Dondoo za Mapishi na Lishe

Jinsi ya kutengeneza Biskuti Za Ufuta Na Jam

VIAMBAUPISHI

Unga vikombe 2

Sukari ya kusaga 1/4 Kikombe

Siagi 250 gms

Jam kisia

Ufuta kisia

Vanilla 1 kijiko cha chai

MAPISHI

Tia kwenye mashine ya kusaga (blender) au mashine ya keki, siagi, yai, sukari na vanilla uchanganye hadi ichanganyike vizuri.
Tia baking powder, na unga na changanya kwa mkono vizuri.
Paka siagi sinia ya kupikia ya oveni.
Tengeneza viduara vidogo vidogo.
Bonyeza kila kiduara katikati kwa kidole, kisha weka jam, halafu juu yake paka mayai na unynyuzie ufuta.
Pika katika moto wa chini 350ºF kwa muda wa dakika 20-25.
Tayari kwa kuliwa.

Mapishi ya Ugali Mchuzi Wa Samaki Nguru Wa Nazi Na Bamia Za Kukaanga

Vipimo Vya Ugali:

Unga wa mahindi/sembe – 4

Maji – 6 takriban

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Chota unga kidogo katika kibakuli uchanganye na maji kidogo .
Weka maji mengineyo katika sufuria kwenye moto.
Changanya na mchanganyiko mdogo ufanya kama uji.
Kisha kidogo kidogo unaongeza sembe huku unakoroga na kuusonga ugali hadi uive.

Vipimo Vya Mchuzi Wa Samaki Wa Nazi

Samaki nguru – 5 vipande

Pilipili mbichi ilosagwa

Kitunguu maji kilosagwa – 1 kimoja

Nyanya ilosagwa – 2

Haldi/tumeric/bizari ya manjano – ¼ kijiko cha chai

Chumvi – kiasi

Ndimu – 2 kamua

Tui la nazi zito – 2 vikombe

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Baada ya kumuosha samaki, weka katika sufuria.
Tia chumvi, ndimu, pilipili mbichi ilosagwa.
Tia vitunguu na nyanya zilosagwa
Mkaushe kwa hivyo viungo, akianza kukauka tia tui la nazi.
Acha kidogo tu katika moto tui liwive mchuzi ukiwa tayari.

Vipimo Vya Bamia

Bamia – ½ kilo takriban

Nyanya kopo – 1 kijiko cha chai

Methi/uwatu/fenugreek seeds ilosagwa – 1 kijiko cha chai

Dania/corriander ilosagwa – ½ kijiko cha chai

Chumvi – kiasi

Mafuta – 1 kikombe cha kahawa

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Katakata bamia kwa urefu.
Weka mafuta katika karai, kisha tia bizari zote na nyanya kopo, kaanga kidogo.
Tia bamia endelea kukaanga, kisha acha katika moto mdogomdogo ufunike.
Kila baada ya muda funua karai ukaange bamia hadi ziwive zikiwa tayari.

Mapishi ya Sponge keki

Mahitaji

Unga wa ngano (self risen flour) 100g
Sukari (sugar) 100g
Siagi isiyokuwa na chumvi (unsalted butter) 100g
Mayai (eggs) 2
Vanila 1 kijiko cha chai
Chumvi pinch
Warm water 3 vijiko vya chakula

Matayarisho

Kwanza washa oven moto wa 200 C. Baada ya hapo saga butter na sukari mpaka viwe laini kisha tia mayai na uendelee kusaga mpaka vichanganyike vizuri kisha tia unga, vanila, chumvi na na maji na usage mpaka upate uji usiokuwa mzito sana au mwepesi sana. Baada ya hapo utie kwenye baking tin na u bake kwa muda wa dakika 25 na mpaka cake yako iive yani juu na chini iwe ya brown na ukidumbukiza kijiti katikati kinatoka kikiwa clean. Baada ya hapo itoe kwenye tin na uiache ipoe. Ikisha poa itakuwa tayari kwa kuliwa.

Jinsi ya kutengeneza Biskuti Ya Keki Kavu (Shortcake)

VIAMBAUPISHI

Unga – 2 Magi (vikombe vya chai)

Sukari iliyosagwa – 2/3 Magi (kikombe cha chai)

Siagi – 220 g

Unga wa mchele – ½ Magi

Yai -1

Vanilla – 1 kijiko cha chai

MAANDALIZI

Changanya vitu vyote hivyo kwenye bakuli mpaka unga ushikamane.
Paka mafuta treya ya kuchomea kisha utandaze kwenye treya ya 20cm kwa 30 cm au (8 in kwa 12 in)
Choma kwenye moto 325˚C kwa muda wa saa nzima au mpaka ibadilike kuwa rangi ya dhahabu.
Epua acha ipoe kisha kata vipande kama mstatili, weak kwenye sahani tayari kunywewa na chai.

NYONGEZA

Kwa unga huo huo unaweza kutengeneza vibiskuti vya duara duara.

Mapishi ya Chapati za Kusukuma kitaalamu

Mahitaji

Unga wa ngano (plain flour 1/2 of kilo)
Siagi (butter vijiko 2 vya chakula)
Yai (egg 1)
Chumvi (1/2 ya kijiko cha chai)
Hiliki (ground cardamon 1/4 ya kijiko cha chai)
Maji ya uvuguvugu (warm water)
Mafuta (vegetable oil)

Matayarisho

Weka unga wa ngano katika bakuli la kukandia, kisha tia chumvi na hiliki na uchanganye kwanza, baada ya hapo tia siagi na uichanganye vizuri na unga mpaka ipotee. Baada ya hapo tia tena yai na uchanganye vizuri. Mchanganyiko ukishachanganyika vizuri sasa unaweza kutia maji ya uvuguvugu kidogo, kidogo huku ukiwa unauchanganya ili kupata donge. Baada ya hapo anza kukanda hilo donge mpaka mabuje yote yapotee na unga uwe mlaini, ambapo itakuchukua kama dakika 15. Baada ya hapo tawanyisha unga katika madonge ya wastani (yasiwe makubwa sana au madogo sana) Ukimaliza hapo, andaa kibao cha kusukumia chapati kwa kukitia unga kidogo ili chapati isinatie kwenye kibao. Sukuma donge moja la chapati mpaka liwe flat na kisha weka kijiko kimoja cha mafuta na usambaze. ukisha maliza ikunje (roll). Fanya hivyo kwa madonge yote yaliyobakia.
Baada ya hapo andaa chuma cha kuchomea (fry-pan) katika moto wa wastani. Kisha anza kusukuma chapati (ni vizuri ukaanza na zile ulizozikunja mwanzo ili kuzipa nafasi zile za mwisho ziweze kulainika) ukiwa unasukuma hakikisha zinakuwa flat (na zisiwe nene sana au nyembamba sana) Ukishamaliza hapo tia kwenye chuma cha kuchomea. Acha iive upande mmoja then igeuze upande wa pili. Tia mafuta ama kijiko kimoja kikubwa upande wa chini wa chapati na uanze kuukandamiza kwa juu uku ukiwa unaizungusha. fanya hivyo uku ukiwa unaigeuza kuiangalia kwa chini ili isiungue. ikishakuwa ya brown, geuza upande wa pili na urudie hivyohiyvo mpaka chapati iive. Rudia hii process kwa chapati zote zilizobakia.

Siri ya chapati kuwa laini ni kutia siagi au mafuta ya kutosha kipindi unazikanda na pia kuzikanda mpaka unga uwe laini.

Mapishi ya Wali Wa Nazi Wa Adesi, Bamia Na Mchuzi Wa Kamba

Mahitaji

Mchele – 2 vikombe

Adesi -1 ½ vikombe

Nazi ya unga – 1 Kikombe

Maji (inategemea mchele) – 3

Chumvi – Kiasi

Vipimo Vya Bamia:

Bamia – ½ kilo

Vitunguu maji – 2 vya kiasi

Nyanya iliyosagwa – 1 kubwa

Nyanya ya kopo – 2 vijiko vya chai

Pilipili manga – ½ kijiko cha chai

Mafuta – 3 vijiko vya chai

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika:

Wali wa adesi

Osha na roweka mchele na adesi .
Chuja nazi kwa vikombe 3 vya maji tia chumvi kisha weka jikoni.
Tui la nazi likishachemka tia mchele na adesi pamoja. Punguza moto, funika wali upikike kwa moto mdogo mpaka ukauke vizuri.

Bamia

Katakata bamia vipande vya kiasi/ Katakakata vitunguu weka kando.
Katika sufuria tia mafuta na kaanga vitunguu hadi viwe rangi ya hudhurungi.
Tia nyanya ilosagwa na nyanya ya kopo na pilipili manga na chumvi.
Kisha Tia bamia punguza moto mdogo mdogo mpaka ziwive.

Vipimo: Mchuzi Wa Kamba

Kamba – 1Lb

Vitunguu vilokatwa katwa – 2

Nyanya ilokatwa katwa – 2

Pilipili mbichi iliyosagwa – 1 Kijiko cha chai

Kitunguu saumu(thomu/galic) – 1 Kijiko cha chai

Bizari ya mchuzi (curry powder) – ½ Kijiko cha chai

Haldi – bizari ya manajano – ½ kijiko cha chai

Nyanya ya kopo – ½ Kijiko cha chai

Ndimu – 1

Chumvi – Kiasi

Mafuta ya kukaangia – 2 Vijiko vya supu

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Kaanga vitunguu kidogo hadi vilainike,
Tia nyanya, thomu na piilipili mbichi. Endelea kukaanga, tia nyanya ya kopo, chumvi, bizari zote.
Tia tia kamba na huku unakoroga mpaka wabadilike rangi na kuwiva. Kamulia ndimu na mchuzi uko tayari.

Mapishi ya Pilau Ya Nyama Ya Ng’ombe Na Nyanya

Vipimo

Mchele (Basmati) – 3 vikombe

Nyama ya ngo’mbe – 1 kg

Pilipili boga – 1 kubwa

Nyanya – 2 kubwa

Vitunguu maji – 2 vikubwa

Kitunguu saumu(thomu/galic) iliyosagwa – 1 kijiko cha supu

Tangawizi – 1 kijiko cha chai

Ndimu – 1

Mafuta ya kupikia – ½ kikombe

Mdalasini – ½ kijiko cha chai

Binzari nyembamba – 1 kijiko cha chai

Pilipili manga – ½ Kijiko cha chai

Hiliki – ½ Kijiko cha chai

Namna ya kutayarisha na Kupika

Roweka mchele wako katika chombo

Chukuwa nyama na ioshe vizuri na itie thomu, tangawizi, ndimu, pilipili manga na chumvi kiasi

Iweke jikoni hadi ikauke maji na kuwa imewiva huku ukiikaanga kaanga kwa hayo hayo mafuta yake hadi kuwa rangi ya hudhurungi

Katakata Vitunguu na nyanya weka pembeni

Chukua pilipili boga, thomu, tangawizi na visage katika mashine ya kusagia

Weka sufuria pembeni na utie mafuta, subiri yapate moto

Kisha tia vitunguu na vikaange hadi kuwa hudhurungi na tia nyanya

Kisha mimina mchanganyiko wako ulio usaga wa pilipili boga, thomu na tangawizi

Koroga kwa dakika kadhaa Kisha mininia nyama uliyokuwa tayari, maji kiasi na chumvi wastani na subiri maji hayo yachemke

Weka mchele humo na koroga kiasi na onja chumvi kama ipo sawa au kama ndogo unaweza kuongeza

Funika na punguza moto na uache uive taratibu

Baada ya kukauka maji kabisa basi ugeuze na subiri tena kwa dakika kama mbili na tayari kuliwa.

Jinsi ya kuandaa Wali Wa Hudhurungi Na Kabeji

VIPIMO VYA WALI

Mchele wa hudhurungi (brown rice)

na (wild rice kidogo ukipenda)Osha na Roweka – 2 Vikombe

Kitungu maji – 1 Kiasi

Kitunguu saumu – 1 Kijiko cha supu

Bizari ya manjano – 1/2 Kijiko cha chai

Mdalasini nzima – 1 kijiti

Iliki iliyosagwa – 1/4 Kijiko cha chai

Chumvi – Kiasi

Pilipili manga – 1/4 Kijiko cha cha

Mafuta – 2 Vijiko vya supu

Majani ya Bay(bay leaves) – 1

Mbegu ya giligilani iliyoponwa (coriander seeds) – 1 Kijiko cha chai

Supu ya kuku ya vidonge – 1

Maji ya wali – 4 vikombe

NAMNA YA KUTAYARISHA NA KUPIKA

Kaanga kitungu, kabla ya kugeuka rangi tia thomu.
Kisha weka bizari zote na ukaange kidogo.
Tia mchele kisha maji na ufunike upike katika moto mdogo.
Na ikishawiva itakuwa tayari kwa kuliwa na kabeji na kuku wa tanduuri.

VIPIMO VYA KABEJI

Kabeji iliyokatwa katwa – 1/2

Karoti iliyokwaruzwa – 1-2

Pilipili mboga kubwa – 1

Figili mwitu (celery) iliyokatwa – 1 au 2 miche

Kitunguu saumu(thomu/galic) iliyosagwa – 1 Kijiko cha supu

Pilipili mbichi – 1

Kisibiti (caraway seed) – 1/4 Kijiko cha chai

Bizari ya manjano ya unga = 1/2 Kijiko cha chai

Giligani ya unga – 1 Kijiko cha chai

Chumvi – Kiasi

Kitungu maji kilichokatwa -1

Kotmiri – upendavyo

Mafuta ya kukaangia – Kiasi

NAMNA YA KUTAYARISHA NA KUPIKA

Kwenye sufuria kaanga kitungu, figili mwitu kisha tia thomu na pilipili zote.
Halafu tia bizari zote na ukaange kidogo.
Kisha weka kabeji na chumvi, ufunike moto mdogo ilainike kidogo na sio sana
Tia karoti na usiwache motoni sana, kisha zima moto na inyunyizie kotmiri juu.

Tofauti kati ya yai la kuku wa kienyeji na la kuku wa kisasa

Kilishe mayai yote ni sawa. Virutubishi vinavyopatikana kwenye yai la kuku wa kienyeji kama protini, vitamini A, madini ya chuma na virutubishi vya aina nyingine, ndivyo hivyo vinavyopatikana pia kwenye yai la kuku wa kisasa.

Tatizo linaweza kutokea pale ambapo wafugaji wa kuku wa kisasa hawafuati taratibu za ufugaji na pengine hawawapi kuku vyakula muhimu wanavyohitaji au wanawapa dawa na vyakula visivyo bora kiafya, hivyo wakati mwingine kiini cha yai la kuku wa kisasa huonekana kupungua rangi ya njano kuliko kiini cha yai la kuku wa kienyeji.

Mtu anashauriwa kula yai bila kujali ni la kuku gani, kwa kutegemea ni yai lipi linapatikana kwa urahisi. Lakini nivizuri kula mayai ambayo yapo salama.

Bisikuti Za Kokoa (Cocoa Biscuits)

Viambaupishi

Siagi 100gm

Unga wa kaukau (cocoa powder) 2 Vijiko vya supu

Maziwa mazito (condensed milk) Moja kikopo (397gm)

Bisikuti za Mary 2 Pakiti

Njugu ½ Kikombe

Karatasi la plastiki

Jinsi ya kuandaa na kupika

1. Vunjavunja bisikuti zote packet mbili ziwe vipande vidogo vidogo.

2. Pasha moto siagi mpaka ipate.

3. Tia kwenya siagi imoto maziwa mazito na cocoa koroga vizuri.

4. Kisha tia kwenye mchanganyiko bisikuti zilizovunjwa na njugu na uchanganye kisha epua motoni.

5. Paka karatasi la plastiki mafuta kidogo halafu tia mchanganyiko kisha kunja (roll).

6. Tia kwenye freeza muda wa saa.

7. Halafu toa karatasi na ukate kate na panga kwenye sahani na itakuwa tayari kwa kuliwa.

Mapishi ya Sambusa za nyama

Mahitaji

Nyama ya kusaga (minced beef 1/4 kilo)
Vitunguu maji vilivyokatwakatwa(diced onion 2 vikubwa )
Kitunguu swaum/ tangawizi (garlic and ginger paste 1 kijiko cha chakula)
Chumvi (salt)
Pilipili iliyokatwakatwa (scotch bonnet 1)
Limao (lemon 1/2)
Curry powder 1/2 kijiko cha chai
Cinnamon powder 1/4 kijiko cha chai
Coriander powder 1/4 kijiko cha chai
Cumin powder 1/4 kijiko cha chai
Unga wa ngano (all purpose flour kidogo)
Manda za kufungia (spring roll pastry)
Giligilani (fresh coriander kiasi)
Mafuta ya kukaangia

Matayarisho

Changanya nyama na limao, chumvi, pilipili,kitunguu swaum, tangawizi na spice zote, kisha pika katika moto wa kawaida mpaka nyama iive na maji yote yakauke. Baada ya hapo kabla hujaipua nyama tia vitunguu na giligilani na uvipike pamoja kwa muda wa dakika 2 na uipue weka pembeni na uache viipoe. Baada ya hapo tia unga kidogo katika bakuli nauchanganye na maji kidogo kupata uji mzito kwa ajili ya kugundishia manda. Baada ya hapo tia nyama katika manda na kisha zifunge kwa kugundishia na unga wa ngano.Ukisha maliza kuzifunga zote zikaange mpaka ziwe za brown na uzitoe. Na hapo zitakuwa tayari kwa kuliwa.

Mapishi ya Pilau Ya Adesi Za Brown Karoti Na Mchicha Kwa Samaki Wa Salmon

Vipimo

Mchele vikombe 3

Karoti 1 ikune (grate)

Mchicha katakata kiasi

Adesi za brown

Kitunguu katakata (chopped)

Supu ya kitoweo chochote upendayo au vidonge vya supu 2

Garama masala (bizari mchanganyiko) kijiko 1 cha kulia

Samli ¼ kikombe

Chumvi kiasi

Vipimo Vya Samaki Wa Salmon

Samaki wa Salmon vipande 4 vikubwa

Tangawizi mbichi ilosagwa kijiko 1 cha kulia

Thomu (garlic/saumu) kijiko 1 cha kulia

Chumvi kiasi

Bizari ya mchuzi kijiko 1 cha kulia

Ndimu 1 kamua

Nyanya 2 kata slice kubwa kubwa

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika Samaki wa Salmon

Changanya viungo vyote upake katika samaki.
Weka katika treya na panga slice za nyanya juu yake.
Oka (grill/choma) katika oven umgeuze samaki upande wa pili.
Akiwa tayari epua.

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika Wali

Roweka mchele kiasi kutegemea aina ya mchele. Tumia basmati (pishori)
Roweka adesi kisha zichemshe katika maji ya kiasi. Chuja maji adesi na maji yatakayobakia tumia katika kupikia pilau hii.
Kaanga vitunguu katika samli iliyoshika moto kwenye sufuria ya kupikia.
Vikianza kugeuka rangi tia karoti, mchicha, adesi, bizari mchanganyiko kisha kaanga kidogo.
Tia mchele ukaange kidogo kisha tia supu au maji pamoja na kidonge cha supu.
Tia chumvi ukoroge funika upike kama pilau.
Epua upakue katika sahani utolee kwa samaki wa salmon

Mapishi ya Pilau Ya Nyama Ng’ombe Karoti Na Zabibu

Vipimo – Nyama

Nyama ng’ombe ya mifupa ilokatwa vipande – 1 kilo

Tangawizi na thomu (somu/garlic) ilosagwa – 2 vijiko vya supu

Bizari mchanganyiko/garama masala – 1 kijiko cha chai

Chumvi – Kiasi

Vipimo – Wali

Mchele – 4 glass

Mbatata/viazi menya katakata – 3 kubwa

Vitunguu katakata – 5

Kitunguu thomu kilosagwa (garlic/somu) – 1 kijiko cha supu

Hiliki ya unga – 1 kijiko cha chai

Bizari nzima ya pilau/cumin – 1 mti

Samli au mafuta – 2 Vijiko vya supu

Karoti zilokatwakatwa nyembamba – 6-7

Zabibu – Kiasi

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Katika sufuria weka mafuta kijiko kimoja cha supu tia nyama na viungo vyake.
kaushe katika moto hadi ikaribie kukauka kisha tia maji kiasi cha kuivisha na kubakisha supu ya mchele.
Katika sufuria ya kupikia weka samli au mafuta ishike moto.
Tia mbatata/viazi kaanga, tia vitunguu kaanga kidogo.
Tia kitunguu thomu, hiliki, bizari ya pilau endelea kukaanga hadi viwe rangi ya brown kidogo.
Tia mchele kaanga kidogo, kisha mimina nyama na supu yake. Funika wali uwive.
Weka kikaangio katika moto, tia samli kijiko kimoja kisha tia karoti na zabibu, kaanga kwa sekunde chache tu kwa ajili ya kulainisha karoti na zabibu.
Utakapopakuwa wali, pambia juu karoti na zabibu.

Jinsi ya kupika Mkate

Mahitaji

Unga wa ngano ( self risen flour) kikombe 1 na 1/2
Hamira (yeast) 1 kijiko cha chai
Sukari (sugar) 1 kijiko cha chakula
Chumvi (salt) 1/2 kijiko cha chai
Siagi iliyoyeyushwa (melted butter) 1 kijiko cha chakula
Maji ya uvuguvugu ( warm water) kiasi

Matayarisho

Changanya vitu vyote katika bakuli kubwa kisha aanza kukanda mpaka upate donge laini.Baada ya hapo liweke hilo donge kwenye bakuli la plastic na weke katika sehemu yenye joto ili unga uumuke. Hakikisha unga unaumuka zaidi (yani unaji double size) unaweza kuchukua kama saa 1 na nusu hivi. Baada ya hapo ukande tena na uache uumuke tena kwa mara ya pili, Ukisha umuka pakaza butter katika baking tin (chombo cha kuokea) na upakaze mkate butter kwa juu,kisha uoke katika oven kwa muda wa dakika 30 (katika moto wa 200C) (hakikisha juu na chini unakuwa wa brown Na hapo mkate wako utakuwa tayari

Jinsi ya kupika Viazi Vya Nazi Kwa Nyama

Mahitaji

Viazi – 3lb

Nyama – 1lb

Kitunguu – 1

Nyanya – 2

Kitunguu saumu(thomu/galic) – 1 kijiko cha chai

Manjano – ½ kijiko cha chai

Curry powder – ½ kijiko chai

Nyanya kopo – 1 kijiko cha chai

Pilipili ya unga – kiasi upendavyo

Chumvi – kiasi

Kidonge cha supu – 1

Tui la nazi – 1 kopoau zaidi

Mtindi ukipenda – 3 vijiko vya supu

Kotmiri – kiasi ya kupambia

Nazi ya unga – 4 vijiko vya supu

Mafuta – 2 vijiko vya supu

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Kata nyama vipande vipande kisha chemsha na chumvi mpaka iive.
Menya maganda viazi na ukate slice kubwa weka pembeni
Kata kata kitunguu kisha kaanga na mafuta mpaka vibadilike rangi
Tia thomu, bizari ya manjano, pilipili ya unga, nyanya kopo
Kata kata nyanya nzima vipande vidogo tia na kidonge cha supu.
Kisha tia viazi, nyama na tui la nazi finika mpaka viazi viwive lakini visiwe vikavu.
Tia mtindi na nazi ya unga kama vijiko 4 vya supu iache motoni kidogo kisha pakua, tupia kotmiri juu na itakuwa tayari kuliwa.

Mapishi ya Boga La Nazi

Vipimo

Boga la kiasi – nusu yake

Tui zito la nazi 1 ½ gilasi

Sukari ½ kikombe

Hiliki ½ kijiko cha chai

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Menya boga kisha katakata vipande vya kiasi.
Weka katika sufuri tia maji kiasi ya kuchemshia na kuwiva bila ya kubakia maji mengi.
Changanya tui na sukari na hiliki kisha mimina juu ya boga wacha katika moto dakika chache tu bila ya kufunika.
Epua mimina katika chombo likiwa tayari.

Mapishi ya Maini ya kuku

Mahitaji

Maini ya kuku 1/2 kilo
Vitunguu vikubwa 2
Hoho 1
Pilipil 1
Limao 1/2
Swaum/tangawizi 1 kijiko cha chai
Curry powder 1/2 kijiko cha chai
Mafuta ya kupikia

Matayarisho

Safisha maini weka pembeni. Baada ya hapo kaanga vitunguu,swaum na tangawizi pamoja (hakikisha vitunguu visiwe vya brown), kisha tia maini, curry powder, pilipili, chumvi ,hoho na limao kisha changanya vizuri na ufunike. Pika mpaka maini yaive na hakikisha yanakuwa na rojo kidogo. Baada ya hapo ipua na yatakuwa tayari kwa kuliwa na chochote upendacho kama vile chapati, chips, ugali, wali.

Mapishi ya tambi za kukaanga

Kupika tambi ni kama ifuatavyo

VIAMBA UPISHI

Tambi pakti moja

Sukari ¾ kikombe cha chai

Mafuta ½ kikombe cha chai

Iliki kiasi

Maji 3 Vikombe vya chai

Vanilla / Arki rose 1-2 Tone

Zabibu Kiasi (Ukipenda)

JINSI YA KUPIKA TAMBI ZAKO

1. Zichambue tambi ziwe moja moja.

2. Mimina mafuta kwenye sufuria yakisha pata moto mimina
tambi,zigeuzegeuze mpaka zibadilike rangi na kuwa brown.

3. Punguza mafuta kwa kuyachuja na zirudishe jikoni.

4. Nyunyizia iliki zilizosagwa koroga kidogo na mimina maji na tia arki
na acha zichemke mpaka maji yakikaribia kukauka mimina sukari
koroga kidogo na punguza moto.
5. Kisha tia zabibu ukipenda, zifunike ili zikaukie vizuri.

6. Zikishakauka pakua kwenye sahani tayari kwa kuliwa

Kidokezi: Itategemea na aina za Tambi unazopika kwa kukisia maji, kama utaona hazijaiva unaweza kuongeza maji kidogo.

Jinsi ya kupika Biriani Ya Nyama Mbuzi Ya Mtindi Na Zaafaraan

Vipimo – Nyama

Nyama mbuzi – 1 kilo

Kitunguu menya katakata – 1

Nyanya/tungule – 2

Thomu (kitunguu saumu/garlic) saga – 5 chembe

Tangawizi mbichi – kuna/grate au saga – 1 kipande

Pilipili mbichi saga – 2

Bizari ya pilau nzima (cumin seeds) – ½ kikombe cha kahawa

Mdalasini – 1 kijiti

Karafuu nzima – 5 chembe

Gilgilani/dania (coriander seeds) – ½ kikombe cha kahawa

Bizari ya mchuzi – 1 Kijiko cha supi

Chumvi – Kiasi

Mtindi – 1 glass

Hiliki ilopondwa – 2 vijiko vya chai

Vitunguu – menya katakata slices kwa ajili ya kukaanga- 7- 9

Mafuta – Kiasi ya kukaangai vitunguu

Vipimo – Wali

Mchele wa pishori/basmati – 4 glass

Zaafarani roweka katika kikombe cha kahawa – Kiasi

Mafuta – Kiasi

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Katika sufuria, changanya nyama pamoja, kitunguu kimoja, tangawizi, thomu, nyanya, na viungo vyake isipokuwa mtindi, hiliki na vitunguu vilobakia.

Tia maji kisha funika ichemke mpaka iwive nyama na ikauke supu.

Tia mtindi na hiliki changanya pamoja.

Weka mafuta katika karai, kaanga vitunguu mpaka viwe rangi ya hudhurungi. Toa uchuje mafuta. Kisha viponde ponde kwa mkono uchanganye na nyama.

Chemsha mchele uive nusu kiini, mwaga maji.

Mimina katika nyama utie zaafarani, funika upike wali hadi uwive.

Epua ukiwa tayari.

Jinsi ya kupika Wali Wa Samaki Na Mboga

VIPIMO VYA SAMAKI

Samaki wa sea bass vipande – 1 1/2 LB (Ratili)
Kitunguu saumu(thomu/galic) -1 Kijiko cha supu
pilipili mbichi iliyosagwa – 1 Kijiko cha chai
Bizari ya manjano au ya pilau – 1/2 Kijiko cha chai
Paprika ya unga au pilipili ya unga – 1 kijiko cha chai
Chumvi – Kiasi
Ndimu
Mafuta – 3 Vijiko vya supu

NAMNA YA KUTAYARISHA NA KUPIKA

Roweka samaki kwa viungo hivyo vyote kwa muda wa robo saa hivi.

Washa oven moto wa 400F.
Kisha weka samaki katika trea na choma kwa muda wa dakika 15 na weka moto wa juu dakika za mwisho ili ipate rangi nzuri.
Ikishaiva epua na itakuwa tayari kuliwa.

VIPIMO VYA MBOGA

Gwaru (green beans) – 1 LB
Kitunguu saumu(thomu/galic) – 1 kijiko cha supu
Karoti – 4-5
Chumvi – Kiasi
Bizari ya manjano – 1/2 Kijiko cha chai
Pilipili manga – 1/4 kijiko cha chai
Mafuta ya zaituni – Kiasi

NAMNA YA KUTAYARISHA NA KUPIKA

Kata kata karoti na toa sehemu ya mwisho za binzi.
Weka mafuta katika sufuria kisha kaanga karoti na gwaru
Kisha weka moto mdogo na funika ili ziwive na sio kuvurujika.
Karibu na kuiiva tia thomu kaanga kidogo,tia bizari ,chumvi na pilipili manga.
Ikisha changanyikana vizuri epua na tayari kuliwa na wali na samaki.

Shopping Cart
23
    23
    Your Cart
    🏠 Home 📖 Reading 🖼️ Gallery 💬 AI Chat 📘 About