Author name: SW - Melkisedeck Shine

Usiyoyajua kuhusu pesa haya hapa

Habari za Leo Rafiki yangu wa Muhimu sana. Ni furaha yangu kujua unaendelea vyema sana na majukumu yako.

Ni wakati mwingine tena tunaenda kujifunza pamoja juu ya mambo mbalimbali ili tuweze kufikia mafanikio kila siku. Leo tunakwenda kujifunza kuhusu pesa na utajua mambo mengi sana juu ya pesa.

Ni siri gani ipo ndani ya fedha na wengi hawaijui?

Kwanini watu wengi wanakua matajiri halafu wanapoteza utajiri wao wote na kuwa maskini tena?

Ulishawahi kuona watu maarufu wamekua na pesa nyingi lakini baada ya muda wanapotea na pesa zao zinapotea na kurudi kuwa watu wa kawaida kabisa?

Hujawahi kuona watu wakiuza mashamba ya urithi kwa mamilioni ya pesa na wakabadilisha aina ya maisha wanayoishi lakini baada ya muda pesa zinapotea na wanarudia hali yao ya zamani?

Hujakutana na vijana waliochimba madini wakajikuta wamepata mawe wakawa milionea lakini ghafla baada ya muda Fulani wanarudi kule kule walipokua?

Wengi wakiona hayo utawasikia wanasema pesa za mashamba hazika! Pesa za madini zina mashetani! Ni siri gani ipo kwenye hii pesa?

Inawezekana umeshajiuliza sana maswali haya na hata kuogopa kuwa nayo. Ukaamua kuwa mtu wa kawaida tu kwasababu ya hofu hizi zinazokujia unapofikiri kuwa tajiri kisha uje upoteze pesa zako zote!

Watu wengi wamekuwa na fikra kwamba pesa ni mbaya, zinaharibu watu, zinawafanya watu kuwa wachoyo, zinawafanya watu kuwa na tamaa pamoja na mengine mengi unayoyafahamu.

Ukweli ni kwamba pesa haina tatizo lolote pesa haina shetani wala pepo lolote linaloifanya imharibu mtu anapokuwa nayo nyingi. Pesa sio kiumbe hai. Pesa tunaitumia kununua bidhaa mbalimbali au kulipia huduma tunazozihitaji katika maisha yetu ya kila siku.

Ukweli kuhusu pesa ni huu hapa. Kwanza pesa haimbadilishi mtu bali inamfanya awe Zaidi ya vile alivyokuwa mwanzo yaani kama mtu alikuwa ni mchoyo akipata pesa atakuwa mchoyo maradufu, kama alikua mlevi akipata pesa anazidisha kuwa mlevi Zaidi.

Na wengine wakiwa hawana pesa kuna tabia nyingi wanakuwa nazo ndani zimejificha hawazionyeshi wakishapata pesa zile tabia zinafunguka na kuwa wazi.

Kama mtu alikuwa Malaya akipata pesa ndio utaona anaanza kubadilisha wanawake. Pesa zinabaki kuwa pesa na tabia za mtu zinabakia kuwa tabia za mtu.

Kama mtu alikua mtoaji akipata pesa atakuwa mtoaji Zaidi.
Kama alikua mcha Mungu akipata pesa atakwenda kuabudu Zaidi.
Hivyo pesa sio tatizo watu ndio wenye matatizo ndani yetu.

“Having more money won’t change you as a person. It will, however, magnify
the person you already are.” – Bob Proctor

Huwa napenda kuutumia mfano wa chombo. Watu wengi wanaopata pesa nyingi ghafla na kuzipoteza zote ni kama maji yaliyojaa kwenye ndoo utake kuyaweka yote kwenye kikombe cha chai.

Ukweli ni kwamba kikombe kitajaa lakini yale yaliyobaki yatamwagika yote chini hivyo hivyo na pesa zinazopatikana ghafla ni sawa na kuziweka kwenye kikombe ambacho ni uwezo wa akili yako.

Kama Akili yako bado haijaweza kupangilia milioni ishirini hivyo hata ukipewa leo zote zitapotea na zitabaki kile kiwango ambacho akili yako inaweza kutawala na kuendesha. Hivyo njia sahihi ya wewe kuweza kumiliki mamilioni ya shilingi na kubakia nayo ni kuanza kubadili ufahamu wako. Kuza ufahamu wako kidogo kidogo ili uweze kuendesha utajiri mkubwa. Na hili halitokei ndani ya siku moja ni kadiri unavyojifunza kila siku. Kwa kusoma vitabu na kufanyia kazi yale unayojifunza.

Jambo moja na muhimu la kufanya ni kutokuweka akili yako yote kwenye pesa. Usiweke malengo yako kwenye pesa unapofanya biashara unafanya ili upate pesa lakini siku zote pesa hazikai huwa zinaisha hivyo badala ya wewe kuweka nguvu zako na mawazo yako kwenye pesa weka Zaidi katika kuwasaidia watu kama unauza nguo kazana Zaidi katika kuwafanya watu wafurahie huduma yako pesa zitakuja.

Kama unatoa huduma hakikisha unatoa huduma bora ili kuvutia wateja Zaidi kila siku. Pesa utaziona kwako na zitaongezeka kila wakati.

Wekeza pia muda wako kwenye kutengeneza mifumo mbalimbali ambayo itakuwa inakuingizia pesa bila kuwa na kikomo. Unapotegemea mfereji mmoja wa kipato lazima utabakia pale pale siku zote.

Jambo la muhimu la kufanya ili uweze kubakia juu kwenye mafanikio siku zote ni kujifunza na kujijengea misingi ambayo itakuwezesha wewe usiyumbe na ubakie na utajiri wako.

Kuwa mwaminifu, kua mtoaji, wapende wengine, kuwa muadilifu, usidhulumu mtu, kabla hujafanya lolote angalia lina manufaa gani kwako na kwa wengine.

Nikutakie wakati mwema Asante sana kwa kusoma Makala hii.

FURSA HAIJI MARA MBILI: Jinsi unavyoweza kupata faida au hasara ukitumia Nafasi au fursa uliyonayo

Kwenye maisha fursa moja tu inatosha kabisa
kubadilisha hali yako ya sasa na kukuweka kwenye
kiwango kingine kabisa cha mafanikio.Kuna watu
wengi sana ambao waliwahi kufikiria kuwa maisha
yao yatachukua miaka mingi sana kabla
hayajabadilika na kwa mshangao wao walipoanza
kufanya vitu sahihi wakakutana na mabadiliko
makubwa sana katika maisha yao kwa kupitia
fursa moja tu.

Kufanikiwa kwenye maisha ni matokeo ya kujua
mambo sahihi ya kuyafanya.Ni kama ilivyo wakati
unapotaka kufungua mlango
uliofungwa,unachohitaji ni ufunguo sahihi wa
kutumia na sio vinginevyo.
Ili ufanikiwe lazima uwe mtu mwenye bidii na
ambaye unawathamini watu bila kujali hali zao za
sasa.Ili kutoka hapo ulipo na kwenda kule
unakotaka unahitaji watu wa kukuunganisha na
fursa mpya,kukuonyesha njia nzuri ya kufanya
mambo,wa kukurekebisha na watu ambao
unaweza kujifunza kwao.

Mwaka 2012 mmiliki wa kampuni kubwa ya vifaa
vya michezo ya Modell nchini marekani,bwana
Mitchell Modell alifanya tukio la ajabu sana lililotoa
funzo kubwa la mafanikio katika maisha yetu ya
kila siku.Aliamua kujibadilisha mwonekano wake
kwa kunyoa nywele zake zote na kuweka ndevu
nyingi sana za bandia na pia kuvaa hereni sikio
moja.Kisha baada ya hapo alienda kuomba kazi
kwenye kampuni yake na akaanza kufanya kazi ya
daraja la chini kabisa.
Akiwa ameajiriwa bila watu kujua kuwa ndiye
mmiliki alikutana na wafanyakazi wengi sana wa
aina mbalimbali.Kati ya wafanyakazi katika tawi lile
alikuwepo dada mmoja anayeitwa Angel ambaye
alikuwa ana watoto 3 ila hakuwa anakaa na mume
wake na kwa muda wa miaka 2.Lakini pia,Angel na
watoto wake wamekuwa wanaishi kwenye vibanda
kwani hakuweza kulipia pango kwenye nyumba
nzuri ya kuishi.Gharama zote za
chakula,ada,matibabu na mavazi ya watoto yote
ilikuwa juu yake.
Pamoja na hali yake hiyo,Angel alikuwa ni
mfanyakazi anayewahi kazini kila siku na alikuwa
anafanya kazi kwa bidii sana.Hata wakati wengine
walikuwa wanalamika juu ya mshahara,yeye kazi
yake ilikuwa ni kuwatia moyo na kuwahamasisha
wafanye kazi kwa bidii sana akiamini ipo siku
mambo yatakuwa mazuri.Kila wakati Bwana
Mitchell alipokuwa anamkuta Angel,alikuta
anafanya kazi zake kwa umakini na hata akikuta
anaongea na wenzake basi itakuwa ni kuwatia
moyo na kuwapa hamasa na kuwataka waaache
kulalamika.
Wakati Bwana Mitchell akiwa kama mfanyakazi
mpya alihitaji sana msaada wa kufundishwa jinsi
mfumo unavyofanya kazi na mambo mengine.Kila
mmoja alikuwa hayuko tayari kumfundisha,ila
Angel alikuwa tayari kumfundisha na kumsaidia
hata na kazi ambazo alikuwa hawezi kuzifanya
kutokana na ugeni wake.Na kwa sababu ya ukaribu
wake ndipo alipoweza kumfahamu Angel na
kuyajua maisha yake kwa undani.
Baada ya siku kadhaa za kufanya kazi bila mtu
yoyote kujua kuwa ndiye mmiliki,ndipo alipoamua
kufanya kitu kikubwa kwa Angel.Kwanza
alimpandisha cheo na kumfanya kuwa meneja
msaidizi na kisha alimpa zawadi ya dola laki mbili
na hamsini(Takribani shilingi milioni 500 za
kitanzania) ili aweze kupata nyumba nzuri ya
kuishi.
Baada ya tukio hili kutokea wafanyakazi wengi
sana walijilaumu na walitamani sana kupata fursa
upya kama wangejua kuwa yule alikuwa ni mmiliki.
Ndivyo maisha yalivyo na ndivyo safari ya
mafanikio ilivyo.mara zote huwezi kujua ni wakati
gani fursa kubwa inayohusu maisha yako
itakutokea.Kilichomfanya Angel kufanikiwa ni ile
hali ya kuwa ni mtu ambaye hakuruhusu jambo
lolote limzuie kufanya kazi kwa bidii na kwa ufanisi
kila wakati hata kipindi ambacho maisha yake
yalikuwa magumu.
Mara nyingi unaweza kujikuta katika hali ambazo
zinakatisha tamaa na zinakupa uhalali wa kila
namna wa wewe kuwa mtu wa kulalamika na
kukata tamaa.Hebu fikiria mama wa watoto
watatu,analipwa mshahara mdogo lakini bado
anawahi ofisini na huwa halalamiki.Kuna fursa
nyingi kwenye maisha unazikosa kwa sababu ya
malalamiko juu ya hali inayokuzunguka.Kitu cha
msingi unachotakiwa kujua ni kuwa kulalamikia
kitu au mtu hakuwezi kubadilisha hali yako ya sasa
lakini kufanya kwa bidii kunaweza kufungua fursa
nyingi kubwa katika maisha yako.
Inawezekana kazi unayoifanya ni ndogo
ukilinganisha na ndoto kubwa
uliyonayo,inawezekana mshahara unaolipwa sio
mkubwa kama unavyotaka,inawezekana biashara
yako bado haifanyi vizuri kama mipango yako
ilivyo ama hauna mtaji kiwango
unachotaka.Katikati ya hali hii unachotakiwa
kufanya sio kuanza kulalamika na kukata
tamaa,unatakiwa kuwa kama Angel,weka kiwango
kikubwa cha bidii kwani kwa kufanya hivyo
utakuwa unajifungulia milango mikubwa zaidi
katika maisha yako.
Kuanzia leo fanya maazimio katika maisha yako
kuwa utakuwa mtu wa kufanya kwa bidii kile
ambacho unakifanya hata kama itakuwa kwenye
mazingira magumu,kwani kwa kufanya hivyo
utakuwa unajitengenezea fursa kubwa sana mbele
yako.Ukiamua kuishi kwa mtazamo huu,muda
mfupi sana ujao utafanikiwa.
Kitu kingine cha msingi cha kukizingatia hapa ni
kuwa usidharau watu katika maisha yako.Kati ya
mafumbo makubwa ambayo Mungu ameyafumba
ni kuhusu hatima za watu ambao tunakutana nao
kila siku katika maisha yetu.Hakuna kitu kibaya
kama kumdharau mtu eti kwa sababu anaonekana
kwa wakati huo hawezi kukusaidia
chochote.Jifunze kumuheshimu na kumthamini
kila mtu.
Ilil ufanikiwe katika maisha yako jifunze kuishi
kama Angel,jifunze kuwa na bidii ya kazi hata
katika mazingira magumu lakini pia jifunze
kuthamini kila mtu ambaye unakutana naye-
Kuanzia mdada wa kazi
nyumbani,mlinzi,mfagizi,kondakta wa daladala
hadi dereva wako.Kila mtu ni muhimu na ana
mchango katika maisha yako.Kanuni ya maisha
inasema-“Husiana na watu kama wewe unavyotaka
watu wengine wahusiane na wewe pia”. Kuanzia leo
ishi na kila mtu kama “Mitshell wako” wa
kukuunganisha na fursa kubwa uliyokuwa
unaisubiria.
Sina shaka kuwa fursa yako kubwa iko njiani
inakuja,usikate tamaa.
Kumbuka kuwa ndoto Yako Inawezekana,
See You AT The Top.
©Joel Nanauka

Tabia za kuepuka ili uweze kuwa tajiri

UKIWA NA HIZI TABIA 9, JIANDAE KUFA MASKINI…………
By Kashindi Edson

“Umasikini hauji kwa bahati mbaya kama ubaguzi wa rangi au ukoloni, umaskini hutokana na matendo ya kila siku ya mwanadamu” (Nelson Mandela, R.I.P)

“Kila mtu anataka kufanikiwa, lakini si kila mtu yuko tayari kushika majukumu na wajibu wa kumpeleka kwenye mafanikio”(Mwl Nyerere, R.I.P).

“Kile unahokifanya muda huu ndicho kinachoashiria na kutoa picha kamili ya baadae yako”(Mahatma Gandhi, R.I.P)

“Ukizaliwa maskini sio kosa lako, ila ukifa maskini hilo ni kosa”(Bill Gate, The richest man in the world).

Mwalimu wangu wa chuo aliwahi kuniambia kuwa, “mstari unaomtenganisha maskini na tajiri ni mwembamba sana, kwa hiyo ni rahisi sana kuwa tajiri pia ni rahisi sana kuwa maskini”. Mpaka leo sijaelewa alimaanisha nini.

Watu wote waliofanikiwa katika nyanja mbalimbali za maisha, kwenye uongozi, biashara, kilimo, elimu, siasa, michezo, uandishi, muziki, afya, imani, utangazaji, nk huwa hawana hizi tabia 9 nilizokuandalia leo, kwa hiyo kama una kiu ya mafanikio kwa hicho unachopambania, achana na haya mambo 9 yafuatayo;

1. KUTOKUJARIBU.

Katika kutafuta mafanikio huwa kuna vitu viwili tu vya kuchagua. Tambua kuwa maisha ni vita. “Chagua kufa, au kupambana”. “Siogopi kufa, naogopa kutokujaribu'(Jay Z). Hakuna alie zaliwa anajua, jiamini, jaribu utafanikiwa.

2. KUTOKUJIFUNZA.

Che Guava mpaka anafariki library yake ilikuwa na vitabu zaidi ya 2000, mwenzangu na Mimi sijui hata kama una Biblia au Quran ghetoni kwako. Nkwameh Nkrumah library yake ilikuwa na vitabu zaidia ya 3000, Obama anakuambia kila akiamka asbuhi lazima asome kitu kipya. “JOSEPH=Jifunze, Ona, Soma, Elimika, Pitia, Hamasika.(Prof Jay)

3. WOGA & WASIWASI.

“Tunaweza tukamsamehe mtoto anayeogopa gizani, lakini sio mtu mzima anaeogopa mchana”(Plato, R.I.P). Kitu cha kuogopa katika maisha ni woga wenyewe. Kama hujiamini hutakuja kuwa mshindi katika jambo lolote. Fanya hicho unachofikiria kukifanya kwa moyo wa dhati, kama unaamini ni cha harali na kia manufaa kwako na familia yako, na jamii nzima. Acha tabia ya kuogopa kitu ambacho hakijatokea.

4. KUJILINGANISHA.

Kuna baadhi ya watu, huwa wangetamani kuwa kama watu Fulani. Kuwa wewe pia jiamini. Usitamani kuwa Magufuli, Kassim Majaliwa au Paul Makonda. Kila mtu ni wa pekee na maalumu. Jikubali kwanza afu wengine ndo watakukubali wewe. Weka nguvu kwenye ubora wako na sio kwenye madhaifu yako. Ukijilinganisha sana utakosa furaha ya nafsi maisha yako yote.

*5. KUWEKA VINYONGO.**

“Kuweka chuki na konyongo moyoni ni sawa na kunywa sumu ukidhani atakufa mtu mwingine”. Onesha upendo, sambaza upendo, hayo ndo mafanikio ya kweli.

6. UONGO

“Uongo utakupa ushindi wa siku moja, ukweli utaishi milele”(WEUSI), “Muongo hata akiongoea ukweli usimuamini”(FID Q). Ukiwa muongo huwezi kufanikiwa hata siku moja. “Unaweza ukawadanganya watu, lakini huwezi kuwadanganya watu wote, wakati wote”(Bob Marley). Ukweli kama jua, katika safari ya mafanikio huwezi kuvificha.

7. UVIVU & UZEMBE

“Nyumba yenye njaa ukisizi unapata zero”(Fid Q). Mafanikio huja kwa kupenda unachokifanya. Neno “kazi” katika biblia limeandikwa mara 600. Dangote analala masaa 3 tu kila siku, Mohammed Dewj anaamka saa 11 asbuhi kila siku. We kwepa majukumu tu, kesho utakula magodoro. “Uvivu unalipa muda huu, bidii & juhudi vinalipa baadae”.

8. STAREHE & ANASA KUPINDUKIA

Pombe, sigara, ngono, unga, bange, shisha, cocaine, nk vitu vibaya sana. Ni ngumu sana kufikia mafanikio makubwa kama una tabia kama hizi. “Sisi ni kile tunacho kula”. Mafanikio ya kwanza huanzia kwenye afya yako”. Afya ni utajiri. Pia starehe hupoteza muda sana. “Mavuno ya uzee, ni swaga za ujana, kwa ukila ujana kumbuka kula kiungwana”(Nikki Mbishi,).

9. LAWAMA & UMBEA

“Watu wenye uwezo mkubwa wa kufikiria hujadili kuhusu mawazo, uwezo wa kati hujadili kuhusu matukio na wale wenye uwezo wa chini, hujadili kuhusu watu” We upo kwenye kundi gani? Bora ukawa kundi la kati kuliko hilo la chini kabisa, hilo ni la “wachawi”. Tusilamike, tupambane,lawama hazisaidii chochote.Ukiweka malengo yako, vizuri na ukaacha hizo tabia hapo juu, muda si mrefu itazifikia ndoto zako

Mambo 13 katika pesa ambayo unapaswa kuzingatia

1. Usikope pesa ya riba ili uanzishe biashara.
Usitegemee pesa ya mkopo kuianzishia biashara, upate faida kisha uirudishe pesa ya mkopo na riba yake.

2. Usitumie pesa ambayo bado haipo mikononi mwako.
Wala usije ukamuahidi mtu kumpa pesa ambayo umeahidiwa mahali fulani.

Kama kuna mtu kakwambia, Flan njoo kesho nikulipe deni lako- Basi ww usiende kukopa vitu dukani au kumuahidi mtu mwingine kumpa pesa ambayo na ww umeahidiwa

3. Kama unataka kuhifadhi/kutunza pesa, kila unapopata pesa usianze kuitumia kwanza kisha ukategemea kutunza kiasi kitakachosalia.

Hivyo basi, ukipata tu pesa, weka pembeni kiasi unachodhani kinafaa kutunzwa/kuhifadhiwa kisha tumia kiasi kilichobaki.

4. Ukipata nafasi ya kuonana na mtu tajiri, kamwe usiombe pesa.
Omba maarifa ya kutengeneza pesa kama yeye, tena kwa mtaji mdogo.

Maarifa ndio mtaji wa kwanza.
Unaweza kupewa/kusaidiwa pesa iwapo una mawazo mazuri ya kuzalisha pesa. Baadhi husema, “Omba ndoano, usiombe samaki”

5. Usitunze mbegu badala ya kuipanda.
Watu wengi hufurahia pesa wanayolipwa/kuipata kisha wanaiweka bank au nyumbani bila kuiwekeza.
Wekeza pesa ili uzalishe zaidi. Usiogope kuingia hasara, kila aliefanikiwa alipoteza kwanza kabla hajafanikiwa.Wengi walipoteza muda, pesa, afya na hata matumaini ya kufanikiwa, ila kwa uthubutu wao, mwisho wa siku walifanikiwa”

6. Kamwe usimkopeshe mtu pesa ambayo unahisi hatorudisha.

Unapomkopesha mtu huyo pesa, jiridhishe mwenyewe moyoni kuwa kama hatoweza kulipa basi deni lake-halitoathiri urafiki wenu. Ukihisi kwamba kushindwa kwake kulipa kunaweza kuathiri urafiki wenu, basi mshauri aende bank akakope”

7. Usikubali kumdamini mtu ambae huna uhakika kuwa atalipa kile unachomdhamini.
Kumbuka- dhamana maana yake utawajibika iwapo atashindwa kulipa

8. Epuka kutembea na pesa nyingi ambazo hata huna matumizi nazo wakati huo.
Unaweza kujikuta unafanya matumizi ambayo hayakuwa kwenye ratiba sababu ya ushawishi wa pesa ya mfukoni.
Ili kuepuka haya, tembea na pesa uliyopanga kuitumia katika safari yako.
Pesa nyingine itunze mahali pengine palipo salama”

9. Epuka kutunza pesa mahali pasipo sahihi.
Maeneo kama kwenye soksi, sidiria, chini ya mto wa kulalia, chini ya begi, kwenye kopo au hata kwenye begi la safari, si maeneo salama.
~Ni rahisi kusahau, kuibiwa au kupoteza pesa zako.

Ni bora ukatunza pesa kieletroniki; yaani bank au kwenye simu au kwenye pochi yenye kamba ngumu ya kuivaa mabegani au wallet ambayo inatosha kwenye mifuko imara na yenye vifungo kwenye nguo zako hasa uwapo safarini.

10. Usitumie pesa kwa kitu ambacho hakikuwa kwenye ratiba yako.

Jiulize kwanza kabla hujanunua,
“Bila kitu hiki, maisha yataenda au lah?”
Ukiona maisha yataenda bila kitu hicho, acha kukinunua. Tabasamu kisha ondoka.

12. Matumizi yako ya pesa yasizidi pato lako.

Unaweza kuwa una ndoto kubwa/matumizi makubwa ya pesa kuzidi pato lako.

Unapaswa kuwa bahili katika matumizi yako. Cheza na pato lako.
Fanya matumizi makubwa pale tu pato lako litakapoongezeka. Hii itakuepushia kushindwa kufanya baadhi ya mambo ya msingi na kisha ukajikuta unaishia kwenye madeni makubwa.
13. Una ndoto kubwa hapo baadae; labda kujenga nyumba, kununua gari, kununua kiwanja, simu nzuri hata pikipiki.

Usikurupuke, ukanunua kitu cha ndoto yako sasa eti tu sababu umekipata kwa bei ya punguzo.

Usichanganye kati ya mahitaji ya baadae na ya sasa.

Pesa unayotumia kutimizia ndoto sasa itumie kwa mahitaji ya sasa. Ndoto ibaki kuwa ndoto.

Hii itakuepushia kuingia katika madeni au kuishi kwa shida sababu ya tamaa.
Jipange taratibu kutimiza ndoto yako.

*Mwendo*

Jinsi ya Kufuga vizuri kware Kwa Faida

Kware au Kwale au Kereng’ende ni jamii ya ndege ambao kwa sasa wanafugwa majumbani na wanaotaga mayai kama kuku ama bata na kwa wingi sana.

Ndege hawa ni wadogo 280gm – 300gm, rangi ya kwale ni kahawia au kijivu na wana michirizi au madoa. Mara nyingi miguu yao ni myekundu au rangi ya manjano na koo lao ni jekundu, jeupe, jeusi au rangi ya manjano.

Chakula

1. Kware anakula chakula chochote anachoweza kula kuku ikiwemo chakula cha broiler. Kama utaamua kuwapa chakula cha broiler unawapa “starter” kware wenye umri kuanzia siku moja hadi wiki ya tatu baada ya hapo unawapa Falcon au hill.

2. Ukiweza kuwatengenezea chakula chako mwenye kutumia pumba nk. Ni vizuri zaidi kwa mayai yenye lishe 100%

3. Kware 100 wenye umri wa mwezi hutumia kiroba cha kilo 20 kwa wiki 3.

4. Kware hawamalizi chakula kama kuku.

5. Pia kware hupewa majani kama mchicha nk.

Kutaga na kuatamia kwa Kware

Kware dume humpanda jike kwa muda kidogo, Hapo jike anakuwa tayari kutaga na hutaga mayai 290 hadi 310 kwa mwaka (hii hulingana na lishe nzuri atakayopatiwa).

Mayai ya Kware huatamiwa kwa siku 18 na huanza kuanguliwa vifaranga kwa muda wa siku 2, kuanzia siku ya 18 na hadi 20.

Njia bora ya kutotolesha mayai ya Kware ni kwa kutumia incubator ambapo mayai huatamiwa kwa wingi ndani ya siku 18.

Utunzaji wa vifaranga vya kware na chakula

Utunzaji wa vifaranga vya kware Siku 1 – 7

Vifaranga wapatiwe chakula “STARTER PELLET” na maji masafi ya kutosha. Siku ya 1 wawekee ‘GLUCOSE’ kwenye maji, Packet moja kwa lita 20 za maji, na siku ya pili hadi ya tano wawekee Amin Total kwenye maji, Wape maji pekee siku ya sita na siku ya saba wapatie chanjo ya Newcastle. Utawapatia joto kwa njia ya umeme kwa ‘BULB’ mbili (2) za 200watts kwa kila vifaranga 300, ama unaweza kuweka taa ya ‘Energy Server’ pamoja na jiko la mkaa uliofunikwa na majivu ambao utakidhi kuwapatia joto sawia kwa masaa 24 kwa siku 7. (Majivu yanasaidia moto kukaa kwa muda mrefu)

Banda/box lako liwe la ukubwa wa 1.5m x 1.5m (au eneo la ukubwa huo ndani mwa banda kubwa la kufugia kuku) lazima uzingatie usalama wa vifaranga dhidi ya panya, paka au vicheche. Unatakiwa kuweka magazeti au mabox chini kwenye sakafu yatakayosaidia usafi. Kwa week ya kwanza chakula kitawekwa chini na tunashauri utumie chakula cha pellet ili kusaidia vifaranga wasiteleze na kuathiri miguu. NOTE: Weka gololi au mawe kwenye drinkers zako ili kuzuia vifaranga wasizame ndani ya (drinkers) maji na kufa.

Utunzaji wa vifaranga vya kware Siku 8-14

Vifaranga wataendelea kupewa chakula “STARTER PELLET” na maji safi. Wataendelea kuhitaji ‘mwanga’ wa kutosha muda wote na joto la wastani bulb 2 za watts 100 au moja ya watts 200

Utunzaji wa vifaranga vya kware Siku 15-21

Uhitaji wa joto utapungua, ila ni kipindi ambacho wanakula chakula zaidi kwa ajili ya kukua. Ni vizuri waendelee kupata taa ili kupata mwangaza utakayowawezesha kula mchana na usiku.

Utunzaji wa vifaranga vya kware Siku 21 na Kuendelea

Kware wako hawatahitaji joto tena wawekee taa tu za energy server kipindi cha usiku, wape chakula na maji ya kutosha zaidi kwa ajili ya kukua.

UTAGAJI WA KWARE

WIKI YA SITA

Wiki ya sita kuelekea ya saba Kware wako wataanza kutaga mayai kila siku, kwa wastani Kware mmoja hutaga mayai 300 kwa mwaka.

Magonjwa ya Kware

Kware ni ndege wenye kinga kubwa na ni vigumu sana kushambuliwa na magonjwa kama kuku na mara wanapougua ni rahisi sana kutibika. Magonjwa yanayoweza kuwapata Kware ni typhoid, mafua na kuharisha .

Tiba za asili za kware

Waweza kuwatibu vifaranga au Kware wako kwa kutumia njia ya asili ambayo pia ni rahisi, gharama nafuu na bora zaidi kuliko kutumia madawa yaliyochanganywa na kemikali na yenye gharama.

Vifuatazo ni vitu vya asili vinavyotumika kutibu magonjwa mbali mbali kwa Kware na yanayopatikana kwa wingi katika maeneo ya mfugaji. Madawa haya hutumika kwa kiwango cha wastani na hayana kipimo maalum kwani hata ukiyazidisha hayana madhara.

Mwarobaini na Aloe Vera:

Madawa haya hutumika kutibu kuharisha damu pamoja na mafua kwa vifaranga vya Kware. Chukua kiasi kidogo cha mwarubaini kisha twanga vizuri kupata maji maji. Kamua maji yale, kisha weka katika maji uliyoandaa kuwanywesha vifaranga wako. Kata vipande vidogovidogo vya aloe vera (jani moja laweza kutosha) na tia katika maji yaliyochanganywa na mwarobaini, kisha wapatie vifaranga wanywe (Aloe Vera itaendelea kujikamua yenyewe ikiwa ndani ya maji huku vifaranga wakiendele kunywa).

Kitunguu swaumu:

Hii hutumika kukinga na kutibu vifaranga vya kware wanaosumbuliwa na kuharisha damu. Unachukua kitunguu swaumu na kuondoa maganda ya nje kisha kusafisha na kukata vipande vidogo sana, na kuwawekea kama chakula. Vifaranga wanapenda sana vitunguu hivyo na watakula kwa kasi kama chakula lakini ni tiba tayari. Unaweza kuwapatia kila siku hadi watakapo pona.

Maziwa:

Maziwa yanayotokana na ng’ombe pia hutumika kutibu ugonjwa wa kuhara pamoja na kuwapa nguvu Kware waliolegea. Mnyweshwe maziwa hayo Kware anayeumwa bila kuyachemsha na umnyweshe maziwa ya kutosha kiasi cha kushiba. Unamnywesha mara tatu kwa siku. Hakikisha maziwa unayotumia yanatoka kwa ng’ombe wanaotibiwa kila mara.

Angalizo

Siyo lazima Kware waugue ndipo uwapatie tiba hizi. Hakikisha unawapa tiba kabla hata hawajaugua hivyo utawakinga na magonjwa hayo. Waweza kuchanganya madawa hayo yote kwa wakati mmoja kwani hayana madhara.

Endapo madawa ya asili hayapatikani katika eneo la mfugaji basi waweza kuwatibu Kware kwa madawa yafuatayo ambapo vipimo huelezwa moja kwa moja kwa maandishi katika madawa hayo au kuelezwa na muuzaji pale utakaponunulia; Amprolium kwa ugonjwa wa kuharisha damu (Coccidiosis), Fluban,Coridix au Doxyco kutibu mafua (Coryza) na Esb3,Trisulmycine au Trimazine hutumika kwa homa ya matumbo (Typhoid).

ZINGATIA:

Wanapokosa madini ya kutosha kwenye chakula huweza kupata madhara yafuatayo:-
1. Kuharisha
2. Kunyonyoka manyoya
3. Kupunguza kasi ya kutaga mayai.

Chanjo Ya kware

Siku ya 7 lazima vifaranga wapatiwe chanjo ya “kideri/mdondo”
(respiratory & digestive diseases) kwa dawa inayoitwa ‘newcastle’. Chanzo cha maambukizi ni maji na chakula kilichochafuliwa na kinyesi na pia husababishwa na virusi kwa njia ya hewa.

Siku ya 14 lazima wapewe chanjo ya “gumboro”. Chanzo cha
maambukizi ni maji na chakula kilichochafuliwa na kinyesi na pia husababishwa na virusi kwa njia ya hewa.

Siku ya 21 lazima warudie chanjo ya “Newcastle (aina ya IBDL)”. Chanzo cha maambukizi ni maji na chakula kilichochafuliwa na kinyesi na pia husababishwa na virusi kwa njia ya hewa.

Siku ya 35 lazima wapate chanjo ya “Ndui”.

Soko la kware

Mayai ya Kware ni bidhaa adimu sana hapa nchini kwa kuwa ni wafugaji wachache waliojikita katika ufugaji huu, Ufuatao ni muhtasari wa wastani wa bei ya bidhaa za Kware sokoni

1. Trei ya (mayai 30) ya KWALE inauzwa shilingi 30,000 .
2. Kifaranga wa Kware wa siku moja anauzwa shilingi 2500 – 3000
3. Kware wa week 4 (mwezi mmoja) anauzwa kwa shilingi 10,000– 12,000
4. Kware aliyeanza kutotoa (week 6) huuzwa shillingi 20,000 – 25,000
5. Kware kwa aliyekomaa kwa ajili ya kitoweo huuzwa kwa shilingi 25,000
6. DROPING za Kware huuzwa kwa shilingi 10,000 kwa 50kg kwa wafugaji wa samaki

Soko la KWALE liko juu sana kwa mayai na nyama. KWALE pia hutofautiana bei kwa jike na dume.

FAIDA ZA KUFUGA KWALE

Ufugaji wa kwale hua na faida ukilinganisha na ufugaji wa ndege wengine

· Chanzo cha kipato kwa wafugaji.
· Hawana gharama sana katika suala kufuga.
· Hawataji utaalam sana katika kuwafuga.
· Mayai yake ni tiba ya magonjwa mbalimbali.
· Mayai yake hayakosi soko.

Shopping Cart