Author name: DIN - Melkisedeck Leon Shine

Maswali na Majibu kuhusu Marehemu

Ufufuko wa wafu maana yake nini?

Ufufuko wa wafu maana yake mwisho wa dunia watu wote watafufuka na miili yao na kwenda nayo katika furaha ya milele au moto wa milele. (Ayu 19:25-26, Mt 22:30-32, Yh 28-29)


Baada ya kifo cha mtu nini hutokea?

Baada ya kifo roho yake inafika mbele ya Mungu kwa hukumu ya mtu binafsi.


Matokeo ya hukumu hiyo ni nini?

Matokeo ya Hukumu hiyo ni roho kwenda Mbinguni, Toharani au Motoni. (Mt 25:34-46)


Mbinguni ni mahali pa namna gani?

Mbinguni ni makao mema ya heri na furaha (2Kor 5:1, Ufu, 2:17).
Waendao mbinguni ni wale wanaokufa katika hali ya neema ya utakaso na urafiki na Mungu na waliotakaswa kikamilifu


Motoni ni nini?

Motoni ni makao mabaya kwa Shetani walaaniwa wakaapo mbali na Mungu wakiteswa milele. (Mt 25:41, Mik 9:42-43, 1Yoh 14:15)


Uzima wa milele ni nini?

Uzima wa milele ni maisha ya kukaa mbinguni na Mungu yasiyokua na mwisho.


Toharani ni mahali gani?

Toharani ni mahali pa mateso zinakosafishwa roho ambazo hazikutimiza kitubio vizuri baada ya kuungama dhambi. (1Kor 3:15, 1Pet 1:7).


Je, hatuwezi kupunguza mateso ya roho za marehemu waliokwenda toharani?

Ndiyo: twaweza kupunguza hata kuyamaliza kwa kuwasalia na kuwapatia rehema na hasa kwa kuadhimisha Misa kwa ajili yao. (2Mik 12:38-46)


Mambo makuu manne ya mwisho ni yapi?

Mambo hayo ni;
1. Kifo
2. Hukumu
3. Jehanamu (Motoni)
4. Paradiso. (Toharani/Mbinguni)


Je, ufufuko wa Yesu ni muhimu kwetu pia?

Ndiyo, ufufuko wa Yesu ni muhimu kwetu pia, kwa sababu kwa njia yake tu tunatiwa uzima: sasa rohoni kwa kuondolewa dhambi, na siku ya mwisho mwilini pia kwa kufufuliwa.
Mwenyewe alisema, “Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi ajapokufa, atakuwa anaishi; naye kila aishiye na kuniamini hatakufa kabisa hata milele” (Yoh 11:25- 26).
“Kristo amefufuka katika wafu, limbuko lao waliolala. Maana kwa kuwa mauti ililetwa na mtu, kadhalika na kiyama ya wafu ililetwa na mtu” (1Kor 15:20-21).
“Alitolewa kwa ajili ya makosa yetu, na kufufuka ili tupate kuhesabiwa haki” (Rom 4:25).


Je, ni muhimu tujiandae kufa?

Ndiyo, ni muhimu tujiandae kufa wakati wowote na namna yoyote kwa kuishi kitakatifu sasa na kwa kujiombea neema tutakazohitaji saa ya kufa kwetu, tukijua tumewekewa “kufa mara moja, na baada ya kufa hukumu” (Eb 9:27).
“Katika mambo yako yote uukumbuke mwisho wako, hivyo hutakosa kamwe hata hatima” (YbS 7:36).
“Hamjui yatakayokuwako kesho! Uzima wenu ni nini? Maana ninyi ni mvuke uonekanao kwa kitambo, kisha hutoweka” (Yak 4:14).
“Kesheni, mwombe, msije mkaingia majaribuni” (Math 26:41).


Je, ina thamani machoni pa Bwana mauti ya mtu aliyemcha?

Ndiyo, “ina thamani machoni pa Bwana mauti ya wacha Mungu wake” (Zab 116:15).
Hasa utiifu wa Yesu msalabani umegeuza laana ya kifo iwe baraka kwa waamini wake.
“Heri wafu wafao katika Bwana tangu sasa. Naam, asema Roho, wapate kupumzika baada ya taabu zao; kwa kuwa matendo yao yafuatana nao” (Ufu 14:13).


Tutakapofariki dunia itatutokea nini?

Tutakapofariki dunia roho yetu isiyokufa, mbali na mwili unaooza, itapewa tuzo au adhabu tuliyostahili kwa maisha yetu. “Ikawa yule maskini alikufa, akachukuliwa na malaika mpaka kifuani kwa Ibrahimu. Yule tajiri naye akafa, akazikwa. Basi, kule kuzimu aliyainua macho yake, alipokuwa katika mateso, akamwona Ibrahimu kwa mbali, na Lazaro kifuani mwake” (Lk 16:22-23). “Kwangu mimi kuishi ni Kristo, na kufa ni faida… ninatamani kwenda zangu nikae na Kristo, maana ni vizuri zaidi sana” (Fil 1:21,23). “Nasi tunaona ni afadhali kutokuwamo katika mwili na kukaa pamoja na Bwana” (2Kor 5:8). Kwa kuwa kifo ni “mavumbi kuirudia nchi kama yalivyokuwa, nayo roho kumrudia Mungu aliyeitoa” (Mhu 12:7). Siku ya ufufuo roho na mwili vitaungana tena kwa ajili ya uzima au moto wa milele. “Pumzi iliwaingia, wakaishi, wakasimama kwa miguu yao, jeshi kubwa mno” (Ez 37:10).

Je baada ya kufa ni hapo hapo roho inaenda motoni au mbinguni, Au ni mpaka Siku ya hukumu Yesu Atakaporudi?

Ni siku ile ile Roho ya mtu aliyekufa inaenda Mbinguni, toharani au Motoni. Yesu alimwahidi yule mtu waliyesulubiwa pamoja kuwa watakuwa peponi pamoja siku hiyo hiyo na sio siku ya hukumu.
“Kisha akasema, “Ee Yesu! Unikumbuke wakati utakapoingia katika ufalme wako.” 43 Yesu akamwambia, “Nakwambia kwa hakika, leo utakuwa pamoja nami peponi.” (Luka 23:42-43)
Sauli aliweza kuongea na Samweli hata baada ya kufa na Samweli alimbashiria mambo yatakayotokea kwa Sauli maanake ni kwamba Japokuwa alikuwa amekufa bado anayomuungano na Mungu ndio maana aliweza kumwambia Sauli mambo yatakayompata,
“7Basi Sauli akawaambia watumishi wake, “Nitafutieni mwanamke mwenye pepo wa utambuzi ili nimwendee nipate kuuliza kwake. Watumishi wake wakamwambia, “Yuko mwanamke mmoja huko Endori.” 8Hivyo Sauli akajigeuza kwa kuvaa mavazi mengine, naye usiku akiwa amefuatana na watu wawili wakaenda kwa huyo mwanamke. Akamwambia, “Nibashirie na unipandishie huyo nitakayekutajia,” 9Huyo mwanamke akamwambia, “Wewe unajua lile alilofanya mfalme Sauli. Amewakatilia mbali wapunga pepo, wapiga ramli wote na wachawi katika nchi. Mbona umenitegea maisha yangu ili wapate kuniua?” 10Sauli akamwapia huyo mwananmke kwa Jina la BWANA, akasema, “Kwa hakika kama BWANA aishivyo, hutaadhibiwa kwa ajili ya jambo hili.” 11Ndipo yule mwanamke akauliza, “Je unataka nikupandishie nani? Sauli akasema, “Nipandishie Samweli.” 12Yule mwanamke alipomwona Samweli alipiga yowe kwa sauti kuu, naye akamwuliza Sauli, “Mbona umenidanganya? Wewe ndiwe Sauli.” 13Mfalme akamwambia, “Usiogope. Unaona nini? Yule mwanamke akasema, “Naona Mungu anapanda kutoka ardhini.” 14Sauli akamwuliza, “Ni mfano wa nini?” Yule mwanamke akasema, “Ni mwanaume mzee amevaa joho anayepanda.” Ndipo Sauli akatambua kwamba ni Samweli. Sauli akasujudu kifudifudi uso wake hadi ardhini. 15Samweli akamwuliza Sauli, Kwa nini unanitaabisha, kunipandisha juu?” Sauli akasema, “Mimi ninasumbuka sana, kwa maana Wafilisti wanapigana vita dhidi yangu, naye Mungu ameniacha. Hanijibu tena wala kwa njia ya manabii wala kwa ndoto. Kwa hiyo nimekuita wewe ili unijulishe lakufanya.” 16Samweli akamwuliza, “Kwa nini uniulize mimi, maadam BWANA amekuacha na kuwa adui yako? 17BWANA ametenda lile alilotangulia kusema kwa kupitia kwangu. BWANA ameurarua ufalme kutoka mikononi mwako, naye amempa mmoja wa jirani zako, yaani, Daudi. 18Kwa sababu wewe hukumtii BWANA, wala hukumtimizia ghadhabu yake kali juu ya Waamaleki, BWANA amekutendea mambo haya leo. 19Zaidi ya hayo, BWANA atawatia Israeli pamoja na wewe mkononi mwa Wafilisti na kesho wewe na wanao mtakuwa pamoja nami. BWANA pia atalitia jeshi la Israeli mkononi mwa Wafilisti.
Mfano Wa Tajiri Na Maskini Lazaro Yesu alisimulia hivi
19 Akasema, “Palikuwa na tajiri mmoja aliyevaa nguo za rangi ya zambarau na kitani safi, nguo za gharama kubwa, kila siku. 20 Na maskini mmoja, jina lake Lazaro, mwenye vidonda mwili mzima, alikuwa akiletwa mlangoni kwa huyo tajiri kila siku. 21 Lazaro alikuwa akitamani kula makombo yaliyodondoka mezani kwa tajiri. Hata mbwa walikuwa wakiramba vidonda vyake. 22 “Hatimaye, yule maskini alikufa. Malaika wakamchukua akakae pamoja na Ibrahimu mbinguni. Yule tajiri naye pia akafa, akazikwa. 23 Alipokuwa kuzimuni ambapo alikuwa akiteseka, alita zama juu, akamwona Ibrahimu kwa mbali na Lazaro karibu yake. 24 Akaita, ‘Baba Ibrahimu, nionee huruma umtume Lazaro achovye japo ncha ya kidole chake katika maji aupoze ulimi wangu maana ninateseka kwenye moto huu.’ 25 Lakini Ibrahimu akamjibu, ‘Mwa nangu, kumbuka kwamba ulipokuwa hai ulipata kila kitu kizuri uli chotaka, ambapo Lazaro alipokea mabaya. Lakini sasa anafarijika hapa na wewe unateseka. 26 Isitoshe, kati yetu na ninyi huko, kumewekwa bonde kubwa lisilopitika ili wale wanaotaka kutoka huku kuja huko au kutoka huko kuja huku wasiweze.’ 27 Akasema, ‘Basi, baba, tafadhali umtume Lazaro aende nyumbani kwa baba yangu, 28 awaonye ndugu zangu, wasije wao pia wakaletwa mahali hapa pa mateso watakapokufa.’ 29 Ibrahimu akamjibu, ‘Ndugu zako wanazo sheria za Musa na maandiko ya Manabii. Itawapasa watii hayo.’ Lakini yule tajiri akazidi kumsihi, 30 ‘Hapana baba Ibrahimu, ndugu zangu hawatashawishiwa na hayo. Lakini mtu kutoka kuzimu akitumwa kwao watatubu na kuziacha dhambi zao.’ 31 “Ibrahimu akamwambia, ‘Wasiposikiliza na kutii sheria za Musa na Maandiko ya manabii, hawatashawishika kutubu hata kama mtu akifufuka kutoka kuzimu.”’ (Luka 16:19-31)
Wakati Yesu anabadilika Sura walitokea Musa na Eliya.
“Baada ya siku sita, Yesu aliwachukua Petro, Yakobo na Yohane nduguye, akaenda nao peke yao juu ya mlima mrefu. 2 Huko, wakiwa wanamtazama, akageuka sura, uso wake ukang’aa kama jua na mavazi yake yakawa meupe kama nuru. 3 Mose na Eliya wakawatokea, wakawa wanazungumza naye. 4 Hapo Petro akamwambia Yesu, “Bwana, ni vizuri sana kwamba tupo hapa! Ukipenda nitajenga vibanda vitatu: kimoja chako, kimoja cha Mose na kimoja cha Eliya.” (Mathayo 17:1-5)
Yesu alituambia kuwa Mungu sio wa wafu bali wa walio hai ndio maana akaitwa Mungu wa Ibrahimu, Isaka na Yakobo kwa kuwa Wote wako hai kwake.
37Hata Mose alidhihirisha kuwa wafu wanafufuka, kwa habari ya kile kichaka kilichokuwa kikiwaka moto bila keteketea, alipomwita Bwana ‘Mungu wa Abrahamu, Mungu wa Isaki na Mungu wa Yakobo.’ 38Yeye Mungu si Mungu wa wafu bali wa walio hai, kwa kuwa Kwake wote ni hai.” (Luka 20:37-38)
Yesu alimwahidi yule mtu waliyesulubiwa pamoja kuwa watakuwa peponi pamoja siku hiyo hiyo na sio siku ya hukumu.
“Kisha akasema, “Ee Yesu! Unikumbuke wakati utakapoingia katika ufalme wako.” 43 Yesu akamwambia, “Nakwambia kwa hakika, leo utakuwa pamoja nami peponi.” (Luka 23:42-43)
Angalia pia wakati Stefano akipigwa Mawe aliikabidhi roho yake kwa Mungu baada ya kuona mbingu zimefunguka hii ni kama Yesu alivyokuwa pale msalabani aliikabidhi Roho yake kwa Baba yake.
55Lakini yeye Stefano akiwa amejazwa Roho Mtakatifu, alikaza macho mbinguni, akaona utukufu wa Mungu, naye Yesu akiwa amesimama mkono wa kuume wa Mungu. 56Akasema, “Tazameni! Naona mbingu zimefunguka na Mwana wa Adamu amesimama upande wa kuume wa Mungu.’’ 57Lakini wao wakapiga kelele kwa sauti kubwa, wakaziba masikio yao, wakamrukia kwa nia moja. 58Wakamtupa nje ya mji, wakampiga kwa mawe. Nao mashahidi wakaweka nguo zao miguuni mwa kijana mmoja aitwae Sauli. 59Walipokuwa wakimpiga mawe, Stefano aliomba, “Bwana Yesu, pokea roho yangu” 60Kisha akapiga magoti, akalia kwa sauti kubwa akasema, “Bwana usiwahesabie dhambi hii.’’ Baada ya kusema haya, akalala. (Mdo 7:55-60)
Kwenye Ufunuo tunasoma (Ufunuo 6:9-10) “Na alipoifungua muhuri ya tano, nikaona chini ya madhabahu roho zao waliochinjwa kwa ajili ya neno la Mungu, na kwa ajili ya ushuhuda waliokuwa nao. Wakalia kwa sauti kuu, wakisema, Ee Mola, Mtakatifu, Mwenye kweli, hata lini kutokuhukumu, wala kuipatia haki damu yetu kwa hao wakaao juu ya nchi? Nao wakapewa kila mmoja nguo ndefu, nyeupe, wakaambiwa wastarehe bado muda mchache, hata itakapotimia hesabu ya wajoli wao na ndugu zao, watakaouawa vile vile kama wao.”
Kwa hiyo mtu akifa anaenda mbinguni au motoni kulingana na alivyoishi.
“Nasi tunaona ni afadhali kutokuwamo katika mwili na kukaa pamoja na Bwana” (2Kor 5:8). Kwa kuwa kifo ni “mavumbi kuirudia nchi kama yalivyokuwa, nayo roho kumrudia Mungu aliyeitoa” (Mhu 12:7).
Siku ya ufufuo roho na mwili vitaungana tena kwa ajili ya uzima au moto wa milele.
“Kwangu mimi kuishi ni Kristo, na kufa ni faida… ninatamani kwenda zangu nikae na Kristo, maana ni vizuri zaidi sana” (Fil 1:21,23).
Mtume Petro ameandika hivi…
“18 Kwa maana Kristo naye aliteswa mara moja kwa ajili ya dhambi, mwenye haki kwa ajili yao wasio haki, ili atulete kwa Mungu; mwili wake akauawa, bali roho yake akahuishwa,19 ambayo kwa hiyo aliwaendea roho waliokaa kifungoni, akawahubiri; 20 watu wasiotii hapo zamani, uvumilivu wa Mungu ulipokuwa ukingoja, siku za Nuhu, safina ilipokuwa ikitengenezwa; ambamo ndani yake wachache, yaani, watu wanane, waliokoka kwa maji.” (1Petro 3:18-20)


Je, sisi wanyonge tunaweza kushiriki uzima wa milele wa Mungu?

Ndiyo, sisi wanyonge tunaweza kushiriki uzima wa milele wa Mungu: hapa duniani katika mwanga hafifu wa imani, na kisha kufa katika uangavu wa utukufu usiofifia kamwe. Kwa kuwa lengo la Baba ni kwamba tuungane na Yesu Mwanae kwa uwezo wa Roho Mtakatifu ili tuwe na utukufu wake.
“Na uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma” (Yoh 17:3).
“Kwa kuwa uweza wake wa Uungu umetukirimia vitu vyote vipasavyo uzima na utauwa, kwa kumjua yeye aliyetuita kwa utukufu wake na wema wake mwenyewe. Tena kwa hayo ametukirimia ahadi kubwa mno, za thamani, ili kwamba kwa hizo mpate kuwa washirika wa tabia ya Uungu, mkiokolewa na uharibifu uliomo duniani kwa sababu ya tamaa” (2Pet 1:3-4).
Sisi tuliobatizwa tunaitwa “wana wa Mungu; na ndivyo tulivyo!” (1Yoh. 3:1).
Kwa sababu tumesadiki kwamba “Mungu ni upendo” (1Yoh 4:8) na kwamba “hakuna lisilowezekana kwa Bwana” (Lk 1:37).
“Na kwa kuwa ninyi mmekuwa wana, Mungu alimtuma Roho wa Mwanawe mioyoni mwetu, aliaye, ‘Aba!’ yaani, ‘Baba!’ Kama ni hivyo, wewe si mtumwa tena bali u mwana; na kama u mwana, basi, u mrithi kwa Mungu” (Gal 4:6-7).


Aliyezungumzia moto wa milele ni nani?

Aliyezungumzia moto wa milele ni hasa Yesu: akitufunulia ukuu wa upendo wa Mungu, aliye heri yetu pekee, alituangalisha juu ya hatari ya kutengana naye milele kwa dhambi. Mwenyewe atatoa hukumu hiyo:
“Ondokeni kwangu, mliolaaniwa, mwende katika moto wa milele, aliowekewa tayari Ibilisi na malaika zake” (Math 25:41).
“Humo funza wao hafi, wala moto hauzimiki” (Mk 9:48).
“Na moshi wa maumivu yao hupanda juu hata milele na milele, wala hawana raha mchana wala usiku” (Ufu 14:11).


Toharani maana yake nini?

Toharani maana yake kuna hali ya muda ambayo huruma ya Mungu inawatakasa marehemu waliofariki dunia katika urafiki naye lakini bila ya usafi kamili unaotakiwa kwa kuingia mbinguni. Sisi tunaweza kuharakisha utakaso wao kwa kumtolea Mungu sala na sadaka, hasa ekaristi. Yuda Mmakabayo “alichanga fedha kwa kila mtu jumla drakma elfu mbili, akazipeleka Yerusalemu kutoa sadaka ya dhambi.
Kwa kufanya hivi alitenda vema na kwa haki, kwa kuwa aliukumbuka ufufuo wa wafu. Maana kama asingalitumaini ya kuwa wale waliokufa watafufuka, ingalikuwa kazi bure isiyo na maana kuwaombea wafu. Lakini kwa kuwa aliufikiri utukufu wa thawabu waliowekewa wale wafao katika utauwa, wazo lake lilikuwa takatifu na la kicho. Ndiyo sababu alifanya upatanisho kwa wafu ili wafunguliwe dhambi zao” (2Mak 12:43-46). Imani hiyohiyo iliongoza Wakristo wa kwanza kuwafanyia marehemu ibada ambayo haieleweki vizuri, lakini hailaumiwi na Mtume Paulo: “Kama wafu hawafufuliwi kamwe, kwa nini kubatizwa kwa ajili yao?” (1Kor 15:29).


Je, mwili utakaofufuliwa ni huuhuu tulionao sasa?

Ndiyo, mwili utakaofufuliwa ni huuhuu tulionao sasa, lakini katika hali tofauti: > “hupandwa katika uharibifu; hufufuliwa katika kutokuharibika” (1Kor 15:42).
Siku ya ufufuo “ndipo watakapomwona Mwana wa Adamu akija katika wingu pamoja na nguvu na utukufu mwingi” (Lk 21:27).
“Saa yaja ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake. Nao watatoka; wale waliofanya mema kwa ufufuko wa uzima, na waliotenda mabaya kwa ufufuo wa hukumu” (Yoh 5:28-29).
“Na hao watakwenda zao kuingia katika adhabu ya milele; bali wenye haki watakwenda katika uzima wa milele” (Math 25:46).


Siku ya ufufuo Kristo mfalme atatuhukumu vipi?

Siku ya ufufuo Kristo mfalme atatuhukumu kwa kudhihirisha misimamo ya watu wote ambao, kwa kupokea au kukataa upendo wa Mungu moyoni mwao, wametenda mema au la.
“Imetupasa sisi sote kudhihirishwa mbele ya kiti cha hukumu cha Kristo ili kila mtu apokee ijara ya mambo aliyotenda kwa mwili, kadiri alivyopenda, kwamba ni mema au mabaya” (2Kor 5:10).
“Basi ninyi msihukumu neno kabla ya wakati wake, hata ajapo Bwana; ambaye atayamulikisha yaliyositirika ya giza, na kuyadhihirisha mashauri ya mioyo; ndipo kila mtu atakapoipata sifa yake kwa Mungu” (1Kor 4:5).
“Hapo atakapokuja Mwana wa Adamu katika utukufu wake, na malaika watakatifu wote pamoja naye, ndipo atakapoketi katika kiti cha utukufu wake. Na mataifa yote watakusanyika mbele zake; naye atawabagua kama vile mchungaji abaguavyo kondoo na mbuzi; atawaweka kondoo mkono wake wa kuume, na mbuzi mkono wake wa kushoto. Kisha Mfalme atawaambia wale walioko mkono wake wa kuume, ‘Njoni, mliobarikiwa na Baba yangu, urithini ufalme mliowekewa tayari tangu kuumbwa ulimwengu; kwa maana nalikuwa na njaa, mkanipa chakula; nalikuwa na kiu, mkaninywesha; nalikuwa mgeni, mkanikaribisha; nalikuwa uchi, mkanivika; nalikuwa mgonjwa, mkaja kunitazama; nalikuwa kifungoni, mkanijia… Amin, nawaambia, kadiri mlivyomtendea mmojawapo wa hao ndugu zangu walio wadogo, mlinitendea mimi’” (Math 25:31-36,40).
“Heri wenye rehema, maana hao watapata rehema” (Math 5:7).


Baada ya hukumu ya mwisho itakuwaje?

Baada ya hukumu ya mwisho, waadilifu watatukuzwa mwili na roho pamoja na Yesu, na ulimwengu pia utageuzwa.
“Kama ilivyo ahadi yake, tunatazamia mbingu mpya na nchi mpya, ambayo haki yakaa ndani yake” (2Pet 3:13).
“Na Roho na Bibi arusi wasema, ‘Njoo!’ naye asikiaye na aseme, ‘Njoo!’… Yeye mwenye kuyashuhudia haya asema, ‘Naam, naja upesi’. Amina. Na uje, Bwana Yesu! Neema ya Bwana Yesu na iwe pamoja nanyi nyote. Amina” (Ufu 22:17,20-21).


Kanisa linaheshimu marehemu kwa namna gani?

Kanisa linaheshimu marehemu kwa kuwafanyia mazishi huku likiwaombea kwa Mungu.
“Watu watauwa walimzika Stefano, wakamfanyia maombolezo makuu” (Mdo 8:2).
Yeye kama mfiadini, aliyefikia upeo wa upendo kwa kutoa uhai wake, hakuhitaji kuombewa. Lakini wafu wengine walitolewa sala na sadaka tangu Israeli ilipoanza kusadiki ufufuo.
“Kama asingalitumaini kuwa wale waliokufa watafufuka, ingalikuwa kazi bure isiyo na maana kuwaombea wafu. Lakini kwa kuwa aliufikiri utukufu wa thawabu waliowekewa wale wafao katika utauwa, wazo lake lilikuwa takatifu na la kicho. Ndiyo sababu alifanya upatanisho kwa wafu ili wafunguliwe dhambi yao” (2Mak 12:44-46).
“Kama wafu hawafufuliwi kamwe, kwa nini kubatizwa kwa ajili yao?” (1Kor 15:29).

Maswali na Majibu kuhusu Mapokeo ndani ya Kanisa Katoliki

Mapokeo ya Mitume ndiyo nini?

Mapokeo ya Mitume ndiyo yale yote ambayo Yesu aliwakabidhi Mitume wake, na kwa uwezo wa Roho Mtakatifu yatadumu hata mwisho wa dunia katika mafundisho, liturujia na maisha ya Kanisa.
“Nawasifu, kwa sababu mmenikumbuka katika mambo yote, nanyi mmeyashika yale mapokeo vilevile kama nilivyowatolea… Kwa maana naliwatolea ninyi hapo mwanzo yale niliyoyapokea mimi mwenyewe” (1Kor 11:2; 15:3).
“Ilinde ile amana nzuri kwa Roho Mtakatifu akaaye ndani yetu… Mambo yale uliyoyasikia kwangu mbele ya mashahidi wengi, hayo uwakabidhi watu waaminifu watakaofaa kuwafundisha na wengine” (2Tim 1:14; 2:2).
Tukikata huo mnyororo wa mapokeo, hata kama ni kwa kisingizio cha kushikilia Biblia, tunaachana na asili ya Kanisa.
“Basi, ndugu, simameni imara, mkayashike mapokeo mliyofundishwa, ama kwa maneno, ama kwa waraka wetu… Ndugu, twawaagiza katika jina la Bwana Yesu Kristo, jitengeni nafsi zenu na kila ndugu aendaye bila utaratibu, wala si kwa kufuata mapokeo mliyoyapokea kwetu” (2Thes 2:15; 3:6).


Tunatambuaje Maandiko Matakatifu kati ya maandishi yote ya binadamu?

Tunatambua Maandiko Matakatifu kati ya maandishi yote ya binadamu kwa njia ya Mapokeo, yaani kwa sababu yametumiwa na Kanisa tangu mwanzo kwa kulisha kwa hakika imani yake.
Tunahitaji Mapokeo kwa kuwa Maandiko yenyewe hayataji orodha ya vitabu vyake vyote, Sanasana Yesu alividokeza baadhi akisema yanamzungumzia na kutimia ndani yake,
“Ni lazima yatimizwe yote niliyoandikiwa katika Torati ya Musa, na katika Manabii, na Zaburi” (Lk 24:44).
Halafu Barua ya Pili ya Mtume Petro ikalinganisha “na Maandiko mengine” nyaraka zote ambazo Paulo aliziandika “kwa hekima aliyopewa” (2Pet 3:15-16).


Sababu nyingine za Biblia kutojitosheleza ni zipi?

Sababu nyingine za Biblia kutojitosheleza ni kwamba mambo mengi muhimu hayakuandikwa,
“Kuna mambo mengine mengi aliyoyafanya Yesu, ambayo yakiandikwa moja moja, nadhani hata ulimwengu usingetosha kwa vile vitabu vitakavyoandikwa” (Yoh 21:25).
Tena barua ni nusu tu ya kuonana; hivyo Yesu hakuandika lolote, nao Mitume hawakupenda kuandika yote.
“Kwa kuwa ninayo mambo mengi, sitaki kuyaandika kwa karatasi na wino; lakini nataraji kuja kwenu, na kusema nanyi mdomo kwa mdomo, ili furaha yetu iwe imetimizwa” (2Yoh 12).
“Nalikuwa na mambo mengi ya kukuandikia, lakini sipendi kukuandikia kwa wino na kalamu. Lakini nataraji kukuona karibu, nasi tutasema mdomo kwa mdomo” (3Yoh 13-14).
Hasa ibada haziwezi kufanyika kwa barua; k.mf. kuwekea mikono ili kumshirikisha Roho Mtakatifu. Paji la namna hiyo halipitii Maandiko, bali Mapokeo tu. Hatimaye Biblia ikipotoshwa haipingi, kwa kuwa si mtu hai anayeweza kujitetea.


Je, inafaa tushike neno lolote la Agano la Kale kama Wayahudi?

Hapana, haifai tushike neno lolote la Agano la Kale kama Wayahudi wasiozingatia jinsi Yesu alivyolitimiliza kwa maneno na matendo hata wakamshutumu kutenda kinyume:
“Mtu huyo hakutoka kwa Mungu, kwa sababu haishiki sabato” (Yoh 9:16).
Alipofafanua amri 10 za Mungu alikariri:
“Mmesikia watu wa kale walivyoambiwa… lakini mimi nawaambieni…” (Math 5:21,27,31,33,38,43).
Alipouliziwa unajisi wa vyakula kadhaa, alisisitiza,
“’Hivi hata ninyi hamna akili? Hamfahamu ya kwamba kila kitu kilicho nje ya mtu, kikimwingia, hakiwezi kumtia unajisi; kwa sababu hakimwingii moyoni, ila tumboni tu; kisha chatoka kwenda chooni?’ Kwa kusema hivi alivitakasa vyakula vyote” (Mk 7:18- 19).
“Basi, mtu asiwahukumu ninyi katika vyakula au vinywaji, au kwa sababu ya sikukuu au mwandamo wa mwezi, au sabato; mambo hayo ni kivuli cha mambo yajayo; bali mwili ni wa Kristo” (Kol 2:16-17).
Hakika, mwili ni mzito kuliko kivuli chake.
Vile vile katika Warumi 4:16. Tunasoma “Kwa sababu hiyo, jambo hili lategemea imani, hivyo kwamba ahadi hiyo yatokana na neema ya Mungu, na kwamba ni hakika kuwa ahadi hiyo ni kwa ajili ya wote:si kwa wale tu wanaoishika sheria, bali kwa wale waishio kwa Imani kama Abrahamu. Yeye ni Baba yetu sote.”
Wakristo wengine wanachanganywa na wale wasioyajua maandiko na kuwataka washike sheria na Torati,basi tukisema ni lazima kushika sheria tutakua tunakataa kua Abrahamu hakuwa mtu wa Mungu maana kwa Abrahamu hatukuwa na Sheria wala Torati na alipata kibali machoni Pa Mungu tuu kwa Imani. Kumbuka pia Abrahamu alitahiriwa baada ya Kuwa tayari mtu wa Mungu kwa Imani yake na sio kwamba Kutahiriwa ndio kulifanya mtu wa Mungu.
Tumekombolewa kwa Imani na sio kwa Sheria. Wagalatia 5:18 “Lakini Mkiongozwa na Roho hampo chini ya sheria”
Hatumtumikii Mungu ili tuwe watu wa Mungu bali tukishakua watu wa Mungu ndio tunamtumikia Mungu.


Tueleweje Maandiko Matakatifu?

Tuelewe Maandiko Matakatifu kwa kuzingatia hasa Mungu alitaka kusema nini kuhusu wokovu wetu kupitia waandishi wengi aliowaongoza kuyatunga kwa lugha na mitindo mbalimbali.
Lakini ebu, “Yamo mambo ambayo ni vigumu kuelewa nayo; na mambo hayo watu wasio na elimu, wasio imara, huyapotoa, kama vile wayapotoavyo na Maandiko mengine, kwa uvunjifu wao wenyewe” (2Pet 3:16).
Utitiri wa madhehebu yanayoshindana yakidai kushikilia Biblia tu unathibitisha uwekezano mkubwa wa kuipotosha kwa namna moja au nyingine.
“Utakuja wakati watakapoyakataa mafundisho yenye uzima; ila kwa kuzifuata nia zao wenyewe watajipatia walimu makundi makundi, kwa kuwa wana masikio ya utafiti; nao watajiepusha wasisikie yaliyo kweli, na kuzigeukia hadithi za uongo” (2Tim 4:3-4).
Njia pekee ya kukwepa fujo hiyo ni kuelewa Maandiko ndani ya Kanisa, kadiri ya Mapokeo yake hai.
“Lakini mtu yeyote akitaka kuleta fitina, sisi hatuna desturi kama hiyo, wala makanisa ya Mungu” (1Kor 11:16).
Biblia nje ya Kanisa ni kama samaki nje ya maji.


Je, ufunuo wa Mungu unaweza kufafanuliwa rasmi na kila mtu?

Hapana, ufunuo wa Mungu unaweza kufafanuliwa rasmi na umoja wa Maaskofu tu, kwa kuwa ndio waandamizi wa Mitume 12 wa Yesu.
“Au je, neno la Mungu lilitoka kwenu? Au kuwafikia ninyi peke yenu?” (1Kor 14:36).
“Hakuna unabii katika Maandiko upatao kufasiriwa kama apendavyo mtu fulani tu. Maana unabii haukuletwa popote kwa mapenzi ya mwanadamu” (2Pet 1:20-21).
Tunahitaji unyenyekevu wa Mwafrika ambaye shemasi Filipo alimsikia “anasoma chuo cha nabii Isaya; akanena, ‘Je, yamekuelea haya unayosoma?’ Akasema, ”Nitawezaje kuelewa, mtu asiponiongoza?’ Akamsihi Filipo apande na kuketi pamoja naye” (Mdo 8:30-31).


Tupokeeje ufunuo wa Mungu?

Tupokee ufunuo wa Mungu kwa kusadiki mafundisho ya Kanisa lake, ili tuzidi kumjua na kuambatana naye bila ya kudanganyika. Yesu aliwaambia Mitume wake,
“Awasikilizaye ninyi anisikiliza mimi, naye awakataaye ninyi anikataa mimi; naye anikataaye mimi amkataa yeye aliyenituma” (Lk 10:16).
“Sisi nasi twamsukuru Mungu bila kukoma, kwa kuwa, mlipopata lile neno la ujumbe la Mungu mlilolisikia kwetu, mlilipokea si kama neno la wanadamu, bali kama neno la Mungu; na ndivyo lilivyo kwelikweli, litendalo kazi pia ndani yenu ninyi mnaoamini” (1Thes 2:13).


Je, Mungu amegawanyika sehemu tatu?

Hapana, Mungu hagawanyiki hata kidogo, bali daima ni Umoja kamili.
“Bwana Mungu wetu ni Bwana mmoja” (Mk 12:29).
Tumuabudu yeye peke yake katika nafsi tatu, na Utatu wa nafsi katika Umoja wa hali yake, tusichanganye nafsi wala kugawa Umungu. Baba si Mwana wala Roho Mtakatifu. Mwana si Baba wala Roho Mtakatifu. Roho Mtakatifu si Baba wala Mwana. Lakini milele yote nafsi hizo tatu ni Mungu yuleyule pasipo tofauti ya kuzitenganisha: kila moja imo ndani ya nyingine.
“Mimi na Baba tu umoja” (Yoh 10:30).


Biblia ni nini? Asili, Historia, waandishi na mipaka yake

Biblia ni mkusanyiko wa vitabu mbalimbali vinavyohusu kazi ya Mungu ya kuwakomboa mwanadamu kuanzia enzi za Mababu na manabii Wa Waisraeli, Enzi za Yesu na za Mitume wa Yesu.

Je, Biblia ilipatikanaje? Nini chanzo na asili ya Biblia.

Biblia iliundwa kwa kukusanya vitabu vya dini vya wakristo hapo awali na kuunda kitabu kimoja. Kwa maana hii, Biblia ni vitabu teule vya dini vilivyoonekana vinafaa kutumika kwa waumini Wakristo ili kusaidia Imani yao. Hivyo basi, kama Biblia ni vitabu teule tuu vipo vitabu vingine vya dini ambavyo havikuwekwa Kwenye Biblia.
Wakristo wa kwanza walichagua vitabu kadhaa na kuviweka pamoja na kisha kuvita Biblia. Biblia ni mkusanyiko wa vitabu muhimu tuu vya dini mpaka kufikia Enzi za Mitume.

Je, Biblia ndicho kitabu pekee cha neno la Mungu?

Hapana, Biblia sio kitabu pekee cha neno la Mungu isipokua Biblia ni kitabu kilichoidhinishwa rasmi kutumika Kama kitabu kikuu cha Wakristo. Hii ni kwa sababu Biblia imeundwa na vitabu muhimu tuu vilivyochaguliwa na wakristo wa kwanza vilivyoonekana vinafaa kwa kufundishia, Ibada na kukuza Imani. Kwa hiyo basi vipo vitabu vingine ambavyo haikuwekwa Kwenye Biblia ambavyo ni Maneno ya Mungu.
Hii ndiyo sababu kwa nini Wakatoliki wana vitabu vingi kuliko madhehebu Mengine. Yaani sababu ni kwamba madhehebu Mengine walivitoa vitabu vingine vilivyounda Biblia. Na Wakatoliki waliweka vitabu vingine vya dini Kwenye Biblia walivyoona vinafaa pia kutumika.

Je nje ya Biblia hakuna Neno la Mungu au Maandiko matakatifu?

Nje ya Biblia kuna Neno la Mungu na Maandiko Matakatifu. Hii Inamaanisha kuwa Biblia sio kitabu pekee cha neno la Mungu. Zipo nyaraka na Vipo vitabu vingine vingi ambavyo viliandikwa na Manabii na Mitume ambavyo havikuwekwa kwenye Biblia lakini ni mafundisho ya Mungu. Biblia ni mkusanyiko wa vitabu vikuu vya Mungu.
Kumbuka kuwa sio nyaraka zote za Mitume ziliandikwa Kwenye Biblia. Vile vile manabii walikuwa ni wengi kuliko waliowekwa Kwenye Biblia.

Je Biblia ndiyo mafundisho ya Mungu pekee?

Hapana, Biblia sio mafundisho pekee ya Mungu. Hii ni kwa sababu sio mambo yote aliyofanya na kusema Mungu yaliandikwa na vilevile Mitume hawakua watu wa Mwisho kupokea Roho mtakatifu na kupokea neno la Mungu.

Biblia inatuthibitishia yenyewe kuwa haijakamilika na Si mambo yote yameandikwa Kwenye Biblia

Biblia inatuthibitishia kuwa haijakamilika tunaposoma (Yohane 21:25)
Biblia inatuambia hivi…”Kuna mambo Mengine mengi aliyofanya Yesu, ambayo Kama yangeandikwa yote, moja baada ya jingine, nadhani hata ulimwengu wenyewe usingetosha kuviweka vitabu ambavyo vingeandikwa.”…Kwa mstari huu Biblia inatuthibitishia kuwa haikuandikwa vitu vyote.

Je Biblia ni mwisho wa Maandiko ya Mungu?

Biblia sio mwisho wa Maandiko ya Kimungu.
Biblia ni sehemu ya maneno ya Mungu mpaka miaka ya Mitume
Hata sasa Mungu anafanya kazi na watu wake kupitia Roho Mtakatifu na kwa kwa sababu hii Biblia sio mwisho wa kazi ya Mungu ya kusema na watu wake.
Mungu yu hai na anafanya kazi na watu wake mpaka sasa kwa kutumia vinywa vya watu Kama aliyofanya hapo awali.
Hata maneno unayohubiriwa sasa yanaweza kuwa ni kutoka kwa Mungu kwa maana hata waandishi wa Biblia walitumiwa na Mungu Kama wahubiri wa sasa. Mungu ni yule yule, Roho Mtakatifu ni yuleyule na Neno ni lile lile.
Kwa hiyo Biblia ni maneno yaliyochaguliwa mpaka enzi za Mitume. Vitabu vilivyofwata Baada ya Mitume japokuwa viliandikwa kwa Roho Mtakatifu havikuwekwa Kwenye Biblia.

Sababu ya Kanisa katoliki kutumia mapokeo na Maandiko ya Watakatifu

Kanisa katoliki linatumia mapokeo na Makala za watakatifu kwa Imani kuwa Mungu yule yule aliyefanya kazi tangu zamani anafanya kazi na watu wake mpaka sasa na hivyo Maandiko ya watu wa Mungu yanafaa kutumika kama yalivyotumika ya watu wa kale.

Yesu alituambia nini kuhusu Neno la Mungu na Mwendelezo wa kazi ya Mungu ya kusema na watu?

Yesu alituambia hivi katika (Yohane 16:12-15)..”Ninayo mengi ya kuwaambieni Ila kwa sasa hamuwezi kuyastahimili. Lakini atakapokuja huyo Roho wa Ukweli atawaongoza kwenye ukweli wote. Maana hatasema kwa Mamlaka yake mwenyewe bali atasema atakayoyasikia na kuwajulisheni yatakayokuja. Yeye atanitukuza Mimi kwa kuwa atawajulisheni Yale atakayoyapata kutoka kwangu “…
Sasa basi,kama Roho Mtakatifu ni yuleyule na kazi zake ni Zile Zile za tangu Mitume, kwa nini hatukubali kuwa Anafanya kazi mpaka sasa kupitia watu wa Mungu? Kwa nini tunakataa mafundisho yao? Kwa nini tunashindwa kuelewa kuwa Biblia haikuwa mwisho wa Neno la Mungu? Kwa nini tunakana Mapokeo ya Watakatifu? Kwa nini hatuwaamini watumishi wake wa sasa?

Maswali na Majibu kuhusu Malaika

Kwanza Mungu aliumba nini?

Kwanza Mungu aliumba Malaika (Kol 1:16)


Malaika ni viumbe gani?

Malaika ni viumbe vya Mungu vilivyo roho tu wenye akili na utashi. (Zab 91:11, Ebr 1:7, Ufu 12:7-9)


Mungu aliumba Malaika katika hali gani?

Mungu aliumba Malaika katika hali njema na heri kubwa.


Malaika wote walidumu katika hali njema na ya heri?

Siyo, Malaika wengine walikosa kwa kumkaidi Mungu, Wakatupwa Motoni.
Ndio Mashetani ambao Mkubwa wao ni Lusiferi. (Yoh 8:44, Uf 12:7-9)


Kwa nini Mungu ameumba Malaika?

Mungu ameumba Malaika ili wamtukuze, wafurahi naye Mbinguni, na wawe matarishi wake kwa wanadamu. (Tob 12:12, Lk 16:22)


Malaika wema kazi yao ni nini?

Malaika wema kazi yao ni kutuombea, kutumwa na Mungu kwetu, na wanatulinda kama Malaika wetu Walinzi. (Ebr 13:2)


Kila Mwanadamu anaye Malaika wake wa kumlinda?

Ndiyo, Kila Mwanadamu anaye Malaika wake wa kumlinda ndiye Malaika Mlinzi. (Mt. 18:10)


Malaika Walinzi wanatutendea nini?

Malaika walinzi hutupenda, hutuongoza, na kutulinda roho na mwilini (Zab 90:11)


Je Malaika wote ni sawa?

Hapana. Malaika wote sio sawa, maana kuna;
1. Malaika wakuu
2. Malaika wanaomtumikia Mungu Mbinguni yaani Makerubi na Maserafi
3. Malaika Walinzi


Malaika wakuu wako watatu ambao ni?

Malaika wakuu wako watatu: Mikaeli, Raphaeli na Gabrieli (Dn 10:13, Tobiti 12:15, Lk 1:26)


Makao ya shetani ni wapi na anatamani nini?

1. Mashetani kazi yao ni kuteswa Motoni
2. Hutaka kutudhuru roho na mwili na kutupoteza milele (1 Petro 5:8, Yoh 8:44)


Kisha kuumba Malaika Mungu aliumba nini?

Kisha kuumba Malaika Mungu aliumba Mbingu na dunia, na viumbe vingine vingi vyenye kuonekana mimea na watu. (Mwanzo 1;31)


Viumbe vyenye hiari ni vipi?

Malaika na watu ndio viumbe pekee vyenye hiari ya kuchagua wenyewe wachangie mpango wa Mungu au la.
“Nazishuhudiza mbingu na nchi juu yenu hivi leo, kuwa nimekuwekea mbele yako uzima na mauti, baraka na laana; basi, chagua uzima, ili uwe hai, wewe na uzao wako; kumpenda Bwana, Mungu wako, kuitii sauti yake, na kushikamana naye; kwani hiyo ndiyo uzima wako” (Kumb 30:19-20).


Malaika na watu wanaweza kuchagua hata nini?

Malaika na watu wanaweza kuchagua hata wawe wema au wabaya milele.
“Kulikuwa na vita mbinguni: Mikaeli na malaika zake wakapigana na yule joka, yule joka naye akapigana nao pamoja na malaika zake; nao hawakushinda, wala mahali pao hapakuonekana tena mbinguni” (Ufu 12:7-8).
Chaguo letu binadamu linafanyika siku kwa siku kwa kuchukua misimamo mizuri au mipotovu kuhusu dini na maadili.
“Mwayachunguza Maandiko, kwa sababu mnadhani kwamba ninyi mna uzima wa milele ndani yake; na hayo ndiyo yanayonishuhudia. Wala hamtaki kuja kwangu mpate kuwa na uzima” (Yoh 5:39-40).


Malaika wakoje?

Malaika ni roho tupu walioumbwa na Mungu ili wamtukuze milele, wamlinde kila mtu na kumtumikia Bwana Yesu katika kutuokoa.
“Angalieni, msidharau mmojawapo wadogo hawa, kwa maana nawaambia ya kwamba malaika zao mbinguni sikuzote huutazama uso wa Baba yangu aliye mbinguni” (Math 18:10).


Je, toka mwanzo sisi watu tunaasi mpango wa Mungu peke yetu?

Hapana, toka mwanzo sisi watu tunaasi mpango wa Mungu kwa kuvutwa na mashetani, yaani malaika waliokataa moja kwa moja kumtumikia; baada ya dhambi ya asili hao wanatutumia sisi pia tuangushane na wenzetu.
Lakini Mungu aliwahi kumuambia Shetani:
“Nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao wako, na uzao wake; huo utakuponda kichwa, na wewe utamponda kisigino” (Mwa 3:15).
“Hata ulipowadia utimilifu wa wakati, Mungu alimtuma Mwanawe ambaye amezaliwa na mwanamke” (Gal 4:4).

Maswali na Majibu kuhusu Liturujia

Misa Takatifu ina sehemu kuu ngapi?

Misa Takatifu ina sehemu kuu mbili
1. Litrujia ya Neno
2. Liturujia ya Ekaristi


Litrujia ya Ekaristi ina sehemu kuu ngapi?

Litrujia ya Ekaristi ina sehemu kuu tatu
1. Matayarisho ya vipaji
2. Sala ya Ekaristi
3. Ibada ya Komunyo


Liturujia ni nini?

Liturujia ni tendo la Kristo mwenyewe na Kanisa la kumtukuza na kumwabudu Mungu Baba; na hivyo kutekeleza fumbo la Wokovu kwa kuwatakasa watu


Liturujia ina nafasi gani katika Kanisa?

Liturujia ambayo ni tendo takatifu kuliko yote ndiyo chemichemi ambayo nguvu ya uhai wa Kanisa inabubujika na Kristo anaendeleza Kazi ya Ukombozi wetu


Katika liturujia waamini wanafanya nini?

Katika Liturujia waamini wanashiriki kwa matendo na kwa Ibada adhimisho lote yaani sala, nyimbo na matendo yote ya Ibada; na asiposhiriki matendo hayo kikamilifu, anakosa mafao kamili ya neema ipatikanayo katika Ibada hiyo.


Kilele cha Liturujia ni nini?

Kilele cha liturujia ni Sadaka Takatifu ya Misa


Kwa namna gani Mungu Baba ndiye asili na lengo la Liturujia?

Mungu Baba ndiye asili na lengo la Liturujia kwa sababu katika liturujia anatujaza Baraka zake katika Mwanae Yesu Kristo, naye anatumiminia Roho Mtakatifu mioyoni mwetu


Katika Liturujia Roho Mtakatifu anatenda nini kuhusiana na Kanisa?

Katika Liturujia Roho Mtakatifu analiandaa Kanisa likutane na Bwana wake


Ni nani hupanga Taratibu za Liturujia?

Mama Kanisa ndiye mwenye kupanga taratibu zote za Liturujia Katika mwaka mzima.
Huu mpango huitwa mwaka wa kanisa


Katika mwaka wa kanisa tunakumbuka nini?

Katika Mwaka wa Kanisa tunakumbuka natunaadhimisha matukio na mafumbo yote ya ukombozi wetu na hivyo twapata neema zake


Adhimisho la Liturujia Hutumia Ishara na Alama zipi?

Adhimisho la Liturujia Hutumia Ishara na Alama zinazohusiana na uumbaji, maisha ya binadamu na historia ya wokovu; nazo ni;
  1. mwanga,
  2. maji,
  3. moto,
  4. kuosha mikono/kupaka mafuta
  5. kumega mkate,
  6. kuwekea mikono n.k


Nani huadhimisha Liturujia?

Liturujia iliyo kazi ya Kristo Kuhani Mkuu na kichwa cha Kanisa huadhimishwa na kusanyiko lote, kila mmoja kulingana na kazi yake.


Liturujia inaadhimishwa wapi?

Liturujia inaadhimishwa pale waamini walipokusanyika kwa lengo hilo; kwa sababu Ibada katika Roho na Kweli ya Agano Jipya haifungwi na mahali fulani tuu, kwani dunia yote ni Takatifu


Liturujia Ifanyike mahali pa namna gani?

Liturujia ifanyike mahali palipoandaliwa vizuri iwezekanavyo kwa kuwa katika tendo la Ibada tunakutana na Mungu


Mwaka wa Kanisa una vipindi vikubwa vingapi?

Mwaka wa Kanisa una vipindi vikubwa vitano ambavyo ni;
1. Majilio = Majuma manne
2. Noeli = Kuzaliwa hadi Epifania
3. Kwaresma = Majuma sita na Juma Kuu
4. Pasaka = Siku ya Pasaka hadi Pentekoste
5. Kipindi cha mwaka majuma 34


Majilio ni nini?

Majilio ni kipindi cha Dominika nne cha kujiandaa na Sherehe ya Kuzaliwa Bwana wetu Yesu Kristo, yaani NOELI.
Kinawakilisha karne zote za Agano la Kale


Kwaresma ni nini?

Kwaresma ni kipindi cha siku 40 cha kujiandaa kuadhimisha Sherehe kuu ya PASAKA yaani kufufuka kwa Bwana wetu Yesu Kristo.
Tunajiandaa kwa Kufunga Kusali, Kutubu, na Matendo Mema.


Wakati wa kwaresma yawapasa waamini kufanya nini?

Waamini wanapaswa kujitakasa zaidi kwa;
  1. kusali,
  2. kufunga,
  3. toba na
  4. matendo mema


Kipindi cha Pasaka hudumu kwa siku ngapi?

Kipindi cha Pasaka hudumu kwa siku 50;
Yaani kuanzia Sherehe ya Pasaka hadi Sherehe ya Pentekoste


Siku za Dominika Kanisa huadhimisha nini?

Kila Dominika Kanisa Huadhimisha kumbukumbu ya Fumbo la Pasaka; Yaani;
Mateso, Kifo na Ufufuko wa wa Bwana, katika hali ya kutomwagika damu tena.


Kwa nini Jumapili inapaswa kuitwa siku ya Bwana au Dominika?

Jumapili inapaswa kuitwa Siku ya Bwana au Dominika kwa sababu ndiyo siku Bwana amefufuka Mshindi wa Dhambi na Mauti


Kipindi cha Mwaka ni nini?

Kipindi cha Mwaka ni kipindi cha kufurahi kuishi matunda ya ukombozi wetu


Sikukuu Kubwa Kupita zote Katika Kanisa ni ipi?

Sikukuu Kubwa Kupita zote Katika Kanisa ni PASAKA

Maswali na Majibu kuhusu Kuabudu kwa Wakatoliki

Wakatoliki tunamwabudu Mungu kwa namna gani?

Tunamwabudu Mungu kwa sala , sadaka na matendo mema


Je, tuna ruhusa ya kuwaabudu Watakatifu?

Hatuna ruhusa ya kuwaabudu Watakatifu tunawaheshimu tu.


Je sanamu zimekatazwa?

Sanamu hazijakatazwa, ila tunaziheshimu kwa sababu zinatukumbusha Mungu na Watakatifu. (Kut 25:18-22).
18 Nawe fanya makerubi mawili ya dhahabu; uyafanye ya kazi ya kufua, katika hiyo miisho ya kiti cha rehema, huku na huku. 19 Weka kerubi moja mwisho mmoja, na kerubi la pili mwisho wa pili; fanya hayo makerubi ya kitu kimoja na kiti cha rehema, mwisho huku na mwisho huku. 20 Na hayo makerubi yatainua mabawa yao juu, na kukifunika hicho kiti cha rehema kwa mabawa yao, na nyuso zao zitaelekeana hili na hili; nyuso za hayo makerubi zitaelekea kiti cha rehema. 21 Weka kiti cha rehema juu ya hilo sanduku, kisha utie huo ushuhuda nitakaokupa ndani ya sanduku. 22 Nami nitaonana nawe hapo, na kuzungumza nawe pale nilipo juu ya kiti cha rehema, katikati ya hayo makerubi mawili yaliyo juu ya sanduku la ushuhuda, katika mambo yote nitakayokuagiza kwa ajili ya wana wa Israeli. Kutoka 25 :18-22.
Vile vile Mungu alishawahi kuwaagiza Waisraeli Wachonge sanamu ya nyoka na yeyote atakayeumwa na nyoka akiiangalia atapona.


Mfano wa sanamu takatifu ni zipi?

Sanamu ya Bikira Maria, Mtoto Yesu, Mt. Yosefu, Moyo wa Yesu na za Watakatifu.


Ni nanai ana kosa kumuabudu Mungu?

Anayekosa kumuabudu Mungu ni yule;
1. Anayeacha kusali au anayesali hovyo
2. Anayemkufuru Mungu
3. Anayeamini na kushika mambo ya kipagani


Ni nini maana ya kuabudu sanamu?

Kuabudu sanamu ni kukipa kiumbe chochote heshima au upendo anaostahili Mungu peke yake.


Kutokumuabudu Mungu ni kwa namna gani?

Ni kuruhusu kitu chochote kimtawale mtu badala ya Mungu, mfano cheo, pombe, mali, shetani, tuisheni, kazi, na kutoadhimisha Jumapili au kutoshiriki.


Mkatoliki anaabuduje?

Mkatoliki anaabudu kwa kupiga goti au magoti mawili na ni mbele ya sakramenti ya Ekaristi Takatifu tuu hasa wakati wa kuingia na kutoka kanisani


Je magoti yanayopigwa wakati mwingine tofauti na wakati wa kuabudu yana maana gani?

Magoti yanayopigwa wakati wa sala mfano kanisani, nyumbani, mbele ya sanamu, jumuiyani, shuleni yanaitwa Mkao wa sala


Kwa nini wakatoliki wanaweka sanamu Kanisani?

Tunaweka sanamu Kanisani kwa sababu tunaheshimu anayewakilishwa na sanamu hiyo kwa mfano Yesu Kristo, Mama Bikira Maria, Malaika na Watakatifu; na kamwe hatuziabudu. (Kutoka 25:18-22)
Hata Waisraeli kwenye hekalu lao walikua na sanamu kama tunavyosoma hapa;
“18 Nawe fanya makerubi mawili ya dhahabu; uyafanye ya kazi ya kufua, katika hiyo miisho ya kiti cha rehema, huku na huku. 19 Weka kerubi moja mwisho mmoja, na kerubi la pili mwisho wa pili; fanya hayo makerubi ya kitu kimoja na kiti cha rehema, mwisho huku na mwisho huku.20 Na hayo makerubi yatainua mabawa yao juu, na kukifunika hicho kiti cha rehema kwa mabawa yao, na nyuso zao zitaelekeana hili na hili; nyuso za hayo makerubi zitaelekea kiti cha rehema. 21 Weka kiti cha rehema juu ya hilo sanduku, kisha utie huo ushuhuda nitakaokupa ndani ya sanduku. 22 Nami nitaonana nawe hapo, na kuzungumza nawe pale nilipo juu ya kiti cha rehema, katikati ya hayo makerubi mawili yaliyo juu ya sanduku la ushuhuda, katika mambo yote nitakayokuagiza kwa ajili ya wana wa Israeli. (Kutoka 25 :18-22.)
Kwa hiyo kama Mungu mwenyewe aliagiza Sanamu za Malaika zichongwe na kusema atakua hapo na kuongea na watu wake. Je sio vyema zaidi kuwa na sanamu na Picha ya Mwanae wa Pekee Yesu Kristo na kuongea na Mungu mbele yake kama alitaka ya malaika ambao sio Mungu?
Mfano mwingine ni pale Mungu alivyomwabia Musa achonge Sanamu ya Nyoka wa shaba.
“BWANA akamwambia Mose, “Tengeneza nyoka wa shaba na umweke juu ya mti, ye yote aliyeumwa na nyoka anaweza kumtazama na akaishi tena.’’ 9Kwa hiyo Mose akatengeneza nyoka wa shaba na kumweka juu ya mti. Kisha wakati mtu ye yote alipoumwa na nyoka, naye akamtazama yule nyoka wa shaba, aliishi.” (Hesabu 21:8-9).
Kwa Mfano huu Je tunaweza kusema kuwa sanamu ya nyoka ina nguvu ya uponyaji kuliko ya Yesu aliye Mungu? Kumbuka hapa watu walioona sanamu hii ya nyoka hawakukoponywa na nguvu ya sanamu ya shaba bali kwa nguvu ya neema ya Mungu kupitia Imani kwa Mungu. Kwa hiyo unaposali mbele ya picha au sanamu hautegemei nguvu ya sanamu bali unategemea neema ya Mungu kwa njia ya Imani yako kwa Mungu.
Kama vile Sanamu hii ya nyoka aliyoagiza Mungu iwekwe ilivyowekwa kwa nia ya uponyaji kwa yule aitazamaye vivyo hivyo Sanamu na Picha za Kanisani zinawekwa kwa nia maalumu na kwa neema maalumu. Ndiyo maana hazifanani. Na zinabarikiwa kwa kuombewa Baraka Ili zizae neema kwa wanaozitumia.

Sanamu au picha sio haramu bali maana ya hiyo sanamu au picha ndio inaiharamisha.

Kuna tofauti kati ya kuabudu na kuheshimu. Wakatoliki wanaweka sanamu kwa heshima na sio kwa kuabudu, ndio maana unaposali mbele ya picha ya Yesu hausali ee sanamu nisaidie bali unasema ee Yesu nisaidie.
Je tuseme tunamwabudu Raisi kwa kuheshimu picha yake kwa kuiinamia? Je tunaabudu bendera kwa kuheshimu na kupigia saluti? Je taratibu zabunge za kutoa heshima na taratibu za mahakama ni kuabudu?. Je kuapa mbele ya picha ya Raisi ni kumuabudu Raisi? Je kuapa na Biblia ni kuabudu Biblia? Je tunapobusu Biblia na kuitunza kwa heshima tunaiabudu? Tofauti ya Biblia na sanamu ni nini? Je, kwenye Biblia kinachoheshimiwa ni karatasi au maana ya yale maneno kwenye karatasi. Pengine usingeheshimu kama hujajua kuyasoma.
Kuna tofauti gani kati ya biblia yenye Maandishi na msalaba wa kuchonga wenye kuonyesha kile kinachosemwa na biblia? kama unaweza kuheshimu biblia yenye karatasi tena pale unapoweza kuzisoma na pengine ungeizarau kama ni ya lugha tofauti na hujui kilichoandikwa? Je Msalaba uliobeba maana ya kile kilichoandikwa kwenye Biblia unaona si kitu? Kama Kinachoheshimiwa kwenye Biblia sio karatasi bali maana maneno yaliyoandikwa vivyo hivyo kinachoheshimiwa kwenye picha au sanamu sio chuma yake au mti ukiochongwa bali ni maana ya hiyo sanamu.
Hii ndio maana nasema kuna tofauti ya kuabudu na kuheshimu.
Kumbuka kuwa picha au sanamu yoyote ya Kikatoliki lazima ibarikiwe kwanza ndio uweze Kusali mbele yake. Inapobarikiwa inaombewa uwepo wa yule anayewakilishwa na picha/sanamu hiyo uwe pale sanamu ilipo na anayesali pale sala yake Ifike kwa mlengwa anayeonekana kwa ishara ya sanamu/picha. Kwa Mfano askofu au padri anapobariki sanamu ya Yesu anaomba kuwa “Yesu awepo pale kwenye sanamu na Neema zake”, kwa hiyo yeyote anayesali mbele ya sanamu hiyo anaamini kuwa Yesu yuko pale na anasali Mbele yake. Kwa hiyo kinachopewa heshima sio ile sanamu bali ni yule anayeonekana kwa ishara ya ile sanamu au picha.

Tofauti ya Sanamu za Kikatoliki na za kipagani ni Kwamba,

Sanamu za Kipagani: Sanamu hizi huchukuliwa kama Mungu na huabudiwa na kutolewa Sadaka kama Mungu Mwenyewe.

Sanamu za Kikatoliki: Sanamu hizi huchukuliwa kama ishara ya kile inachokiwakilisha, haiabudiwi kamwe bali inaheshimiwa tuu.

Daima Tumia Sanamu na Picha zilizobarikiwa kwani zimenuiwa uwepo wa yule inayemuwakilisha na utaongea naye hapo. Sisi tunaamini kwamba kwenye Sanamu ya Yesu kuna uwepo wa Yesu. Kama vile Mungu anavyowaambia Waisraeli katika (Kutoka 25 :22) baada ya kuwaagiza wachonge sanamu za Makerubi (Malaika) 22 Nami nitaonana nawe hapo, na kuzungumza nawe pale nilipo juu ya kiti cha rehema, katikati ya hayo makerubi mawili yaliyo juu ya sanduku la ushuhuda, katika mambo yote nitakayokuagiza kwa ajili ya wana wa Israeli. (Kutoka 25 :22)Sanamu au picha ni ishara wazi ya uwepo wa kile kisichoonekana.

Jifunze kupitia Sanduku la Agano na Msalaba wa Yesu

Kwenye Agano la kale: Ndani ya hekalu la Waisraeli walikua na Sanduku la agano, sanduku hilo lilikua na vibao vya Amri za Mungu ambavyo ni Ishara ya Agano lao na Mungu na ndani ya sanduku kulikuwepo pia Mfano wa Kiti ambacho kimezugukwa na sanamu za viumbe kama malaika nyuso zao zikielekea kiti hicho Kutoka 25:10-22. Waisraeli walikua wanasali kuelekea sanduku la Agano wanapokuwa Hekaluni na hata wakiwa majumbani mwao walisali kuelekea upande lilipo Hekalu. Waisraeli walisali kuelekea Sanduku la Agano wakiamini kwamba Mungu yupo kati ya sanduku lile. Lakini sanduku lile halikuwa Mungu. Waisraeli waliona fahari juu ya Sanduku lile na walilithamini na kuliheshimu kwa kuwa lilionyesha uwepo wa Mungu na popote lilipokuwa waliamini Mungu yupo.
Kwenye Agano jipya: Wakristu wanasali Mbele ya Msalaba wa Yesu ambao unaonyesha kazi ya wokovu alioufanya Yesu kwa wanadamu ya Kuwakomboa watu kwa kifo chake Msalabani. Na Msalaba huo ni Ishara ya Ukombozi wa Agano jipya na la Milele. Kama ilivyokuwa kwa Sanduku la Agano, Wakristu wanaheshimu msalaba ambao ni ishara ya wokovu wao na wanaamini kuwa Mungu yupo kati ya Msalaba huo lakini Msalaba huo sio Mungu. Wakristu wanaona fahari juu ya msalaba wa Yesu kwa kuwa ndio ishara ya wokovu wao.
FUNZO:Kupitia Mfano wa Sanduku la Agano na Msalaba tunajifunza kuwa Vyote havikuwa Mungu ila vinaheshimiwa kwa Imani kuwa Mungu yupo pale. Vilevile, vyote ni ishara ya wazi ya Agano la Mungu na Wanadamu.

Kwa nini tunasali mbele ya Picha/Sanamu na Hasa kufanya Ishara ya msalaba?

Tunasali mbela ya sanamu kwa sababu tunaamini sanamu inaakisi uwepo wa mhusika aliyechorwa au kuchongwa kwenye hiyo sanamu/picha. Ndio maana wakatoliki wanasali kwenye picha au sanamu iliyobarikiwa tuu kwa sababu Sanamu inapobarikiwa inaombewa uwepo wayule anayewakilishwa pale.
Tunafanya ishara ya msalaba kwenye sanamu kama sala ya utangulizi ambayo inathibitisha kuwa hatuabudu kile kilichoko pale bali kile tunachokifanya tunakifanya huku tukikiri Umungu na Heshima ya Utatu Mtakatifu (Mungu; Baba, Mwana na Roho Mtakatifu.). Vile vile tunamtukuza Mungu katika Utatu Mtakatifu kwa sababu ya yule anayewakilishwa na picha au sanamu.

Kwa nini watu wanabusu picha na sanamu?

Hii ni ishara ya Upendo kwa yule anayewakilishwa kwenye picha au sanamu husika. Hata katika maisha ya kawaida watu hubusu picha za wazazi na wapendwa wao. Maana ni ile ile.


Mungu akiwa Roho, viungo ambavyo pengine anapewa vina maana gani?

Mungu akiwa Roho, viungo ambavyo pengine anapewa vinamaanisha tu sifa fulani: k.mf. macho ujuzi wake, mikono uwezo wake, mabawa ulinzi wake, n.k. “Roho haina mwili na mifupa” (Lk 24:39).


Je, ni halali kuheshimu sanamu?

Ndiyo, ni halali kuheshimu sanamu kama viwakilishi vya Yesu, Mama yake na watakatifu wake, ambao zinaleta sura zao.
Kwa msingi huo walimsihi Yesu “waguse hata pindo la vazi lake tu. Na wote waliogusa wakaponywa kabisa” (Math 14:36).
“Mimi, hasha, nisione fahari juu ya kitu chochote il msalaba wa Bwana wetu Yesu Kristo” (Gal 6:14).
Shopping Cart