Dondoo za Mapishi na Lishe

Mapishi ya Ugali Kwa Mchuzi Wa Kamba Wa Nazi, Kisamvu Na Kachumbari Ya Papa Mkavu

Vipimo – Ugali

Maji – 4 vikombe kiasi inategemea na unga wenyewe.

Unga wa sembe – 2 vikombe

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Tia maji kiasi katika sufuria, weka motoni, yakipata moto korogea unga wa sembe kiasi na ufanye uji mzito uache uchemke vizuri huku ukikoroga.
Chota kibakuli kimoja cha uji huo weka pembeni kisha mimina unga wote uliobaki upigepige uchanganyike vizuri kwenye uji huo mpaka ushikamane
Punguza moto anza kuusonga taratibu huku ukiongeza ule uji ulioweka pembeni kidogo kidogo mpaka uone sasa umeshikamana vizuri.
Endelea kusonga mpaka ulainike kisha mimina kwenye bakuli au sahani iliyolowanishwa na maji kisha upete pete huku ukiugeuza geuza mpaka ukae shepu nzuri ya duara.Weka tayari kwa kuliwa.

Vipimo – Mchuzi wa kamba wa nazi

Kitunguu – 1

Nyanya – 2

Kamba waliomenywa – 1 Kilo

Pilipili mbichi iliyosagwa – ½ kijiko cha chai

Kitunguu saumu na tangawizi ilivyosagwa – 1 kijiko cha supu

Nazi nzito iliyochujwa – 1 kikombe

Bizari ya mchuzi – ½ kijiko cha chai

Chumvi – Kiasi

Ndimu – Nusu

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Safisha na osha kamba vizuri kisha mtie katika sufuria. Katia kitunguu, nyanya, tia chumvi, pilipili mbichi ya kusaga, thomu na tangawizi, bizari ya mchuzi na ndimu. Tia maji kidogo kiasi acha ichemke.
Watakapoiva na karibu kukauka, mimina tui la nazi taratibu koroga kiasi
Punguza moto aacha ichemke kidogo ukiwa mchuzi tayari.

Vipimo – Kisamvu

Kisamvu – 2 vikombe

Kunde mbichi zilizochemshwa – 1 kikombe

Kitunguu – 1

Nazi nzito iliyochujwa – 1 vikombe

Chumvi – Kiasi

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Weka kisamvu katika sufuria, katia kitunguu, tia chumvi, maji kidogo acha kichemke.
Huku ikichemka mimina kunde mbichi zilizochemshwa acha zipikikie kidogo mpaka kisamvu kikaribie kukauka na kunde kuiva.
Mimina nazi nzito punguza moto acha ichemke kidogo, mimina kwenye bakuli tayari kwa kuliwa.

Vipimo – Kachumbari Ya Papa

Papa mkavu (au nguru) – kipande

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Muoshe papa vizuri atoke mchanga kisha mchome kwenye jiko la mkaa au unaweza kumtia kwenye treya kisha kwenye oven kwa moto wa 350 kwa dakika 15 mpaka 20.
Akikauka mchambue chambue weka kando.
Tengeneza kachumbari, kwa kukata kitunguu, nyanya na pilipili mbichi, tia ndimu na chumvi.
Changanya na papa mkavu uliyemchambu ikiwa tayari.

MAANA YA MANENO YANAYOTUMIKA KATIKA MASUALA YA LISHE

1. Chakula

ni kitu chochote kinacholiwa au kunywewa na kuupatia mwili virutubishi mbalimbali Chakula huupatia mwili nguvu, kuulinda na kuukinga dhidi ya maradhi mbalimbali .Mfano wa chakula ni ugali, wali, maharagwe, ndizi, viazi, mchicha, nyama, samaki.

2. Lishe

ni mchakato unaohusisha hatua mbalimbali za jinsi mwili unavyokitumia chakula kilicholiwa, hatua hizi ni kuanzia chakula kinapoliwa, jinsi mwili unavyokisaga na kukiyeyusha, umetaboli, na hatimaye virutubishi kufyonzwa na kutumika mwilini.

3. Virutubishi

ni viini vilivyoko kwenye chakula ambavyo vinauwezesha mwili kufanya kazi zake, karibu vyakula vyote huwa na kirutubishi zaidi ya kimoja ila hutofautiana kwa kasi na ubora. Kila kirutubishi kina kazi yake mwilini na mara nyingi hutegemeana ili viweze kufanya kazi yake kwa ufanisi. Hakuna chakula kimoja chenye virutubishi vya aina zote isipokuwa maziwa ya mama kwa miezi sita ya mwanzo ya maisha ya mtoto, ni mhimu kula vyakula vya aina mbalimbali ili kuwezesha mwili kupata virutubishi mchanganyiko vinavyohitajika.

4. Mlo kamili

ni ule ambao hutokana na chakula mchanganyiko kutoka katika makundi yote ya chakula na una virutubishi vyote muhimu kwa ajili ya lishe na afya bora. Mlo huu unapoliwa kwa kiasi cha kutosha kulingana na mahitaji ya mwili angalau mara tatu kwa siku huupatia mwili virutubisho vyote muhimu.

5. Ulaji unaofaa

hutokana na kula chakula mchanganyiko na cha kutosha (mlo kamili) ili kukidhi mahitaji ya mwili. Ulaji unaofaa pia huzingatia matumizi ya kiasi kidogo cha chumvi, mafuta, sukari, ulaji wa nyama nyekundu kwa kiasi kidogo. Ni muhimu kuzingatia ulaji wa mboga mboga, matunda, na vyakula vya jamii ya kunde kwa wingi ili kudumisha uzito wa mwili unaotakiwa na kupunguza magonjwa yasiyo ya kuambukiza.

6. Nishati- lishe

ni nguvu inayopatikana baada ya virutubishi (kabohaidreti, mafuta) kuvunjwa vunjwa mwilini. Mwili huitumia nguvu hiyo kufanya kazi mbalimbali Kama kulima, kutembea, kupumua, kuziweka seli za mwili katika hali inayotakiwa n.k.

7. Kalori au kilo kalori

ni kipimo kinachotumika kupima nishati -lishe

8. Makapi mlo

ni sehemu ya chakula ambayo mwili hauwezi kuyeyusha lakini ni muhimu katika uyeyushwaji wa chakula. Mfano wa vyakula venye makapi mlo kwa wingi ni mboga za majani, matunda( maembe, machungwa, mapera, machenza, mafenesi, unga usiokobolewa( dona) na vyakula vya jamii ya kunde.

9. Lehemu

ni aina ya mafuta yanayopatikana hasa kwenye vyakula vya asili ya wanyama na pia hutengenezwa mwilini. Lehemu inayotokana na vyakula ikizidi mwilini huleta madhara ya kiafya. Vyakula venye lehemu kwa kiasi kikubwa ni pamoja na maini, figo, mayai, nyama iliyonona kama nundu, nyama ya nguruwe yenye mafuta, mkia wa kondoo, samli, siagi, ngozi ya kuku n.k.

10. Utapiamlo

ni hali ya kupungua au kuzidi kwa baadhi ya virutubishi mwilini ambapo husababisha lishe duni au unene uliozidi.

11. Antioxidants

ni viini ambavyo vina uwezo wa kukinga seli za mwili zisiharibiwe na chembe chembe haribifu (free radicals) ambazo huweza kusababisha saratani. Viini hivyo huungana na chembechembe hizo haribifu na kuzidhibiti ili zisisababishe madhara. Mifano ya antioxidants ni pamoja na beta-carotene, lycopene, vitamin C, E, na A.

Mapishi ya Ugali na dagaa

Mahitaji

Dagaa (dried anchovies packet 1)
Unga wa ugali (corn meal flour 1/4 kilo) (unaweza kutumia unga wa choice uipendayo)
Nyanya ya kopo (tin tomato 1/2)
Kitunguu maji (onion 1)
Limao (lemon 1/4)
Pilipili mbuzi nzima bila kukata (scotch bonnet pepper1, do not chop)
Chumvi (salt 1/4 ya kijiko cha chai)
Mafuta (vegetable oil)
Hoho (green pepper)

Matayarisho

Chambua dagaa kwa kutoa vichwa vyao na utumbo, baada ya hapo waloeke katkika maji ya moto kwa muda wa dakika 5 na uaoshe tena katika maji ya baridi na uwakaushe uwaweke pembeni. Ukishamaliza katakata kitunguu na uandae nyanya tayari kwa upishi. Bandika sufuria ya kupikia dagaa jikoni na utie mafuta, yakishapata moto tia vitunguu pamoja na dagaa. Kaanga mpaka dagaa wawe light brown kisha tia nyanya, chumvi na pilipili. Pika nyanya mpaka ziive (ukitaka kujua kama nyanya zimeiva utaona zinatengana na mafuta) Baada ya hapo kamulia limao kidogo sana na tia pilipili hoho na zipike kama dakika mbili. kisha ipua.
Ukisha maliza kupika dagaa andaa chungu cha ugali. Kwanza unatakiwa kuchemsha maji ya moto, kisha koroga pembeni unga kiasi katika maji ya baridi na utie kwenye maji yanayochemka, Fanya kama unatengeneza uji, uji wa ugali ukishachemka tia unga na uanze kuusonga mpaka ugali uive. Ukisha iva pakua na usevu na mboga tayari kwa kuliwa.

Mchemsho wa samaki na viazi

Mahitaji

Samaki mbichi (1)
Viazi mbatata (3)
Nyanya (1)
Kitunguu maji
Limao
Kitunguu saumu
Tangawizi
Chumvi
Pilipili
Vegetable oil

Matayarisho

Safisha samaki kisha mmarinate na tangawizi, kitunguu swaum, chumvi na limao kwa muda wa masaa mawili. Baada ya hapo menya viazi na uvikate vipande vidogo kisha vioshe na viweke kwenye sufuria yenye maji kiasi kwa ajili ya kuvichemsha. Viinjike jikoni na uviache vichemke kwa dakika 7. Vikisha chemka tia samaki, katia kitunguu,pilipili, chumvi, limao, vegetable oil na nyanya na uache supu ichemke mpaka samaki na viazi vitakapoiva. baada ya hapo supu itakuwa tayari kwa kuliwa.

Jinsi ya kupika Biriani ya Nyama Ng’ombe Na Mtindi

Mahitaji

Mchele wa biriani – 5 gilasi

Nyama ya ngombe ya mifupa – 1 ½ kilo na nusu

Vitunguu – 2 kilo

Tangawizi mbichi – ¼ kikombe

Thomu (saumu/garlic) – 3 vijiko vya supu

Mtindi – 2 vikombe

Nyanya ilokatwakatwa (chopped) – 3

Nyanya kopo – 1 kikombe

Masala ya biriani – 2 vijiko vya supu

Hiliki ya unga – 2 vijiko vya chai

Pilipili mbichi ilosagwa – 3 kiasi

Kotmiri ilokatwakatwa – 1 msongo (bunch)

Rangi ya biriani ya manjano – ½ kijiko cha chai

Zaafarani au zaafarani flavour – 1 kijiko cha supu

Mafuta ya kukaangia

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Katakata vitunguu ukaangae katika mafuta mpaka vigeuke rangi ya brown ilokoza.
Weka nyama iwe ilokatwakatwa katika treya au bakuli kubwa la oveni.
Chaganya pamoja na tangawizi, thomu, nyanya, nyanya kopo, mtindi, masala ya biriani, chumvi, pilipili.
Acha irowanike kwa muda wa masaa mawili takriban.
Funika kwa karatasi ya jalbosi (foil paper) utie katika oveni upike muda wa dakika 45 takriban mpaka nyama iwive na huku unachanganya changanya sosi. Ikiwa ina maji ongezea nyanya kopo iwe nzito.
Epua funua, kisha vuruga vitungu umwagie pamoja na kotmiri na umwagie mafuta ya moto kiasi.
Ongezea kutia masala ya biriani na hiliki ya unga.
Chemsha mchele nusu kiini, mwaga maji chuja, umwagie juu ya sosi ya nyama ukipenda kuchanganya au chemsha wali pekee.
Nyunyizia rangi ya biriani pamoja na zaafarani flavour au zaafarani yenyewe ukipenda.
Mimina mchele juu ya masala ya nyama, funika urudishe ndani ya oven upike muda wa kiasi ya dakika ishirini.
Epua upake kwa kuchota wali kwanza kisha masala uwekee juu yake, kiwa tayari.

Mapishi ya Kachori

Mahitaji

Viazi mbatata (potato 4 vya wastani)
Nyama ya kusaga (mince beef 1 kikombe cha chai)
Kitunguu (onion 1 cha wastani)
Carrot 1
Hoho (green pepper 1/2)
Kitunguu swaum (garlic)
Tangawizi (ginger )
Binzari nyembamba (ground cumin 1/2 kijiko cha chai)
Binzari manjano (turmeric 1/2 kijiko cha chai)
Curry powder 1/2 kijiko cha chai
Limao (lemon 1/2)
Pilipili ya unga (chilli powder 1/2 kijiko cha chai)
Giligilani (coriander kiasi)
Chumvi (salt)
Mafuta (vegetable oil)
Unga wa ngano kiasi

Matayarisho

Katakata vitunguu na hoho katika vipande vidogo vidogo na kisha kwangua carrot na uweke pembeni. Chemsha viazi na chumvi kidogo vikiiva viponde na uviweke pembeni, Baada ya hapo tia nyama limao, chumvi, kitunguu swaum na tangawizi ichemshe mpaka iive na uhakikishe maji yote yamekauka. Kisha Tia binzari zote, pilipili, curry powder, giligilani, vitunguu, hoho na carrot. Pika mchanganyiko huo kwa muda wa dakika 3 na kisha ipua. Baada ya hapo changanya na viazi kisha tengeneza maduara ya kiasi na uyaweke pembeni. Chukua unga wa ngano kiasi na uchanganye na maji kupata uji usiokuwa mzito au mwepesi sana. baada ya hapo chovya madonge katika huo uji na uyachome katika mafuta. Hakikisha zinaiva na kuwa rangi ya brown na hapo zitakuwa tayari kwa kuliwa.Unaweza ukazisevu na chatney yoyote unayopendelea.

Mapishi ya wali kuku wa Kisomali

Mahitaji ya wali

Mchele – 3 vikombe

Vitunguu (viliokatwa vidogo vidogo) – 2

Mafuta – 3 vijiko vya supu

Kitunguu saumu(thomu/galic) na tangawizi iliyosagwa – 1 kijiko cha chai

Bizari ya pilau – 1 kijiko cha supu

Mdalasini – 1 kijiti

Hiliki – 3 chembe

Pilipili manga nzima – chembe chache

Siagi – Vijiko 2 vya supu

Chumvi – kiasi

Mahitaji kwa kuku

Kuku kidari (Breast) kata vipande vipande – 2 LB

Mafuta – 3 vijiko vya supu

Kitunguu saumu(thomu/galic) na tangawizi iliyosagwa – 1 kijiko cha supu

Pilipili mbichi iliyosagwa – 1 kijiko cha supu

Kotmiri iliyokatwa ndogo ndogo – kiasi

Bizari ya pilau (cummin au jiyrah) – 1 kijiko cha chai

Pilipili kubwa tamu la kijani – 1

Pilipili kubwa tamu nyekundu – 1

(zikate vipande vipande)

Karoti iliyokunwa – 1 – 2

Chumvi – Kiasi

Mapishi ya Wali:

Roweka mchele kwa muda fulani kutegemea mchele
Katika sufuria tia mafuta na kaanga vitunguu hadi vibadilike rangi kidogo.
Tia thomu iliyosagwa, mdalasini, bizari ya pilau, hiliki, pilipili manga na chumvi, kaanga kidogo.
Tia mchele kaanga kidogo, kisha tia maji ya moto kiasi kutegemea na aina ya mchele kama kawaida ya kupika wali kama pilau.
Tia sigai, funika upikike wali hadi uwive.

Mapishi ya Kuku:

Mchanganye kuku pamoja na thomu/tangawizi iliyosagwa, chumvi, pilipili mbichi.
Katika karai tia mafuta yapate moto vizuri.
Mtie kuku, bizari ya pilau (jiyrah) na ukaange, karibu na kuiva tia vitunguu.
Tia mapilipili makubwa, kotmiri, na kaanga kwa dakika moja tu uzime moto na epua weka kando.

Jinsi ya kutengeneza juisi ya nyanya

Viamba upishi

Nyanya 1 kg
Maji Iita ½
Chumvi kijiko kidogo 1
Sukari

Hatua

• Osha nyanya, katakata na chemsha na maji mpaka zilainike.
• Chuja juisi.
• Pima juisi – vikombe 2 vya juisi kwa kikombe 1 cha sukari, weka
kwenya sufuria safi .
• Ongeza chumvi, chemsha ukikoroga mpaka ichemke.
• Mara ikichemka epua, pozesha na weak kwenya chombo safi kwa
kunywa.

Mapishi ya Supu ya makongoro

Mahitaji

Makongoro (miguu ya ng’ombe) kiasi
Limao 1 kubwa
Kitunguu swaum
Tangawizi
Chumvi
Pilipili

Matayarisho

Safisha makongoro kisha yatie kwenye pressure cooker. Kisha tia kitunguu swaum, tangawizi, chumvi,limao na maji kiasi. Baada ya hapo yachemshe mpake yaive na yawe malaini na pia ubakize supu kiasi inaweza kuchukua kama dk 45 au saa 1 hivi. Baada ya hapo yaipue na upakue supu yako kwenye bakuli katia pilipili kiasi kisha itakuwa tayari kwa kuliwa.

Note:
Ukiwa unanunua makongoro hakikisha unachukuwa yale yasiyokuwa na manyoya na pia
hakikisha usiyachemshe kupitiliza kwani yakiwa malaini sana utashindwa kuyaenjoy.

Mapishi ya tambi za kukaanga

Kupika tambi ni kama ifuatavyo

VIAMBA UPISHI

Tambi pakti moja

Sukari ¾ kikombe cha chai

Mafuta ½ kikombe cha chai

Iliki kiasi

Maji 3 Vikombe vya chai

Vanilla / Arki rose 1-2 Tone

Zabibu Kiasi (Ukipenda)

JINSI YA KUPIKA TAMBI ZAKO

1. Zichambue tambi ziwe moja moja.

2. Mimina mafuta kwenye sufuria yakisha pata moto mimina
tambi,zigeuzegeuze mpaka zibadilike rangi na kuwa brown.

3. Punguza mafuta kwa kuyachuja na zirudishe jikoni.

4. Nyunyizia iliki zilizosagwa koroga kidogo na mimina maji na tia arki
na acha zichemke mpaka maji yakikaribia kukauka mimina sukari
koroga kidogo na punguza moto.
5. Kisha tia zabibu ukipenda, zifunike ili zikaukie vizuri.

6. Zikishakauka pakua kwenye sahani tayari kwa kuliwa

Kidokezi: Itategemea na aina za Tambi unazopika kwa kukisia maji, kama utaona hazijaiva unaweza kuongeza maji kidogo.

Mapishi ya Borhowa

Mahitaji

Daal (lentils) nyekundu au/na kijani – 1 Kikombe kikubwa

Bizari ya manjano ya unga – 1/2 Kijiko cha chai

Pili pili ya unga – 1/2 kijiko cha chai

Chumvi – Kiasi

Maji ya ndimu – 3 Vijiko vya supu

Kitunguu – 1 kiasi

Kitunguu saumu(thomu/galic) – 1 Kijiko cha chai

Bizari ya unga (cummin powder) – 1 Kijiko cha chai

Mafuta ya kukaangia – Kiasi

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Safisha daal kwa kutoa mawe ikiwa yapo, kisha osha na roweka dakika 15 hivi.
Kisha chemsha kwa kutia maji, bizari ya manjano, chumvi, pili pili ya unga na maji ya ndimu hadi iive na kuvurujika.
Halafu chukua kisufuria na kaanga kitungu, kisha thomu na mwisho tia bizari ya pilau.
Kisha mimina mchanganyiko wa kitunguu kwenye sufuria ya daal (iliyokwisha iiva)na uchanganye na iwache motoni kidogo itokote.
Ukipenda mimina mchanganyiko kwenye blenda na usage mpaka iwe laini.
Tia kwenye bakuli na itakuwa tayari kuliwa na wali na samaki ukipenda

Jinsi ya kutengeneza Keki Ya Mbegu Za Mchicha

Viamba upishi

Unga ngano vikombc 3
Unga mbegu za mchicha kikombe 1
Baking powder vijiko vidogo
Maziwa kikombe 1
Sukari kikombe 1
Blue band kikombe ½
Mayai 10-12

Hatua

• Chagua, osha, kausha mbegu za mchicha mweupe, kisha saga zilainike.
• Chekecha unga wa ngano, unga wa mbegu za mchicha na baking powder Kwenye bakuli kubwa.
• Ongeza sukari na changanya.
• Ongeza mayai kidogo, kidogo ukikoroga na mwiko kwenda njia moja mpaka ilainike.
• Kama rojo ni zito ongeza mayai, au maziwa ili iwe laini, ongeza vanilla na koroga.
• Paka mafuta kwenye chombo cha kuoka au sufuria na chekechea unga kidogo.
• Mimina rojo ya keki na oka kwenye oveni au kama ni sufuria funika, weka moto mwingi juu, chini weka moto kidogo.
• Ukinusia harufu nzuri ya vanilla, funua, choma kisu katikati ya keki, kama ni kavu epua, pozesha na pakua kama kitafunio.

Mapishi ya Kidheri – Makande

Mahitaji

Nyama (kata vipande vidogodogo) – ½ kilo

Maharage – 3 vikombe

Mahindi – 2 vikombe

Kitunguu – 1

Nyanya – 2

Kabichi lililokatwa – 2 vikombe

Kitunguu saumu(thomu/galic) – 1 kijiko cha chai

Vidonge vya supu – 2

Chumvi – kiasi

Mafuta -1au 2 vijiko vya chakula

Namna Yakutayarisha

Chemsha mahindi mpaka yawive na maji yakauke kiasi.
Chemsha maharage pembeni nayo mpaka yawive na maji yakaukie kiasi.
Tia mafuta kwenye sufuria anza kukaanga vitunguu , thomu na vidonge vya supu koroga kiasi.
Kisha mimina nyama iliyokatwa vipande acha ikaangike kidogo na chumvi.
Nyama ikishakaangika tia nyanya funika kwa moto mdogo mpaka nyama iwive.
Kisha mimina mahindi na maharage yaliyochemshwa na maji yake kiasi koroga mpaka ichanganyike na mwisho mimina kabichi funikia mpaka kabichi iwive onja chumvi kama imekolea
Halafu malizia kukoroga mpaka ichanganyike na ikaukie kisha pakua kwenye sahani tayari kwa kuliwa.

Mapishi ya Wali Wa Kukaanga Kwa Kidari Cha Kuku (Chicken Breast) Wa Kukausha

Viambaupishi

Vipimo vya Wali:

Mchele 3 vikombe

*Maji ya kupikia 5 vikombe

*Kidonge cha supu 1

Samli 2 vijiko vya supu

Chumvi kiasi

Hiliki 3 chembe

Bay leaf 1

Viambaupishi: Kuku

Kidari (chicken breast) 1Kilo

Kitunguu 1

Tangawizi mbichi ½ kipande

Kitunguu saumu(thomu/galic) 7 chembe

Pilipili mbichi 3

Ndimu 2

Pilipilimanga 1 kijiko cha chai

Mdalasini ½ kijiko cha chai

Jira/Cummin ya unga 1 kijiko cha chai

Maji ¼ kikombe

Jinsi ya kuandaa na kupika

Wali:

Osha na roweka mchele kisha weka sufuria katika moto tia samli ipashe moto.

Tia hiliki, bay leaf, kaanga, kisha tia mchele ukaange kidogo.

Tia maji, chumvi na kidonge cha supu, upike wali kama unavyopika pilau.

*Maji kisia kwa kutegemea mchele ulivyo.

  • Unaweza kutumia supu yoyote badala ya kidonge.

Kuku:

Katakata kidari cha kuku vipande vya kiasi, weka katika sufuria, tia ndimu, bizari zote, chumvi.

Katakata kitunguu vipande vidogodogo, pilipili, na kitunguu thomu (chopped), tia katika kuku.

Chuna tangawizi mbichi tia katika kuku. Changanya vitu vyote vizuri.

Tia maji kiasi ¼ kikombe tu kiasi cha kumkaushia kuku. Weka katika moto mpike huku unageuzageuza. Anapokaribia kukauka epua akiwa tayari kuliwa na wali (na saladi upendayo)

Mapishi ya samaki aina ya salmon

Wakati mwingine mtu unakuwa umechoka na usingependa kupoteza muda jikoni, so mlo wa chapchap unakuwa ni wazo zuri, Mlo huu ni rahisi kuuanda na hata haikuchukui zaidi ya dakika ishirini chakula kinakuwa tayari mezani.

Mahitaji

Salmon fillet 2
Potatao wedge kiasi
Lettice kiasi
Cherry tomato
Limao 1
Swaum
Chumvi
Olive oil

Matayarisho

Mmarinate samaki na chumvi, swaum na nusu ya limao kisha muweke pembeni, baada ya hapo washa oven kisha tia potato wedge zikisha karibia kuiva anza kumpika samaki, tia mafuta kidogo sana kama kijiko kimoja cha chai hivi katika frypan isiyoshika chini yakisha pata moto kiasi muweke samaki wako (upande wenye ngozi chini kwanza) Mpike mpaka uone rangi ya kahawia kwa chini kisha mgeuze upande wa pili, uku samaki wako akiwa anaendelea kuiva, tayarisha salad yako kwa kusafisha lettice na nyanya kisha zichanganye pamoja kisha tengeneza salad dressing pembeni , kamua limao kisha tia olive oil na chumvi kidogo, Baada ya hapo samaki na potato wedge vitakuwa vimeiva, andaa mlo wako na utakuwa tayari kwa kuliwa.

Mapishi ya Pilau Ya Nyama Na Mtindi

MAHITAJI

Nyama iliyokatwa vipande – 1 Ratili(LB)

Mchele Basmati – 2 Magi

Chumvi ya wali – kiasi

Kitungu kilichokatwa katwa – 1 kikubwa

Kitunguu saumu(thomu/galic) na tangawizi – 1 kijiko cha supu

Mtindi (yogurt) – ½ kikombe

Mchanganyiko wa bizari ya pilau ya tayari – 2 vijiko vya supu

Mafuta kidogo yakukaangia

Rangi ya manjano (ukipenda)

NAMNA YA KUTAYARISHA NA KUPIKA

Osha mchele na roweka nusu saa .

Weka mafuta katika sufuria na kaanga vitungu mpaka viwe rangi ya hudhurungi (brown).

Tia thomu na tangawizi na ukaange kidogo.

Kisha weka bizari ya pilau halafu nyama huku unakaanga hadi nyama isiwe nyekundu tena.

Tia maji gilasi 1½- 2 ichemke mpaka nyama iwive na karibu kukauka.

Mimina mtindi na iachie moto mdogo ikauke kidogo.

Kwenye sufuria nyingine chemsha mchele pamoja na chumvi na mafuta kidogo mpaka uive.

Mimina wali juu ya nyama, kisha nyunyiza rangi (ukipenda) kama vile wali wa biriani na ufunike kwa dakika kumi hivi.

Changanya wali na nyama pamoja ikiwa tayari kuliwa.

Jinsi ya kuandaa Pilau ya sosi ya soya, nyama na mboga

Mahitaji

Nyama isiyokuwa na mifupa – 1 ½ Lb(ratili)
Mchele wa Basmati (rowanisha) – 3 Magi
Vitunguu maji – 2
Mchanganyiko wa mboga za barafu – 1 Magi
(karoti, mahindi, njegere)
Pilipili Mbichi – 3
Pilipili mboga kijani na nyekundu – 1
Pilipili manga – ½ kijiko cha chai
Chumvi – Kiasi
Sosi ya soya (soy sauce) – 5 Vijiko vya supu
Kitunguu saumu(thomu/galic) na tangawizi iliyosagwa – 1 Kijiko cha supu
Mchanganyiko wa bizari (garam masala) – 1 Kijiko cha supu
Kotmiri iliyokatwa – ½ Kikombe
Mafuta ya kukaangia – Kiasi

Namna Ya Kutaarisha

Ndani ya sufuria, tia mafuta yakipata moto kaanga vitunguu mpaka ziwe rangi ya hudhurungi.
Kisha tia nyama iliyokatwa vipande vidogo vidogo pamoja na maji ya kiasi na viungo vyote isipokuwa mchele, mboga zote na kotmiri. chemsha mpaka nyama iwive na maji yakauke.
Halafu changanya na mboga na iwache kwa muda wa dakika kumi kisha tia kotmiri na umimine kwenye bakuli au treya ya oveni na uweke kando.
Chemsha mchele na chumvi uwive kama kawaida ya kupika wali wa kuchuja, kisha umwagie juu ya ile treya ya nyama.
Nyunyizia mafuta na sosi ya soya na ipike katika oveni moto wa 350° kwa muda wa dakika 20 hivi.
Ukishawiva, uchanganye ukiwa tayari kwa kuliwa

Jinsi ya kupika Mchuzi Wa Ngogwe Na Bamia

Viamba upishi

Ngogwe ½ kg
Kitunguu 2
Bamia ¼ kg
Karoti 2
Mafuta vijiko vikubwa 8
Maji vikombe 3 Mayai 2
Nyanya 2
Chumvi

Hatua

• Osha, menya na katakata nyanya na vitunguu.
• Osha, menya na kata karoti virefu virefu.
• Osha, kata ncha za bamia pande zote na kama ndefu sana kata
vipande viwili.
• Osha, kata vikonyo vya ngongwe, kama ni kubwa kata vipande viwili.
• Kaanga vitunguu, ongeza nyanya, korogoa mpaka zilainike.
• Ongeza ngogwe, karoti, bamia na chumvi, koroga mpaka
zionekane kukolea rojo.
• Ongeza maji vikombe 2 koroga na funikia kwa dakika 10-15 au
mpaka ziive. Punguza moto.
• Koroga mayai kwenye maji mpaka iwe kama maziwa, ongeza
kwenye mboga na koroga polepole usiponde ngogwe wala bamia
kwa dakika 5.
• Onya chumvi, pakua za moto kama kitoweo.

Jinsi ya kupika Mishkaki ya kuku

Kidali cha kuku 1 kikubwa
Swaum,tangawizi 1 kijiko cha chai
Limao 1/2
Pilipili ya unga 1/2 kijiko cha chai
Curry powder 1/2 kijiko
Paprika 1/2 kijiko cha chai
Hoho jekundu 1/2
Hoho la njano 1/2
Kitunguu 1/2
Chumvi
Olive oil

Matayarisho

Katakata kuku ktk vipande vya mishkaki ya kawaida kisha vimarinate na vitu vyote, kasoro hoho na kitunguu.Ni vizuri kuziacha either usiku mzima au kwa masaa machache ili spice ziingie vizuri. Baada ya hapo katakata hoho na vitunguu vipande vya wastani kiasi. Baada ya hapo Taarisha vijiti vya mishkaki kisha tunga nyama pamoja na hoho na vitunguu kisha nyunyuzia mafuta na kisha uzichome kama mishkaki ya kawaida. Itakapoiva itakuwa tayari kwa kuliwa na chochote upendacho kama ndizi za kuchoma, viazi na n.k.

Mapishi ya Biriani Ya Kuku Wa Kuchoma (Grilled)

Mahitaji

Mchele wa Basmati /Pishori – 4 vikombe

Kuku

Vitunguu – 3

Nyanya/Tungule – 2

Tangawizi mbichi ilosagwa – 2 vijiko vya supu

Kitunguu saumu(thomu/galic) kilosagwa – 1 kijiko cha supu

Pilipili mbichi nzima – 3

Ndimu – 2

Garama Masala/bizari mchanganyiko – 1 kijiko cha supu

Haldi/tumeric/bizari manjano – 1 kijiko cha chai

Pilipilu ya unga nyekundu – 1 kijiko cha chai

Mtindi /yoghurt – 3 vijiko vya supu

Mafuta ½ kikombe

Namna Ya Kutayarisha Na Kupika

Osha mchele, roweka.
Safisha kuku vizuri, mkate vipande vya saizi ya kiasi weka katika bakuli.
Katika kibakuli kidogo, changanya tangawizi mbichi, thomu, bizari zote, pilipili nyekundu ya unga, chumvi, mtindi, kamulia ndimu.
Punguza mchanganyiko kidogo weka kando.
Mchanganyiko uliobakia, tia katika bakuli la kuku uchanganye vizuri arowanike (marinate) kwa dakika chache hata nusu saa au zaidi.
Weka kuku katika treya ya kuoka au kuchoma katika oveni kisha mchome (grill) uwe unageuzageuza hadi aive.
Epua, weka kando.
Katakata vitunguu, nyanya/tungule, pilipili boga weka kando.
Katika sufuria ya kupikia biriani, tia mafuta, kaanga vitunguu hadi vigeuke rangi ya hudhurungi (brown).
Tia nyanya na pilipili mbichi, pilipili boga na mchanganyiko uliopunguza awali.
Tia kuku uchaganye vizuri.
Wakati unakaanga vitunguu ili uokoe muda, huku chemsha mchele uive nusu kiini, mwaga maji, chuja.
Punguza masala nusu yake weka kando.
Mimina wali kiasi juu ya masala, kisha mimina masala yaliyobakia kisha juu yake tena mimina wali.
Funika upike katika oveni hadi uive.
Changanya unapopakua katika sahani.

Shopping Cart
🏠 Home 📖 Reading 🖼️ Gallery 💬 AI Chat 📘 About