Klementi VII (1523-1534), aliyesimama upande wa Ufaransa, kukataa kabisa kuuitisha.
Wazo hilo lilipata nguvu tena chini ya mwandamizi wake, Papa Paulo III (1534-1549), ambaye mwaka 1536 aliitia kwanza Mantova halafu Vicenza maaskofu na maabati wote, pamoja na wafalme wadogo wengi wa Dola takatifu la Kijerumani.
Baada ya juhudi mbalimbali kushindikana, mwaka 1542 uamuzi ulifikiwa wa kuitisha mtaguso huko Trento kwa sababu ni mji wa Italia lakini ulikuwa ndani ya mipaka ya dola hilo. Hatimaye (Novemba 1544) papa aliweza kutoa hati ya kuitisha mtaguso inayoitwa Laetare Jerusalem.
Mtaguso ulifunguliwa rasmi tarehe 13 Desemba 1545 katika kanisa kuu la Mt. Vigilio.
Mwanzoni mtaguso ulikuwa na maaskofu wachache, karibu wote kutoka Italia, ukatawaliwa na wajumbe wa papa. Kati ya makardinali wapya (Contarini, Sadoleto, Carafa, Fisher na huyo Pole) wengi walipenda urekebisho.
Zilijadiliwa na kupitishwa hasa dogma dhidi ya mafundisho ya Waprotestanti, kama vile kuhusu utakaso na wokovu. Pamoja na kupitisha tafsiri rasmi ya Biblia katika Kilatini iliyo maarufu kwa jina la Vulgata, kati ya maamuzi muhimu zaidi upo ule wa kudai maaskofu waishi katika majimbo yao ili kufanya uchungaji uliowapasa.
Baada ya mtaguso kuhamishiwa Bologna, Papa Paulo III aliusimamisha mnamo Septemba 1549.
Papa Julius III (1550-1555) aliuitisha tena kuanzia tarehe 1 Mei 1551 na zikatolewa hati juu ya sakramenti za Ekaristi, Kitubio na Mpako wa wagonjwa. Polepole waliohudhuria waliongozeka, 8
wakiwemo Waprotestanti wengi pia, wakidai wanateolojia wao wawe na haki ya kupiga kura na hati zilizokwishatolewa zifutwe. Ndipo ilipoonekana wazi kwamba tofauti katika imani ni kubwa mno.
Majeshi ya Kiprotestanti yalipokaribia Trento, Papa alikubali kusimamisha tena mtaguso tarehe 28 Aprili 1552.
Sehemu ya mwisho ya mtaguso baada ya kuitishwa ilichelewa kuanza hadi tarehe 18 Januari 1562, tena ilikabili matatizo mengi, lakini iliokolewa na kutawaliwa na askofu wa Milano Karolo Borromeo, mpwa wa Papa Pius IV (1559-1565) aliyemalizia haraka mtaguso wakiwemo wajumbe 255.
Katika sehemu hiyo yalitolewa mafundisho rasmi kuhusu Misa, Daraja takatifu na Ndoa, Toharani, sala kwa watakatifu, heshima kwa masalia na rehema. Pia Kanisa la Roma lilikubaliwa kama mama na mwalimu wa makanisa yote. Maaskofu wote walitakiwa kuahidia utiifu kwa Papa, ambaye peke yake ana haki ya kuitisha mtaguso mkuu. Kwa msingi huo, mtaguso ulimuachia Papa kuthibitisha maamuzi yote, naye alifanya hivyo bila kujali upinzani wa maofisa wake huko Roma.
Isitoshe, mwishoni, maamuzi mbalimbali yaliachwa mikononi mwa Papa na ofisi zake, yakachukuliwa miaka iliyofuata; kati yake, urekebisho wa Breviari na Misale, kwa kusawazisha liturujia za majimbo ya magharibi (isipokuwa chache, kama ya Milano na Lyon) kulingana na mapokeo ya Roma. Halafu ikatolewa Katekisimu ya Trento na Orodha ya vitabu vilivyokatazwa (Index librorum prohibitorum).

Mtaguso I wa Vatikano (1869-1870)

Mtaguso I wa Vatikano unatazamwa na Kanisa Katoliki kama mtaguso mkuu wa ishirini katika historia yake.
Uliitishwa rasmi na Papa Pius IX (1846-1878) mnamo 29 Juni 1867 na vikao vyake viliendelea katika Basilika la Mt. Petro huko Vatikano mjini Roma kuanzia tarehe 8 Desemba 1869 hadi vilipokatika mnamo 1870, kutokana na jeshi la Italia kuteka Roma tarehe 20 Septemba.
Walishiriki maaskofu na mapadri 774 (kati ya 1050 wenye haki ya kuhudhuria), ambao kwa mara ya kwanza walitokea mabara yote. Pia ilikuwa mara ya kwanza ya kutokuwepo wawakilishi wa serikali. Kumbe wajumbe wa Waorthodoksi na wa Waprotestanti walialikwa pia, lakini hawakufika.
Tarehe 24 Aprili 1870, baada ya majadiliano mengi, ilipitishwa hati Dei Filius juu ya Mungu, ufunuo, imani, na uhusiano kati ya imani na akili.
Ingawa lengo halikuwa hilo, tokeo kuu la kazi ya mtaguso huo ni tangazo la dogma ya Papa kuwa na karama ya kutokosea katika mafundisho ya imani na maadili anayoyatoa ili yadumu moja kwa moja pale anapotimiza masharti fulani (kwa kifupi: akisema “ex cathedra”, yaani “kutoka ukulu).
Dogma hiyo iliimarisha mamlaka ya Papa na umoja wa Kanisa dhidi ya maelekeo ya kitaifa ambayo yalitawala karne zilizotangulia yakisababisha matatizo mengi.

Mtaguso II wa Vatikano (1962-1965)

Malengo ya Mtaguso II wa Vatikano

Muda mfupi baada ya kuchaguliwa Papa, mwenye heri Yohane XXIII alitangaza uamuzi wake wa kuitisha mtaguso mkuu akiamini kwamba utaweza kuandaa na kusababisha ustawi mpya wa maisha ya Kanisa. Lengo kuu la mtaguso lilikuwa kuliamsha Kanisa likumbuke wito wake na kwa kujifanya upya kwa ndani lipate msukumo mpya wa kimisionari ili kuwatangazia watu wote ujumbe wa milele wa wokovu, amani na umoja.
Tangazo hilo lilitolewa tarehe 25-1-1959. Baada ya maandalizi, Mtaguso II wa Vatikano ulifunguliwa tarehe 11-10-1962. Vikao vinne vikafanyika mpaka ulipofungwa tarehe 8-12-1965. Kila kikao kilianza Oktoba na kumalizika Desemba ya miaka hiyo.
Kwa kuwa Yohane XXIII alifariki tarehe 2-6-1963, vikao vitatu vya mwisho viliongozwa na mwandamizi wake, Paulo VI, na hati zote kumi na sita zikatolewa chini yake pia kwa kupigiwa kura ya ndiyo karibu kwa kauli moja. Maaskofu na wakuu wa mashirika kadhaa wenye haki ya kupiga kura walikuwa kama elfu tatu, wakiwakilisha karibu Kanisa lote duniani, isipokuwa nchi zile zenye kuwadhulumu Wakristo.

Ni nini imani ya Kanisa Katoliki kuhusu matakwa ya Mungu na mapenzi ya binadamu?

Kanisa Katoliki linatambua kuwa Mungu aliumba ulimwengu na binadamu kwa mapenzi yake, lakini pia Mungu alitupa uhuru wa kuchagua. Ni wajibu wa binadamu kutimiza matakwa ya Mungu na kuishi maisha yanayoambatana na mapenzi yake.

Katika Waraka wa Yohane Paulo II, Fides et Ratio, Kanisa Katoliki linatilia mkazo kwamba binadamu ana jukumu la kutafuta ukweli na kuelewa mapenzi ya Mungu. Kupitia kwa imani na akili, binadamu anaweza kufikia maarifa ya ukweli huu.

Katika Maandiko Matakatifu, tunaona jinsi ambavyo Mungu anatutaka kufuata mapenzi yake. Mtume Paulo aliandika katika Waraka wa Waebrania 10:36, "Kwa hiyo, ninyi mnahitaji subira ili mtimize mapenzi ya Mungu na mpokee ahadi yake." Hii inamaanisha kuwa kwa kumtii Mungu na kufuata mapenzi yake, tunaweza kufikia ahadi zake.

Kanisa Katoliki linamfundisha mtu anapaswa kumtii Mungu na kusubiri mapenzi yake. Hii inamaanisha kuwa tunapaswa kufuata amri za Mungu na kuishi maisha yenye haki na kwa upendo. Katika KKK 2822, inasemekana, "Tunatafuta mapenzi ya Mungu katika maisha yote, hasa katika maamuzi yetu muhimu."

Katika Maandiko Matakatifu, tunajifunza kwamba Mungu anataka tufanye kazi yetu kwa bidii na kwa upendo. Paulo aliandika katika Waraka wa Wakolosai 3:23-24, "Kila mfanyalo, fanyeni kwa moyo wenu wote, kama kwa Bwana, si kwa ajili ya wanadamu, kwa maana mnajua ya kuwa mtapokea ujira wa mrithi kutoka kwa Bwana."

Kanisa Katoliki linatilia mkazo kwamba inatupasa kufanya kazi kwa heshima na kwa uaminifu, kwa kuwa kwa kufanya hivyo tunamfurahisha Mungu. Kanuni ya Maadili ya Kikatoliki inatufundisha kuwa tunapaswa kutoa kazi yetu kwa Mungu na kuifanya kwa uangalifu na upendo, ili kuonyesha upendo wetu kwa Mungu.

Kwa hiyo, Kanisa Katoliki linatambua kwamba tunapaswa kutimiza matakwa ya Mungu na kuishi maisha yanayoambatana na mapenzi yake. Tunapaswa kumtii Mungu, kufanya kazi yetu kwa bidii na kwa upendo, na kutafuta ukweli na maarifa ya mapenzi yake. Kwa kufanya hivyo, tunapata baraka za Mungu na kupokea ujira wake wa milele.

JE,SHERIA YA MAPADRE KUTOOA NA KUISHI USEJA IMEANDIKWA WAPI KATIKA BIBLIA AU IMETUNGWA TU NA PAPA?

Pengine umewahi kuulizwa swali hili wakati fulani.Na jibu lake ni kama ifuayavyo:
Mtu anapouliza kila kitu kimeandikwa wapi katika Biblia ni kudhihirisha kutokuijua au kuielewa vizuri Biblia Takatifu na historia yake.Mtu anapong’ang’ania “nionyeshe kitu fulani kimeandikwa wapi kwenye Biblia”ni kutaka kujiona ya kwamba yeye anaielewa sana Biblia na ameisoma yote kwa hiyo kila kitu kilichopo kwenye Biblia anakifahamu kumbe haijui Biblia bali anakariri Biblia!
Na hili suala la kushupalia swala la kuoa linadhihirisha jinsi gani tulivyo kizazi cha zinaa,ni kama tunadhani kuwa UZIMA upo katika kujamiiana!La hasha.
Paulo anasema “Kwasababu ya zinaa ni bora kuoa na kuolewa”(1Wakorintho 7:2.9) haya sio maneno ya kufurahia na kuchekelea tu maana “YANAWALENGA WALE WALIOSHINDIKANA KATIKA YALE YAPENDEZAYO”(1Wakorintho 7:1.8)sasa ni lazima tujiulize je tumeshindikana kiasi hicho?,hiyo sio sifa!
1Wakorintho 7:1.8
“Basi kwa habari ya mambo yale mliyoandika,ni heri mwanaume asimguse mwanamke,8.Lakini nawaambia wale wasiooa bado na wajane heri wakae kama mimi nilivyo”
Na Paulo Mtume anasema “Ni bora kuoa au kuolewa” lakini hakusema “Ni LAZIMA kuoa au kuolewa”
Suala la kutooa kwa mapadre kadiri ya historia lilianza tangu zamani kabisa mwanzoni mwa milenia ya pili katika mtagusi wa pili wa Laterani mwaka wa 1139 ili waweze kumtumikia Mungu kwa uhuru na bila mawaa wala pasipo vikwazo(1wakorintho 7:32-35)
1wakorintho 7:32-35
“32Lakini nataka msiwe na masumbufu.Yeye asiyeoa hujishughulisha zaidi na mambo ya Bwana ampendezeje Bwana;33.bali yeye aliyeoa hujishughulisha zaidi na mambo ya dunia hii,jinsi atakavyompendeza mkewe.34-Tena iko tofauti kati ya mke na mwanamwali.Yeye asiyeolewa hujishughulisha na mambo ya Bwana ili apate kuwa mtakatifu mwili na Roho.Lakini yeye aliyeolewa hujishughulisha na mambo ya dunia hii,jinsi atakavyompendezesha mumewe.,35.Nasema hayo niwafaidie ninyi,si kwamba niwategee tanzi,bali kwaajili ya vile vipendezavyo,tena mpate kumhudumia Bwana pasipo kuvutwa na mambo mengine”
Maandiko hayo hapo juu yanajieleza wala sidhani kama yanahitaji kufafanuliwa zaidi ya yanavyojifafanua yenyewe.
Watu wengine wanafikiri kwamba kutooa ni dhambi,kama ni hivyo basi hata Yesu mwenyewe alikosa maana hata yeye mwenyewe hakuoa.
Yesu mwenyewe anafundisha kuhusu ubikira(Mathayo 19:10-12)
Mathayo 19:10-12,
“Wanafunzi wake wakamwambia,kama mambo ya mme na mke yakiwa hivyo ni afadhali kutuooa kabisa.Lakini Yeye akawaambia ‘SI WOTE WAWEZAO KULIPOKEA NENO HILO,ILA TU WALE WALIOJALIWA,maana wako MATOWASHI waliozaliwa katika hali hiyo toka matumboni mwa mama zao;tena wako matowashi waliofanywa na watu kuwa matowashi,tena wako Matowashi WALIOJIFANYA WENYEWE KUWA MATOWASHI KWAAJILI YA UFALME WA MBINGUNI’,awezaye kulipokea neno hili na alipokee”
Yesu mwenyewe analifafanua jambo hili kwa mapana,katika orodha ya matowashi Yesu aliowataja,Mapadre ni Matowashi waliojifanya hivyo kwaajili ya huduma ya kanisa na ufalme wa Mungu.
Tena Yesu anatuambia waziwazi kwamba”sio wote wawezao kulipokea neno hilo”yaani sasa sio wote wawezao kuwa Matowashi(Mapadre)bali ni wale tu waliojaliwa na Mungu neema hiyo.wale wasioweza kuishi upadre huoa na kuwa na familia.Tena Yesu anamalizia kwa kusema “Awezaye kulipokea fundisho hili na alipokee”,kwa maana nyingine ni kusema “Fundisho au Utowashi huu sio wa lazima”anayeweza kuishi maisha hayo basi na ayapokee na yule asiyeweza basi aache!
Vilevile Mitume ili kumfuata Yesu kikamilifu waliyaacha yote waliokuwa nayo ikiwepo familia zao ili wamtumikie Bwana(Mathayo 19:27.29)
Mathayo 19:27.29:
“Ndipo Petro akajibu akamwambia ‘Tazama sisi tumeacha vyote tukakufuata wewe,tutapata nini basi?29.Amini nawaambia,kila mtu aliyeacha nyumba au ndugu wa kiume au wakike,au baba au mama au watoto au mashamba KWAAJILI YA JINA LANGU,atapokea mara mia zaidi na kuurithi uzima wa milele”
katika injili hiyo,Yesu anadhihirisha kwamba aliyeacha hayo yaliotajwa si kwasababu hawezi kuyapata la hasha,bali ameyaacha hayo yote KWAAJILI YA JINA LA YESU atapokea mengi hapa duniani halafu tena ataurithi ufalme wa mbinguni.
Mapadre wameyaacha hayo yote,wameacha nyumba,familia zao na kila kitu SIO KWASABABU HAWANA UWEZO AU HAWAWEZI KUPATA MAMBO HAYO bali WAMEACHA KWASABABU YA KUMTUMIKIA MUNGU KWA KADIRI YA MAANDIKO MATAKATIFU na kwakutaka kwao kuyaishi kimamilifu MASHAURI YA INJILI ikiwepo USEJA.
Maneno ya Paulo na yale ya Yesu mwenyewe kuhusu kumtumikia Mungu bila kuoa sio ya bahati mbaya bali ndiyo njia bora na inayofaa sana na kukubalika mbele ya Mungu.
Kwahiyo unapowaona mapadre hawaoi ujue sababu yake ni hiyo kwamba “Wamejitoa kwaajili ya kulihudumia kanisa”
(Na pia huwa nawashangaa mno watu wanaowapiga vita Mapadre kwamba kwanini hawaoi,najiuliza je,hao Mapadre wamewakataza wao kwamba wasioe?.)..na kama jibu ni hapana,sasa Je,”Pilipili ya shamba usiyoila inakuwashia nini?”
TUMSIFU YESU KRISTO!

Ni nini imani ya Kanisa Katoliki kuhusu upendo na huruma?

Karibu kwenye makala yangu kuhusu imani ya Kanisa Katoliki kuhusu upendo na huruma. Katika kanisa Katoliki, upendo ni jambo muhimu sana katika maisha yetu ya Kikristo. Kulingana na Biblia, Mungu ni upendo na ametualika sisi sote tuweze kuishi kwa upendo (1 Yohana 4:8).

Kanisa Katoliki linatueleza kuwa upendo ni kitu ambacho kinatoka kwa Mungu na kinapaswa kuongoza maisha yetu. Tunapaswa kuwapenda wenzetu kama tunavyojipenda wenyewe (Marko 12:31). Kwa hivyo, Kanisa Katoliki linatufundisha kufurahia upendo wa Mungu na kuwa na upendo kwa jirani yetu.

Katika kufuata njia ya upendo, Kanisa Katoliki pia linatufundisha kuhusu huruma. Huruma ni tendo la upendo ambalo linatupatia fursa ya kuonyesha upendo huo kwa wengine. Kama vile Mungu alivyotupatia huruma na msamaha kupitia Yesu Kristo, tunaweza pia kuwa na huruma kwa wengine.

Kwa kufuata kanuni za Kanisa Katoliki, tunapaswa kujitolea kwa wengine na kuwa tayari kuwasaidia wakati wanapohitaji msaada. Kwa kufanya hivyo, tunakuwa chombo cha upendo na huruma ya Mungu katika ulimwengu huu.

Kanisa Katoliki pia linatufundisha kuwa na huruma kwa wale wanaohitaji. Kama vile Yesu Kristo alivyowaonyesha huruma wenye shida, tunapaswa kuwa tayari kuwasaidia wale wanaohitaji msaada wetu. Kwa kufanya hivyo, tunakuwa vyombo vya upendo na huruma ya Mungu katika maisha yetu.

Kanisa Katoliki linatufundisha kuwa na huruma pia kwa wale ambao wametukosea. Kama vile Mungu alivyotupatia msamaha wetu kupitia Yesu Kristo, tunapaswa kuwa tayari kuwasamehe wale ambao wametukosea. Kwa kufanya hivyo, tunakuwa vyombo vya upendo na huruma ya Mungu katika ulimwengu huu.

Kwa kumalizia, Kanisa Katoliki linatueleza kuwa upendo na huruma ni muhimu sana kwa maisha yetu ya Kikristo. Kwa kufuata njia ya upendo na huruma, tunakuwa vyombo vya upendo na huruma ya Mungu katika ulimwengu huu. Kwa hivyo, tunapaswa kuwa tayari kuwa na upendo na huruma kwa wengine katika maisha yetu ya kila siku. Kama vile Catechism ya Kanisa Katoliki inatueleza, "Upendo ni roho ya maisha ya Kikristo".

Je, Kanisa Katoliki linahubiri na kufundisha Ekaristi Takatifu kuwa Mwili na Damu ya Yesu Kristo?

Je, Kanisa Katoliki linahubiri na kufundisha Ekaristi Takatifu kuwa Mwili na Damu ya Yesu Kristo?

Ndio, Kanisa Katoliki linahubiri na kufundisha kuwa Ekaristi Takatifu ni Mwili na Damu ya Yesu Kristo. Katika Mafundisho ya Kanisa Katoliki, Ekaristi Takatifu ni chanzo na kilele cha maisha ya kikristo. Ni kwa njia ya Ekaristi Takatifu tu ndipo tunapata nguvu na neema za kimungu za kuendeleza maisha ya kikristo.

Katika Injili ya Yohane, Yesu Kristo alisema "Mimi ndimi chakula cha uzima. Anayeja kwangu hataona njaa kamwe na anayeniamini hataona kiu kamwe" (Yohane 6:35). Yesu alikuwa anafundisha umuhimu wa Ekaristi Takatifu kwani ndio chanzo cha uzima wa milele.

Pia, katika Agano Jipya, tunaona jinsi Yesu alivyobadilisha mkate na divai kuwa Mwili na Damu yake wakati wa karamu ya mwisho (Mathayo 26:26-28). Kwa kuwa Kanisa Katoliki linamwamini Yesu kuwa ni Mungu na mwanadamu, linahubiri na kufundisha kuwa wakati wa Misa Takatifu, mkate na divai vinabadilishwa kuwa Mwili na Damu ya Yesu Kristo.

Kwa mujibu wa Catechism of the Catholic Church, "Ekaristi Takatifu ni Mwili na Damu ya Kristo, na kwa ajili hiyo ina Kristo mzima, Mungu na mwanadamu, katika uhalisi wake wa kweli" (CCC 1374). Kanisa Katoliki linamwamini Yesu kuwa ni Mungu na mwanadamu, na kwa hivyo, Ekaristi Takatifu ni Mwili na Damu yake wakati wa Misa Takatifu.

Kanisa Katoliki linahubiri na kufundisha Ekaristi Takatifu kwa sababu ina nguvu ya kiroho ya kumpa mwanadamu neema na uzima wa milele. Kwa hiyo, ni muhimu kwa kila Mkristo kushiriki katika Misa Takatifu na kupokea Mwili na Damu ya Yesu Kristo kama njia ya kuyakaribisha maisha ya kiungu ndani mwetu.

Kwa kumalizia, Kanisa Katoliki linahubiri na kufundisha kuwa Ekaristi Takatifu ni Mwili na Damu ya Yesu Kristo. Kwa hivyo, ni muhimu kwa kila Mkristo kushiriki katika Misa Takatifu na kupokea Mwili na Damu ya Yesu Kristo kama njia ya kuyakaribisha maisha ya kiungu ndani mwetu.

Je, Kanisa Katoliki linawahimiza waamini kuishi maisha matakatifu na kuwa mashuhuda wa Injili?

Je, Kanisa Katoliki linawahimiza waamini kuishi maisha matakatifu na kuwa mashuhuda wa Injili? Jibu ni ndio! Kanisa Katoliki linatamani sana waamini kuishi maisha matakatifu na kuwa mashuhuda wa Injili. Ni wito wa Mungu kwetu sote kuishi maisha matakatifu na kushuhudia Injili kwa wengine. Katika makala hii, tutaangalia jinsi Kanisa Katoliki linawahimiza waamini wake kuishi maisha matakatifu na kuwa mashuhuda wa Injili.

Kanisa Katoliki linakumbusha waamini wake kuwa wao ni watu wa Mungu na wanapaswa kuishi maisha yao kama sehemu ya mpango wa Mungu. Maisha matakatifu ni maisha yenye utakatifu, upendo, na wema. Tunapaswa kuwa na nia njema kwa wengine, kujitolea, na kuishi katika haki na ukweli. Tumeitwa kuwa watakatifu, na Kanisa linatuhimiza kushiriki katika utakatifu wa Mungu. Kama ilivyoandikwa katika kitabu cha Waebrania 12:14, "Badilisheni maisha yenu, mpate kuwa watu watakatifu kama vile Mungu, Baba yenu, alivyo mtakatifu."

Kanisa Katoliki linatuhimiza pia kuwa mashuhuda wa Injili. Injili ni ujumbe wa upendo wa Mungu kwa wanadamu, na sisi kama waamini tunaitwa kuishuhudia kwa wengine. Tunapaswa kuonyesha upendo kwa wengine, kusamehe, na kuwa na huruma. Kanisa linatuhimiza kuwa wajumbe wa amani na upendo, kama ilivyoandikwa katika kitabu cha Mathayo 5:9, "Heri wenye amani, kwa sababu wao watapewa jina la wana wa Mungu."

Kanisa Katoliki linatukumbusha kuwa Utakatifu ni wito wa wote. Katika Catechism of the Catholic Church, inasema, "Utakatifu ni wito wa wote: "Hii ndiyo mapenzi ya Mungu, utakatifu wenu" (1 Thesalonians 4:3). Utakatifu unamaanisha kuwa mtu anakaribia Mungu na kuwa sehemu ya jamii ya waamini watakatifu. Utakatifu unafanana na mwanga wa Mungu unaowaongoza watu wote, na tunapaswa kuuweka mwanga huu ukiwaka ndani yetu na kuwaonyesha wengine.

Kanisa Katoliki linatumia sakramenti kama njia ya kutusaidia kuishi maisha matakatifu. Tunapopokea sakramenti ya Ekaristi Takatifu, tunakutana na Kristo mwenyewe na kuwa na nguvu ya kukuza upendo na utakatifu katika maisha yetu. Tunapopokea sakramenti ya Upatanisho, tunaweza kuungana tena na Mungu na wengine na kuwa na nia njema ya kubadilisha maisha yetu. Kanisa linatuhimiza kutumia sakramenti kama njia ya kukuza maisha yetu ya utakatifu.

Kanisa Katoliki linatukumbusha kuwa kujitolea ni sehemu muhimu ya kuishi maisha matakatifu. Tunapaswa kujitolea kwa wengine, hasa wale wanaohitaji msaada. Kama ilivyoandikwa katika kitabu cha 1 Yohana 3:18, "Watoto wangu, mapenzi yangu si kuzungumza tu kuhusu upendo, bali kuhusu kutenda." Tunapaswa kuwa wajenzi wa jamii ya upendo, kujitolea kwa wengine, na kuhakikisha kuwa wote wanafurahia maisha.

Kwa hiyo, Kanisa Katoliki linawahimiza waamini kuishi maisha matakatifu na kuwa mashuhuda wa Injili. Tunapaswa kujitahidi kuwa na utakatifu, upendo, na wema. Tunapaswa kuishi kama watu wa Mungu na kushuhudia Injili kwa wengine. Tunapaswa kutumia sakramenti kama njia ya kukuza maisha yetu ya utakatifu. Na tunapaswa kujitolea kwa wengine na kuhakikisha kuwa wote wanafurahia maisha. Hivyo, tuishie kwa neno la Mtakatifu Paulo katika kitabu cha Wafilipi 4:13, "Ninaweza kufanya kila kitu kwa nguvu yake yeye anayenipa nguvu."

Ufanyialo wengine ndilo utakalofanyiwa

Siku niliposoma hili andiko kwa mara ya kwanza nakumbuka, kwanza nilipata mshtuko flani baada ya kulisoma, halafu nikajikuta nikitafakari vitu vingi sana.

Hebu kwanza tusome pamoja andiko hili

ZABURI 109

17 Naye alipenda kulaani, nako kukampata.Hakupendezwa na kubariki, kukawa mbali naye

▶Huu mstari wa 17 umenishangaza sana, halafu ukanifungua na kunifundisha vitu vya msingi sana katika haya maisha tunayoishi

Ngoja tuuchambue kidogo hapa ili tuelewane vizuri

_Alipenda kulaani?………………………….Nako (laana/kulaaniwa) kukampata_

_Hakupendezwa na kubariki……………………(Kubarikiwa) kukawa mbali nae_

NET BIBLE inasema hivii

“He loved to curse others, so those curses have come upon him, He had no desire to bless anyone, so he has experienced no blessings” Kumbe the more ninakuwa na shauku ya kuona wengine wakibarikiwa, the more baraka zinanijia mimi and vice versa

Hapa nikajifunza kwamba kumbe yale mabaya tunayowafanyia au kuwawazia watu kuna uwezekano mkubwa sana yakatupata sisi wenyewe

Na tunapotamani kubarikiwa na kuinuliwa wakati hatufurahii kuona wengine wakiinuliwa, kuinuliwa kutakuwa mbali nasi

Huu mstari unaniongezea maarifa na kunifundisha namna ya kuishi katika ulimwengu huu

Nimewaza pia inawezekana wakati mwingine kuna vitu hatupati ni kwasababu tuu hatufurahii wala hatuombi wengine wapate hivyo

Kumbe kubarikiwa kwangu kunategemea na namna ambavyo ninakuwa baraka kwa wengine na kutamani kuona wengine wakibarikiwa

Shauku yangu ya kutamani wengine wabarikiwe na kuinuliwa ndio nyenzo ya kuinuliwa kwangu na moyo mbovu wa kufurahi kuona wengine wakikwama ndio sababu ya kukwama kwangu?

_”Hii ni kanuni ya ajabu”
Ndugu yangu, unajua hapa najifunza kwamba kumbe kuna uwezekano mkubwa kwamba mikwamo mingine tumekuwa tukijikwamisha sisi wenyewe

Ni kweli ninataka kubarikiwa, lakini ni mara ngapi nimefurahi au kuombea wengine ili wabarikiwe?

Unatamani kupandishwa cheo sawa, lakini wengine wakipandishwa vyeo unanuna? Au ukiona ofisini ndio anapewa safari nyingi za nje unakasirika?

Unatamani kuoa/kuolewa halafu wengine wakioa na kuolewa unaona uchungu juu yao, unawanunia, unapunguza ukaribu?

Unatamani kupata gari zuri lakini wengine wakipata unakasirika?

Nikiwa mtoto mdogo nakumbuka mwalimu mmoja aliwahi fundisha kwamba nisipende sana kujiombea mwenyewe, na akasema kama unahitaji kitu, waombee wengine wasionacho wapate, nawe utajibiwa pia, andiko hili limenifanya nielewe kwanini mwalimu yule alifundisha vile

Na wakati mzaburi anaongea maneno haya hapa chini sikumuelewaga, nilijua ni kawaida tuu, nilisoma kikawaida tuu, lakini sasa ndio nimefunguka ufahamu zaidi

*ZABURI 35*

13 Bali mimi, walipougua wao, Nguo yangu ilikuwa gunia. Nalijitesa nafsi yangu kwa kufunga; Maombi yangu yakarejea kifuani mwangu

Bila kujali watu walikuwa wakimuwazia na kumfanyia nini, alipowaombea tuu, maombi yale yalirejea, yalifanya kazi na katika maisha yake. Kumbe kuomba kwaajili ya wengine wafanikiwe, wainuliwe, wabarikiwe na wapandishwe kunarejesha matunda kwetu pia

Ubaya unaomfanyia mwingine si ajabu ukakupata

Kuanguka unakomuombea mwingine kutakujia wewe

Kanuni hii inanifundisha pia kuwa YESU aliposisitiza tupendane alikuwa na maana kuu

Alijua kwamba ukiwa na chuki kwa mwingine chuki ile itakuathiri wewe

Ukiwa na moyo wa kufurahi wengine wanaposhindwa, kushindwa kutakupata wewe

Kwanini sasa tusichague kubariki wengine ili baraka zile zitupate na sisi pia?

Kwanini tusiwaombee mema wengine ili maombi yale ya mema yatutendee mema sisi?
Ni vyema sasa tukachagua kuwa na moyo wa upendo, moyo utakaowawazia na kuwatendea mema wengine kwasababu mema yale tuwafanyiayo wengine yatatuletea mema maishani mwetu pia

Jipime, jiangalie, jichunguze

Waza mema kwaajili ya wengine, mema yaje kwaajili yako

MITHALI 17

13 Yeye arudishaye mabaya badala ya mema,Mabaya hayataondoka nyumbani mwake

If you love to curse others, those curses will come upon you

If you have NO desire to bless others, then you will experience NO blessings

CHOOSE TO BLESS OTHERS,BLESSING WILL FOLLOW YOU

Je, Kanisa Katoliki linamwamini Yesu Kristo kama Mungu na mwanadamu kamili?

Je, Kanisa Katoliki linamwamini Yesu Kristo kama Mungu na mwanadamu kamili?

Ndio! Kanisa Katoliki linamwamini Yesu Kristo kama Mungu na mwanadamu kamili. Hii ni kwa msingi wa mafundisho ya imani yetu ya Utatu Mtakatifu. Kwa maana hiyo, Yesu Kristo ni Mungu wa kweli na mwanadamu wa kweli. Hii inamaanisha kuwa Yesu Kristo alikuwa na asili mbili, yaani, asili ya kimungu na asili ya kibinadamu.

Kwa kuwa Yesu Kristo ni Mungu, anayo sifa zote za Mungu, kama vile kuwa mwenye nguvu, mwema, mwenye hekima, na mwenye uwezo wa kuumba na kusimamia ulimwengu.

Pia, kwa kuwa Yesu Kristo ni mwanadamu, Alipitia kila kitu tunachopitia sisi kama wanadamu, kama vile majaribu, mateso, na hata kifo. Hii inamaanisha kuwa Yesu alikuwa na uwezo wa kuelewa matatizo yetu na kuhisi maumivu yetu, kwa sababu yeye mwenyewe alipitia hayo.

Tunawezaje kuwa na uhakika kuwa Yesu Kristo ni Mungu na mwanadamu kamili? Ni muhimu kuzingatia maandiko Matakatifu, ambayo yanaeleza waziwazi ukweli huu. Kwa mfano, katika Yohana 1:1 tunasoma kuwa "Neno alikuwako mwanzo, naye Neno alikuwa na Mungu, naye Neno alikuwa Mungu." Hii inaonyesha kwamba Yesu Kristo ni Mungu.

Kwa upande mwingine, katika Wafilipi 2:6-8 tunasoma kuwa "Aliyekuwa katika hali ya Mungu, hakufikiria kuwa sawa na Mungu kuambatana nayo; bali alijinyenyekeza mwenyewe, akachukua namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu. Akajionyesha kuwa mtu." Hii inaonyesha kwamba Yesu Kristo ni mwanadamu kamili.

Kwa kuongezea, mafundisho ya Kanisa Katoliki yanathibitisha kwamba Yesu Kristo ni Mungu na mwanadamu kamili. Kwa mfano, Kanisa linakiri kuwa Yesu Kristo alizaliwa kwa Bikira Maria, aliteswa, akafa na kufufuka kutoka kwa wafu. Katika tafsiri hii ya imani, Kanisa linadhihirisha kuwa Yesu Kristo ni Mungu na mwanadamu kamili.

Kwa hiyo, kama Wakatoliki, tunapaswa kumwamini Yesu Kristo kwa moyo wote kama Mungu na mwanadamu kamili. Tunapaswa kumpenda, kumtii, na kumwabudu kama Bwana na mwokozi wetu. Tumwombe Yesu Kristo ili atusaidie kufuata mfano wake na kuwa karibu naye katika maisha yetu yote.

Huruma ya Mungu: Mwanga katika Giza la Dhambi

Huruma ya Mungu: Mwanga katika Giza la Dhambi

  1. Kama Wakristo, tunajua kwamba Mungu ni muumba wetu, na kwamba tunapata maisha yetu kutoka kwake. Kupitia huruma yake, Mungu anatupa nafasi ya kufufuka kutoka kwa dhambi zetu na kutangaza upendo wake kwetu.

  2. Kwa mujibu wa Biblia, Mungu ni mwenye huruma na upendo kwetu. Zaburi 103:8 inasema, "Bwana ni mwenye huruma na neema; si mwepesi wa hasira na ni mwingi wa upendo." Kwa hiyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu hatutupi kamwe, na kwamba kila wakati yuko tayari kuwa msamaha na kusamehe dhambi zetu.

  3. Kwa kupitia nguvu ya Roho Mtakatifu, tunaweza kushinda dhambi na kuishi maisha safi. Galatia 5:16 inasema, "Basi nasema, enendeni kwa Roho, wala hamtazitimiza kamwe tamaa za mwili." Kwa hiyo, tunahitaji kufuata mwongozo wa Roho Mtakatifu ili tuweze kushinda mawazo ya dhambi na kuishi maisha safi.

  4. Katika Catechism ya Kanisa Katoliki, tunajifunza kwamba huruma ya Mungu ina jukumu muhimu katika maisha yetu. Kifungu cha 1422 kinasema, "Kanisa limepokea kutoka kwa Bwana shughuli ya kuwasamehe dhambi za waamini kwa njia ya Sakramenti ya Kitubio." Kwa hiyo, tunaweza kumwomba Mungu sakramenti ya kitubio ili tupate msamaha wa dhambi zetu.

  5. Huruma ya Mungu pia inaonekana katika maisha ya watakatifu. Kwa mfano, Mtakatifu Maria Faustina Kowalska alikuwa na maono ambayo yalimwonyesha huruma ya Mungu kwa wanadamu. Katika Kitabu cha Dagala ya Mtakatifu Maria Faustina Kowalska, tunasoma maneno haya kutoka kwa Yesu: "Roho yangu imetolewa kabisa kwa ajili ya walioumbwa, na hakuna kitu chochote kinachoweza kuzuiwa kutoka kwangu kupita ukosefu wao wa mapenzi yangu, lakini wao hataki kuikubali huruma yangu. Ni lazima niwaadhibu, lakini huruma yangu inanilazimisha kufanya kazi kama hiyo. " Kwa hiyo, huruma ya Mungu ni nguvu inayotuongoza kuelekea upendo na msamaha.

  6. Tunahitaji kuwa na imani na kumwomba Mungu kwa ajili ya huruma yake. Marko 11: 24 inasema, "Kwa hiyo nawaambia, yote mnayoyaomba katika sala, aminini kuwa mmeishapata, nanyi mtapewa." Kwa hiyo, tunahitaji kuomba na kumwamini Mungu kwa yote tunayotaka katika maisha yetu.

  7. Huruma ya Mungu inatupa tumaini kwa siku zijazo. Warumi 8:28 inasema, "Tunajua pia kwamba wale wanaompenda Mungu, mambo yote yanafanya kazi pamoja kwa ajili ya wema wao, kwa wale waliopewa wito kulingana na kusudi lake." Kwa hiyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu anatufanyia kazi kila wakati.

  8. Huruma ya Mungu inatupa nguvu ya kuwa na upendo na msamaha kwa wengine. Mathayo 6:15 inasema, "Lakini kama hamtoisamehe watu makosa yao, Baba yenu hatawasamehe makosa yenu." Kwa hiyo, tunahitaji kuwa na upendo na msamaha kwa wengine kama vile Mungu anavyotuonyesha huruma.

  9. Huruma ya Mungu inatupatia uhuru wa kweli katika maisha yetu. Yohana 8:36 inasema, "Kwa hiyo, kama Mwana atawaweka huru, mtakuwa huru kweli kweli." Kwa hiyo, kupitia huruma ya Mungu tunaweza kuwa huru kutoka kwa dhambi na kushinda majaribu katika maisha yetu.

  10. Kwa hiyo, tunahitaji kushikamana na huruma ya Mungu katika maisha yetu. Kupitia sala, sakramenti, na maisha ya kiroho, tunaweza kuwa na nguvu ya kuishi maisha safi na yenye furaha. Kama Wakristo, tunapaswa kuwa wamisionari wa huruma ya Mungu kwa wengine, kuwafikia wale walio katika giza la dhambi na kuwaongoza kuelekea mwanga wa Mungu.

Je, unafikiri nini juu ya huruma ya Mungu? Una maoni gani kuhusu jinsi tunavyoweza kuishi maisha safi na yenye furaha kupitia huruma ya Mungu? Tafadhali shiriki mawazo yako kwenye sehemu ya maoni hapa chini.

Je, Kanisa Katoliki linahubiri na kufundisha umuhimu wa sala katika maisha ya Kikristo?

Sala ni sehemu muhimu katika maisha ya Kikristo. Kanisa Katoliki linahubiri na kufundisha umuhimu wake katika maisha ya waumini. Kupitia sala, tunaweza kuwasiliana na Mungu na kumwomba msaada katika maisha yetu. Sala inatusaidia kupata amani ya nafsi na kuimarisha imani yetu. Ni kwa sababu hii Kanisa Katoliki linahimiza waumini wake kusali mara kwa mara.

Katika Biblia, tunasoma maneno ya Yesu yaliyosema, “Omba na utapewa; tafuta na utapata, piga hodi na mlango utafunguliwa” (Mathayo 7:7). Hii inaonyesha kuwa sala ni njia ya kuomba msaada kutoka kwa Mungu. Pia, Biblia inatueleza kuwa Yesu mwenyewe alikuwa akipenda kwenda peke yake kusali. Kwa hivyo, kama wafuasi wa Yesu tunapaswa kufanya hivyo pia.

Kanisa Katoliki linatumia sala kama sehemu ya ibada. Sala ni sehemu ya liturujia, ambayo ni ibada ya Kanisa Katoliki. Liturujia inajumuisha sala, nyimbo, na maandiko kutoka kwa Biblia. Kupitia sala, waumini wanashiriki katika ibada ya Kanisa na wanapata baraka kutoka kwa Mungu.

Kanisa Katoliki pia linatumia sala kama njia ya kutubu dhambi zetu. Katika sala ya kitubio, waumini wanakiri dhambi zao kwa padri na kupata msamaha wa Mungu. Kwa kufanya hivyo, tunaweza kusafisha roho zetu na kuanza upya.

Kanisa Katoliki linatufundisha kuwa sala ni zaidi ya kuomba msaada kutoka kwa Mungu. Sala ni njia ya kuimarisha uhusiano wetu na Mungu. Kupitia sala, tunaweza kumjua Mungu vizuri zaidi na kupata ufahamu wa mapenzi yake. Sala inatuwezesha kusikiliza sauti ya Mungu na kufuata njia yake.

Kanisa Katoliki linatufundisha sala za kawaida kama vile Sala ya Bwana, Salamu Maria, na Tafakari ya Rozari. Sala hizi zinahimizwa kwa waumini ili kusali mara kwa mara na kuimarisha uhusiano wao na Mungu. Sala za kawaida pia zinafaa kama njia ya kufundisha watoto wetu umuhimu wa sala na kujifunza Biblia.

Kwa ujumla, sala ni sehemu muhimu ya maisha ya Kikristo. Kanisa Katoliki linahubiri na kufundisha umuhimu wake kwa waumini wake. Kupitia sala, tunaweza kuwasiliana na Mungu, kusafisha roho zetu, na kuimarisha uhusiano wetu na Mungu. Kwa hivyo, tunahimizwa kusali mara kwa mara na kufuata mafundisho ya Kanisa Katoliki kuhusu sala. Kama Catechism ya Kanisa Katoliki inasema, “Sala ni moyo wa maisha ya kiroho; ni sehemu muhimu ya uhusiano wetu na Mungu” (CCC 2558).

Ni nini imani ya Kanisa Katoliki kuhusu sakramenti ya Ndoa?

Sakramenti ya Ndoa ni muhimu sana katika Kanisa Katoliki. Kwa mujibu wa imani ya Kanisa, ndoa ni sakramenti inayofungamanisha mume na mke kwa maisha yote. Kupitia sakramenti hii, wawili hao wanakuwa kitu kimoja mbele ya Mungu na Kanisa. Kwa hiyo, kuna taratibu nyingi na sheria zinazohusiana na sakramenti hii ambazo zinapaswa kufuatwa kwa umakini.

Kanisa Katoliki linazingatia ndoa kuwa ni muhimu sana katika kuleta upendo, umoja na amani katika familia. Kwa mujibu wa imani ya Kanisa, ndoa inapaswa kufungwa kwa upendo, heshima, uaminifu na uwazi. Mume na mke wanapaswa kuwa wawazi kuhusu mambo yote yanayohusiana na ndoa yao, na wanapaswa kuelewana kwa kila hali ili ndoa yao iwe na baraka za Mungu.

Kuna taratibu nyingi ambazo wanandoa wanapaswa kufuata kabla ya kufunga ndoa. Wanandoa wanapaswa kuhudhuria kikao cha maandalizi ya ndoa kinachoendeshwa na padri wao. Kikao hiki ni muhimu sana kwani kinawapa wanandoa mafunzo juu ya imani ya Kanisa kuhusu ndoa na jinsi ya kuishi kama mume na mke.

Kanisa Katoliki linaamini kwamba ndoa ni sakramenti inayofungamanisha mume na mke kwa maisha yote. Kwa hiyo, ndoa haiwezi kuvunjwa isipokuwa kwa sababu za kikatili kama vile ndoa ya kulazimishwa, ndoa iliyopigwa marufuku na Kanisa au ndoa iliyofungwa kinyume cha sheria za Kanisa. Kwa mujibu wa Katekisimu ya Kanisa Katoliki (CCC), ndoa ni ahadi ambayo imefungwa kwa upendo na inapaswa kudumu hadi kifo. (CCC, 1660)

Kanisa Katoliki linahimiza wanandoa kuishi kwa upendo na heshima kwa kila mmoja. Wanaume wanapaswa kumpenda na kumheshimu mke wao kama Kristo alivyompenda Kanisa lake. (Waefeso 5:25) Wanawake wanapaswa kuwatii waume zao kama vile Kanisa linavyomtii Kristo. (Waefeso 5:22) Kupitia upendo na heshima hizi, wanandoa wanaweza kuwa mfano bora wa maisha ya Kikristo kwa watoto wao na kwa watu wengine.

Kwa hiyo, ni muhimu sana kuheshimu ndoa na kuzingatia taratibu zote zinazohusiana na sakramenti hii. Ndoa ni baraka kubwa kutoka kwa Mungu, na ni jukumu letu kuitunza na kuilinda. Kwa kufuata mafundisho ya Kanisa Katoliki na kuishi kwa upendo na heshima, tunaweza kujenga ndoa yenye baraka za Mungu na yenye furaha katika maisha yetu.

Njia Bora ya Kuelewa Masomo ya Misa ya Dominika ya Jumapili

Njia Bora ya Kuelewa Masomo ya Misa ya Dominika ya Jumapili

Moyo wangu unajaa furaha na shangwe ninapokukaribisha katika mfululizo huu wa makala, ambao utakusaidia kuelewa masomo ya Misa ya Dominika ya Jumapili. Kupitia mfululizo huu, tutajifunza jinsi ya kuichukua Biblia yetu takatifu na kuitumia ili kupata ufahamu kamili wa Neno la Mungu lililotolewa katika masomo ya kila Jumapili.

Kwa kuwa wewe ni Mkristo Mkatoliki, tunaelewa kwamba Misa ya Dominika ni kitovu cha maisha yetu ya kiroho. Ni wakati tunapokutana na familia yetu ya kiroho katika hekalu la Bwana. Kwa hivyo, ni muhimu kuelewa na kufahamu kikamilifu masomo yanayosomwa katika Misa ya Dominika.

Hebu tuitumie Biblia yetu takatifu kuongoza safari hii ya kufahamu masomo ya Misa ya Dominika. Kuanzia na sala ya kufungua Misa hadi somo la Injili, kila sehemu ya liturujia ina ujumbe maalum ambao Mungu anataka kutuambia. Kwa njia hii, tutakuwa na ufahamu sahihi wa mahubiri na tutaweza kulifanya Neno la Mungu kuwa sehemu muhimu ya maisha yetu ya kila siku.

Kwa mfano, katika somo la kwanza la Misa ya Dominika ya Jumapili, tunaweza kuzingatia andiko kutoka kitabu cha Mwanzo. Katika andiko hili, tunaona jinsi Mungu alivyoumba ulimwengu na viumbe vyote vilivyomo. Tunaambiwa kwamba Mungu aliona kila kitu alichokiumba kuwa kizuri na kwa hivyo, tunahimizwa kumshukuru kwa ajili ya uumbaji wake.

Biblia inasema katika Mwanzo 1:31, "Mungu akaona kila kitu alichokifanya, na tazama, ilikuwa ni njema sana." Kwa kutumia aya hii, tunaweza kujihamasisha kila siku kuwa walinzi wa uumbaji wa Mungu na kuenzi na kutunza kazi ya mikono yake.

Somo la pili la Misa ya Dominika linajumuisha barua kutoka kwa Mitume au vifungu vingine vya Maandiko Matakatifu. Kwa mfano, andiko kutoka katika barua ya Mtume Paulo inaweza kutuonyesha jinsi tunavyopaswa kuishi kama Wakristo. Tunaweza kuichukua aya moja kwa mfano, kama vile Warumi 12:2, ambapo tunahimizwa "Msiifuatishe namna ya dunia hii; bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu."

Kwa kutumia aya hii, tunahimizwa kuacha kuiga tabia na mienendo ya ulimwengu huu, badala yake, sisi tunapaswa kuishi kulingana na mapenzi ya Mungu na kubadilika kuwa watu wapya. Ikiwa tutafuata mafundisho haya, tutakuwa chumvi na mwanga wa ulimwengu kama Wakristo. Tunaweza kufurahia maisha yetu kwa kuzingatia neno la Mungu katika masomo ya Misa ya Dominika.

Katika somo la Injili, tunapata nafasi ya kusikiliza maneno ya Yesu Kristo mwenyewe. Tunajifunza kutoka kwake jinsi tunavyopaswa kuishi kama wafuasi wake. Injili ni sehemu muhimu ya Misa ya Dominika, kwani inawasilisha mafundisho ya Yesu kwa njia ya moja kwa moja.

Kwa mfano, tunaweza kuitumia aya kutoka Injili ya Mathayo 5:14-16, ambapo Yesu anasema, "Ninyi ni nuru ya ulimwengu. Mji hauwezi kusitirika ukiwa juu ya mlima. Wala watu hawaiwashi taa na kuiweka chini ya pishi, bali juu ya kinara cha taa, iangaze wote walio katika nyumba. Vivyo hivyo na nuru yenu iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni."

Kwa kutumia aya hii, tunaelewa kwamba tunapaswa kuwa vyombo vya nuru na matumaini katika dunia hii yenye giza. Tunapaswa kuishi kwa njia ambayo injili itaonekana kupitia matendo yetu mema. Kwa kufanya hivyo, tutakuwa mashahidi wazuri wa imani yetu kwa wengine.

Kwa hivyo, wapendwa, tuchukue fursa hii ya kusoma na kufahamu masomo ya Misa ya Dominika kwa njia bora. Tutumie muda wetu kusoma na kutafakari Neno la Mungu, na kuweka mafundisho yake katika vitendo katika maisha yetu ya kila siku. Kwa kufanya hivyo, tutakuwa tayari kushirikiana kikamilifu na familia yetu ya kiroho katika Misa ya Dominika, tukiwa na moyo wa shukrani na furaha.

Basi, na tuwe watu wa sala na tafakari, tukizingatia Neno la Mungu na tukiishi kulingana na mafundisho yake. Tufuate mwongozo wa Roho Mtakatifu katika kuelewa masomo ya Misa ya Dominika kwa undani zaidi. Na katika kufanya hivyo, tutakuwa tunafanya Misa ya Dominika kuwa chanzo cha baraka na furaha katika maisha yetu ya kiroho. Asante Mungu kwa neno lako takatifu na neema yako isiyo na kikomo!

Nafasi ya Bikira Maria Katika Kanisa Katoliki

Kanisa katoliki linamthamini Bikira Maria kama Mama wa Mungu, Mama wa Kristu, Mama wa Mkombozi pia Mama wa uhai kuna maneno kadhaa hutumika pia kufafanua zaidi hiyo heshima mfano HYPERDULIA zaidi ya…. Bikira Maria tunamheshimu zaidi ya watakatifu, PROTODULIA ikiwa na maana ya heshima kwa Bikira Maria zaidi ya Mt. Yoseph na pia LATRIA likiwa na maana ya heshima kwa Mungu peke yake kwani ndani yake kuna kunakuabudu pia!!!
🌻Bikira Maria anatuelekeza kwa mwanae kama alivyo waelekeza waliokuwa harusini kana lolote atakalo waambieni fanyeni Yoh.2:5
🌻Bikira Maria ni Mama wa uhai, mlei, muuguzi wa kwanza/ muhudumu wa kwanza alienda kwa haraka kuanzisha kliniki ndogo nyumbani mwa Zakaria amhudumie Elizabeti Mama wa Yohane Mbatizaji aliyekuwa mjamzito
🌻Tunasema Bikira Maria ni mzazi bora wa kuiga kwani alitetea uhai, Mama huyo hakutoa mimba japo misuko suko ilikuwa mingi Mfano maneno ya pembeni ya watu kwa vile mimba haikuwa ya Yoseph mumewe, hali mbaya ya uchumi na ukiangalia hivyo Familia takatifu ya Maria na Yosefu haikuwa na hali nzuri kifedha Lk. 2:22-24 Bikira Maria alivumilia hali hiyo kwani angetoa angemuua Mkombozi wetu, na sababu hizo ndizo hata dunia ya leo zina wafanya watu watoe mimba Ikiwa kutoa ni kuua na hatimaye tunapoteza
-Mama wa watoto wa kesho
-Baba wa watoto wa kesho
-Padre wa kesho
-Mtawa wa kesho
-Raisi wa kesho n.k
🌻Bikira Maria alikombolewa kwaajili ya mastahili ya mwanae tena kwa namna ya pekee sana, aliangaliwa na…..
-Baba kama Binti yake Mpenzi
-Mwana, mama mheshimiwa
-Roho Mtakatifu, hekalu lake
SWALI: Sisi nasi kama tunaamini heshima anayopaswa kupewa Bikira Maria ni sawa na kwamba pia sisi tunaelewa kwamba tumekombolewa kupitia yeye?
Nafasi ya Bikira Maria Katika Biblia ya kanisa katoliki
🌻Sisi kama wanakatoliki tunasema Bikira Maria ni Mama wa Mungu kweli kwa kzingatia mambo makuu mawili ambayo ni kama ifuatavyo:
1. Kwanza lazima Bikira Maria awe mama halisi wa Yesu
2. Pili ni kuwa Yesu aliyemzaa Ni Mungu.
1. BIKIRA MARIA NI MAMA HALISI WA YESU
🌻Sote tunapaswa kufahamu kama kweli BiKira Maria ni Mama halisi wa Yesu kupitia vifungu vifuatavyo na hii ndio nguzo pekee ya kujinasua katika makundi yasiyo amini kama Bikira Maria anastahili heshima twende pamoja sasa:
-Lk. 1:30-31 neno linasema
Malaika akamwambia ‘ usiogope Mariamu, kwa maana umepata neema kwa Mungu, tazama utachukua mimba na kuzaa mtoto mwanamume na jina lake utamwita Yesu kwahiyo ni dhahiri kwamba huyu ni mama halisi wa Yesu ambae sisi tunamuimba kila leo.
-Mt. 1:18 neno linasema:
kuzaliwa kwake Yesu Kristu kulikuwa hivi: Mariamu mama yake alipokuwa ameposwa na Yusufu, kabla hawajakaribiana, alionekana ana mimba kwa uweza wa Roho Mtakatifu huu ni ushahidi tosha kuwa Bikira Maria ni Mama halisi wa Yesu kwani ndiye aliye pewa hadhi zaidi ya wanawake wote kuzaa kitakatifu Mwana wa Mungu.
-Rom 1:3 neno linasema hivi
yaani habari za mwanawe, aliye zaliwa katika ukoo wa Daudi kwa jinsi ya mwili ikikumbuka wakati tunasali nasadiki kama sehemu ya kuikiri imani yetu kuna maneno huwa tunatamka kwamba akapata mwili kwa uwezo wa Roho Mtakatifu kwake yeye Bikira Maria, akawa mwanadamu hivyo ni connection nzurii sana kwetu kuendelea kumheshimu Mama yetu Maria kwa kutuunganisha na Mungu kwa ubinadamu wetu!
-Nabii Isaya 7: 14 anatabili:
kwahiyo Bwana mwenyewe atawapa ishara, tazama , Bikira atachukua mimba , atazaa mtoto mwanamume naye atamwita jina lake Imanueli(yaani Mungu pamoja nasi tazama maneno haya yalitabiliwa na Nabii huyu juu ya mama huyu Mtakatifu atakavyo tuletea ukombozi kwann tusimheshimu na kumtetea mpaka tunapotoshwa?
– Mate 1:14 neno linasema
hawa wote walikuwa wakidumu kwa Moyo mmoja katika kusali, pamoja nao wanawake na mariamu mama yake Yesu na ndugu zake wanawake wengine walihesabiwa pamoja lakini mama Maria anasemwa kwa upeke yake ktokana na uzito wake kupita wanawake wengine kwani ndiye mama wa Yesu Kristu ni heshima kubwa!!!
2. Yesu ni Mungu na Bikira Maria ni Mama wa Mungu
🌻katika sehemu ya jambo letu la pili ni kwamba je alichozaa Mama Maria ni Mungu? Kama ni muhimu kujua hilo hebu tuone uthibitisho wa hili kupitia baadhi ya vifungo bdani ya Biblia zetu ambazo pia wenzetu wanaopinga Habari ya mama yetu Maria waone twende pamoja:
-Yoh. 1:1-2 neno linasema
hapo mwanzo kulikuwako Neno naye Neno alikuwako kwa Mungu naye Neno alikuwa Mungu Huyo Mwanzo alikuwako kwa Mungu kwa maneno hayo na ukiendelea kusoma ukitafakari utaona anaezungumziwa na Yesu Kristu ambaye ndie nuru halisi ya ulimwengu ni ndie uzima wetu kwa Mungu na huyu Yesu basi alizaliwa na Bikira Maria hivyo alichozaa Maria ni Mungu kweli.
-Rom 9:6 neno linasema:
ambao mababu ni wao, na katika hao alitoka Kristo kwa jinsi ya Mwili, ndiye aliye juu ya mambo yote, Mungu mwenye kuhimidiwa milele. Amina hayo ni maneno yanayo tambulisha koo ya kibinadamu kwamba ndiko pamoja ubinadamu wetu amezaliwa Mungu soma injili ya mtakatifu Mathayo sura ya kwanza aya ya kwanza na kuendelea habari za ukoo wa Yesu naamini hapa Tmcs tunapasikia sana!!!
– Fil 1:6-7 neno linasema:
nami niliaminilo ndilo hili, ya kwamba yeye aliyeanza kazi njema mioyoni mwenu ataimaliza hata siku ya Kristo Yesu nakuendelea……….. maneno hayo yanaonyesha kuwa Kristo ndie mambo yote katika kuupata uzima wa milele na huyu anae onekana ni mwisho wa yote amaezaliwa na Mwanamke Maria.
-Mitume nao walikiri kuwa Yesu ni Mungu mtu Yoh. 20:28
Tomaso akajibu, akamwambia Bwana wangu na Mungu wangu kutokana na matendo na kazi ya Yesu Kristu iliwafanya mitume waone kuwa ufalme wake sio wa dunia hii tu bali ni wa milele na kazi yake ni Takatifu na sio hapo tu kumbuka pia wale wanafunzi walio kuwa wanasema yatufaa sasa tujenge vibanda vitatu kimoja cha Musa na kingine cha Eliya mara sauti ikasikika ikisema huyu ni mwanangu mpendwa wangu msikieni yeye na mara akageuka sura maneno hayo ilikuwa ni uthibitisho juu ya umungu wa Yesu Kristu ambaye huyu alizaliwa na Bikira Maria.
– Lk. 1:35 neno linasema
Malaika akajibu akamwambia “Roho Mtakatifu atakujilia juu yako , na nguvu zake aliyejuu zitakufunika kama kivuli, kwasababu hiyo hicho kitakachozaliwa kitaitwa kitakatifu mwana wa Mungu” haya maneno ni dhahiri yanatufundisha kwamba Bikira Maria alimzaa Mungu katika ubinadamu wake.
-Gal. 4:4 neno linasema:
huyu ni mwana wa Mungu, ni mwana wa mwanamke, huyo mwana wa Mungu, pia ni mwana wa Maria tuseme nn sasa tusiyumbishwe yumbishwe na maneno yasiyo na tija juu ya mama Maria kwani kupitia yeye tunakuwa salama katika Roho na Mwili
Maneno ya Busara
-Mt. Germanus alishwahi kusema *Maria mahali pa kuishi pa Mungu*
-Mt. Jerome alisema Maria Hekalu la mwili wa Bwna
-Martine Luther, hata baada ya kujiengua kutoka kanisa katoliki alikiri kuwa Bikira maria ni Mama wa Mungu akisema:
hakuna jambo kubwa zaidi ya hili kuwa Bikira Maria alipata kuwa Mama wa Mungu ambalo kwalo zinatoka zawadi(heri) kubwa na Nyingi ambazo amepewa inakuaje leo tusione umhimu wa heshima kwa mama huyu?
-Mt. Bernado alisema Maria alimpendeza Mungu kwa ubikira wake, na alichukua mimba kwa unyenyekevu wake
MWISHO: FUNDISHO MAISHANI
– Sote ambao tupo chini ya utawala wa Yesu Kristo tunawajibu wa kutetea uhai kwa nguvu zote tukipiga marufuku utoaji mimba kwa visingizio mbalimbali
– Eva alishindwa kumtii Mungu akaleta mauti lakini Bikira Maria alitii kubaki mwamnifu na kumtunza Kristu na hatimaye ameleta uhai na neema zote , akina dada na mama zetu igeni mfano wa Maria na Elizabeti katika malezi bora!!
-Sisi sote tuliowabatizwa tunapapaswa kuwa wanyenyekevu kama Maria na familia yao yote kwani unyenyekevu umejengwa juu ya upendo pia ni mama wa fadhila nyingi utii, uchaji, ibada, uvumilivu, kiasi, upole na amani.

Je, Bikira Maria ni Bikira Daima au alizaa watoto wengine?

Jibu fupi ni kwamba Bikira Maria hakuzaa watoto wengine na hakuwa na watoto wengine zaidi ya Yesu
Hapo zamani hakuna mkristu au dehebu lolote lililokuwa linapinga kuwa Bikira Maria sio Bikira Daima hata Waprotestanti/walokole waliamini Bikira Maria ni Bikira Hata Baada ya Kumzaa Yesu. Kwenye Miaka ya 1400-1600 Watu wote wakwanza waliopinga Kanisa Katoliki walikubali kuwa Bikira Maria ni Bikira daima wakiwemo Martin Lutha aliyeanzisha kanisa la Lutheran, John Calvin aliyeanzisha Ulokole/Protestanti, Mchungaji Ulrich Zwingli, Heinrich Bullinger, and Thomas Cranmer. Kwa miaka zaidi ya 350 Waprotestant/walokole waliendelea kuamini kuwa Bikira Maria ni Bikira Daima.
Lakini baadae wakristo wengi walianza kupinga kuwa Bikira Maria ni Bikira Daima.

Tunaweza kuthibitisha kuwa Bikira Maria hakuzaa watoto wengine kwa kunukuu Biblia Kama ifuatavyo;

1. Bikira Maria Alikuwa Bikira Kabla ya kumzaa Yesu

Biblia inatuambia wazi kwamba Bikira Maria alikuwa Bikira Kabla ya kumzaa Yesu Kama tunavyosoma katika Luka 1:26-35
26 Mnamo mwezi wa sita, malaika Gabrieli alitumwa na Mungu aende kwenye mji uitwao Nazareti huko Galilaya, 27 kwa msichana mmoja aitwaye Maria, mchumba wa mtu mmoja jina lake Yosefu, wa ukoo wa Daudi. 28 Malaika akamwendea, akamwambia, “Salamu Maria! Umejaliwa neema nyingi! Bwana yu pamoja nawe.” 29 Maria aliposikia maneno hayo alifadhaika sana, akawaza: maneno haya yanamaanisha nini? 30 Malaika akamwambia, “Usiogope Maria, kwa maana Mungu amekujalia neema. 31 Utachukua mimba, utamzaa mtoto wa kiume na utampa jina Yesu. 32 Yeye atakuwa mkuu na ataitwa Mwana wa Mungu Mkuu. Bwana Mungu atampa kiti cha mfalme Daudi, babu yake. 33 Kwa hivyo atautawala ukoo wa Yakobo milele, na ufalme wake hautakuwa na mwisho.” 34 Maria akamjibu, “Yatawezekanaje hayo, hali mimi ni bikira?” 35 Malaika akamjibu, “Roho Mtakatifu atakushukia, na uwezo wake Mungu Mkuu utakujia kama kivuli; kwa sababu hiyo, mtoto atakayezaliwa ataitwa Mtakatifu, Mwana wa Mungu. (Luka 1:26-35)

2. Biblia Haiwataji ndugu wa Yesu wakati Yosefu na Maria walipokimbilia Misri kumficha Yesu na wakati waliporudi

19 Baada ya kifo cha Herode, malaika wa Bwana alimtokea Yosefu katika ndoto kule Misri, 20 akamwambia, “Amka! Mchukue mtoto pamoja na mama yake, urudi tena katika nchi ya Israeli, maana wale waliotaka kumwua mtoto huyo wamekwisha kufa.” 21 Basi, Yosefu aliamka, akamchukua mtoto pamoja na mama yake, akarejea katika nchi ya Israeli. 22 Lakini Yosefu aliposikia kwamba Arkelao mwanawe Herode alikuwa mfalme wa Yudea mahali pa baba yake, aliogopa kwenda huko. Naye baada ya kuonywa katika ndoto, alikwenda katika mkoa wa Galilaya, 23 akahamia katika mji uitwao Nazareti. Ndivyo yalivyotimia maneno yaliyonenwa kwa njia ya manabii: “Ataitwa Mnazare.” Matayo 2:19-23
Kama wangekuwepo wadogo zake Yesu Biblia ingetuambia kwamba walikuwa wapi wakati huo na walikuwa na Yesu au la.

3. Biblia haituambii kuwa Yesu alikua na wadogo zake alipokuwa na miaka 12

Wakati wa Maria, Yoseph na Yesu walipoenda Yerusalemu Yesu akiwa na miaka 12 Biblia haituambii kuwa Yesu alikuwa na wadogo zake na walikuwa wapi. Kumbuka walikuwa na Desturi ya kwenda Yerusalemu kila mwaka kwa ajili ya Pasaka familia nzima kama familia. Je hao watoto wengine walikuwa wapi. Kwa nini walikuwa na Yesu Mwenyewe? Maana yake ni kwamba Yesu hakuwa na Wadogo zake.
41 Wazazi wa Yesu walikuwa na desturi ya kwenda Yerusalemu kila mwaka wakati wa sikukuu ya Pasaka. 42 Mtoto alipokuwa na umri wa miaka kumi na miwili, wote walikwenda kwenye sikukuu hiyo kama ilivyokuwa desturi. 43 Baada ya sikukuu, walianza safari ya kurudi makwao, lakini Yesu alibaki Yerusalemu bila wazazi wake kuwa na habari. 44 Walidhani alikuwa pamoja na kundi la wasafiri, wakaenda mwendo wa kutwa, halafu wakaanza kumtafuta miongoni mwa jamaa na marafiki. 45 Kwa kuwa hawakumwona, walirudi Yerusalemu wakimtafuta. 46 Siku ya tatu walimkuta Hekaluni kati ya walimu, akiwasikiliza na kuwauliza maswali. 47 Wote waliosikia maneno yake walistaajabia akili yake na majibu yake ya hekima. 48 Wazazi wake walipomwona walishangaa. Maria, mama yake, akamwuliza, “Mwanangu, kwa nini umetutenda hivyo? Baba yako na mimi tumekuwa tukikutafuta kwa huzuni.” 49 Yeye akawajibu, “Kwa nini mlinitafuta? Hamkujua kwamba inanipasa kuwa katika nyumba ya Baba yangu?” 50 Lakini wazazi wake hawakuelewa maana ya maneno aliyowaambia. 51 Basi, akarudi pamoja nao hadi Nazareti, akawa anawatii. Mama yake akaweka mambo hayo yote moyoni mwake. 52 Naye Yesu akaendelea kukua katika hekima na kimo; akazidi kupendwa na Mungu na watu. (Luka 2:41-52).
Kwa hiyo Biblia haionyeshi kuwa Yesu alikuwa na kaka na dada wakati akiwa na miaka 12. Kama wangekuwepo wangetajwa hapa kuwa walikuwa pamoja na Wazazi wao kama Yesu au walikuwa na Yesu wakati anapotea. Biblia haituambii chochote kwa hiyo wakati huo hapakuwa na wadogo zake Yesu.

4. Kukosekana kwa neneo “Binamu” kwenye lugha ya Yesu

Wakristu wa kwanza pamoja na Yesu aliongea Kiaramaiki au Kiebrania. Katika lugha zote hizo hakuna neno “Binamu” kwa hiyo mabinamu walijulikana kama dada na kaka wa mtu. Kwenye Agano jipya Neno kaka na Dada lilitumika pia kuwakilisha binamu.
Biblia inapotuambia kuwa Kaka na dada zake Yesu haimaanishi kaka wa kuzaliwa bali ndugu au Binamu
55 Je, huyu si yule mwana wa seremala? Je, mama yake si anaitwa Maria, na ndugu zake si kina Yakobo, Yosefu, Simoni na Yuda? 56 Na dada zake je, si wote wako hapa pamoja nasi? Basi amepata wapi haya yote?” (Mathayo 13:55-56)
Kwa hiyo wanaotajwa hapa ni ndugu wa Yesu kwa maana maneno kama; ndugu, kaka au dada lilitumika badala ya Binamu yaani mtoto wa shangazi au mjomba. Hapa juu Yosefu ametajwa kama kaka yake Yesu lakini tunajua kuwa Yosefu ni Baba yake Yesu. Baba na mwana hawawezi kuwa na jina sawa.

5. Biblia haitumii neno Ndugu, kaka au dada ikimaanisha ndugu wa kuzaliwa mama mmoja na baba mmoja

Sio mara zote Biblia imetumia neno Ndugu kumaanisha ndugu (Dada na Kaka) wa kuzaliwa yaani kaka na dada kwa mfano
Kwa kuangalia lugha ya Kiswahili na Kiingereza 1 Wakorintho 15:6 tunaona tafsiri tofauti.
KISWAHILI 6 Kisha aliwatokea ndugu zaidi ya mia tano kwa mara moja; wengi wao wanaishi bado, lakini baadhi yao wamekwisha kufa.
ENGLISH 6 After that, he appeared to more than five hundred of the brothers and sisters at the same time, most of whom are still living, though some have fallen asleep.
Kwa hiyo hapa neno kaka dada na ndugu linaonekana wazi halikumaanisha ndugu au kaka wa damu.

6. Undugu wa Yakobo, Simoni, Yosefu na Yuda kwa Yesu Sio wa mtu na kaka zake

Wasemao kuwa Bikira maria alikuwa na wana zaidi ya Yesu wananukuu kifungu hiki;
55 Je, huyu si yule mwana wa seremala? Je, mama yake si anaitwa Maria, na ndugu zake si kina Yakobo, Yosefu, Simoni na Yuda? 56 Na dada zake je, si wote wako hapa pamoja nasi? Basi amepata wapi haya yote?” (Mathayo 13:55-56)
Kumbuka kulikuwa na Yakobo wawili wakati wa Yesu, Vifungu vifuatavyo yunaweza kuona kuwa kulikuwa na yakobo wawili ambao walikuwa ndugu za Yesu lakini sio kaka wa kuzaliwa kwa mama.
35 Yakobo na Yohane, wana wa Zebedayo, walimwendea Yesu wakamwambia, “Mwalimu, tunataka utufanyie kitu tutakachokuomba.” (Marko 10:35)
55 Mahali hapo walikuwapo wanawake wengi wakitazama kwa mbali. Hao ndio wale waliomfuata Yesu kutoka Galilaya wakimtumikia. 56 Miongoni mwao walikuwa Maria Magdalene, Maria mama yao Yakobo na Yosefu, pamoja na mama yao wana wa Zebedayo. (Matayo 27:55-56)
Tunaweza kuona Undugu huu na Yesu kwa kusoma;
19 Lakini sikuwaona mitume wengine isipokuwa Yakobo, ndugu yake Bwana. (Wagalatia 1:19)
Lakini Yuda anasema;
1 Mimi Yuda, mtumishi wa Yesu Kristo, ndugu yake Yakobo, nawaandikia ninyi mlioitwa na Mungu na ambao mnaishi katika upendo wa Mungu Baba, na katika ulinzi wa Yesu Kristo. (Yuda 1:1)
Kwa hiyo Yakobo na Yohane walikuwa watoto wa Mama mwingine ambao baba yao ni Zebedayo. Na Yakobo na Yosefu walikuwa watoto wa Maria Mwingine. Kwa hiyo ni Yakobo wa wili wa Mama wengine Tofauti na Maria. Yuda alikuwa ni ndugu yake Yakobo. Yakobo vilevile alikuwa ndugu yake Yesu.
Kuthibitisha kuwa Hawa kina Mama ndio waliokuwa Mama zao kina Yakobo wote hao wawili na wengine tunaweza kusoma;
25 Karibu na msalaba wake Yesu walikuwa wamesimama mama yake, na dada ya mama yake, Maria mke wa Kleopa, na Maria Magdalene. (Yohana 19:25)
Kwa hiyo kwenye (Yohana 19:25) tunaona Kuwa ni kwenye Msalaba wa Yesu alikuwepo Mama yake Yesu (Bikira Maria), Dada yake Bikira Maria, Mke wa Cleopa na Maria Magdalena. Na kwenye (Matayo 27:55-56) wamwtajwa ni Mama za kina nani kama inavyoonekana kwenye kifungu kifuatachi;.
55 Mahali hapo walikuwapo wanawake wengi wakitazama kwa mbali. Hao ndio wale waliomfuata Yesu kutoka Galilaya wakimtumikia. 56 Miongoni mwao walikuwa Maria Magdalene, Maria mama yao Yakobo na Yosefu, pamoja na mama yao wana wa Zebedayo. (Matayo 27:55-56).
Kwa hiyo hii ina maanisha kulikua na wanawake watatu wenye majina sawa ya Maria waliokuwa chini ya Msalaba. Yakobo na Yuda walikuwa watoto wa Maria Mke wa Cleofasi, na sio Mama wa Yesu, na hivyo sio kaka za Yesu.

7. Yesu alimwacha Mama yake kwa Yohane kwa kuwa hakuwa na Kaka na dada wakumwachia mamaye

26 Yesu alipomwona mama yake, na karibu naye amesimama yule mwanafunzi aliyempenda, akamwambia mama yake: “Mama! Tazama, huyo ndiye mwanao.” 27 Halafu akamwambia yule mwanafunzi: “Tazama, huyo ndiye mama yako.” Na tangu saa ile huyo mwanafunzi alimchukua akae nyumbani kwake.
Ndiyo maana Bikira Maria tangu siku ile alihamia kwa Yohani kwa kuwa hakuwa na watoto wengine.

Siri ya kamba nyekundu

Miaka zaidi ya 3000 iliyopita katika mji wa Yeriko alikuwepo mwanamke mmoja kahaba, jina lake Rahabu. Huyu mwanamke aliwaokoa wapelelezi wa Israel waliotumwa kwenda kufanya uchunguzi ktk nchi yao.

Wakati wana wa Israel wanatoka Misri kuelekea nchi ya Kaanani, Mungu aliwaahidi kuwapa mji wa Yeriko. Kwahiyo walipofika ng’ambo ya mto Yordani, Yoshua akatuma wapelezi wawili kwenda kuipeleleza Yeriko kabla wana wa Israel kuivamia na kuitwaa. Wale wapelelezi walipofika mji wa Yeriko mfalme akapelekewa taarifa kuwa kuna watu wawili wameingia kuipeleleza nchi.

Kwahiyo mfalme akaagiza wakamatwe na wauawe. Wale wapelelezi wakaingia ktk nyumba ya mwanamke kahaba aitwaye Rahabu akawaficha darini. Akawafunika kwa mabua ya kitani. Wale askari walipofika na kumuuliza Rahabu kwamba wako wapi waisrael wawili walioingia humu ndani, Rahabu akajibu kuwa wameondoka.

Akasema ni kweli waliingia ktk nyumba yangu lakini walitoka kabla lango la mji halijafungwa. Akawaambia wafuateni haraka kabla hawajafika mbali. Wale askari wakatoka kuwafuata wale wapelelezi hadi katika vilima vya nje ya mji lakini wasiwaone. Ilipofika usiku Rahabu akawashusha darini wale wapelelezi na kuwaelekeza namna ya kutoroka mji wa Yeriko. Akawaelekeza wapite njia nyingine tofauti na ile waliyoiendea wale askari. Akawashusha kupitia dirishani ili watu wa mji ule wasiwaone.

Kwa ukarimu aliowatendea wale wapelelezi wakaweka agano nae kwamba siku wana wa Israel wakija kuiangamiza Yeriko, BWANA ataiponya nyumba ya Rahabu na ndugu zake wote. Ili kutimiza agano hilo wale wapelezi wakamwambia Rahabu weka kamba nyekundu katika dirisha lako kama alama, ili jeshi la Israel liltakapouteketeza mji nyumba yako isiangamizwe.

Yoshua 2:17 &18 “Wale wapelelezi wakamwambia Rahabu, Sisi tunataka tusiwe na hatia kwa ajili ya kiapo hiki ulichotuapisha. Angalia, tutakapoingia katika nchi hii, funga kamba hii nyekundu katika dirisha hili ulilotuteremshia; nawe uwakusanye nyumbani mwako, baba yako, mama yako, na ndugu zako, na watu wote wa nyumba ya baba yako.”

Rahabu akafanya hivyo, na siku Jeshi la Israel lilipovamia Mji wa Yeriko ili kuuteketeza, Rahabu na ndugu zake walipona.

Yoshua 6:23 &24 “Basi wale vijana wapelelezi wakaingia, wakamtoa Rahabu, na baba yake, na mama yake, na ndugu zake, na vitu vyote walivyokuwa navyo, wakawatoa na jamaa zake wote pia; wakawaweka nje ya matuo ya Israeli. Kisha wakauteketeza mji kwa moto, na vitu vyote vilivyokuwa ndani yake…”

MORAL OF THE STORY.!
Habari hii ina mengi ya kutufundisha lakini leo nataka nikufundishe kuhusiana na siri ya kamba nyekundu ambayo Rahabu aliiweka katika dirisha lake na jinsi ilivyomuokoa.

Rahabu hakua mtakatifu, hakuwa mteule wa Mungu wala hakuwa kizazi cha Israel. Alikua mwanamke wa mataifa, tena kahaba. Hakuwa mwema sana machoni pa Mungu. Lakini aliokoka kwa sababu ya “kamba nyekundu” dirishani mwake. Pengine wapo maaskofu, wachungaji, mitume au manabii walioangamizwa, lakini kahaba Rahabu akaokolewa yeye na ndugu zake licha ya kwamba alikua kahaba. Siri ni “kamba nyekundu” dirishani mwake.

Jiulize je wewe unayo kamba nyekundu? Kuna watu katika maisha wanaonekana wenye dhambi, wachafu, dhaifu au wasiofaa, lakini Mungu huwanyanyua na kuwabariki na kuwaacha wale tunaodhani ni watakatifu au wenye haki. Mungu anaangalia “kamba nyekundu”. Unaweza kuwa mtakatifu lakini huna “kamba nyekundu” itakayomfanya Mungu akurehemu.

Unaweza kuwa umemaliza masomo yako na umefaulu vizuri, lakini kila unapoomba kazi huitwi hata kwenye usaili, na ukiitwa hupati kazi, miaka inazidi kwenda. Unaamua kwenda kwenye maombi. Kila siku unafanya maombi lakini bado hufanikiwi. Unajiuliza tatizo liko wapi. Unaji-asses na kuona hakuna tatizo mahali. Kumbe huna “kamba nyekundu”

Au unaweza kuwa una biashara yako lakini haifanikiwi. Hupati wateja. Umehitahidi kwa kila hali lakini bado huoni faida. Unadhani tatizo labda Mungu amekuacha. Unaamua kuwa mtu wa maombi. Unazunguka makanisa mbalimbali kuonbewa lakini bado haufanikiwi. Kumbe huna “kamba nyekundu”.

“Kamba nyekundu” imekuwa siri ya mafanikio ya watu wengi bila kujalisha mahusiano yao kiroho na Mungu. Bila kujalisha kama ni wakristo au si wakristo. Kamba nyekundu imewasaidia hata wenye dhambi kubarikiwa. Rahabu alikua kahaba lakini yeye na ndugu zake waliokolewa kwa sababu ya “kamba nyekundu”.

Je kamba nyekundu ni nini? Kamba nyekundu ni mfumo wako wa maisha; jinsi unavyoishi na unayowatendea watu wengine, hasa “wateule” wa Mungu.

Kuna wakati Mungu huamua kukubariki si kwa sababu wewe ni mwema sana, bali kwa sababu kuna watu wema wanaoomba kwa ajili yako. Inawezekana tangu uanze kuomba, maombi yako hayajawahi kufika kwa Mungu lakini unabarikiwa, kwa sababu ya kamba nyekundu.

Kuna watu ambao ni “wateule” wa Mungu, kwahiyo kadri unavyowatendea mema hao watu baraka zinakuja kwako “automatically” hata kama wewe si mkristo. Rahabu aliwatendendea mema wapelelezi wa Israel baraka zikaenda kwake “automatically” bila kujalisha kwamba alikua kahaba.

Yatima, wajane, maskini, wazee, wagonjwa na wengine wenye uhitaji ni wateule wa Mungu. Kwahiyo ukiwatendea mema watu hawa baraka zinakuja kwako hata kama wewe ni mwenye dhambi.

Kwa mfano kama kuna watoto yatima unawasomesha, au kuna wajane unawasaidia mahitaji yao, au wagonjwa unawasaidia matibabu, si rahisi Mungu kuondoa mkono wake wa baraka kwako hata kama wewe ni mwenye dhambi. Mungu akiondoa baraka kwako watu wake watateseka.

Wale yatima, wajane, wagonjwa ambao wewe ni msaada kwao kila wakiomba Mungu huongeza baraka kwako ili uzidi kuwahudumia. Inawezekana maombi yako hayafikagi kwa Mungu lakini unabarikiwa kwa sababu ya maombi ya hao unawaosaidia.

Kuna wakati Mungu anaweza kuamua kuzipiga dhoruba biashara za wenzako, lakini ya kwako ikasimama imara. Si kwa sababu wewe ni mwema sana, bali kwa sababu kuna watu wanamlilia Mungu kwa ajili yako. Kuna wanategemea ada za shule kwenye hiyo biashara yako. Kuna watu wanategemea pesa za matibabu kwenye biashara yako. Kwa hiyo Mungu akiyumbisha biashara yako atakua anawaumiza watu hao. So ili asiwaumize anaamua kukuaacha. Hiyo ni kamba nyekundu.!

Kuna wakati wenzio wakifanya makosa madogo kazini wanafukuzwa kazi, lakini unajishangaa wewe umefanya makosa makubwa na hufukuzwi. Si kwa sababu una bahati sana. Ni kamba nyekundu. Kuna watu walioko nyuma yako ambao ni wateule wa Mungu. Kuna yatima wanategemea kulipiwa ada kwa mshahara wako, kuna wagonjwa wanategemea kusaidiwa hela za matibabu kwenye mshahara wako, kuna wajane wanategemea hela ya kuishi kutoka kwako. Kwahiyo Mungu akikuadhibu anakua amewaadhibu na wao. Kwahiyo ili wapone inabidi akulinde hata kama umefanya kosa kazini. Unashangaa tu kesi imeisha hata kwa namna ambayo hujui. Hiyo ni kamba nyekundu.!

Kuna mtu ambaye ni maskini wa kutupwa hana hata uwezo wa kununua sukari. Lakini anamuomba Mungu kwa imani kuwa ampe sukari aweze kunywa chai kila siku. Kwa kuwa huyo maskini huwa anapata sukari kutoka kwako, Mungu atazidi kukubariki ili uendelee kumhudumia huyo maskini. Hiyo ni Kamba nyekundu.!

Kamba nyekundu ilimuokoa Rahabu na ndugu zake licha ya kwamba alikua kahaba. Jiulize wewe una kamba nyekundu? Je kuna watu wako nyuma yako ambao Mungu akiwaangalia anakubariki, anakuokoa hata kama upo kwenye hatari?

Kama unamsomesha mwanao shule ya “mamilioni” kwa mwaka wakati mtoto wa jirani yako hana hata uniform za kuendea shule, au unatumia “mamilioni” kwa pombe na starehe wakati kuna wagonjwa wanaokufa kwa kukosa panadol, siku Mungu akitaka kukuadhibu hajiulizi mara mbili maana huna “kamba nyekundu” nyuma yako.

Lakini yule anayesaidia wenye uhitaji, kama yatima, wagonjwa, wazee, wajane,walemavu, au maskini atazidi kubarikiwa tu hata kama ni mwenye dhambi, maana anayo kamba nyekundu.

Hii ni kwa sababu Mungu akitaka kumuadhibu, kabla hajamtizama yeye anatizama kwanza yatima walioko nyuma yake anaowasaidia, anatizama wagonjwa wanaomtegemea kwa matibabu, anatizama wajane. Anaona akimuadhibu, atakuwa ameadhibu na hao wanaomtegemea. Kwa hiyo anaamua kumuacha.

Hii ina maana kuwa baraka na utakatifu ni vitu viwili tofauti. Unaweza usiwe mtakatifu lakini Mungu akakubariki na akakulinda. Unaweza kubarikiwa si kwa sababu unastahili, bali kwa sababu kuna “wanaostahili” wapo nyuma yako wakikupigania kwa baba yao (Yehova). Ndio maana kuna watu wengi wasio Wakristo wanabarikiwa kila siku hata kama hawamjui Mungu. Ni kwa sababu wana “kamba nyekundu”.

Malisa G.J

Huruma ya Mungu: Ulinzi na Ukombozi katika Kila Hali

Huruma ya Mungu: Ulinzi na Ukombozi katika Kila Hali

Hakuna kitu cha thamani zaidi kuliko kuwa na huruma ya Mungu katika maisha yetu. Ni jambo la ajabu sana kujua kuwa Mungu wetu ni Mungu wa huruma na upendo. Kwa bahati mbaya, maisha yetu yanaweza kuwa magumu na kujaa changamoto nyingi, lakini huruma ya Mungu inaweza kutusaidia kuwa imara katika imani yetu na kutupa ulinzi na ukombozi wetu.

  1. Huruma ya Mungu ni kwa ajili ya wote: Hakuna mtu anayeweza kuzuia huruma ya Mungu. Huruma yake inafikia kila mtu bila kujali dini, rangi, au utamaduni. Kama ilivyoelezwa katika Zaburi 145:9, "Bwana ni mwema kwa wote, na rehema zake ziko juu ya kazi zake zote."

  2. Huruma ya Mungu inatusaidia wakati wa majaribu: Tunapopitia majaribu na changamoto, tunahitaji huruma ya Mungu ili kutusaidia kupitia. Kama ilivyoelezwa katika Waebrania 4:16, "Kwa hiyo na tukikaribia kwa ujasiri kiti cha neema, tupate huruma na kwa neema tukapata msaada wakati unaofaa."

  3. Huruma ya Mungu inatusamehe dhambi zetu: Tunapotubu dhambi zetu, huruma ya Mungu inatusamehe na kutuhurumia. Kama ilivyoelezwa katika Zaburi 103:8, "Bwana ni mwenye huruma na neema, si mwepesi wa hasira, na ni mwingi wa rehema."

  4. Huruma ya Mungu inatutia moyo: Wakati wowote tunapohitaji kutiwa moyo, tunaweza kuomba huruma ya Mungu. Kama ilivyoelezwa katika Isaya 41:10, "Usiogope, kwa maana mimi ni pamoja nawe. Usitetemeke, kwa maana mimi ni Mungu wako. Nitakutia nguvu, naam, nitakusaidia."

  5. Huruma ya Mungu inatuponya: Mungu anaweza kutuponya kutoka kwa magonjwa ya kimwili na kiroho. Kama ilivyoelezwa katika Yeremia 30:17, "Kwa maana nitakuponya, nitakuponya jeraha lako, asema Bwana, kwa sababu wao wamekuita, ‘Wewe ni mzigo.’

  6. Huruma ya Mungu inatupatia amani: Tunapohitaji amani, tunaweza kuomba huruma ya Mungu. Kama ilivyoelezwa katika Yohana 14:27, "Acha ninyi amani yangu, ninawapa. Sitawapa kama vile ulimwengu unavyotoa. Msitishwe, wala msifadhaike."

  7. Huruma ya Mungu inatupa upendo: Mungu anatupenda sana na anatupatia upendo wake kupitia huruma yake. Kama ilivyoelezwa katika Zaburi 103:13, "Kama baba anavyowahurumia watoto wake, ndivyo Bwana anavyowahurumia wanaomcha."

  8. Huruma ya Mungu inatusaidia kukabiliana na huzuni: Tunapohisi huzuni na uchungu, tunaweza kuomba huruma ya Mungu. Kama ilivyoelezwa katika Zaburi 34:18, "Bwana yu karibu na wale wenye moyo uliovunjika, na huyaokoa roho za waliopondeka."

  9. Huruma ya Mungu inatupa nguvu za kuvumilia: Tunapopitia magumu na kukata tamaa, tunaweza kuomba huruma ya Mungu ili kutupa nguvu za kuvumilia. Kama ilivyoelezwa katika 2 Wakorintho 12:9, "Naye akaniambia, ‘Neema yangu inakutosha, maana nguvu zangu hukamilishwa katika udhaifu.’"

  10. Huruma ya Mungu inatuhakikishia uzima wa milele: Tunapomwamini Yesu Kristo, tunapata uzima wa milele kupitia huruma ya Mungu. Kama ilivyoelezwa katika Yohana 3:16, "Kwa maana Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele."

Kutafuta huruma ya Mungu ni muhimu katika maisha yetu ya kila siku. Tunapojua kuwa Mungu wetu ni Mungu wa huruma, tunaweza kuwa na uhakika kwamba atakuwa nasi katika kila hali. Kama ilivyoelezwa katika Catechism of the Catholic Church, "Huruma ni ukweli wa Mungu wa kuwapatia watu wake ushiriki wa upendo wake wote na wema wake wote" (CCC 270). Kwa hiyo, tunaweza kuwa na amani katika maisha yetu kwa sababu tunajua kwamba tunaweza kutegemea huruma ya Mungu daima.

Kama ilivyoelezwa katika "Diary of Saint Maria Faustina Kowalska," "Mtu yeyote anayetumaini huruma ya Mungu na kufanya wema, atapata uzima wa milele" (47). Kwa hiyo, tunaalikwa daima kutafuta huruma ya Mungu na kuishi kwa njia ya upendo na wema. Tunapofanya hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba tutakuwa na ulinzi na ukombozi wetu.

Je, unahisi huruma ya Mungu katika maisha yako? Je, unatafuta huruma yake katika kila hali? Tuombe pamoja ili tupate nguvu ya kutegemea huruma ya Mungu daima na kuishi kwa njia ya upendo na wema. Amina.

Thamani ya Kazi ya Upadre

UPADRE NI KAZI YA PEKEE YA HEKIMA, UWEZO NA MAPENDO YA UMUNGU WA KRISTU. KAMWE USIMSHAMBULIE PADRE. “Yesu Maria na Yosefu nawapenda, ziokoeni Roho. KUMTETA PADRE [Haya ni maelezo ya Bwana wetu kwa Mutter Vogel.] ” Kamwe mtu asimshambulie Padre hata anapokuwa katika makosa badala yake umwombee na fanya toba ili niweze kumpa tena NEEMA.
Ni yeye peke yake anaye niwakilisha mimi hata awe haishi kulingana na mimi. Endapo Padre anaanguka tumnyoshee mkono wa msaada kwa njia ya SALA na sio KUMSHAMBULIA. Ni mimi pekee nitakuwa HAKIMU wake si mwingine ila mimi”. “Mtu yeyote anapotamka HUKUMU dhidi ya padre ananihukumu mimi”. 
Mwanangu kamwe usiruhusu padre ashambuliwe, jitahidi kuwa upande wake na umtetee”. Mwanangu kamwe usimhukumu mwungamishi wako bali umwombee sana na tolea KOMUNIO TAKATIFU kwa ajili yake, kila siku ya ALHAMISI kupitia MIKONO au MAMA YANGU MTUKUFU. 
Tena kamwe usikubali neno lolote la kumdhalilisha Padre na kusema neno baya dhidi yake (yao), HATA KAMA INGELIKUWA NI KWELI! Kila Padre ni WAKILI wangu na moyo wangu utahuzunika na kusikia uchungu kwa ajili hiyo. Usikiapo HUKUMU dhidi ya Padre, sali SALAMU MARIA. Umwonapo Padre anayeadhimisha MISA TAKATIFU akiwa katika halo isiyostahili, usiongee nae lolote kumhusu yeye bali nieleze mimi tu! Huyo huwa nasimama naye ALTERANI”. ” Oh waombeeni mapadre wangu ili watamani USAFI NA WEUPE WA ROHO kuliko jambo lolote ili waweze kutolea sadaka TAKATIFU kwa moyo na mikono iliyotakata. Ni ukweli kwamba Misa ni ile ile hata ikiadhimishwa na Padre mwenye hali isiyostahiki lakini NEEMA zinazowashukia watu sio zile zile. [MARIA, MALKIA WA MAPADRE UWAOMBEE.]

Je, Kanisa Katoliki linatambua na kufundisha umuhimu wa kuishi imani katika matendo mema?

Je, Kanisa Katoliki linatambua na kufundisha umuhimu wa kuishi imani katika matendo mema? Jibu ni ndio! Katika Kanisa Katoliki, imani na matendo mema ni vitu viwili visivyotenganishwa. Imani ni muhimu sana katika maisha yetu na lazima iendane na matendo mema ili kuwafanya wengine waone upendo wa Mungu ndani yetu.

Kanisa linatambua kuwa tunapaswa kuishi kwa kufuata mfano wa Yesu Kristo, ambaye alitufundisha kuhusu umuhimu wa kuishi imani katika matendo mema. Kama ilivyoelezwa katika Yakobo 2:14-17 "Ndugu zangu, imani yoyote kama haina matendo, imekufa kwa asili yake. Lakini mtu atamwambia, Wewe una imani, nami nina matendo; nionyeshe imani yako pasipo matendo yako, nami nitakudhihirishia imani yangu kwa njia ya matendo yangu." Kwa hiyo, Kanisa linatufundisha kuwa imani bila matendo mema haiwezi kutufikisha kwenye wokovu.

Kanisa Katoliki pia linatufundisha kuwa matendo mema hutufanya tuweze kuwatumikia wengine na kusaidia katika mahitaji yao. Kwa mfano, katika Mathayo 25:35-36, Yesu Kristo anasema "Kwa kuwa nilikuwa na njaa, mkanipa chakula; nilikuwa na kiu, mkaninywesha; nilikuwa mgeni, mkanikaribisha; nilikuwa uchi, mkanivika; nilikuwa mgonjwa, mkanitazama; nilikuwa gerezani, mkanitembelea." Hii inaonyesha umuhimu wa kutenda mema kwa wengine, ili waweze kuona upendo wa Mungu ndani yetu.

Kanisa Katoliki pia linatufundisha juu ya sakramenti za Kanisa ambazo zinatupa neema ya kutenda matendo mema. Kwa mfano, katika sakramenti ya Ekaristi, tunapata neema ya kuwa na nguvu ya kuendelea kuishi kwa kufuata mfano wa Yesu Kristo na kutenda mema kwa wengine. Kama ilivyoelezwa katika KKK 1391 "Katika Ekaristi, Kristo anatupa chakula cha uzima wa milele; hii ndiyo chakula chenye nguvu za kuwasaidia waamini wanaotenda mema, kukua katika upendo kwa Mungu na jirani."

Kanisa Katoliki linatufundisha kuwa tunapaswa kuwa mashuhuda wa Kristo kwa wengine kwa kufanya matendo mema. Kama ilivyoelezwa katika KKK 2472 "Mashuhuda wa Kristo wanapaswa kuwa waaminifu na waaminifu, watu wa dhamira ya juu, wenye kuishi kulingana na imani yao, na kuonyesha katika matendo yao kwamba wanaamini katika Kristo." Kwa hiyo, Kanisa linatutia moyo kufanya matendo mema na kuwa mashuhuda wa Kristo kwa wengine.

Kanisa Katoliki linatambua na kufundisha umuhimu wa kuishi imani katika matendo mema. Imani na matendo mema ni vitu viwili visivyotenganishwa. Lazima tuwe mashuhuda wa Kristo kwa wengine kwa kufanya matendo mema na kuwa waaminifu katika imani yetu. Kama ilivyoelezwa katika Luka 6:46-49, "Kwa nini mnaniita Bwana, Bwana, na hamfanyi ninayowaamuru?" Kwa hiyo, tunaalikwa kuwa waaminifu katika imani yetu na kutenda mema kwa wengine ili kuwa mashuhuda wa Kristo.

Je, Kanisa Katoliki linamwomba Bikira Maria?

Je, Kanisa Katoliki linamwomba Bikira Maria?

Ndio, Kanisa Katoliki linamwomba Bikira Maria kwa sababu yeye ni Mama wa Mungu na Mama yetu pia. Tunaamini kuwa Bikira Maria ni mtakatifu na mwenye nguvu ya kuombea kwa ajili yetu kwa Mungu. Tunaomba Bikira Maria kwa sababu tunajua kuwa yeye anajua mahitaji yetu na anaweza kuwasilisha mahitaji yetu kwa Mungu.

Katika Injili ya Luka, tunasoma kuwa Malaika Gabrieli alimwambia Bikira Maria kuwa atakuwa Mama wa Mungu. Maria alisema "tazama, mimi ni mtumishi wa Bwana; iwe kwangu kama ulivyosema." (Luka 1:38). Bikira Maria alikuwa mtii kwa Mungu na aliitikia wito wa Mungu kwa unyenyekevu mkubwa. Hivyo, Bikira Maria anatupatia mfano wa kuigwa katika utii kwa Mungu na kujikabidhi kwa mapenzi ya Mungu.

Kanisa Katoliki linatambua kuwa Bikira Maria ni mpatanishi wetu kwa Mungu. Kwa hiyo, tunaweka matumaini yetu kwa Bikira Maria, tunawaomba awakumbuke watoto wake na kutuletea baraka za Mungu. Bikira Maria ni Mama yetu wa huruma ambaye daima yuko tayari kutusaidia. Kupitia sala zetu kwa Bikira Maria, tunaweza kuzidi kuimarisha uhusiano wetu na Mungu.

Kanisa Katoliki linatambua kuwa Bikira Maria ni mtakatifu na ndio sababu tunamwomba. Tunajua kuwa yeye anasikiliza maombi yetu na anatuombea kwa Mungu. Kama vile Yesu alivyomwambia mama yake msalabani "Mama yako" na kumkabidhi kwa wanafunzi wake kuwa mama yao, tunaona kuwa Bikira Maria ni Mama yetu pia (Yohana 19:27).

Kanisa Katoliki limejenga mafundisho ya kuwaomba watakatifu, na hii inajumuisha Bikira Maria. Katika Catechism of the Catholic Church, tunasoma kuwa "katika kumwomba Bikira Maria, tunajiongezea tunaomba kwa watakatifu wote" (CCC 2679). Kama vile tunamwomba Bikira Maria, tunawajibika kuomba kwa watakatifu wengine pia. Kuwaomba watakatifu kunatupa nafasi ya kujifunza kutoka kwao na kusali kwa ajili ya baraka zao.

Kwa hiyo, jibu ni ndio, Kanisa Katoliki linamwomba Bikira Maria. Tunamwomba kwa sababu yeye ni Mama yetu wa Mbinguni na mpatanishi wetu kwa Mungu. Tunajua kuwa yeye anatusikiliza na tunamwamini kuwa anaweza kutuletea baraka za Mungu. Tunamwomba Bikira Maria ili kutia moyo na kuimarisha uhusiano wetu na Mungu. Kwa hiyo, tunasali, "Salamu Maria, Mama wa Mungu na Mama yetu."

Ni nini imani ya Kanisa Katoliki kuhusu sakramenti ya Upatanisho?

Kanisa Katoliki linayo imani thabiti kuhusu sakramenti ya Upatanisho. Ni sakramenti ambayo inakubaliwa na kanisa zote duniani kama njia ya kupata msamaha wa dhambi. Upatanisho unawakilisha neema kubwa ya Mungu kwa wapenzi wake, ambao wanaamua kuungana tena na Mungu kwa dhati ya mioyo yao.

Kulingana na Katekismu ya Kanisa Katoliki (CCC 1424), "Upatanisho ni sakramenti ya toba, ambayo inaruhusu waamini kupata msamaha wa dhambi zao kutoka kwa Mungu na Kanisa, na kurejeshwa katika neema ya wokovu." Kwa hivyo, sakramenti hii inawakilisha upatanisho kati ya Mungu na mwanadamu.

Waamini wa Kanisa Katoliki wanaamini kuwa sakramenti ya Upatanisho inakuja na namna tatu za toba ambazo ni: kutubu kwa kinywa, kufanya matendo ya toba na kukiri dhambi zetu kwa kuhani. Kutubu kwa kinywa ni kwa kusema au kuomba msamaha kutoka kwa Mungu, wakati kufanya matendo ya toba ni kubadili tabia zetu na kuacha kufanya mambo ambayo sio sawa. Kukiri dhambi zetu kwa kuhani ni hatua ya mwisho ya sakramenti ya Upatanisho.

Katika Biblia, Yesu alitoa mamlaka ya kufanya upatanisho kwa wafuasi wake wakati alisema: "Kama mkisamehe dhambi za mtu yeyote, zitasamehewa; na kama mkihifadhi dhambi za mtu yeyote, zitahifadhiwa " (Yohana 20:23). Kwa hivyo, Kanisa linajua kuwa kuhani ana mamlaka ya kusamehe dhambi zetu kwa jina la Yesu Kristo.

Kuna faida nyingi za kupokea sakramenti ya Upatanisho. Kwanza kabisa, inatupa upya wa maisha yetu ya kiroho na kumweka Mungu kwa nafasi yake sahihi katika maisha yetu. Pia, inasaidia katika kujenga uhusiano na wengine kwa kufanya matendo mema, badala ya kushikilia chuki au kukasirika. Kupokea sakramenti ya Upatanisho husaidia katika kufanya maisha yetu kuwa ya amani na ya furaha.

Kwa hiyo, ni muhimu kwa wapenzi wa Kanisa Katoliki kupokea sakramenti ya Upatanisho mara kwa mara, kama njia ya kudumisha uhusiano wao na Mungu na kusafisha maisha yao ya kiroho. Kwa kufanya hivi, tunaweza kukua katika imani yetu na kuwa wapenzi wazuri wa Yesu Kristo.

Biblia inavyothibitisha kuwa Bikira Maria Mama wa Yesu ni Mama wa Wakristu Wote

Ufunuo 12:17
17Kisha lile joka likapatwa na hasira kali kwa ajili ya huyo mwanamke, likaondoka ili kupigana vita na watoto waliosalia wa huyo mwanamke, yaani, wale wanaozitii amri za Mungu na kuushika ushuhuda wa Yesu Kristo.
Kwa hiyo Bikira Maria ni Mama wa Wakritu wote yaani, wale wanaozitii amri za Mungu na kuushika ushuhuda wa Yesu Kristo

Ukisoma kwa urefu inasomeka hivi

Ufunuo 12:1-18

1 Kukaonekana ishara kuu mbinguni: Palikuwa na mwanamke aliyevikwa jua na mwezi ukiwa chini ya miguu yake na taji ya nyota kumi na mbili ilikuwa kichwani mwake. 2Alikuwa na mimba naye akilia kwa uchungu kwa kuwa alikuwa anakaribia kuzaa. 3Kisha ishara nyingine ikaonekana mbinguni: Likaonekana joka kubwa jekundu lenye vichwa saba na pembe kumi na taji saba katika vichwa vyake. 4Mkia wake ukakokota theluthi ya nyota zote angani na kuziangusha katika nchi. Ndipo lile joka likasimama mbele ya yule mwanamke aliyekuwa karibu kuzaa ili lipate kumla huyo mtoto mara tu atakapozaliwa. 5Yule mwanamke akazaa mtoto mwanamume, atakayeyatawala mataifa yote kwa fimbo yake ya utawala ya chuma. Lakini huyo mtoto akanyakuliwa na kupelekwa kwa Mungu kwenye kiti Chake cha enzi. 6Yule mwanamke akakimbilia nyikani, ambako Mungu alikuwa amemtayarishia mahali ili apate kutunzwa huko kwa muda wa siku 1,260. 7 Basi palikuwa na vita mbinguni: Mikaeli na malaika zake wakapigana na hilo joka, nalo joka pamoja na malaika zake likapigana nao. 8Lakini joka na malaika zake wakashindwa na hapakuwa tena na nafasi kwa ajili yao mbinguni. 9Lile joka kuu likatupwa chini, yule nyoka wa zamani aitwaye Ibilisi au Shetani, aupotoshaye ulimwenguni wote. Akatupwa chini duniani, yeye pamoja na malaika zake. Ushindi 10Kisha nikasikia sauti kuu mbinguni ikisema, “Sasa Wokovu na uweza na Ufalme wa Mungu wetu umekuja na mamlaka ya Kristo wake. Kwa kuwa ametupwa chini mshtaki wa ndugu zetu, anayewashtaki mbele za Mungu usiku na mchana. 11Nao wakamshinda kwa damu ya Mwana-Kondoo na kwa neno la ushuhuda wao. Wala wao hawakuyapenda maisha yao hata kufa. 12Kwa hiyo, furahini ninyi mbingu na wote wakaao humo! Lakini ole wenu nchi na bahari, kwa maana huyo Shetani ameshuka kwenu, akiwa amejaa ghadhabu, kwa sababu anajua ya kuwa muda wake ni mfupi!’ 13Lile joka lilipoona kuwa limetupwa chini duniani, lilimfuatilia yule mwanamke aliyekuwa amezaa mtoto mwanamume. 14Lakini huyo mwanamke akapewa mabawa mawili ya tai mkubwa, kusudi aweze kuruka mpaka mahali palipotayarishwa kwa ajili yake huko nyikani, ambako atatunzwa kwa wakati na nyakati na nusu wakatia ambako yule joka hawezi kufika. 15Ndipo lile joka likamwaga maji kama mto kutoka kinywani mwake, ili kumfikia huyo mwanamke na kumkumba kama mafuriko. 16Lakini nchi ikamsaidia huyo mwanamke kwa kufungua kinywa na kuumeza huo mto ambao huyo joka alikuwa ameutoa kinywani mwake. 17Kisha lile joka likapatwa na hasira kali kwa ajili ya huyo mwanamke, likaondoka ili kupigana vita na watoto waliosalia wa huyo mwanamke, yaani, wale wanaozitii amri za Mungu na kuushika ushuhuda wa Yesu Kristo. Lile joka likasimama kwenye mchanga wa bahari. 18Yule joka akajikita katika mchanga ulioko ufuoni mwa bahari.

Tunajifunza nini

Mwanamke ni Bikira Maria

Mwanamke aliyetukuzwa Uf 12:1

1 Kukaonekana ishara kuu mbinguni: Palikuwa na mwanamke aliyevikwa jua na mwezi ukiwa chini ya miguu yake na taji ya nyota kumi na mbili ilikuwa kichwani mwake.

Anamzaa mtoto

Analindwa nyoka asimdhuru

Nyoka anapambana na wanawe

IShara ya joka kama Shetani

Akisubiri kuzaliwa kwa mtoto ili amdhuru kisha alishindwa na kutupwa duniani na kutaka kupambana na yule mwanamke Akashindwa na kuishia kupambana na watoto wa Yule mwanamke yaani, wale wanaozitii amri za Mungu na kuushika ushuhuda wa Yesu Kristo Uf 12:17

Mtoto Aliyezaliwa mwenye mamlaka

Ambaye ndiye Yesu Kristu

Kwa hiyo, Bikira Maria Aliwezeshwa kumshinda Shetani na ni Mama wa Wakristu wote

Shopping Cart
1
    1
    Your Cart
    🏠 Home 📖 Reading 🖼️ Gallery 💬 AI Chat 📘 About