Mbinu za Kilimo na Ufugaji Kukuongezea Mapato

Jinsi ya kutumia mashonanguo kama dawa ya kuzuia wadudu kwenye mimea

Mashonanguo kwa kiingereza ni Blackjack au kwa kisayansi yanajulikana kama (Bidens
pilosa)
Mashona nguo yanazuia wadudukama vile Vidukari, Siafu, bungo, katapila, chenene (crickets), nyenyere, siafu na inzi weupe.

Jinsi ya Kutayarisha na kutumia mashonanguo

  1. Jaza kikombe kilichojaa mbegu ambazo zimekomaa na maji;
  2. Chemsha kwa dakika kumi au loweka kwenye maji kwa saa ishirini na nne, kisha upooze.
  3. Ongeza lita moja ya maji na kijiko kimoja kidogo cha sabuni;
  4. Kisha unyunyizie mimea.

Matumizi mengine

  1. Mbegu zinaweza kutawanyishwa karibu na vichaka kuvutia mchwa.
  2. Mmea waweza kupondwa au kufikichwa kisha maji yake yatumike kunyunyizia mimea.

Angalizo: Kiasi kingi cha dawa hii chaweza kudhuru baadhi ya maua ya mimea.

Jinsi ya kuandaa mbangimwitu kama Dawa ya magonjwa na ya kuulia wadudu shambani

Mbangi mwitu au kwa kisayansi ni African marigold / (Tagetes erecta) Unazuia Bakteria, fungusi na wadudu kama vile Siafu, bungo pamoja na aina nyingine za wadudu.

Hatua za Maandalizi ya dawa na kutumia

  1. Ponda gramu 100-200 za matawi, mizizi na maua;
  2. Weka lita moja ya maji yaliyochemka;
  3. Loweka kwa masaa ishirini na nne;
  4. Ongeza lita moja ya maji baridi,
  5. Nyunyiza kwenye mimea au mchanga.

Mambo makubwa yanayosababisha kulazimika kulima au kutifua udongo

Kutifua udongo ni jambo la muhimu sana ili kuufanya udongo kuwa bora.

Umuhimu wa kutifua udongo ni kama ifuatavyo
1. Hulainisha udongo ili kuruhusu mizizi ya mimea kupenya kwa urahisi.
2. Kutifua kunaboresha uwezekano wa kupenya kwa nitrogen na oxygen kutoka kwenye hewa.
3. Kunawawezesha viumbe hai waliopo kwenye udongo kufanya kazi zao ipasavyo.
4. Kunasaidia Kuandaa sehemu ya kuwekea mbegu.
5. Kutifua kunauongeza uwezekano wa maji kupenya kwenye udongo na kupunguza uyeyukaji wa maji.
6. Kuchanganya mabaki ya mimea na samadi kwenye udongo

Mambo 5 ya muhimu kuzingatia kuhusu mahali unapotaka kuweka mizinga ya nyuki

Ukitaka kujua kuwa eneo unalotaka kuweka mizinga ya nyuki ni sahihi unatakiwa kuzingatia yafuatayo:

1. Haishauriwi kuweka mzinga shambani au karibu na shamba. Unatakiwa uweke umbali wa mita 150-200 kutoka kwenye mazao au nyumbani. Hii ni Kulingana na hali ya kujilinda ya nyuki wa Afrika

2. Mzinga ni lazima uwekwe sehemu ambayo haitasababisha upotevu wa nyuki wanaporudi kutoka nje ya mzinga. Mfano wasiingie kwenye kundi lisilokuwa lao.

3. Mizinga inatakiwa isiwekwe mbalimbali sana ili kuepusha usumbufu wa kutembea mbali kwa mfugaji wakati anapokagua.

Sifa ya eneo la kuweka mizinga
• Iwe Kimya na mbali ya jumuia kama vile hospitali, shule, na viwanja vya michezo vile vile isiwe karibu na maeneo ya biashara au viwanda.
• Karibu na maji masafi-kandokando ya mto, mabwawa ya samaki, mabeseni ya maji au sehemu ya matone.
• Sehemu ya kuweka mizinga Iwe ni karibu na chakula cha nyukimimea inayochanua, miparachichi, nazi, euculptus, migunga n.k
• Iwe sehemu ambayo ni kavu na isiwe sehemu ya tindiga kwani unyevu unyevu husababisha ugonjwa wa ukungu (magonjwa ya fangasi yaani fungal disease) na pia huzuia utengenezaji mzuri wa asali.
• Mahali pa mizinga pawe mbali na watu waharibifu na iliyojificha kuepuka waharibifu.
• Sehemu ya kuweka mizinga ni lazima iwe inafikika kirahisi kwa kipindi chote cha mwaka ili iwe rahisi kuhamisha nyuki pale inapohitajika.
• Panatakiwa pawe kivuli cha kutosha hasa wakati wa mchana jua linapokuwa kali, na kusiwe na upepo mkali.

4. Mizinga ya nyuki Iwe mbali na mashamba, ambapo dawa za kuulia wadudu zinatumika.

5. Vichaka au wigo unaotenganisha mizinga na kuzuia wavamizi ni muhimu ili kupunguza ukali wa nyuki.

Mambo muhimu ya kuzingatia kwenye ufugaji wa nyuki wa asali

Mtaalamu wa nyuki

Unapohitaji unahitaji kufuga nyuki ni lazima uwe na uelewa wa mzunguko wa maisha ya nyuki. Unapoanza ni lazima uulize mtaalamu wa nyuki, wafugaji wenzako ambao wana uzoefu wa kutosha, au kujiunga katika kikundi cha ufugaji ili apate ufahamu zaidi juu ya ufugaji wa nyuki.

Sehemu salama kwa ajili ya mzinga

Unahitaji kutafuta mahali pazuri, salama, na penye sifa ya kufugia nyuki. Vifaa vyote vikishapatikana kinachofuata ni kuchagua mahali gani pa kuweka mzinga. Hakikisha sehemu hii ni mahali ambapo makundi ya nyuki hukusanyika mara kwa mara.

Uwekaji Bora wa Mizinga

Ukishatafuta ya sehemu ya kuweka mizinga, kinachofuata ni kuandaa mizinga kwa ajili ya kuweka panapotakiwa.

Mambo ya muhimu ya kuzingatia
• Kwanza Safisha mzinga kuondoa uchafu wote, utando wa buibui na aina nyingine za wadudu.
• Kisha Weka chambo kwenye mzinga (maranyingi nta hutumika kama chambo) kwa kuipaka katika kuta za mzinga kwa ndani.
• Halafu Mzinga unaweza kutundikwa kwenye mti, kwenye nguzo, kuweka kwenye jukwaa au kwenye miamba. Hii inategemea wewe mwenyewe anapendelea njia ipi.

Shopping Cart